موسوعة الإيمان
كتاب "الإيمان الذي فرضه الله على عباده مما ورد في القرآن الكريم والسنة النبوية" من تأليف أ.د. محمد بن عبد الله السحيم ود. سامي بن محمد الخليل، هو كتاب شامل لجميع أصول ومهمات الاعتقاد ومسائله. يتميز الكتاب بربط المسائل العقدية بالكتاب الكريم والسنة النبوية المطهرة، ويحرص على تأسيس العقيدة بطريقة مختصرة وشاملة باستخدام عبارات ميسرة. يتناول الكتاب مسائل الاعتقاد بعيداً عن المباحث الكلامية والفلسفية، ويهدف إلى تقديم موضوعات الاعتقاد بأسلوب يسهل على جميع المستويات العلمية فهمها واستيعابها.
Ensaiklopedia ya imani aliyowafaradhishia Mwenyezi Mungu waja wake kutoka katika yale yaliyokuja katika Qur'ani Tukufu na Sunna za Mtume.
(Ni ensaiklopidia inayojumuisha misingi yote na mambo muhimu ya itikadi na masuala yake. Ina sifa maalumu ya kufungamanisha masuala ya itikadi na Qur'ani Tukufu, na Sunna za Mtume zilizosafika, huku ikifanya juhudi kubwa katika kuweka msingi madhubuti wa itikadi kwa njia fupi na ya kujumuisha mambo yote, kwa kutumia maneno rahisi kueleweka wakati wa kubainisha na kuweka wazi masuala ya itikadi. Ensaiklopidia hii pia imesalimika kutokana na mijadala ya kimantiki na kifalsafa).
Utangulizi wa Ensiklopedia hii
Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu
Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliyemteremshia mja wake Kitabu na hakukifanya kuwa ni chenye kwenda upande. Na ninashuhudia ya kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, asiye na mshirika yeyote, Ufalme ni wake, na ni zake sifa njema, na Yeye ni Muweza juu ya kila kitu. Na ninashuhudia ya kwamba Muhammad ni mja wake, na ni Mtume wake, na ni wa kuaminiwa juu ya Ufunuo wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie.
Ama baada ya hayo: Elimu ya itikadi ndiyo elimu tukufu zaidi na kuu zaidi kuliko elimu zote; kwa sababu inazungumza juu ya Mtukufu zaidi ambaye ni Yeye wa haki, Mtakatifu, Mtukufu - na makusudio matukufu zaidi - ambayo ni kumpwekesha Yeye na kumuamini - na mwisho mtukufu zaidi - ambao ni kumuona Mola Mlezi Mtukufu katika nyumba ya neema, na kumfuata Nabii Mtukufu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na kufuata njia iliyonyooka. Basi ndiyo maana, tumekusudia kuandika kitabu ambacho kinajumuisha masuala ya itikadi, tukitafuta uongofu katika hilo kutoka katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na Sunna za Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, mbali na istilahi za kisasa zinazozungumza juu ya itikadi, na kubainisha kwa urefu maneno mbalimbali, na kupambanua nguzo mbalimbali, na masharti mbalimbali, na kujaribu kukifanya kiweze kufikiwa na kila mtu, ili aweze kufaidika nacho mwanazuoni na wanafunzi katika vyuo vikuu na sehemu zinginezo, na Waislamu kwa ujumla.
Sababu ya kuandika kitabu hiki:
Wema wetu waliotangulia walifanya juhudi kubwa katika kubainisha itikadi sahihi, na kubainisha yanayopingana nayo, na kuwajibu wale wenye kwenda kinyume nayo. Kitabu hiki kimekuja kuleta karibu yale waliyoyaandika watangulizi kwa wanafunzi na kwa Waislamu kwa ujumla. Tumekusanya masuala ya Itikadi katika kitabu kimoja kilichokusanya maswala yote, na tumeeleza itikadi sahihi pekee pasina kuingia katika kujibu hoja za wenye kwenda kinyume. Pia tumekuwa makini katika utungaji kwa kuweka ibara rahisi na za wazi, na kuzipangalia kikamilifu.Tunatumai kwamba kwa kufanya hivyo tutakuwa tumetimiza malengo mawili: Moja wapo: Kuchangia kuileta karibu zaidi elimu ya wema waliotangulia. Na lengo jingine: Kuziba hitajio kubwa katika Maktaba ya maswala ya itikadi, nalo ni: Kuleta kitabu chenye ibara nyepesi kilichokusanya maswala yote yanayohusu Itikadi.
Mfumo tuliotumia katika utungaji wa kitabu hiki:
Kubainisha aya na hadithi zinazohusu kila maudhui katika maudhui za itikadi, na kutoa ufupisho kutoka katika aya hizo.
Kubainisha mada zote za vitabu vya itikadi, sawa vitabu vikubwa vikubwa, au vile vilivyofupishwa, au vile vya maelezo ya vitabu vilivyofupishwa; ili kuhakikisha kwamba kutoa kwetu mafundisho ya itikadi katika aya na hadithi hizo kumekusanya yale yote waliyoandika waandishi wa vitabu vya itikadi.
Linapokuja suala la kiitikadi katika Qur'ani Tukufu au katika Sunna za Mtume kwa sura moja; tunatosheka na dalili moja au mbili zilizotaja suala hilo. Ama ikiwa suala hilo litatajwa katika Qur'ani Tukufu au Sunna za Mtume kwa njia nyingi - kama vile (Mwenyezi Mungu) sifa yake ya kuzungumza, kuwa kwake juu, na kuwa na mkono, na waumini kumuona Mola wao Mlezi katika mahali pa kusimama siku ya Kiyama, na Peponi, basi tunataja dalili moja kwa kila moja miongoni mwa dalili hizo, lakini hatulazimiki kutaja yote yaliyotajwa katika mlango huo.
Tunaweza kutaja baadhi ya vipengele vya suala katika mlango fulani, kisha tukavirudia tena na kuvikamilisha katika mlango mwingine, kama vile tulivyotaja habari za uumbaji wa Malaika katika mlango wa uumbaji, na tukamalizia mazungumzo juu ya hilo katika kitabu cha kuamini Malaika, na tukataja katika mlango wa kuamini uwepo wa Mwenyezi Mungu baadhi ya aya zinazoonyesha uwepo wake. Na aya hizo hizo zinaweza kutajwa katika mlango wa Ulezi (Rubuubiyya) kwa sababu ya ukaribu wa milango hiyo. Kwa hivyo makusudio ya mlango wa kuamini uwepo wa Mwenyezi Mungu ni kuweka wazi hoja za uwepo wa Mola Mlezi ambazo wasiomuamimi Mwenyezi Mungu (Wapagani) wanazikataa. Wakati makusudio ya mlango wa kuamini Uungu wa Mwenyezi Mungu ni kuthibitisha Uungu wake unaohitaji mtu pia kuamini uungu wa Mwenyezi Mungu ambao washirikina wanaujadili sana. Na tunaweza kutaja aya au hadithi tukufu katika sehemu zaidi ya moja kulingana na namna ya kuzitumia kama ushahidi, na kulingana na haja ya kufanya hivyo.
Inapohitajika, tunaweza kutaja baadhi ya nukuu kutoka kwa maimamu wema waliotangulia, ambazo zinafafanua makusudio ya Aya na hadithi, na tunataja tu kile ambacho kinabainisha kauli ya haki bila kutaja fikira potofu au kauli ya mwenye kwenda kinyume na hilo; ili mwanafunzi asipokee fikira hiyo potofu, au kujiingiza katika kujibu kauli za wapinzani kabla ya kumakinika katika elimu kisawa sawa na kuielewa ndani ya moyo wake. Tunatumaini kwamba hili litampa msomaji - Mwenyezi Mungu akipenda - kinga dhidi ya kuteleza katika suala hili, kwa sababu limezungukwa na tofauti za kiitikadi maarufu kama vile masuala ya sifa za Mwenyezi Mungu, Kadari, na mengineyo.
Ibn Abi Zamanin Al-Maliki, Mwenyezi Mungu amrehemu, amesema: (Hakika, nimeshakujulisha kuhusu maneno ya maimamu wa uongofu na wajuzi wakubwa wa elimu kuhusiana na uliyouliza juu yake, na katika mambo mengine yasiyokuwa hayo miongoni mwa yale yanayoulizwa kuhusu misingi ya Sunna ambayo ndani yake watu wa matamanio potofu walikiuka Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtume na Nabii wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Na lau kuwa sio wanavyuoni wakubwa kabisa wanaochukia maneno yao kuandikwa na yasalie katika kitabu, ningekwambia kuhusu kukengeuka kwao na upotofu wao, jambo ambalo lingekuongezea hamu ya kuwakimbia, tunajikinga kwa Mwenyezi Mungu kutokana fitina zao, na Mwenyezi Mungu atulinde sisi na nyinyi kutokana na fitina zenye kupoteza, na atuwezeshe kufikia yale yanayomridhisha katika maneno na matendo, na atulete karibu naye zaidi na zaidi. Usulus-Sunna, cha Ibn Abi Zamanin (309, 310).
Tumeziacha kwa makusudi maana za meneno, na istilahi za falsafa za kisasa ambazo Mwenyezi Mungu hakuziteremshia hoja za wazi.
Tumekifanya kitabu hiki kuwa kwa njia ya milango na sura, kama walivyofanya wale wa mwanzo walioandika katika elimu ya Sheria tukufu, na hatukutumia migawanyiko ya kisasa. Na tumekipanga kulingana na misingi ya imani. Ibn Abil-Izz al-Hanafi alisema: "Na njia bora zaidi ambayo kitabu cha Misingi ya imani kinaweza kupangwa ni kama ilivyokuja katika jibu la Mtume rehema na amani ziwe juu yake kwa Jibril amani imshukie, alipomuuliza kuhusu imani. Akasema: "Ni kumuamini Mwenyezi Mungu na Malaika wake..." Kwa hivyo inafaa kuanza na tauhid, sifa zake Mwenyezi Mungu, na yale yanayofungamana nayo, kisha kuzungumza juu ya Malaika, n.k." (Sharḥ al-ʻAqīda at-Tahāwīyah (2/689)
Tuliweka muhtasari wa kila mlango mwanzoni ambapo tunaorodhesha hapo masuala yote ya mlango huo bila ya ushahidi.
Ama kuhusu kueleza daraja za hadithi, tulifanya hivyo kwa kutumia hadithi sahihi kwa njia ya muhtasari. Tulianza na vitabu sita vya hadithi kulingana na mpangilio wake unaojulikana, kisha tukavipanga kulingana na vifo vya waandishi wake. Na kwa kuwa tulitaka kufupisha kitabu hiki, tumetaja tu mahali ambapo hadithi inapatikana bila kuziongelea hadithi hizo kwa kina, isipokuwa katika sehemu chache tu.
Sifa maalumu za kitabu hiki:
Kuunganisha masuala ya kiitikadi na Kitabu Kitakatifu na Sunna za Mtume zilizosafishwa ili iwe wazi kwa mwanafunzi kuwa masuala haya yamechukuliwa wapi.
Kufanyia Muhtasari masuala makuu ya itikadi yanayohusiana na kila mlango wa itikadi.
Kupupia juu ya kuweka msingi wa itikadi kwa njia fupi iliyokusanya nukta muhimu zote kwa maneno rahisi wakati wa kubainisha na kufafanua masuala ya itikadi, ili hilo lisaidie kuelewa kisawa sawa.
Kitabu hiki kimesalimika na masuala yasiyofaa yanayozungumza kuhusu Mwenyezi Mungu, na ya kifalsafa, na tumerahisisha ibara zake kuwa na maana za karibu mno, na kujiweka mbali na maneno ambayo yalitajwa katika baadhi ya vitabu vya itikadi baada ya kuibuka kwa watu wa matamanio.
Nasi hatudai kwamba tumechunguza masuala yote ya itikadi, lakini tumejaribu kwa kadiri ya uwezo wetu katika hilo, kwa hivyo tunatarajia kutoka kwa kila mmoja aweze kukiboresha kitabu hiki au kukinyoosha, au kuongeza kilichoachwa nje, ili tuweze kufaidisha wengine kwa hayo katika chapa zake zifuatazo. Na linatutosha kwamba tulirejea katika vyanzo vya Ufunuo (Wahyi) wa Mwenyezi Mungu, na tukachambua humo maudhui za elimu tukufu zaidi. Na tumewawekea kitabu hiki wanafunzi huku tukitaja ushahidi juu ya kila suala aya au hadithi au vyote viwili. Tunamuomba Mwenyezi Mungu aifanye kazi hii kuwa ya kuukusudia uso wake mtukufu, na iafikiane na Sunna ya Nabii wake, kipenzi chake, na muaminifu wake juu ya ufunuo wake, yenye kuwanufaisha waja wake, na iwe hoja na shahidi wetu siku tutakayokutana na Mola wetu Mlezi.
Tunamshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu aliyetufanyia wepesi elimu hii, na akatufanya kuitumikia dini yake, na kupanua masuala ya nguzo za kumuamini Mwenyezi Mungu, na kutaja ushahidi wake kutoka katika Kitabu na Sunna.
Na tunamshukuru kila mtu ambaye alitufanyia uzuri, na anayestahili zaidi kushukuriwa miongoni mwa watu ni wazazi wetu. Basi Mwenyezi Mungu wasamehe, uwarehemu, na uwalipe kwa sababu yetu malipo mazuri unayomlipa mzazi kwa sababu ya mwanawe.
Kisha tunawashukuru waheshimiwa ambao walipitia vizuri Kitabu hiki na kutoa maoni na marekebisho yenye baraka, nao ni: Amiri Daktari Su'ud bin Salman bin Muhammad Aal Su'ud, Profesa Mshiriki wa somo la Itikadi (Aqida) katika Chuo Kikuu cha Mfalme Su'ud, na Daktari Sahl bin Rifaa' Al-'Utaibi, Profesa Mshiriki wa somo la Itikadi (Aqida) katika Chuo Kikuu cha Mfalme Su'ud. Na ustadhi daktari Abdullah bin Salih Al-Barrak, ustadhi wa Itikadi katika Chuo Kikuu cha King Saud, na Daktari Abdullah bin Abdulaziz Al-Anqari, ustadhi mshirika wa somo la Itikadi katika Chuo Kikuu cha Mfalme Saud, na tunamuomba Mwenyezi Mungu awalipe kwa sababu yetu na kwa sababu ya elimu na watu wake, malipo mazuri juu ya ushauri wao wa dhati na maoni yaliyo sawa sawa.
Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa viumbe vyote, na rehema na amani za Mwenyezi Mungu na baraka zake ziwe juu ya mbora wa viumbe vyake, na juu ya familia yake, na Maswahaba zake wote.
Makka Al-Mukarrama
Siku ya 8 ya Dhu-Hijja
Mwaka 1438 Hijria
Utangulizi
Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu
Na kwake tunatafuta msaada, na hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, aliye juu, Mkuu.
Sifa zote njema ni zake Mwenyezi Mungu Mtukufu, na ninashuhudia kwamba hakuna mungu mwingine anayestahiki kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika yeyote. Ni wake ufalme, ni zake sifa njema, naye ni Muweza juu ya kila kitu. Na ninashuhudia kwamba Muhammadi ni mja wake na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na asalimike kwa salamu nyingi. Ama baada ya hayo:
Hiki ni kitabu ambacho tunataja ndani yake kile ambacho Muislamu anapaswa kukiamini kutokana na yale yaliyokuja katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna, na tunaweza kutaja baadhi ya maneno ya Maswahaba wa Mtume na wale waliokuja baada yao na wale wa baada ya hao ili kufafanua aya au hadithi, au kuleta kauli inayofafanua maana ya aya fulani au hadithi. Na tumekigawanya katika milango na sura mbalimbali, na tumejizatiti kukifanya kuwa kifupi iwezekanavyo, na kuangazia masuala yanayohitajika tu, na tumeacha kuzama katika maneno waliyozama ndani yake watu wa sasa na pia istilahi ambazo hazikuja katika kitabu cha Mwenyezi Mungu au katika Sunna za Mtume, rehema na amani ziwe juu yake. Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mtukufu anasema akihimiza juu ya kufuata dini yake, na kushikamana na kamba yake, na kufuata mfano wa Mtume wake, rehema za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Na shikamaneni na kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyokuwa nyinyi kwa nyinyi ni maadui, naye akaziunganisha nyoyo zenu; basi kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye akawaokoa kutokana nalo. Namna hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anawabainishia Ishara zake ili mpate kuongoka." [Al-Imran: 103]. Na amesema Mwingi wa baraka, Mtukufu: "Na fuateni yaliyo mazuri zaidi katika yale yaliyoteremshwa kwenu kutoka kwa Mola wenu Mlezi, kabla haijawajia adhabu kwa ghafla, na hali hamtambui." [Az-Zumar: 55].
Kwa hivyo, tunasema -Wabillaahit taufiiq- tunataraji taufiki ya Mwenyezi Mungu:
Kitabu kinachohusu mwanzo wa uumbaji
Muhtasari wa Kitabu
Tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa vitu vyote, na kwamba Mwenyezi Mungu alikuwepo na hakuna chochote kingine kilichokuwepo isipokuwa Yeye, na wala hakuna chochote kilichokuwa kabla yake, na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji, na aliumba maji kabla ya kuumba mbingu na dunia, kisha akaumba mbingu na dunia, na viwili hivyo vilikuwa vimeshikana, kisha akavitenganisha.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ameufanya uumbaji huu kuwa ni ushahidi juu ya umola wake, ambao unalazimu pia kuamini katika uungu wake. Kwa hivyo, Yeye ndiye Muumba wa kweli, na vinginevyo visivyokuwa Yeye vimeumbwa, Mola wetu Mlezi Aliyetakasika na kutukuka. Yeye ndiye Mungu wa kweli, na vyote visivyokuwa Yeye ni viumbe na havistahili kuabudiwa, au kutumainiwa, au kukusudiwa na yeyote yule.
Na tunaamini kwamba Kiti kitukufu cha Enzi (Arshi) ndicho kiumbe kikubwa zaidi kati ya viumbe vya Mwenyezi Mungu.
Na tunaamini kwamba Malaika wamezunguka Kiti cha enzi cha Mwingi wa rehema, na kwamba Mwenyezi Mungu Mwenye baraka nyingi, Mtukufu yuko juu ya Kiti chake cha Enzi, juu ya Mbingu zake, kando na viumbe vyake.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba Kalamu iliyoandika hatima ya kila kitu, na kuwa kuna maandiko mbalimbali ya majaliwa (Makadirio) mbalimbali.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba Kursi (tandiko la kuweka miguu), ambacho ndicho kiumbe kikubwa zaidi baada ya Kiti cha Enzi (Arshi).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba mbingu na dunia na kila kilicho kati ya viwili hivyo katika siku sita za Mwenyezi Mungu, na kwamba Mwenyezi Mungu aliinua mbingu juu bila ya nguzo zozote, na kwamba Mwenyezi Mungu aliumba viumbe hivi vikubwa kwa hekima kubwa ambayo haiwezi kuzungukwa (kwa kuijua vilivyo) na yeyote isipokuwa Yeye tu, na kwamba Mwenyezi Mungu ameumba hivyo kama vilivyo kwa ufundi na ustadi mkubwa.
Na tunaamini kwamba ulimwengu huu pamoja na mbingu zake, dunia yake, milima yake, na kila kitu kilichomo vitakuwa na hali nyingine Siku ya Kiyama.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba jua na mwezi kwa haki, kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu alivifanya viwili hivyo kutii kwa amri yake, na akaumba nyota na sayari kwa ajili ya hekima kubwa, na kwamba nyota na sayari hazinufaishi wala hazidhuru, na haziathiri katika matukio ya mbinguni na duniani, na yeyote anayeamini kwamba zinaathiri zenyewe tu, basi kwa hakika atakuwa amekufuru au amefanya ushirikina.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba Malaika kutokana na Nuru, na akawafanya kutofautiana katika maumbile.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba majini kutokana na ulimi wa moto, na kwamba uumbaji wa majini ulitangulia uumbaji wa Adam, na kwamba mkuu wa Mashetani ni Ibilisi, na yeye ndiye aliyewapoteza wazazi wetu wawili (Adam na Hawa), amani iwe juu yao, mpaka alipowatoa kutoka katika Bustani ya mbinguni.
Na tunaamini kwamba ibilisi alitia kiburi akakataa kumsujudia Adam, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akamkasirikia, akamlaani, na akamfukuza, na majini pia sheria za Mwenyezi Mungu zinawahusu, na kwamba wanawajibu wa kubeba sheria hizo.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaambia Malaika wake kwamba ataweka duniani khalifa (msimamizi) ili aiimarishe kwa ibada. Naye Mtukufu akabainisha kwamba khalifa huyo (msimamizi) ni Adam, na kwamba atamuumba kutokana na mavumbi, na vumbi hii Mwenyezi Mungu akaifanya kuwa udongo, na kisha akamuumba kwa awamu.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kwa mkono wake Mtukufu, akawafanya Malaika wake kumsujudia, na akamuumbia mke kutokana na yeye mwenyewe ili apate utulivu kwake, ambaye ni Hawa, na akawafanya kuishi katika Bustani ya mbinguni, na kisha akawashusha hadi duniani.
Na tunaamini kwamba watu wote ni uzao wa Adam, na Adam ametokana na mavumbi, kwa hivyo hakuna ubora kwa yeyote juu ya yeyote isipokuwa kwa uchaji Mungu.
Na tunashuhudia kwamba Mwenyezi Mungu aliumba watu kwa umbile la asili la kumtambua Yeye.
Na tunaamini kwamba roho ni katika mambo ya Mwenyezi Mungu, na kwamba wanadamu hawajui chochote kuhusu roho hiyo isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu amewajulisha tu, na kwamba roho zimeumbwa na Mwenyezi Mungu.
Na tunaamini kwamba roho zinakufa, na kifo chake ni kutengana na kiwiliwili.
Na tunaamini kwamba kila kitu kinachotembea kwenye Ardhi miongoni mwa wanyama ni umma na ni viumbe kama sisi.
Na tunajua kwamba Mwenyezi Mungu aliumba kila mnyama kutokana na maji, na akaumba kila kitu viwili viwili, na viumbe hawa wote wataangamia, isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu, Mtukufu atakiondolea hilo.
Mlango wa: Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa vitu vyote.
Tunashuhudia kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu. Mwenyezi Mungu, Mola wetu, Mtukufu amesema: "Huyo ndiye Mwenyezi Mungu, Mola wenu Mlezi, hapana mungu isipokuwa Yeye, Muumba wa kila kitu. Basi muabuduni Yeye tu. Naye ni Mtegemewa wa kila kitu." [Al-An'am: 102]. Na amesema Yeye wa Haki Aliyetukuka na wa juu: "Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu." [Az-Zumar: 62] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na Yeye ndiye anayeanzisha uumbaji, kisha ataurudisha mara nyingine. Na jambo hili ni jepesi zaidi kwake." [Ar-Rum: 27].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alikuwako, na hakukuwa na chochote zaidi yake Yeye, na wala hakikuwepo chochote kabla Yake. Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka amesema: "Yeye ndiye wa Mwanzo na ndiye wa Mwisho, naye ndiye wa Dhahiri na wa Siri, naye ndiye Ajuaye zaidi kila kitu." [Al-hadid: 3].
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Ewe Mwenyezi Mungu, Wewe ndiye wa kwanza, na hakuna chochote kabla yako. Na Wewe ndiye wa mwisho, na hakuna chochote baada Yako. Na Wewe ndiye wa dhahiri, na hakuna chochote kilicho juu Yako. Na Wewe ndiye wa ndani, na hakuna chochote chini yako." (Imesimuliwa na Muslim 2713, Abu Daud 5051, At-Tirmidhi 3400), na Ibn Majah 3831)
Na imesimuliwa kutoka kwa Imran bin Huswain, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Wakati mmoja nilikuwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, tazama, alijiwa na kaumu kutoka katika kabila la Banu Tamim na akasema: "Ikubalini bishara njema enyi Banu Tamim." Wakasema: "Umetubashiria bishara njema, basi tupe." Kisha watu fulani kutoka Yemen wakaingia, akasema: "Ikubalini bishara njema enyi watu wa Yemen, kwa maana Banu Tamim hawakuikubali." Wakasema: "Tumeikubali. Tumekujia ili tuifahamu dini yetu, na kukuuliza jambo hili (Uumbaji) ulianza lini?" Akasema: "Mwenyezi Mungu alikuwako, na hakikuwepo kitu kabla yake, na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji, kisha akaumba mbingu na dunia, na akaandika katika Kumbukumbu kila kitu." (Imesimuliwa na Bukhari 7418, na At-Tirmidhi 3951). Na katika riwaya nyingine hadithi hii imekuja kwa tamko la: "Mwenyezi Mungu alikuwako, wala hapakuwa na kitu kingine isipokuwa Yeye, na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji". (Imesimuliwa na Al-Bukhari 3191).
Na tunaamini kwamba kila kitu kinachotembea kwenye Ardhi miongoni mwa wanyama ni umma kama sisi. Amesema Yeye wa Haki Aliyetukuka na wa juu: "Na hakuna mnyama yeyote katika Ardhi, wala ndege anayeruka kwa mbawa zake mbili, isipokuwa ni umma kama nyinyi. Hatukupuuza katika Kitabuni kitu chochote. Kisha kwa Mola wao Mlezi watakusanywa. [Al-An'am: 38]. Na tunajua kwamba Mwenyezi Mungu aliumba kila mnyama kutokana na maji. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na Mwenyezi Mungu ameumba kila kinyama kutokana na maji. Wengine katika wao huenda kwa matumbo yao, na wengine huenda kwa miguu miwili, na wengine huenda kwa miguu minne. Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu." [An-Nur: 45]. Na akafanya kila kitu ni jozi (Pea), akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie." [Dhariyat: 49]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwamba Yeye ndiye aliyeumba jozi, dume na jike." [An-Najm: 45].
Na tunaamini kwamba viumbe hivi, licha ya utofauti na wingi wake, vina uwiano, hakuna hata kimoja kati ya hivyo kinachovuka mipaka yake na kwenda hadi katika mipaka ya kingine, wala hata aina moja juu ya nyingine. Amesema Yeye wa Haki, Mtukufu: "Na Ardhi tumeitandaza na humo tumeweka Milima, na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake." [Al-Hijr: 19].
Na viumbe hawa wote siku moja wataondoka. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Kila kilichoko juu yake kitatoweka * Na atabakia Mwenyewe Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu." (Ar-Rahman: 26-27) Isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu amekiweka mbali na kuzimia ambako viumbe watazimia katika kauli yake Yeye Mtukufu na Mwenye mamlaka makuu: "Na litapulizwa baragumu, wazimie waliomo mbinguni na waliomo katika Ardhi, isipokuwa yule aliyemtaka Mwenyezi Mungu. Kisha litapulizwa mara nyengine. Hapo watainuka wawe wanangojea." [Az-Zumar: 68].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alifanya uumbaji huu kuwa ni ushuhuda juu ya uleaji wake, ambao unalazimu mtu pia kuamini katika uungu wake. Kwa hivyo, wakati mwingine hufanya uumbaji wake viumbe hawa kuwa ni ushahidi juu ya hayo, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye! Lakini madhalimu wamo katika upotovu uliyo dhahiri." [Luqman: 11]. Na wakati mwingine, Yeye hutaja kuwa kiumbe kikubwa zaidi kati ya hivyo - ambacho ni Kiti chake cha Enzi - ni ishara inayoonyesha hilo, kama ilivyo katika kauli yake Yeye wa Haki Mtakatifu: "Mwenyezi Mungu, hapana mungu isipokuwa Yeye, Mola Mlezi wa 'Arshi kuu." [An-Naml: 26], Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: “Ametakasika Mwenyezi Mungu kwa idadi ya viumbe vyake. Ametakasika Mwenyezi Mungu kwa ridhaa ya nafsi yake. Ametakasika Mwenyezi Mungu kwa uzito wa Kiti chake cha Enzi. Ametakasika Mwenyezi Mungu kwa wino wa maneno yake." (Imesimuliwa na Muslim: 2726, An-Nasa'i: 1351/1, Tirmidhi: 3555, na Ibn Majah: 3808). Kwa hivyo, uzito wa Kiti cha Enzi ndio uzito mkubwa zaidi. Na wakati mwingine hufanya viumbe vikubwa kuwa ni ishara juu ya hayo, kama ilivyo katika kauli yake: "Yeye ndiye aliyewaumbia vyote vilivyomo katika Ardhi. Tena akazielekea mbingu, na akazifanya mbingu saba. Naye ndiye Ajuaye zaidi kila kitu." [Al-Baqarah: 29]. Na wakati mwingine anafanya moja ya viumbe hivi kuwa ni ishara juu ya hayo, kama ilivyo katika maneno yake Mtakatifu: "Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu ameteremsha maji kutoka mbinguni, na kwayo tumeyatoa matunda yenye rangi mbali mbali. Na katika milima imo mistari myeupe na myekundu yenye rangi mbali mbali, na myeusi sana." [Fatir: 27].
Na wakati mwingine hufanya kiumbe dhaifu zaidi na mdogo zaidi kuwa ni ishara juu ya hayo, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu haoni haya kutoa mfano hata wa Mbu na ulio wa zaidi yake. Ama wale walioamini, hujua ya kwamba hiyo ni haki iliyotoka kwa Mola wao Mlezi. Lakini wale waliokufuru, husema: Ni nini analokusudia Mwenyezi Mungu kwa mfano huu?" [Al-Baqara: 26]. Yeye ndiye Muumba wa kweli, na chochote kisichokuwa Yeye kimeumbwa. Mola wetu Mlezi ni mwenye baraka nyingi, Mtukufu. Naye ndiye Mola wa kweli, na chochote kisichokuwa Yeye kinalelewa naye, hakistahili kuabudiwa, au kutumainiwa, au kukusudiwa.
Mlango wa kuumbwa kwa Kiti Kikuu cha Enzi (Arshi)
Na tunaamini kwamba Kiti cha Enzi ni kiumbe kikubwa miongoni mwa viumbe vya Mwenyezi Mungu. Bali ndicho kiumbe chake kikubwa zaidi. Na ikiwa Yeye Mkuu anakielezea kwamba ni kikuu, basi hicho - kwa hakika - ni kikuu. Amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Mwenyezi Mungu, hapana mungu isipokuwa Yeye, Mola Mlezi wa 'Arshi kuu." [An-Naml: 26] Na alikielezea kwamba ni kitukufu, amesema Mola Mtukufu: "Mwenye Kiti cha Enzi kitukufu." [Al-Buruuj: 15], Amesema bin Jarir, Mwenyezi Mungu amrehemu, katika tafsiri yake: Wasomaji wa Qur'ani wametofautiana katika kusoma kauli yake: "Al-Majid" (Mtukufu). Kwa hivyo, wasomaji wengi wa Madina, Makka, Basra na baadhi ya watu wa mji wa Kuufa waliisoma wakiifungamanisha na kauli yake: (Mwenye Arshi) wakiifanya kuwa ni katika sifa za Mwenyezi Mungu Mwenye utajo Mtukufu. Na wasomaji wote wa mji wa Kuufa waliisoma kwa kuitilia kasra ili kuifanya iwe ni sifa ya Arshi. Lakini kauli iliyo sahihi katika hilo kwa upande wetu ni kwamba hivyo vyote ni visomo viwili vinavyojulikana, na kwa chochote kile atakachokisoma msomaji, basi yuko sahihi. Jami’ Al-Bayan (24/346). Nacho pamoja na ukuu wake, ni kiumbe kilicho chini na usimamizi wa Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Ni nani Mola Mlezi wa mbingu saba na Mola Mlezi wa 'Arshi Kuu?" [Al-Muminun: 86]. Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: «...Naye akaumba kiti chake cha Enzi juu ya maji." (Imesimuliwa na Tirmidhi: 3109, Ibn Majah: 182, Tayyalisi: 1189, Ahmad: 16188 na Ibn Abi Asim katika As-Sunna: 625). Na kina miguu. Amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Watu watazimia Siku ya Kiyama, kisha mimi nitakuwa wa kwanza kuzinduka, na tazama, nitamuona Musa akiwa ameshika mguu katika miguu ya Kiti cha Enzi." Imesimuliwa na Al-Bukhari (3398), Muslim (2374), na Abu Dawud (4668).
Na kiti hiki cha Enzi kiko juu ya mbingu, na Mwenyezi Mungu yuko juu ya Kiti cha Enzi. Amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika Kiti chake cha Enzi kilivyo juu ya mbingu zake ni kama hivi - na akaashiria kwa kidole chake kama vile anachora kuba juu yake - na hakika, kinatoa sauti ya kuelemewa kwa sababu yake kama vile tandiko linavyotoa sauti ya kuelemewa kwa sababu ya yule aliyepanda juu yake." (Imesimuliwa na Abu Daawud 4726, Othman bin Said Ad-Daarami katika Arradu Alal-Jahmiyyah 24, Ibn Abu 'Asim katika As-Sunna 587, na Ibn Khuzayma katika Tawhid 147). Na katika riwaya, ilikuja hadithi hii hivi: "Hakika Mwenyezi Mungu yuko juu ya Kiti chake cha Enzi, na Kiti chake hicho cha Enzi kiko juu ya mbingu zake." (Imesimuliwa na Abu Daawud: 4726, Othman bin Said Ad-Daarami katika Arradu Alal-Jahmiyyah 24, Ibn Abu 'Asim katika As-Sunna 587, na Ibn Khuzayma katika Tawhid 147).
Na tunaamini kwamba chini ya Kiti cha Enzi kuna hazina za kimungu ambazo Mwenyezi Mungu pekee tu ndiye anayeweza kukadiria kiwango chake. Amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Nami nilipewa Aya hizi za mwisho wa Suratul Baqara kutoka katika hazina iliyo chini ya Kiti cha Enzi, ambayo hakuwahipewa Nabii yeyote kabla yangu". (Imesimuliwa na Muslim 522 bila ya kutaja mahali penye ushahidi, Tayalasi 418, Ibn Abī Shaiba katika Al-Muṣannaf 32306, na Ahmad 23251 na matamshi haya ni yake, na wengineo).
Na katika hadithi ya Abu Dharri, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Aliniamrisha kipenzi changu, rehema na amani ziwe juu yake, mambo saba, na akataja miongoni mwake: "Na akaniamuru niseme kwa wingi: Hakuna uwezo wa nguvu isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu. Kwa maana hayo ni hazina kutoka chini ya Kiti cha Enzi." (Imesimuliwa na Al-Bazzar 3966, Ibn Abī Shaiba katika Al-Muṣannaf 35491, Hannād katika Az-Zuhd 1013, Ahmad katika Al-Musnad 21415 na matamshi haya ni yake, na katika Az-Zuhd 401).
Na tunaamini kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake, atasujudu chini ya kiti cha enzi siku ya Kiyama mpaka aombe ule uombezi mkubwa. Na katika hadithi ndefu ya Uombezi, kumeelezwa kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: “Basi nitaondoka na nifike chini ya kiti cha enzi, kisha nianguke chini nimsujudie Mola wangu Mlezi Mtukufu. Kisha atanifungulia kutoka katika sifa zake na namna ya kumsifu,kitu ambacho hakuwahi kumfungulia yeyote kabla yangu. Kisha patasemwa, "Ewe Muhammad, inua kichwa chako na uombe, utapewa hicho ulichoomba." Kwa hivyo, nitainua kichwa changu, na niseme, "Umma wangu, ewe Mola wangu Mlezi. Umma wangu, ewe Mola wangu Mlezi..." (Imesimuliwa na Al-Bukhari 4712, Muslim 194, Tirmidhi 2434, na Ibn Majah 3307).
Na tunaamini kwamba roho za waliokufa mashahidi zimehifadhiwa katika taa zilizoning'inizwa kwenye kivuli cha kiti cha enzi. Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Wakati ndugu zenu walipopatwa na umauti huko Uhud, Mwenyezi Mungu alifanya roho zao kuwa ndani ya ndege wa kijani kibichi, na wakawa wanaenda kunywa katika mito ya Bustani ya mbinguni, na wanakula katika matunda yake, na wanaenda kutulia katika taa za dhahabu zilizoning'inizwa katika kivuli cha kiti cha enzi..." (Imesimuliwa na Abu Dawud 2520, Ibn Al-Mubarak katika Al-Jihad 62, Ibn Abī Shaiba 19678, na Ahmad 2388).
Na aliambiwa Ibnul-Mubarak: Tutamjuaje Mola wetu Mlezi? Akasema: "Ni kuwa yeye yuko juu ya mbingu ya saba juu ya kiti cha enzi, amejitenga kando na viumbe wake." (Arradu Alal Jahmiyyah cha Ad-Darami uk. 47, Al-Asma wa As-Sifat, Al-Bayhaqi 2/336, Al-Fatwa Al-Hamawiyya Al-Kubra uk. 333, na Sharh At-Tahawiyyah chapa ya Dar As-Salam uk. 219).
Na amesema Imam Ad-Darmi, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka yuko juu ya kiti chake cha enzi, juu ya mbingu zake, na amejitenga na viumbe wake. Kwa hivyo yeyote asiyemjua kwa sifa hizo basi hamjui Mungu wake anayemwabudu, na elimu yake kutoka juu ya Arshi ya kukijua kiumbe chake kilicho mbali zaidi na kilicho karibu zaidi ni moja (haitofautiani), na hakuna kitu kilicho mbali naye, "Wala hapana kinachofichikana kwake hata chenye uzito wa chembe tu, si katika mbingu wala katika ardhi." [Saba': 3]. Ametakasika na ametukuka juu ya yale ambayo wanamuelezea kwayo watu wenye kukanusha sifa zake, kutukuka kukubwa mno." (Arraddu alal-Jahmiyyah uk. 47).
Na tunaamini kwamba kiti cha enzi kimebebwa na Malaika, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wale wanaobeba 'Arshi, na wale wanaoizunguka, wanamsabihi na kumhimidi Mola wao Mlezi, na wanamuamini, na wanawaombea msamaha wale walioamini kwa kusema: Mola wetu Mlezi! Umekienea kila kitu kwa rehema na elimu. Basi wasamehe wale waliotubu na wakaifuata Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu." [Ghafir: 7]. Na amesema Mtukufu: "Na Malaika watakuwa pembezoni mwa mbingu; na wanane juu ya hawa watakuwa wamebeba Kiti cha Enzi cha Mola wako Mlezi." [Al-Haqqa: 17].
Na alieleza Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuhusu baadhi ya sifa za wabebaji wa kiti cha enzi, akasema: "Nimeruhusiwa kuzungumza juu ya Malaika miongoni mwa Malaika wa Mwenyezi Mungu miongoni mwa wale wanaobeba kiti cha enzi. Hakika kati ya ndewe (Nyama ya sikio ya chini) ya sikio lake hadi bega lake ni mwendo wa miaka mia saba". (Imesimuliwa na Abu Daud 4727, Al-Tabrani katika Al-Wusta 1709, Abu al-Sheikh katika Al-'Udhma 476, na Ibn Shahin katika Al-Fawaid 19).
Na tunaamini kwamba Malaika wamezunguka kiti cha enzi cha Mwingi wa rehema, amesema Mola wa Haki: "Na utawaona Malaika wakizunguka pembeni mwa Kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu, wakimtakasa na kumsifu Mola wao Mlezi. Na patahukumiwa baina yao kwa haki na patasemwa: Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote!" [Az-Zumar: 75].
Na kiti cha enzi pamoja na kitabu kilichotajwa katika kauli yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu alipomaliza uumbaji, aliandika katika kitabu chake, nacho kiko kwake juu ya kiti cha enzi: Hakika huruma yangu imeshinda hasira zangu." (Imesimuliwa na Al-Bukhari 3194, Muslim 2751, Tirmidhi 3543, na Ibn Majah 189, 4295). Hivyo viwili ndivyo viumbe vya juu zaidi. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: «... "Mkimuomba Mwenyezi Mungu, basi muombeni Bustani ya mbinguni iitwayo Al-Fidaws. Kwani hakika hiyo ndiyo Bustani ya katikati zaidi, na ya juu zaidi, na juu yake kipo Kiti cha Enzi cha Mwingi wa rehema, na kutoka humo inapasuka mito ya Bustani za mbinguni." (Imesimuliwa na Al-Bukhari 7423).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu yuko juu ya Kiti chake cha Enzi kwa njia inayonasibiana na ukuu wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mola wenu Mlezi ni Mwenyezi Mungu aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Kisha akainuka juu ya Kiti cha Enzi." [Al-A'araf: 54], Na amesema Mola wa Haki: "Ambaye ameziumba mbingu na ardhi, na vilivyo ndani yake kwa siku sita. Kisha akalingana sawa juu ya 'Arshi, Arrahman (Mwingi wa rehema)! Uliza habari zake kwa wamjuaye." [Al-Furqan: 59].
Na aliulizwa Rabia Ar-Raiy kuhusu kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwingi wa rehema yuko juu ya Kiti cha Enzi" [Taha: 5]: Vipi yuko juu yake? Akasema: "Jinsi ya hilo haijulikani, na kuwa juu ni jambo linajulikana akilini, na ni wajibu kwangu mimi na nyinyi tuamini hayo yote." (Al-Asmaa Wasswifaati cha Al-Baihaqi 2/306, na Sherhu- usuulu iitikadi Ahlus-Sunna wal-Jamaa 3/582).
Na mtu mmoja alimjia Malik bin Anas na akasema: Ewe Abu Abdullah, "Mwingi wa Rehema amelingana juu ya Kiti cha Enzi" Amelingana sawa vipi? Akasema: Hatukuwahi kumuona Malik amebadilika kama alivyobadilika kwa maneno yake haya, na akapatwa na jasho jingi, na akaanza kugongagonga kitu, nasi tukasubiri tuone anaamrisha nini kuhusiana naye. Akasema: Kisha Malik akarudi kuwa katika hali yake ya kawaida, na akasema: "Namna alivyo juu haijulikani, na kuwa kwake juu ni jambo linajulikana, na kuamini hilo ni wajibu, na kuuliza yupoje juu ni uzushi, nami ninahofu kwamba huenda ukawa umepotea." Kisha akaamrisha yule bwana akatolewa nje." (Arraddu Alal Jahmiyyah cha Ad-Darami uk. 66, Sharhu usuulu Iitiqaadi Ahlus-Sunna wal-Jama' 3/441, Hilyatul-Awliyaa watwabaqaatul Al-Asfiyaa 6/325, na AI-itiqaadi cha Al-Bayhaqi uk. 116, Sharh As-Sunna cha Al-Baghawi 1/171, na Al-Asmaai Wasswifaati cha Al-Bayhaqi 2/306).
Imam Ahmad alikuwa akisema katika maana ya kuwa juu: "Ni kuinuka na kuwa juu. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu hajaacha kuwa juu kabla ya kuumba kiti chake cha enzi. Yeye yuko juu ya kila kitu. Lakini Mwenyezi Mungu alikichagua kiti cha enzi kwa sababu ndani yake kuna maana inayokwenda kinyume na vitu vingine vyote. Na kiti cha enzi ndicho kiumbe bora zaidi na kilicho juu zaidi. Kwa hivyo Yeye Mtukufu akajisifu mwenyewe kwamba yuko juu ya kiti cha enzi. Na imesimuliwa kutoka kwa 'Abdur-Rahman bin Mahdi kutoka kwa Malik kuwa, "Mwenyezi Mungu Mtukufu yuko juu ya kiti chake cha enzi kitukufu kama alivyojulisha, na kwamba elimu yake iko kila mahali." (Al-Aqiidatu, riwayatu Abii Bakr Al-Khalil uk. 108).
Na umola wa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka juu ya kiti cha enzi ni ushahidi wa kustahiki kwake kuabudiwa na sio yeyote mwingine. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lau wangelikuwamo humo miungu wengine zaidi ya Mwenyezi Mungu, basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeliharibika. Mwenyezi Mungu ametakasika, Mola Mlezi wa 'Arshi (Kiti cha Enzi) mbali na hayo wanayoyazua." [Al-Anbiya: 22] Na amesema Mtukufu: "Sema: Ni nani Mola Mlezi wa mbingu saba na Mola Mlezi wa 'Arshi Kuu?" [Al-Muminun: 86]. Na amesema Mola Mtukufu: "Sema: Lau wangelikuwa pamoja naye miungu mingine kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Kiti cha Enzi." [Al-Israa: 42].
Mlango wa kumbwa maji
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu aliumba maji kabla ya kuumba mbingu na ardhi. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu alikuwako, wala hapakuwepo kitu chochote kabla yake, na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji, kisha akaumba mbingu na ardhi." (Imepokewa na Muslim 2713, Abu Dawud 5051, Tirmidhi 3400, na Ibn Majah 3831) Na Mwenyezi Mungu alifanya kila kitu kilicho hai kutokana na maji. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na tukajaalia kwa maji kila kitu kuwa hai." [Al-Anbiya: 30] Na kwamba Mwenyezi Mungu aliyafanya hayo kuwa miongoni mwa ishara za umola wake na uungu wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "(Mwenyezi Mungu) ambaye amewafanyia hii ardhi kuwa kama tandiko, na mbingu kama paa, na akateremsha maji kutoka mbinguni, na kwayo akatoa matunda yawe riziki zenu. Basi msimfanyizie Mwenyezi Mungu washirika, na hali nyinyi mnajua." [Al-Baqara: 22].
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na katika ardhi vimo vipande vilivyokaribiana, na zipo bustani za mizabibu, na mimea mingine, na mitende yenye kuchipua kwenye shina moja na isiyochipua kwenye shina moja, nayo inatiliwa maji yale yale. Na tunaifanya baadhi yake kuwa bora kuliko mingine katika kula (Ladha). Hakika katika hayo zimo ishara kwa watu wanaotia mambo akilini." [Ar-Ra'd: 4] Na amesema Mtukufu: "Naye ndiye aliyezipeleka bahari mbili, hii ni tamu mno, na hii ni ya chumvi chungu. Na akaweka baina ya bahari mbili hizo kinga na kizuizi kizuiacho* Naye ndiye aliyemuumba mwanadamu kutokana na maji, akamjaalia kuwa na nasaba na ushemeji. Na Mola wako Mlezi ni Muweza." [Al-Furqan: 53, 54] Kwa hivyo, akafanya bahari mbili tofauti kutokana na maji hayo, na akaweka kati ya bahari mbili hizo kinga na kizuizi, ili bahari moja isiingiliane na nyingine, kama vile alivyoumba wanadamu kutokana na maji, na akafanya nasaba na ushemeji kwa wanadamu. Basi ni Mwenye baraka nyingi Mwenyezi Mungu Mbora zaidi wa waumbaji. Na mifano ya aya hizi ni mingi mno.
Kama vile Mwenyezi Mungu alivyoyafanya kuwa ishara juu ya kufufuliwa. Amesema Mtukufu: "Na katika Ishara zake ni kwamba unaiona ardhi nyonge, lakini tunapoiteremshia maji, mara unaiona inataharaki (Inachangamka) na kuumuka. Bila ya shaka yule aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu. Hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu." [Fusswilat: 39].
Na aliyafanya kuwa moja kati ya majeshi yake, na akawanusuru kwayo vipenzi wake. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Alipowafunika kwa usingizi ili uwe ni wa kuwapa amani kutoka kwake, na akawateremshia maji kutoka mbinguni ili kuwasafisha kwayo na kuwaondolea uchafu wa Shetani, na ili kuzipa nguvu nyoyo zenu, na kuifanya imara miguu yenu." [Al-Anfal: 11] Na akawaangusha kwayo maadui zake, amesema Mtukufu: "Basi (Nuhu) akamuomba Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika mimi nimeshindwa, basi ninusuru! * Basi tukaifungua milango ya mbingu kwa maji yanayomiminika * Na tukazipasua ardhi kwa chemchemi, yakakutana maji hayo kwa jambo liliokadiriwa." [Al-Qamar: 10-12] Pamoja na hali nyinginezo ambazo Mwenyezi Mungu alifanya maji kuwa sababu ya kuwasaidia vipenzi wake au kuwaangusha maadui zake.
Mlango wa kuumbwa Kalamu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba kalamu iliyoandika majaliwa (Kadari) zote. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika mwanzo alipoiumba Mwenyezi Mungu kalamu, aliiambia, "Andika." Ikasema, 'Mola Mlezi, niandike nini?' Akasema, "Andika Kadari ya kila kitu mpaka Saa ya Kiyama itakapokuja." (Imesimuliwa na Abu Dawud 4700, Tirmidhi 2155, 3319, At-Tayyalisi 578, Ahmad 22705, 22707, na Ibn Abi Asim katika As-Sunna 115).
Na tunaamini kwamba kalamu ziko aina nyingi. Amesema, Mtume rehema na amani ziwe juu yake - huku akisimulia kuhusu Al-Israa wal-Mi'raj (Safari ya usiku kwenda mbinguni): "Kisha nikapandishwa juu hadi nikainuka juu ya kiwango ambacho niliweza kusikia sauti za kuandika kwa Kalamu." (Imesimuliwa na Bukhari 349, na Muslim 163).
Na imerudiwa katika Qur'ani na Sunna habari kuhusu Malaika kuandika matendo ya waja, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Na hakika bila ya shaka wapo walinzi juu yenu.* Waandishi wenye heshima.* Wanayajua mnayoyatenda." [Al-Infitwar: 10-12].
Na amesema Mtukufu: "Wanapopokea wapokeaji wawili, wanaokaa kuliani na kushotoni.* Hatamki neno isipokuwa karibu yake yupo mwangalizi tayari." [Qaf: 17, 18].
Na amesema Mtukufu: "Na tunapowaonjesha watu rehema baada ya shida waliyoipata, utawaona wana vitimbi dhidi ya Ishara zetu. Sema: Mwenyezi Mungu ni Mwepesi zaidi wa kupanga. Hakika wajumbe wetu wanayaandika mnayoyapanga." [Yunus: 21]
Na amesema Mtukufu: "Au wanadhani kwamba hatusikii siri zao na minong'ono yao? Wapi! Na wajumbe wetu wapo karibu nao, wanayaandika." [Zukhruf: 80].
Na katika vitabu vya hadithi sahihi, imekuja kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake amesema: "Hakuna yeyote miongoni mwenu, wala nafsi yoyote yenye roho, isipokuwa imeandikiwa mahali pake katika Bustani za mbinguni au Motoni, na tena imeshaandikiwa kama itakuwa ya mashakani (Ovu) au katika furaha." (Imesimuliwa na Bukhari 4948, Muslim 2647, Abu Dawud 4694, At-Tirmidhi 2136, 3344, na Ibn Majah 78).
Pia alisema: "Mmoja wenu akiufanya Uislamu wake kuwa mzuri, basi kila tendo zuri atakalofanya litaandikwa kama zuri mara kumi mfano wake hadi mizidisho mia saba. Na kila ovu atakalofanya, litaandikwa kwa mfano wake tu." (Imesimuliwa na Bukhari 42, 7501, Muslim 128, 129, 130, na At-Tirmidhi 3073).
Mlango wa kuumbwa Kursi
Na tunaamini kwamba Kusri ndicho kiumbe kikubwa zaidi baada ya Kiti cha enzi. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema akibainisha ukuu wake" "Kursi yake imetanda mbinguni na duniani." [Al-Baqara: 255].
Na Kursi ipo mbele ya Kiti cha enzi, ambapo ni mahali inapokanyaga miguu. Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, alisema katika tafsiri ya aya hii: "Kursi ni mahali pa kukanyaga miguu miwili, na Kiti cha enzi hakuna anayeweza kupima ukubwa wake." (Imesimuliwa na Darqutni katika Sifa mbalimbali 36 huku imefika kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na mara haikufika kwake (Hadithi Marfu'u na Mauquuf). Na imesimuliwa na Uthman bin Said ad-Daarmi katika kumjibu Bishr Al-Mirrisi 84, 89, Abdullah bin Ahmad katika As-Sunna 586, Ibn Khuzaimah katika Tauhid 154, na Abu Sheikh katika Al-Adhwama: 216, 217). Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hazikuwa Mbingu saba kwa kulinganisha na Kursi isipokuwa ni kama pete iliyoangushwa juu ya ardhi pana mno. Na ubora wa Kiti cha enzi juu ya Kursi ni kama ubora wa ardhi hiyo pana kwa pete hiyo. (Imesimuliwa na Ibn Hibban 361, na katika Al-Majruhin 3/130, na Tabrani katika Al-Kabir 1651, na katika Al-Makarim 1, na Al-Ajurri katika Al-Arba'in 40, na Abu Sheikh katika Al-Adhama 259, na Abu Nu'aim katika Al-Hilya 1/18 na 166 - 168, na Al-Bayhaqi katika Al-Asma uk. 510 - 511, na katika Ash-Shu'ab 4325 na 7668, na Ibn Abd Al-Barr katika Tamhid 9/199). Nayo ni hadithi ndefu, na hadithi yetu hii hapa ni sehemu katika hiyo hadithi ndefu. Na hadithi hii ilikuja kupitia njia nyingi, lakini hizo zote ni dhaifu na sio sahihi, na Al-Aqili alitaja baadhi ya njia hizi na akaashiria kwenye udhaifu wake. Ibn 'Adiy pia alizitaja na kusema, “Hii ni hadithi iliyokataliwa ambayo imesimuliwa kwa njia hii kutoka kwa Ibn Juraij kutoka kwa 'Atwa kutoka kwa 'Ubaid bin Umair kutoka kwa Abu Dharr. Na hadithi hii haina njia za upokezi isipokuwa kutoka kwa simulizi ya Abu Idris Al-Khawlani na Al-Qasim bin Muhammad kutoka kwa Abu Dharr. Na ya tatu ni hadithi ya Ibn Juraij, na hii ndiyo simulizi iliyokataliwa zaidi.” Lakini hadithi hii ni maarufu, na hakuna nyingineyo iliyowahi kusimuliwa huku imefikishwa kwa Mtume, Rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu na amani, kuhusu Kursi, na ndiyo maana tukaitaja licha ya udhaifu wake na kukataliwa kwake.
Pia Al-Baihaqi amesimulia kutoka kwa Al-Abbas bin Muhammad kuwa alisema: Nilimsikia Abu 'Ubaid akisema: Hadithi hizi ambazo ndani yake kumetajwa kwamba: Mola wetu Mlezi alicheka (kwa sababu ya) kukata tamaa kwa waja wake na ukaribu wa ghera yake, na kwamba Jahannamu haitajaa mpaka Mola wako Mlezi aweke mguu wake ndani yake, na kwamba Kursi ni mahali pa kukanyaga miguu miwili, hadithi hizi katika riwaya zake kwetu sisi ni za kweli, na baadhi yao walizisimulia kutoka kwa baadhi yao, isipokuwa tukiulizwa juu ya tafsiri yake, hatuzifasiri, na wala hatukuwahi kumsikia yeyote akizifasiri." (Al-Asmaa Wasswifaati, cha Al-Baihaqi 2/198).
Mlango wa kuumbwa Mbingu na Ardhi
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba mbingu na Ardhi na vyote vilivyo kati yake katika siku sita za kimungu, wala hakuguswa na machofu. Amesema Mola Mtukufu: "Na bila ya shaka Sisi tumeziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina yake katika siku sita; na wala hayakutugusa machofu yoyote." [Qaf: 38] Na amesema Mtukufu: "Je, hao waliokufuru hawakuona kwamba mbingu na ardhi zilikuwa zimeambatana, kisha Sisi tukaziachanisha?" [Al-Anbiya: 30] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Sema: Hakika, hivi nyinyi mnamkufuru yule aliyeumba ardhi katika siku mbili, na mnamfanyia washirika? Huyu ndiye Mola Mlezi wa walimwengu wote.* Na akaweka humo milima juu yake, na akabarikia humo na akakadiria humo chakula chake katika siku nne. Haya ni sawa kabisa kwa wanaouliza.* Kisha akazielekea mbingu, na zilikuwa moshi, akaziambia hizo na ardhi, 'Njooni mlete kwa hiari au kwa nguvu!' Vyote viwili vikasema, 'Tumekuja na tumeleta huku tumetii.* Basi akazifanya mbingu saba kwa siku mbili, na akazipangia kila mbingu mambo yake. Na tukaipamba mbingu ya chini kwa mataa na kwa ulinzi. Hiki ndicho kipimo cha Mwenye Nguvu, Ajuaye zaidi." [Fusswilat: 9-12].
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, ni vigumu zaidi kuwaumba nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliyezijenga! * Akainua kimo chake, na akaitengeneza vizuri. * Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana wake. * Na juu ya hivyo ameitandaza ardhi. * Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake. * Na milima akaisimamisha. * Kafanya hayo yote ili iwe ni starehe kwenu na mifugo yenu." [An-Naziat: 27-33].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliziinua mbingu bila nguzo, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ndiye aliyeziinua mbingu bila ya nguzo mnazoziona, kisha akainuka juu ya 'Arshi, na akafanya jua na mwezi vimtii, kila kimoja kinakwenda kwa kiwango maalumu. Anayaendesha mambo, na anazipambanua Ishara ili mpate kuwa na yakini ya kukutana na Mola wenu Mlezi." [Ar-Ra'd: 2] Na amesema Mtukufu: "Ameziumba mbingu bila ya nguzo mnazoziona; na akaweka katika ardhi milima ili ardhi isiwayumbishe; na akatawanya humo kila namna ya wanyama; na tukateremsha maji kutoka mbinguni, na tukaotesha katika ardhi mimea mizuri ya kila namna." [Luqman: 10].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu anashikilia mbingu na ardhi zisiondoke. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu ndiye anayezuilia mbingu na ardhi zisiondoke. Na zikiondoka, hapana yeyote wa kuzizuia isipokuwa Yeye. Hakika Yeye ni Mstahamilivu, Mwingi wa kusamehe." [Fatwir: 41].
Na tunaamini kwamba Yeye Mtakatifu ndiye anayeshikilia mbingu isiiangukie Ardhi isipokuwa kwa idhini yake. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Na amezishika mbingu zisianguke juu ya ardhi isipokuwa kwa idhini yake." [Al-Hajj: 65].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtakatifu huendesha mambo ya viumbe hawa, anawahifadhi, na wala hayo hayahamuelemei. Anasema Mola wa Haki: "Kursi yake imetanda mbinguni na duniani; na wala haelemewi na kuvilinda hivyo. Na Yeye ndiye aliye juu, na ndiye Mkuu." [Al-Baqara: 255].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba viumbe hivi vikubwa kwa hekima kubwa ambayo haiwezi kuzungukwa kwa kuidhibiti kwa maarifa, na kwamba Mwenyezi Mungu amewaumba sawa sawa vilivyo na kwa ufundi wa ustadi mkubwa. Mwenyezi Mungu amesema: "Na utaiona milima ukaidhania imetulia; nayo inakwenda kama mwendo wa mawingu. Huo ndio ufundi wa Mwenyezi Mungu aliyetengeneza vilivyo kila kitu. Hakika Yeye anazo habari za yote myatendayo." [An-Naml: 88] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina yake kwa mchezo." [Ad-Dukhan: 38] Na alisema Mola wa Haki Mtukufu: "Na ardhi tumeitandaza na humo tumeweka milima, na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake. * Na tumewajaalia humo vitu vya maisha yenu, na ya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku. * Na hakuna chochote isipokuwa hazina ya riziki yake ipo kwetu; na wala hatuiteremshi isipokuwa kwa kipimo maalumu." [Al-Hijr: 19-21].
Na Mwenyezi Mungu alitumia ushahidi wa uumbaji wake mbingu na Ardhi juu ya umola wake, ambao unalazimu mtu pia kuamini uungu wake, akasema Mtukufu: "Au ni nani aliyeziumba mbingu na ardhi, na akawateremshia maji kutoka mbinguni, na kwa hayo maji tukaziotesha bustani zenye kupendeza? Nyinyi hamna uwezo wa kuiotesha miti yake. Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali hao ni watu waliopotoka." [An-Naml: 60] Na amesema Mtukufu: "Na ukiwauliza; Ni nani aliyeumba mbingu na ardhi na akafanya jua na mwezi kutiii amri yake? Bila ya shaka, watasema: Mwenyezi Mungu. Wapi basi wanakogeuziwa wakaacha kumuabudu yeye?" [Al-Ankabut: 61] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Na ukiwauliza: Ni nani anayeteremsha maji kutoka mbinguni, na akaihuisha ardhi baada ya kufa kwake? Bila ya shaka watasema: Ni Mwenyezi Mungu. Sema: Alhamdu Lillahi (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu). Bali wengi katika wao hawafahamu." [Al-Ankabut: 63].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliifanya dunia kuwa ni mahali pa majaribio (Mitihani), Mwenyezi Mungu amesema: "Na Yeye ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji, ili awafanyie mtihani ajulikane ni nani miongoni mwenu mzuri zaidi wa vitendo. Na wewe ukisema: Nyinyi hakika mtafufuliwa baada ya kufa; wale waliokufuru husema: Hayakuwa haya isipokuwa ni uchawi uliyo wazi." [Hud: 7] Na pia aliifanya kuwa thabiti, na mahali pa kuishi, na yenye kukusanya, Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema: "Kutokana nayo (ardhi) tumewaumba, na humo tutawarudisha, na kutoka humo tutawatoa mara nyingine." [Taha: 55] Na amesema Mtukufu: "Kwani hatukuifanya ardhi kuwa yenye kukusanya? * Walio hai na maiti." [Al-Mursalaat: 25, 26].
Na tunaamini kwamba ulimwengu huu mkubwa unamtukuza Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu, Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Zinamtakasa mbingu saba zote na ardhi na vyote vilivyo ndani yake. Na hapana kitu isipokuwa kinamtakasa kwa sifa zake. Lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake. Hakika Yeye ni Mstahamilivu, Mwenye msamaha." [Al-Isra: 44] Na vinanyenyekea kwa sababu ya ukuu wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kisha akazielekea mbingu, na zilikuwa moshi, akaziambia hizo na ardhi: Njooni, kwa hiari au kwa nguvu! Vyote viwili vikasema: Tumekuja nasi ni watiifu." [Fusswilat: 11].
Na ulimwengu huu unahofu kubwa kwa sababu ya waja kumuasi Mola Mlezi Aliyetakasika, Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Zinakaribia mbingu kuchanikachanika kwa hilo, na ardhi kupasuka, na milima kuanguka vipande vipande * Kwa kudai kwao kuwa Arrahmani (Mwingi wa rehema) ana mwana." [Maryam: 90, 91].
Mlango wa kuumbwa Jua na Mwezi
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba jua na mwezi. Amesema Mola wa Haki: "Na Yeye ndiye aliyeumba usiku na mchana na jua na mwezi, vyote katika anga vinaogelea." [Al-Anbiya: 33].
Na tunaamini kwamba jua na mwezi vinakwenda mbio, kama alivyoeleza Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Ajuaye zaidi. * Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka unakuwa kama karara (Tawi la mnazi) kongwe. * Haliwezi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita mchana. Na vyote vinaogelea katika njia zao." [Yasin: 38-40] Basi ni Mwenye baraka nyingi Mwenyezi Mungu mbora wa waumbaji wote.
Na katika rehema zake kwa waja wake ni kwamba alivifanya kutii kwa amri yake; ili yapatikane manufaa ya waja wake. Amesema Mola wa Haki, aliye juu: "Na akalitiisha jua na mwezi kwa manufaa yenu daima na kwa wakati wote, na akautiisha usiku na mchana kwa manufaa yenu." [Ibrahim: 33] Na amesema Mtukufu: Na jua, na mwezi, na nyota, vyote vimetiishwa kwa amri yake." [Al-A'araf: 54]
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu aliumba jua na mwezi kwa ajili ya hekima kubwa kubwa ambazo hakuna anayeweza kuzijua vilivyo. Na katika hekima hizo ni yale yaliyokuja katika kauli yake Mola wa Haki Mtukufu: "Ndiye anayepambazua mwangaza wa asubuhi; na ameufanya usiku kwa mapumziko na utulivu, na jua na mwezi kwenda kwa hesabu. Hayo ndiyo makadirio ya Yule aliyetukuka Mwenye nguvu, Ajuaye zaidi." [Al-An'am: 96] Amesema bin Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie: "Na jua na mwezi huenda kwa hesabu." [Al-An 'am: 96] inamaanisha kwa idadi maalumu ya siku, miezi na miaka. (Tafsir Tabari 11/558). Na Mwenyezi Mungu Mtukufu pia alisema katika kubainisha baadhi ya hekima za kuumbwa jua na mwezi: "Yeye ndiye aliyelifanya jua kuwa ni mwangaza, na mwezi ukawa ni nuru, na akaupimia vituo ili mjue idadi ya miaka na hesabu. Mwenyezi Mungu hakuviumba hivyo isipokuwa kwa Haki. Anazipambanua Ishara kwa watu wanaojua." [Yunus: 5].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alivifanya hivi kuwa miongoni mwa ishara zake kuu zinazoonyesha umola wake unaolazimu mtu pia kuamini uungu wake, Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na ukiwauliza; Ni nani aliyeumba mbingu na ardhi na akafanya jua na mwezi kutii amri yake? Bila ya shaka, watasema: Mwenyezi Mungu. Wapi basi wanakogeuzwa wakaacha kumuabudu mola wao?" [Al-Ankabut: 61] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na katika Ishara zake ni usiku na mchana, na jua na mwezi. Basi msilisujudie jua wala mwezi, bali msujudieni Mwenyezi Mungu aliyeviumba, ikiwa nyinyi mnamuabudu Yeye tu." [Fusswilat: 37]. Na katika vitabu vya hadithi sahihi amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika jua na mwezi ni ishara mbili miongoni mwa ishara za Mwenyezi Mungu. Havipatwi kwa sababu ya kifo cha mtu yeyote, wala uhai wake. Lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu anawahofisha waja wake kwa hivyo." (Imesimuliwa na Bukhari 1048, na An-Nasaai 1459).
Na tunaamini kwamba jua na mwezi vinamsujudia Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote - kama wanavyosujudu viumbe wengineo. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Je, huoni kwamba vinamsujudia Mwenyezi Mungu vilivyo mbinguni na vilivyo katika ardhi, na jua, na mwezi, na nyota, na milima, na miti, na wanyama, na wengi miongoni mwa watu. Na wengi imewastahiki adhabu. Na anayefedheheshwa na Mwenyezi Mungu, hana wa kumheshimisha. Hakika Mwenyezi Mungu hutenda apendayo." [Al-Hajj: 18].
Na tunaamini kwamba jua linasujudu chini ya kiti cha Enzi kila siku, kama alivyoeleza mkweli anayeaminiwa, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Imesimuliwa kutoka kwa Abu Dharri, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimwambia wakati jua lilipozama, "Je, unajua linakwenda wapi?" Nikasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanaojua zaidi." Akasema: "Linakwenda mpaka linasujudu chini ya kiti cha enzi, kisha linaomba ruhusa, na linaruhusiwa. Na umekaribia wakati litasujudu, na halitokubaliwa, na liombe idhini wala halitorusiwa kutoka kwake. Na litaambiwa, "Rudi kutokea huko ulikokujia." Basi litachomozea Magharibi mwake. Na hiyo ndiyo kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Ajuaye zaidi." [Yasin: 38]. (Imepokewa na Bukhari 3199, Muslim 159, Abu Dawud 4002, na Tirmidhi 2186, 3227).
Mlango wa kuumbwa nyota
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba nyota na sayari kwa ajili ya hekima kubwa, ambazo baadhi yake alizitaja Mola wa Haki Mtukufu Aliye juu, katika kauli yake: "Na alama nyengine. Na kwa nyota wao wanajiongoza." [An-Nahl: 16] Amesema Katada, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Na (maana ya) alama: Ni nyota, na kwamba Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka aliziumba nyota hizi kwa ajili ya mambo matatu: Alizifanya kuwa ni mapambo ya mbingu, na akazifanya za kuwaongoza watu, na akazifanya kuwa vimondo vya kuwapigia mashetani. Kwa hivyo yeyote anayeamini kuhusiana nazo yasiyokuwa hayo, basi amepoteza maoni yake, kakosa bahati yake, kapoteza fungu lake, na kajisumbua na asichokijua." (Tafsiri Twabari 17/185).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Musa, Mwenyezi Mungu awe radhi naye kuwa alisema: Tuliswali Magharib pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, kisha tukasema: Kwa nini tusikae mpaka tuswali Ishaa pamoja naye. Akasema: Basi tukaketi, kisha akatoka akatujia na akasema: "Bado mko hapa?" Tukasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tuliswali Magharibi pamoja nawe, kisha tukasema: Kwa nini tusikae hadi tuswali Ishaa pamoja nawe. Akasema: "Mmefanya vizuri" au "Mmefanya lililo sahihi." Anasema: Kisha akainua kichwa chake mbinguni, na alikuwa mara nyingi akiinua kichwa chake mbinguni, na akasema: "Nyota ndiyo amani ya mbingu. Na nyota zitakapoondoka, mbingu itajiwa na kile ilichoahidiwa. Na mimi ndiye amani ya Maswahaba wangu. Na nitakapoondoka, Maswahaba wangu watajiwa na kile walichoahidiwa. Na Maswahaba wangu ndio amani ya umma wangu. Na Maswahaba wangu watakapoondoka, umma wangu utajiwa na kile ulichoahidiwa." (Imepokelewa na Muslim 2531).
Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na kwa hakika tumeupamba Uwingu wa Dunia kwa mataa, na tumeyafanya kuwa vimondo ili kuwapigia mashetani." [Al-Mulk: 5].
Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: Mwanamume mmoja katika Answari (Watu wa Madina) miongoni mwa Masahaba wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, aliniambia kuwa walipokuwa wamekaa usiku pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nyota fulani ilirushwa, na ikang'aa sana. Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akawaambia: "Mlikuwa mkisema nini katika zama za Ujinga kinapotupwa mfano wa hiki?" Wakasema: Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanaojua zaidi, tulikuwa tukisema: Usiku huu mtu mkubwa amezaliwa, na mtu mkubwa amekufa. Basi Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Nyota hizo hakika hazirushwi kwa sababu ya mauti ya mtu yeyote wala kwa sababu ya uhai wake. Lakini Mola wetu Mlezi, Aliyetukuka jina lake, Mwingi wa baraka anapopitisha jambo, Malaika wanaobeba Kiti cha Enzi humtakasa, kisha wanamtakasa wakazi wa mbingu inayofuata mpaka kutakasa huko huwafikia wakazi wa mbingu hii ya karibu, kisha wanasema wale wanaowafuata Malaika wanaobeba Kiti cha Enzi: Mola wenu Mlezi amesema nini? Kwa hivyo, wanawaambia kile alichosema. Akasema: "Kisha wakazi wa kila mbingu wanaulizana hivyo mpaka habari hiyo ifike katika mbingu hii ya chini, kwa hivyo majini wanaisikiliza kwa siri, na wanairusha kwa marafiki zao. Kwa hivyo, wanachosema kama kilivyo, basi ni cha kweli, lakini wao wanatia uongo ndani yake na kuzidisha." (Imepokelewa na Muslim 2229).
Na mashetani walikuwa wakisikiliza kwa siri, lakini wakati Mtume wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, alipotumwa kuwa Nabii, wakazuiwa kukaa katika makao yao ya kusikiliza kwa siri. Mola Mtukufu amesema juu ya hilo: "Na hakika tulikuwa tukikaa humo katika baadhi ya makao ili kusikiliza; lakini sasa anayetaka kusikiliza, atakuta kimondo kinamvizia!" [Al-Jinn: 9] Na amesema Mtukufu: "Hakika Sisi tumeipamba mbingu ya karibu kwa pambo la nyota * Na ulinzi dhidi ya kila shetani muasi * Wasiweze kuwasikiliza viumbe watukufu. Na wanafukuzwa huko kila upande * Wakifurushwa, na wanayo adhabu ya kudumu * Isipokuwa anayenyakua kitu kidogo, na mara humfwatia kimondo kinacho ng'aa." [As-Swaffat: 6-10].
Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: "Majini walikuwa wakipanda mbinguni wakisikiliza Ufunuo, na wanapokwisha sikia neno, wanaongeza humo maneno tisa. Ama neno walilolisikia, hilo linakuwa ni la kweli. Na ama yale waliyoongeza ndani yake, hayo yanakuwa batili. Na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie, alipopewa unabii, wakazuiwa kukaa katika mahali pao pa kusikilizia. Kwa hivyo wakamuambia hilo Ibilisi, na hawakuwa wakitupiwa nyota kabla ya hapo. Basi Ibilisi akawaambia: Hili halikuwa hivyo isipokuwa kwa sababu ya jambo lililotokea katika ardhi. Basi akatuma majeshi yake, wakamkuta Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesimama anaswali kati ya milima miwili - huko Makka - basi wakarudi kwa Ibilisi na wakamjulisha hilo, akasema: "Hili ndilo tukio lililotokea katika ardhi." (Imepokelewa na Tirmidhi 3324, Ahmad 2482, An-Nasai katika Al-Kubra 11562, na Abu Ya'la 2502).
Na tunaamini kwamba nyota na sayari hazinufaishi wala kudhuru, wala haziathiri katika matukio ya mbinguni na duniani, na mwenye kuamini kwamba zinaathiri zenyewe tu, basi atakuwa amekufuru au amefanya shiriki. Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye kuwa alisema: Watu walinyeshewa na mvua katika za Mtume Muhammad, basi Mtume, rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Wamefikiwa asubuhi watu fulani huku ni wenye shukrani, na baadhi yao hali ya kuwa wamekufuru." Wakasema: 'Hii ni rehema ya Mwenyezi Mungu.' Na baadhi yao wakasema: 'Hakika nyota fulani na fulani imesema ukweli.' Akasema: Basi aya hii ikateremka: "Basi ninaapa kwa maanguko ya nyota." [Al-Waqi'a: 75] mpaka akafika "Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu mnafanya kuwa mnakadhibisha?" [Al-Waqia: 82] (Imepokelewa na Muslim 73).
Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Ninachowahofia zaidi umma wangu katika nyakati zake za mwisho ni kuamini nyota, na kupinga kadari, na udhalimu wa viongozi." (Imepokewa na Ar-Rawyani 1245, na Twabarani katika Al-Kabir 8113).
Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikataza kutazama nyota (ili kujua ghaibu) Alisema: "Atakayechukua sehemu katika elimu ya nyota, atakuwa kachukua sehemu ya uchawi, itaongezeka kila anapoongeza kuichukuwa elimu hiyo." (Imepokelewa na Abu Daud 3905, Ibn Majah 3726, Ibn Abī Shayba 26159, Ahmad 2000, na 'Abd ibn Humayd 714).
Hairuhusiwi kujifunza elimu ya nyota isipokuwa kwa kiasi cha kuongozwa nazo katika nchi kavu au baharini, kwa sababu kujifunza elimu hiyo inamfanya mtu kujiingiza katika ukuhani. Imenukuliwa kutoka kwa Saidi ibn Jubair alisema: “Mwanaume mmoja alikuja kwa Abdullah bin Abbas, akasema: "Ewe Abu Abbas, niusie." Akasema: Ninakuusia umche Mwenyezi Mungu, na jiepushe na kuwataja Maswahaba wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kwa ubaya. Kwani wewe kwa hakika haujui ni nini walikitanguliza miongoni mwa wema. Na jiepushe na mambo ya kutazamia nyota isipokuwa tu kwa ajili ya kuongozwa nazo katika nchi kavu au baharini, kwani hizo humfanya mtu kujiingiza katika ukuhani. Na jiepushe na kukaa pamoja na wale wanaokadhibisha Kadari ya Mwenyezi Mungu. Na yeyote anayependa dua yake ijibiwe, na matendo yake yatakaswe na yakubalike kutoka kwake, basi na awe mkweli katika mazungumzo yake, na atekeleze amana yake, na kifua chake kiwe safi kwa Waislamu." (Imepokewa na Ibn Battwa katika Al-Ibana 1987).
Mlango wa kuumbwa Malaika
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaumba Malaika kwa nuru. Imesimuliwa katika hadithi sahihi kutoka kwa 'Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, amesema: "Malaika waliumbwa kutokana na nuru, na majini waliumbwa kutokana na ulimi wa moto, na Adam aliumbwa kutokana na kile mlichoelezwa." (Imesimuliwa na Muslim 2996).
Na Mwenyezi Mungu aliwafanya Malaika kuwa tofauti katika maumbile, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: “Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Muumba wa mbingu na ardhi, aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa, mbili-mbili, na tatu- tatu, na nne-nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.” [Faatir: 1].
Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alieleza kwamba alimuona Jibrili, na kwamba alikuwa na mbawa mia sita; na alikuwa na umbile kubwa sana; Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Ishaq Ash-Shaibani kuwa alisema: Nilimuuliza Zarr bin Hubeishi kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Akawa ni kama baina ya pinde mbili, au karibu zaidi. Basi (Mwenyezi Mungu) akamfunulia mja wake kile alichomfunulia." [An-Najm: 9,10] Akasema: Ibn Mas'ud alitusimulia kuwa, "(Mtume) alimuona Jibril akiwa na mbawa mia sita." (Imesimuliwa na Bukhari 3232, Muslim 174, na Tirmidhi 3277). Na imesimuliwa kutoka kwa 'Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: "Yeyote anayedai kwamba Muhammad alimuona Mola wake Mlezi, basi hakika atakuwa amesema jambo kubwa mno. Lakini alimuona Jibril hali ya kuwa yuko katika umbile lake, na umbile lake hilo kubwa lilikuwa limeziba vilivyo katikati ya upeo wa macho." (Imesimuliwa na Bukhari 3234, Muslim 177, na Tirmidhi 3068).
Tutaelezea zaidi juu ya hadithi inayohusiana na Malaika katika Kitabu cha kuamini Malaika, Mwenyezi Mungu akipenda, na hapa nitafupisha mazungumzo juu ya kuumbwa kwao tu.
Mlango wa kuumbwa majini na mashetani
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba majini kutokana na ulimi wa moto. Mola wa Hakika Mtukufu anasema: "Na majini tuliwaumba kabla, kwa moto mkali." [Al-Hijr: 27], Pia alisema: "Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto." [Ar-Rahman: 15] Na amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Malaika waliumbwa kutokana na nuru, na majini waliumbwa kutokana na ulimi wa moto, na Adam aliumbwa kutokana na kile mlichoelezwa." (Imesimuliwa na Muslim 2996).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba majini na wanadamu ili wamwabudu. Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka amesema: "Nami sikuwaumba majini na watu isipokuwa kwamba waniabudu Mimi." [Dhariyat: 56]. Na majini pia wanatumiwa waonyaji miongoni mwao, wala hawatumiwi Mitume miongoni mwao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na wakati tulipowaleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur'ani. Basi walipoihudhuria, walisema: Sikilizeni! Na ilipokwishasomwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya." [Al-Ahqaf: 29]. Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, alisema: "Mitume ni kutoka kwa wanadamu, na waonyaji ni kutoka miongoni mwa majini." (Tafsir Ibn Kathir 3/340).
Ama kauli ya Mwenyezi Mungu: "Enyi makundi ya majini na watu! Je, hawakuwajia Mitume kutokana na nyinyi wenyewe wakiwabainishia Aya zangu." Maana yake ni nyinyi kwa ujumla na si nyinyi nyote (mlijiwa na Mitume), kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Na akaufanya mwezi ndani ya viwili hivyo uwe nuru." Na kauli yake: "Lakini walimkadhibisha na wakamchinja Ngamia." japokuwa aliyemchinja na mtu mmoja tu miongoni mwao.
Na tunaamini kuwa uumbaji wa majini ulitangulia uumbaji wa Adam, na ndiyo maana akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na majini tuliwaumba kabla, kwa moto mkali." [Al-Hijr: 27] Na mkuu wa mashetani ni Ibilisi - Mwenyezi Mungu alitulinde kutokana naye - Mwenyezi Mungu alimuumba kutokana na moto kama alivyowaumba majini na mashetani wengineo, amesema Mtukufu akieleza kuhusu Ibilisi kwamba alisema: "Mimi ni bora kuliko yeye. Umeniumba kwa moto, naye umemuumba kwa udongo." [Al-A'araf: 12] Na kwamba Ibilisi alikuwa miongoni mwa majini, amesema Mtukufu: "Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam! Walimsjudia isipokuwa Ibilisi. Yeye alikuwa miongoni mwa majini, na akavunja amri ya Mola wake Mlezi." [Al-Kahf: 50].
Na Ibilisi ndiye aliyewapoteza wazazi wetu wawili Adam na Hawa, amani iwe juu yao, mpaka alipowatoa katika Bustani ya mbinguni, ambapo aliwatia wasiwasi, na akawaapia kuwa yeye hakika ni miongoni mwa washauri wazuri, kwa hivyo akawaonyesha kwa hadaa, nao wakala matunda ya mti huo, anasema Mola wa Haki: "Na wewe, Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani hii ya mbinguni, na kuleni humo mpendapo. Wala msiukaribie mti huu, mkawa katika wale waliodhulumu (nafsi zao) * Basi Shetani akawatia wasiwasi ili kuwafichulia tupu zao walizofichiwa, na akasema: Mola wenu Mlezi hakuwakataza mti huu isipokuwa msije mkawa Malaika, au msije mkawa katika wanaoishi milele * Naye akawaapia: Kwa yakini mimi ni miongoni wa wanaowashauri. * Basi akawateka kwa hadaa. Na walipouonja mti ule, tupu zao zikafichuka na wakaanza kujibandika majani ya Bustanini. Mola wao Mlezi akawaita: Je, sikuwakataza mti huo, na kukwambieni ya kuwa hakika Shetani ni adui yenu wa dhahiri? * Wakasema: Mola wetu Mlezi! Tumejidhulumu nafsi zetu, na kama hutotusamehe na kuturehemu, hakika tutakuwa miongoni mwa wenye kuhasirika." [Al-A'araf: 19-23].
Na tunaamini kwamba Shetani alitakabari akakataa kusujudu, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akamkasirikia, akamlaani, na akamfukuza kutoka katika Bustani ya milele ya mbinguni, na kwamba alimuomba Mwenyezi Mungu ampe muhula hadi Siku ya Kiyama; kwa hivyo Mwenyezi Mungu akampa muhula, na kwamba aliapa kwa utukufu wa Mwenyezi Mungu kwamba lazima atawapotosha wanadamu wote isipokuwa waja wateule wa Mwenyezi Mungu, amesema Mola wa Haki akieleza juu ya vitimbi vyake hivi: "Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitaumba mtu kutokana na udongo. * Na nitakapomkamilisha na kumpulizia roho inayotokana nami, basi muangukieni msujudu kwa kumtii * Basi Malaika wakasujudu wakatii wote pamoja * Isipokuwa Ibilisi; alijivuna na akawa katika makafiri * Mwenyezi Mungu akamwambia: Ewe Ibilisi! Kipi kilichokuzuia kusujudu kumtii yule niliyemuumba kwa mikono yangu? Je, umejiona mkubwa, au umekuwa katika wakuu kweli? * Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye. Umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo * Akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe umefukuziliwa mbali * Na hakika laana yangu itakuwa juu yako mpaka Siku ya Malipo * Akasema: Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watakayofufuliwa viumbe * Mwenyezi Mungu akasema: Basi umekwisha kuwa miongoni mwa waliopewa muhula * Mpaka siku ya wakati maalumu * Akasema (Ibilisi): Ninaapa kwa utukufu wako, bila ya shaka nitawapoteza wote * Isipokuwa wale waja wako miongoni mwao walioteuliwa." [Swad: 71-83]. Ibilisi akasema kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza kuhusu yeye: Akasema: Kwa kuwa umenipotosha, basi hakika nitawakalia katika njia yako iliyonyooka * Kisha nitawazukia mbele yao na nyuma yao na kuliani kwao na kushotoni kwao. Wala hutawakuta wengi wao ni wenye shukrani." [Al-A'araf: 16, 17].
Na majini pia yanawahusu matamko ya sheria ya Mwenyezi Mungu na wanawajibika kisheria, na wana uwezo wa kusikia Ufunuo wa Mwenyezi Mungu, kuuelewa kutoka kwa Mitume na waonyaji; na ndiyo maana walisema waliposikia Qur'ani, kama alivyoeleza Mwenyezi Mungu kuhusu wao: "Na wakati tulipowaleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur'ani. Basi walipoihudhuria, walisema: Sikilizeni! Na ilipokwishasomwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya * Wakasema: Enyi Watu wetu! Hakika sisi tumesikia Kitabu kilichoteremshwa baada ya Musa, kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na kinachoongoza kwenye Haki na kwenye njia iliyonyooka." [Al-Ahqaf: 29, 30].
Na tunajua kwamba majini wako miongoni mwao wema, na baadhi yao hawako hivyo. Kwa hivyo, mwenye kuamini miongoni mwao, basi maishio yake ni katika Bustani za mbinguni. Na mwenye kukufuru miongoni mwao, basi maishio yake ni Motoni, amesema Mola wa Haki: "Na hakika katika sisi wamo walio wema, na wengine wetu ni kinyume na hivyo. Tumekuwa njia mbali mbali." [Al-Jin: 11], Kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema: "Na hakika wamo katika sisi Waislamu, na wamo kati yetu wanaoacha haki. Basi wale waliosilimu, hao ndio waliotafuta uongofu * Na ama wanaoacha haki, hao watakuwa kuni za Jahannamu." [Al-Jin: 14, 15].
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza namna Malaika watakavyowadhalilisha waovu miongoni mwa watu na majini Siku ya Kiyama: "Enyi makundi ya majini na watu! Je, hawakuwajia Mitume kutokana na nyinyi wenyewe wakiwabainishia Aya zangu, na wakiwaonya mkutano wa Siku yenu hii." [Al-An'am: 130] Na Mwenyezi Mungu Mtukufu pia alisema: "Mwenyezi Mungu atasema: Ingieni Motoni pamoja na umma zilizopita kabla yenu za majini na watu." [Al-A'araf: 38].
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alibainisha kuwa sababu ya wao kuingia Motoni ni kwamba hawakusikia uongofu kusikia kwa kukubali, Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na tumeiumbia Jahannamu majini wengi na watu. Wana nyoyo, lakini hawafahamu kwazo. Na wana macho, lakini hawaoni kwayo. Na wana masikio, lakini hawasikii kwayo." [Al-A'araf: 179], Aya hii ilionyesha kwamba majini wana mioyo, masikio, na macho. Na mashetani wana sauti za kuchochea viumbe, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika: "Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu." [Al-Al-Israa: 64].
Na Mwenyezi Mungu alikwishawaaidhi wanadamu ili Shetani asiwahadae kama alivyowahadaa wazazi wao wawili, Mola Mtukufu akasema: "Enyi wanadamu! Asije Shetani kuwafitini kama alivyowatoa wazazi wenu katika Bustani za mbinguni, akawavua nguo zao kuwaonyesha tupu zao. Hakika yeye na kabila yake wanawaona, na nyinyi hamuwaoni. Hakika Sisi tumewafanya Mashetani kuwa ni marafiki wa wale wasioamini." [Al-A'araf: 27].
Na tunaamini kwamba Shetani - pamoja na kujua kwamba hawezi kuwapoteza waja wateule wa Mwenyezi Mungu - anajaribu yeye na majeshi yake kuwashawishi na kuwaharibia ibada zao, Mola Mtukufu anasema: "Na vivyo hivyo tumemfanyia kila Nabii maadui mashetani wa kibinadamu, na kijini, wakifundishana wao kwa wao maneno ya kupamba-pamba, kwa udanganyifu. Na angelitaka Mola wako Mlezi, wasingelifanya hayo. Basi waache na wanayoyazua." [Al-An'am: 112]. Na imekuja katika hadithi kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika Ifriti mmoja miongoni mwa majini alinijia jana - au neno kama hilo - ili kunikatia Swala, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akaniwezesha kumdhibiti, nilitaka kumfunga kwenye nguzo miongoni mwa nguzo za msikiti ili mkifika asubuhi mumuone nyote, lakini nikakumbuka maneno ya ndugu yangu Suleiman: "Mola wangu Mlezi! Nipe ufalme ambao hapasi kuwa nao yeyote baada yangu.'" Rauhu akasema: "Kwa hivyo, akamrudisha akiwa ameambulia patupu." (Imesimuliwa na Bukhari 461, na Muslim 541). Na imesimuliwa na Ibn Masud, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Hakuna yeyote miongoni mwenu isipokuwa amewekewa mwenza miongoni mwa majini. Wakasema, "Hata wewe, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema, "Hata mimi, lakini Mwenyezi Mungu alinisaidia akasilimu. Kwa hivyo, haniamrishi isipokuwa heri." (Imesimuliwa na Muslim 2814).
Na imesimuliwa kutoka kwa Sabrah bin Abi Fakiha, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa amesema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akisema: "Hakika Shetani amemkalia mwanadamu katika njia zake. Amemkalia katika njia ya Uislamu. Akamwambia, "Unasilimu ndiyo uiache dini yako, na dini ya baba zako, na dini ya baba zako, na dini ya babu zako. "Basi akamuasi na akasilimu. Kisha akamkalia kwenye njia ya Hijra (kuhama), kwa hiyo akasema, "Unahama ndiyo uache Ardhi yako na mbingu yako. Na hakika mfano wa mwenye kuhama ni kama farasi aliyefungwa kwenye kamba." Lakini akamuasi na akahama. Kisha akamkalia kwenye njia ya Jihadi, na akamwambia, "Unafanya Jihadi? Hilo ni kupambana na nafsi na mali. Utapigana, uuawe na mke wako ataolewa na wengine. " Lakini akamuasi na akafanya Jihadi. Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Kwa hivyo, mwenye kufanya hivyo, ni haki juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kumuingiza katika Bustani ya mbinguni. Na mwenye kuuawa, basi itakuwa haki juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kumuingiza Bustani ya mbinguni. Na akizama, itakuwa haki juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kumuingiza katika Bustani ya mbinguni, au ikiwa ataumizwa na mnyama aliyempanda, itakuwa haki juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kumuingiza katika Bustani ya mbinguni." (Imesimuliwa na Al-Nasai 3134 na katika Al-Kubra 4327, Ibn Abī Shayba 19675, Ahmad 15958, na Ibn Habban 4593).
Na ikiwa muovu huyu hakati tamaa ya kutafuta mamlaka juu ya Manabii, amani iwe juu yao, basi kwa wengineo ndio haki zaidi awafanyie hivyo. Imesimuliwa kutoka kwa Abul 'Ala kwamba 'Othman bin Abil-'Aas, Mwenyezi Mungu amridhie, alimjia Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika shetani amezuia baina yangu na Swala zangu na kisomo changu; ananichanganya katika hayo. Kwa hivyo, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Huyo ni shetani anayeitwa Khinzab. Kwa hivyo, unapomhisi, basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu kutokana naye, na tema mate vitonetone kushoto kwako mara tatu. Akasema: Kwa hivyo, nikafanya hivyo, na Mwenyezi Mungu akamuweka mbali na mimi." (Imesimuliwa na Muslim 2203).
Na katika Sahihi Bukhari, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Hakika shetani hupita ndani ya mwanadamu kwa kupitia mapito ya damu." (Imesimuliwa na Bukhari 2038, 7171). Na Ibn Battah, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango wenye maana hii katika kitabu chake "Al-Ibanah", na akasema: "Mlango wa kuamini kwamba Shetani ni kiumbe mwenye mamlaka juu ya wanadamu, anakwenda ndani yao kama vile damu inavyokwenda, isipokuwa kwa yule ambaye Mwenyezi Mungu alimlinda kutokana naye. Na mwenye kukataa hilo, basi yeye ni katika makundi yatakayoangamia." (Al-Ibana Al-Kubra, cha Ibn Batta 4/61).
Na tunajua kwamba mwanadamu anajiwa na Malaika, na pia anajiwa na Shetani. Na Mtume wetu rehema na amani ziwe juu yake, alitubainishia jinsi ya kujikinga kutokana na mipenyezo ya kishetani inayotujia. Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Hakika Shetani ana athari kwa mwanadamu, na Malaika pia ana athari kwake. Ama athari ya shetani, ni kwa kumzoesha uovu na kukadhibisha haki. Na ama athari ya Malaika, yeye humzoesha kufanya heri na kusadikisha haki. Kwa hivyo, mwenye kuhisi hivyo, basi na ajue kwamba hilo limetoka kwa Mwenyezi Mungu, kwa hivyo na amshukuru Mwenyezi Mungu. Na mwenye kuhisi lile lingine, basi na ajilinde kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shetani aliyelaaniwa, kisha akasoma: "Shetani anakutieni hofu ya ufakiri na anakuamrisheni mambo machafu." [Al-Baqara: 268] (Imesimuliwa na Tirmidhi 2988, Ibn Al-Mubarak katika Az-Zuhd 1435, na Ahmad katika Az-Zuhd 854, na Abu Dawud katika Az-Zuhd 164).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu huwalinda waja wake waumini dhidi ya hila za mashetani maadamu wanaomba msamaha. Katika "Al-Musnad" kuna kwamba: "Hakika Ibilisi alisema: Ninaapa kwa nguvu zako, ewe Mola Mlezi, sitaacha kuwahadaa waja wako, maadamu roho zao bado ziko katika miili yao. Mola Mlezi akasema: Ninaapa kwa nguvu zangu na utukufu wangu, sitaacha kuwasamehe maadamu wananiomba msamaha." (Imesimuliwa na Ahmad 11237, na Abdul bin Humaid 932, na Abu Ya'la 1273, 1399, na Tabarani katika Al-Wusta 8788, na katika Dua 1779).
Na tunajua kwamba Shetani anaweza kuchukua sura ya mwanadamu au sura yoyote ile ambayo Mwenyezi Mungu anamruhusu. Katika "Sahihi Bukhari" kutoka kwa Abu Hurairah, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu , rehema na amani zimshukie, alinikabidhi kusimamia Zaka ya Ramadhani, kwa hivyo akanijia mwenye kunijia na akaanza kuchota chakula, nikamkamata. Nikasema: Nitakupeleka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie - kisha akataja kisa chote - na akasema: "Unapoenda kwenye malazi yako, soma Ayatul-Kursi, kwa maana, hautaacha kuwa na mlinzi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, wala hakuna shetani atakayekukaribia mpaka ufike asubuhi.' Mtume, rehema na amani zimshukie, akasema: "Amekwambia ukweli, ilhali yeye ni muongo mno. Huyo ni shetani." (Imesimuliwa na Bukhari 3275, 5010, bila ya kuifikisha kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na ikitoka kwa sheikh wake 'Othman bin Al-Haitham katika sehemu mbili.)
Na watu zama za Ujinga - kwa sababu ya ujinga wao mwingi - walikuwa wakitafuta kimbilio kwa mabwana wa majini, kwa hivyo hilo likawa linawazidishia hofu na dhambi, Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza juu ya hilo: "Na hakika walikuwako wanaume katika watu waliokuwa wakitafuta kujikinga kwa wanaume wa kijini; kwa hivyo wakawazidishia madhambi." [Al-Jin: 6].
Na tunaamini kwamba wale wanoabudu masanamu, hao wanaabudu majini tu. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza juu ya uhakika wa miungu yao hiyo: "Na siku atakayowakusanya wote, kisha atawaambia Malaika: Je, hawa walikuwa wakikuabudu nyinyi? * Watasema: Sub-haanaka (Umetakasika). Wewe ndiye kipenzi chetu si hao. Bali wao walikuwa wakiwaabudu majini; wengi wao wakiwaamini hao." [Saba': 40, 41].
Na tunajua kwamba Shetani humhadaa mwanadamu ili akufuru, kisha hukimbia akamwacha katika dunia hii, kama Mwenyezi Mungu Mtukfu alivyosema juu yake: "Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: Kufuru. Na alipokufuru, akamwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi ninamhofu Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote." [Al-Hashr: 16] Na kama anavyomhadaa ili akufuru, pia humhadaa afanye uchawi, na kumfundisha uchawi huo. Amesema Mola wa Haki juu ya hilo: "Bali mashetani ndio waliokufuru, wakiwafundisha watu uchawi." [Al-Baqarah: 102].
Na tunajua kwamba shetani atawaacha vipenzi wake huko Akhera, na atawalaumu kwa kumfuata. Amesema Mola wa Haki akijulisha juu ya Shetani kwamba atasimama katika Moto wa Jahannam akiwaambia: "Na Shetani atasema itakapokatwa hukumu: Hakika Mwenyezi Mungu aliwaahidi ahadi ya kweli. Nami naliwaahidi; lakini sikuwatimizia. Na sikuwa na mamlaka yoyote juu yenu, isipokuwa kwamba niliwaita tu, nanyi mkaniitikia. Basi msinilaumu mimi, bali jilaumuni wenyewe. Mimi siwezi kuwa mtetezi wenu, wala nyinyi hamuwezi kuwa watetezi wangu. Hakika mimi nilikataa tangu zamani kunishirikisha na Mwenyezi Mungu. Hakika madhalimu watakuwa na adhabu chungu." [Ibrahim: 22].
Mlango wa kuumbwa mwanadamu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaambia Malaika wake kwamba atamuweka duniani khalifa (msimamizi) ili aiimarishe kwa ibada, amesema Mtukufu: "Na pale Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitamweka katika ardhi Khalifa (mtawala). Wakasema: Utaweka humo atakayefanya uharibifu na kumwaga damu nyingi, ilhali sisi tunakutakasa kwa sifa zako na tunakutaja kwa utakatifu wako? Akasema: Hakika Mimi ninayajua msiyoyajua." [Al-Baqarah: 30] Na Mola wa Haki akabainisha kwamba atamuumba Adam kwa udongo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika mfano wa Isa kwa Mwenyezi Mungu ni kama mfano wa Adam; alimuumba kwa udongo kisha akamwambia: Kuwa! Basi akawa." Na amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu alimuumba Adam kwa mshiko wa mkono aliouchukua kutoka katika ardhi yote, kwa hivyo wanadamu wakawa wameumbwa kulingana na namna sehemu mbalimbali za ardhi zilivyo. Wakawa miongoni mwao weupe, wekundu, weusi, na kati ya hizo, na waovu, wema, wepesi, wenye huzuni, na kati hayo." (Imesimuliwa na Abu Daud 4693, na Tirmidhi 2955, na Abdul Razzaq katika Tafsir 41, na Ahmad 19582, na Al-Bazar 3025, 3026). Na vumbi hilo Mwenyezi Mungu alilifanya kuwa udongo, kisha akaliumba kwa awamu, amesema Mola wa Haki: "Na hakika tumemuumba mwanadamu kutokana na asili ya udongo * Na majini tuliwaumba kabla, kwa moto mkali * Na Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitamuumba mtu kwa udongo unaotoa sauti, unaotokana na matope yaliyotiwa sura * Basi nitakapomkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia * Basi Malaika wote pamoja walimsujudia." [Al-Hijr: 26-30] Na amesema Mtukufu: "Na kwa yakini tumemuumba mwanadamu kutokana na asili ya udongo". [Muminun: 12]. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Hebu waulize: Je, wao ni wenye umbo gumu zaidi au hao wengine tuliowaumba. Hakika Sisi tuliwaumba wao kwa udongo unaonata." [As-Saffat: 11].
Na amesema Imam Ahmad, Mwenyezi Mungu amrehemu - baada ya kuzitaja Aya ambazo ndani yake kunatajwa kuumbwa kwa Adam, amani imshukie: "Tunasema: Huu ndio mwanzo wa kuumbwa kwa Adamu. Mwenyezi Mungu alimuumba mara ya kwanza kutoka katika mavumbi, kisha kutokana na udongo: mwekundu, mweusi, mweupe, na kutokana udongo mzuri na wa chumvi. Na ndiyo maana, uzao wake kuna mzuri na mbaya, mweusi, mwekundu, na mweupe. Kisha akayafanya mavumbi hayo kuwa chepe kisha yakawa udongo. Na hayo ndiyo kauli yake: "Kutoka katika udongo". Na pindi udongo huo uliposhikana wenyewe kwa wenyewe, ukawa udongo unaonata, kisha akasema: "Kutoka katika asili ya udongo." kisha ukanuka, ukawa matope yaliyotiwa sura, kwa hivyo akaumbwa kutoka kwa matope hayo yenye sura. Na ulipokauka, ukawa udongo wa kinamo (unaovutika). "Na hivi ndivyo kulivyokuwa kuumbwa kwa Adam. Na ama kauli yake: "Na kisha akajaalia uzao wake utokane na kizazi cha maji madhaifu." [Sajdah: 8], huu ni mwanzo wa kuumbwa kwa uzao wake, kutoka katika "kizazi cha maji madhaifu" ni manii yanapotoka kwa mwanadamu. Na hiyo ndiyo kauli yake, "Utokane na maji." inamaanisha manii." (Arraddu Alal Jahmiyyah wa Zzanadiqa, uk 179-180, chapa ya Daghash Al-Ajmi).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kwa mkono wake Mtukufu, na akawafanya Malaika wake kumsujudia, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Basi nitakapomkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia * Basi Malaika wote pamoja walimsujudia." [Al-Hijr: 29, 30] Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu atawakusanya Waumini siku ya Kiyama, na watasema: "Kwa nini tusifanye uombezi kwa Mola wetu Mlezi." Kwa hivyo na watamjia Adam, na watasema: "Wewe ni baba wa watu, Mwenyezi Mungu alikuumba kwa mkono wake, na akawafanya Malaika wake kukusujudia." (Imesimuliwa na Bukhari 4476, Muslim 193, na Ibn Majah 4312).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimuumba Adam, amani imshukie, kwa sura yake. Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: "Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kwa sura yake, urefu wake ulikuwa futi sitini." (Imesimuliwa na Bukhari 6227, na Muslim 2841). Na imesimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mmoja wenu anapopigana na ndugu yake, basi na ajiepushe na uso, kwa maana Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kwa sura yake." (Imesimuliwa na Bukhari 2559, Muslim 2612 na lafudhi ya haditi hii ni yake). Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mmoja wenu anapopiga, basi na ajiepushe kupiga uso, na wala asiseme: Mwenyezi Mungu aufanye uso wako kuwa mbaya, na uso wa fulani unafanana na uso wako, kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu alimuumba Adam kwa sura yake." (Imesimuliwa na Abdul Razzaq 17952, Al-Humaidi 1153, Ahmad 7420, Bukhari katika Al-Adab Al-Mufrad 173, na Ibn Abi Asim katika As-Sunna 531).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimuumbia Adam mke, ambaye ni Hawa kutokana na Adam mwenyewe ili apate utulivu kwake. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Yeye ndiye aliyewaumba kutokana na nafsi moja; na katika huo huo udongo akamfanya mwenzi wake, ili akae naye kwa utulivu." [Al-A'araf: 189]. Na amesema Mtukufu: “Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi aliyewaumba kutokana na nafsi moja, na akamuumba mkewe kutoka nafsi ile ile. Na akaeneza kutokana na wawili hao wanaume wengi na wanawake. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwaye mnaombana, na jamaa zenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mchunga juu yenu.” [An-Nisaa: 1].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaumba Adam na Hawa, na akawafanya wakae katika Bustani ya mbinguni. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tulisema: Ewe Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani ya mbinguni, na kuleni humo maridhawa popote mpendapo." [Al-Baqara: 35] Na aliwakataza wasile matunda ya mti huo, lakini Shetani - kwa sababu ya kuwaonea wivu - aliwatia wasiwasi na wakala matunda yake, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akawatoa katika Bustani hiyo ya mbinguni, na akawateremsha katika dunia, anasema Mola wa Haki juu ya hilo: "Na wewe, Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani hii, na kuleni humo mpendapo. Wala msiukaribie mti huu, mkawa katika wale waliodhulumu (nafsi zao) * Basi Shetani aliwatia wasiwasi ili kuwafichulia tupu zao walizofichiwa, na akasema: Mola wenu Mlezi hakuwakataza mti huu ila msije mkawa Malaika, au msije mkawa katika wanaoishi milele * Naye akawaapia: Kwa yakini mimi ni miongoni wa wanaowanasihi * Basi akawateka kwa hadaa. Na walipouonja ule mti, tupu zao zilifichuka na wakaingia kujibandika majani ya Bustanini humo. Mola wao Mlezi akawaita: Je, sikuwakataza mti huo, na kuwaambia ya kwamba hakika Shetani ni adui yenu wa dhahiri? * Wakasema: Mola wetu Mlezi! tumejidhulumu nafsi zetu, na kama hutotusamehe na kuturehemu, hakika tutakuwa katika wenye kuhasirika * Akasema: Teremkeni! Mtakuwa nyinyi kwa nyinyi ni maadui. Na kwenye ardhi itakuwa ndio makao yenu na starehe yenu mpaka ufike muda * Akasema: Humo mtaishi, na humo mtakufa, na kutoka humo mtatolewa." [Al-A'araf: 19-25].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimfanya Adamu kuwa Kiongozi katika dunia, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na pale Mola wako Mlezi alipowaambia Malaika: Hakika Mimi nitamweka katika ardhi Khalifa (Mtawala). Wakasema: Utaweka humo atakaye fanya uharibifu humo na kumwaga damu, ilhali sisi tunakutakasa kwa sifa zako na tunakutaja kwa utakatifu wako? Akasema: Hakika Mimi ninayajua msiyoyajua." [Al-Baqara: 30]
Na Mwenyezi Mungu alimjaribu, naye akasahau na akaasi, kisha Mola wake Mlezi akamteua na akamuongoa, amesema Mola wa Haki: "Na hakika hapo zamani tuliagana na Adam, lakini alisahau, wala hatukuona kwake azimio kubwa." [Taha: 115] Kisha Adam akapokea kutoka kwa Mola wake Mlezi maneno ambayo yalikuwa ni sababu ya Mwenyezi Mungu kumsamehe na kumkubalia toba yake, anasema Mola Mtukufu: "Kisha Adam akapokea maneno kutoka kwa Mola wake Mlezi, na Mola wake Mlezi akamkubalia toba yake; hakika Yeye ndiye Mwingi wa kukubali toba, Mwingi wa kurehemu * Tukasema: Shukeni nyote kutoka humo; na kama ukiwafikia uongofu utokao kwangu, basi watakaofuata uongofu wangu huo haitakuwa hofu juu yao wala hawatahuzunika" [Al-Baqara: 37, 38].
Na tunaamini kuwa haya yote yaliandikwa na Mwenyezi Mungu kwa Adam miaka arobaini kabla hajamuumba. Imesimuliwa katika hadithi sahihi kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: “Adam na Musa walihojiana, basi Musa akamwambia: Ewe Adam, wewe ndiwe baba yetu uliyetuangusha, na ukatutoa katika Bustani ya mbinguni. Na Adam akamwambia: Ewe Musa! Mwenyezi Mungu alikuteuwa kwa mazungumzo yake, na akakuandikia kwa mkono wake mwenyewe. Je, unanilaumu kwa yale Mwenyezi Mungu aliyoniandikia kabla hajaniumba kwa muda wa miaka arobaini? Basi Adam akawa amemshinda Musa kwa hoja. Basi Adam akawa amemshinda Musa kwa hoja." (Mtume alirudia hilo) Mara tatu. (Imesimuliwa na Bukhari 6614, Muslim 2652, Abu Dawud 4701, Tirmidhi 2134, na Ibn Majah 80).
Na tunaamini kwamba mwanzo wa uumbaji wa uzao wa Adam ni kama vile Mwenyezi Mungu alivyomwambia katika kauli yake Mtukufu: "Enyi watu! Ikiwa nyinyi mna shaka ya kufufuliwa, basi kwa hakika Sisi tuliwaumba kutokana na udongo, kisha kutokana na manii, kisha kutokana na kipande cha damu iliogandana, kisha kutokana na kipande cha nyama chenye umbo na kisicho kuwa na umbo, ili tuwabainishie. Nasi tunakiweka katika matumbo ya uzazi tunachokitaka mpaka muda uliowekwa. Kisha tunawatoa kwa hali ya mtoto mchanga, kisha mfikie kutimia akili. Na wapo katika nyinyi wanaokufa, na wapo katika nyinyi wanaorudishwa kwenye umri wa unyonge kabisa, hata mtu awe hajui kitu baada ya kuwa (alikuwa) akikijua." [Al-Hajj: 5] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na kwa yakini tumemuumba mtu kutokana na asili ya udongo * Kisha tukamjaalia awe tone la mbegu ya uzazi katika mahali tulivu, palipo madhubuti * Kisha tukaliumba tone hilo la mbegu ya uzazi kuwa damu iliyoganda, na tukaiumba damu hiyo kuwa pande la nyama, kisha tukaliumba pande hilo la nyama kuwa mifupa, na mifupa hiyo tukaivisha nyama. Kisha tukamfanya kuwa kiumbe mwingine. Basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa baraka, Mbora zaidi wa waumbaji." [Muminun: 12-14]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alitusimulia - naye ndiye mkweli anayeaminika - akasema: "Hakika, mmoja wenu, uumbaji wake unakusanywa tumboni mwa mama yake kwa siku arobaini, kisha anakuwa pande la damu kwa kipindi cha kiasi hicho, kisha anakuwa pande la nyama kwa kipindi cha muda huo, kisha Mwenyezi Mungu anamtuma Malaika na anamuamuru maneno manne, na anaambiwa: Andika matendo yake, riziki yake, muda wa maisha yake, na kwamba ni muovu au mwema, kisha anapuliziwa roho." (Imesimuliwa na Bukhari 3208), Muslim 2643, Abu Dawud 4708, Tirmidhi 2137, na Ibn Majah 76).
Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alieleza namna ambavyo mtoto humfanana baba yake, na wakati mwingine humfanana mama yake, pale Abdullah bin Salam alipomuuliza na kumwambia: "Hakika mimi ninakuuliza kuhusu mambo matatu ambayo ni nabii tu anayeyajua." Ni nini alama ya kwanza ya Saa ya Kiyama? Na ni nini chakula cha kwanza watakachokila watu Bustani ya mbinguni? Na vipi mtoto hufanana na baba yake au mama yake?" Akasema: "Jibril ameniambia kuhusu hayo sasa hivi." Ibn Salam akasema: "Huyo ndiye adui wa Mayahudi katika Malaika." Akasema: "Ama alama ya kwanza ya Saa ya Kiyama ni moto utakaowakusanya watu kutoka Mashariki hadi Magharibi. Na ama chakula cha kwanza ambacho wakazi wa Bustani ya mbinguni watakula, hicho kitakuwa ni sehemu ya ziada ya ini la nyangumi. Na ama kuhusu mtoto, maji ya mwanaume yakitangulia maji ya mwanamke, mtoto huyo atamfanana baba, na ikiwa maji ya mwanamke yatatangulia maji ya mwanaume, basi mtoto huyo atafanana na mama." Akasema: Ninashuhudia ya kuwa hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu, na ya kuwa wewe hakika ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. (Imesimuliwa na Bukhari 3938).
Na tunaamini kwamba watu wote ni uzao wa Adam, na Adam ametokana na udongo, kwa hivyo hakuna mtu mwenye ubora juu ya mwingine isipokuwa kwa uchaji Mungu. amesema Mola wa Haki: "Enyi watu! Hakika Sisi tumewaumba kutokana na mwanamume na mwanamke. Na tumewajaalia kuwa ni mataifa na makabila ili mjuane. Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu kwa Mwenyezi Mungu ni huyo aliye mchamungu zaidi katika nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua vyema, Mwenye habari zote. [Al-Hujurat: 13] Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu amewaondolea mzigo wa zama za ujinga, na kujifahiri kwao na baba zao. Mtu sasa ni Muumini mcha Mungu, au muovu aliye katika tabu. Nyinyi ni wana wa Adam, na Adam katokana na mavumbini...." (Imesimuliwa na Abu Dawud 5116, Tirmidhi 3956, Al-Muaafa bin Imran katika Az-Zuhd 147, Ibn Wahab katika Al-Jaami 30, na Ahmad 8736).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kutokana na mavumbi, na akamuumbia mkewe kutokana naye ambaye ni Hawa, amani iwe juu yao, na akaumba wanadamu wengineo kutokana na maji dhaifu, isipokuwa Isa, amani iwe juu yake. Mwenyezi Mungu alimuumba kutokana na mama bila baba, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza kuhusu hilo katika kauli yake Mtukufu: "Na pale Malaika waliposema: Ewe Maryamu! Hakika Mwenyezi Mungu anakubashiria (mwana) kwa neno litokalo kwake. Jina lake ni Masihi Isa mwana wa Maryamu, mwenye heshima katika dunia na Akhera, na miongoni mwa waliowekwa karibu (na Mwenyezi Mungu) * Naye atazungumza na watu katika utoto wake na katika utuuzima wake, na atakuwa katika watu wema * Maryamu akasema: Mola wangu Mlezi! Vipi nitampata mwana na hali mwanadamu hajanigusa? Mwenyezi Mungu akasema: Ndivyo vivyo hivyo, Mwenyezi Mungu huumba apendacho. Anapohukumu jambo, huliambia: Kuwa! Likawa." [Al-Imran: 45-47].
Na tunaamini kwamba Isa, amani iwe juu yake - hata kama uumbaji wake ni wa ajabu - ni mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Amesema Mola wa Haki, Mtukufu: "Hakuwa yeye (Isa) ila ni mja tuliyemneemesha na tukamfanya ni mfano kwa Wana wa Israili." [Mapambo: 59] Yeye ni mwanadamu tu miongoni mwa wanadamu, anakula chakula, na si mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Masihi mwana wa Maryam si chochote ila ni Mtume. Wamekwishapita Mitume kabla yake. Na mama yake ni mwanamke mkweli. Wote wawili walikuwa wakila chakula. Angalia jinsi tunavyowabainishia Aya, kisha angalia vipi wanavyogeuzwa." [Al-Maida: 91].
Na tunakuta katika Kitabu cha Mola wetu Mlezi, kwamba Mwenyezi Mungu anawajibu wale wanaodai kwamba Masihi ni mungu kwa ushahidi mwingi, na miongoni mwa ushahidi huu ni kauli yake Mola wa Haki, mwenye baraka nyingi, Mtukufu: "Mwenyezi Mungu hakujifanyia mwana yeyote, wala hana mungu mwingine. Ingekuwa hivyo, basi kila mungu angelichukua vile alivyoumba, na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Mwenyezi Mungu ametakasika mbali na sifa hizo wanazomsifia [Muminun: 91] Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Hakika wamekufuru wale waliosema: Mwenyezi Mungu ni Masihi mwana wa Maryamu. Sema: Ni nani mwenye kumiliki chochote mbele ya Mwenyezi Mungu ikiwa Yeye angetaka kumuangamiza Masihi mwana wa Maryamu, na mama yake, na wote waliomo katika ardhi? Na mamlaka ya mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake ni vya Mwenyezi Mungu. Huumba apendavyo. Na Mwenyezi Mungu anao uweza juu ya kila kitu." [Al-Maida: 91].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba watu kwa umbile la asili, amesema Mtukufu: "Basi uelekeze uso wako sawasawa kwenye Dini. Ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo Dini iliyonyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui." [Ar-Rum: 30]. Bin Zaid, Mujahid na Ikrima walisema: Umbile la asili ni Uislamu. (Tafsir Twabari 20/98).
Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie, na Ibrahim An-Nakha'i, na Said bin Jubair, na Mujahid, na Ikrima, na Qatada, na Dhahhak, na Ibn Zaid walisema kuhusu kauli yake, "Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu.“ yaani, dini ya Mwenyezi Mungu.” Al-Bukhari, katika Sahihi yake, alisema: "Mlango wa 'Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu: Yaani: katika dini ya Mwenyezi Mungu. "Mfumo wa watu wa tokea zamani." Yaani: dini ya watu wa kale. Na Al-Fitrah (umbile la asili) ni Uislamu.
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Kila mtoto huzaliwa katika umbile la asili, kisha wazazi wake wanamfanya kuwa Myahudi, au Mkristo, au Majusi (waabudu moto), kama vile mnyama anavyomzaa mnyama, je, mnaona ndani yake ulemavu wowote?" Kisha Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, anasema: "Ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu." [Ar-Rum: 30]. (Imesimuliwa na Bukhari 4775, Muslim 2658, Abu Dawud 4714, na Tirmidhi 2138).
Na imesimuliwa kutoka Iyadh bin Himar Al-Mujashii, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema siku moja katika hotuba yake: Sikilizeni! Hakika Mola wangu Mlezi aliniamrisha niwafundishe yale ambayo hamyajui, katika yale aliyonifundisha leo. Kila mali niliyompa mja, ni halali. Nami hakika Niliwaumba waja wangu hali ya kuwa ni wanyoofu wote, lakini mashetani waliwajia na wakawaondoa kutoka katika Dini yao, na wakawaharamishia yale niliyowahalalishia, na wakawaamrisha kwamba wanishirikishe na yale ambayo sikuyateremshia hoja yoyote..." (Imesimuliwa na Muslim 2865).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alivunja hoja za wale wanaokanusha kufufuliwa wafu, pale alipowakumbusha mwanzo wa kuumbwa kwao kutokana na mavumbi, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo atakayeihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika? * Sema: Ataihuisha huyo huyo aliyeiumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba." [Yasin: 78, 79].
Pia aliwakumbusha kuwa amewaumba kwa maji dhaifu, basi vipi wanamfanyia kiburi Mola wao Mlezi na wanaona kwamba haiwezekani kufufuliwa kwao na kukusanywa?! Amesema Mola wa Haki: "Ambaye ametengeneza vizuri umbo la kila kitu; na akaanzisha kumuumba mtu kwa udongo * Na kisha akajaalia uzao wake utokane na kizazi cha maji madhaifu * Kisha akamtengeneza, na akampulizia roho yake, na akawajaalia kusikia na kuona, na nyoyo za kufahamu. Ni machache mno mnayoshukuru * Nao husema: Tutakapokwishapotea chini ya ardhi, ni kweli tutarudishwa katika umbo jipya? Bali wao wanakanusha kwamba watakutana na Mola wao Mlezi * Sema: Atawafisha Malaika wa mauti aliyewakilishwa juu yenu; kisha mtarejeshwa kwa Mola wenu Mlezi." [Sajdah: 7-11].
Na tunaamini kuwa kuumba kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu waja wake ni ushahidi kwamba Yeye pekee ndiye anayestahiki kuabudiwa. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Enyi watu! Muabuduni Mola wenu Mlezi aliyewaumba nyinyi na wale wa kabla yenu, ili mpate kuokoka" [Al-Baqarah: 21].
Kama alivyotueleza Mwenyezi Mungu katika Qur'ani Tukufu kwamba Nuh aliwakumbusha watu wake kuwa Mwenyezi Mungu aliwaumba kwa awamu, kwa hivyo kwa nini hawampi heshima Mwenyezi Mungu?! Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Mna nini hamweki heshima ya Mwenyezi Mungu? * Na hali Yeye aliwaumba daraja baada ya daraja?" [Nuh: 13, 14].
Na mwanadamu ana hali mbalimbali katika maisha ya kaburini, na yatakuja maelezo ya kina kuhusiana na maisha ya nyumba ya Akhera - Mwenyezi Mungu akipenda - katika Kitabu cha kuamini Siku ya Mwisho.
Mlango wa kuumbwa roho
Na tunajua kwamba roho ni katika mambo ya Mwenyezi Mungu tu, na kwamba wanadamu hawajui juu yake isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu amewajulisha. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na wanakuuliza habari za Roho. Sema: Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi. Nanyi hamkupewa katika elimu ila kidogo tu." [Al-Al-Israa: 85] Na kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amridhie, amesema: "Nilipokuwa pamoja na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika shamba akiwa kaegemea kwenye mti mdogo, mara wakapita Mayahudi, wakasema kuambizana: "Muulizeni kuhusu Roho." Mmoja wao akasema: "Mnamuonaje?" Na baadhi yao wakasema: Asijewajibu kwa kitu mnachokichukia. Basi wakasema: Muulizeni. Basi wakamuuliza kuhusu Roho, Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akanyamaza bila ya kuwajibu kitu. Wakajua kuwa anateremshiwa wahyi (ufunuo). Kwa hivyo nikasimama mahali hapo nilipokuwa, na ufunuo huo ulipokwishateremka, akasema: "Na wanakuuliza habari za Roho. Sema: Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi." (Imesimuliwa na Bukhari 4721, Muslim 2794, na Tirmidhi 3141).
Na tunaamini kwamba roho zimeumbwa. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu." [Al-Zumar: 62]. Wakati Mwenyezi Mungu alipomaliza kumuumba Adam, amani iwe juu yake, akampulizia roho yake. Amesema Mola Mtukufu: "Basi nitakapomkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia." [Al-Hijr: 29]. Na mimba inapokamilisha miezi minne ndani ya tumbo la mama yake, Mwenyezi Mungu huitumia Malaika, na anapoipulizia roho. Imepokelewa kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: "Alituambia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - naye ndiye mkweli anayeaminiwa - akasema: "Hakika, mmoja wenu hukusanywa tumboni mwa mama yake siku arobaini, kisha anakuwa pande la damu kwa muda mfano wa huo, kisha anakuwa pande la nyama kwa muda mfano wa huo, kisha Mwenyezi Mungu anamtumia Malaika na anaamrishwa mambo manne: Riziki yake, muda wa maisha yake, atakuwa muovu au mwema, kisha roho inapulizwa ndani yake." (Imesimuliwa na Bukhari 3208, Muslim 2643, Abu Dawud 4708, Tirmidhi 2137, na Ibn Majah 76). Isipokuwa Masihi, amani iwe juu yake, yeye mwanzo wa ujauzito wake ulikuwa kutokana na Malaika kumpulizia Maryamu. Amesema Mola wa Haki: "Na mwanamke aliyelinda uke wake, na tukampulizia katika roho yetu, na tukamfanya yeye na mwanawe kuwa ni Ishara kwa walimwengu." [Al-Anbiya: 91] Na amesema Mtukufu: "Hakika Masihi Isa mwana wa Maryamu ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na neno lake tu alilompelekea Maryamu, na ni roho iliyotoka kwake." [An-Nisaa: 171]
Na tunaamini kwamba roho huchukuliwa wakati wa usingizi, na kisha hurudishwa mwilini. Amesema Mola wa Haki: "Mwenyezi Mungu huzipokea roho zinapokufa. Na zile zisiokufa wakati wa kulala kwake, huzishika zilizohukumiwa kufa, na huzirudisha nyengine mpaka ufike wakati uliowekwa." [Az-Zumar: 42].
Abdullah Ibn Abi Qatada alisimulia kwamba baba yake, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Tulikuwa tunasafiri pamoja na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, usiku moja, basi baadhi ya watu hao wakasema: "Lau tungalipumzike katika masaa ya mwisho ya usiku ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu.' Akasema: "Ninahofia mtalala mpitwe na swala." Bilal akasema: "Mimi nitawaamsha." Kwa hivyo wakalala, na Bilal akauegemeza mgongo wake kwenye ngamia wake wa kusafiria, lakini jicho lake likamshinda kwa hivyo akalala. Basi Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akaamka hali ya kuwa tayari jua limeshachomoza. Akasema, "Ewe Bilal, yako wapi yale uliyoyasema?" Akasema: "Kamwe sijawahi kulala hivi." Akasema: "Hakika Mwenyezi Mungu alizichukua roho zenu alipotaka, na akazirudisha kwenu alipotaka." (Imesimuliwa na Bukhari 595, Abu Dawud 439, 440, na An-Nasa'i 846).
Na imesimuliwa na Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mmoja wenu anapokuwa katika malazi yake, basi naakung'ute malazi yake kwa ndani ya shuka lake, kwa maana hajui ni nini kilichokuja hapo nyuma yake. Kisha aseme: Kwa jina lako, Mola wangu Mlezi, nimeuweka chini ubavu wangu, na kwa sababu yako nitauinua. Ukishika roho yangu, basi irehemu. Na ukiiachia nafasi basi ihifadhi kwa kile unachowahifadhi kwacho waja wako wema." (Imesimuliwa na Bukhari 6320, Muslim 2714, Abu Daud 5050, Tirmidhi 3401, na Ibn Majah 3874).
Na tunaamini kwamba roho huondoka katika mwili wakati wa kifo. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Kila nafsi itaonja mauti. Kisha mtarudishwa kwetu." [Al-Ankabut: 57] Na roho huondoka mwilini kabisa wakati wa mauti, na macho huifuata. Ummu Salama alisimulia kwamba: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, aliingia alimokuwa Abuu Salama huku macho yake yameshakodoka, akayafumba, kisha akasema: "Hakika, roho inapochukuliwa, macho huifuata." (Imesimuliwa na Muslim 920, Abu Dawud 3118, na Ibn Majah 1454). Kwa hivyo, roho haifi kama mwili unavyokufa. Kifo chake ni kuachana na mwili.
Na tunaamini kwamba Malaika hutoa roho katika miili wakati wa kufa, na roho hiyo pia inapata neema au adhabu. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na lau ungeliwaona madhalimu wanavyokuwa katika mahangaiko ya mauti, na Malaika wamewanyooshea mikono wakiwambia: Zitoeni roho zenu! Leo mtalipwa adhabu ya fedheha kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyasema juu ya Mwenyezi Mungu yasiyo ya haki, na mlivyokuwa mkizifanyia kiburi Ishara zake." [Al-An 'am: 93].
Kwa hivyo, Malaika hao huitoa nafsi, kisha inapata adhabu au furaha kama vile mwili pia unapata adhabu au furaha. Imesimuliwa na Al-Baraa bin Azib, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: "Tulitoka kwenda pamoja na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika mazishi ya mmoja katika Maanswari (Watu wa Madina) tulipofika kaburini mwanandani ilikuwa bado haijachibwa. Kwa hivyo, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akaketi chini, nasi tukaketi kando kando yake, kana kwamba kuna ndege juu ya vichwa vyetu (kwa namna tulivyokuwa na utulivu). Naye alikuwa na fimbo mkononi mwake huku akichora kwayo juu ya ardhi. Kisha akainua kichwa chake, na akasema, "Jikingeni kwa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya kaburini." Akalisema hilo mara mbili. Kisha akasema: "Hakika mja Muumini anapokuwa amekaribia kutengana na dunia hii, na kuelekea Akhera, hushukiwa na Malaika kutoka mbinguni wenye nyuso nyeupe, kana kwamba nyuso zao ni jua, huku wamebeba sanda kutoka katika sanda za Bustani ya mbinguni, na manukato kutoka katika manukato ya Bustani ya mbinguni mpaka wanapoketi mbali naye kwa umbali wa mwisho wa kuangalia kwa macho. Kisha Malaika wa mauti amani iwe juu yake anakuja mpaka aketi karibu na kichwa chake. Anasema: "Ewe nafsi nzuri, ondoka uende katika msamaha wa Mwenyezi Mungu na radhi zake." kisha akasema: "Kwa hivyo inatoka ikitiririka kama linavyotitirika tone kutoka katika mdomo wa chupa, kisha anaichukua. Na anapoichukua, Malaika hao wengine hawaiachi katika mkono hata kwa kiasi cha kupepesa macho ila wanakuwa wameshaichukua, kisha wanaitia katika sanda hiyo, na katika manukato hayo, kisha inatoka katika nafsi hiyo harufu nzuri zaidi ya miski inayopatikana juu ya uso wa dunia." Akasema: "Kisha wanapanda naye, na hawapiti - yaani na nafsi hiyo - kwa kundi la Malaika isipokuwa wanasema, "Ni roho gani hii nzuri?" Hao walioibeba wanasema: "Ni fulani mwana wa fulani." wanamuita kwa majina yake mazuri zaidi ambayo walikuwa (Watu) wakimuita katika dunia. Mpaka wanapofika nayo katika mbingu ya chini, wanaomba kufunguliwa, kwa hivyo anafunguliwa, kisha anasindikizwa katika kila mbingu na wakazi wake wale walio karibu na Mwenyezi Mungu hadi katika mbingu inayofuata, mpaka wanapofika nayo katika mbingu ya saba, Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mtukufu anasema: "Andikeni kitabu cha mja wangu katika 'Iliyyin (walio juu zaidi), na mrudisheni katika ardhi. Kwani, tuliwaumba kutokana nayo (Ardhi), na humo tunawarudisha, na kutoka humo tutawatoa mara nyingine." Akasema: 'Kisha roho yake hiyo inarudishwa katika mwili wake." (Imesimuliwa na Abuu Dawud 3212, An-Nasa'i 2001, Ibn Majah 1548, Abu Dawud At-Tayalisi 789, Abdul Razzaq 6324, 6737, Ahmad 18534 na matamshi haya ni yake.) Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akawa ametaja katika hadithi hii kwamba roho hutoka nje, na hutiririka, na huchukuliwa, na huvishwa sanda, na wanapanda nayo juu, na inarudishwa katika ardhi. Na haya yote ni katika sifa za viumbe.
Na tunaamini kwamba roho baada ya kutengana kwake na mwili, zinakaa kwa furaha au adhabu hadi Siku ya Kiyama. Imesimuliwa kutoka kwa Ka'ab bin Malik, Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: "Hakika roho ya muumini iko katika (umbile la) ndege aliye katika miti ya Bustani za mbinguni mpaka Mwenyezi Mungu Mtukufu atakapomfufua na iende katika mwili wake Siku ya Kiyama." (Imesimuliwa na An-Nasa'i 2073, Tirmidhi (1641), Ibn Majah (4271), Abdul Razzaq katika Tafsir (484, 2681), Al-Humaidi (897), na Ahmad (15776, 15777).
Na imesimuliwa kutoka kwa Masruq kuwa alisema: Tulimuuliza Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu amridhie, kuhusu aya hii: "Wala kabisa usiwadhanie wale waliouliwa katika Njia ya Mwenyezi Mungu kuwa ni maiti. Bali hao wako hai, wanaruzukiwa kwa Mola wao Mlezi.” [Al-Imran 3: 169] Akasema: Hakika sisi pia tuliuliza juu ya hilo, na akasema: "Roho zao ziko ndani ya ndege wa kijani kibichi, ambao wana taa zinazoning'inia kwenye kiti cha enzi, wanapaa katika Bustani za mbinguni watakako, kisha wakarudi kutulia katika taa hizo..." (Imesimuliwa na Muslim (1887), Tirmidhi (3011), na Ibn Majah (2801).
Kitabu cha Dini.
Muhtasari wa kitabu
Tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliridhia kwamba Uislamu uwe ndiyo dini, ambao ndiyo dini ya manabii na mitume wote, amani iwe juu yao, nao ndiyo umbile la asili ambalo Mwenyezi Mungu aliwaumba watu juu yake, nao ndilo agano ambalo Mwenyezi Mungu alilichukua kutoka kwa Adam na kizazi chake.
Na tunaamini kwamba Uislamu huu ndio wasia wa Ibrahim, amani iwe juu yake, kwa wanawe, nao pia ndio wasia wa Yaaqub, amani iwe juu yake, kwa wanawe, nao ndiyo dini bora zaidi, kamilifu zaidi, na kwamba Mwenyezi Mungu hatakubali dini nyingine yoyote isipokuwa hiyo.
Na tunaamini kwamba dini hii ndiyo dini ambayo Jibril, muaminifu, aliteremka nayo kwa Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nayo ni daraja mbalimbali ambazo ni: Uislamu, Imani, na Ihsani, na kila moja katika hizi ina nguzo zake.
Na kwamba dini hii inajumuisha mema yote, yakiwemo matendo ya mioyo na viungo.
Na tunajua kwamba imani ni kauli, matendo, na itikadi, na kwamba wenye imani wanatofautiana katika matendo yao. Na tunaamini kwamba imani huongezeka na kupunguka. Huongezeka kwa utii na hupungua kwa uasi.
Na tunashuhudia kwamba watu wenye imani ndio watu waliofaulu katika dunia na Akhera, na kwamba watu wa dini hii ya kweli, hatima yao ni katika Bustani za mbinguni, bila kujali kutofautiana kwao katika daraja na vyeo.
Na tunajua kwamba zimekuja aya nyingi tukufu na hadithi tukufu zikiamrisha kutekeleza daima Sunna na kushikamana nayo, na kuonya dhidi ya kukiuka hilo, na pia zikakataza kutengana na kutofautiana.
Mlango wa: Hakika Dini ya haki kwa Mwenyezi Mungu ni Uislamu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliridhia kwamba Uislamu ndiyo dini ya haki. Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema: "Na nimewapendelea Uislamu uwe ndiyo Dini." [Al-Maida: 91]. Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Bila ya shaka Dini (ya haki) mbele ya Mwenyezi Mungu ni Uislamu." [Al-Imran: 19] Na ndiyo dini ya Manabii na Mitume wote, amani iwe juu yao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu Nuhu, amani iwe juu yake, kwamba alisema: "Na nimeamrishwa kwamba niwe miongoni mwa Waislamu." [Yunus: 72] Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema kuhusu Ibrahim, amani iwe juu yake: "Na Mola wake Mlezi alipomwambia: Silimu, nyenyekea! Alinena: Nimesilimu, nimenyenyekea kwa Mola wa walimwengu wote."
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ametukamilishia Dini, kwa hivyo haina upungufu wowote kwa namna yoyote ile. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Leo nimewakamilishia Dini yenu, na nimewatimizia neema yangu, na nimewapendelea Uislamu uwe ndiyo Dini." [Al-Maida: 3] Na ndiyo dini bora zaidi, iliyokamilika zaidi. Na dini hii ndiyo Haniifiyya (Uongofu), mila ya Ibrahim, amani iwe juu yake. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na ni nani ana dini bora kuliko yule aliyeusilimisha uso wake kwa Mwenyezi Mungu, naye akawa mwema, na akafuata mila ya Ibrahim muongofu? Na Mwenyezi Mungu alimfanya Ibrahim kuwa ni rafiki mwandani." [An-Nisaa: 125] Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka amesema: "Na ni nani atajitenga na mila ya Ibrahim isipokuwa yule anayeitia nafsi yake katika upumbavu? Na kwa yakini Sisi tulimteuwa yeye katika dunia; na hakika yeye katika Akhera atakuwa miongoni mwa watu wema." [Al-Baqarah: 130]. Na amesema Mola wa Haki Mtukufu, mwenye majina matakatifu kuhusiana na Ibrahim Al-Khalil (kipenzi), amani iwe juu yake: "Ibrahim hakuwa Yahudi wala Mkristo, lakini alikuwa muongofu Muislamu, wala hakuwa katika washirikina." [Al-Imran: 67].
Nayo ndiyo maumbile ya asili ambayo Mwenyezi Mungu aliwaumba watu wakiwa juu yake, anasema Mtukufu: "Basi uelekeze uso wako sawasawa kwenye Dini - ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilo waumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo Dini iliyonyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui." [Ar-Rum: 30].
Na alisema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kila mtoto huzaliwa katika umbile la asili, kisha wazazi wake wanamfanya kuwa Myahudi, au Mkristo, au Majusi (wanaoabudu moto), kama vile mnyama anavyomzaa mnyama. Je, mnaona ndani yake kasoro yoyote?", Kisha anasema Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amuwie radhi: "Umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo Dini iliyo nyooka sawa." [Ar-Rum: 30]. (Imesimuliwa na Bukhari (1385), Muslim (2658), Abu Dawud (4714), na Tirmidhi (2138).) Nalo ndilo agano ambalo Mwenyezi Mungu alilichukua kutoka kwa Adam na kizazi chake. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: “Na pale Mola wako Mlezi alipochukua kutoka kwa wanadamu, kutoka migongoni mwao kizazi chao, na akawashuhudisha juu ya nafsi zao, akawaambia: Je, Mimi si Mola Mlezi wenu? Wakasema: Bila shaka! Tumeshuhudia. Msije mkasema Siku ya Kiyama sisi tulikuwa tumeghafilika na hayo." [Al-'Araf: 172].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakubali dini nyingine isiyokuwa hiyo. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema: “Na anayetafuta dini isiyokuwa Uislamu, haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa katika wenye kupata hasara.” [Al-Imran: 85].
Mlango wa Uislamu
Na tunaamini kuwa dini hii ni ile aliyoteremka nayo Jibril kwa Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na kwamba ina daraja ambazo ni: Uislamu, Imani, na Ihsani, na kila moja ya hizo ina nguzo zake. Imesimuliwa na Omar bin Khattab, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Siku moja tulipokuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, tazama, mwanamume mmoja alitutokezea. Naye alikuwa ana nguo nyeupe mno, mwenye nywele nyeusi mno, haionekani juu yake athari yoyote ya safari mpaka alipokaa karibu na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, kisha akashikanisha magoti yake na magoti ya (Mtume) na akaweka mikono yake juu ya mapaja yake na akasema: "Ewe Muhammad, niambie kuhusu Uislamu?" Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, akasema: "Uislamu ni ushuhudie kwamba hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na usimamishe swala, na utoe zaka, na ufunge saumu ya Ramadhani, na uhiji Nyumba tukufu ikiwa utapata uwezo wa kuifikia." Akasema: “Umesema ukweli." (Omar) Akasema: "Basi tukamstaajabu. Anamuuliza, kisha anasema kwamba amesema ukweli!!." (Malaika) akasema: "Basi niambie kuhusu imani." Akasema: "Ni umwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na vitabu vyake, na mitume wake, na siku ya Mwisho, na uamini Kadari; njema na mbaya." Akasema: "Umesema kweli." Akasema: "Basi niambie kuhusu ihsani." Akasema: "Ni umwabudu Mwenyezi Mungu kana kwamba unamuona. Na ikiwa humuoni, basi Yeye anakuona." Akasema: "Niambie kuhusu Saa. (Kiyama)" Akasema: "Aliyeulizwa juu ya hilo si mjuzi zaidi kuliko muulizaji." Akasema: "Basi, nieleze kuhusu alama zake." Akasema: "Ni kijakazi kumzaa bwana yake, na utakapowaona watu walio pekupeku, uchi, maskini, wachungaji wa kondoo wakishindana kujenga majengo marefu." (Omar) Anasema: "Kisha akaondoka, na nikakaa kwa muda, kisha (Mtume) akaniambia: “Ewe Omar, unajua ni nani muulizaji huyo?" Nikasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wajuao zaidi." Akasema: "Huyo ni Jibril, amekujieni ili akufundisheni Dini yenu." (Imepokewa na Muslim (8), Abu Daud (4695), Tirmidhi (2610), An-Nasa’i (4990), na Ibn Majah (63).
Na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alieleza nguzo za Uislamu katika hadithi nyinginezo, akisema: "Uislamu umejengwa juu ya nguzo tano: Kushuhudia kwamba hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kusimamisha Swala, na kutoa Zaka, na kufanya Hija, na kufunga mwezi wa Ramadhani" (Imesimuliwa na Bukhari (8), Muslim (16), Tirmidhi (2609), na An-Nasa'i (5001). Na imekuja kutoka kwa Twalha bin 'Ubaidillah, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Mwanaume mmoja alikuja kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, kutoka kwa watu wa Najidi huku ametimka nywele zake, huku ukisikika mvumo wa sauti yake kubwa, lakini hakieleweki anachosema, mpaka alipokaribia, punde, akauliza kuhusu Uislamu. Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ni swala tano mchana na usiku." Akasema: "Je, inanilazimu swala nyingineyo?" Akasema: "Hapana isipokuwa ukijitolea tu." Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Na kufunga saumu ya Ramadhani." Akasema: "Je, kunanilazimu kufunga kwingineko?" Akasema: "Hapana isipokuwa ukijitolea tu." (Twalha) akasema: Kisha Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akamtajia Zaka, akasema: "Je, inanilazimu zaka nyingineyo?" Akasema: "Hapana, isipokuwa ukijitolea tu." Akasema: Kisha mwanaume huyo akageuza mgongo wake akaondoka huku akisema: "Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, sitazidisha juu ya haya, wala sitapunguza kwayo kitu." Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: “Atafaulu, ikiwa anasema kweli." (Imesimuliwa na Bukhari (46), Muslim (11), Abu Dawud (391), na An-Nasa'i (458).
Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu, na washike Sala, na watoe Zaka. Na hiyo ndiyo Dini madhubuti." [Al-Bayyina: 5]. Na amesema Mtukufu: "Lakini wakitubu, wakashika Sala, na wakatoa Zaka, basi waachilieni. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe mno, Mwingi wa kurehemu." [Tauba: 5] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi wakitubu na wakashika Sala na wakatoa Zaka, basi ni ndugu zenu katika Dini." [Tauba: 11]. Na amesema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Nimeamrishwa nipigane na watu mpaka washuhudie kuwa hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu na kuwa Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na wasimamishe swala, na watoe zaka, na pindi watakapofanya hivyo, watakuwa wamezikinga kutokana nami damu zao na mali zao isipokuwa kwa haki ya Uislamu na hesabu yao itakuwa juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu". (Imesimuliwa na Bukhari (25), na Muslim (22).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Musa, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Walisema (Maswahaba): Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni upi Uislamu ulio bora zaidi? Akasema: “Ni yule ambaye Waislamu wanasalimika kutokana na ulimi wake na mkono wake.” (Imesimuliwa na Bukhari - 11, Muslim (42), Tirmidhi 2504, na An-Nasa'i (4999).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Mja anaposilimu, kisha akaufanya Uislamu wake kuwa mzuri, Mwenyezi Mungu humfutia kila baya alilotanguliza, na kinakuwa ni kisasi baada ya hapo: Jema moja kwa mara kumi mfano wake, hadi mizidisho mia saba. Na baya moja ni kwa mfano wake isipokuwa ikiwa Mwenyezi Mungu atalisamehe." (Imesimuliwa na Bukhari - Hadith Mu'llaq - (41), na An-Nasa'i (4998).
Mlango wa Imani
Na tunaamini kwamba daraja la pili la dini ni imani. Nayo ni kama ilivyokuja katika jibu la Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipomjibu Jibril wakati alipomuuliza kuhusu imani. Alisema: "Basi niambie kuhusu imani." Akasema: "Ni kwamba umuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake, na Mitume wake, na Siku ya Mwisho, na uamini Kadari yake, njema na mbaya." Akasema: "Umesema kweli." Akasema: Kisha akaondoka, na nikaka kwa muda, kisha akaniambia: "Ewe Omar, unajua muulizaji huyo ni nani?" Nikasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wajuao zaidi." Akasema: "Huyo ni Jibril, amewajia ili awafundishe Dini yenu." (Imepokewa na Muslim (8), Abu Dawud (4695), Tirmidhi (2610), An-Nasa’i (4990), na Ibn Majah (63).
Na Imani, hata kama Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliifasiri katika hadithi iliyotangulia ya Jibril, amani iwe juu yake, kwa maana maalumu, ambayo ni kauli yake: “Ni kumuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu Vyake, na Mitume Wake, na Siku ya Mwisho, na uamini Kadari, njema na mbaya." isipokuwa pia huwa na maana ya jumla zaidi, ambayo inajumuisha kila heri miongoni mwa matendo ya mioyo na viungo. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hakika Waumini ni wale ambao anapotajwa Mwenyezi Mungu, nyoyo zao hujaa hofu, na wanaposomewa Aya zake, huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi." Hao ambao wanashika Sala na wanatoa katika yale tunayowaruzuku * Hao kweli ndio Waumini. Wao wana vyeo, na maghfira (Msamaha), na riziki bora, kwa Mola wao Mlezi." [Al-Anfal: 2-4].
Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliufasiria maana ya imani Msafara wa Abdul-Qais kwa ibada mbali mbali za dhahiri. Katika vitabu vya hadithi sahihi imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Hakika Msafara wa Abdul-Qais ulipomjia Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasema: Nyinyi ni watu gani?" au "Nyinyi ni Msafara gani?" Wakasema: "Wa Rabi'a." Akasema: "Karibuni enyi watu." au "wageni" msijihisi unyonge, wala majuto." Wakasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika sisi hatuwezi kukujia isipokuwa katika mwezi mtukufu, na baina yetu na wewe, kuna kabila hili la Mudhwari. Basi tuamrishe amri ya mkato, ambayo tutawajulisha wale walio nyuma yetu, na tuingie kwayo katika Bustani za mbinguni." Na pia wakamuuliza kuhusu vinywaji, naye akawaamrisha manne na akawakataza manne: Aliwaamrisha kumuamini Mwenyezi Mungu peke yake. Akasema: "Je, mnajua ni nini kumuamini Mwenyezi Mungu peke yake?" Wakasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wajuao zaidi." Akasema: "Ni kushuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kuwa Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kusimamisha Swala, na kutoa Zaka, na kufunga saumu katika mwezi wa Ramadhani, na kutoa moja ya tano (humusi) ya ngawira." Na akawakataza kufanya mambo manne: "Al-hantam." Nao ni mtungi uliopakwa mafuta ambao ulikuwa ukitumiwa kubebea mvinyo (pombe). (An-Nihaaya fi Gharib al-Hadith 448/1). "Na Dubba" ambayo ni kibuyu walichokuwa wakitia tende ndani yake ili ziwe pombe haraka. (An-Nihaaya fi Gharib al-Hadith 96/1). "Na Naqir" ambayo ni shina la mtende ambalo linatobolewa katikati, kisha zinatiwa tende ndani yake pamoja na maji ili kinywaji hicho kiweze kulewesha. (An-Nihaaya fi Gharib al-Hadith 104/5)" Na vyungu vilivyopakwa lami" Na akasema: "Yahifadhini haya, na muwaambie wale walio nyuma yenu." (Imesimuliwa na Bukhari (53), Muslim (17), Abu Dawud (3692), Tirmidhi (2611), na An-Nasa'i (5031).
Imam Bukhari, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango katika kitabu chake cha hadithi sahihi kuhusiana na suala hili akasema: "Mlango wa mambo ya imani, na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa Mashariki na Magharibi. Bali wema ni wa anaye muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii, na anawapa mali, kwa kupenda kwake, jamaa na mayatima na masikini na wasafiri, na waombao, na katika kuwakomboa watumwa (Waachwa huru), na akawa anashika Sala, na akatoa Zaka, na wanaotimiza ahadi yao wanapoahidi, na wanaovumilia katika shida na madhara na wakati wa vita; hao ndio waliosadikisha, na hao ndio wacha Mungu." [Al-Baqarah: 177].
Na tunaamini kwamba imani ni kauli, vitendo na itikadi. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Imani ni zaidi ya matawi sabini au zaidi ya sitini, bora yake ni kusema: Hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na ya chini yake zaidi ni kuondoa udhia barabarani. Na staha (Haya) ni tawi katika imani". (Imepokewa na Bukhari (9), Muslim (35) na maneno ni yake, Abu Dawud (4676), Tirmidhi (2614), An-Nasa’i (5005), na Ibn Majah (57).
Na tunaamini kuwa watu wenye imani wanatofautiana katika matendo yao. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Said Al-Khudri, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: "Watu wa Bustani ya mbinguni wataingia katika Bustani hizo, na watu wa Motoni wataingia Motoni, kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu atasema: "Mtoeni Motoni yule mwenye chembe ya haradali (mfano wa ulezi) ya imani moyoni mwake." Kwa hivyo watatoka ndani yake wakiwa weusi, kisha watatupwa katika mto wa uzima, nao watamea kama vile nafaka inavyomea kando ya njia ya mafuriko. Je, huoni kwamba inatoka hali ya kuwa ni njano imejipinda?!" (Imesimuliwa na Bukhari (22), Muslim (184).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Umama bin Sahl bin Hanif kwamba alimsikia Abuu Saidi Al-Khudri, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, akisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Nilipokuwa nimelala, niliona watu wakiwekwa mbele yangu huku wamevaa mashati. Kuna yale yaliyokuwa yamefikia kwenye matiti, na baadhi yake hayakufikia hapo. Na Omari bin Khatwab aliwekwa mbele yangu hali ya kuwa amevaa shati analiburura chini." Watu wakauliza: Ulilifasiri vipi hilo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Akasema, "Dini!" (Imesimuliwa na Bukhari (23), Muslim (2390), Tirmidhi (2285) na pia imesimuliwa hivi kutoka kwa baadhi ya masahaba wa Nabii, na An-Nasa'i (5011).
Na tunaamini kuwa imani inaongezeka na inapungua, inaongezeka kwa utiifu na inapungua kwa uasi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sisi tunakusimulia habari zao kwa haki. Hakika wao walikuwa ni vijana waliomuamini Mola wao Mlezi. Na Sisi tukawazidisha uongofu." [Al-Kahf 13]. Na alisema: "Na wazidi Imani wale walioamini" [Al-Mudathir: 31].
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Atatoka Motoni yeyote yule aliyesema: Hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu hali ya kuwa moyoni mwake kuna heri uzito wa shairi. Na atatoka Motoni yeyote yule atakayesema: Hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu hali ya kuwa moyoni mwake kuna heri uzito wa ngano. Na atatoka Motoni yeyote yule atakayesema: Hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu hali ya kuwa moyoni mwake kuna heri uzito wa chungu (punje ndogo). (Imepokewa na Bukhari (44), Muslim (193), na Tirmidhi (2593).
Omari bin Abdulaziz alimwandikia 'Adiy bin Adiy kuwa: "Hakika, Imani ina faradhi zake, sheria, mipaka, na Sunna zake. Kwa hivyo, yeyote atakayeyakamilisha, atakuwa amekamilisha imani. Na yeyote asiyeyakamilisha, basi hatakuwa amekamilisha imani. Na kama nitaishi, basi nitawabainishia hayo ili myatende. Na ikiwa nitakufa, basi mimi sipupii sana kuendelea kuishi pamoja nanyi." (Imesimuliwa na Bukhari - kutoa maoni - (1/10), na Ibn Abī Shaiba katika Muṣannaf (31084) na katika Iman (135), na Al-Khallal katika Sunna (1162, 1553), na Ibn Battā katika Al-Ibānah (1166), na Al-Lālākani katika Sharh Usul Itikad Ahlus-Sunna wala-Jamaa (1572).
Muammar, na Sufian Thawri, Malik bin Anas, Ibn Juraij, na Sufian bin Uyaina walikuwa wakisema: "Imani ni kauli na matendo, huongezeka na kupungua." (Al-Ibana Al-Kubra (2/806), na Sharia, cha Al-Aajurri (2/606).
Na amesema Al-Hafidh Abuu Bakari Abdullah bin Al-Zubair Al-Humaidi : ".. Na kwamba imani ni kauli na matendo, huongezeka na kupungua, na wala hainufaishi kauli tu bila ya matendo, wala kauli na matendo isipokuwa kwa nia, wala kauli, matendo, nia isipokuwa kwa kufuata Sunna za Mtume." (Usuulu-ssunna cha Al-Humaidi (uk. 37).
Na amesema Al-Khalal: "Abdul-Maliki Al-Maimuni aliniambia: Ya'la ibn Ubaidi aliniambia zaidi ya miaka sitini iliyopita: Imani ni kauli na matendo. Na hakika mwenye kufunga saumu, kusali na kufanya matendo mema ana imani zaidi kuliko yule anayeiba na kuzini." (As-Sunna cha Al-Humaidi, uk. 37).
Ibn Abī Hātim alisema: "Nilimuuliza baba yangu na Abuu Zur'a juu ya mafundisho ya watu wa Sunna kuhusu misingi ya dini, na kile walichokipata wanachuoni kutoka katika miji yote wakifanya, na kile ambacho wao wawili wanaitakidi katika hayo. Wakasema: Tuliwakuta wanachuoni kutoka katika miji yote - Hijazi, Iraq, Sham, na Yemen - na ilikuwa ni katika kauli yao kwamba: Imani ni kauli na matendo, huongezeka na kupungua." (Sharhu Iitiqaadi Ahlissunna Waljama'a (1/198), na Aqiidatus Salaf - Muqaddimat ibni Abi Zaid Al-Qayrawani kwenye kitabu chake Ar-Risala uk. 29).
Al-Lalakaai alisema: "Imani ni kauli na matendo, na hivyo ndivyo walivyosema wanazuoni kama vile: Malik bin Anas, Abdulaziz bin Abi Salama Al-Maajshun, Al-Laith bin Saad, Al-Awzaii, Said bin Abdulaziz, Ibn Juraij, Sufian bin Uyainah, Fudhail bin Iyadh, Nafi bin Omari Al-Jumahi, Muhammad bin Muslim At-Taifi, Muhammad bin Abdullah bin Amri bin Othman bin Affan, Al-Muthanna bin Swabah, Shafi'i, Abdullah bin Zubair Al-Humaidi, Abuu Ibrahim Al-Muzani, Sufian Thawri, Shariq, Abuu Bakari bin Iyashi, Waki', Hamad bin Salama, Hamad bin Zaid, Yahya bin Saidi Al-Qattan, Abdullah bin Al-Mubarak, Abu Is-haq Al-Fazarii, Nadhiri bin Muhammad Al-Mirwazii, Nadhr bin Shumail, Ahmad bin Hambal, Is-haq bin Rahweih, Abuu Thawri, Abu Ubaid. (Sharhu Usuulu Iitiqaadi Ahlus-Sunna wal-Jama'a, cha Imam Al-Laalakai (4/913).
Na alisema Abuu Abdullah bin Abi Zamanain katika kitabu chake "Usuulus-Sunna": "Mlango wa Imani ni kauli na matendo: Hakika imani ni moyo kumkusudia Mwenyezi Mungu pekee, na kushuhudia kwa ulimi, na kutenda matendo kwa viungo, kwa nia nzuru (Ikhlaswi), na kufuata Sunna za Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake." (Usul-Sunna, uk. 207).
Mlango wa Ihsan
Tunaamini kwamba daraja la tatu la dini ni Ihsan, nayo ni kama Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alivyomjibu Jibril alipomuuliza kuhusu ihsan, alisema: "Niambie kuhusu ihsan." Akasema: "Ni umuabudu Mwenyezi Mungu kana kwamba unamuona, na kama humuoni, basi hakika Yeye anakuona...". Akasema: Kisha akaenda zake, nami nikakaa kwa muda, kisha akaniambia: "Ewe Omari, unajua muulizaji huyo ni nani?" Nikasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wajuao zaidi." Akasema: "Huyo ni Jibril aliwajia ili awafundishe Dini yenu." (Imesimuliwa na Muslim (8), Abu Dawud (4695), Tirmidhi (2610), An-Nasa'i (4990), na Ibn Majah (63).
Alisema Mola wa Haki Mtukufu kwamba watu wa dini hii ya haki hatima yao ni katika Bustani za mbinguni bila kujali daraja na vyeo vyao - sawa iwe walio katika daraja la Uislamu, au walio katika daraja la Imani, au walio katika daraja la Ihsan. Akasema Mola Mtukufu: "Na hayo tuliyokufunulia kutoka Kitabuni ni Kweli yenye kusadikisha yale yaliyokuwa kabla yake. Hakika Mwenyezi Mungu kwa waja wake ni Mwenye habari zote na Mwenye kuona yote * Kisha tumewarithisha Kitabu hao ambao tuliwateuwa miongoni mwa waja wetu. Kati yao yupo aliyejidhulumu nafsi yake, na yupo wa katikati, na yupo aliyetangulia katika mambo ya heri, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo fadhila kuu * Mabustani ya milele watayaingia. Huko watavikwa vikuku vya dhahabu, na lulu, na nguo zao humo ni za hariri * Na watasema: Alhamdulillahi (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu) aliyetuondolea huzuni zote. Hakika Mola wetu Mlezi bila ya shaka ni Mwenye kusamehe mno, Mwingi wa shukrani." [Suratu Faatir: 31-34]
Mlango wa kudumu katika Sunna na kushikamana nayo
Na zimekuja Aya tukufu na hadithi tukufu kwa wingi zikiamrisha kudumu katika Sunna na kushikamana nayo, na kuonya dhidi ya kuzikiuka na zimekataza kugawanyika na kutofautiana. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Hakika bila shaka mnao mfano mwema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa mwenye kumtarajia Mwenyezi Mungu na siku ya Mwisho na akamtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi." [Surat Ahzaab: 21] Na akasema Mtukufu: "Hakika walio igawa Dini yao na wakawa makundi makundi, huna uhusiano wowote nao." [Al-An'am: 159]. Na akasema Mtukufu: "Amewaamrisha Dini ile ile aliyomuusia Nuhu na tuliyokufunulia wewe, na tuliyowausia Ibrahim na Musa na Isa, kwamba shikeni Dini wala msifarikiane ndani yake." [Ash-Shuraa: 13].
Imesimuliwa kutoka kwa Jabir bin Abdallah, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Ama baada ya hayo. Hakika mazungumzo bora zaidi ni Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na uongofu bora zaidi ni uongofu wa Muhammad, na mambo maovu zaidi ni ya uzushi, na kila uzushi ni upotofu." (Imesimuliwa na Muslim katika (867), An-Nasa'i (1578), Abu Dawud (2954), na Ibn Majah (45).)
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Umma yangu wote wataingia katika Bustani za mbinguni isipokuwa wale watakaokataa." Wakasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nani atakataa?" Akasema: "Mwenye kunitii, ataingia katika Bustani za mbinguni. Na mwenye kuniasi, basi hakika amekataa." (Imesimuliwa na Bukhari 7280).
Imesimuliwa kutoka kwa Irbadh bin Sariya kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alituaidhi siku moja baada ya Swala ya Adhuhuri kwa mawaidha ambayo macho yetu yalilia kwa sababu yake, na nyoyo zetu zikaingiwa na hofu kwa sababu yake. Kwa hivyo, Mtu mmoja akasema: "Hakika, haya ni mawaidha ya anayeaga. Basi unatuusia nini ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema: "Ninawausia kumcha Mwenyezi Mungu, na kusikia na kutii. Hata kama itakuwa ni kumtii mtumwa Mhabeshi. Kwa maana, atakayeishi miongoni mwenu, ataona kutofautiana kwingi. Na jitahadharini na mambo ya uzushi. Hayo ni upotofu. Na mwenye kuishi akayafikia hayo miongoni mwenu, basi ashikamane na Sunna zangu na Sunna za Makhalifa wanyoofu waongofu. Zishikeni kwa magego." (Imesimuliwa na Abu Dawud (4607), Tirmidhi (2676), Ibn Majah (42), Ahmad (17416), Al-Darmi (96), na Tirmidhi alisema kwamba hadithi hii ni sahihi.)
Na alisema Bukhari katika "Sahih" yake katika Kitabu cha Kushikamana na Kitabu na Sunna: Mlango wa kuiga Sunna za Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, na kauli ya Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na Kutukuka: "Na utujaalie tuwe viongozi kwa wachamungu." [Al-Furqan: 74]. Akasema: "Viongozi ambao tunafuata mfano wa wale waliotutangulia, na wanatufuata watakaokuja baada yetu." Na Ibn Aun alisema: "Mambo matatu ninayapenda mimi mwenyewe, na ninawapendelea ndugu zangu: Sunna hii, kwamba wajifunze na kuuliza mambo hayo, na Qur'ani waifahamu na kuuliza juu yake, na waachane na mambo ya watu ila yale yenye heri." (Sahih Bukhari 8/139).
Mlango wa kumuamini Mwenyezi Mungu
Muhtasari wa Kitabu.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye wa kwanza, na hakuna kitu chochote mbele yake. Na yeye ni wa mwisho, na hakuna chochote baada yake. Na alitueleza juu ya nafsi yake kwamba yeye ndiye aliyeumba mbingu na dunia, na kwamba yeye ndiye mmiliki wa kweli wa mbingu na dunia, na anaingiza usiku katika mchana na anaingiza mchana katika usiku, ametakasika na ametukuka, na kwamba ulimwengu huu unaoshuhudiwa ni ushahidi kwamba yeye ndiye Muumba peke yake na hakuna Muumba mwingine pamoja naye.
Alitaja miongoni mwa ishara zake zinazoashiria kwamba yeye ndiye Muumba wa ulimwengu huu ishara nyingi ambazo haziwezi kudhibitiwa kwa idadi, na akatusimamishia hoja dhidi yetu kwa kile tunachokiona katika nafsi zetu na kile tunachokiona karibu nasi.
Na tunaamini kile ambacho Manabii na Mitume waliamini, na tuna yakini na kile walichokuja nacho miongoni mwa ushahidi na hoja zinazomuashiria Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na Kutukuka.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Muumba, na hakuumba viumbe wake bure. Bali ulikuwa uumbaji wa ustadi kwa sababu ya kusudio kubwa.
Pamoja na yasiyokuwa hayo miongoni mwa yale yanayotajwa mara nyingi katika Qur'ani Tukufu - kama ilivyo katika "Surat Al-An'am" na "An-Nahl" na nyinginezo - miongoni mwa ushahidi usiohesabika, na hoja zisizodhibitika, ambazo zote ni ushahidi juu ya kuwepo kwake na umola wake, na ni ushahidi wa kiakili, na hoja kubwa, hakuna mtu anayeweza kuja na mfano wake au hata kinachozikaribia. Nazo katika utofauti wake zinafaa kwa viumbe vyote, na zinatosha kusimamisha hoja dhidi yao, hata kama makafiri watakataa, na watu wa batili wakachukia. Na je, makafiri wana ushahidi wowote isipokuwa kukanusha tu na kukataa?!
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika umola wake, na kwamba Yeye pekee ndiye Muumba, na kwamba Yeye ndiye aliyeanzisha uumbaji na hakuna mtu aliyeshiriki katika uumbaji huo pamoja naye, na kwamba Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka huumba kwa amri yake kupitia sababu anazozitaka, na kwamba kila kitu kinginecho kisichokuwa Yeye kimeumbwa.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mola Mlezi wa kila kitu, muumbaji wake, mwendeshaji wake, na mmiliki wake, na Yeye ndiye anayevipeleka atakavyo, na hakuna kiumbe yeyote aliye na uwezo wa kuendesha jambo lake mwenyewe, au kuendesha jambo la wengine isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu amemuwezesha.
Na tunaamini kwamba yeye ndiye mmiliki wa haki, na kila kitu kisichokuwa Yeye kinamilikiwa, na kila mmiliki, umiliki wake huo ni batili au ni wa muda tu na utaondoka.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu pekee ndiye anayefufua watu, na kwamba yeye ndiye aliyeumba mauti na uhai, na kwamba yeye ndiye anayefisha nafsi.
Na tunaamini kwamba yeye ndiye anayeruzuku, mwenye nguvu, aliye madhubuti, na hakuna mwingine anayeruzuku kando na yeye, wala hakuna anayetosheleza asiyekuwa yeye. Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu amezunguka kila kitu kwa elimu, kwa hivyo hakitoki nje ya elimu yake kitu kidogo au kikubwa, na kwamba yeye Mtukufu ndiye ajuaye ghaibu na yanayoonekana.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu ameshinda kila kitu kwa nguvu na hukumu.
Na tunaamini kwamba Mola wetu Mlezi Mtukufu ni wake Uumbaji na amri, na hakuna mola mwingine, wala mwengine anayetunga sheria. Yeye ndiye aliyeumba viumbe, na akaweka sheria, na akaamrisha mambo ya lazima, na akaibainisha dini naye ndiye mmiliki wao, na Yeye peke yake ndiye anayeweza kuwafanyia hesabu na kuwalipa.
Na tunaamini kwamba Mola wetu Mlezi ndiye aliyewaumba waja, na ndiye aliyeumba matendo yao.
Na tunaamini kwamba kuamini Umola wa Mwenyezi Mungu pekee haitoshi kwa mtu kuwa muumini, na imani hii haimuingizi mtu katika Bustani za mbinguni; kwa sababu hakuamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muabudiwa wa haki, kwamba hafai kuabudiwa isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee.
Tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika uungu wake, na kwamba hakuna mungu mwingine ila Mwenyezi Mungu peke yake, na kwamba hana mshirika, na kwamba yeye ndiye wa haki, na kwamba vile wanavyoomba kando na yeye ni batili. Jambo hili kubwa ndilo kwa ajili yake Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu, na akatuma Mitume, na akaumba Bustani za mbinguni na Moto, na wanazuoni wote wamekubaliana juu yake, na umbile la asili likalionyesha, na akili timamu zikalishuhudia. Na tunajua kwa elimu ya yakini kwamba msingi wa wito wa manabii kwa watu wao ni kuwaita katika kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuacha kuabudu vinginevyo.
Ibada ya kweli ni ile iliyokusudiwa Mwenyezi Mungu tu, Mola Mlezi wa viumbe vyote, kwa mujibu wa muongozo wa bwana wa Mitume; kwani ibada ya kila anayeabudiwa asiyekuwa Yeye ni batili.
Nguzo hii, ni nguzo kubwa na ya msingi na thabiti katika dini ya Mwenyezi Mungu - ambayo ni kuthibitisha uungu wa Mwenyezi Mungu peke yake na kukataa ibada ya kitu kingine chochote - na ndiyo kiini cha dini, na nguzo ya wito wa mitume, na maana yake ni kumpwekesha Muumba kwa matendo ya viumbe.
Katika Qur'ani, Mwenyezi Mungu mara nyingi anaweka hoja mbele ya waja wake kwa kutumia ishara za umola wake ambazo zinalazimu kumwabudu Yeye pekee, Mtukufu.
Na tunaamini kwamba Muumba wa ishara hizi kuu za kiulimwengu ni Mwenyezi Mungu, na kama vile hakuna muumba pamoja naye, basi pia hakuna mwingine anayepaswa kuabudiwa zaidi yake.
Na Mwenyezi Mungu ametofautisha katika ushahidi aliouweka juu ya uungu wake kwa njia ambayo hoja inawasimamia viumbe na njia inakuwa wazi kwazo, ili watu wasiwe na hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu.
Na kukiri uungu kwa Mwenyezi Mungu, pamoja na kushuhudia kuwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - ni Mtume, ndilo jambo ambalo Mwenyezi Mungu alilifanya kuwa mpaka kati ya imani ya mwanadamu kwa Mwenyezi Mungu na ukafiri.
Na ili kumuamini Mwenyezi Mungu, ni lazima kukufuru Taghuti (Vyenye kuabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu), na kujiweka mbali na ushirikina na washirikina.
Imani hii haitoshi kuwa moyoni tu, lakini lazima itamkwe kwa ulimi, na imani hii haipatikani hadi aifanyie matendo kwa viungo, na imani moyoni inatofautiana, kuna wakati huzidi na kuna wakati hupungua.
Na mja anapaswa kumkusudia Mwenyezi Mungu tu Mola Mlezi wa walimwengu katika Imani, na kwamba awe mnyoofu bila kuwa na shaka, na kwamba imani yake itokane na kuwa na elimu, ikhlas, kukubali, kujisalimisha, kufuata, na ukweli katika kauli yake, matendo yake, na itikadi yake, pamoja na kuipenda dini hii, na yule aliyeiweka kuwa Sheria, yule aliyekuja nayo, na yeyote anayeifuata.
Na kama vile Mwenyezi Mungu alivyobainisha uhakika wa imani na yale yanayohitajika, na nguzo zake na masharti yake. Alivunjilia mbali itikadi potofu za washirikina wanaopinga, na akabainisha kuwa hawana hoja juu ya ushirikina wao huo, kwa sababu masanamu yao hayo yaliumbwa na yanaendeshwa, hayaumbi chochote, wala hayamiliki uzito wa punje ndogo mbinguni wala duniani.
Na Mwenyezi Mungu alibainisha kuwa washirika hawa wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu hawasikii maombi ya wale wanaowaomba, na hata kama wangesikia, wasingeliwaitikia, na Siku ya Kiyama wataukataa ushirikina wao huo, na watajiweka mbali nao.
Kama vile alivyobainisha kwamba washirika hawa wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu hawanufaishi wala hawadhuru, basi vipi wanaabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu?!
Na Mwenyezi Mungu alibatilisha kuabudiwa kwa Malaika, na akabainisha kwamba - ingawa wako karibu na Mwenyezi Mungu - lakini hawafanyi uombezi isipokuwa baada ya idhini yake. Kwa hivyo ikiwa hii ndiyo hali ya Malaika, basi vipi wataabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu?!
Na Manabii na Mitume, amani iwe juu yao - pamoja na nafasi za juu walizonazo duniani na Akhera - lakini hawamilikii manufaa wala madhara juu ya nafsi zao. Basi vipi kwa wengineo?!
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika sifa zake za ukamilifu na ukuu wake, na kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu ana majina mazuri zaidi na sifa za juu zaidi, akili kamilifu zinashuhudia hili, na umbile la asili linajisalimisha kwake kuhusiana na hilo, na wanazuoni wa Umma huu wa kiislamu wamekubaliana juu ya hilo. Bali jumbe zote za Mwenyezi Mungu zilikuja ili kubainisha sifa za Mwenyezi Mungu na majina yake na matendo yake. Na Mwenyezi Mungu aliwaonyesha kasoro za miungu ya washirikina kwamba haisikii na haioni.
Na tunaamini kwamba kama alivyojielezea mwenyewe, na kama alivyoelezewa na Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, yeye Mtukufu hana kitu mfano wake naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona. Kwa hivyo tunapaswa kumthibitishia Mwenyezi Mungu kile alichojithibitishia yeye mwenyewe au Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na tunakanusha juu yake kile alichojikanushia mwenyewe, au Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, bila ya kuzikana sifa zake, wala kuzifananisha na sifa za viumbe, wala kuuliza namna yake ikoje, wala kuzipotosha.
Na tunajua kwa yakini kwamba Mola wetu Mlezi alisifika kwa sifa zake kabla ya kuumba viumbe, na kwamba yuko katika kiwango cha juu zaidi cha ukamilifu, utukufu, na uzuri kutokea zamani hadi milele; kwa kuwa yeye ndiye wa kwanza na wa mwisho. Yeye ndiye wa kwanza ambaye hakuna chochote mbele yake, na ni wa mwisho ambaye hakuna chochote baada yake. Yeye ndiye wa kwanza kwa majina yake na sifa zake za ukamilifu na utukufu, na ni wa Mwisho kwa majina yake na sifa zake za ukamilifu na utukufu.
Na tunaamini kwamba baadhi ya sifa za Mwenyezi Mungu ni sifa zisizoachana naye, kama vile uhai, elimu, kusikia, kuona, mkono, na vidole, na kwamba baadhi ya sifa zake zinahusiana na utashi wake, kama vile hasira, kuridhia, na kushuka.
Na tunaamini kuwa yeye ndiye anayefanya anachotaka. Anafanya apendapo, apendacho, apendavyo. Humtukuza amtakaye, na humuangusha amtakaye, na hakuna anayeweza kurudisha amri yake, wala wa kuhukumu baada ya maamuzi na hukumu yake (wa kukata rufaa).
Na tunaamini kwamba sifa za Mwenyezi Mungu ziko zilizokuja pasina kikomo, kwa hivyo tutamsifu Mwenyezi Mungu pasina kikomo kama zilivyokuja, kama kusikia, na uhai, na kuona, na sifa zinginezo, na ziko zilizotajwa kwa kikomo, kwa hivyo zitabakia katika kikomo chake, kama kumsifu Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwa yeye hupanga njama dhidi ya maadui zake pale wanapopanga njama, na anawasahau maadui zake pale wanapomsahau.
Na miongoni mwa sifa zake ni: Elimu, kusikia, kuona, uhai, usimamizi, na kuzungumza, naye anasifika kwa sifa ya kuzungumza kabla ya kuumba viumbe na kuwazungumzisha, na maneno ya Mola wetu Mlezi yanaambatana na matashi yake, kwa hivyo wakati wowote anapotaka anazungumza. Na habari kuhusu sifa ya kuzungumza kwa Mwenyezi Mungu imetajwa katika Qur'ani kwa njia nyingi. Ikatajwa kuwa huwasemesha waja wake, na humnong'oneza na kumuita amtakaye miongoni mwao, na atawasemesha viumbe siku ya Kiyama, na viumbe watasikia maneno ya Mwenyezi Mungu siku ya Kiyama.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu amejificha dhidi ya viumbe wake kwa pazia la nuru, kwa hivyo hawawezi kumuona duniani, hata kama baadhi ya Manabii Wake walisikia maneno Yake alipozungumza nao kutoka nyuma ya pazia, kama alivyomsemesha Musa, amani iwe juu yake.
Na maneno ya Mola wetu Mlezi husifika baadhi yake kuwa ni mapya kuliko mengine, na baadhi yake ni bora kuliko mengine.
Na miongoni mwa maneno yake ni: Qur'ani, na vitabu vyote vya kiungu vilivyoteremshwa kwa Mitume wake, kama vile nyaraka za Ibrahimu na Musa, Torati, Injili, na Zaburi - vyote ni maneno ya Mwenyezi Mungu, na vyote hivyo Mwenyezi Mungu alizungumza, na maneno hayo akayasikia Jibrili pasina muwakilishi, na Jibrili akayateremsha kwa Manabii wa Mwenyezi Mungu na Mitume wake, amani iwe juu yao. Torati ilitofautishwa na vitabu vingine kwakuwa Mwenyezi Mungu aliiteremsha ikiwa imeandikwa katika vibao - na ni maneno ya Mwenyezi Mungu na ibara Zake, wala hayakuumbwa, na maneno ya Mwenyezi Mungu ni tofauti na viumbe vyake, je! Huoni kwamba alitenganisha kati ya uumbaji na amri, na tunatofautisha kati ya maneno ya Mwenyezi Mungu ya kiulimwengu na maneno Yake kisheria.
Na miongoni mwa sifa zake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni: Utukufu (Izza), utenzaji nguvu, Ujabari, Ufalme wa juu, Kiburi, Utukufu (Adhwama), Uendeshaji, na matashi, na uwezo na huruma, na huruma hii ni moja ya sifa zake, nayo inaambatanishwa kwa Mwenyezi Mungu, yaani kuambatanisha sifa kwa msifiwa.
Na miongoni mwa sifa zake: Ni kuwa juu, nako ni kuwa juu kwa utenzaji nguvu, na kuwa juu kwa cheo, na kuwa juu kwa dhati, zote hizi tatu ni sifa zake zinazoonyesha ukamilifu wake. Na imeonyesha Qur'ani tukufu na Sunna tukufu ya Mtume na akili na maumbile vyote vinathibitisha juu ya kuwa kwake juu kwa njia mbali mbali, bali ushahidi unaoonyesha kwamba Mwenyezi Mungu yuko juu uko aina nyingi, na chini ya kila aina kuna vipengele visivyohesabika.
Na miongoni mwa sifa zake Aliyetakasika na kutukuka ni: Kuwa juu ya kiti cha enzi (Arshi), na Mwenyezi Mungu ameitaja sifa hii katika maeneo saba ndani ya kitabu chake.
Na miongoni mwa sifa zake ni: Upendo. Na katika sifa zake pia ni: Kuridhia. Na miongoni mwa sifa zake pia ni: Kuwachukia kwake maadui zake; hiyo ni kwa sababu walichukia radhi zake, na wakachukia aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake rehema na amani ziwe juu yake.
Na miongoni mwa sifa zake ni: Hasira dhidi ya adui zake na kuchukizwa: Nako ni kuwachukia kwake makafiri.
Na miongoni mwa sifa zake ni: Kuwachukia maadui zake wanaowachukia vipenzi vyake. Na miongoni mwake ni: Kusikitika nayo ni hasira kali. Na miongoni mwa sifa zake ni: Kumhadaa anayemhadaa, Mwenyezi Mungu anawahadaa wanafiki wanaomhadaa. Na katika sifa zake Mtukufu ni kwamba anamdhihaki anayemdhihaki, Ametakasika na Kutukuka.
Na miongoni mwa sifa zake ni kucheka, kustaajabu, na kuja Siku ya Kiyama ili kutoa hukumu kati ya watu.
Na tunaamini sifa ya kushuka, na kuwa Mola wetu Mlezi anashuka hadi mbingu ya dunia kushuka halisi kunakoendana na utukufu wake na ukuu wake, nako si sawa na kushuka kwa viumbe, lakini hii ni kama sifa zingine zote ambazo tunaziamini, na tunazijua, na wala hatujiingizi kutaka kujua namna ya ushukaji wake, au kujilazimisha kuikataa sifa hii; bali tunaiamini kama ilivyoelezwa na Mtume wetu mkweli mwenye kusadikishwa, rehema na amani ziwe juu yake.
Na tunaamini sifa ya Mwenyezi Mungu ya kuwa pamoja na waja wake Mola Mlezi wa walimwengu, na kwamba Mwenyezi Mungu yuko pamoja na viumbe vyake. Na kuwa pamoja huku kuna aina mbili: Upamoja maalum, na huu unakuwa kwa vipenzi wa Mwenyezi Mungu na Mitume wake, amani iwe juu yao, na malengo yake ni kuwapa ushindi na msaada, na upamoja wa jumla wa kuwa pamoja na viumbe wote, waumini na makafiri, na lengo lake ni: Elimu (kuwajua), na kuwazingira, na uwezo, na mamlaka.
Na upamoja huu haulazimu kuingia ndani wala kujichanganya pamoja nao, na wala haupingani na kuwa juu kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu; kwa sababu maana yake kwa itifaki ya wanachuoni ni: Kuwa na elimu (ya matendo yao) na kuwazingira; yaani: Mwenyezi Mungu yuko pamoja nasi kwa elimu yake, kutuzingira kwake na uwezo wake.
Na tunamthibitishia Mwenyezi Mungu kuwa ana uso unaonasibiana na utukufu wake na ukuu wake, na mkono unaoendana na utukufu wake na ukamilifu wake, na imekuja habari kuhusu mkono katika Qur'ani na Sunna kwa namna nyingi. Kuna wakati mikono imetajwa miwili, na kwamba Mwenyezi Mungu huikunja na kuikunjua, na kwamba Mola Mlezi atazikunjakunja mbingu kwa mkono wake, na Ardhi atakuwa kaikamata Mtukufu, na kuwa mkono umesifika kuwa una vidole. Na yote haya yanathibitisha kuwa mkono ulioelezwa katika Qur'ani na Sunna ni mkono halisi unaostahili utukufu wake, na wala hatujisumbui kuufasiri, kuulinganisha, au kupotosha aya na hadithi zinazoonyesha juu ya hilo. Na miongoni mwa sifa zake ni: Sifa ya vidole.
Na tunaamini kuwa waumini watamuona Mola wao Mlezi siku ya Kiyaama, na hili limethibitishwa na Kitabu (Qur'ani), na habari za Mtume wetu rehema na amani ziwe juu yake zimekuja kwa wingi katika yale aliyowapa habari njema waumini kuwa watamuona wazi kwa macho Mola wao Mlezi siku ya Kiyama.
Kama alivyojisifu mwenyewe kwa sifa za ukamilifu, uzuri, utukufu, na ukuu na kiburi, basi pia amekana sifa za kutokamilika, na kukanusha katika sifa, si asili ndani ya Qur'ani na Sunna; kwa sababu asili ni kuthibitisha sifa, na Qur'ani na Sunna zimejaa kuweka wazi sifa za Mwenyezi Mungu Mtukufu, kama inavyotakiwa katika utukufu wake na ukuu wake na ukamilifu wake, na Mola Mlezi Aliyetakasika na kutukuka, anapokanusha sifa yoyote juu ya nafsi yake, basi anaikanusha ima; kwa kuonyesha ukamilifu wa kinyume chake, au ni kwa sababu wanadamu wamemnasibishia mapungufu mwenye Utukufu na ukamilifu, hapo Mola Mlezi hukanusha mapungufu yaliyohusishwa kwake.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ana majina mazuri zaidi, na kuwa majina yake yamefikia kilele cha uzuri, hakuna majina bora kuliko hayo, na kila jina la Mwenyezi Mungu ndani yake kunapatikana sifa, na majina yake hayana kikomo cha idadi maalum.
Mola wetu Mlezi ametuonya dhidi ya kukanusha majina yake au kuyapinga, au kukataa maana zake, au kukataa kuwa hana majina wala sifa.
Yaliyotajwa katika Qur'ani na Sunna miongoni mwa majina na sifa za Mwenyezi Mungu ni makubwa zaidi kuliko kuzungukwa kitabu hicho na majina na sifa hizo, na sisi tunaamini majina haya na sifa hizi kwa namna aliyoikusudia Mola wetu Mlezi, na kwa namna aliyomaanisha Mtume wetu, rehema na amani zimshukie, na tunajua kwamba uhalisia wake hakuna mwanadamu aujuaye, na wala hawawezi kuuelewa kikamilifu, na wala akili zao haziwezi kuufikia, na wala hatujisumbui kuufasiri.
Mlango wa kuamini uwepo wa Mwenyezi Mungu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye wa kwanza na hakuna kitu kabla yake. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Yeye ndiye wa Mwanzo na ndiye wa Mwisho, naye ndiye wa Dhahiri na wa Siri." [Al-Hadid: 3] Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Mwenyezi Mungu alikuwako, wala hapakuwapo na kitu kingine kabla yake, na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji." (Imepokelewa na Bukhari 7418, na At-Tirmidhi 3951). Bukhari aliipokea miongoni mwa hadithi za 'Imran bin Husawin, na katika simulizi yake - pia kuna kwamba: "Mwenyezi Mungu alikuwako, wala hapakuwapo na kitu kingine ila Yeye, na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji." (Imepokelewa na Bukhari 3191). Na alijitambulisha kwetu kwamba yeye ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi, na kwamba yeye ndiye mmiliki wa mbingu na ardhi, na kwamba anauingiza usiku katika mchana, na anauingiza mchana katika usiku. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yeye ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita; kisha akatulizana juu ya kiti cha enzi. Anayajua yanayoingia katika ardhi na yanayotoka humo, na yanayoteremka kutoka mbinguni, na yanayopanda humo. Naye yu pamoja nanyi popote mlipo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona mnayoyatenda * Ufalme wa mbingu na ardhi ni wake. Na mambo yote yanarejeshwa kwa Mwenyezi Mungu * Anaingiza usiku katika mchana, na anaingiza mchana katika usiku. Na Yeye ni Mwenye kuyajua yaliomo vifuani." [Al-Hadid: 4-6].
Na Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka, alisisitiza kwamba ulimwengu huu unaoshuhudiwa ni ushahidi kwamba Yeye pekee ndiye Muumbaji, na hakuna Muumbaji mwingine pamoja naye. Amesema Mwenyezi Mungu: "Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye!?" [Luqman: 11] Na ndiyo maana alitaja ishara zake nyingi zinazoonyesha kwamba yeye ndiye Muumba wa ulimwengu huu. Miongoni mwake ni kwamba humtoa aliye hai kutoka kwa mfu, na hutoa mfu kutoka kwa aliye hai. Na miongoni mwake ni kwamba aliumba wanadamu kutokana na udongo. Na miongoni mwake ni kuwa alituumbia wake kutokana na sisi wenyewe. Na miongoni mwake ni tofauti za lugha na rangi za viumbe. Na miongoni mwake ni kulala kwa waja na kutafuta kwao riziki mchana. Na miongoni mwake ni kwamba hufanya umeme kuwa ni sababu ya hofu na matumaini, na kwamba hushusha maji kutoka mbinguni. Na miongoni mwake ni kwamba Yeye ndiye aliyeanzisha uumbaji, kama alivyosema Yeye Mtukufu Msifwa: "Hukitoa kilicho hai kutokana na kilicho kufa, na hukitoa kilicho kufa kutokana na kilicho hai. Na huihuisha ardhi baada ya kufa kwake. Na hivyo ndivyo mtakavyo fufuliwa * Na katika Ishara zake ni kuwa kakuumbeni kwa udongo. Kisha mkawa watu mliotawanyika kote kote * Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanaofikiri * Na katika Ishara zake ni kuumba mbingu na ardhi, na kutofautiana ndimi zenu na rangi zenu. Hakika katika hayo zipo Ishara kwa wajuzi * Na katika Ishara zake ni kulala kwenu usiku na mchana, na kutafuta kwenu fadhila zake. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanaosikia * Na katika Ishara zake hukuonyesheni umeme kwa kukutieni hofu na tamaa. Na hukuteremshieni maji kutoka mbinguni, na kwa hayo huifufua ardhi baada ya kufa kwake. Hakika katika hayo zipo Ishara kwa watu wanaozingatia * Na katika Ishara zake ni kuwa mbingu na ardhi zimesimama kwa amri yake. Kisha atakapo kuiteni mwito mmoja tu, hapo mtatoka kwenye ardhi * Na ni vyake Yeye vilivyo mbinguni na katika ardhi. Vyote vinamtii Yeye * Na Yeye ndiye anayeanzisha uumbaji, kisha ataurudisha mara nyingine. Na jambo hili ni jepesi zaidi kwake." [Ar-Rum: 19-27].
Na katika hilo pia ni kwamba alisimamisha hoja juu ya viumbe kwamba yeye ndiye aliyewaumba kutoka katika nafsi moja. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Amewaumba nyinyi kutokana na nafsi moja. Kisha akamfanya mwenziwe katika nafsi ile ile. Na akawaletea wanyama wa mifugo jozi nane. Anawaumba katika matumbo ya mama zenu, umbo baada ya umbo, katika viza vitatu. Huyu ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi. Ufalme ni wake. Hapana mungu isipokuwa Yeye. Basi nyinyi mnageuzwa wapi?" [Az-Zumar: 6] Akataja mwanzo wa uumbaji, na kwamba wanyama wote kawaumba Yeye, kisha akasimamisha hoja dhidi yetu kwamba alituumba katika matumbo ya uzazi katika giza mbalimbali, na kwamba hakuna mwingine asiyekuwa yeye anayeweza kuumba manii yawe mwanadamu.
Kwa hivyo, katika aya zilizotangulia, alitaja uthibitisho mkubwa zaidi wa uwepo wake - ambao ni kuumba kwake mbingu na ardhi na vilivyomo na vilivyo kati yake.
Na katika hilo pia ni kwamba alisimamisha hoja juu ya viumbe kwa ushahidi wa utunzaji wake kwao na kile wanachokipata katika nafsi zao na vizazi vyao. Na hilo ni kwamba aliwatoa katika matumbo ya mama zao hali ya kuwa hawajui kitu kisha akawatunza hadi wakakamilika katika maumbile yao na elimu yao. Amesema Yeye Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu amewatoa matumboni mwa mama zenu, hali ya kuwa hamjui kitu, na amewajaalia masikio na macho na nyoyo ili mpate kushukuru." [An-Nahl: 78]. Na kama vile alivyoumba kila kitu na kukitayarisha, basi aliongoza viumbe wake wote kufikia yale yenye masilahi yao. Amesema Mtukufu akieleza kuhusu Firauni kwamba alisema: "(Firauni) akasema: Basi Mola wenu Mlezi ni nani, ewe Musa?" [Twaha: 49] Kisha likawa jibu la kimungu ni: "Akasema: Mola wetu Mlezi ni yule aliye kipa kila kitu umbo lake, kisha akakiongoa." [Taha: 50].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu aliitandaza ardhi, na akaiweka milima madhubuti juu yake, na akaotesha ndani yake kila kitu kwa kiasi chake. Kwa hivyo, uwiano unaoshuhudiwa ndani yake ni ushuhuda bora zaidi kwamba Yeye ndiye Muumba, kama vile kuteremsha mvua katika hali maalumu ambayo wanadamu hawawezi kuiteremsha hivyo, wala hata kuhifadhi kile kilichoteremka kutoka mbinguni, ni ushahidi kwamba Muumba ni Mwenyezi Mungu Mmoja tu, Mshindi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ardhi tumeitandaza na humo tumeweka milima, na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake * Na tumewajaalia nyinyi vitu vya maisha yenu, na vya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku * Na hakuna chochote ila asili yake inatokana na Sisi; wala hatukiteremshi ila kwa kipimo maalumu * Na tunazipeleka pepo za kupandishia, na tunateremsha kutoka mbinguni maji, kisha tukakunywesheni maji hayo. Wala si nyinyi mnaoyaweka." [Al-Hijr: 19-22].
Na tunayaamini yale ambayo Manabii na Mitume waliyaamini, na tuna yakini katika ushahidi na uthibitisho waliokuja nao, wenye kumuelezea Yeye Aliyetakasika na kutukuka, kama alivyoeleza Mola wa Haki kwamba Ibrahim, amani iwe juu yake, alisimamisha hoja dhidi ya Nimrud kwamba Mwenyezi Mungu huleta jua kutoka Mashariki na wengine hawawezi kulileta kutoka Magharibi kwenda Mashariki. Amesema Yeye Mtukufu: "Ibrahim aliposema: Mola wangu ni yule ambaye huhuisha na kufisha. Na (Nimrodi) akasema: Mimi pia nahuisha na kufisha. Ibrahim akasema: Mwenyezi Mungu hulichomozesha jua Mashariki, basi wewe lichomozeshe Magharibi." [Al-Baqarah: 258].
Pia alisimamisha hoja dhidi ya watu wake kwamba ni Mwenyezi Mungu aliyemuongoa, akamlisha na kumpa maji, na anapo ugua anamponya, na kwamba Yeye ndiye anayemfanya afe na kumhuisha. Akasema kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza: "Ambaye aliyeniumba mimi, na Yeye ndiye ananiongoa * Na ambaye ndiye ananilisha na kuninywesha * Na ninapougua, ni Yeye ndiye anayeniponya * Na ambaye atanifisha, na kisha atanihuisha." [Ash-Shu'ara: 78-81] Na akasema akieleza kuhusu Musa, amani imshukie, kuwa alijadiliana na Firauni akamwambia kuwa Mola wake Mlezi ni: "Yule aliyekipa kila kitu umbo lake, kisha akakiongoa." [Twaha: 50] Na imekuja katika Qur'ani kwamba Mwenyezi Mungu alijitakasa nafsi yake kutokana na kila upungufu, na akajitambulisha kwetu. Akasema aliyetakasika na kutukuka: "Litakase jina la Mola wako Mlezi aliye juu kabisa * Aliyeumba, na akaweka sawa * Na ambaye amekadiria na akaongoa." [Al-A'ali: 1-3].
Na Mwenyezi Mungu aliyetakasika alisimamisha ushahidi kuwa Yeye ndiye Muumba wa ulimwengu huu na hakuna muumba mwingine, kwamba yeye ndiye aliyeotesha bustani nzuri nzuri, na kwamba wanadamu hawawezi kuotesha miti yake. Pia alisimamisha hoja juu ya hilo kwamba aliifanya ardhi kuwa thabiti, na akafanya ndani yake mito na milima madhubuti, na akaweka kizuizi kati ya bahari mbili; ili hii isije ikachanganyika na hii. Na kwamba yeye peke yake ndiye anaye mjibu mwenye shida kubwa anapomuomba - hata kama si muumini - na kwamba yeye ndiye anayewaongoza watu katika viza vya nchi kavu na baharini, na kwamba yeye ndiye anayetuma pepo kuwa bishara njema kabla ya mvua, na kwamba yeye ndiye anayeturuzuku, hakuna mwingine mwenye kuruzuku, wala Mola mlezi mwingine, wala Muumba mwingine yeyote. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Au ni nani yule aliyeziumba mbingu na ardhi, na akawateremshia maji kutoka mbinguni, na kwa hayo tukaziotesha bustani zenye kupendeza? Nyinyi hamna uwezo wa kuiotesha miti yake. Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali hao ni watu waliopotoka * Au ni nani aliyeifanya ardhi mahali pa kutua, na akajaalia ndani yake mito, na akaweka milima madhubuti? Na akaweka baina ya bahari mbili kizuizi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali wengi wao hawajui * Au ni nani anayemjibu mwenye shida kubwa pale anapomuomba, na akaiondoa dhiki, na akawafanya nyinyi warithi wa ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ni machache tu mnayoyazingatia * Au ni nani yule anayewaongoa nyinyi katika viza vya bara na bahari, na akazipeleka pepo kuleta bishara njema kabla ya rehema zake? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ametukuka Mwenyezi Mungu juu ya hao wanaowashirikisha naye * Au ni nani anayeuanzisha uumbaji, kisha akaurejesha? Na ni nani anayewaruzuku nyinyi kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Sema, "Leteni hoja zenu kama nyinyi ni wakweli." [An-Naml: 60-64].
Na amesema Mola Mwenye sifa tukufu, na Mwenye majina matukufu: "Naye ndiye aliyeitandaza ardhi na akaweka humo milima na mito. Na katika kila matunda akafanya dume na jike. Huufunika usiku juu ya mchana. Hakika katika haya zimo Ishara kwa watu wanaotafakari * Na katika ardhi vimo vipande vilivyokaribiana, na zipo bustani za mizabibu, na mimea mingine, na mitende yenye kuchipua kwenye shina moja na isiyochipua kwenye shina moja, nayo inatiliwa maji yale yale. Na tunaifanya baadhi yake kuwa bora kuliko mingine katika kula (Ladha). Hakika katika hayo zimo ishara kwa watu wanaotia mambo akilini." [Ar-Ra'd: 3, 4]. Kwa hivyo Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka akathibitisha kwamba Yeye pekee ndiye aliyeitandaza ardhi, na akaumba kwa jozi (pea) miti yote na matunda, na kwamba Yeye peke yake ndiye anayefunika usiku juu ya mchana. Alisimamisha hoja juu ya hilo kwamba vipande vya ardhi vilivyokaribiana vinaotesha matunda yanayofanana na yasiyofanana ilhali hunyweshwa maji yale yale, kwa hivyo Mwenyezi Mungu ametakasika, ambaye hakuna Mola Mlezi mwingine, wala Muumba mwingine asiyekuwa yeye.
Na alibainisha kwamba milima - pamoja na uthabiti wake - ina uumbwaji wa ajabu, ambao unaonyesha ubunifu wa Muumba. Amesema Mtukufu: "Na katika milima imo mistari ya rangi nyeupe na nyekundu yenye rangi mbali mbali, na myeusi sana." [Fatwir: 27].
Na katika hayo ni yale ambayo Mwenyezi Mungu Mtukufu alitubainishia kwamba yeye ndiye aliyeumba hawa walimwengu, na akawatiisha kwa ajili ya mwanadamu, kama vile kuzipeleka safina baharini. Amesema Mola wa haki, mwenye sifa za utukufu: "Mwenyezi Mungu ndiye aliyeifanya bahari iwatumikie nyinyi, ili humo zipite marikebu (Safina) kwa amri yake, na ili mtafute katika fadhila zake, na mpate kushukuru * Na amefanya viwatumikie vilivyomo mbinguni na vilivyomo katika ardhi, vyote vimetoka kwake. Hakika katika hayo zimo Ishara kwa watu wanaotafakari." [Al-Jathiya: 12, 13].
Na Mwenyezi Mungu alituonyesha uwepo wake kwa kututengenezea kutoka kwa wanyama hawa wa mifugo vipando, mavazi, vyakula na vinywaji, na kwamba anawashikilia ndege angani. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, hawawaoni ndege walivyo watiifu katika anga la mbingu? Hapana mwenye kuwashikilia isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hakika katika haya zipo ishara kwa watu wanaoamini * Na Mwenyezi Mungu amewajaalia nyinyi majumba yenu yawe ni maskani yenu, na amewajaalia kutokana na ngozi za wanyama nyumba mnazoziona nyepesi wakati wa safari zenu na wakati wa kutua kwenu. Na kutokana na sufi zao na manyoya yao na nywele zao mnafanya matandiko na mapambo ya kutumia kwa muda * Na Mwenyezi Mungu amewafanyia vivuli katika vitu alivyoviumba, na amewafanyia maskani milimani, na amewafanyia nguo za kuwakinga kutokana na joto, na nguo za kuwakinga katika vita vyenu. Ndivyo hivyo anawatimizia neema zake ili mpate kutii." [An-Nahl: 79-81]. Yote haya ni ushahidi wa uwepo wake na umola wake. Ni nani mwingine aliyeviumba isipokuwa Yeye, Mtakatifu?! Hakuna mwingine aliyeviumba asiyekuwa Yeye, wala hakuna Mola Mlezi mwingine isipokuwa Yeye.
Na alisimamisha ushahidi mkubwa ambao unajirudia rudia kila siku, ukishuhudia uwepo wake na ukuu wake Yeye Aliyetakasika na kutukuka. Na ushahidi huo ni kwamba Yeye ndiye anayepambazua mwangaza wa asubuhi, na ndiye mpasuaji mbegu na kokwa, zikachipua. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu ndiye mpasuaji mbegu na kokwa, zikachipua. Humtoa aliye hai kutokana na maiti, naye ni mtoaji maiti kutokana na aliye hai. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu. Basi vipi mnageuzwa? Ndiye anayepambazua mwangaza wa asubuhi; na ameufanya usiku ni kwa ajili ya mapumziko na utulivu, na jua na mwezi kwenda kwa hesabu. Hayo ndiyo makadirio ya Aliyetukuka, Mwenye nguvu, Ajuaye zaidi." [Al-An 'am: 95, 96].
Na kama vile alivyofanya jua na mwezi kuwa ni ishara mbili, aliufanya usiku na mchana kuwa ni ishara za kuwepo kwake na umola wake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tumefanya usiku na mchana kuwa ishara mbili. Tena tukaifuta ishara ya usiku, na tukaifanya ishara ya mchana ni yenye mwangaza." [Al-Al-Israa: 12].
Na Yeye Mtukufu alibainisha kwamba kufanya kwake bahari moja kuwa ni tamu na nyingine ya chumvi chungu, na kwamba zinatoka humo nyama laini na tamu - ni ushahidi juu ya kuwepo kwake. Amesema Mtukufu: "Yeye ndiye aliyeifanya bahari iwatumikie, ili kutokana na humo mpate kula nyama laini, na mtoe humo mapambo mnayoyavaa. Na unaona merikebu (Safina) zikikata maji humo." [An-Nahl: 14] Na amesema Mol wa Haki, Mtukufu: "Naye ndiye aliyeziunganisha bahari mbili, hii tamu inayoondoa kiu, na hii ni ya chumvi kali. Na akaweka baina yake kinga na kizuizi kizuiacho." [Al-Furqan: 53].
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alibainisha kwamba akili salama zinatambua kwamba ulimwengu huu usingeweza kupatikana bila ya kuwepo mwenye kuumba. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Yeye ndiye anayehuisha na kufisha, na yake Yeye mabadiliko ya usiku na mchana. Basi je! Hamtumii akili?" [Muminun: 80] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Akasema: Basi nyinyi mnawaabudu wasiokuwa Mwenyezi Mungu wasiowafaa kitu wala kuwadhuru? * Aibu yenu nyinyi na hivyo mnavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu! Basi nyinyi hamtii akilini?" [Al-Anbiyaa: 66, 67]. Je! Umeona ishara kubwa kuliko hizi zinazoonyesha uwepo wake na umola wake, Yeye Aliyetakasika na Kutukuka?!
Mwenyezi Mungu aliwapinga wale waliofungamanisha uumbaji na wengine wasiokuwa Yeye, na akawauliza swali la kukemea na kukanusha: Je, waliumbwa pasina kutokana na kitu chochote? Au wao ndio walijiumba wenyewe, na wakaziumba mbingu na ardhi? Au je wana hazina za Mwenyezi Mungu? Au je wao ndio wenye mamlaka? Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji? * Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana yakini * Au wanazo hazina za Mola wako Mlezi au wao ndio wenye madaraka?" [Tur: 35-37]. Aya hii ni moja ya ushahidi mkubwa zaidi juu ya kuwepo kwa Muumba, na kwa sababu hii ilithibiti kwamba Jubairi bin Mut'im alisema: Nilimsikia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akisoma katika swala ya Magharibi surat Tur, na alipofikia aya hizi: "Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji? * Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana yakini * Au wanazo hazina za Mola wako Mlezi au wao ndio wenye madaraka?" Akasema: "Moyo wangu ulikaribia kupuruka (kuruka kama ndege)". (Imesimuliwa na Bukhari (4854), Muslim (463), Abu Daudi (811), An-Nasa'i (987), na Ibn Majah (832). Na Jubair, Mwenyezi Mungu amridhie, alizisikia aya hizi kabla ya kusilimu, kwa hivyo ikabainika wazi kuwa wao wameumbwa na wanalelewa, na wanadhibitiwa. Kwa hivyo ametakasika Mwenyezi Mungu dhidi ya hayo wanayomsifu nayo.
Na amesema Mola wa Haki, Mtukufu: "Sikuwashuhudisha kuumbwa kwa mbingu na ardhi, wala kuumbwa kwa nafsi zao. Wala sikuwafanya wapotezao kuwa ndio wasaidizi." [Al-Kahf: 51] Na ikiwa mwanadamu hajui uumbaji wa mbingu na hajui uumbaji wake mwenyewe, basi anawezaje kumkana muumba wake na yule aliyemfanya kuwepo?!
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakuwaumba viumbe wake bure; bali uumbaji wake ni madhubuti na aliufanya kwa lengo tukufu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina yake kwa mchezo * Kama tungelitaka kufanya mchezo, tungejifanyia Sisi wenyewe, lau kwamba tungelikuwa ni wafanyao mchezo." [Al-Anbiyaa: 16, 17].
Na alijibu madai ya Wakristo kwamba Masihi ni Mungu Muumba, na Mola Mlezi mwenye kuendesha mambo ya ulimwengu huu, na akabainisha kwamba Mwenyezi Mungu hakifichikani kwake chochote duniani au mbinguni, na kwamba yeye ndiye anayewaunda wanadamu tumboni. Na katika wale aliowaumba Mwenyezi Mungu, na akawaunda ni Masihi, amani iwe juu yake, amesema Mola Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hakifichikani chochote kwake, duniani wala mbinguni * Yeye ndiye anayewaunda ndani ya matumbo ya wazazi kwa namna apendayo. Hapana mungu ila Yeye, Mwenye nguvu na Mwenye hekima." [Al-Imran: 5, 6] Na mengineyo mengi miongoni mwa yale yanayotajwa kwa wingi katika Qur'ani Tukufu, kama ilivyo katika "Surat Al-An' am", "An-Nahl" na nyinginezo, miongoni mwa hoja zisizohesabika, na ushahidi usiodhibitika, ambayo yote ni ushahidi juu ya kuwepo kwake na umola wake.
Mlango wa kuamini umola wa Mwenyezi Mungu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika umola wake (Uumbaji na ulezi), na kwamba yeye ndiye Muumba peke yake, na ndiye aliyeanzisha uumbaji na hakuna yeyote aliyeshiriki pamoja naye katika hilo. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Mwenyezi Mungu huanzisha uumbaji, tena akaurudisha mara ya pili, na kisha mtarejeshwa kwake." [Ar-Rum: 11] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Sema: Je, yupo katika miungu yenu ya ushirikina aliyeanzisha kuumba viumbe, na kisha akavirejesha? Basi ni vipi mkadanganywa?" [Yunus: 34].
Na kwamba Mwenyezi Mungu anaumba kwa amri yake Mtukufu, amesema aliyetakasika na kutukuka: "Hakika amri yake anapotaka kitu ni kukiambia tu: Kuwa! Na kikawa." [Yasin: 82]. Naye Aliyetakasika na kutukuka anaumba kupitia atakacho miongoni mwa sababu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Na kwa hayo tukatoa namna mbali mbali za mimema." [Taha: 53] Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na katika kila matunda akafanya dume na jike." [Ra'd: 3] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie." [Dhariyat: 49].
Na ameeleza Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka kuwa Yeye ndiye Muumba wa kila kitu, kwa hivyo kila kitu kisichokuwa Yeye kimeumbwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu. " [Az-Zumar: 62].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mola Mlezi wa vitu vyote na Muumba wake na Mwendeshaji wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Muabuduni Mola wenu Mlezi aliyewaumba nyinyi na wale wa kabla yenu, ili mpate kuokoka * (Mwenyezi Mungu) ambaye amewafanyia hii ardhi kuwa kama tandiko, na mbingu kama paa, na akateremsha maji kutoka mbinguni, na kwayo akatoa matunda yawe riziki zenu. Basi msimfanyizie Mwenyezi Mungu washirika, na hali nyinyi mnajua." [Al-Baqarah: 21, 22]. Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hakika Mola wenu Mlezi ni Mwenyezi Mungu, ambaye ameziumba mbingu na ardhi kwa siku sita, kisha akatulizana juu Arshi (Kiti chake cha Enzi), anayapangilia mambo." [Yunus: 3] Kwa hivyo, yeye ndiye Muumba na Mmiliki wa mbingu na ardhi, na ndiye Mwenye kuziendesha. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yeye anazo funguo za mbingu na ardhi. Na wale waliozikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, hao ndio waliopata hasara." [Az-Zumar: 63] Hakuna kiumbe aliye na uwezo wa kusimamia mambo yake mwenyewe au mambo ya wengine isipokuwa yale ambayo Mwenyezi Mungu amemwandikia. Wala Malaika wala Manabii, amani iwe juu yao, wala Mawalii (Vipenzi wa Mwenyezi Mungu) hawawezi kutoa maamuzi katika ulimwengu au kuleta manufaa au kuzuia madhara, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Waiteni mnaowadai kuwa ni badala ya Mwenyezi Mungu. Hawamiliki hata uzito wa chembe ndogo katika mbingu wala ardhi. Wala hawana ushirika wowote humo. Wala Yeye hana msaidizi miongoni mwao." [Saba': 22]
Na tunaamini kwamba yeye ndiye mmiliki wa haki, na kila kisichokuwa Yeye kinamilikiwa, na kila Mfalme au umiliki basi umiliki wake ni wa muda mfupi na utaondoka, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenye Kumiliki Siku ya Malipo." [Al-Fatiha: 4], Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Sema: Ewe Mwenyezi Mungu Mmiliki wa ufalme! Wewe humpa ufalme umtakaye, na humuondolea ufalme umtakaye, na humtukuza umtakaye, na humdhalilisha umtakaye. Heri yote iko mkononi mwako. Hakika Wewe ni Muweza juu ya kila kitu." [Al-Imran: 26] Na vyote visivyokuwa Yeye vinalelewa, na vimetenzwa nguvu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hapana yeyote aliomo mbinguni na ardhini ila atafika kwa Al-Rahmani (Mwingi wa rehema) huku ni mja wake tu." [Maryam: 93].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi, na kwamba anaukunja usiku juu ya mchana, na anaukunja mchana juu ya usiku, na kwamba yeye ndiye aliyelitiisha jua na mwezi, kila kimoja kikikimbia kwa muda maalum, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Ameumba mbingu na ardhi kwa haki. Huufunika usiku juu ya mchana, na huufunika mchana juu ya usiku. Na amefanya jua na mwezi vitumike. Kila kimoja wapo kinakwenda kwa kipindi kilichowekewa. Jueni mtanabahi! Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kusamehe mno!" [Az-Zumar: 5] Na kwamba Yeye Mtukufu ndiye aliyelifanya Jua kuwa na mwangaza na Mwezi kuwa na nuru, na akafanya tofauti ya usiku na mchana kuwa ishara ya ukuu wa uumbaji wake na ubora wa usimamizi wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yeye ndiye aliyelijaalia jua kuwa na mwangaza, na mwezi ukawa na nuru, na akaupimia vituo ili mjue idadi ya miaka na hesabu. Mwenyezi Mungu hakuviumba hivyo ila kwa Haki. Anazipambanua Ishara kwa watu wanaojua * Hakika katika kuhitilafiana usiku na mchana, na katika vile alivyoumba Mwenyezi Mungu miongoni mwa mbingu na ardhi, zipo Ishara kwa watu wanaomcha Mwenyezi Mungu." [Yunus: 5, 6] Na kwamba yeye ndiye aliyetuumba kutoka katika nafsi moja, na akamfanya mke wake kutoka kwake, na akaumba wanyama wote. Anasema Mola Mtukufu: "Amewaumba nyinyi kutokana na nafsi moja. Kisha akamfanya mwenziwe katika nafsi ile ile. Na akawaletea wanyama wa mifugo jozi nane. Anawaumba katika matumbo ya mama zenu, umbo baada ya umbo, katika viza vitatu. Huyu ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi. Ufalme ni wake. Hapana mungu isipo kuwa Yeye. Basi nyinyi mnageuzwa wapi?" [Az-Zumar: 6].
Na tunaamini kuwa yeye ndiye mwenye kuruzuku, mwenye nguvu, madhubuti. Kwa hivyo hakuna mwenye kuruzuku asiyekuwa yeye, wala hakuna wa kutosheleza asiyekuwa yeye. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti." [Dhariyat: 58] Na amesema Yeye Mtukufu: "Na hakuna mnyama yoyote katika ardhi ila riziki yake iko kwa Mwenyezi Mungu. Naye anajua makao yake na mapitio yake. Yote yamo katika Kitabu chenye kubainisha." [Hud: 6].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu amekizunguka kila kitu kwa elimu, Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Anayajua yaliyo mbele yao na yaliyo nyuma yao; wala wao hawajui chochote katika vile vilivyo katika ujuzi wake, ila kwa atakalo mwenyewe." [Al-Baqarah: 255] Kwa hivyo, hakifichikani chochote akakosa kukijua; kidogo au kikubwa. Mola Mtukufu amesema: "Mwenye kujua ya ghaibu! Hapana kinachofichikana kwake hata chenye uzito wa chembe tu, si katika mbingu wala katika ardhi, wala kilicho kidogo kuliko hivyo, wala kikubwa zaidi; ila vyote hivyo vimo katika Kitabu chake chenye kubainisha." [Saba': 3] Na elimu yake inazunguka kila kitu katika ulimwengu huu. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na ziko kwake funguo za ghaibu; hakuna azijuaye ila Yeye tu. Na Yeye anajua kilichoko nchi kavu na baharini. Na halidondoki jani ila analijua. Wala punje katika giza la ardhi, wala kibichi, wala kikavu ila kimo katika Kitabu kinachobainisha." [Al-An 'am: 59] Pia alisema akieleza sehemu katika elimu hii inayozunguka kila kitu: "Na hapana mnyama katika ardhi, wala ndege anayeruka kwa mbawa zake mbili, ila ni umma kama nyinyi. Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote. Kisha kwa Mola wao Mlezi watakusanywa." [Al-An'am: 38].
Na tunaamini kwamba Yeye Mtakatifu anajua ya ghaibu na yanayoonekana. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Yeye ndiye Mwenye kujua yasiyoonekana na yanayoonekana; Mkubwa, Aliyetukuka." [Ra'd: 9] Na kwamba hamdhihirishii yeyote siri yake katika viumbe wake, isipokuwa Mtume wake aliyemridhia. Amesema Yeye Mtukufu: "Yeye ndiye Mwenye kujua ya siri, wala hamdhihirishii yeyote siri yake * Isipokuwa Mtume wake aliyemridhia. Naye humuwekea walinzi mbele yake na nyuma yake." [Al-Jinn: 26, 27] Na kila mwenye kudai kwamba anajua kisichoonekana, basi huyo ni muongo mzushi. Na Mitume hawajui mambo ya ghaibu, na Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, aseme kuwa: "Sema: Mimi siwambii nyinyi kuwa ninazo hazina za Mwenyezi Mungu. Wala sijui mambo yaliyo fichikana." [Al-An'am: 50].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuhuisha na kufisha. Yeye Mtukufu amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu anao ufalme wa mbingu na ardhi; huhuisha na hufisha. Nanyi hamna Mlinzi yeyote wala Msaidizi isipokuwa Mwenyezi Mungu." [Tauba: 116] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na Yeye ndiye aliyewahuisha kisha akawafisha, na kisha atawafufua. Hakika mwanadamu ni mwenye kukufuru mno." [Al-Hajj: 66] Na kwamba Yeye ndiye aliyeumba mauti na uhai, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ambaye ameumba mauti na uhai ili kuwajaribu ni nani miongoni mwenu mwenye vitendo vizuri zaidi. Na Yeye ni Mwenye nguvu, Mwingi wa kusamehe." [Al-Mulk: 2] Na kwamba yeye ndiye anayefisha roho. Anasema Mola Mlezi Mtukufu: "Mwenyezi Mungu huzipokea roho zinapokufa." [Az-Zumar: 42].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ameshinda kila kitu kwa utukufu na hukumu, kama Mola wetu Mlezi alivyotuambia katika kauli yake: "Na vilivyomo mbinguni na katika ardhi vinamsujudia Mwenyezi Mungu tu vikitaka visitake. Na pia vivuli vyao vinamsujudia asubuhi na jioni." [Ra'd: 15] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Siku watakayodhihiri wao. Hapana kitakachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu, Mmoja, Mshindi." [Ghafir: 16].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliumba mbingu, na akainyanyua bila ya nguzo, Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Ameziumba mbingu bila ya nguzo mnazoziona; na ameweka katika ardhi milima ili ardhi isiwayumbishe." [Luqman: 10] Na aliwatiishia viumbe vyote vilivyomo mbinguni na vilivyomo ardhini. Amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Na amefanya viwatumikie nyinyi vilivyomo mbinguni na vilivyomo katika ardhi, vyote vimetoka kwake. Hakika katika hayo zimo Ishara kwa watu wanaofikiri." [Al-Jathiya: 13].
Na tunaamini kwamba uumbaji na amri ni vyake Mola Mlezi Mtukufu. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Fahamuni! Kuumba na amri ni zake. Ametukuka kabisa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-A'araf: 54] Basi hakuna Mola Mlezi mwingine asiyekuwa Yeye, wala mtunga sheria ila Yeye, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Amewaamrisha nyingi Dini ile ile aliyomuusia Nuhu na ile tuliyokufunulia wewe." [Shura: 13] Na amesema Mtukufu: "Kila mmoja katika nyinyi tumemuwekea sheria yake na njia yake." [Al-Maida: 48] Yeye ndiye anayetunga sheria, na kuweka mambo ya wajibu, na kufafanua dini. Na Mtukufu aliwakanusha wale waliowafanya makasisi wao na watawa wao kuwa ni miungu, na wakakubali kutoka kwao yale waliyoyafanya kuwa ndiyo sheria ya dini yao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wamewafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu." [Tauba: 31] Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Au hao wana miungu wa kishirikina waliowatungia dini asiyo itolea idhini Mwenyezi Mungu?" [Shura: 21].
Kama vile Yeye Mtukufu ndiye aliyeumba viumbe, Yeye ndiye mmiliki wao, na ndiye aliyewatungia sheria, na ndiye peke yake anayeweza kuwahesabu na kuwalipa. Amesema Mola Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu ameziumba mbingu na ardhi kwa haki, na ili kila nafsi ilipwe yale iliyoyachuma. Nao hawatadhulumiwa." [Al-Jathiya: 22] Na amesema Mtukufu: "Hakika Saa itakuja bila ya shaka. Nimekaribia kuificha, ili kila nafsi ilipwe kwa iliyoyafanya." [Taha: 15].
Na tunaamini kwamba Mola Mlezi Mtukufu ndiye Muumba wa waja na muumba wa matendo yao. Amesema Mola wa Haki Mtakatifu: "Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba nyinyi na hivyo mnavyovifanya!" [As-Saffat: 96].
Na tunamshuhudia kuwa Yeye Ndiye Mola wa Haki, kwa ushuhuda wa kweli, nakuwa Yeye Mtukufu alifanya kila ishara moja miongoni mwa ishara zake za kiulimwengu ni ushahidi na ni ishara kwamba Yeye ndiye Muumba, na akasisitiza hilo kwa kauli yake: "Ati anayeumba ni kama asiyeumba? Basi hebu, hamkumbuki?" [An-Nahl: 17]. Naye Mtukufu aliwakanusha wale waliomfanyia washirika katika umola wake au uungu wake, kwa sababu yeye peke yake ndiye Muumba Aliyetakasika, akasema: "Au wamemfanyia Mwenyezi Mungu washirika walioumba kama alivyoumba Yeye, na viumbe hivyo vikawafanania kitu kimoja? Sema: Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu. Na Yeye ni Mmoja, Mshindi!" [Ra'd: 16].
Washirikina walikuwa wakiamini Umola wa Mwenyezi Mungu, na walijua kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Muumba, Aliye Hai, Mhuishaji, Mfishaji, na kwamba Yeye ndiye mwenye kunufaisha, na mwenye kudhuru, na kwamba masanamu yao hayo na miungu yao hainufaishi wala haidhuru, na waliamini kwamba ni njia zinazowaleta karibu zaidi na Mwenyezi Mungu, na pamoja na hayo Mwenyezi Mungu hakukubali hilo kutoka kwao. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Na ukiwauliza; Ni nani aliyeumba mbingu na ardhi na akafanya jua na mwezi kutiii amri yake? Bila ya shaka, watasema: Mwenyezi Mungu. Wapi basi wanakogeuzwa * Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki, na humdhikishia amtakaye katika waja wake. Kwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu * Na ukiwauliza: Ni nani anayeteremsha maji kutoka mbinguni, na akaihuisha ardhi baada ya kufa kwake? Bila ya shaka watasema: Ni Mwenyezi Mungu. Sema: Alhamdu lillahi (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu). Bali wengi katika wao hawatumii akili" [Al-Ankabut: 61-63] Na ingawa wanatafuta msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu wakati wa shida, na kumgeukia Yeye wanapoguswa na msiba, hilo halikuwanufaisha; kwa kuwa bado wako kwenye ushirikina wao na ukafiri wao, Mola Mtukufu amesema: "Na wanapopanda katika merikebu (Safina), humuomba Mwenyezi Mungu kwa kumsafia (kumtakasia) utiifu. Lakini anapowavusha wakafika nchi kavu, mara wanamshirikisha (na miungu mingine)* Wapate kuyakana yale tuliyowapa, na wajistareheshe. Lakini watakujajua!" [Al-Ankabut: 65, 66].
Mlango wa kuamini Uungu wa Mwenyezi Mungu
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika uungu wake, na kwamba hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu peke yake ambaye hana mshirika, na kwamba yeye ndiye wa haki, na kwamba vile wanavyoviomba badala yake ni batili, na kwamba jambo hili kuu ndilo kwa ajili yake Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu, na akatuma Mitume, na akaumba Bustani ya mbinguni na Moto, na limeashiriwa na maumbile ya asili, na likashuhudiwa na akili zilizo salama. Na tunajua kwa yakini kwamba msingi wa wito wa Manabii kwa watu wao ni kuwalingania kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuacha kuabudu vitu vinginevyo, amesema Mola Mtukufu: "Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia ya kwamba hapana mungu isipokuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu." [Al-Anbiya: 25]. Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Taghut (Shetani na kila anayeabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu)." [An-Nahl: 36]. Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na waulize Mitume wetu tuliowatuma kabla yako: Je, tulifanya miungu mingine iabudiwe badala ya Ar-Rahmani (Mwingi wa rehema)?" [Az-Zukhruf: 45] Na kila Nabii aliwaambia watu wake, 'Muabuduni Mwenyezi Mungu! Nyinyi hamna Mungu ila Yeye.' Tangu wa kwanza wao ambaye ni Nuhu mpaka wa mwisho wao, ambaye ni Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Mwenyezi Mungu amesema, akieleza kuhusu Nuhu, amani imshukie, yakuwa alisema: "Enyi kaumu yangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu ila Yeye." [Al-A'araf: 59] Na alieleza kuhusu wa mwisho wao, Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Sema: Hakika mimi ni muonyaji tu; na hapana mungu ila Mwenyezi Mungu Mmoja, Mshindi." [Swad: 65] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Huyo ndiye Allah, Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu, hapana mungu ila Yeye, Muumba wa kila kitu. Basi muabuduni Yeye tu. Naye ni Mtegemewa wa kila kitu." [Al-An'am: 102].
Na jambo hili kuu ndilo ambalo kwa ajili yake Mwenyezi Mungu aliumba viumbe. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi." [Dhariyat: 56] Maana ya "Waniabudu," ni wanipwekeshe. Amesema Bukhari, Mwenyezi Mungu amrehemu, wakati akitafsiri aya hii: "Sikuumba watu wenye furaha miongoni mwa watu wa makundi mawili haya isipokuwa wanipwekeshe." (Hivyo ndivyo ilivyo katika Bukhari bila ya kuinasibisha na yeyote 6/49, na Ibn Hajar aliitaja katika "Al-Fat-h" kwamba haya ni maneno ya Al-Farra 8/600).
Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema,Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alipomtuma Mu'adhi bin Jabal kwa watu wa Yemen, alimwambia: "Hakika wewe unawaendea watu miongoni mwa watu wa Kitabu (Mayahudi na Wakristo). Basi na liwe jambo la kwanza kuwalingania ni kwamba wampwekeshe Mwenyezi Mungu Mtukufu." (Imesimuliwa na Bukhari (1458), na Muslim (19). Na Bukhari, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango wa hilo kwa kauli yake: "Mlango wa yale yaliyokuja kuhusiana na kulinganiaMtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, umma wake katika kumpwekesha Mwenyezi Mungu, mwingi wa baraka, Mtukufu."
Ibada ya kweli ni ile iliyokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote, kwa mujibu wa muongozo wa bwana wa Mitume. Kwani kuabudu chochote kisichokuwa Yeye ni batili. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Hayo ni kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Wa Kweli, na kwamba wale wanaowaomba badala yake, ni baatili, na hakika Mwenyezi Mungu ndiye Aliye Juu, na ndiye Mkubwa." [Al-Hajj: 62] Na maana ya: "Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu": Ni kwamba hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hili limeonyeshwa na aya iliyotangulia.
Na kumuamini Mwenyezi Mungu peke yake na kumuabudu badala ya visivyokuwa yeye ndiyo maana ya: Hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu. Na neno hili kuu linajumuisha kukanusha asiyekuwa Mwenyezi Mungu kustahiki kuabudiwa, na kukanusha uungu wa kweli kwa kila kinachoabudiwa isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kuthibitisha uungu wa kweli kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na kwamba ibada sahihi haiwi isipokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu pekee. Na neno hili lilikuja mara nyingi kwa matamshi yake katika Qur'ani. Na aya nyingi zilikuja zikiwa na maana yake ya kukataa na kuthibitisha, kama vile katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Taghut (Shetani na viabudiwa vyote visivyokuwa Mwenyezi Mungu)." [An-Nahl: 36] Na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Muabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na chochote." [An-Nisaa: 36].
Na hii ni nguzo kubwa na msingi thabiti wa dini ya Mwenyezi Mungu - ambayo ni kuthibitisha uungu kwa Mwenyezi Mungu peke yake, na kukataa kuabudiwa visivyokuwa yeye - nayo ndiyo kiini cha dini, na nguzo ya wito wa Mitume, na maana yake ni kumpwekesha Muumba kwa matendo ya viumbe, na utakuja kuona kwamba ni vigumu kupata sura yoyote ya Qur'ani bila jambo hili, ima kwa namna ya kutaja kama msingi au kusisitiza. Na Mwenyezi Mungu alisimamisha hoja juu ya viumbe kwa ushahidi mwingi, na hoja nyingi ambazo haziwezekani kudhibitiwa wala kuzizunguka kwa idadi. Na ushahidi mkubwa zaidi juu ya jambo hili ni ushahidi wake, Mwenyezi Mungu Mtukufu aliposema: "Sema: Kitu gani ushahidi wake mkubwa kabisa? Sema: Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye shahidi baina yangu na nyinyi. Na nimefunuliwa Qur'ani hii ili kwayo niwaonye nyinyi na kila inayemfikia. Ati kweli nyinyi mnashuhudia kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu wapo miungu wengine? Sema: Mimi sishuhudii hayo. Sema: Hakika Yeye ni Mungu mmoja tu, nami niko mbali na mnaowashirikisha (Naye)." [Al-An'am: 19].
Na Mwenyezi Mungu, Mtukufu alishuhudia, na pia akashuhudia shahidi mtukufu zaidi katika viumbe wake, ambao ni Malaika na watu wenye elimu, juu ya kishuhudiwa kitukufu zaidi, ambacho ni Upweke wake na uungu wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu, na Malaika, na wenye elimu, wameshuhudia kuwa hakika hapana mungu ila Yeye, ndiye Mwenye kusimamisha uadilifu; hapana mungu ila Yeye Mwenye nguvu na Mwenye hekima." [Al-Imran: 18] Basi wakawa Malaika na watu wenye elimu wameshuhudia kile ambacho Mwenyezi Mungu alikuwa amejishuhudia mwenyewe: "Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi." [An-Nisaa: 79].
Na Mwenyezi Mungu alisimamisha hoja juu ya viumbe wake kwamba Yeye ndiye Muumba wa kila kitu kilichomo katika ulimwengu huu. Bali alifanya kila ishara ya kiulimwengu kuwa ni ushahidi juu ya kustahiki kwake uungu na kuabudiwa. Na ndiyo maana wameulizwa mara nyingi katika Qur'ani juu ya jambo hili na kukiri kwao kwamba Yeye ndiye Muumba, Mwenye kuruzuku, anayehuisha, anayefisha, kisha akawakemea kwa nini hawamuabudu au kwa nini wanaabudu mwingine pamoja naye, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ukiwauliza; Ni nani aliyeumba mbingu na ardhi na akafanya jua na mwezi kutiii amri yake? Bila ya shaka, watasema: Mwenyezi Mungu. Wapi basi wanakogeuzwa? * Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake na humkunjia amtakaye. Kwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu * Na ukiwauliza: Ni nani anayeteremsha maji kutoka mbinguni, na akaihuisha ardhi baada ya kufa kwake? Bila ya shaka watasema: Ni Mwenyezi Mungu. Sema: Alhamdulillahi (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu). Bali wengi wao hawatumii akili." [Al-Ankabut: 61-63] Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ukiwauliza: Ni nani aliyeziumba mbingu na ardhi? Bila ya shaka watasema: Kaziumba Mwenye nguvu, Mjuzi * Ambaye aliwafanyia ardhi kama tandiko, na akawafanyia ndani yake njia mbalimbali ili mpate kuongoka. Na ambaye ndiye aliyeteremsha kutoka mbinguni maji kwa kiasi, na kwa hayo tukaifufua ardhi iliyokufa. Na namna hivyo ndivyo mtakavyotolewa. Na ambaye ndiye aliyeumba katika kila kitu jike na dume, na akawafanyia merikebu (Safina) na wanyama mnaowapanda." [Az-Zukhruf: 9-12].
Mwenyezi Mungu aliwasimamishia hoja waja wake kwamba kukiri kwao neema zake juu yao ambazo zinawalazimu kumuabudu yule aliyewaneemesha kwazo, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Ni nani anayewaruzuku nyinyi kutoka mbinguni na ardhini? Au ni nani anayemiliki kusikia na kuona? Na ni nani amtoaye aliye hai kutoka kwa maiti, na akamtoa maiti kutoka kwa aliye hai? Na ni nani anayeyapangilia mambo yote? Watasema: Allah, Mwenyezi Mungu. Basi sema: Je, hamumchi? * Basi huyo ndiye Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu wa haki. Na kipo kitu gani baada ya haki, isipokuwa upotovu tu? Basi huwaje mkageuzwa?" [Yunus: 31, 32].
Katika Qur'ani, Mwenyezi Mungu mara nyingi huwasimamishia hoja waja kwa ishara za umola wake, ambazo zinamlazimu mja pia kumuabudu Yeye peke yake, na kwamba Muumba wa ishara hizi kuu za kiulimwengu ni Yeye Mwenyezi Mungu peke yake, na kwamba kwa kuwa hakuna Muumba mwingine asiyekuwa Yeye, basi haifai kumuabudu mwingine asiyekuwa Yeye. Na ndiyo maana, akahitimisha aya hizi zifuatazo kwa kusema, "Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu?" Nazo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Au ni nani aliyeziumba mbingu na ardhi, na akawateremshia maji kutoka mbinguni, na kwa hayo tukaziotesha bustani zenye kupendeza? Nyinyi hamna uwezo wa kuiotesha miti yake. Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali hao ni watu waliopotoka * Au ni nani yule aliyeifanya ardhi mahali pa kutua, na akajaalia ndani yake mito, na akaweka milima? Na akaweka baina ya bahari mbili kiziwizi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Bali wengi wao hawajui * Au ni ani yule anayemjibu mwenye shida kubwa pale anapomuomba, na akaiondoa dhiki, na akawafanya nyinyi kuwa warithi wa ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ni machache ndiyo mnayoyazingatia * Au ni nani yule anayewaongoza katika giza la bara na bahari, na akazipeleka pepo kuleta bishara kabla ya rehema zake? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ametukuka Mwenyezi Mungu juu ya hao wanaowashirikisha naye." [An-Naml: 60-63].
Na alipotaja viumbe vikubwa vinavyoashiria umola wake, ambao unalazimu pia kuamini uungu wake katika Surat Ar-Rum, ambayo ni kauli yake Mtukufu: "Na katika Ishara zake ni kuwa aliwaumba nyinyi kwa udongo. Kisha mkawa watu mliotawanyika kila mahala * Na katika Ishara zake ni kuwa amewaumbia wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanaofikiri * Na katika Ishara zake ni kuumba mbingu na ardhi, na kutofautiana ndimi zenu na rangi zenu. Hakika katika hayo zipo Ishara kwa wale wanaojua * Na katika Ishara zake ni kulala kwenu usiku na mchana, na kutafuta kwenu katika fadhila zake. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanaosikia * Na katika Ishara zake huwaonyesha umeme kwa kuwatia hofu na tamaa. Na huwateremshia maji kutoka mbinguni, na kwayo huifufua ardhi baada ya kufa kwake. Hakika katika hayo zipo Ishara kwa watu wanaotumia akili * Na katika Ishara zake ni kuwa mbingu na ardhi zimesimama kwa amri yake. Kisha atakapowaita mwito mmoja tu, hapo mtatoka kwenye ardhi * Na vyake Yeye vilivyo mbinguni na katika ardhi. Vyote vinamtii Yeye. Na Yeye ndiye anayeanzisha uumbaji, kisha ataurudisha mara nyingine. Na jambo hili ni jepesi zaidi kwake. Naye ndiye mwenye mfano bora zaidi katika mbingu na ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hekima* Amewapigia mfano kutokana na nafsi zenu. Je, katika hao iliyowamiliki mikono yenu ya kulia mnao washirika katika hivyo tulivyowaruzuku, mkawa nyinyi katika hivyo ni sawa sawa, mnawaogopa kama mnavyoogopana wenyewe kwa wenyewe? Namna hivyo ndivyo tunavyozipambanua Aya zetu kwa watu wanaotumia akili* Bali wale waliodhulumu wamefuata mtamanio ya nafsi zao pasina kujua. Basi ni nani atamuongoa ambaye Mwenyezi Mungu amemuacha apotee? Wala hao hawatakuwa na wa kuwanusuru." [Rum: 20-29]. Alifungua kila aya kwa kusema, "Na katika ishara zake."; Yaani, za kiulimwengu zinazoonyesha umola wake ambao unalazimu pia kuamini uungu wake ni kile alichokitaja. Kisha akazifuatisha kwa kutaja mfano ambao Mwenyezi Mungu alimpigia mwenye kumlinganisha na chochote katika viumbe wake. Akasema: "Je, kuna mmoja wenu awezaye kumshirikisha mtumwa wake katika malazi yake na mkewe?! Vivyo hivyo, Mwenyezi Mungu haridhii kushirikishwa na yeyote katika viumbe wake."; kauli hii kaisema Katada: (Tafsir Al-Tabari (20/95) Kisha akahitimisha kwa kauli kuwa akili ya kawaida inahitaji kumuabudu Yeye yake Aliyetakasika na kutukuka, na ndio maana akasema: "Basi uelekeze uso wako sawa sawa kwenye Dini - ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilo waumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo Dini iliyo nyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui." [Ar-Rum: 30].
Na Mwenyezi Mungu ameweka ushahidi anuwai (wa aina zaidi ya moja) juu ya uungu wake kwa njia ambayo kwayo inasimama hoja, na njia inakuwa wazi, ili watu wasiwe na hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu. Na kama vile Mwenyezi Mungu alivyosimamisha hoja juu ya watu kwa ushahidi wa kukata na hoja wa wazi wazi, na akasimamisha ushahidi wa kushangaza unaoashiria umoja wake, pia alipiga mifano, na akaja na haki Yeye Aliyetakasika na kutukuka, amesema Mola Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu anapiga mfano wa watu wawili. Mmoja wao ni bubu, hawezi chochote, naye ni mzigo kwa bwana wake. Popote anapomuelekeza haleti kheri. Je, huyo anaweza kuwa sawa na yule anayeamrisha uadilifu, naye yuko juu ya Njia iliyonyooka?" [An-Nahl: 76] Amesema bin Jariri, Mwenyezi Mungu amrehemu, wakati wa kutafsiri aya hii: “Huu ni mfano ambao Mwenyezi Mungu Mtukufu ameupiga kuhusu yeye mwenyewe na miungu inayoabudiwa badala yake, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akasema: "Na Mwenyezi Mungu anapiga mfano wa watu wawili. Mmoja wao ni bubu, hawezi chochote?" akimaanisha kwa hilo yale masanamu kwamba hayasikii chochote, na hayatamki, kwa sababu masanamu hayo ima ni mbao zilizochongwa, au shaba iliyotengenezwa, ambayo haiwezi kuwanufaisha wale wanaoitumikia, wala kuwazuilia madhara, nao ni mzigo kwa bwana wake. Anasema: Bubu huyo ni mzigo kwa binamu yake na washirika wake na watu wanaosaidiana naye, basi vile vile masanamu hayo ni mzigo tu kwa wale wanaoyaabudu, kwa kuwa anahitaji kuyabeba, na kuyaweka chini na kuyatumikia, kama vile bubu miongoni mwa watu ambaye hawezi kufanya chochote, basi huwa mzigo kwa wasimamizi wake kama binamu zake na wengineo. "Popote anapomuelekeza haleti kheri." kwa sababu haelewi yale anayoambiwa, na hawezi kujieleza anachotaka, kwa hivyo haelewi, wala hakieleweki kitu kutoka kwake. Basi vile vile sanamu haifahamu inachoambiwa, ili iamrishe amri yoyote, wala haitamki kitu ili iamrishe na kukataza. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Je, huyo anaweza kuwa sawa na yule anayeamrisha uadilifu?" Yaani: Je, ni sawa bubu huyu ambaye ni mzigo kwa bwana wake, ambaye haleti heri yoyote popote anapoelekea, na yule ambaye anatamka na kuzungumza na kuamrisha haki, na analingania kwa hiyo, ambaye ni Mwenyezi Mungu, Mmoja, Mshindi, ambaye anawalingania waja wake kumpwekesha na kumtii. Anasema kwamba Yeye Mtukufu hawezi kuwa sawa na sanamu ambalo sifa yake imeelezwa. (Tafsir Twabari 17/262).
Na Mwenyezi Mungu pia alipiga mfano wa mungu batili na Mungu wa haki kama Mujahid alivyosema: (Tafsir Twabari: 21/285). Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa mtu mwenye mabwana washirika wanao gombana, na wa mtu mwingine aliye husika na bwana mmoja tu. Je! Wako sawa katika hali zao? Alhamdulillahi, Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu! Lakini wengi wao hawajui." [Aئ-Zumar: 29].
Na jambo hili - yaani kukiri upweke wa Mwenyezi Mungu, pamoja na kumshuhudilia Mtume (rehema na amani ziwe juu yake ) utume -, ndilo jambo ambalo Mwenyezi Mungu alilifanya kuwa mpaka kati ya imani ya mwanadamu kwa Mwenyezi Mungu na ukafiri. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ikiisha miezi mitukufu, basi wauweni washirikina popote muwakutapo, na washikeni na wazungukeni, na wavizieni katika kila njia. Lakini wakitubu, wakashika Sala, na wakatoa Zaka, basi waachilieni." [At-Tauba: 25] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Basi wakitubu na wakashika Swala na wakatoa Zaka, basi ni ndugu zenu katika Dini." [At-Tawbah: 11] Na imesimuliwa kutoka kwa bin Omari na Ammari bin Yaasir - Mwenyezi Mungu awawie radhi kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - alisema: "Nimeamrishwa nipigane na watu mpaka washuhudie kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na wasimamishe Swala, na watoe Zaka, kwa hivyo watakapofanya hivyo, watazilinda damu zao na mali zao kutokana na mimi isipokuwa kwa haki ya Uislamu, na hesabu yao ni kwa Mwenyezi Mungu." (Imesimuliwa na Bukhari 1399, 7284, Muslim 20, Abu Daud 1556, Tirmidhi 2607, na An-Nasa'i 2443).
Imani hii haitoshi kuwa moyoni, lakini ni lazima izungumzwe kwa ulimi; ndiyo maana Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema: "Nimeamrishwa nipigane na watu mpaka waseme: 'Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu." (Imesimuliwa na Bukhari 25, na Muslim 22). Imani haipatikani hadi viungo viitie katika matendo. Alisema Yeye wa Haki - na kauli yake ni ya Haki: "Hakika Waumini ni wale ambao anapotajwa Mwenyezi Mungu, nyoyo zao hujaa hofu, na wanaposomewa Aya zake, huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi * Hao ambao wanashika Swala na wanatoa katika yale tunayowaruzuku * Basi, hao ndio Waumini wa kweli." [Al-Anfaal: 2-4] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi. Bali wema ni wa anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii, na anawapa mali, kwa kupenda kwake, jamaa na mayatima na masikini na wasafiri, na waombao, na katika ukombozi, na akawa anashika Sala, na akatoa Zaka, na wanaotimiza ahadi yao wanapoahidi, na wanaovumilia katika shida na dhara (dhiki) na wakati wa vita; hao ndio waliosadikisha, na hao ndio wacha Mungu." [Al-Baqara: 177].
Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Yeyote atakayeona uovu kati yenu, basi na aubadilishe kwa mkono wake. Na ikiwa hawezi, basi kwa ulimi wake. Na ikiwa hawezi, basi kwa moyo wake, na hiyo ndiyo imani dhaifu zaidi." (Imepokelewa na Muslim 49, Abu Daud 1140, Tirmidhi 2172, An-Nasa’i 5008, na Ibn Majah 1275). Hadithi hii ikawa imeashiria kwamba imani inatofautiana moyoni.
Na ni lazima pamoja na kumwamini Mwenyezi Mungu, kukufuru Taghuti (Kila mwenye kuabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu). Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi anaye mkataa Shetani na akamuamini Mwenyezi Mungu bila ya shaka amekamata kishikio madhubuti, kisicho vunjika. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua." [Al-Baqara: 256] Na kujitenga mbali na ushirikina na washirikina. Kwa hivyo, mtu hawezi kumpwekesha Mwenyezi Mungu mpaka ajitenge mbali na shirki na watu wake. Mola Mtukufu amesema: "Na pale Ibrahim alipo mwambia baba yake na kaumu yake: Hakika mimi ninajitenga mbali na hayo mnayo yaabudu." [Az-Zukhruf: 26].
Na imani hii lazima mja awe mkweli ndani yake kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu, amesema Mtukufu: "Yeye ndiye aliye Hai - hapana mungu isipo kuwa Yeye. Basi muabuduni Yeye mkimsafishia Dini Yeye. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote." [Ghafir: 65] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu." [Al-Bayyina: 5] Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, amesema: Ilisemwa: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nani atakayepata furaha zaidi kwa uombezi wako Siku ya Kiyama? akasema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Nilifikiri sana – Ewe Abuu Huraira – kwamba hakuna yeyote angeniuliza kuhusu Hadithi hii kabla yako, kwa sababu nimeona pupa yako juu ya Hadithi. Mtu atakayepata furaha zaidi ya watu wote kwa uombezi wangu Siku ya Kiyama, ni yule atakayesema: Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, kwa ikhlasi kutoka moyoni mwake au katika nafsi yake." (Imepokelewa na Bukhari 99, 6570)
Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kwani hakika Mwenyezi Mungu amemharamishia kuingia Motoni mwenye kusema: Hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, akitaka kwa neno hilo (Kuuona) uso wa Mwenyezi Mungu (Ambayo ndiyo neema ghali zaidi kwa watu wa peponi)". (Imepokelewa na Bukhari 425, Muslim 33, An-Nasai 788, na Ibn Majah 754).
Na lazima awe na yakini wala asiwe na shaka, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Hakika Waumini ni wale waliomuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake tena wasitie shaka kabisa." [Al-Hujrati: 15]. Na Mwenyezi Mungu alisema akieleza kuhusu yule kafiri mmiliki wa ile Bustani, yakwamba alisema: "Wala sidhani kuwa hiyo Saa (ya Kiyama) itatokea. Na ikiwa nitarudishwa kwa Mola wangu Mlezi, bila ya shaka nitapata marejeo bora zaidi kuliko haya." [Al-Kahf: 36]
Na kwamba imani yake iwe imejengeka juu ya elimu, akawa anajua uhakika wa imani na kile inachokihitaji na kinyume chake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi jua ya kwamba hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu." [Muhammad: 19]
Ni lazima pamoja na kuwa na elimu na ikhlas mtu akubali yale aliyokujanayo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, na yale yaliyomo katika imani, ambayo yanaashiriwa na neno: 'Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu.' kama vile kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuacha kuabudu kitu kingine chochote. Kwa hivyo, mwenye kuyasema haya, kisha asikubali kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, anakuwa miongoni mwa wale ambao Mwenyezi Mungu alisema juu yao: "Wao walipokuwa wakiambiwa Laa ilaaha illa Llaahu, Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu tu, wanajivuna * Na wanasema: Hivi sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu?" [As-Saffat: 35, 36].
Na ajisalimishe na afuate amri, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mwenye kuuelekeza uso wake kwa Mwenyezi Mungu, naye akawa anafanya wema, basi huyo hakika amekwisha kamata fundo lilio madhubuti. Na mwisho wa mambo yote ni kwa Mwenyezi Mungu." [Luqman: 22].
Na awe mkweli katika maneno yake, matendo yake na imani yake ili apate yale aliyobashiriwa na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika kauli yake: "Hakuna yeyote anayeshuhudia kwamba hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, huku moyo wake una yakini na hayo, isipokuwa Mwenyezi Mungu anamharamishia Moto." (Imepokelewa na Bukhari 128, Muslim 32).
Na aipende dini hii, na yule aliyeifanya kuwa sheria, na yule aliyekuja nayo, na yeyote anayeichukua kuwa dini yake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na katika watu wapo wanaowafanya waungu wasiokuwa Mwenyezi Mungu, wanawapenda kama kumpenda Mwenyezi Mungu, lakini wale walioamini wanampenda Mwenyezi Mungu zaidi sana." [Al-Baqara: 165] Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hataamini mmoja wenu mpaka niwe mimi ndiye mpendwa zaidi kwake kuliko mwanawe, baba yake, na watu wote." (Imesimuliwa na Bukhari 15, Muslim 44, An-Nasa'i 5013, na bin Majah 67). Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mambo matatu ikiwa yatakuwa ndani ya mtu yeyote, basi atapata utamu wa imani: Awe Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wapendwa zaidi kwake kuliko yeyote yule, na kwamba ampende mtu si kwa chochote isipokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake, na kwamba achukie kurudi kwenye ukafiri kama atakavyochukia kutupwa ndani ya Moto." (Imepokelewa na Bukhari 16, Muslim 43, Tirmidhi 2624, Nasai 4987, na Ibn Majah 4033).
Na kama vile Mwenyezi Mungu alivyoelezea uhakika wa imani na matakwa yake, nguzo zake na masharti yake, alivunjilia mbali fikira potofu za washirikina wasiotii, na akaeleza wazi kuwa hawana hoja yoyote juu ya ushirikina wao huo, kwa sababu hawa miungu waliumbwa, na wanaendeshwa, hao hawaumbi chochote, na wala hawamiliki uzito wa chembe mbinguni wala duniani, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ati wanawafanya viumbe kuwa ni washirika wa Mwenyezi Mungu, nao hawaumbi, bali wao ndio wanaumbwa? * Na wala hawana uwezo wa kuwanusuru wala wenyewe hawawezi kujinusuru * Na mkiwaita kwenye uongofu, hawakufuateni. Ni mamoja kwenu ikiwa mtawaita au mkinyamaza * Hakika hao mnao waomba kinyume na Mwenyezi Mungu ni waja mfano wenu nyinyi. Hebu waombeni, nao wakuitikieni, kama nyinyi ni wakweli * Je, wao wanayo miguu ya kwendea? Au wanayo mikono ya kujitetea? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio ya kusikilizia? Sema: Ieteni hio miungu yenu ya ushirikina. Kisha nifanyieni mimi vitimbi, wala msinipe muhula * Hakika Mlinzi wangu ni Mwenyezi Mungu aliye teremsha Kitabu. Naye ndiye awalindae walio wema * Na hao mnao waomba kinyume na Mwenyezi hawawezi kukunusuruni, wala hawawezi kujinusuru wenyewe * Na mkiwaita kwenye uongofu hawasikii. Na unawaona wanakutazama, nao hawaoni." [Al-A'araf: 191-198]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Waiteni mnao wadaia kuwa ni badala ya Mwenyezi Mungu. Hawamiliki hata uzito wa chembe ndogo mbinguni wala ardhini. Wala hawana ushirika wowote humo. Wala Yeye hana msaidizi miongoni mwao * Wala uombezi mbele yake hautafaa kitu, isipokuwa kwa aliyempa idhini." [Saba': 22, 23] Na aya hii ilivunjilia mbali mahusiano ya ushirikina yote.
Na alibainisha Mola wa Haki kwamba hawa masanamu wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu hawasikii maombi ya wale wanaowaomba, na hata kama wangelisikia, wasingeliweza kuwaitikia, na Siku ya Kiyama wataikufuru shirki yao hiyo, na watajitenga mbali nao, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hata mkiwaomba, hawasikii maombi yenu; na hata wakisikia, hawakujibuni. Na Siku ya Kiyama watakataa ushirikina wenu. Na hapana atakayekupa habari vilivyo kama Yeye Mwenye habari. " [Fatwir: 14]
Na vile vile alibainisha kwamba masanamu hawa wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu hawanufaishi kitu, wala hawadhuru. Basi vipi wanaabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu. Amesema Mtukufu: "Na wamechukua badala yake miungu ambayo haiumbi chochote, bali hiyo inaumbwa, haijimilikii nafsi zao madhara wala manufaa, wala haimiliki mauti, wala uhai, wala kufufuka." [Al-Furqan: 3].
Na Mwenyezi ameweka wazi kwamba masanamu hao hawawamilikii wafuasi wao riziki, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na badala ya Mwenyezi Mungu wanawaabudu wasio wamilikia riziki kutoka mbinguni wala ardhini, wala hawawezi kitu." [An-Nahl: 73]. Wanawezaje kuwaabudu wale ambao hawamiliki chochote na hawawezi kuruzuku, wala kunufaisha, wala kudhuru?!
Na aliwasimamishia hoja kwamba wanapopatwa na madhara au wakaingia katika shida, wanamkimbilia Mwenyezi Mungu peke yake huku wamemsafishia Dini. Na pindi anapowaokoa, wanarudi kwenye ushirikina wao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na wanapo panda katika merikebu (Safina), humuomba Mwenyezi Mungu kwa kumsafia utiifu. Lakini anapowavusha wakafika nchi kavu, mara wanamshirikisha." [Al-Ankabut: 65].
Na kama vile alivyobatilisha madai ya washirikina juu ya kumfanyia Mwenyezi Mungu washirika, pia alibatilisha kila madai ya kwamba Mwenyezi Mungu alijifanyia mwana, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu hana mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine. Ingekuwa hivyo basi kila mungu angelichukua alivyoumba, na baadhi yao wangeli washinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa wanazo msifu." [Al-Mu’minun: 91] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Lau wangelikuwamo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeliharibika. Subahana 'Llah, Ametakasika Mwenyezi Mungu, Bwana wa A'rshi (Kiti cha Enzi), na hayo wanayoyazua." [Al-Anbiya: 22]. Na akabainisha Mtukufu kuwa Mayahudi na Wakristo walidai kuwa Mwenyezi Mungu ana mwana. Basi Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka akasema: "Na Mayahudi wanasema: Uzeiri ni mwana wa Mungu. Na Wakristo wanasema: Masihi ni mwana wa Mungu. Hiyo ndiyo kauli yao kwa vinywa vyao. Wanayaiga maneno ya walio kufuru kabla yao. Mwenyezi Mungu awaangamize! Wanageuzwa namna gani hawa!" [Tauba: 30], Na Mwenyezi Mungu alivunjilia mbali itikadi yao hiyo toka mwanzo; kwa maana mwanadamu anayekula chakula anawezaje kuwa mungu?! Na Mungu hali, wala hanywi, na wala hahitaji kile wanadamu wanahitaji, amesema Mola Mtukufu: "Masihi mwana wa Maryam si chochote ila ni Mtume. Wamekwisha pita Mitume kabla yake. Na mama yake ni mwanamke mkweli. Wote wawili walikuwa wakila chakula. Angalia jinsi tunavyo wabainishia Aya, kisha angalia vipi wanavyo geuzwa * Sema: Je! Mnawaabudu, badala ya Mwenyezi Mungu, wale ambao hawawezi kukudhuruni wala kukufaeni? Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kusikia, Mwenye kujua." [Al-Maida: 75, 76].
Mwenyezi Mungu Mtukufu alibatilisha suala la kuwaabudu Malaika, na akabainisha wazi kwamba - ijapokuwa wako karibu na Mwenyezi Mungu - hawamiliki uombezi ila baada ya idhini yake - akasema Mola wetu Mlezi: "Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia." [An-Najm: 26], Na wanamhofu Mola wao Mlezi aliye juu yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na vyote vilivyomo mbinguni na ardhini, wakiwemo wanyama na Malaika, vinamsujudia Mwenyezi Mungu, na wala havitakabari * Hakika wao wanamuogopa Mola wao Mlezi aliye juu yao, na wanatenda wanayo amrishwa" [An-Nahl: 49, 50], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Masihi hataona unyonge kuwa mtumwa wa Mwenyezi Mungu, wala Malaika walio kurubishwa. Na watakao ona uvunjifu utumwa wa Mwenyezi Mungu na kufanya kiburi, basi atawakusanya wote kwake." [An-Nisa: 172], Ikiwa hivi ndivyo ilivyo hali ya Malaika, basi wanawezaje kuabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu?
Vivyo hivyo, Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, pamoja na kiwango chao cha juu cha nafasi yao katika dunia hii na Akhera, hawamiliki uwezo wa kujinufaisha wenyewe wala kujidhuru, kwa hivyo watakuwaje wale walio chini yao?! Amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka akieleza kuhusu Manabii kuwa wanamuabudu Mola wao Mlezi kwa shauku na hofu: "Hakika wao walikuwa wepesi wa kutenda mema, na wakituomba kwa shauku na khofu. Nao walikuwa wakitunyenyekea." [Al-Anbiya: 90], Na akamuamrisha Mtume wake Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake aseme kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza kuhusu yeye kwa kauli yake: "Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara, ila apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa ninayajua ya ghaibu ninge jizidishia mema mengi, wala ovu lisinge nigusa. Mimi si chochote ila ni muonyaji na mbashiri kwa watu wanao amini." [Al-A'araf: 188], Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipowaapiza wale waliomuudhi miongoni mwa washirikina katika vita vya Uhudi, Mwenyezi Mungu alimteremshia kauli yake Mtukufu: "Wewe huna lako jambo katika haya - ikiwa atawahurumia au atawaadhibu, kwani wao ni madhalimu." [Al-Imran: 128]. Imesimuliwa kutoka kwa Az-Zuhri kuwa alisema: Salim alinisimulia kutoka kwa baba yake, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, anapoinua kichwa chake kutoka katika rukuu katika rakaa ya mwisho ya swala ya Alfajiri, anasema: "Ewe Mwenyezi Mungu, mlaani fulani, na fulani na fulani." Baada ya kusema, "(Samiallaahu liman hamidah, Rabbanaa walakal hamdu) Mwenyezi Mungu amemsikia mwenye kumsifu. Ewe Mola wetu Mlezi ni zako sifa njema." Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu akataremsha: "Wewe huna lako jambo katika haya." hadi katika kauli yake: "kwani wao ni madhalimu." (Imesimuliwa na Bukhari 4559, na Nasai 1078).
Mlango wa kuamini majina ya Mwenyezi Mungu na sifa zake
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ni mmoja katika sifa zake za ukamilifu na ukuu wake, na kwamba Mwenyezi Mungu ana majina mazuri zaidi na sifa za juu ambazo maandiko mengi ya Kitabu na Sunna yalitaja, na akili kamilifu zinashuhudia hilo, na maumbile ya asili yaliyo salama yanajisalimisha kwa hilo, na wanazuoni wa Umma huu walikubaliana juu ya hilo. Bali jumbe zote za kimungu zilikuja kubainisha sifa, majina na matendo ya Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu aliwashutumu washirikina kuabudu kwao masanamu, kwa sababu masanamu hayo yameubwa kama wao. Bali hayo hata yako chini zaidi yao na ni mapungufu zaidi. Hayaoni, wala hayasikii. Tena hayana miguu ya kutembea kwayo, na hayana mikono ya kushika kwayo. Amesema Mola wa Haki Aliyetakasika: "Hakika hao mnaowaomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu ni waja mfano wenu nyinyi. Hebu waombeni, nao wakuitikieni, kama mnasema kweli * Je, wao wanayo miguu ya kwendea? Au wanayo mikono ya kujitetea? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio ya kusikilizia? Sema: Leteni hio miungu yenu ya ushirikina. Kisha nifanyieni mimi vitimbi, wala msinipe muhula." [Al-A'araf: 194, 195]. Na amesema Mtukufu: "Na baada yake (Musa) walimtengeneza ndama kutokana na mapambo yao (ili waabudu), kiwiliwili tu kilicho kuwa na sauti. Hivyo, hawakuona kuwa hawasemezi wala hawaongoi njia? Wakamuabudu, na wakawa wenye kudhulumu." [Al-A'araf: 148].
Na tunaamini kwamba kama alivyojielezea mwenyewe, na kama vile Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alivyomuelezea Yeye aliyetakasika hakuna kitu mfano wake. Naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hapana kitu kama mfano wake. Naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona." [Ash-Shuraa: 11]. Kwa hivyo tunamthibitishia Mwenyezi Mungu yale aliyojithibitishia Mwenyewe, au Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na tunamkanushia Yeye yale aliyojikanushia Mwenyewe, au Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliyomkanushia, bila ya kuyapinga, wala kuyafananisha, wala kusema namna yalivyo, wala kuyapotoa. Na tunajua kwa yakini kwamba Mola wetu Mlezi alisifika kwa sifa zake kabla ya kuumba viumbe, na kwamba Yeye yuko katika kiwango cha juu kabisa cha ukamilifu, utukufu, na uzuri tangu zamani hadi milele, kwani Yeye ndiye wa kwanza na wa mwisho. Yeye ndiye wa kwanza ambaye hakuna chochote kabla yake, na wa mwisho ambaye hakuna chochote baada yake. Yeye ndiye wa kwanza katika majina na sifa zake, kwa ukamilifu na utukufu. Naye ndiye wa mwisho katika majina na sifa zake kwa ukamilifu na utukufu.
Na tunaamini kwamba Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu, kama vile viumbe haviwezi kumzunguka kwa elimu, vivyo hivyo macho yao hayawezi kumfikia yakamtambua, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yeye anajua yaliyo mbele yao, na yaliyo nyuma yao. Wala wao hawawezi kumjua Yeye vilivyo." [Twaha: 110], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Macho hayamfikii bali Yeye anayafikia macho. Naye ni Mjuzi, Mwenye habari." [Al-An'am: 103]. Amesema Imam bin Kutaiba Mwenyezi Mungu amrehemu: "Ni wajibu juu yetu kuishia katika sifa za Mwenyezi Mungu pale ambapo aliishia katika kuelezea sifa zake, au pale ambapo Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliishia, na wala tusiliondoe neno kutoka katika maana ambayo Waarabu wanaijua na ambayo wanaitumia, na tunajizuilia mbali na yasiyokuwa hayo." (Al Ikhtilaafu fil lafdhi warraddu A'lal-Jahmiyya, cha Ibn Qutaibah uk. 44).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ana sifa zisizoachana naye, kama vile uhai, elimu, kusikia, kuona, mkono, na vidole. Na pia kuna sifa zake zinazohusiana na matashi yake, kama vile hasira, kuridhia, na kushuka. Na tunaamini kwamba yeye ndiye anayefanya atakacho. Anafanya apendapo, apendacho, apendavyo. Humtukuza amtakaye, na humdhalilisha amtakaye. Hakuna anayeweza kuzuia amri yake, wala hakuna wa kurekebisha mapitisho yake na hukumu yake.
Na tunaamini kwamba katika sifa za Mwenyezi Mungu kuna zile zilizokuja moja kwa moja kama alivyo; kwa hivyo tunamsifu Mwenyezi Mungu kwazo hivyo hivyo bila ya kuzizuilia, kama vile kusikia, uhai, kuona, na nyinginezo. Na miongoni mwake kuna zile zilizozuiliwa (zenye kikomo); kwa hivyo zinabakishwa hivyo hivyo, kama vile kumuelezea Mwenyezi Mungu Mtukufu kwamba huwapangia njama maadui zake ikiwa wao watampangia njama, na huwasahau maadui zake ikiwa wao pia watamsahau.
Na tunaamini kwamba baadhi ya sifa zilikuja zikimuelezea Mwenyezi Mungu kwa njia moja, kama vile sifa ya uhai, usimamizi wa kila kitu milele, na ukuu, ndiyo utaona zimetajwa katika Qur'ani au Sunna kwa namna moja. Na tunapata baadhi ya sifa zimetajwa katika Qur'ani Tukufu au Sunna kwa namna nyingi, kama vile sifa ya kuzungumza, kuinuka juu, mkono, waumini kumuona Mola wao Mlezi katika uwanja wa siku ya Kiyama, na Peponi.
Na miongoni mwa sifa zake Aliyetakasika na kutukuka ni elimu na kusikia, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Alisema: Mola wangu Mlezi anayajua yasemwayo mbinguni na ardhini. Na Yeye ni Mwenye kusikia Mwenye kujua." [Al-Anbiya: 4].
Na miongoni mwa sifa zake ni kuona, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kusikia Mwenye kuona." [Ghafir: 20], Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Yunus Sulaim bin Jubair, mtumwa huru wa Abu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: "Nilimsikia Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, akisoma Aya hii: "Hakika Mwenyezi Mungu anakuamrisheni mzirudishe amana kwa wenyewe." [An-Nisa: 58] hadi katika kauli ya Mwenyezi Mungu: "Mwenye kusikia, Mwenye kuona." akasema: "Nilimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akiweka kidole gumba chake kwenye sikio lake, na kile kinachokifuata juu ya jicho lake." Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, akasema: "Nilimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akiisoma na akaweka vidole vyake viwili." Ibn Yunus akasema: Al-Muqri alisema: Alimaanisha: "Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona." akimaanisha kwamba Mwenyezi Mungu ana uwezo wa kusikia na kuona. (Imesimuliwa na Abuu Daud 4728, Hafs bin Omar katika Juz'u Qiaraat An-Nabii 33, Ibn Khuzaima katika Tawhid 49, na Ibn Abu Hatim katika Tafsir 5524).
Na katika sifa zake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni jicho, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "...na ili ulelewe mbele ya macho yangu." [Taha: 39] Na akasema: "Na ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi. Kwani wewe hakika uko mbele ya macho yetu, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi unapo simama" [Tur: 48] Na amesema Mwenye sifa tukufu: "Na unda jahazi mbele ya macho yetu" [Hud: 37] Na akasema Mtukufu: "Ikawa inakwenda kwa uangalizi wetu." [Al-Qamar: 14], Na imesimuliwa kutoka kwa Nafi 'kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Dajali alitajwa na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake akasema: "Hakika Mwenyezi Mungu hafichikani kwenu. Hakika, Mwenyezi Mungu si chongo - na akaashiria kwa mkono wake kwenye jicho lake - na hakika Masihi Dajali ni chongo kwenye jicho la kuume, ni kana kwamba jicho lake hilo ni zabibu inayoelea." (Imesimuliwa na Bukhari 7407, Muslim 169, Abu Daud 4757, na Tirmidhi 2241).
Na katika sifa zake Yeye Mtukufu ni uhai, na kusimamia mambo yote milele. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Mwenyezi Mungu, hakuna mungu ila Yeye Aliye Hai, Msimamizi wa yote milele." [Al-Imran: 2].
Na miongoni mwa sifa zake ni kuzungumza. Naye amesifika kwa sifa hii ya kuzungumza hata kabla ya kuumba viumbe na kuwazungumzisha. Na maneno ya Mola wetu Mlezi yanafungamana na matashi yake. Anapotaka, anazungumza. Zimekuja habari kuhusu sifa hii ya Mwenyezi Mungu ya kuzungumza katika Qur'ani kwa namna nyingi. Kwa hivyo kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu alieleza juu yake mwenyewe kwamba anaamuru au anakataza , basi hicho kinaashiria kuzungumza kwake, kama vile kauli yake: "Hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha kufanya uadilifu, na hisani, na kuwapa jamaa wa karibu; na anakataza uchafu, na uovu, na dhulma. Anakuwaidhini ili mpate kukumbuka." [An-Nahl: 90]. Na yote ambayo Mwenyezi Mungu alieleza kumhusu Yeye mwenyewe kuwa alisema, au anasema, basi hayo yanaashiria sifa yake hii ya kuzungumza, kama kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Pale Mwenyezi Mungu alipo sema: Ewe Isa! Mimi nitakufisha, na nitakunyanyua kwangu." [Al-Imran: 55]. Na yote yaliyopokelewa ndani yake kuhusu habari ya Manabii huku yakifungamanishwa na Mwenyezi Mungu basi hayo yanaashiria kuthibitisha sifa hii ya Mwenyezi Mungu ya kuzungumza, Mola Mlezi wa walimwengu. Anasema Mola wa Haki: "Akasema: Ni nani aliyekwambia haya? Mtume akasema: Kaniambia Mjuzi Mwenye khabari zote!" [At-Tahrim: 3].
Na yote yayolikuja yakihusiana na kuita au kunong'ona huku yamefungamanishwa na Mwenyezi Mungu ni ushahidi juu ya sifa ya kuzungumza kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu, kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tulimuita upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye." [Maryam: 52]. Na kila kauli iliyokuja huku imefungamanishwa na Mwenyezi Mungu, au mazungumzo yaliyokuja katika Qur'ani huku yamefungamanishwa na Mwenyezi Mungu, basi hayo ni ushahidi juu ya sifa yake ya kuzungumza. Na hayo ni mengi wala hayahesabiki, na miongoni mwake ni kwamba Yeye Mtukufu alizungumza na Malaika, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na pale Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Mimi nitamuweka katika ardhi Khalifa (kiongozi)." [Al-Baqarah: 30], Na alinena na Adam: "Na tulisema: Ewe Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani, na kuleni humo maridhawa popote mpendapo." [Al-Baqara: 35], Na alinena na Musa, amani iwe juu yake: "(Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Musa! Mimi nimekuteua uende kwa watu na Ujumbe wangu na maneno yangu." [Al-A'araf: 144].
Na maneno ya Mola wetu Mlezi kuna yale ambayo ni kuita, kama alivyomuita Ibrahim, ambaye ndiye rafiki wake mwandani, amani iwe juu yake, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Tulimuita: Ewe Ibrahim!" [As-Saffat: 104], Na baadhi yake ni kunong'ona, kama Mola wetu Mlezi alivyonong'ona na Musa, amani iwe juu yake: "Na tulimuita upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye." [Maryam: 52], Bin Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema kuhusiana na Aya hii: "Mpaka aliposikia sauti za kuandika kwa kalamu." (Imesimuliwa na Ibn Abi Shaiba 32506, Hannad katika Az-Zuhd 149, ʻAbdallah bin Aḥmad katika As-Sunna 1231, Tabari katika Tafsir 15/559, na Al-Hakim 3472). Na alisema As-Suddi: "Na tukamsogeza karibu." Alisema: "Inamaanisha kuwa aliingizwa mbinguni na akaongeleshwa'" (Tafsir Ibn Kathir 5/238, na Al-Durr Al-Manthur Fi Tafsir Bilmaathur 5/515). Na maneno ya Mola wetu Mlezi Malaika wanayasikia, kama ilivyokuja katika kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hata itapo ondolewa khofu kwenye nyoyo zao watasema: Mola wenu Mlezi kasema nini? Watasema: Yaliyo kweli! Na Yeye ndiye Aliye juu, Mkubwa." [Saba': 23], Na imesimuliwa kutoka kwa Masruq, kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Mwenyezi Mungu anaposema kwa ufunuo, wakazi wa mbinguni husikia sauti hiyo kutoka katika mbingu kama vile kukokota kwa mnyororo juu ya mawe, basi huzimia. Kisha wanaendelea kuwa hivyo mpaka Jibril awajie, na anapowafikia, nyoyo zao zinaondolewa hofu. Akasema: Wanasema: Ewe Jibril, Mola wako Mlezi amesema nini? Husema: Ni kweli. Nao wanasema: Ni kweli, ni kweli." (Imepokelewa na Abuu Daud 4738, Uthman bin Said Ad-Darimi katika Ar-Radd Alal-Jahmiyya 158, Abdullah bin Ahmad katika As-Sunnah 536, na Muhammad bin Nasr katika Tadhim Qadr As-Swala 217).
Na atazungumza na viumbe siku ya Kiyama kama Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alivyoeleza: “Hakuna yeyote miongoni mwenu ila Mola wake Mlezi atazungumza naye, hapatakuwa na mkalimani yeyote kati yake na Mola wake, na wala hapatakuwa na pazia la kumzuia." (Imepokelewa na Bukhari 7443, Muslim 1016, Tirmidhi 2415, na Ibn Majah 185).
Siku ya Kiyama viumbe vitasikia maneno ya Mwenyezi Mungu, kama ilivyo katika Hadithi ambayo Abdullah bin Unais, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisimulia akisema: Nilimsikia Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akisema: “Mwenyezi Mungu atawakusanya waja wake, kisha atawaita kwa sauti atakayoisikia aliye mbali kama atakavyoisikia aliye karibu, 'Mimi ndiye Mfalme, Mimi ndiye Mlipaji'.” (Imepokelewa na Bukhari kama hadithi Mu'allaq 9/141, na katika Al-Adab Al-Mufrad 970, na katika Khalq Af'al Al-Ibad 90, na Ahmad 16042).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka amejizuia kuonekana kwa viumbe wake, kwa hivyo hawawezi kumuona katika dunia hii, na anazungumza na yeyote amtakaye katika Malaika wake na Mitume wake, amani iwe juu yao, kutokea nyuma ya pazia, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na haikuwa kwa mwanadamu kwamba Mwenyezi Mungu amsemeshe ila kwa Wahyi (Ufunuo), au kwa nyuma ya pazia, au kumtuma Mjumbe. Naye humfunulia ayatakayo kwa idhini yake. Hakika Yeye ni Mtukufu, Mwenye hekima." [Ash-Shuraa: 51].
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Musa, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, halali, na wala haimfailii kulala. Yeye hushusha mizani ya uadilifu na huinyanyua. Yanapandishwa kwake matendo ya usiku kabla ya matendo ya mchana, na matendo ya mchana kabla ya matendo ya usiku. Pazia lake ni nuru, na kama angeliondoa, basi utukufu wa uso wake ungeunguza viumbe vyake mpaka pale ambapo macho yake yanafikia." (Imepokelewa na Muslim 179, Ibn Majah 195).
Na maneno ya Mola wetu Mlezi yanasifika kuwa baadhi yake ni mapya kuliko mengine. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hayawafikii mawaidha mapya kutoka kwa Mola wao Mlezi ila huyasikiliza na huku wanafanya mchezo." [Al-Anbiya: 2], Na baadhi yake ni bora kuliko mengine. Imesimuliwa kutoka kwa Abu Said Al-Khudri, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa mwanamume mmoja alimsikia mwanamume mwingine akisoma: "Sema: Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee." huku akiirudiarudia. Ilipofika asubuhi, alimjia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, na akamueleza hilo. Na ni kana kwamba mwanamume huyo aliona jambo hilo ni tendo dogo. Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake akasema: “Ninaapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mkononi mwake. Hakika, hiyo ni sawa na theluthi moja ya Qur'ani." (Imesimuliwa na Bukhari 5013, Abu Daud 1461, na Nasai 995).
Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wawili, kuwa alisema: Jibril alipokuwa ameketi pamoja na Mtume Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisikia sauti kutokea juu yake, akainua kichwa chake na akasema: “Huu ni mlango miongoni mwa milango ya mbinguni ambao ulifunguliwa leo, na haukuwahi kufunguliwa kamwe isipokuwa leo. Kwa hivyo akashuka Malaika kutoka humo na akasema: Huyu ni Malaika aliyeshuka duniani, na hajawahi kushuka kamwe isipokuwa leo tu. Kisha akasalimia na akasema: Pokea bishara njema ya nuru mbili ulizopewa ambazo hakuna Nabii aliyewahi kupewa kabla yako: Suratul-Fatiha na aya za mwisho za Suratul-Baqara. Hautasoma herufi moja katika hizo isipokuwa utapewa malipo yake.” (Imepokelewa na Muslim 806, na Nasai 912).
Na Qur'ani na vitabu vyote vya kiungu vilivyofunuliwa kwa Mitume wa Mwenyezi Mungu, amani iwe juu yao, kama vile nyaraka za Ibrahimu na Musa, amani iwe juu yao, na Taurati, Injili, na Zaburi - vyote ni maneno ya Mwenyezi Mungu, na vyote Mwenyezi Mungu ndiye aliyezungumza, naye Jibril, amani iwe juu yake, akasikia kutoka kwake bila kuwepo yeyote katikati yao. Na Mwenyezi Mungu aliishusha Taurati huku imeandikwa katika mbao. Na Jibril ndiye aliyekuwa akishuka na Ufunuo wa Mwenyezi Mungu kwa Manabii wa Mwenyezi Mungu na Mitume wake, amani iwe juu yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ameuteremsha Roho muaminifu (Jibril)* Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji." [Ash-Shu'ara: 193, 194], Na amesema Mola Mtukufu: "Basi muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake asiyejua kusoma na kuandika, ambaye anamuamini Mwenyezi Mungu na maneno yake. Na mfuateni yeye ili mpate kuongoka." [Al-A'araf: 158]. Na mazungumzo ya Mwenyezi Mungu na maneno yake hayakuumbwa; na ndiyo maana Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akitafuta ulinzi kwa maneno ya Mwenyezi Mungu akisema: "Yeyote atakayeshuka mahali popote, kisha akasema, 'Ninajikinga kwa maneno kamili ya Mwenyezi Mungu kutokana na shari ya kile alichoumba, basi hakuna chochote kitakachomdhuru, mpaka aondoke mahali hapo." (Imepokelewa na Muslim 2708, Tirmidhi 3437, na Ibn Majah 3547). Na lau kuwa maneno ya Mwenyezi Mungu yangelikuwa yameumbwa, basi Mtume wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, asingelitafuta kimbilio kwayo. Na maneno ya Mwenyezi Mungu hayakuumbwa, kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu alitenganisha kati ya kauli yake na viumbe vyake, na wala hakuviita kauli? Akasema: "Fahamuni! Kuumba ni kwake na amri ni yake." [Al-A'araf: 54] Aliposema, "Fahamuni! Kuumba ni kwake" hakuna kitu chochote kilichoumbwa kilichobakia isipokuwa kiliingia ndani yake. Kisha akataja kile ambacho hakikuumbwa. Akasema: "Na amri ni yake." kwa maana amri yake ni kauli yake. Mwenyezi Mungu ametakasika, Mola Mlezi wa walimwengu wote kiasi kwamba kauli yake haiwezi kuwa imeumbwa. (Tazama: Ar-Radd Alal-Jahmiyyah, cha Imam Ahmad uk. 224).
Na tunatofautisha kati ya maneno ya Mwenyezi Mungu ya kiulimwengu yaliyotajwa mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hakika walikanushwa Mitume wa kabla yako. Nao wakavumilia kule kukanushwa, na kuudhiwa, mpaka ilipowafikia nusura yetu. Na hapana wa kubadilisha maneno ya Mwenyezi Mungu. Na bila ya shaka zimekujia baadhi ya habari za Mitume hao." [Al-An'am: 34], Na kauli yake Mtukufu: "Sema: Lau kuwa bahari ndiyo wino kwa maneno ya Mola wangu Mlezi, basi bahari ingelimalizika kabla ya kumalizika maneno ya Mola wangu Mlezi, hata tungeli ileta mfano wa hiyo ili kuongezea." [Al-Kahf: 109], Na maneno yake ya kisheria mfano yaliyoko katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na yametimia maneno ya Mola Mlezi wako kwa kweli na uadilifu. Hapana awezaye kuyabadilisha maneno yake. Na Yeye ndiye Mwenye kusikia na Mwenye kujua." [Al-An'am: 115], Na kauli yake Mtukufu: "Na Mola wake Mlezi alipomjaribu Ibrahim kwa kumpa amri fulani, naye akazitimiza." [Al-Baqara: 124].
Amesema Imam Darami: "Na hakuna anayepinga kwamba Mwenyezi Mungu anazungumza isipokuwa yule anayetaka kubatilisha yale ambayo Mwenyezi Mungu aliteremsha. Na yule aliyewafunza waja kuzungumza, na akavitamkisha viumbe vyote anawezaje kukosa kuzungumza?!". (Ar-Radd Alal-Jahmiyyah, cha Darmi, uk. 155).
Na miongoni mwa sifa zake Yeye aliyetakasika ni kwamba ni Mwenye Nguvu (utukufu na enzi). Amesema Mola wa Haki: "Subhana Rabbi'l'Izzat (Ametakasika Mola Mlezi Mwenye enzi) na yale wanayomzulia." [As-Saffat: 180], Na akasema Mtukufu: "Mwenye kutaka utukufu, basi utukufu wote uko kwa Mwenyezi Mungu." [Fatir: 10].
Na miongoni mwa sifa zake Aliyetakasika na kutukuka, ni ushindi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema, "Hakika mimi ni muonyaji tu; na hapana mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu Mmoja, Mshindi." [Swad: 65].
Na miongoni mwa sifa zake ni kufanya atakalo, ufalme, ukubwa, na ukuu. Na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akisema katika kusujudu kwake: "Ametakasika yule mwenye kufanya atakavyo, mwenye ufalme, mwenye ukubwa na ukuu." (Imepokelewa na Abu Daud 873, Nasai 1049, Ahmad 23980, Tirmidhi katika Shamaail 314, na Al-Bazzar 2750). Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema, "Ukubwa ni vazi langu la juu, na ukuu ni vazi langu la chini. Kwa hivyo yeyote atakayeshindana nami katika moja ya hayo, nitamtupa Motoni." (Imepokelewa na Abuu Daud 4090, Ibn Majah 4174, Al-Humaidi 1183, Ibn Abi Shaiba 27111, na Ahmad 7382).
Na miongoni mwa sifa zake ni kutaka na kupenda, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu anawatakia yaliyo mepesi wala hawatakii mazito." [Al-Baqara: 185], Na kauli yake: "Na Mwenyezi Mungu anataka ahakikishe haki kwa maneno yake, na aikate mizizi ya makafiri." [Al-Anfal: 7], Na kauli yake: "Wala nyinyi hamtataka isipokuwa atake Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote." [At-Takwir: 29].
Na miongoni mwa sifa zake ni uwezo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na katika Ishara zake ni kuumba mbingu na ardhi, na wanyama aliowaeneza. Naye ni Mwenye uwezo wa kuwakusanya apendapo." [Ash-Shura: 29], Na kauli yake: "Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu." [Al-Baqara: 20].
Na miongoni mwa sifa zake ni rehema. Amesema Mwingi wa kurehemu, Mwingi wa rehema, Mtakatifu: "Na Rehema yangu imeenea kila kitu." [Al-A'araf: 156] Na amesema Mwenyezi Mungu, aliyetakasika na kutukuka: "Mola wenu Mlezi amejilazimisha rehema." [Al-An'am: 54], Rehema hii ni miongoni mwa sifa zake, nayo inafungamanishwa na Mwenyezi Mungu kwa njia ya kuifungamanisha sifa na anayesifiwa kwayo. Na rehema inaweza kuja katika Kitabu na Sunna huku imefungamanishwa na Mwenyezi Mungu kwa njia ya kufungamanisha kiumbe na Muumba wake, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Naye ndiye anayezituma pepo kuwa bishara njema kabla ya rehema yake, na tunayateremsha kutoka mbinguni maji safi." [Al-Furqan: 48]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akisema: "Hakika Mwenyezi Mungu aliumba rehema, siku alipoziumba huku zikiwa rehema mia moja." (Imepokelewa na Bukhari 6469, Muslim 2752, Tirmidhi 3541, na Ibn Majah 4293). Kwa hivyo hii ni rehema iliyoumbwa ambayo imefungamanishwa na Mwenyezi Mungu kwa njia ya kufungamanisha kiumbe na Muumba wake.
Na miongoni mwa sifa zake ni kwamba yuko juu. Na huku ni kuwa juu kwa njia ya ushindi, na kwa njia ya cheo, na dhati yake Yeye mwenyewe. Na zote tatu ni sifa zake, ambazo zinaashiria ukamilifu wake. Qur'ani tukufu na Sunna ya Mtume, na akili, na maumbile ya asili yameonyesha kwamba yuko juu kwa namna nyingi. Kwa hivyo kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu au Mtume wake, amani imshukie, walitujulisha kwamba Yeye ndiye Aliye juu au ndiye wa juu zaidi, basi hayo yote yanaonyesha kuwa yuko juu. Na kila habari ambayo ndani yake kuna kushuka kwa vitu vingine kutoka kwake kama vile kushuka kwa ufunuo, na amri, na kwamba Yeye huja na kwamba atakuja Siku ya Kiyama kutoa hukumu, au kwamba Yeye hushuka chini kila usiku, na usiku wa kuamkia siku ya 'Arafa, na kushuka kwa Malaika, basi hayo yote yanaonyesha kuwa yuko juu. Na pia kila habari ambayo ndani yake imeeleza kwamba yuko mbinguni, au kwamba Yeye yuko juu ya kiti cha enzi, au kwamba ameinuka juu ya kiti cha enzi, basi hayo yote yanaashiria kwamba yuko juu. Na vile vile kila kitu ambacho ndani yake kuna kupanda kwenda kwake na mfano wa hayo yote yanaashiria kuwa yuko juu.
Hii ni pamoja na kwamba Malaika wanamhofu Mola wao Mlezi kutoka juu yao, na kwamba wanapanda kwenda kwake, na kwamba matendo yananyanyuliwa kwenda kwake, na kwamba Mwenyezi Mungu alimnyanyua Isa, amani iwe juu yake, na akamsafirisha usiku Nabii wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na akampandisha mbinguni. Yote haya yanaonyesha kuwa yuko juu. Bali ushahidi wote unaoonyesha kwamba Mwenyezi Mungu yuko juu ni wa aina nyingi, na chini ya kila aina kuna vipengele vingi ambavyo havihesabiwi isipokuwa kwa ugumu mkubwa.
Na miongoni mwa ushahidi huu ni kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ni vyake vilivyomo mbinguni, na vilivyo katika ardhi. Na Yeye ndiye Aliye juu, Mkuu." [Ash-Shura: 4], Na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hayo ni kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye wa Kweli, na kwamba wale wanaowaomba badala yake, ni batili, na hakika Mwenyezi Mungu ndiye Aliye Juu na ndiye Mkubwa." [Al-Hajj: 62], Na kauli yake: "Kwake Yeye hupanda maneno mazuri, na matendo mema huyainuwa maneno hayo." [Fatir: 10], Na kauli yake Mola wa haki, Mtakatifu: "Na hiki ni Kitabu tulichokiteremsha, kilichobarikiwa. Basi kifuateni, na mcheni Mungu ili mrehemewe." [Al-An 'am: 155], Na kauli yake: "Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani kwa Kiarabu ili mpate kuzingatia." [Yusuf: 2], Na kauli yake aliyetakasika: "Wanamuhofu Mola wao Mlezi aliye juu yao, na wanafanya wanayoamrishwa." [An-Nahl: 50], Na kauli yake: "Mimi nitakufisha, na nitakunyanyua kwangu." [Al-Imran: 55], Na kauli yake: "Malaika na Roho hupanda kwenda kwake katika siku ambayo kipimo chake ni miaka hamsini elfu!" [Al-Maarij: 4] Na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ni yule ambaye ameziumba mbingu saba, na ardhi kwa mfano wa hizo. Amri zake zinashuka baina ya hizo, ili mjue kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kwa kukijua vilivyo kwa elimu yake." [At-Talaq: 12] Na kauli yake Mola wa Haki, aliyetakasika: "Bali Mwenyezi Mungu alimnyanyua kwenda kwake, na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima." [An-Nisaa: 158]. Na kauli ya Mola wetu Mlezi Mtukufu: "Ametakasika yule aliyemchukua mja wake usiku mmoja kutoka Msikiti Mtukufu (Makka) mpaka Msikiti wa mbali (Palestina), ambao tumevibariki vilivyo uzunguka, ili tumuonyeshe baadhi ya Ishara zetu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia na Mwenye kuona." [Al-Israa: 1].
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu alipomaliza uumbaji, aliandika kitabu kilicho pamoja naye: "Rehema yangu inashinda ghadhabu yangu." Au alisema: "Rehema yangu ilitangulia hasira yangu." Nacho kiko kwake juu ya kiti cha enzi." (Imesimuliwa na Bukhari 7553, Muslim 2751, Tirmidhi 3543, na Ibn Majah 189). Na imesimuliwa kutoka kwa Muawia bin Al-Hakam As-Sulamii, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Wakati nilipokuwa ninaswali pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, pale mtu mmoja miongoni mwetu alipiga chafya. Nikasema: "Yarhamukallah (Mwenyezi Mungu akurehemu)." Watu wote wakanitupia macho, nami nikasema: "Ewe msiba wa kumpoteza mamangu! (Nimepata hasara) Kwa nini mnaniangalia?" Basi, wakaanza kupiga mikono yao juu ya mapaja yao, na nilipowaona wakininyamazisha nilinyamaza kimya. Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake alipomaliza swala na akatoa salamu, (kwa kile nilichokiona kwake) ninaapa kumtoa fidia baba yangu na mama yangu kwa ajili yake! Kamwe sikuwahi kuona mwalimu bora kuliko yeye, kabla yake wala baada yake. Wallahi! Hakunikemea, wala hakunipiga, wala hakunitukana, lakini alisema: "Hakika, hii swala haifai ndani yake kitu chochote katika maneno ya watu. Bali Swala hii ni kufanya Tasbihi (kumtakasa Mwenyezi Mungu), na Takbir (kumtukuza Mwenyezi Mungu), na kusoma Qur'ani tu." au kama alivyosema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake. Nikasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi nimesilimu tu hivi karibuni, na bila shaka Mwenyezi Mungu ameleta Uislamu huu, na hakika miongoni mwetu kuna wanaume ambao wanawaendea makuhani (waaguzi)." Akasema: "Usiwaendee (makuhani)" Nikasema: "Na miongoni mwetu, kuna wanaume ambao wanaathirika na ndege kwa kuamini mikosi (au vitu mfano wake)." Akasema: "Hicho ni kitu wanachokipata katika vifua (mioyo) yao, lakini kamwe kusiwazuie (Kutofanya jambo kwa kuamini mikosi)." Ibn Swabah anasema: "Kamwe kusiwazuie." Akasema (Mu'awiya) Nikasema: "Na miongoni mwetu, kuna wanaume wanaochora mistari (kisha wanatabiri kwayo)." Akasema: "Kulikuwa na Nabii miongoni mwa Manabii aliyekuwa akichora mistari. Kwa hivyo, mwenye kuiafiki mistari yake, basi (jambo lake) linakuwa hivyo." Akasema: "Nilikuwa na mtumishi wa kike ambaye alikuwa akiwachunga kondoo wangu upande wa Uhud na Jawania. Siku moja, nilimwangalia (akiwa anawachunga) nikakuta kuwa mbwa mwitu alikuwa amekwenda na kondoo mmoja katika kondoo hao. Na mimi ni mwanadamu, ninakasirika kama wanavyokasirika (watu wengine). Kwa hivyo, nikampiga kofi. Kisha nikamjia Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake na akaliona hilo kuwa kitu kibaya sana juu yangu. Nikasema: "Je, nimuache huru?" (Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie) akasema: "Mlete kwangu." Kwa hivyo, nikampeleka kwake, akamuuliza, "Mwenyezi Mungu yuko wapi?" Akasema: "Juu mbinguni." Akasema: "Mimi ni nani?" Akasema: "Wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu." Akasema: "Muache huru, kwa hakika huyu ni Muumini." (Imesimuliwa na Muslim 537, Abu Daud 930, na Nasai 1218).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi nae, alisema kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: “Wanabadilishana kwenu nyinyi Malaika wa usiku na Malaika wa mchana, nao wanakusanyika katika swala ya Alfajiri na swala ya Lasiri, kisha wale waliokuwa pamoja nanyi usiku wanapanda juu, na anawauliza, ilhali Yeye ndiye ajuaye zaidi: Je, mmewaachaje waja wangu?" Wanasema: "Tumewaacha wakiwa wanaswali, na tuliwakuta wakiwa wanaswali." (Imesimuliwa na Bukhari 7553, Muslim 2751, Tirmidhi 3543, na Ibn Majah 189). Na katika hadithi ya Abuu Razin Al-'Uqaili, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema, 'Nilisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mola wetu Mlezi alikuwa wapi kabla hajaumba viumbe wake?' Akasema: "Alikuwa juu ya wingu ambalo chini yake kuna hewa, na juu yake kuna hewa, na aliumba kiti chake cha enzi juu ya maji". (Imepokelewa na Tirmidhi 3109, Ibn Majah 182, Tayalisi 1189, Ahmad 16188 na Ibn Abi Asim katika Sunnah 625). Haya na mengine mengi zaidi ya haya miongoni mwa Aya na hadithi zinazoonyesha kuwa Mwenyezi Mungu yuko juu.
Na ushahidi unaoonyesha kwamba Mwenyezi Mungu yuko juu ni mwingi zaidi kuliko inavyoweza kuhesabiwa. Na wanachuoni wa Kiislamu walikubaliana juu ya kuthibitisha hilo, kama lilivyoonyeshwa na akili na maumbile ya asili yaliyo salama, amesema Imam Ibn Battah, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Na Waislamu walikubaliana kuanzia kwa Maswahaba na wale waliofuata baada yao na wanazuoni wote waumini kwamba Mwenyezi Mungu mwingi wa baraka, Mtukufu yuko juu ya kiti chake cha enzi, juu ya mbingu zake, bila ya kuchanganyika na viumbe wake, na kwamba elimu yake imezunguka viumbe wake wote." (Al-Ibana Al-Kubra, cha Ibn Batta 7/136).
Na alinukuu Ad-Darmi, Mwenyezi Mungu amrehemu, kauli ya Ibn Mubarak akisema alipoulizwa: "Tunamjuaje Mola wetu Mlezi?" Akasema: Nikuwa yuko juu ya kiti cha enzi, juu ya mbingu ya saba, juu ya kiti cha enzi, bila ya kuchanganyika na viumbe vyake." (Arraddu Alal-Jahmiyyah, cha Darmi uk. 98).
Miongoni mwa sifa zake ni: Kutulizana juu ya kiti cha enzi, Mwenyezi Mungu amelitaja hilo katika sehemu saba ndani ya kitabu chake, ikiwemo kauli yake: "Hakika Mola Mlezi wenu ni Mwenyezi Mungu aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Kisha akatulizana juu ya Kiti cha Enzi. Huufunika usiku kwa mchana, ufuatao upesi upesi. Na jua, na mwezi, na nyota zinazofanya kazi kwa amri yake. Fahamuni! Kuumba ni kwake na amri ni Yake. Ametukuka kabisa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-A'araf: 54], Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwamba alisema kuwa: Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mwenyezi Mungu alipomaliza uumbaji, aliandika kitabu kilicho kuwa kwake kimeandikwa: "Rehema yangu imeshinda ghadhabu yangu." au alisema: "Rehema yangu ilitangulia hasira yangu. Nacho kiko kwake juu ya kiti cha enzi." (Imesimuliwa na Bukhari 7553, Muslim 2751, Tirmidhi 3543, na Ibn Majah 189). Na aliandika Al-Lalakaii kutoka kwa Ibn Uyaina kwamba alisema: Aliulizwa Rabi’a kuhusu kauli yake: “Arrahmani (Mwingi wa Rehema), ametulizana juu ya Kiti cha Enzi.” [Taha: 5]: Ametulizana vipi juu? Akasema: 'Kuinuka juu ni jambo linalojulikana, lakini namna ilivyo ndiyo haijulikani, na kilicho kwa Mwenyezi Mungu ni kutuma ujumbe, na wajibu wa Mtume ni kufikisha ujumbe, na wajibu wetu ni kusadikisha." (Sharh Usul Itikad Alhus-Sunna Wal-Jamaa' 3/442, Al-'Arsh cha Dhahabi 2/213). Na kauli kama hii iliripotiwa kutoka kwa Imamu wa Dar al-Hijrah, Imam Malik, Mwenyezi Mungu amrehemu. (Imesimuliwa na Abuu Nu'aim katika Al-Hilya 6/325, 326, na Baihaqi katika Al-Asmaa Was-Swifaat 304/2, na Ibn 'Abd-al-Barr katika Tamhid 7/138. Na Dhahabi, Mwenyezi Mungu amrehemu, alisema: "Wanachuoni walichukua kutoka kwa kauli ya Imamu Malik, "kuinuka juu ni jambo linalojulikana, lakini namna lilivyo hilo haswa haijulikani, na kuliamini ni wajibu, na kuuliza juu yake ni uzushi." kuwa ni kanuni waliyoifuata katika mlango huu." Tazama: Al-'Uluu cha Dhahabi 1/117).
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu ni upendo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi Mwenyezi Mungu atawaleta watu anaowapenda nao wanampenda." [Al-Maida: 54], Amesema Imam Darmi, Mwenyezi Mungu amrehemu: “Kwa hivyo akawa amaeunganisha kati ya mapenzi mawili: Upendo wa Muumba na upendo wa kiumbe kwa pamoja, kisha akatofautisha kati ya kile kinachopendwa na kisichopendwa; Ili viumbe wake wajue kwamba hayo mawili ni kinyume na hayaingiliani. Akasema: "Mwenyezi Mungu hapendi kutoa maneno ya kutangaza ubaya." [An-Nisa: 148], na akasema: "Hakika Yeye hawapendi watumiayo kwa fujo." [Al-An'am: 141]. (Naqdh Ad-Darmi 2/865).
Na amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wanaotubu, na huwapenda wanaojisafisha." [Al-Baqara: 222] Na imesimuliwa kutoka kwa Sahl bin Saad, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema: Alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake siku ya vita Khaibari: "Hakika kesho nitampa bendera mwanaume ambaye ushindi utapatikana kupitia mikono yake, anampenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na Mwenyezi Mungu na Mtume wake wanampenda pia." (Imesimuliwa na Bukhari 3009, Muslim 2406, na Abu Dawud 3661). Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake “Hatokuwa na sifa ya imani mmoja wenu mpaka niwe kipenzi zaidi kwake kuliko baba yake na mtoto wake na watu wote." (Imesimuliwa na Bukhari 15, Muslim 44, Nasai 5013, na Ibn Majah 67).
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu ni kuridhia, amesema Mola wa haki Mtukufu: "Na wale waliotangulia, wa kwanza, katika watu wa Makkah (Waliohama) na watu wa Madina (Waliowapokea), na waliowafuata kwa wema, Mwenyezi Mungu ameridhika nao, na wao wameridhika naye." [Tauba: 100] Imesimuliwa kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Nilikosa kumuona Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, usiku mmoja kwenye malazi, kwa hivyo nikamtafuta, na mkono wangu ukashika ndani ya miguu yake huku akiwa msikitini, na miguu hiyo ilikuwa imesimamishwa huku akisema: "Ewe Mwenyezi Mungu, ninajikinga kwa radhi zako kutokana na ghadhabu yako, na kwa usalama wako kutokana na adhabu yako, na ninajikinga kwako kutokana na wewe, wala siwezi kuhesabu sifa zako, kama ulivyojisifu wewe mwenyewe." (Imepokelewa na Muslim 486, Abu Daud 879, Tirmidhi 3493, An-Nasai 169, na Ibn Majah 3841).
Na katika sifa zake Mtukufu ni kuchukia kwake maadui zake. Na hilo ni kwa sababu walichukia radhi zake, na walichukia kile ambacho Mwenyezi Mungu alimteremshia Mtume wake, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na amani, amesema Mtukufu : "Hayo ni kwa sababu wao waliyafuata yaliyomchukiza Mwenyezi Mungu na wakachukia yanayomridhisha, basi akaviporomosha vitendo vyao." [Muhammad: 28] Na kauli yake: "Lakini Mwenyezi Mungu kachukia kutoka kwao, na kwa hivyo akawazuia na ikasemwa: Kaeni pamoja na wanaokaa!" [At-Tauba: 46]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa amesema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu alisema: "Pindi mja wangu anapopenda kukutana nami, mimi pia ninapenda kukutana naye. Na pindi anapochukia kukutana nami, mimi pia ninachukia kukutana naye." (Imesimuliwa na Bukhari 7504, na An-Nasai 1835).
Na miongoni mwa sifa zake ni kuwaghadhibikia maadui zake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu awakasirikie, na awalaani." [Al-Fat-h: 6] Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: "Ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iliongezeka juu ya yule aliyeuliwa na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake katika njia ya Mwenyezi Mungu. Ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iliongezeka juu ya watu walioutoa damu uso wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake. (Imesimuliwa na Bukhari 4074).
Na katika sifa zake Mtukufu ni kuwachukia makafiri, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika wale waliokufuru watatatangaziwa: Bila ya shaka Mwenyezi Mungu kukuchukieni ni jambo kubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu." [Ghaafir :10].
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu: Ni kuwapangia njama maadui zake ambao wao pia huwapangia njama vipenzi vyake. Mola Mtukufu anasema: "Basi wakapanga njama yao, na Sisi tukapanga njama yetu, bila ya wao kutambua * Basi angalia ulivyokuwa mwisho wa njama yao, ya kwamba tuliwaangamiza wao pamoja na watu wao wote." [An-Naml: 50, 51].
Na katika sifa zake Mtukufu: Ni ghadhabu kubwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Walipotukasirisha mno, tuliwapatiliza tukawazamisha wote!" [Az-Zukhruf: 55] Katada na As-Suddi wanasema: "Nayo inamaanisha kwamba pindi "walipotukasirisha mno". (Tafsir Tabari 21/622).
Na miongoni mwa sifa zake ni kuwahadaa wale wanaomhadaa, Mwenyezi Mungu huwahadaa wanafiki wanaomhadaa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wanatafuta kumdanganya Mwenyezi Mungu na wale walioamini, lakini hawadanganyi ila nafsi zao; nao hawatambui." [Al-Baqara: 9], Na amesema: "Hakika wanafiki wanamhadaa Mwenyezi Mungu, na hali Yeye ndiye mwenye kuwahadaa wao." [An-Nisaa: 142].
Na alibainisha Mola wa haki kwamba atawasahau maadui zake kama walivyosahau suala la kukutana naye, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ambao waliifanya dini yao kuwa ni pumbao na mchezo, na maisha ya dunia yakawadanganya. Basi leo Sisi tunawasahau kama walivyousahau kukutana na Siku yao hii." [Al-A'araf: 51].
Miongoni mwa sifa zake Mtukufu: Ni kwamba anawadhihaki wale wanaomdhihaki, amesema Mwenyezi Mungu: "Mwenyezi Mungu anawadhihaki wao na anawaacha katika upotofu wao wakitangatanga ovyo." [Al-Baqara: 15]. Amesema bin Abbas, Mwenyezi Mungu awaridhie: "Anawadhihaki ili kuwaadhibu." (Tafsir Twabari 1/304, na Ibn Abi Hatim katika Tafsir 143).
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu: Ni kucheka. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwamba alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu: "Mwenyezi Mungu anawacheka watu wawili, mmoja anaua mwingine, kisha wote wawili wanaingia Peponi." (Imesimuliwa na Bukhari 2826, Muslim 1890), An-Nasai 3166, na Ibn Majah 191). Katika hadithi ndefu ya Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuhusu kumuona Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama, na akataja ndani yake kisa cha mtu wa mwisho kuingia Peponi: “...Kisha Mwenyezi Mungu atasema: Ole wako, ewe mwanadamu. ni ukubwa ulioje wa kuvunja kwako ahadi! Je, hukutoa ahadi na maagano kuwa hutaomba kitu chochote zaidi ya kile ulichopewa? Atasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Usinifanye kuwa mbaya mno kati ya viumbe vyako. Basi Mwenyezi Mungu Mwenye Nguvu na Mtukufu atacheka kwa sababu ya kitendo chake hiki, kisha atamruhusu aingie Peponi." (Imesimuliwa na Bukhari 806).
Amesema Wakii: "Mkiulizwa: Je, Mola wetu Mlezi anacheka? Basi semeni: "Ndivyo tulivyosikia." (Sharh Usul Itikad Ahlus-Sunna wala-Jamaa 3/477).
Hafidhi bin Battah, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango katika kitabu chake Al-Ibanah "Mlango wa kuamini kwamba Mwenyezi Mungu anacheka" na akasema ndani yake: "Jueni - Mwenyezi Mungu awarehemu - kwamba moja ya sifa za waumini miongoni mwa watu wa haki ni kusadikisha simulizi zilizo sahihi, na kuzipokea kwa kuzikubali, kuacha kuzipa mgongo kwa sababu ya kuzilinganisha (Qiyas), na kuchagua kusema tu kwa maoni na matamanio, imani ni kusadikisha, na muumini ni yule anayesadikisha. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "La! Ninaapa kwa Mola wako Mlezi! Hawataamini mpaka wakufanye wewe ndiye muamuzi katika yale wanayohitalifiana, kisha wasione uzito katika nyoyo zao juu ya hukumu utakayotoa, na wanyenyekee kabisa." [An-Nisa: 65]. Na katika alama za waumini ni kumwelezea Mwenyezi Mungu kwa yale aliyojielezea yeye mwenyewe, na kwa yale aliyomuelezea Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika yale waliyoyanukuu wanazuoni wanaoaminika katika yale waliyoyasimulia miongoni mwa mambo ya halali na ya haramu na Sunna na simulizi zinginezo. Haifai kusema kuhusiana na chochote kilichotoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwa njia sahihi, "Vipi? wala kwa nini?" Badala yake, wanafuata na wala hawazui. Na wanasalimu amri wala hawapingi. Na wana yakini na wala hawana shaka. Kwa hivyo ikajulikana kwamba yale yaliyosimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwa njia sahihi ambayo yamesimuliwa na watu waadilifu na wale ambao inawalazimu waumini kukubali simulizi zao na kuacha kuwapinga katika kuamini kuwa: Mwenyezi Mungu Mtukufu anacheka. Kwa hivyo, halipingi hilo wala halikatai hilo isipokuwa mzushi ambaye anakashifiwa hali yake mbele ya wanazuoni." (Al-Ibana Al-Kubra, cha Ibn Batta 7/91).
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu: Ni kujongea na kuja siku ya Kiyama ili kutoa hukumu kati ya watu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wanangoja jingine ila wawafikie Malaika, au awafikie Mola wako Mlezi, au zifike baadhi ya Ishara za Mola wako Mlezi?" [Al-An'am: 158], Na amesema Mtukufu: "Na akaja Mola wako Mlezi na Malaika safu safu." [Al-Fajr: 22], Na amesema Mtukufu: "Je wanangoja mpaka Mwenyezi Mungu awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika, na hukumu iwe imekwishatolewa? Na kwa Mwenyezi Mungu ndiko hurejeshwa mashauri yote." [Al-Baqara: 210]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa amesema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Atawakusanya Mwenyezi Mungu watu wote siku ya Kiyama, kisha atasema: "Yeyote aliyekuwa akiabudu kitu, basi na akifuate..." Na akaendelea kuisimulia hadithi hii hadi katika kauli yake: “Na umma huu utabaki, nao watasema: Tutabaki mahali hapa mpaka atakapotujia Mola wetu Mlezi, na atakapokuja Mola wetu tutamjua, kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu atawajia na kuwaambia: Mimi ndiye Mola wenu Mlezi. Nao watasema: Wewe ndiye Mola wetu Mlezi. Kisha watamfuata." (Imesimuliwa na Bukhari 806, Muslim 182, Abu Daud 4730, Tirmidhi 2554, na Ibn Majah 178).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Aaliya kuhusiana na maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je wanangoja mpaka Mwenyezi Mungu awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika?" [Al-Baqara: 210] Anasema: "Malaika watakuja katika vivuli vya mawingu, na Mwenyezi Mungu atakuja kama apendavyo." (Al-Asmaa wal-Swifat, cha Al-Baihaqi 2/370).
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu: Ni kwamba Yeye hushuka hadi mbingu ya chini kabisa kushuka kwa kweli ambako kunaendana na utukufu wake na ukuu wake. Na kushuka huku si kama kushuka kwa viumbe, lakini huko ni kama sifa zake zinginezo ambazo tunaziamini na tunazijua, wala hatusemi jinsi zilivyo haswa, wala kujisumbua kuzikataa; badala yake, tunaziamini kama alivyotueleza Mtume wetu mkweli, anayeaminika, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Inapopita nusu ya usiku, au theluthi mbili yake, Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka hushuka kwenye mbingu ya chini, na kusema: Je, kuna yeyote anayeomba, ili apewe? Je, kuna yeyote anayeomba dua ili aitikiwe? Je, kuna anayetaka msamaha ili asamehewe? Mpaka asubuhi iingie." (Imepokelewa na Muslim 758).
Imam wa Maimamu, Muhammad bin Khuzaima, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango katika kitabu chake "Attauhid" Alisema: “Mlango wa habari zenye msururu wa wasimulizi madhubuti, zenye msingi sahihi, ambazo zilisimuliwa na wanazuoni wa Hijazi na Iraq kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuhusiana na kushuka kwa Mola Mlezi hadi kwenye mbingu ya chini kabisa kila usiku. Tunashuhudia ushahidi wa mwenye kukiri kwa ulimi wake, na mwenye kusadikisha kwa moyo wake, na ana yakini juu ya yale yaliyo katika simulizi kuhusu kutajwa kushuka kwa Mola Mlezi, bila ya kuelezea namna kushuka huko kulivyo; Kwa sababu Nabii wetu mteule hakutueleza jinsi Muumba wetu anavyoteremka hadi kwenye mbingu ya chini, na alitufahamisha kuwa anashuka, na Mwenyezi Mungu Mtukufu na Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hawakupuuza kueleza wanachohitaji Waislamu katika masuala ya dini yao. Kwa hivyo, sisi tunasema na kusadikisha yale ambayo simulizi hizi zinataja juu ya kushuka, bila ya kujitwika mzigo wa kusema ni vipi lilivyo hilo, kwa maana Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakutuelezea namna kulivyo kushuka huko." (Tauhid, cha Ibn Khuzaima 1/289).
Hafidhi bin Battah, Mwenyezi Mungu amrehemu, alisema katika kitabu chake "Al-Ibana": "Mlango wa imani na kusadikisha kuwa Mwenyezi Mungu hushuka kila usiku kwenye mbingu ya chini bila kutoka aliko wala kuelezea namna linavyofanyika haswa. Kisha, Mwenyezi Mungu amrehemu, akasema: “Jueni - Mwenyezi Mungu awarehemu - kwamba Mwenyezi Mungu amewawajibishia waja wake Waumini kumtii Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na kuyakubali yale aliyoyasema na kuja nayo, na kuamini kila lililosimuliwa kutoka kwake kwa njia sahihi, na kusalimu amri katika hilo kwa kuacha kuyapa mgongo na kuyapigia mifano, na kuyalinganisha na vinginevyo, na kusema: Kwa nini? wala vipi?... Ilisimuliwa kwa njia sahihi kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: “Mola wetu Mlezi Aliyetakasika na kutukuka hushuka kila usiku kwenye mbingu ya chini inapobakia theluthi ya mwisho ya usiku, na anasema: “Ni nani anayeniomba ili nimuitikie? Ni nani anayenitaka kitu ili nimpe? Ni nani anayeniomba msamaha ili nimsamehe?" Katika hadithi ndefu tutakayoitaja, Mwenyezi Mungu akipenda, kwa ukamilifu wake, iliyosimuliwa na maimamu wa kisasa, wa waaminifu, wa kuaminika na wanazuoni wa Fiqh wacha Mungu, ambao walitufikishia sheria ya Uislamu na nguzo zake, kama vile swala, Zaka, kufunga saumu, Hija, jihadi, na hukumu nyinginezo kama vile ya kuoa, talaka, biashara, halali na haramu. (Al-Ibana Al-Kubra, Ibn Batta 7/201. Hadithi hii imepokelewa na Bukhari 1145, Muslim 758, Abu Dawud 1315, Tirmidhi 446, na Ibn Majah 1366).
Na tunaamini sifa ya kuwa pamoja kwa Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu, na kwamba Mwenyezi Mungu yuko pamoja na viumbe vyake kwa elimu yake, na kuvidhibiti, na mapenzi yake. Na hilo limethibitishwa na Kitabu na Sunna, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu anajua vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi? Hauwi mnong'ono wa watu watatu ila Yeye huwa ni wanne wao, wala wa watano ila Yeye huwa ni wa sita wao. Wala wa wachache kuliko hao, wala walio wengi zaidi, ila Yeye yu pamoja nao popote pale walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawaambia waliyo yatenda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu." [Al-Mujadilah: 7].
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: “Zioneeni huruma nafsi zenu na muhifadhi sauti zenu. Kwa maana nyinyi kwa hakika hamumuombi kiziwi wala asiyekuwepo, nyinyi kwa hakika mnamuomba Mwenye kusikia vyema, aliye karibu, naye yu pamoja nanyi.” (Imesimuliwa na Bukhari 4205, Muslim 2704, Abuu Daud 1526, na Tirmidhi 3461).
Na kuwa kwake pamoja nanyi huku ni kwa aina mbili:
Kuwa kwake pamoja nanyi maalumu, ambako ni kwa Mitume wa Mwenyezi Mungu, amani iwe juu yao, na vipenzi wake, na muktadha wake ni: Kuwanusuru na kuwasaidia, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Akasema: Msiogope! Hakika Mimi ni pamoja nanyi. Nasikia na ninaona." [Twaha: 46].
Kuwa kwake pamoja nanyi kwa ujumla: Nako ni kuwa Mwenyezi Mungu yu pamoja na viumbe vyote, waumini wao na makafiri wao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Naye yu pamoja nanyi popote mlipo " [Al-Hadid: 4] Maana ya upamoja huu ni elimu yake, kuwadhibiti kwake, uwezo wake na mamlaka yake juu yao.
Na upamoja wake huu haupingani na kuwa kwake juu Yeye Mtukufu. Kwa sababu maana yake - kama ilivyotangulia kulingana na makubaliano ya wanazuoni ni elimu yake na kuwazunguka kwake.
Na miongoni mwa sifa zake Mtukufu ni kustaajabu. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Mwenyezi Mungu anawastaajabu watu wanaoingia Peponi wakiwa wamefungwa minyororo." (Imesimuliwa na Bukhari 3010, na Abu Daud 2677). Na imesimuliwa kutoka kwa 'Ukuba bin Amiri, Mwenyezi Mungu amridhie alisema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake akisema: "Mola wenu Mlezi anamstaajabia mchungaji wa kondoo katika kilele cha kipande cha mlima, ambaye anaadhini kwa ajili ya swala, kisha akaswali, kwa hivyo Mwenyezi Mungu anasema: Mtazameni mja wangu huyu, anaadhini, kisha anasimamisha swala kwa kunihofu. Hakika nimeshamsamehe mja wangu huyu, na nimemuingiza katika Bustani za mbinguni." (Imesimuliwa na Abu Daud 1203, Nasa'i 666, Ahmad 17312, Ibn Abi' Asim katika Sunnah 584, na Ar-Ruwayani 232).
Na tunaamini waumini kumuona Mola wao Mlezi siku ya Kiyama, kama inavyothibitishwa na Kitabu (Qur'ani), na habari za Mtume wetu (rehema na amani za Allah zimshukie) juu ya yale aliyowapa habari njema waumini kuwa watamuona Mola wao siku ya Kiyama - na hii - Wallahi namuapa Mwenyezi Mungu - ni neema kubwa zaidi kwa watu wa Peponi - Mwenyezi Mungu anasema: "Zipo nyuso siku hiyo zitao ng'ara * "Zikimwangalia Mola wao Mlezi." [Al-Qiyama: 22, 23], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa wafanyao wema watalipwa wema na zaidi nao nikumuona mola wao." [Yunus: 26], Na kauli yake Mtukufu: "Hasha! Hakika hao siku hiyo bila ya shaka watazuiliwa na neema za Mola wao Mlezi." [Al-Muttaffifin: 15]. Imam Malik aliulizwa: Ewe Abu Abdullah: Je, waumini watamuona Mola wao Mlezi siku ya Kiyaama? Akasema: 'Lau kuwa Waumini hawatamuona Mola wao Mlezi Siku ya Kiyama, basi Mwenyezi Mungu asingeliwakashifu makafiri kuwa watazuiliwa na pazia wasimuone Mola wao siku ya Kiyama." Akasema: "Hasha! Hakika hao siku hiyo bila ya shaka watazuiliwa na neema za Mola wao Mlezi." (Sharhu usuulu Itiqad Ahlus sunna (2/468).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Saidi Al-Khudri Mwenyezi Mungu amrdhie, kuwa: Tulisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Je, tutamuona Mola wetu Mlezi siku ya Kiyama?" Akasema: "Je, mnapata shida yoyote katika kuona jua na mwezi wakati mbingu ni safi?" Tukasema: "Hapana." Akasema: "Kwa hivyo, nyinyi kwa hakika, hamtapata shida yoyote katika kumuona Mola wenu Mlezi siku hiyo kama vile ambavyo hampati shida yoyote katika kuviona hivyo viwili (yani jua na mwezi katika mbingu safi)." Kisha Mtume akasema: "Mwenye kutangaza atatangaza," Na uende kila umma kwa kile walichokuwa wakiabudu." Basi, watu wa msalaba watakwenda pamoja na msalaba wao, na waabudu masanamu pamoja na masanamu yao, na watu wa kila miungu pamoja na miungu yao, mpaka watakapobakia wale waliokuwa wakimwabudu Mwenyezi Mungu, miongoni mwa wema na waovu, na baadhi ya watu kutoka kwa watu wa Kitabu. Kisha Jahannam italetwa mbele yao kana kwamba ni mazigazi, kisha Mayahudi wataambiwa: "Mlikuwa mkiabudu nini?" Watasema: "Tulikuwa tukimuabudu Ezra, mwana wa Mungu." Wataambiwa: "Mmedanganya, kwa kuwa Mwenyezi Mungu hakuwa na mke wala mwana. Basi mnataka nini (sasa)?" Watasema: "Tunataka mtupe maji ya kunywa." Kisha wataambiwa: "Kunyweni," kwa hivyo, wataanguka ndani ya Jahannam, kisha wataambiwa Wakristo: "Mlikuwa mkiabudu nini?' Watasema: "Tulikuwa tukimuabudu Masihi (Yesu), mwana wa Mungu." Itasemwa: "Mmedanganya, kwa kuwa Allah hana mke wala mwana. Sasa mnataka nini? "Watasema: "Tunataka mtupe maji ya kunywa." Wataambiwa: "Kunyweni." kwa hivyo, wataanguka ndani ya Jahannam. Mpaka watakapobaki tu wale waliokuwa wakimuabudu Allah (peke yake), miongoni mwa wema (watiifu) na waasi, nao wataambiwa: "Ni nini kinachokukalisheni hapa ilhali watu wote wameshakwenda?" Watasema: "Sisi tuliachana nao (duniani) wakati tulipokuwa tunawahitaji sana kuliko leo. Nasi kwa hakika, tulisikia mtangazaji akitangaza,' Kila kaumu (watu) wafuate walichokuwa wakiabudu" na sasa sisi tunamsubiri Mola wetu Mlezi." Kwa hivyo, Al-Jabbari (Mwenyezi Mungu Anaye fanya analo litaka) atawajia kwa sura isiyokuwa ile waliyomuona kwayo mara ya kwanza. Na atasema "Mimi ni Mola wenu Mlezi." Na watasema: "Wewe ni Mola wetu Mlezi. Na hakuna atakayezungumza naye isipokuwa Manabii, na kisha wataambiwa: "Je, mnajua ishara yoyote ambayo mnaweza kumjua kwayo?" Watasema: "Muundi." Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu atafunua muundi wake na hapo, kila Muumini atamsujudia." (Imesimuliwa na Bukhari (7439), na Muslim (183)
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakika nyinyi mtamuona Mola wenu Mlezi kama mnavyouona mwezi huu, bila ya kusongamana katika kuuona." (Imesimuliwa na Bukhari (554), Muslim (633), Abu Daud (4729), Tirmidhi (2551), na Ibn Majah (177).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema kuwa: Watu walisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je tutamuona Mola wetu Siku ya Kiyama? Akasema: "Je, mnapata shida yoyote katika kuuona mwezi usiku wa mwezi kamili, ambapo hakuna mawingu?" Wakasema: Hapana, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Akasema: "Je, mnapata shida yoyote katika kuliona jua ambapo hakuna mawingu yoyote mbele yake?" Wakasema: "Hapana." Akasema: "Basi nyinyi kwa hakika mtamuona vivyo hivyo. Watu watakusanywa siku ya Kiyama, kisha atasema: “Aliyekuwa akiabudu chochote, basi na akifuate.” Kwa hivyo, miongoni mwao wapo watakaolifuata jua, na miongoni mwao wapo watakaoufuata mwezi, na miongoni mwao wapo watakaofuata Taghuti (chochote kiabudiwacho badala ya Mwenyezi Mungu), na watabakia umma huu ilhali ndani yao kuna wanafiki wake. Kisha Mwenyezi Mungu atawajia na kuwaambia: "Mimi ndiye Mola wenu Mlezi." Nao watasema: "Sisi tunabakia mahala petu hapa mpaka atakapotujia Mola wetu Mlezi. Na Mola wetu Mlezi atakapotujia, tutamjua." Kisha Mwenyezi Mungu atawajia na atasema: "Mimi ndiye Mola wenu Mlezi.” Watasema: "Wewe ndiwe Mola wetu Mlezi." Kisha atawaita, na itawekwa njia juu ya migongo miwili ya Jahannam, nami nitakuwa wa kwanza katika Mitume kuivuka pamoja na umma wangu, na wala siku hiyo hawatasema ila Mitume tu, na maneno yao siku hiyo yatakuwa: "Ewe Mwenyezi Mungu, tupe salama, tupe salama!". (Imesimuliwa na Bukhari 806, Muslim 182, Abu Daud 4730, Tirmidhi 2554, na Ibn Majah 178).
Kwa hivyo, hadithi za kumuona Mwenyezi Mungu - na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu - ni nyinyi kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake. Na hakuna pingamizi la kumuona katika kauli yake: "Alisema: Mola wangu Mlezi! Nionyeshe nikutazame. Mwenyezi Mungu akasema: Hutoniona. Lakini utazame huo mlima. Ukibaki pahala pake basi utaniona." [Al-A'raf: 143], kwa sababu hilo ni hapa duniani. Na hilo ni sawa na kauli yake Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika jibu lake kwa Abu Dharri, Mwenyezi Mungu amridhie, alipomuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Je, ulimuona Mola wako Mlezi?" Akasema: "Ni nuru, nitamuonaje." (Imesimuliwa na Muslim (178), na Tirmidhi (3282). Kwa hivyo, Nabii wetu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakumuona Mola wake Mlezi usiku wa alipopandishwa mbinguni. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alituambia juu ya ishara alizomtukuza kwazo siku hiyo ya kupandishwa mbinguni, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ametakasika yule aliyemchukua mja wake usiku mmoja kutoka Msikiti Mtukufu wa Makka mpaka Msikiti wa Aqswaa uliopo Palestina, ambao tumevibariki vilivyo uzunguka, ili tumuonyeshe baadhi ya Ishara zetu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia na Mwenye kuona." [Al-Israa: 1]. Na Mwenyezi Mungu hakutaja kuwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimuona Mola wake Mlezi, na kama angemuona Mola wake Mlezi, basi Mwenyezi Mungu angelitaja hilo ili kuonyesha neema yake juu yake.
Vivyo hivyo, kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Macho hayamfikii bali Yeye anayafikia macho. Naye ni Mjuzi, Mwenye khabari." [Al-An 'am: 103], Haionyeshi kukanusha kumuona, kwa sababu kumfikia sawa sawa kuna maana zaidi kuliko kuona tu. Na pia Aya zilizotangulia aya hii zilikuja katika muktadha wa kusisitiza upweke wa Mwenyezi Mungu na kukanusha kuwa kwake na mwana, na sio katika habari za maisha ya akhera ndiyo aya hii ihusiane na kumuona Mwenyezi Mungu.
Amesema Darami, Mwenyezi Mungu amrehemu: Hadithi hizi zote - na nyingine zaidi - zilisimuliwa kuhusiana na kumuona Mwenyezi Mungu, tunazisadikisha na kuziamini kama tulivyowakuta wanazuoni wa Fiqh na maono sahihi miongoni mwa mashehe wetu wakiziamini. Na waislamu hawajaacha kuanzia kitambo na hata leo kuzisimulia na kuziamini, wala hawazifanyii kiburi na kuzikataa. Na mwenye kuzikataa miongoni mwa watu wapotovu walikuwa wakimfanya kuwa ni mpotofu. Bali ilikuwa ni katika matumaini yao makubwa zaidi na thawabu nyingi zaidi za Mwenyezi Mungu kwao ni kuuangalia uso wa Muumba wao kiasi kwamba hawalinganishi hilo na chochote miongoni mwa neema za Bustani za mbinguni. (Arraddu Alal-Jahmiyya, cha Darami (uk. 122).
Amesema Imamu wa wafasiri, Ibin Jariri Al-Ttabari, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Na ama lililo sahihi katika kauli inayohusiana na waumini kumuona Mwenyezi Mungu siku ya Kiyama - ambayo ndiyo dini yetu ambayo tunamuabudu kwayo Mwenyezi Mungu, na ambayo tuliwakuta juu yake Ahlus-Sunna wal-Jamaa - ni kwamba watu wa Bustani ya mbinguni watamuona Mwenyezi Mungu kulingana na habari sahihi zilizosimuliwa kuhusiana na hili kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake." (Swariihus sunna, cha Tabari (uk. 20).
Amesema Ibin Battah, Mungu amrehemu: "Nao walitaka katika kupinga kumuona Mwenyezi Mungu kubatilisha umola wake, kwa maana, pindi watakapokiri uwezekano wa kumuona, basi watakuwa wameshakiri umola wake. Kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu amefanya thawabu za mwenye kumsadikisha kwa ghaibu ni kuwa atamuona kwa macho." (Al-Ibana Al-Kubra, Ibn Batta (2/7).
Al-Walid bin Muslim alisema: Nilimuuliza Al-Awzai, Malik bin Anas, Sufian Thawri, na Al-Laith bin Saad kuhusu hadithi hizi ambazo zinazungumza kuwa waumini watamuona Mwenyezi Mungu, wakasema: "Ziamini hivyo bila kutaka kujua ni vipi hilo." (Asswifaat, cha Darqutni (uk 75).
Na tunamthibitishia Mwenyezi Mungu uso unaoendana na utukufu wake na ukuu wake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kila kitu kitaangamia isipokuwa Uso wake. Hukumu iko kwake, na kwake mtarejezwa." [Al-Qasas: 88], Na amesema Mtukufu: "Na utabakia uso wa Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu." [Al-Rahman: 27]. Na amesema Mtukufu pia: "Na ambao husubiri kwa kutaka radhi ya Mola wao Mlezi." [Ra'd: 22], Na amesema: "Ila ni kutaka radhi za Mola wake Mlezi aliye juu kabisa." [Layl: 20], Na amesema Mtukufu: "kwa kutaka uso wake." [Al-An 'am: 52]. Na imesimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Kuna mabustani mawili ya fedha, vyombo vyake na vyote vilivyomo ndani yake. Na kuna mabustani mawili ya dhahabu, vyombo vyake na vyote vilivyomo ndani yake. Na hakuna kilicho kati ya watu hao na kumuona Mola wao Mlezi ila pazia la ukubwa kwenye uso wake katika Bustani ya milele." (Imesimuliwa na Bukhari (4878), Muslim (180), Tirmidhi (2528), na Ibn Majah (186).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu na Mtukufu, halali, na wala haimstahikii kulala. Hushusha mizani ya uadilifu na huinyanyua. Yanapandishwa kwake matendo ya usiku kabla ya matendo ya mchana, na matendo ya mchana kabla ya matendo ya usiku. Pazia lake ni nuru, na kama angeliondoa, basi utukufu wa uso wake ungeunguza viumbe vyake mpaka pale ambapo macho yake yanafikia." (Imesimuliwa na Muslim (179), na Ibn Majah (195, 196).
Na amesema Abuu Othman Al-Sabuni, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Na wanasema hivyo hivyo katika sifa zote zilizotajwa katika Qur'ani, na habari sahihi zilizonukuliwa kuhusiana na kusikia, kuona, macho, uso, elimu, nguvu, uwezo, utukufu, ukuu, utashi, mapenzi, kuongea, kuridhia, kukasirika, staha, kuwa macho, kufurahi, kucheka, na sifa zinginezo bila kufananisha chochote miongoni mwa hizo na sifa za viumbe. Bali wao hukomea kwa kile ambacho Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema na Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, bila kuongeza juu yake, wala kuelezea jinsi zilivyo haswa, wala kuzifananisha, wala kuzipotosha, wala kuzibadilisha, wala kuzigeuza, wala kuondoa matamshi yake nje ya kile ambacho Waarabu wanakijua kuhusiana nayo, na kuzifasiri kwa tafsiri isiyo sahihi, na wanaziamini kwa maana yake ya dhahiri, na wanamuachia Mwenyezi Mungu Mtukufu maana yake halisi, na wanakiri kwamba hakuna anayejua tafsiri yake isipokuwa Mwenyezi Mungu, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza hilo kuhusiana na wale waliobobea katika elimu kwamba husema, katika kauli yake Mtukufu: "Na wale wenye msingi madhubuti katika elimu husema: Sisi tumeziamini, zote zimetoka kwa Mola wetu Mlezi. Lakini hawakumbuki hayo isipokuwa wenye akili." [Al-Imran: 7] (Aqiidatus salaf Ahlul Hadithi, cha Abu Othman Al-Sabuni (uk. 16, 17).
Na miongoni mwa sifa Zake Aliyetakasika na kutukuka: Ni sifa ya mkono, na imepokelewa katika Qur'ani na Sunna kwa njia nyingi, wakati mwingine imetajwa kwa namna mbili, na wakati mwingine Mwenyezi Mungu Mtukufu anatuambia kuwa huikunja na kuikunjua, na kwamba Mwenyezi Mungu huishika ardhi kwa mkono Wake, na anazikunja mbingu kwa mkono Wake wa kulia Mtukufu, na wakati mwingine unasifika mkono huo kuwa una vidole, na yote hayo yamethibitika kwamba mkono huo umeelezwa katika Qur'ani na Sunna ni mkono wa kweli unaostahiki utukufu wake, hakuna kujilazimisha kuufasiri au kuufananisha, au kupindisha aya na hadithi zilizolieleza hilo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu akamwambia: Ewe Ibilisi! Kipi kilichokuzuia kusujudu kumtii yule niliyemuumba kwa mikono yangu? Je, umejiona mkubwa, au umekuwa katika wenye kujikweza?" [Swad: 75] Na amesema Allah Mtukufu: "Bila ya shaka wanao fungamana nawe, kwa hakika wanafungamana na Mwenyezi Mungu. Mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao." [Al-Fath: 10], Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na wala hawakumheshimu Mwenyezi Mungu kama anavyo stahiki kuheshimiwa. Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume. Sub-haanahu wa Taa'la, Ametakasika na Ametukuka na hayo wanayo mshirikisha nayo." [Az-zumar: 67]
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa amesema: Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Adam na Musa, amani iwe juu yao, walijenga hoja mbele ya Mola wao Mlezi, Adam akamshinda Musa kwa hoja, Musa akasema: "Wewe ni Adam ambaye Mwenyezi Mungu alimuumba kwa mkono wake na akakupulizia katika roho yake." (Imesimuliwa na Bukhari 6614, Muslim 2652, Abu Daud 4701, Tirmidhi 2134, na Ibn Majah 80). Na katika mapokezi mengine: “Adam na Musa walijibizana kwa hoja, Musa akamwambia: "Ewe Adam, wewe ndiye baba yetu ambaye ulitufanya kuambulia patupu tusiishi ndani ya Pepo. Adam akamwambia: Ewe Musa, Mwenyezi Mungu alikuteua kwa kuzungumza naye, akakuandikia kwa mkono wake." (Imesimuliwa na Bukhari 6614, Muslim 2652, Abu Daud 4701, Tirmidhi 2134, na Ibn Majah 80).
Na katika hadithi sahihi, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika waadilifu mbele ya Mwenyezi Mungu watakuwa katika mimbari za nuru, kuliani mwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na mikono yake yote miwili ni kulia. Wale wanaofanya uadilifu katika hukumu zao na familia zao, na mambo yote wanayoyasimamia." (Imesimuliwa na Muslim (1827), na An-Nasa'i (5379).
Na kutoka kwa Abuu Musa Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, amesema: "Mwenyezi Mungu ananyoosha mkono wake wakati wa usiku ili atubie mkosaji wa mchana, na ananyoosha mkono wake wakati wa mchana ili atubu mkosaji wa usiku, mpaka jua litakapochomoza kutoka magharibi yake." (Imesimuliwa na Muslim (2759).
Na katika vitabu vya hadithi sahihi, imenukuliwa kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, amesema: “Je, mmeona alichotoa Mwenyezi Mungu tangu alipoumba mbingu na ardhi? Hicho chote hakikupunguza kilicho mkononi mwake. Na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji. Na mkononi mwake kuna mizani; anashusha na anainua.” (Imepokelewa na Bukhari (4684), Muslim (993), Al-Tirmidhiy (3045), na Ibn Majah (197).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, amesema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: “Mwenyezi Mungu alipomuumba Adam na kumpulizia roho, akapiga chafya na akasema: "Alhamdulillah (sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu)." Basi akawa amemsifu Mwenyezi Mungu kwa idhini yake...” mpaka aliposema: “Kisha Mwenyezi Mungu akamwambia huku mikono yake imefumbata: Chagua kimoja unachotaka” Akasema: "Nimechagua mkono wa kulia wa Mola wangu Mlezi, na mikono yote miwili ya Mola wangu Mlezi ni yenye baraka." Kisha akaukunjua, na tazama, ndani yake alikuwamo Adam na kizazi chake." (Imepokelewa na Al-Tirmidhiy (3368), Ibn Abi Asim katika Al-Sunnah (596), Al-Bazzar (8194), na Al-Nasa’i katika Al-Kubra (9977).
Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika nyoyo zote za wanadamu ziko baina ya vidole viwili katika vidole vya Mwenyezi Mungu kama moyo wa mtu mmoja, anaufanya atakavyo." (Imepokelewa na Muslim (2654).
Na amesimulia Abdullah bin Imam Ahmad katika kitabu chake “As-Sunna”, kwa msururu wa wasimulizi kutoka kwa Wakii’, alisema: "Tunazikubali hadithi hizi jinsi zilivyokuja, na wala hatusemi: Vipi hivi na hivi? Wala: kwa nini ni hivyo?" Akimaanisa mfano wa hadithi ya bin Masudi, Mwenyezi Mungu amuwie radhi: “Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu amezibeba mbingu kwenye kidole kimoja, na milima kwenye kidole kimoja.” Na katika hadithi isemayo kuwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, amesema: "Hakika nyoyo za wanadamu ziko baina ya vidole viwili vya Mwingi wa rehema." (Imepokelewa na Muslim 2654). Na hadithi zinginezo. (As-Sunnah, cha Abdullah bin Ahmad 1/267).
Na alisema Shariki, Mwenyezi Mungu amrehemu, akiwajibu wale waliomuuliza kuhusu mtu anayekanusha baadhi ya hadithi zinazohusiana na sifa za Mwenyezi Mungu: “Hakika wale waliosimulia Hadithi hizi ni wale wale waliosimulia Qur'ani, na kuwa Swala ni tano, na kuhiji nyumba takatifu, na kufunga Swaumu katika Ramadhani. Nasi hatumjui Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa hadithi hizi." (Sunnah, na Abdullah bin Ahmed 1/273).
Amesema Hafidhi bin Battah, Mwenyezi Mungu amrehemu, - baada ya kutaja hadithi zinazoonyesha sifa ya mkono wa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote: “Hadithi hizi na nyingine zinazofanana nazo, na zilizokuja zikiwa na maana kama hiyo, kuhusu ukamilifu wa dini na utimilifu wa Sunna: Ni lazima kuziamini, kuzikubali, kuzipokea bila ya kuzipinga, na kufuata simulizi za wema waliotangulia katika kuzisimulia bila kuuliza jinsi zilivyo wala kwa nini." (Al-Ibana, cha Ibn Battah (3/313).
Na kama alivyojieleza kwa sifa za ukamilifu, uzuri, utukufu, ukubwa pia alijikanushia sifa za upungufu, na kukanusha sifa hakukuwa ndio msingi katika Qur'ani na Sunna. Kwa sababu kanuni ya msingi ni kuthibitisha sifa, na Qur'ani na Sunna zimejaa suala la kubainisha sifa za Mwenyezi Mungu Mtukufu, kama inavyostahiki utukufu wake, ukuu wake, na ukamilifu wake. Na ikiwa Mola wetu Mlezi Mtukufu, atakanusha sifa juu ya nafsi yake, basi anaikanusha ili kubainisha ukamilifu wa kinyume chake; au kwa sababu wanadamu walimnasibishia upungufu Mwenye utukufu na ukamilifu, kwa hivyo Mola Mlezi anaukanusha upungufu huo unaonasibishwa kwake.
Na miongoni mwa mambo ambayo Mola Mlezi amejikanushia ni kusinzia, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu - hapana mungu ila Yeye Aliye hai, Msimamizi wa mambo yote milele. Hashikwi na usingizi wala kulala." [Al-Baqarah: 255] Na alikanusha kusahau, akasema Mola wa Haki: "Na Mola wako Mlezi si mwenye kusahau." [Maryam: 64], naye wa Mola wa Haki, Aliyetakasika na kutukuka alijikanushia kuchoka. Kwa sababu Mayahudi - Mwenyezi Mungu awalaani - walimnasibishia Mwenyezi Mungu uchovu wakati alipoumba viumbe. Lakini Yeye Mtukufu alijikanushia suala la kupumzika baada ya kumalizika uumbaji, akasema: "Na bila ya shaka Sisi tumeziumba mbingu na ardhi na vilio baina yake mnamo siku sita; na wala hayakutugusa machofu." [Qaf: 38].
Na alithibitisha Mola wetu Mlezi kuwa aliumba viumbe kwa hekima kubwa, na hakuviumba viumbe vyake bure, basi Mola wetu Mlezi akajikanushia kufanya upuuzi, akasema: "Je, mlidhani ya kwamba tuliwaumba bure na ya kwamba nyinyi kwetu hamtarudishwa?" [Al-Mu’minun: 115], Na alibainisha Mola wa Haki kuwa hukumu yake ni ya uadilifu na kauli yake ndiyo ya kukata hukumu, na kwamba hamdhulumu yeyote; Kwa sababu ya ukamilifu wa uadilifu wake, amesema Mola wetu Aliyetakasika na kutukuka: "Na watayakuta yote waliyoyatenda yamehudhuria hapo. Na Mola wako Mlezi hamdhulumu yeyote." [Al-Kahf: 49] Na akasema: "Wala Mola wako Mlezi si mwenye kuwadhulumu waja." [Fussilat: 46].
Nao Mayahudi na Wakristo walimnasibisha mwana kwa Mwenyezi Mungu wakijifananisha na wale waliokufuru kabla yao, basi Mwenyezi Mungu akajikanushia kuwa na mwana, akasema Mola Mtukufu: "Mwenyezi Mungu hana mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine." [Muuminuun: 91] Na alibainisha Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka kuwa mwenye mwana ni lazima awe na mke, na Mwenyezi Mungu ametakasika na kuwa na mke na mwana. Akasema Mtukufu: "Yeye ndiye Muumbaji wa mbingu na ardhi Itakuwaje awe na mwana naye hakuwa na mke? Naye ndiye aliye umba kila kitu. Naye ni Mwenye kujua kila kitu." [Al-An'am: 101] Na akasema Mtukufu: "Na kwa hakika utukufu wa Mola wetu Mlezi umetukuka kabisa; hana mke wala mwana." [Al-Jinn: 3].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu ana majina mazuri zaidi, na kwamba majina Yake yamefikia kilele cha uzuri, kwa hivyo hakuna mazuri zaidi yake, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Mwenyezi Mungu! Hapana mungu isipokuwa Yeye. Yeye ana majina mazuri kabisa." [Taha: 8] Na miongoni mwake ni yale yaliyotajwa katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote * Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu * Mwenye kumiliki siku ya malipo." [Al-Fatihah: 2-4] Na katika kauli yake Aliyetakasika na kutukuka: "Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipokuwa Yeye tu. Mwenye kuyajua yaliyo fichikana na yanayo onekana. Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu * Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipokuwa Yeye tu. Mfalme, Mtakatifu, Mwenye salama, Mtoaji wa amani, Mwenye kuyaendesha Mwenyewe mambo yake, Mwenye nguvu, Anaye fanya analolitaka, Mkubwa, Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayo mshirikisha nayo * Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji, Mtia sura, Mwenye majina mazuri kabisa. Kila kilichoko katika mbingu na ardhi kinamtakasa, naye ni Mwenye kushinda, Mwenye hekima." [Al-Hashr: 22-24].
Na majina ya Mwenyezi Mungu yanatolewa ndani yake sifa kutoka kwa kila jina. Kwa hivyo sifa ya rehema imetokana na jina lake Mwingi wa kurehemu. Na sifa ya utukufu imetokana na jina lake Mwenye utukufu. Na sifa ya hekima imetokana na jina lake Mwenye hekima. Na sifa ya uhai imetokana na jina lake Mwenye uhai kamili, na sifa nyinginezo.
Na majina yake hayahesabiki, amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Ninakuomba kwa kila jina ulilojiita kwalo, au uliliteremsha katika kitabu chako, au ulimfundisha yeyote katika viumbe vyako, au ulilificha kwako katika elimu yako ya ghaibu.” (Imepokelewa na Adh-Dhabi katika kitabu chake cha Du’a 6), na Ibn Abi Shaibah katika Al-Musannaf (29930), na katika Al-Musnad (329), na Ahmad (3712), na Al-Harith bin Abi Usama katika Al- Musnad, kama ilivyo katika Bughyat Al-Bahith (1057). Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Hakika Mwenyezi Mungu ana majina tisini na tisa, mia moja kasoro moja, mwenye kuyadhibiti, ataingia Peponi." (Imepokelewa na Bukhari (2736), Muslim (2677), Al-Tirmidhiy (3506), na Ibn Majah (3860).
Na akatutahadharisha Mola wetu Mlezi dhidi ya kuvuka mipaka kuhusiana na majina yake, akasema Aliyetakasika na kutukuka: "Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri kabisa, basi muombeni kwa hayo. Na waacheni wale wanao haribu utakatifu wa majina yake. Hao watakuja lipwa waliyo kuwa wakiyatenda." [Al-A'raf: 180].
Na kupindukia kiwango katika majina ya Mwenyezi Mungu kuna aina nyingi; kama vile kujiita kwa majina yake hairuhusiki kwa yeyote miongoni mwa wanadamu kujiita kwayo kama vile Muumba, Mwingi wa rehema, na mengineyo. Na miongoni mwake ni kuyaita masanamu kwa majina yanayotokana na majina ya Mwenyezi Mungu, kama vile Al-Lat kutoka katika jina 'Allah', na Al-Uzza kutoka katika jina 'Al-Aziz' (Mwenye nguvu). Na miongoni mwake ni kukataa na kukanusha maana zake, au kumvua Mwenyezi Mungu majina yake na sifa zake.
Majina na sifa za Mwenyezi Mungu zilizotajwa katika Qur’ani na Sunna ni nyingi mno kiasi cha kutoweza kudhibitiwa katika kitabu, lakini inatosha kuwa faraja kwetu kuwa tumeashiria baadhi yake ndani ya mlango huu.
Na tunaamini kuwa Muislamu hapaswi kumuelezea Mwenyezi Mungu, wala kumpa jina isipokuwa kwa yale aliyojielezea mwenyewe, au kwa jina alilojiita kwalo mwenyewe au alimuelezea au kumuita kwalo Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, au kukanusha kile alichojikanushia mwenyewe au alikikanusha juu yake Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake na anyamaze juu ya mengineyo yote.
Nasi tunayaamini majina haya na sifa hizi kulingana na alivyotaka Mola wetu Mlezi, na kulingana na alivyotaka Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na tunajua kwamba hakuna mwanadamu anayejua uhakika wake wala hawawezi kuyazunguka kama yalivyo, wala hata ufahamu wao hauwezi kuyafikia, wala hatujisumbui kuyafasiri; Kwa sababu Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake rehema na amani ziwe juu yake, aseme kuwa: "wala mimi si katika wale wenyekujilazimisha kufanya wasiyoyaweza." [Swad: 86] Na kama ambavyo peponi kuna aina mbali mbali za neema zilizotajwa katika Qur'ani na Sunna zenye majina sawa na neema za duniani, isipokuwa kuna tofauti baina yake ambayo hakuna mwanadamu anayeweza kuijua vilivyo uhalisia wake. Basi ikiwa tunaamini neema za Peponi, ilhali hatujawahi kuziona, wala hatujui uhalisia wake na namna zilivyo - basi Mwenyezi Mungu ni mkuu zaidi kuliko hata kufananishwa na wanadamu, kwa sababu tu wanashirikiana naye katika sifa au majina, na hili halipelekei kukataa majina na sifa za Mwenyezi Mungu kwa sababu tu ya kushirikiana huku katika jina.
Na maimamu wa uongofu na elimu wamekuwa wakikiri hilo, amesema bin Abi Zamanin: “Hizi ni sifa za Mola wetu Mlezi ambazo alijisifu nazo ndani ya Kitabu chake, na akamsifu nazo Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na hakuna ndani yake chochote kinachoonyesha kikomo, wala kuzifananisha, wala kusema zilivyo haswa, basi Ametakasika yule ambaye hakuna chochote mfano wake, naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona, macho hayajawahi kumuona na kufahamu jinsi alivyo haswa, lakini mioyo ilimuona katika uhakika wa kumwamini." (Usulus -Sunnah, cha Ibn Abi Zamanain, uk. 74).
Na amesema Abdul Rahman binil-Qassim: “Haifai kwa mtu yeyote kumsifu Mwenyezi Mungu ila kwa yale aliyojisifu kwayo mwenyewe ndani ya Qur’ani, wala asiifananishe mikono yake na kitu chochote, wala uso wake na kitu chochote. Bali aseme: Ana mikono miwili, kama alivyojielezea mwenyewe katika Qur’ani tukufu. Na ana uso kama alivyojisifia mwenyewe, akomee katika yale aliyojisifia kwayo mwenyewe katika Kitabu. Kwani Yeye, mwenye baraka nyingi Mtukufu hana aliye sawa naye wala anayefanana naye. Bali Yeye ni Mwenyezi Mungu, hakuna mungu ila Yeye, kama alivyojisifia mwenyewe, na mikono yake imekunjuka kama alivyoielezea. "Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume." [Az-Zumar: 67] Kama alivyojisifia mwenyewe. (Usul al-Sunnah, cha Ibn Abi Zamanain uk. 75).
Na amesema Imam Al-Humaidi, Mwenyezi Mungu amrehemu: “Na yale yaliyosemwa na Qur’ani na hadithi, kama vile: "Na Mayahudi walisema: Mkono wa Mwenyezi Mungu umefumba. Mikono yao ndiyo iliyofumba." [Al-Ma’idah: 64] Na kama vile: "Na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume." [Az-Zumar: 67] Na ushahidi ulio sawa na huu kutoka katika Qur’ani na Hadithi, hatuongezi ndani yake wala hatuzifasiri, tunasimamia pale ambapo Qur'ani na Sunna zimesimamia." (Al-Uluu Lil-Alii Al-adhim, cha Dhahabi uk. 168).
Na amesema Imam Ahmad: “Tunamuabudu Mwenyezi Mungu kwa sifa zake kama alivyojielezea mwenyewe, na alijielezea vizuri zaidi, wala hatuvuki Qur'ani na Hadithi. Tunasema alivyosema na kumuelezea jinsi alivyojielezea mwenyewe, wala hatuvuki hilo. Tunaiamini Qur'ani yote; yaliyo wazi ndani yake na yenye kutatiza, na wala hatumuondolei Mwenyezi Mungu sifa aliyojisifu kwayo kwa kuona kuwa ni mbaya, wala hatumuondolei kuzungumza alikojisifu mwenyewe, wala kushuka kwake, nakuwa kwake faraghani na mja wake siku ya Kiyama, na kumuekea pazia lake. Haya yote yanaonyesha kwamba Mwenye Mungu ataonekana Akhera. Na kusema namna jinsi hayo yalivyo uhalisia wake ni uzushi, na inampasa mtu kujisalimisha kwa Mwenyezi Mungu kwa amri yake, na Mwenyezi Mungu hajaacha kuendelea kuzungumza, mwenye kujua, mwenye kusamehe sana, ajuaye mambo ya ghaibu na yanayoonekana, Mjuzi zaidi wa ghaibu. Basi hizi ni sifa za Mwenyezi Mungu alizojielezea kwazo mwenyewe, na haifai kuzikataa wala kuzipinga. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu, hakuna mungu ila Yeye Aliye Hai, Msimamizi wa yote milele." [Al-Baqarah: 255] "Hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Mfalme, Mtakatifu, Mwenye salama, Mtoaji wa amani, Mwenye kuyaendesha Mwenyewe mambo yake, Mwenye nguvu, Anaye fanya analolitaka, Mkubwa." [Al-Hashr: 23] Hizi ndizo sifa za Mwenyezi Mungu na majina yake." (Al-Ibanah Al-Kubra, cha Ibn Battah (7/326).
Alisema Imamu (nguzo ya Sunna) Abul-Qaasim - alipoulizwa kuhusu sifa za Mwenyezi Mungu - akasema: “Mafundisho ya Malik, Thawri, Al-Awza’i, Al-Shafi’i, Hammad bin Salama, Hammad bin Zaid, Ahmad bin Hanbal, Yahya bin Said, Abdul-Rahman bin Mahdi, na Is-haq bin Rahawaihi ni kwamba sifa za Mwenyezi Mungu alizojielezea nazo, au ambazo Mtume wake alimuelezea nazo, kama vile kusikia, kuona, uso, mikono, na maelezo yake yote ni kama yanavyoonekana, yanajulikana kwa maana ya dhahiri mashuhuri, bila kufafanua jinsi zilivyo hasa namna anavyofikiri mwenye tafsiri potofu, wala kufananisha wala kuzitafsiri kwa maana zisizo zake." (Al-Ulu Lil'ali al-adhim, cha Dhahabi (2/459).
Pia alisema: “Na ninataja – kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu – kundi la maimamu wetu miongoni mwa wema waliotutangulia walioamini maana hizi, akiwemo: Abuu Abdullah Sufian bin Said bin Masruq Al-Thawri. Yeye alidhihirisha itikadi yake na dhehebu lake katika Sunna katika sehemu zaidi ya moja, na akamsomea Shuaib bin Harb akaandika. Na miongoni mwao ni Abuu Muhammad Sufian bin Uyaina Al-Hilali. Yeye alijibu katika itikadi yake alipoulizwa kuhusu hilo, kama ilivyosimuliwa na Muhammad bin Is-haq Al-Thaqafi. Na miongoni mwao ni Abuu Amri Abdur-Rahman bin Amri Al-Awza’i, imamu wa watu wa Sham. Yeye alidhihirisha itikadi yake katika zama zake, na ikasimuliwa na Ibn Is-haq Al-Fazari. Na miongoni mwao ni Abuu Abdur-Rahman bin Abdullah binil-Mubarak, Imamu wa Khurasan, na Al-Fudhail bin Iyad, na Waki' bin Al-Jarrah, na Yusuf bin Asbaat. Wote walidhihirisha itikadi yao na dhehebu lao katika vitabu vya sunna. Na miongoni mwao ni Sharik bin Abdullah An-Nakha’i, na Yahya bin Saidi Al-Qattan, na Abu Is-haq Al-Fazari. Na miongoni mwao ni Abuu Abdullah Malik bin Anas Al-Asbahi Al-Madani, Imamu wa Dar Al-Hijrah na Faqihi wa Misikiti Miwili Mitukufu. Yeye alidhihirisha itikadi yake katika suala la imani na Qur'ani. Na miongoni mwao ni Abuu Abdullah Muhammad bin Idris Ash-Shafi’i Al-Muttwalibi, bwana wa mafaqihi katika zama zake. Na miongoni mwao ni Abuu Ubaid Al-Qasim bin Sallam, An-Nadhr bin Shumail, na Abuu Yaqub Yusuf bin Yahya Al-Buwaiti, mmoja wa wanafunzi wa Ash-Shafi’i, alionyesha itikadi yake wakati wa mitihani ilipotokea kuhusiana na Qur’ani. Na miongoni mwao ni Abuu Abdullah Ahmad bin Hanbal, bwana wa wanazuoni wa hadithi katika zama zake. Na Abuu Ahmad bin Abi Usama Al-Qurashi al-Harawi alikuwa mmoja wa wanazuoni na mafaqihi bora zaidi huko Khurasan, alimsomea itikadi yake akaiandika. Akasema: Inampasa yule aliyeneemeshwa na Mwenyezi Mungu kwa elimu ya uongofu na heshima ya Sunna, katika watu wema waliobakia kwamba wafuate mfano wa wale waliopita miongoni mwa watu wema waliotangulia, na kwamba dhehebu letu na dhehebu la maimamu wetu miongoni mwa watu wa Hadithi, ni kusema kuwa: Mwenyezi Mungu Mtukufu ni mmoja, hana mshirika yeyote, wala hana mpinzani, wala hana mwenza, wala hana anayefanana naye, Yeye ni Mungu mmoja Mkusudiwa, hana mke wala mwana, wala hakumshirikisha yeyote katika hukumu yake.” (Al-Hujja fi Bayan Al-Muhajjah 2/508).
Pia alisema Mwenyezi Mungu amrehemu: "Njia ya habari zilizokuja kuhusiana na sifa: Ni kuwa tuziamini, wala tusizipinge, na tuzipitishe kama walivyozipitisha wale wema waliotutangulia bila kufananisha wala kuzitafsiri kwa maana ambazo si sahihi." (Attarghiib wattarhiib, cha Qiwama As-Sunnah 1/253).
Na alisema bin Kutaiba, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Na kauli ya uadilifu kuhusu habari hizi - yaani habari za sifa za Mwenyezi Mungu - ni kwamba tuamini yale yaliyo sahihi miongoni mwake yaliyosimuliwa kwa kupitia simulizi za watu waaminifu. Kwa hivyo tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ataonekana na atawadhihirikia watu, na kuwa Yeye anastaajabu, na kwamba anateremka hadi mbingu ya chini, na kwamba yuko juu ya Arshi, na kuwa ana nafsi, na ana mikono, bila ya kusema namna ya hayo yanakoje haswa, au hata kulinganisha ambayo hayakuja kwa kutumia yale yaliyokuja, na tunatumai kwamba kwa kusema hivyo na kuitakidi hivyo tutapata kufaulu kesho, Mwenyezi Mungu Mtukufu akipenda.” (Al-Ikhtilaafu fillafdh warraddu Alal-Jahmiyya, cha bin Qutaibah uk. 53).
Na alisema Az-Zuhri: "Ni juu ya Mwenyezi Mungu kubainisha, na ni juu ya Mtume kufikisha, na ni juu yetu kujisalimisha." (Al-Hujja fi Bayan Al-Muhajjah 2/512, na Sharh As-Sunnah cha Al-Baghawi 1/171).
Kitabu cha kuamini Malaika
Muhtasari wa Kitabu
Na tunaamini Malaika, na tunajua kwa yakini kuwa kuamini Malaika ndiyo nguzo ya pili katika nguzo za Imani.
Na kuamini Malaika kuna maana zifuatazo:
Ya kwanza: Kusadikisha uwepo wao.
Ya pili: Kuwaweka katika vyeo vyao, na kuthibitisha kuwa wao ni waja wa Mwenyezi Mungu na viumbe vyake, kama vile wanadamu na majini, na kwamba wanaamrishwa, wanajukumishwa, hawawezi chochote isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu Mtukufu anawapa uwezo juu yake, na kwamba wao pia wanaweza kufa, lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu amewafanyia muda mrefu wa maisha, kwa hivyo hawafi mpaka waufikie, na wala hawasifiwi kwa chochote ambacho wakisifiwa kwacho kitasababisha kushirikishwa wao na Mwenyezi Mungu - Mwenye utukufu na ukubwa - na wala hawaitwi miungu, kama walivyodai washirikina.
Ya tatu: Kutambua kuwa miongoni mwao wapo Mitume wa Mwenyezi Mungu anaowatuma kwa amtakaye katika watu, na huenda akawatuma baadhi yao kwa wengine, na hii inafuatiwa na kutambua kuwa miongoni mwao wamo wabebaji wa Kiti cha Enzi, na miongoni mwao wamo walio panga safu, na miongoni mwao wapo walinzi wa Pepo, na miongoni mwao wapo walinzi wa Jahannam, na miongoni mwao wapo waandishi wa matendo, na miongoni mwao wapo wanao tembeza mawingu, Qur'ani Tukufu ilieleza hayo yote na zaidi ya hayo. (Shu'ab Al-Iman 1/296).
Ya nne: Kuamini Malaika kwa ujumla na kwa kina tunaamini kuwepo kwa Malaika kwa imani ya jumla, na tunawaamini wale tunaowajua majina yao, sifa zao, na matendo yao kama ilivyoelezwa katika Qur’ani na Sunna kwa imani ya kina.
Na tunaamini wale tunaowajua na tusiowajua, na tunaamini vitendo vyao na sifa zao, na tunajua kwamba yaliyofichika kwetu kuhusu idadi, vitendo na sifa zao ni zaidi ya tunayoyajua, lakini tunayaamini hayo yote, kama tulivyoambiwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na hatutaki kujua namna walivyo, wala tusiwakanushe kwa akili zetu, wala tusiwafikirie kwa maoni yetu, wala tusiwafasiri kwa akili zetu, bali tuseme: Tumeamini, na tumesadikisha na tumekubali.
Na tunaamini ya kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba Malaika kutokana na nuru, hivyo ni katika viumbe wa Mwenyezi Mungu, amewaumba katika umbo maalum, ukweli ambao Mwenyezi Mungu pekee ndiye anajua, ni waja waliobarikiwa, aliwaumba wamwabudu na kutekeleza amri zake, wanamuabudu na wala hawajitengi katika kumuabudu.
Na miongoni mwa ibada zao: Ni kumtakasa, kusujudu, kuhofu, na wasiwasi mkubwa, nao - pamoja na ibada zao nyingi - wanamcha Mola wao kwa hofu kubwa mno. Na miongoni mwa ibada zao ni kuwa wanafanya urafiki na mtu kwa sababu ya Mwenyezi Mungu na wanampenda kwa sababu ya Mwenyezi Mungu.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba katika umbo ambalo hakuna anayeweza kulifahamu isipokuwa yule aliyewaumba hivyo.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwapa mbawa, na aliwapa idhini ya kuja kwa Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, katika umbile la kibinadamu. Na mwenye kudai miongoni mwa washirikina kwamba Malaika ni mabinti wa Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu alikwishamkadhibisha katika hilo.
Na tunaamini kwamba Malaika hawali wala hawanywi; Kwa sababu wao hawana matamanio, na kuwa katika tabia zao ni staha, na wanakereka kwa yale wanayokereka kwayo binadamu.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu ameweka ndani yao nguvu na uwezo usio na kipimo. Na Malaika ni viumbe wengi ambao idadi yao haiwezi kudhibitiwa isipokuwa na yule aliyewaumba.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amewatukuza na amewakabidhi matendo makubwa, mengi na ya aina mbalimbali, na lililo tukufu zaidi ni kuwa wao ni wajumbe baina ya Mwenyezi Mungu na waja wake, wenye kuwaletea Ufunuo. Na Malaika aliyekabidhiwa jukumu la kuwateremshia Ufunuo Manabii na Mitume wa Mwenyezi Mungu, amani iwe juu yao, ni Jibril, amani iwe juu yake. Mwenyezi Mungu anaweza kuwatuma kwa wengine wasiokuwa Manabii iwe ni majaribu na mtihani.
Na miongoni mwa kazi zao: Ni kubeba 'Arshi, kuandika kadari, kusimamia maswala ya tumbo la uzazi na kiumbe kilicho ndani yake - katika masuala ya kukiumba, kukiunda, na kukipulizia roho - na kuwafisha waja, na kuzipuliza roho katika miili katika dunia hii na katika akhera, kushiriki katika Jihadi pamoja na Waumini, kuwaombea Waumini na kuwatakia msamaha, na kuhudhuria katika ibada za Waumini, kunyanyua maneno yao mazuri, na kumjuza Mola Mlezi habari za matendo yao - na Yeye ndiye mwenye habari zaidi, ajuaye mno, ambaye hahitajii yeyote wa kumjuza.
Na miongoni mwa kazi zao: Ni kushuka duniani katika misimu ya imani, kama vile katika siku ya Ijumaa, Siku ya 'Arafa na usiku wa Laitul-Qadri.
Na miongoni mwa kazi zao: Ni kumjulisha Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuhusu namna Umma wake wanavyomswalia.
Na miongoni mwa kazi zao: Ni kuwahifadhi binadamu, kuandika matendo mema na matendo mabaya, kuulinda mji mtukufu wa Madina kutokana na Dajali, kumhoji maiti katika kaburi lake, kuwapa bishara njema ya ushindi mkubwa waumini wakati wa kifo, kuwapokea katika nyumba ya Akhera, na kuwaingiza katika milango ya Pepo, na kuwa watashuka pamoja na Mwenyezi Mungu safu kwa safu Siku ya Kiyama.
Na katika kazi zao: Ni kuwa miongoni mwao yupo mlinzi wa Pepo, na mlinzi wa Moto.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amewapa Malaika vyeo na daraja. Na Malaika wakubwa zaidi katika daraja ni Jibril, Mikaili na Israfil. Na miongoni mwa watukufu wao zaidi ni wale wanaobeba 'Arshi, na vile vile wale waliohudhuria vita vya Badri miongoni mwa Malaika. Na katika kila mbingu kuna Malaika ambao hakuna anayeweza kuihesabu idadi yao isipokuwa Mwenyezi Mungu. Na Malaika hawa kila mmoja wao ana nafasi yake maalumu, na miongoni mwao wapo walio karibu mno na Mwenyezi Mungu.
Mlango wa ulazima wa kuamini Malaika
Na tunaamini Malaika, na tunajua kwa elimu ya yakini kwamba kuamini Malaika ndiyo nguzo ya pili ya katika nguzo za Imani. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola Mlezi wake, na Waumini vile vile. Wote wamemuamini Mwenyezi Mungu na Malaika wake, na Vitabu vyake na Mitume wake." [Al-Baqarah: 285] Na amesema Mola wa Haki, Aliyetakasika na kutukuka: "Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi. Bali wema ni wa yule anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii." [Al-Baqarah: 177] Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa amekaa nje kwa ajili ya watu, kisha mwanaume mmoja akamjia, na akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nini Imani?" Akasema: “Ni kuwa umwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Kitabu chake, na kukutana naye, na Mitume wake, na kuamini ufufuo wa mwisho.” (Imepokelewa na Bukhari 4777, Muslim 9, na Ibn Majah 64).
Al-Baihaqi, Mwenyezi Mungu amrehemu, alisema: “Na kuamini Malaika kuna maana nyingi: mojawapo ni kusadikisha kuwepo kwao. Na nyingine ni kuwaweka katika vyeo vyao, na kuthibitisha kwamba wao ni waja wa Mwenyezi Mungu na viumbe vyake, kama vile wanadamu na majini, na kwamba wanaamrishwa, hupewa majukumu, hawawezi chochote isipokuwa kile ambacho Mwenyezi Mungu Mtukufu anawapa uwezo juu yake, na kwamba wao pia wanaweza kufa, lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu amewapa muda mrefu wa maisha, kwa hivyo hawafi mpaka waufikie, na wala hawasifiwi kwa chochote ambacho wakisifiwa kwacho kitasababisha kuwashirikisha wao na Mwenyezi Mungu - Mwenye utukufu mkubwa - na wala hawaitwi miungu, kama walivyowaita watu wa kale. (Huitwa watu wa kale wakimaanisha wanafalsafa potofu.) Ya tatu: Ni kukiri kwamba miongoni mwao wapo wajumbe wa Mwenyezi Mungu anaowatuma kwa amtakaye miongoni mwa watu, na huenda akawatuma baadhi yao kwa wengine, na hili linafuatiwa na kukiri kwamba miongoni mwao wamo wabebaji wa Kiti cha enzi, na miongoni mwao wapo wajipangao safu, na miongoni mwao wapo walinzi wa Pepo, na miongoni mwao wapo walinzi wa Jahannam, na miongoni mwao wapo waandishi wa matendo, na miongoni mwao wapo wanaotembeza mawingu. Na Qur'ani Tukufu ilieleza hayo yote na mengi katika hayo. (Shu'ab Al-Iman 1/296).
Al-Baihaqi alitaja maana tatu miongoni mwa maana za kuamini Malaika.
Na ya nne: Ni kuamini Malaika kwa ujumla na kwa kina. Kwa hivyo, tunaamini kuwepo kwa Malaika kwa imani ya jumla, na tunawaamini wale tunaowajuwa majina yao, sifa zao, na matendo yao kama ilivyoelezwa katika Qur’ani na Sunna kwa imani ya kina.
Na tunajua kwamba yaliyofichikana kwetu kuhusu idadi yao, vitendo vyao, na sifa zao ni zaidi ya tunayoyajua, lakini tunayaamini hayo yote, kama tulivyoambiwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, bila ya kutafuta kujua jinsi walivyo haswa, wala hatuyakatai kwa akili zetu tu, wala hatuyadhanii kwa maoni yetu tu, wala hatuyafasiri kwa akili zetu tu. Bali tunasema: Tumeamini, na tumesadikisha na tumejisalimisha.
Mlango wa kuumbwa Malaika na wingi wa idadi yao na sifa zao
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaumba Malaika kutokana na nuru. Amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Wameumbwa Malaika kutokana na nuru." (Imepokelewa na Muslim 2996). Nao ni viumbe miongoni mwa viumbe wa Mwenyezi Mungu aliwaumba kwa umbile maalumu, lakini si wenye roho tu, wala nguvu tu. Bali wao ni ulimwengu usioonekana, na waja wanaolelewa. Aliwaumba ili wamuabudu, na watekeleze amri zake. Kwa hivyo, wanamuabudu wala hawajivuni wakaacha kumuabudu.
Na miongoni mwa ibada zao ni kumtakasa Mwenyezi Mungu, kumsujudia, kumhofu, na ibada nyinginezo. Amesema Mola Mtukufu: "Hawamuasi Mwenyezi Mungu kwa anayowaamrisha, na wanatenda wanayoamrishwa." [At-Tahrim: 6] Pia alisema: "Na vyote vilivyo katika mbingu na katika ardhi, tangu wanyama mpaka Malaika, vinamsujudia Mwenyezi Mungu, na wala havitakabari" [An-Nahl: 49] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na utawaona Malaika wakizunguka pembeni mwa Kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu, wakimtakasa na kumsifu Mola wao Mlezi." [Az-Zumar: 75]. Na wao - pamoja na wingi wa ibada yao - wanamhofu Mola wao Mlezi kwa hofu kubwa zaidi. Amesema Mola Mtukufu: "Wanamhofu Mola wao Mlezi aliye juu yao, na wanafanya wanayoamrishwa" [An-Nahl: 50].
Na miongoni mwa ibada zao ni kwamba wao wanafanya urafiki na watu kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na wanapenda kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Amesema Mtume Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu anapompenda mja, humuita Jibril: Hakika Mwenyezi Mungu anampenda fulani, basi mpende, kwa hivyo Jibril anampenda. Kisha Jibril huwaita Malaika wa mbinguni: Hakika Mwenyezi Mungu anampenda fulani, basi mpendeni, kwa hivyo Malaika wa mbinguni wanampenda. Kisha mtu huyo hujaaliwa kukubalika duniani.” (Imepokelewa na Bukhari 3209, Muslim 2637, na Tirmidhi 3161). Nao hufanya uadui na huchukia kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na wanajiepusha na makatazo ya Mwenyezi Mungu, na wanamlaani yule aliye laaniwa na Mwenyezi Mungu. Amesema Mola Mtukufu: "Hakika wale waliokufuru, na wakafa hali ni makafiri, hao iko juu yao laana ya Mwenyezi Mungu na ya Malaika na ya watu wote." [Al-Baqarah: 161]. Na amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Malaika hawaingii katika nyumba yenye sanamu ndani yake au picha." (Imepokelewa na Muslim 2112).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba katika umbo ambalo hakuna anayeweza kulifahamu vilivyo isipokuwa yule aliyewaumba nalo. Imesimuliwa kutoka kwa Jabiri bin Abdullahi, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Nimeruhusiwa kuzungumza juu ya Malaika miongoni mwa Malaika wa Mwenyezi Mungu miongoni mwa wale wanaobeba kiti cha enzi. Hakika kati ya ndewe ya sikio lake hadi begani kwake ni mwendo wa miaka mia saba." (Imepokelewa na Abu Daud 4727, Ibn Twahman katika Masheikh 21, Twabarani katika Al-Awsat 1709, na Abu Sheikh katika Al-Adhama 313).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba na mbawa, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa, mbili-mbili, na tatu-tatu, na nne-nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo." [Fatir: 1]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Masudi, Mwenyezi Mungu awe radhi naye: "Hakika Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alimuona Jibril akiwa na mbawa mia sita." (Imepokelewa na Bukhari 3232, Muslim 174, na Tirmidhi 3277). Na kwamba wana nyoyo, amesema Mola wa Haki, Mtukufu: "Mpaka inapoondolewa hofu kwenye nyoyo zao, wanasema: Mola wetu Mlezi kasema nini? Watasema: Yaliyo kweli! Na Yeye ndiye Aliye juu, Mkubwa." [Saba': 23].
Mwenyezi Mungu akawaruhusu kuwajia Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, katika sura ya wanadamu. Waliingia kwa Ibrahim na Lut, amani iwe juu yao, katika sura ya wageni ambao hawawajui. Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema akieleza juu ya hilo: "Je, imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanaoheshimiwa? * Walipoingia kwake, wakasema: Salama! Na yeye akasema: Salama! Nyinyi ni watu nisiowajua." [Adh-Dhariyat: 24, 25] Na amesema Mtukufu: "Na wajumbe wetu walipokuja kwa Lut', aliwahuzunukia na akawaonea dhiki. Akasema: Hii leo ni siku ngumu!" [Hud: 77] Jibril, amani iwe juu yake, alikuja kwa Mariam, amani iwe juu yake, kwa njia ambayo hakuitambua mara ya kwanza, kama Mwenyezi Mungu alivyotuambia: "Tukampelekea Roho wetu, akajifananisha kwake sawa na mtu * (Maryamu) akasema: Hakika mimi najikinga kwa Mwingi wa Rehema aniepushe nawe, ukiwa ni mchamungu." [Maryam: 17-19] Na imesimuliwa kutoka kwa bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa alisema: “Jibril, amani iwe juu yake, alikuwa akimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake katika sura ya sauti ya nyuki.” (Imepokelewa na Ahmed 5857, Muhammad bin Nasr Al-Mirwazi katika Taadhim Qadr As-Swalaat 372, na Ibn Battwa katika Al-Al-Ibana 831).
Na tunaamini kwamba Malaika hawali wala hawanywi; Kwa sababu hawana matamanio; Na ndiyo sababu walipoingia katika nyumba ya Ibrahim, amani iwe juu yake, na akawapa chakula, hawakula. Mola wa Haki, aliyetakasika alisema akieleza juu ya hilo: "Akaenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliyenona * "Akawakaribisha, akasema: Mbona hamli?* "Kwa hivyo, akahisi kuwaogopa katika nafsi yake. Wakasema: Usiwe na hofu, nao wakambashiria kupata kijana mwenye elimu." [Ad-Dhariyat: 26-28] Na kwamba kuwa na Haya ni katika tabia yao. Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: “Je, nisimuonee haya mtu ambaye Malaika wanamuonea haya?" (Imepokelewa na Muslim 2401).
Na kuwa wanaudhika kwa yale ambayo wanadamu wanaudhika nayo, amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Mwenye kula katika mboga hii, kitunguu saumu." – na mara nyingine alisema: "Mwenye kula kitunguu maji, na kitunguu saumu – asiukaribie msikiti wetu; Kwani hakika Malaika wanaudhika kwa yale ambayo wanadamu wanaudhika nayo.” (Imepokelewa na Bukhari 854, Muslim 564 na matamshi ya hadithi hii ni yake, na Abu Dawud 3822, Tirmidhi 1806, An-Nasai 707, na Ibn Majah 3365).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amewajaalia ndani yao nguvu na uwezo usioweza kuzungukwa, amesema Mtukufu: "Mwenye nguvu na mwenye cheo kwa huyo Mwenye Kiti cha Enzi." [At-Takwir: 20] Na amesema Mola Mtukufu: "Wanausimamia Malaika wakali, wenye nguvu, hawamuasi Mwenyezi Mungu kwa anayowaamrisha, na wanatenda wanayoamrishwa." [At-Tahrim: 6] Na Mwenyezi Mungu alimtuma Malaika katika vijiji vya watu wa Lut, ambavyo vilikuwa vijiji saba, na akavigeuza juu chini. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema: "Basi ilipofika amri yetu, tuliigeuza nchi juu chini, na tukawateremshia mvua ya changarawe za udongo mgumu uliokamatana wa Motoni." [Hud: 82].
Na tunaamini kuwa Malaika ni viumbe wengi, ambao idadi yao haiwezi kuhesabiwa isipokuwa na yule aliyewaumba. Imesimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani zimshukie, alisema: "Kisha ikanyanyuliwa kwangu Baitul-Ma'muri (nyumba iliyoimarishwa kwa ibada), nikamuuliza Jibril, akasema: Hii ni Baitul-Ma'muri, wanaswali ndani yake kila siku Malaika elfu sabini, ambapo wakishatoka, hawarudi humo tena mpaka wa mwisho wao." (Imepokelewa na Bukhari 3207, Muslim 164, Tirmidhi 3346, na An-Nasai 448).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Dharri, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa amesema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: “Hakika mimi ninaona msiyoyaona, na ninasikia msiyoyasikia. Mbingu ilitoa sauti, na kweli ilikuwa na haki ya kutoa sauti hiyo. Kwani hakuna ndani yake nafasi ya vidole vinne isipokuwa kuna Malaika aliyeliweka paji la uso wake hapo kwa kumsujudia Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Al-Tirmidhi 2312, Ibn Majah 4190, Ibn Abī Shayba 27044, Ahmad 21516, na Al-Bazzār 3924, 3925).
Imesimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Jahannam italetwa siku hiyo hali ya kuwa ina mikanda elfu sabini huku kila mkanda umeshikwa na Malaika elfu sabini wakiiburura." (Imepokelewa na Muslim 2842, na Tirmidhi 2573).
Na washirikina walidai kuwa Malaika ni mabinti wa Mwenyezi Mungu, lakini Mwenyezi Mungu akawakadhibisha kwa kuali yake: "Au tumewaumba Malaika kuwa ni wanawake, na wao wanashuhudia?" [As-Saffat: 150]. Na akawapinga kauli yao hiyo kwa kauli yake Yeye Mtukufu: "Je, Mola wenu Mlezi amewateulia wavulana, na yeye akawafanya Malaika ni banati zake? Kwa hakika nyinyi mnasema usemi mkubwa." [Al-Israa: 40].
Mlango wa kazi za Malaika
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amewatukuza na kuwakabidhi matendo makubwa, mengi na ya aina mbalimbali, na lililo tukufu zaidi ni kuwa ni wajumbe baina ya Mwenyezi Mungu na waja wake ambao wanawaletea Ufunuo (wahyi). Na Malaika aliyekabidhiwa jukumu la kuwateremshia Ufunuo Manabii wa Mwenyezi Mungu na Mitume wake, amani iwe juu yao, ni Jibril, amani iwe juu yake, kama alivyosema Mola Mtukufu: "Sema: Ameiteremsha hii Roho mtakatifu kutoka kwa Mola wako Mlezi kwa haki." [An-Nahl: 102] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na bila shaka hii (Qur'ani) ni Uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote * Ameuteremsha Roho muaminifu * Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji* Kwa Lugha ya Kiarabu ulio wazi." [Ash-Shu'ara: 192-195].
Mwenyezi Mungu anaweza kuwatuma kwa wasiokuwa Mitume ili kuwapa majaribu na mtihani, kama ilivyo katika kisa cha wale watu watatu miongoni mwa wana wa Israeli. Imesimuliwa kutoka kwa Abdur-Rahman bin Abi Amra, kwamba Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi alimwambia kuwa alimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie akisema: "Mwenyezi Mungu aliyetukuka alitaka kuwajaribu watu watatu miongoni wana wa Israeli: Mkoma, na mtu mwenye upara, na kipofu. Basi, akawatumia Malaika, akamjia yule mwenye ukoma, akasema: "Je, ni kitu gani unachopenda zaidi?." Akasema: "Rangi nzuri na ngozi nzuri, kwa kuwa watu bila shaka wamenidharau sana." Akasema: Kwa hivyo, Malaika huyo akamgusa na ugonjwa wake ukapona, na akapewa rangi nzuri na ngozi nzuri. Malaika huyo akamuuliza: "Je, ni mali gani unayopenda zaidi?" Akasema: "Ngamia (au ng'ombe)." (Msimulizi alikuwa na shaka kwa kuwa mmoja kati ya mwenye ukoma au mwenye upara ndiye aliomba apewe ngamia, na mwingine akaomba apewe ng'ombe) Kwa hivyo, (mwenye ukoma) akapewa ngamia wa kike mjamzito, na Malaika akamwambia: "Mwenyezi Mungu akubarikie ndani yake." Kisha Malaika huyo akamwendea yule mwenye upara na akasema: "Ni kitu gani unapenda zaidi?" Akasema: "Ninapenda nywele nzuri, na ninataka kuponywa kutokana na ugonjwa huu, kwa maana watu wamenidharau sana." Akasema: Kwa hivyo, Malaika huyo akamgusa na ugonjwa wake ukapona, na akapewa nywele nzuri. Malaika huyo akamuuliza: "Ni mali gani unayoipenda zaidi?" Akajibu: "Ng'ombe" Malaika huyo akampa ng'ombe wa kike mjamzito na akasema: "Mwenyezi Mungu akubarikie ndani yake." Kisha Malaika huyo akamwendea yule kipofu na akamuuliza: "Ni kitu gani unachopenda zaidi?" Akasema: "(Ninapenda) kwamba Mwenyezi Mungu anirudishie macho yangu ili niweze kuwaona watu." Akasema: Kwa hivyo, Malaika huyo akamgusa macho na Mwenyezi Mungu akamrudisha macho yake. Malaika huyo akamuuliza: "Je, ni mali gani unayopenda zaidi?" Akajibu, "Kondoo." Basi Malaika huyo akampa kondoo wa kike mjamzito. Baadaye, wanyama hao watatu wajawazito walizaa watoto, na kuzaliana sana kiasi kwamba mmoja wa watu hao watatu alikuwa na kundi la ngamia lililojaza bonde, na mwingine alikuwa na ng'ombe waliojaza bonde, na wa tatu pia alikuwa na kondoo waliojaza bonde. Kisha Malaika huyo akamjia yule aliyekuwa na ukoma katika sura yake ya awali na muonekano wake (wa ugonjwa wa ukoma) na akasema: "Mimi ni mtu maskini, nimekatikiwa njia zote wakati wa safari. Kwa hivyo, hakuna yeyote atakayenisaidia ila Mwenyezi Mungu kisha wewe. Ninakuomba kwa Jina la Yule aliyekupa rangi nzuri na ngozi nzuri, na mali nyingi, unipe ngamia ili niweze kufika ninakokwenda." Akamwambia, "Hakika nina majukumu mengi (hivyo siwezi kukupa)." Malaika huyo akasema: "Ni kana kwamba ninakujua. Hivi si ulikuwa mkoma ukidharauliwa na watu (kama mimi?), na ulikuwa masikini, na Mwenyezi Mungu akakupa (mali hii yote)?" Akasema: "(Hayo yote ni uongo mtupu) nimerithi mali hii kutoka kwa baba zangu." Malaika akasema: "Ikiwa unasema uongo, basi Mwenyezi Mungu akufanye kama ulivyokuwa hapo awali." Kisha Malaika akamjia yule wa upara katika sura yake ya hapo awali na muonekano wake na akamwambia sawa na alivyomwambia yule wa kwanza, naye pia akajibu majibu sawa na alivyomjibu yule wa kwanza. Malaika akasema: "Ikiwa unasema uongo, basi Mwenyezi Mungu akufanye kama ulivyokuwa hapo awali." Kisha Malaika huyo alimjia yule kipofu katika sura yake ya hapo awali na muonekano wake na akasema: "Mimi ni mtu masikini na msafiri ambaye amekatikiwa na njia zake safarini. Hapana yeyote atakayenisaidia kufika niendako isipokuwa Mwenyezi Mungu kisha wewe. Ninakuomba kwa Jina la Yule aliyekurejeshea macho yako, unipe kondoo mmoja, ili niweze kumtumia kufika niendako katika safari yangu." Mwanaume huyo akasema: "Kwa hakika, nilikuwa kipofu, na Mwenyezi Mungu akanirejeshea macho yangu, na (nilikuwa) masikini, na Mwenyezi Mungu akanifanya kuwa tajiri, kwa hivyo, chukua chochote unachotaka kutoka katika mali yangu. Wallahi! Sitakuzuia kuchukua chochote (unachohitaji) katika mali yangu ambacho utakichukua kwa ajili ya Mwenyezi Mungu." Basi hapo Malaika akasema: "Kaa na mali yako; kwani nyinyi mmejaribiwa, na Mwenyezi Mungu amekuridhia wewe, na amewakasirikia wale wenzako wawili." Imesimuliwa na Bukhari 3464 na Muslim 2964).
Na miongoni mwao wapo wanaobeba Kiti cha Enzi. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na Malaika watakuwa pembezoni mwa mbingu; na wanane juu ya hawa watakuwa wamebeba Kiti cha Enzi cha Mola wako Mlezi." [Al-Haqqa: 17].
Na katika kazi zao ni kuandika kadari. Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika mmoja wenu linakusanywa umbile lake katika tumbo la mama yake kwa muda wa siku arobaini (hali ya kuwa ni manii), kisha anakuwa tone la damu kwa muda kama huo, kisha anakuwa kipande cha nyama kwa muda kama huo, kisha Mwenyezi Mungu anamtumia Malaika, naye anaamrishwa mambo manne. Anaambiwa: "Andika matendo yake, riziki yake, na ajali yake au ni muovu au mwema." (Imepokelewa na Bukhari 3208, Muslim 2643, Abu Daud 4708, Tirmidhi 2137, na Ibn Majah 76).
Na miongoni mwa matendo yao ni kusimamia mambo ya tumbo la uzazi na kile kilicho ndani yake - kuumbwa kwake, kuundwa kwake, na kupuliziwa roho - Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie amesema: "Tone la manii linapomaliza siku arobaini na mbili (katika tumbo la uzazi), Mwenyezi Mungu analitumia Malaika. Kwa hivyo (Malaika huyo) analiunda, na kuumba kusikia kwake, kuona kwake, ngozi yake, nyama yake, na mifupa yake, kisha anasema: "Ewe Mola Mlezi, je, ni wa kiume au ni wa kike?" Mola wako Mlezi anaamua atakalo, na Malaika huyo analiandika. Kisha anasema: "Ewe Mola Mlezi muda wake ni upi?" Mola wako Mlezi anasema atakalo, na Malaika huyo analiandika." (Imepokelewa na Muslim 2645).
Na imesimuliwa kutoka kwa Anas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kutoka kwa Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: "Mwenyezi Mungu amemkabidhi Malaika fulani usimamizi wa tumbo la uzazi, naye husema: "Ewe Mola Mlezi, ni tone la manii. Ewe Mola Mlezi ni damu iliyoganda. Ewe Mola Mlezi ni pande la nyama." Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu anapopitisha kukiumba, Malaika huyo husema: "Ewe Mola Mlezi, ni wa kiume au wa kike? Ni wa mashakani au ni wa furaha? Na riziki yake ni nini? Na muda wake ni upi?" Basi yanaandikwa hivyo katika tumbo la mama yake." (Imepokelewa na Bukhari 6595, na Muslim 2646).
Na miongoni mwa kazi zao ni kuzichukua roho za waja. Amesema Mola wa Haki, na maneno yake ni ya haki: "Mpaka mmoja wenu yakimjia mauti, wajumbe wetu humfisha, nao hawapuuzi chochote." [Al-An'am: 61] Na Mola Mtukufu amesema: "Basi itakuwaje Malaika watakapowafisha wakawa wanawapiga nyuso zao na migongo yao!" [Muhammad: 27].
Na miongoni mwa kazi zao ni kupuliza roho ndani ya miili katika dunia na Akhera, amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika, mmoja wenu, umbile lake linakusanywa tumboni mwa mama yake kwa siku arobaini, kisha anakuwa damu iliyoganda kwa muda kama huo, kisha anakuwa pande la nyama kwa muda kama huo, kisha Mwenyezi Mungu anamtuma Malaika na anamuamuru maneno manne, na anaambiwa: "Andika matendo yake, riziki yake, muda wa maisha yake, na kwamba ni wa mashakani au ni wa furaha, kisha anapuliziwa roho." (Imepokelewa na Bukhari 3208, Muslim 2643, Abu Daud 4708, Tirmidhi 2137, na Ibn Majah 76). Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kisha litapulizwa mara nyingine. Hapo, watainuka wawe wanangojea." [Az-Zumar: 68].
Na miongoni mwa kazi zao ni kupigana Jihad pamoja na Waumini, na kuwafanya kuwa thabiti katika uwanja wa vita, na katika mapambano ya kimaisha, amesema Mola Mtukufu, Mwenye mamlaka matukufu: "Mola wako Mlezi alipowafunulia Malaika: Hakika Mimi ni pamoja nanyi, basi watieni nguvu wale walioamini. Nitatia woga katika nyoyo za wale waliokufuru. Basi wapigeni juu ya shingo na kateni kila ncha za vidole." [Al-Anfal: 12] Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Hakika Shetani ana athari kwa mwanadamu, kama vile Malaika alivyo na athari kwake. Athari ya shetani ni kwa kumzoesha uovu na kukadhibisha haki. Na athari ya Malaika, ni kumzoesha kufanya heri na kusadikisha haki. Kwa hivyo, mwenye kuhisi hivyo, basi na ajue kwamba hilo limetoka kwa Mwenyezi Mungu, kwa hivyo amsifu Mwenyezi Mungu. Na mwenye kuhisi lile lingine, basi na ajilinde kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shetani aliyelaaniwa." Kisha akasoma: "Shetani anawatia hofu ya ufakiri na anawaamrisha mambo machafu." hadi mwisho wa aya [Al-Baqara: 268] (Imepokelewa na Tirmidhi 2988, Ibn Al-Mubarak katika Az-Zuhd 1435, na Ahmad katika Az-Zuhd 854, na Abu Daud katika Az-Zuhd 164).
Na miongoni mwa kazi zao ni kuwaombea waumini na kuwatakia msamaha, amesema Mola Mhimidiwa: "Wale wanaoibeba 'Arshi, na wale wanaoizunguka, wanamtakasa na kumhimidi Mola wao Mlezi, na wanamuamini, na wanawaombea msamaha wale walioamini kwa kusema: Mola wetu Mlezi! Umekienea kila kitu kwa rehema na elimu. Basi wasamehe wale waliotubu na wakaifuata njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu." [Ghafir: 7]
Na miongoni mwa kazi zao ni kuhudhuria katika ibada za Waumini katika misimu ya Imani na heri na nyakati zenye fadhila, kama vile siku ya Ijumaa, Siku ya Arafa, Usiku wa Cheo, na swala ya Alfajiri na Alasiri, na kupandisha maneno yao mazuri, na kumpa habari Mola Mlezi juu ya matendo yao - naye ndiye mwenye habari zote, ajuaye zaidi ambaye hahitaji wa kumjulisha kitu - Mwenyezi Mungu Mwenye utajo mtukufu anasema: "Na Qur'ani ya Al-fajiri. Hakika Qur'ani ya Alfajiri inashuhudiwa daima." [Al-Israa: 78] Na amesema Mola wa Haki, aliyekatasika: "Huteremka Malaika na Roho katika usiku huo kwa idhini ya Mola wao Mlezi kwa kila jambo." [Al-Qadr: 4]
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: “Wanabadilishana kwenu Malaika wakati wa usiku na wakati wa mchana, na wanakusanyika wakati wa swala ya Alfajiri na swala ya Lasiri, kisha wanapanda juu wale waliokuwa nanyi wakati wa usiku, na anawauliza - ilhali Yeye ndiye ajuaye zaidi kuhusu waja wake - "Mmewaachaje waja wangu?" Nao husema: "Tumewaacha ilhali wanaswali na tuliwajia wakiwa wanaswali." (Imepokelewa na Bukhari 555, Muslim 632, na Nasai 485).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika Mwenyezi Mungu anao Malaika wanaozunguka njiani wakitafuta watu wanaomtaja, na wanapowakuta watu wanaomtaja Mwenyezi Mungu, wanaambiana, "Njooni kwa kile mnachohitaji." Akasema: "Kisha wanawafunika kwa mbawa zao hadi mbingu ya Dunia." (Imepokelewa na Bukhari 6408, na Muslim 2689).
Malaika huhudhuria katika misimu ya imani, kama vile siku ya Ijumaa, Siku ya Arafa na Lailatul-Qadiri. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: "Imamu anapotoka, Malaika wanahudhuria ili wasikilize utajo wa Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari 881, Muslim 850, Abu Dawud 351, Tirmidhi 499, na Nasai 1388).
Na katika kazi zao ni kumfikishia Mtume rehema na amani zimshukie dua za rehema kutoka kwa umma wake, amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Na niswalieni, kwani hakika swala zenu hunifikia popote mlipo." (Imepokelewa na Abuu Daud 204, Ahmad 8804, Twabarani katika Al-Awsat 8030, na Al-Baihaqi katika Al-Shu'ab 3865).
Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Hakika Mwenyezi Mungu ana Malaika wanaotalii katika ardhi wanaonifikishia salamu kutoka kwa umma wangu." (Imepokelewa na Nasai 1282, Abdur-Razzaq 3116, na Ibn Abi Shaiba katika Al-Muswannaf 8797, na katika Al-Musnad 269, na Ahmad 3666).
Na miongoni mwa kazi zao ni kuwalinda wanadamu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kila mtu analo kundi la Malaika mbele yake na nyuma yake, linamlinda kwa amri ya Mwenyezi Mungu." [Ar-Ra'd: 11] Na amesema Ally bin Abi Twalha, kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili kwamba neno: "Al-Muaqqibat" katika aya hii: linamaanisha: "Malaika." (Imepokelewa na At-Twabari katika Tafsir 13/463, na Ibn Abi Hatim katika Tafsir 12198).
Na miongoni mwa kazi zao ni kuandika mema na mabaya, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Waandishi wenye heshima." [Al-Infitar: 11] Na amesema Mtukufu: "Wanapopokea wapokeaji wawili, wanaokaa kuliani na kushotoni * Hatamki neno isipokuwa karibu yake yupo mngojeaji tayari kuandika" [Qaf: 17,18] Na amesema: "Na hukutumieni waangalizi." [Al-An'am: 61] Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema juu yao: "Au wanadhani kwamba hatusikii siri zao na minong'ono yao? Wapi! Na wajumbe wetu wapo karibu nao, wanayaandika." [Az-Zukhruf: 80] Na amesema rehema na amani zimshukie: “Mwenyezi Mungu husema: Msimwandikie mpaka alifanye. Akilifanya, basi liandikeni kama lilivyo. Lakini akiliacha kwa ajili yangu, basi liandikeni kuwa ni jema. Na akitaka kufanya jambo jema na hakulitenda, basi liandikeni kuwa ni tendo jema kwake. Na kama atalitenda, basi mwandikieni mara kumi mfano wake, mpaka mizidisho mara mia saba." (Imepokelewa na Bukhari 7501, Muslim 128, na Tirmidhi 3073). Na amesema rehema na amani zimshukie: "Malaika husema: "Ewe Mola Mlezi, mja wako huyo anataka kufanya uovu' - ilhali Yeye ndiye anayemuona zaidi -, naye husema: "Mwangalieni. Akiutenda, mwandikieni kama ulivyo. Lakini akiuacha, mwandikieni kama tendo jema. Kwani hakika ameuacha kwa ajili yangu." (Imepokelewa na Muslim 129)
Na miongoni mwa kazi zao ni kuulinda mji wa Madina dhidi ya Dajali. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: "Kuna Malaika pembezoni mwa Madina, na haitaingia humo tauni (Ugonjwa wa mlipuko) wala Dajali." (Imepokelewa na Bukhari 1880 na Muslim 1379).
Na miongoni mwa kazi zao ni kumhoji maiti kwenye kaburi lake. Imesimuliwa kutoka kwa Al-Baraa bin Azib, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie, alisema kuhusu hali ya mwanadamu anapowekwa kaburini mwake: “Kisha Malaika wawili wanamjia na kumkalisha, kisha wanamwambia: "Ni nani Mola wako Mlezi?" Anasema: "Mwenyezi Mungu ndiye Mola wangu Mlezi." Kisha wanamwambia: "Ni ipi dini yako?" Anasema: "Dini yangu ni Uislamu." Kisha wanamwambia: "Ni mtu gani huyu aliyetumwa miongoni mwenu?" Anasema: "Huyo ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake." (Imepokelewa na Abu Daud 4753, Nasai 2001, Ibn Majah 1548, At-Twayalisi 789, Abdur-Razzaq 6737, na Ibn Abi Shaibah 12185).
Na miongoni mwa matendo yao ni kwamba kuna wale wanaoilinda Pepo. Imesimuliwa kutoka kwa Anas bin Malik, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Nitaujia mlango wa Bustani ya mbinguni Siku ya Kiyama, na kuomba nifunguliwe. Mlinzi wake atasema: "Wewe ni nani?" Nitasema: "Muhammad." Atasema: "Niliamrishwa kuwa nisimfungulie mtu yeyote kabla yako." (Imepokelewa na Muslim 197). Na mlinzi wa Moto, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Nao watapiga kelele waseme: 'Ewe Malik! Na atufishe Mola wako Mlezi!' Naye aseme: Hakika nyinyi mtakaa humo humo!" [Az-Zukhruf: 77]. Na amesema Mola wa Haki, aliyetakasika, na kutukuka: "Juu yake wapo kumi na tisa* Na hatukuwafanya walinzi wa Motoni isipokuwa ni Malaika." [Al-Muddathir: 30, 31] Imethibiti katika vitabu vya hadithi sahihi kutoka kwa Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema kuwa: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: "Jahannam italetwa siku hiyo hali ya kuwa ina minyororo elfu sabini, na kila mnyororo utakuwa na Malaika elfu sabini wakiuburura." (Imepokelewa na Muslim 2842, na Tirmidhi 2573). (Tafsir Al-Qurtubi 19/80).
Mlango wa daraja za Malaika
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu amewaweka Malaika katika nafasi na daraja mbalimbali. Mola wa Haki aliyetukuka alisema akieleza juu yao: "Na hapana katika sisi isipokuwa anapo mahali pake maalumu* Na hakika bila ya shaka sisi ndio wajipangao safu." [As-Saffat: 164-166].
Na Malaika mwenye cheo kikubwa zaidi ni Jibril, Mikaili na Israfil. Ndiyo maaana, Nabii, rehema na amani zimshukie, alikuwa akitafuta njia ya kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia umola wa Mwenyezi Mungu juu ya watatu hawa. Imesimuliwa kutoka kwa Abu Salama bin Abdur-Rahman bin 'Aufu, kuwa alisema: Nilimuuliza 'Aisha, mama wa Waumini, Mwenyezi Mungu amuwie radhi: 'Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akifungua swala yake kwa kitu gani anapoamka usiku?' Akasema: "Alikuwa anapoamka usiku, anaifungua Swala yake kwa kusema: “Ewe Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa Jibril, Mikaili na Israfil, Muumba wa mbingu na ardhi, Mjuzi wa siri na dhahiri, Wewe utahukumu baina ya waja wako katika yale waliyokuwa wakihitilafiana ndani yake. Niongoe kwenye haki katika yale waliyohitalafiana ndani yake kwa idhini yako. Hakika wewe unamuongoa umtakaye kwenye njia iliyonyooka.” (Imepokelewa na Muslim 770, Abuu Daud 767, Nasai 1625, na Ibn Majah 1357).
Na katika watukufu wao zaidi ni wale wanaobeba Kiti cha enzi, na vile vile wale waliohudhuria katika Vita vya Badri miongoni mwa Malaika. Imesimuliwa kutoka kwa Muadhi bin Rifa’a bin Rafi’ Az-Zuraqi, kutoka kwa baba yake, Mwenyezi Mungu amuwie radhi – na baba yake alikuwa miongoni mwa watu wa Badiri – kuwa alisema: Jibril alimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: “Mnawahesabu vipi watu wa Badiri kwenu nyinyi?” Akasema: “Ni katika Waisilamu bora zaidi.” au neno mfano wa hilo - Akasema: "Na vile vile wale waliohudhuria katika vita vya Badiri miongoni mwa Malaika." (Imepokelewa na Bukhari 3992).
Na katika kila mbingu kuna Malaika ambao idadi yao hakuna anayeweza kuidhibiti isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kila mmoja wao ana mahali pake maalumu, na miongoni mwao wapo walio karibu mno na Mwenyezi Mungu. Ndiyo maana Mtume, rehema na amani zimshukie, alisema kuhusu kupanda juu kwa roho ya Muumini baada ya kifo chake: "Kisha wanapanda nayo juu, na hawapiti karibu na kundi lolote la Malaika, isipokuwa wanasema: "Ni Roho gani nzuri kiasi hiki?" Wanasema: "Ni ya fulani mwana wa fulani" wakimuita kwa jina lake zuri zaidi ambalo walikuwa wakimuita kwalo duniani, mpaka waishie kwenye mbingu ya chini kabisa. Hapo, wanaomba afunguliwe, kwa hivyo wanafunguliwa. Kisha anasindikizwa na Malaika walio karibu mno na Mwenyezi Mungu katika kila mbingu hadi mbingu inayofuatia." (Imepokelewa na Abu Daud 3212, An-Nasai 2001, Ibn Majah 1548, Abu Daud At-Twayalisi 789, Abdur-Razzaq 6324, 6737, Ahmad 18534, na matamshi haya ni yake.)
Kitabu cha kuamini Vitabu
Muhtasari wa Kitabu
Na tunaamini vitabu, ambavyo ni: Vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyoteremshwa kwa Mitume na Manabii wake, amani iwe juu yao, ambavyo tunavijua miongoni mwavyo: Vitabu vya Ibrahim na Vitabu vya Musa, Taurati, na Zaburi, na Injili na Qur'ani. Na tunaamini vile tunavyovijua miongoni mwavyo, na vile tusivyovijua.
Na tunaamini kwamba vitabu hivi vyote ni maneno ya Mwenyezi Mungu na ufunuo wake, na kwamba Mwenyezi Mungu aliiandika Taurati kwa mkono wake. Na Vitabu hivi aliviteremsha kwa Mitume wake, amani iwe juu yao, na Jibril Mwaminifu ndiye aliyeteremka navyo. Navyo vilijumuisha sheria, habari, mawaidha, maamrisho na makatazo. Na kila kitabu kilikuwa ndio ufunuo wa Mwenyezi Mungu katika wakati wake, ambacho kilikuwa ni lazima kukifanyia kazi, na kutafuta hukumu kutoka kwacho, kwa taifa ambalo liliteremshiwa kitabu hicho.
Na tunaamini kwamba baadhi yake ni bora kuliko vingine, kwani Mwenyezi Mungu aliiandika Taurati kwa mkono mwake.
Na tunajua kwa elimu ya yakini kwamba kuamini Vitabu vitakatifu ni nguzo ya tatu katika nguzo za imani, kwa hivyo tunaviamini vyote, wala hatuwi kama wale walioamini baadhi yake na wakakufuru baadhi yake.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu hakuweka dhamana ya kuhifadhi vitabu vyote vilivyoitangulia Qur’ani. Bali aliwakabidhi watu walioteremshiwa kukihifadhi. Na ndiyo maana, viliingiwa na upotoshaji na vikapotea na kusahaulika, kisha vikaandikwa na waongo na wakavinasibisha na Mwenyezi Mungu kwa uongo na uzushi. Wanaviandika na kuvisoma kwa ndimi zao ili kuzidi kuwachanganya viumbe, ili wafikirie kwamba vinatoka kwa Mwenyezi Mungu.
Na tunaamini kwamba Qur’ani Tukufu ndicho kitabu kikubwa kabisa cha Mwenyezi Mungu, na kilicho kamili zaidi na kitukufu zaidi. Nacho ndicho cha mwisho katika vitabu hivyo, ambacho alikiteremsha Jibril, amani iwe juu yake juu ya moyo wa Mtume wetu, Muhammad rehema na amani ziwe juu yake, kwa ulimi (Lugha) ya Kiarabu iliyo wazi. Na Mwenyezi Mungu alikiteulia lugha tukufu zaidi, na hilo ni kwa sababu lugha ya Kiarabu ndiyo lugha fasaha zaidi, iliyo wazi zaidi, pana zaidi kati ya lugha zote, na inayoeleza zaidi maana nyingi. Basi akateremsha kitabu kitukufu zaidi kwa lugha tukufu zaidi, kwa Mtume mtukufu zaidi, kupitia Malaika mtukufu zaidi, na hilo lilikuwa katika sehemu tukufu zaidi duniani, na kuteremshwa kwake kulianza katika mwezi mtukufu zaidi wa mwaka, ambao ni mwezi wa Ramadhani, kwa hivyo kikakamilika katika kila namna. Na aya yake ya kwanza aliyoiteremsha Mwenyezi Mungu ni kauli yake Mtukufu: "Soma kwa jina la Mola wako Mlezi aliyeumba." [Al-Alaq: 1] Na katika aya zake za mwisho zilizoteremshwa ni kauli yake Mtukufu: "Leo nimewakamilishia Dini yenu, na nimewatimizia neema yangu, na nimewaridhia kuwa Uislamu uwe ndiyo Dini." [Al-Maida: 3] Iliteremka kidogo kidogo kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, katika miaka ya unabii wake. Na miongoni mwake kuna aya zilizoteremka huko Makka na zilizoteremka Madina. Na idadi ya sura zake ni mia moja na kumi na nne. Na sura zake kubwa zaidi ni "Surat Al-Fatihah". Nayo "Surat Al-Ikhlas" inalingana na theluthi moja ya Qur'ani. Na aya zake tukufu zaidi ni Ayatul-Kursi.
Na Mwenyezi Mungu alikisifu kitabu hiki kikuu, na akakifanya kuwa ni nuru, uongofu, na rehema kwa waumini, na mawaidha na uponyaji kutokana na maradhi ya mioyo na miili.
Na tunaamini kwamba kitabu hiki kitukufu ndicho kitabu kamili zaidi na kilichosheheni zaidi, na kina hoja na uthibitisho wa kimungu, na kina mifano ambayo kwayo hoja inasimama juu ya viumbe hadi itakapofika Saa ya Kiyama. Nacho kinajumuisha kila kitu kilicho katika vitabu vya kimungu vilivyotangulia na hata kinaongezea juu yake. Na kinajumuisha kila kitu ambacho viumbe wanahitaji kama vile misingi ya imani, sheria, uthibitisho, hekima, mawaidha na habari mbalimbali. Nacho ni chenye ufasaha na ubainisho mkubwa zaidi. Na miongoni mwa ushahidi mkubwa zaidi kwamba Qur'an hii ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote ni kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa hajui kusoma wala kuandika, lakini aliteremshiwa kitabu kikubwa zaidi, na kikamilifu zaidi katika ufasaha na ubainisho.
Na tunaamini kwamba Qur’an ni ishara ya ajabu katika maneno yake na maana yake, na Mwenyezi Mungu aliwapa changamoto majini na wanadamu wote kwamba walete mfano wake, au sura kumi, au sura moja mfano wake.
Na tunaamini kuwa Qur’ani hii ni neno la Mwenyezi Mungu lililoteremshwa, ambalo halikuumbwa, na kwamba imehifadhiwa vifuani, imeandikwa ndani ya Misahafu, na inasomwa katika maeneo ya kuswalia yasiyokuwa misikiti, na katika misikiti, na hilo halifanyi kutokuwa maneno ya Mwenyezi Mungu. Na maneno ya Mwenyezi Mungu ni sifa miongoni mwa sifa zake, na chochote ambacho ni sifa ya Mwenyezi Mungu hakiwezi kuwa kimeumbwa. Kwani, kama ingekuwa imeumbwa, basi ingetokewa na yale yanayotokea katika vitu vyote vilivyoumbwa miongoni mwa mambo mapya kama vile kuangamia, kutoweka na kubadilika.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu amedhamini kuihifadhi Qur'ani hii, na hakuwaachia viumbe wake kufanya hivyo. Na aliifanya kuwa wazi sana, na akaifanya kutatiza mahali pengine, na akabainisha kuwa watu wapotofu wanafuata aya zile zenye kutatiza, lakini waumini wanaziamini zote; za wazi sana na zile zenye kutatiza ndani yake.
Na Mwenyezi Mungu ameifanya ni yenye kuhukumu vitabu vyote vilivyotangulia, na yenye kuvitawala, na kwamba kitabu hiki kinatusimulia habari za umma zilizopita, na kinapambanua kati ya Watu wa Kitabu katika yale waliyohitilafiana ndani yake.
Na tunaamini kwamba Qur'ani hii kubwa ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote, ambayo aliteremka nayo Roho Mwaminifu. Na jambo hili kimsingi linajulikana katika dini ya Waislamu kwa wanazuoni na watu wa kawaida, wote wamekubaliana juu ya hilo, na hakuna yeyote miongoni mwao aliyepinga. Na Mwenyezi Mungu ameishuhudia Qur’ani hii kwamba imetoka kwake, nao Malaika pia wakashuhudia kwamba Qur’ani hii ni uteremsho kutoka kwa Mwenye hekima, Mwenye kusifiwa. Na watu wa Kitabu (Mayahudi na Wakristo) wa wakati huu walimshuhudilia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, na Mwenyezi Mungu alitaja kushuhudia huku katika uteremsho wake ulio madhubuti. Na pia shahidi miongoni mwa majini alishuhudia kuwa Qur'ani hii ni uteremsho kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba unaafikiana na yale aliyokuja nayo Musa, amani imshukie. Na makafiri wa kikureshi pia walishuhudia kuwa Qur'ani hii si katika maneno ya wanadamu, na inatofautiana na maneno yao.
Na tunaamini kwamba yale yaliyomo ndani ya Qur'ani kati ya elimu ya Mwenyezi Mungu, hukumu za kisheria, na adabu zinazofaa kuzingatiwa - hayo yote yamethibiti katika maumbile asili ya mwanadamu, na yanaafikiana na yale waliyokuja nayo Manabii, amani iwe juu yao. Na misingi ambayo ilisisitizwa ndani ya Qur'ani ni ile ile waliyoilingania Mitume wote na wakaisisitiza.
Na Qur’ani Tukufu inaafikiana na kile anachotaka Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kutoka kwa viumbe, na inaafikiana na kile ambacho viumbe wanataka kutoka kwa Muumba wao. Hayo ni kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye Muumba, na anajua wanayo hitaji waja kutoka kwake, na anajua yenye kutengeneza dini zao, miili yao, mali zao na majumba yao, wala hakuamrisha kitu isipokuwa ndani yake kuna masilahi makubwa kabisa. Na wala hakukataza kitu isipokuwa katika kukataza kwake huko kuna tahadhari na ulinzi wa hali ya juu.
Na Qur’ani Tukufu inaafikiana na yale yanayohitajiwa na akili, na ndiyo maana Mwenyezi Mungu alipotaja mambo ya msingi yaliyoharamishwa katika “Surat Al-An’am” akayahitimisha kwa kusema: "ili myatie akilini."
Na ushahidi ambao Qur’ani Tukufu ilikuja nao ni ushahidi bainifu wa hali ya juu, na wenye ufasaha, na wa nguvu, na wa karibu na mwepesi. Kila mtu anaweza kuuelewa, na hakuna anayeweza kuutengua wala kuukataa. Na hili halijawahi kutokea katika maneno ya mwanadamu yeyote. Na ushahidi wake huu hauwezi - kwa hali yoyote ile - kuwa ushahidi juu ya batili.
Na Qur'ani Tukufu ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote, na pamoja na hayo yote imerahisishwa kwa kila mtu. Na si jambo la kawaida kwa wanadamu kwamba mmoja wao aandike kitabu, kisha kikawa rahisi kwa kila mtu, na kikamuhusu kila mtu. Hili halitokei isipokuwa kwa kitabu hiki kitukufu tu.
Na Qur'ani tukufu imehifadhiwa kutokana na mabadiliko na mambo yanayohitilafiana. Mwenyezi Mungu aliiandikia kubakia na kudumu hadi siku ya Kiyama. Na kubakia huku, na kudumu na kutobadilika kunaashiria kuwa ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa hekima, Mwingi wa kusifiwa. Na pamoja na kubakia kwake huku, kudumu kwake, na kuhifadhiwa kwake, na pamoja na kutokea kwa elimu na fani mpya, na uvumbuzi mbalimbali, hatujawahi kupata kuwa kuna elimu imeleta kinyume na kile kilichokuja katika Qur'ani. Bali elimu zote zinaafikiana na Qur'ani katika yale yaliyotajwa ndani yake, kama vile kuumbwa mbingu, kuumbwa mwanadamu, na mengineyo.
Na Qur'ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka zaidi, inajumuisha heri zote. Inajumuisha habari juu ya Muumba na viumbe, dunia na Akhera, majini na wanadamu, maamrisho na makatazo, adabu na wajibu mbalimbali, Pepo na Moto. Kwa hivyo, inajumuisha imani, matendo na malipo.
Na Qur'ani Tukufu ni tiba ya maradhi, na hayajawahi kujulikana maneno yoyote ya mwanadamu yenye tiba kwa maradhi ya nyoyo na miili, kama ilivyo katika Qur'ani hii tukufu, ambayo ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu.
Na Qur'ani inatusimulia habari za umma zilizopita kama zilivyotokea, na habari zao hizo hazikuwa zimeenea katika watu wa Makka, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akatusimulia habari hizo kama zilivyotokea. Na hilo ni ushahidi kwamba uteremsho huu ulitoka kwa Mwenye hekima, Msifiwa.
Na Qur’ani hii Tukufu ambayo inajumuisha ubainisho mkubwa mno, na ufasaha, na habari za ghaibu, na sheria za kiuungu, alikuja nayo Mtume asiyejua kusoma wala kuandika, na hili linaashiria kuwa Qur'ani hii ni uteremsho utokao kwa Mwenye hekima, Msifiwa. Na ilikuwa Sura moja katika Qur'ani Tukufu inateremka katika nyakati tofauti tofauti na katika sehemu tofauti tofauti. Lakini pamoja na hilo, sura hiyo inaweza kusomwa kana kwamba iliteremshwa mara moja tu. Na ni jambo la kawaida kwamba mwadamu ana uwezo tofauti tofauti, na wana mbinu tofauti tofauti wanapoandika vitabu katika nyakati mbalimbali.
Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipewa na Mwenyezi Mungu Sunna kama alivyopewa Qur'ani. Na mwenye kuitazama Qur'ani na Sunna, atajua kwamba kuna tofauti ambayo haifichiki baina ya viwili hivyo.
Na kwamba ndani ya Qur'ani kuna maelekezo kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, juu ya kile kinachopaswa kuwa, au kile anachopaswa kufanya.
Mlango wa ulazima wa kuamini Vitabu
Na tunaamini Vitabu, navyo ni Vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyoteremshwa kwa Mitume na Manabii wake, amani iwe juu yao.
Na vitabu tunavyovijua miongoni mwake ni: Vitabu vya Ibrahim, na Vitabu vya Musa, Taurati, na Zaburi, na Injili, na Qur'ani.
Na tunaamini vile tunavyovijua na vile tusivyovijua.
Na tunaamini kwamba vitabu hivi vyote ni maneno ya Mwenyezi Mungu na ni Ufunuo wake, ambao aliuteremsha kwa Mitume wake, amani iwe juu yao aliteremka nao Jibril mwaminfu. Nao unajumuisha sheria za kimungu, habari, mawaidha, maamrisho, na makatazo. Na kilikuwa kila kitabu katika zama zake ndio Ufunuo ambao ni lazima kutenda kwa mujibu wake na kutafuta hukumu kutoka ndani ya ufunuo huo.
Na tunaamini kwamba baadhi yake ni bora kuliko vingine, kwani Mwenyezi Mungu aliiandika Taurati kwa mkono mwake. "Na tukamuandikia katika mbao kila kitu, mawaidha na maelezo ya kina ya mambo yote." [Al-A'araf: 145] Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akieleza kuhusu Adam kwamba alimwambia Musa, amani iwe juu yao wote wawili. "Ewe Musa, Mwenyezi Mungu alikuteua kwa mazungumzo naye, na akakuandikia kwa mkono wake." (Imepokelewa na Bukhari 6614, Muslim 2652, Abu Daud 4701, Tirmidhi 2134, na Ibn Majah 80). Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema kuhusu Taurati: “Hakika Sisi tuliteremsha Taurati yenye uongofu na nuru, ambayo kwayo walihukumu Manabii walionyenyekea kiislamu.” [Al-Maida: 44]. Na amesema Mola wa Haki kuhusiana na Injili: "Na tukampa Injili iliyomo ndani yake uongofu, na nuru na inayosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake katika Taurati, na uongofu na mawaidha kwa wachamungu." [Al-Maida: 46].
Na kuamini Vitabu ndiyo nguzo ya tatu katika nguzo za kumuamini Mwenyezi Mungu, amesema Mola Mtukufu: "Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola Mlezi wake, na Waumini vile vile. Wote wamemuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake na Mitume wake. Hatutafautishi baina ya yeyote katika Mitume wake, na (Waumini) husema: Tumesikia na tumetii. Tunakutaka maghfira Mola Mlezi wetu! Na marejeo ni kwako." [Al-Baqara: 285] Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, alisema: Siku moja Mtume rehema na amani zimshukie, alikuwa nje kwa ajili ya watu, kisha akaja mwanaume mmoja akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, imani ni nini?" Akasema: “Ni umwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Kitabu chake, na kukutana naye, na Mitume wake, na uamini ufufuo wa mwisho.” (Imepokelewa na Bukhari 4777, Muslim 9, na Ibn Majah 64). Wala tusiwe kama wale walioamini baadhi yake na wakakufuru baadhi yake, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza kuhusu wao aliposema Aliyetakasika na kutukuka: "Hakika wale wanaomkufuru Mwenyezi Mungu na Mitume wake, na wanataka kufarikisha baina ya Mwenyezi Mungu na Mitume wake, na wanasema, "Wengine tunawaamini na wengine tunawakufuru." Na wanataka kushika njia iliyo kati kati ya haya." [An-Nisaa: 150] Au kama wale waliokadhibisha vitabu alivyoviteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mitume wake, kama Mola wa Haki alivyosema akieleza kuhusu wao katika kauli yake Mtukufu: "Ambao wamekadhibisha Kitabu na yale tuliyowatuma Mitume wetu nayo. Basi watakuja jua." [Ghafir: 70].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakuchukua dhamana ya kuhifadhi vitabu vyote vilivyoitangulia Qur’ani. Bali aliwakabidhi watu walioteremshiwa vitabu hivyo kuvihifadhi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu. “Hakika Sisi tuliteremsha Taurati yenye uongofu na nuru, ambayo kwayo Manabii walionyenyekea kiisilamu, na wachamungu, na wanazuoni, waliwahukumu Mayahudi; kwani walikabidhiwa kukihifadhi Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Nao wakawa ni mashahidi juu yake." [Al-Ma'ida: 44] Na ndiyo maana, vilipotoshwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi kwa sababu ya kuvunja kwao agano lao, tuliwalaani, na tukazifanya nyoyo zao kuwa ngumu. Wanayabadilisha maneno kutoka pahala pake, na wamesahau sehemu ya yale waliyokumbushwa." [Al-Ma'ida: 13].
Na vitabu hivi vya kiungu vilipotea na vikasahaulika, na wazushi wakaandika yale waliyoandika, kisha wakayanasibisha na Mwenyezi Mungu kwa uongo na uzushi. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Basi ole wao wale wanaoandika kitabu kwa mikono yao, kisha wakasema: Hiki kimetoka kwa Mwenyezi Mungu, ili wachumie kwacho pato dogo. Basi ole wao kwa yale iliyoandika mikono yao, na ole wao kwa yale wanayoyachuma." [Al-Baqara: 79] Na wanavisoma kwa ndimi zao ili kuzidi kuwachanganya viumbe, ili wafikirie kwamba vinatoka kwa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza kuhusu hilo: "Na hakika wapo baadhi yao wanaopindua ndimi zao katika kusoma Kitabu ili mdhanie kuwa hayo yanatoka Kitabuni, na wala hayatoki Kitabuni. Na husema, 'Haya yametoka kwa Mwenyezi Mungu.' Na wala hayatoki kwa Mwenyezi Mungu. Na wanamsingizia Mwenyezi Mungu uongo na wao wanajua." [Al-Imran: 78].
Mlango wa kuiamini Qur'ani Tukufu
Na tunaamini kuwa Qur’ani Tukufu ndicho kitabu kikubwa kabisa cha Mwenyezi Mungu, na kilicho kamili zaidi, na kitukufu zaidi. Nacho ndicho cha mwisho katika vitabu hivyo, ambacho Jibril, amani iwe juu yake, alikiteremsha juu ya moyo wa Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na bila ya shaka hiyo Qur'ani ni uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote* Ameuteremsha Roho muaminifu* Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji." [Ash-Shu'ara: 192-194] Na Mwenyezi Mungu aliichagulia (Qur'ani) lugha bora zaidi, na akaiteremsha kwa lugha ya Kiarabu iliyo wazi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani kwa Kiarabu ili mpate kuzingatia." [Yusuf: 2]. Amesema bin Kutaiba: “Fadhila za Qur’ani zinajulikana tu kwa wale wanaoitazama kwa makini, na wana elimu kubwa, na wanaelewa mafundisho ya kiarabu na kuvutiwa kwao na mifumo, na yale ambayo Mwenyezi Mungu ameijaalia lugha yao juu ya lugha nyingine zote. Kwani sio mataifa yote yana taifa ambalo limepewa upana, uwazi na upana wa upeo ambao Waarabu wamepewa hasa na Mwenyezi Mungu. Alipofanya elimu yake juu ya Mtume rehema na amani zimshukie na akamtaka athibitishe unabii wake kwa Kitabu, akampa elimu yake, kama alivyompa elimu kila Nabii miongoni mwa Mitume, inayofanana zaidi na yale yaliyokuwa katika wakati wake ambao alitumwa.” (Ta'wil Mushkil Al-Qur'an, uk. 17).
Na cha kwanza ambacho Mwenyezi Mungu alikiteremsha katika Qur'ani ni kauli yake Mtukufu: "Soma kwa jina la Mola wako Mlezi aliyeumba." [Al-Alaq: 1] Imesimuliwa kutoka kwa mama wa waumini, Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema kuhusu jambo la kwanza aliloanzishwa nalo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: Mpaka haki ilipomjia, huku akiwa katika pango la Hira. Malaika akamjia na akasema: "Soma, akasema: Mimi sio msomaji, akasema: Akanibana hadi ikanipata dhiki kisha akaniachia na akasema: Soma, na nikasema: Mimi sio msomaji, kwa hivyo akanichukua tena, na akanibana mara ya pili hadi ilipo nipata mimi dhiki, kisha akaniachilia, na akasema: Soma, na nikasema: Mimi sio msomaji, akanichukua tena kwa mara ya tatu, akanifunika, akanibana hadi ilipo nipata dhiki kisha akaniachilia, kisha akasema: "Soma kwa jina la Mola wako Mlezi aliyeumba * Amemuumba binadamu kwa tone la damu * Soma! Na Mola wako Mlezi ni Mkarimu kushinda wote!" [Al-Alaq: 1-3] Akarudi Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake huku moyo wake ukikitetemeka. (Imepokelewa na Bukhari 3, Muslim 160, na Tirmidhi 3632). Na miongoni mwa mambo ya mwisho aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu ni kauli yake Mtukufu: "Leo nimewakamilishia Dini yenu, na nimewatimizia neema yangu, na nimewapendelea Uislamu uwe ndiyo Dini." [Al-Ma'ida: 3].
Qur'ani iliteremka kidogo kidogo juu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, katika miaka ya unabii wake. Na miongoni mwake kuna aya zilizoteremka huko Makka na zilizoteremka Madina. Na idadi ya sura zake ni mia moja na kumi na nne. Na sura zake kubwa zaidi ni "Surat Al-Fatiha". Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa alisema: Jibril alipokuwa amekaa na Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisikia sauti kutokea juu yake, akainua kichwa chake na akasema: “Huu ni mlango wa mbinguni uliofunguliwa leo, na haukuwahi kufunguliwa isipokuwa leo.” kisha Malaika akateremka kutoka humo na akasema: Huyu ni Malaika aliyeteremka ardhini, na hajawahi kushuka isipokuwa leo. Kisha akatoa salamu na akasema: Pokea bishara njema ya nuru mbili ulizopewa ambazo hakuwahi kupewa nuru hizo Nabii yeyote kabla yako: Suratul-Fatiha na aya za mwisho za Suratul-Baqara. Hutasoma herufi katika hizo isipokuwa utapewa malipo yake." (Imepokelewa na Muslim 806 na An-Nasai 912). Na “Surat Al-Ikhlas” ni sawa na theluthi moja ya Qur’ani, Kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, amesema: Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie, alitujia na akasema: “Nitawasomeeni theluthi ya Qur’ani" Akasoma: “Sema: Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee. Mwenyezi Mungu Mkusudiwa." Mpaka akaihitimisha. (Imepokelewa na Muslim 812).
Na Aya yake kuu ni Ayat al-Kursi. Kutoka kwa Ubaiya bin Kaab, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, amesema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: “Ewe Abuu Mundhiri, unajua ni aya gani katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu kilicho pamoja nawe ni bora zaidi?" Anasema: Nikasema: Mwenyezi Mungu na Mtume wake wanajua zaidi. Akasema: “Ewe Abuu Mundhiri, je, unajua ni aya gani katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu ulicho pamoja nacho ambayo ni bora zaidi?” Akasema: {Mwenyezi Mungu hakuna mungu ila Yeye Aliye Hai, Msimamizi} [Al-Baqarah: 255]. Akasema: Alipiga kwenye kifua changu na akasema: “Wallahi ubarikiwe katika elimu yako, ewe Abuu Mundhiri". (Imepokelewa na Muslim 810, na Abuu Daud 1460).
Mwenyezi Mungu alijisifu mwenyewe kwa uteremsho wa kitabu hiki, akasema aliye tukuka sifa zake: "Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliye mteremshia mja wake Kitabu, wala hakukifanya kupinda." [Al-Kahf: 1]. Kama vile Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyokisifu kitabu hiki kikubwa, akasema Mola wa Haki Mtukufu, na Mwenye Mamlaka: "Lau tungeliiteremsha hii Qur’ani juu ya mlima, ungeuona ukiwa mnyenyekevu na kuporomoka kwa sababu ya kumcha Mwenyezi na hiyo mifano tunawatolea watu huenda wakatafakari." [Al-Hashr: 21] Na amesema pia Mwenyezi Mungu Aliyetakasika: "Hata kama Qur'ani itapitishwa katika milima au ardhi ikakatwa, au kama wafu watasemeshwa kwayo." [Ar-Ra'd: 31] Na akaifanya kuwa ni uongofu na rehema kwa Waumini, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hizi ni dalili za wazi kwa watu wote na ni uongozofu na rehema kwa watu wenye yakini." [Al-Jathiya: 20] Na ni mawaidha na ponyo kutokamana na magonjwa ya mioyo na miili, akasema Mola wa Haki aliye tukuka katika jambo lake: "Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha la yaliyomo vifuani, na uongofu, na rehema kwa Waumini" [Yunus: 57] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na tunateremsha katika Qur’ani yaliyo ni ponyo na rehema kwa Waumini, na haiwazidishii madhalimu ila hasara." [Al-Israa: 82].
Na tunaamini kwamba kitabu hiki kikubwa ni kitabu chenye ukamilifu na chenye kueleza zaidi kati ya vitabu vya Mwenyezi Mungu, na kina hoja na uthibitisho na mifano ambayo itakuwa ni ushahidi juu ya viumbe hadi Siku ya Kiyama amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Umekufikieni ushahidi kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Na tumekuteremshieni Nuru iliyo wazi." [An-Nisaa: 174] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Wala hawatakuletea mfano wowote, isipokuwa na Sisi tutakuletea (jawabu) kwa haki, na tafsiri iliyo bora zaidi." [Al-Furqan: 33] Na amesema Mtukufu: "Na hakika tumewaeleza watu katika hii Qur'ani kwa kila mfano. Lakini watu wengi wanakataa isipo kuwa kukufuru tu." [Al-Israa: 89] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na tumekwisha bainisha katika Qur'ani hii ili wapate kukumbuka. Lakini haikuwazidishia ila kuwa mbali nayo." [Al-Israa: 41] Amesema bin Jariri: Na anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hakika tumekwisha wabainishia" washirikina hawa wanaomsingizia Mwenyezi Mungu "katika Qur'ani hii" mazingatio, ishara na hoja mbalimbali, na tukawapigia mifano humo na tukawatahadharisha ndani yake, na tukawaonya, "ili wapate kukumbuka" hoja hizo zilizo juu yao, na ili wapate kufahamu makosa wanayoendelea kuyafanya, na wazingatie mazingatio na wawaidhike kwayo, na watubie kutokana na ujinga wao, lakini hawazizingatii, wala hawazikumbuki Ishara na maonyo yanayowajia. (Tafsir Twabari 17/185).
Qur'ani hii kubwa ina kila kitu kilichoko katika vitabu vitakatifu vilivyotangulia, na ikaongeza juu yake, Mwenyezi Mungu anasema: "Na limetimia neno la Mola Mlezi wako kwa haki na uadilifu, na hapana awezaye kuyabadilisha maneno yake. Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua zaidi." [Al-An'am: 115] Na imekusanya kila kitu wanachokihitaji viumbe, kuanzia misingi ya imani, sheria, hoja, hekima, mawaidha na habari, amesema Mola wa Haki Aliyetukuka: "Hakika hii Qur'ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka kabisa." [Al-Isra: 9] Na amesema Mtukufu: "Sisi tunasimulia simulizi nzuri kwa kukufunulia Qur'ani hii." [Yusuf: 3]. Nayo kwenye upeo wa ufasaha sana na ubainifu, amesema Mwenyezi Mungu aliye tukuka: "Mwenyezi Mungu ameteremsha hadithi nzuri kabisa, Kitabu chenye kufanana na kukaririwa." [Az-Zumar: 23]. Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Nimetumwa kwa sentensi fupi zilizokusanya (Maana zote), na nimenusuriwa na hofu." (Imepokelewa na Bukhari 2977, Muslim 523, Tirmidhi 1553, na An-Nasai 3087).
Na miongoni mwa ushahidi mkubwa zaidi kwamba Qur'ani hii ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote ni kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa hajui kusoma wala kuandika, lakini aliteremshiwa kitabu kikubwa zaidi, na kikamilifu zaidi katika ufasaha na ubainisho, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na wewe hukuwa kabla yake unasoma kitabu chochote, wala hukukiandika kwa mkono wako wa kulia. Ingelikuwa hivyo wangelifanya shaka wavunjifu." [Al-Ankabut: 48] Na amesema Mtukufu: "Muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake asiyejua kusoma na kuandika, ambaye anamuamini Mwenyezi Mungu na maneno yake. Na mfuateni Yeye ili mpate kuongoka." [Al-A'araf: 158].
Na tunaamini kuwa Qur'ani ni muujiza wa kushangaza katika matamshi yake, na maana yake, na Mwenyezi Mungu aliwapa changamoto majini na wanadamu wote kuja na mfano wake, au kwa sura kumi kama hiyo, au kwa sura moja, ametakasika Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu wote, na amesema Mola wa Haki Aliyetukuka: "Sema: Wangeli kusanyika watu na majini ili walete mfano wa hii Qur'ani basi (kamwe!) wasingeleta mfano wake, hata wakisaidiana wao kwa wao." [Al-Israa: 88] Na amesema Mtukufu: "Au wanasema: Ameizua? Sema: Basi leteni Sura kumi zilizo zuliwa mfano wa hii, na waiteni muwawezao badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli." [Hud: 13]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ikiwa mna shaka kwa hayo tuliyo mteremshia mja wetu basi leteni sura moja ya mfano wake, na muwaite mashahidi wenu badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli." [Al-Baqara: 23].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amedhamini kuihifadhi Qur'ani hii, na hakuwaachia viumbe wake kufanya hivyo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Sisi ndio tulio teremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutakaoulinda." [Al-Hijr: 9]. Na amesema Mtukufu: "Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hekima, Msifiwa." [Fusswilat: 42] Na akakifanya chote kuwa wazi kwa mujibu wa uwazi wa ujumla. Amesema Mola Mtukufu: "Alif Lam Ra. Hiki ni Kitabu ambacho Aya zake zimewekwa wazi, kisha zikapambanuliwa, kilichotoka kwa Mwenye Hekima na Mwenye habari zote." [Hud:1] Kama alivyokifanya pia kuwa cha mifano (chenye kufanana) chote, amesema Mola wa Haki, aliyetakasika: "Mwenyezi Mungu ameteremsha hadithi nzuri kabisa, Kitabu chenye kufanana na kukaririwa." [Az-Zumar: 23] Na akajalia ndani yake aya zilizo wazi na aya zenye kutatiza, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yeye ndiye aliye kuteremshia Kitabu hichi. Ndani yake zimo Aya muhkam, zenye maana ya wazi. Hizo ndizo msingi wa Kitabu hichi. Na ziko nyingine za mifano. Ama wale ambao nyoyoni mwao umo upotovu wanafuata zile za mifano kwa kutafuta fitina, na kutafuta maana yake; na wala hapana ajuaye maana yake ila Mwenyezi Mungu. Na wale wenye msingi madhubuti katika elimu husema: Sisi tumeziamini, zote zimetoka kwa Mola wetu Mlezi. Lakini hawakumbuki hayo isipokuwa wenye akili." [Al-Imran: 7] Na akabainisha kwamba watu wa upotovu wanafuata zile za mkanganyo, na waumini wanaziamini zote za wazi zake na za mifano ndani yake.
Na Mwenyezi Mungu ameifanya ni yenye kuhukumu vitabu vyote vilivyotangulia, na yenye kuvitawala. Amesema Mwenyezi Mungu aliyetukuka: "Na tumekuteremshia wewe, kwa haki, Kitabu hiki kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake katika Vitabu na kuyalinda." [Al-Maida: 48]. Na akabainisha Mola wa Haki kuwa hakika kitabu hiki kinatusimulia habari za umma zilizopita, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hizi ni katika habari za ghaibu tulizokufunulia. Na hukuwa pamoja nao walipoazimia shauri lao, walipofanya njama zao wakizua vitimbi." [Yusuf: 102] Na ipo mifano mingi inayofanana na hii, na Qur’ani inapambanua baina ya Watu wa Kitabu katika yale waliyohitilafiana. Amesema Mola Mtukufu: "Hakika Qur'ani hii inawasimulia Wana wa Israeli mengi wanayohitilafiana ndani yake." [An-Naml: 76].
Na alisema Omari bin Khattwab Mwenyezi Mungu amridhie, akiwa juu ya mimbari yake: "Hakika Qur’ani hii ni maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu. Basi iwekeni mahali pake, wala musifuate matamanio yenu ndani yake. (Imepokelewa na Ahmad katika Az-Zuhd 191, Ad-Darmi 3398, Abdullah bin Ahmad katika As-Sunna 117, Al-Ajurri katika Ash-Sharia 155, na matamshi haya ni yake, na Ibn Battwa katika Al-Ibana 23).
Na alisema Omari bin Khattwab pia, Mwenyezi Mungu amridhie: "Qur’ani ni maneno ya Mwenyezi Mungu, basi msiichanganue kulingana na maoni yenu." (Imepokelewa na Al-Ajurri katika Ash-Sharia 156).
Na imesimuliwa kutoka kwa Farwa bin Naufal Al-Ashja’i kuwa alisema: “Khabbab bin Aratti, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alikuwa jirani yangu, na aliniambia siku moja: Ewe Hana, jiweke karibu na Mwenyezi Mungu uwezavyo, na jua ya kwamba hutajiweka karibu naye kwa kitu chochote anachokipenda zaidi kuliko maneno yake." (Imepokelewa na Abu 'Ubaid katika Fadhail-AlQur'an, uk. 77, Ibn Abī Shaiba 30722, Ahmad katika Az-Zuhd 192, 'Uthman ibn Sa 'īd ad-Dārimī katika Ar-Raddu alal-Jihmiyyah 160, na 'Abdullah ibn Ahmad katika As-Sunna 111).
Na tunaamini kwamba Qur’ani hii ni maneno ya Mwenyezi Mungu, yaliyoteremshwa na hayakuumbwa, na kuwa yamehifadhiwa vifuani, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Bali hii (Qur'ani) ni Ishara zilizo wazi katika vifua vya wale waliopewa elimu. Na hawazikatai Ishara zetu isipokuwa wenye kudhulumu." [Al-Ankabut: 49] Ni sawa iwe imeandikwa katika misahafu, au inasomwa katika maeneo ya kuswalia yasiyokuwa misikiti, na katika misikiti, basi hilo haliifanyi kutokuwa maneno ya Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika wale wanaosoma Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na wakashika Swala, na wakatoa kwa siri na kwa dhahiri katika vile tulivyowaruzuku, hao hutaraji biashara isiyobwaga." [Fatwir: 29] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Bila shaka hiki ni kitabu kilichokusanya kila yanayohitajiwa na chenye heshima * Katika Kitabu kilicho hifadhiwa kwelikweli * Hapana akigusaye ila waliotakaswa * Ni uteremsho unaotoka kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote." [Al-Waqia': 77-80]
Na Qur’ani tukufu ni maneno ya Mwenyezi Mungu, na maneno yake ni sifa miongoni mwa sifa zake, na chochote ambacho ni sifa miongoni mwa sifa za Mwenyezi Mungu, hakiwezi kuwa kimeumbwa, kwakuwa kama kingekuwa kimeumbwa basi yangeyatokea yale yanayovitokea vitu vyote vilivyoumbwa miongoni mwa mambo mapya kama vile kuangamia, kutoweka na kubadilika, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hivi hawaizingatii hii Qur'ani? Na lau ingekuwa imetoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, bila ya shaka wangelikuta ndani yake kuhitilafiana kwingi." [An-Nisaa: 82] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na ikiwa mmoja wapo katika washirikina akikuomba ulinzi, basi mpe ulinzi apate kusikia maneno ya Mwenyezi Mungu. Kisha mfikishe pahala pake pa amani. Haya ni kwa kuwa hao ni watu wasiojua kitu." [Tauba: 6].
Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akiwatafutia ulinzi wa Mwenyezi Mungu Al-Hasan na Al-Husein akisema: “Hakika baba yenu alikuwa akiwatafutia Ismail na Is'haq ulinzi wa Mwenyezi Mungu kwa hayo akisema: Ninajikinga kwa maneno makamilifu ya Mwenyezi Mungu, kutokana na kila shetani na kila chenye sumu, na kutokana na kila jicho lenye husuda." (Imepokelewa na Bukhari 3371, Abu Daud 4737, na akasema: Huu ni ushahidi kwamba Qur'ani haikuumbwa, na Tirmidhi 2060, na Ibn Majah 3525).
Na Ismail bin Abi Uwais alisimulia makubaliano ya watu wa Madina kwamba Qur'ani haijaumbwa, akasema: “Maliki na wanazuoni wa raia wa nchi yetu walikuwa wakisema: “Qur’ani imetokana na Mwenyezi Mungu, na hakuna chochote kinachotokana na Mwenyezi Mungu kilichoumbwa. Na wanazuoni wa watu wa Madina katika zama za Maliki bin Anas walikuwa ni: Muhammad bin Abdur-Rahman bin Abi Dhi'b, Abdul Aziz bin Abi Salama Al-Majshun, na Abubakari bin Abi Swabra, na Ibrahim bin Sa'ad Az-Zuhri, na Said bin Abdur-Rahman Al-Jumahi, Hatim bin Ismail, Abdullah bin Abdulaziz Al-Amri Az- Zaahid, Abu Dhwamra Anas bin 'Iyyadh, na Muhammad bin Ismail bin Abi Fudaiki. (Sharh Usul I'tikad Ahlul-sunna wal-jamaa 2/300).
Na amesema Shuaib bin Harb: Nilimwambia Abuu Abdullah Sufian bin Said Ath-Thauri: Nisimulie hadithi kutoka katika Sunna ambayo ataninufaisha nayo Mwenyezi Mungu Mtukufu nitakaposimama mbele ya Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika, na kutukuka, na akaniuliza juu yake, akaniambia: Uliyachukua haya wapi? Nitasema: Ewe Mola Mlezi, ni Sufian Ath-Thauri alinisimulia hadithi hii, na nikaichukua kutoka kwake, kwa hivyo nikaokoka, nawe ukachukuliwa makosa.' Akasema: Ewe Shuaib, huku ni kusisitiza. Na ni kusisitiza kulioje! Andika: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu: Qur'ani ni maneno ya Mwenyezi Mungu ambayo hayakuumbwa, kwake yalianza na kwake yatarudi.' (Sharh Usul I'tikad Ahlus-sunna wal-jamaa 1/170).
Na amesema imamu Ibin Jariri Twabari: "Alitusimulia bin Uyaina, akasema: Nilimsikia Amri bin Dinari akisema: Niliwakuta mashekhe wetu tangu miaka sabini huku wakisema: Qur'ani ni maneno ya Mwenyezi Mungu, kwake yalianza na kwake yatarudi." (Swariih As-sunna, cha Twabari, uk. 19).
Na imesimuliwa kutoka kwa Al-Hasan bin Ayub kuwa alisema: "Nilimsikia Ahmad bin Hanbal akisema kuhusu Al-Fariyabi: Nilimsikia Ath-Thauri - akimaanisha Sufian - akisema: Yeyote mwenye kusema: Qur'ani imeumbwa, basi huyo ni zandiki (muongo mkubwa)." Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Ahmad bin Hanbal alisema: Nilimsikia baba yangu akisema: Ilinifikia kutoka kwa Ibrahim bin Sa'ad, na Saidi bin Abdur-Rahman Al-Jumahi, na Wahb bin Jariri, na Abuu Nadhiri Hashim bin Qassim, na Suleiman bin Harb walisema kuwa: Qur'ani haikuumbwa. (Sharh Usul I'tikad Ahlus-sunna wal-jamaa 2/277).
Imamu wa Maimamu, Muhammad bin Khuzaima, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango juu ya suala hili na akasema: "Mlango wa ushahidi unaoonyesha kwamba Qur'an ni maneno ya Mwenyezi Mungu, Muumba, na kauli yake haikuumbwa." (At-Tauhid, cha Ibn Khuzaima 1/404).
Na amesema Abuu Saidi Ad-Darmi: “Kwa hivyo, katika hadithi hizi kuna maelezo kuwa Qur’ani haikuumbwa; Kwa sababu hakuna tofauti yoyote baina ya viumbe katika ubora ulio baina yao, kama ulivyo ubora ulio baina ya Mwenyezi Mungu na viumbe wake. Kwa maana ubora ulio kati ya viumbe unaweza kufikiwa, lakini haiwezekani kuufikia ubora wa Mwenyezi Mungu kwa viumbe wake, na wala hakuna anayeweza kuudhibiti, na vile vile ubora wa maneno yake juu ya maneno ya viumbe. Na kama ingekuwa ni maneno yaliyoumbwa, basi haungekuwa ubora ulio kati yake na maneno mengineyo kama ubora wa Mwenyezi Mungu juu ya viumbe vyake, wala hata kama moja ya ishirini ya sehemu milioni moja, wala hata karibu na hivyo. Basi fahamuni hilo. Kwani hapana chenye mfano wake. Kwa hivyo, hakuna maneno kama maneno yake, wala hayatawahi letwa kamwe kama maneno yake." (Ar-Raddu Alal-Jahmiyyah, cha Ad-Darmi, uk. 188).
Na amesema Abuu Yusuf, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Ama kuhusu Qur'ani, hiyo ni maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, na ni ufunuo wake na ni uteremsho wake. Hivi ndivyo nilivyomkuta Abuu Hanifa na Maimamu wakiamini, na hawakuwa wakiamini kwamba imeumbwa, wala yenye kuumba." (Al-I'tikad, cha Naisaburii, uk 135).
Mlango wa Qur'ani Tukufu ni uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote.
Na tunaamini kuwa Qur'ani hii tukufu ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote, aliteremka nayo Roho Mwaminifu (Jibril). Na hili linajulikana katika dini ya Waislamu kama jambo la kimsingi. Na Waislamu wote wamekubaliana juu ya hilo, na wala hakuna yeyote miongoni mwao aliyelipinga. Na jambo hili - yaani kuwa imetoka kwa Mola Mlezi wa walimwengu - linaonyeshwa na ushahidi mwingi ambao hauwezekani kudhibitiwa, wala kuzungukwa, na miongoni mwake ni:
Ushahidi wa Mwenyezi Mungu kwa Qur'ani hii kuwa imetoka kwa Mwenyezi Mungu, amesema Mola wa Haki na kauli yake ni ya kweli: "Sema: Kitu gani ushahidi wake ni mkubwa kabisa? Sema: Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye shahidi baina yangu na nyinyi. Na nimefunuliwa Qur'ani hii ili kwayo niwaonye nyinyi na kila inayemfikia." [Al-An'am: 19] Na amesema Mtukufu: "Lakini Mwenyezi Mungu anayashuhudia aliyo kuteremshia wewe. Ameyateremsha kwa kujua kwake." [An-Nisaa: 166]
Na miongoni mwake ni ushahidi wa Malaika kwamba Qur'ani hii ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa hekima na Msifiwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lakini Mwenyezi Mungu anayashuhudia aliyokuteremshia wewe. Ameyateremsha kwa kujua kwake - na Malaika pia wanashuhudia. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi." [An-Nisaa: 166]
Na miongoni mwake ni kuwa inaafikiana na yale waliyokuja nayo Manabii, amani iwe juu yao, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote isipokuwa Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie maneno ya kuwaudhi Wala usiwakemee. Na sema nao kwa maneno ya heshima." [Al-Israa: 23]. Hadi katika kuali yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Haya ni katika hekima alizokufunulia Mola wako Mlezi. Wala usimweke pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwingine, usije ukatupwa katika Jahannamu ukilaumiwa na kufurushwa." [Al-Israa: 39].
Na amesema Mtukufu: "Amekuteremshia Kitabu kwa haki, kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake. Na aliteremsha Taurati na Injili." [Al-Imran: 3]. Basi misingi hii yote iliyotajwa kwa kusisitizwa ni ile ambayo mitume walilingania na kuisisitiza.
Na miongoni mwake ni ushahidi wa Mayahudi na Wakristo walioishi katika zama za Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, Mwenyezi Mungu akautaja ushahidi huu katika ufunuo wake madhubuti, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Mwaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi mkayakataa, na akashuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa Israeli juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mkafanya kiburi? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu." [Al-Ahqaf: 10]. Na katika vitabu vya hadithi Sahihi katika habari za Waraqa baada ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kumwambia aliyoyaona: “Waraqa akamwambia: "Huyu ndiye Malaika ambaye Mwenyezi Mungu alimteremshia Musa." (Imepokelewa na Bukhari 6227, na Muslim 2841).
Na katika habari ya Ja'fari, Mwenyezi Mungu amridhie, Mfalme Najashi alipomuuliza: Je, una chochote katika yale aliyokuja nayo Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake? Basi akamsomea, kisha Mfalme Najashi akasema: "Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, hakika maneno haya na maneno aliyokuja nayo Musa yalitoka katika chanzo(mahali) pamoja.” (Imepokelewa na Ishaq bin Rahwaihi 1835, Ahmad 22498, Ibn Khuzaimah 2260, Twahawi katika Sharh Mushkil Al-Aay 5598, Abu Nu'aim katika Al-Hilya 1/115, na katika Dalail An-Nubuwwa 194).
Na miongoni mwake ni ushahidi wa majini kwamba Qur’ani hii ni ufunuo kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na kwamba inaafikiana na yale aliyokuja nayo Musa, amani iwe juu yake. "Na wakati tulipowaleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur'ani. Basi walipoihudhuria, walisema: Sikilizeni! Na ilipokwisha somwa, walirudi kwa watu wao kwenda kuwaonya * Wakasema: Enyi watu wetu! Hakika sisi tumesikia Kitabu kilichoteremshwa baada ya Musa, kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na kinachoongoza kwenye Haki na kwenye Njia iliyonyooka." (Al-Ahqaf: 29, 30) Na amesema Mtukufu: "Sema: Imefunuliwa kwangu ya kuwa kundi moja la majini lilisikiliza, na likasema: Hakika sisi tumeisikia Qur'ani ya ajabu! * Inaongoza kwenye uongofu, kwa hivyo tumeiamini, wala hatutamshirikisha yeyote na Mola wetu." [Al-Jinn: 1,2]
Na miongoni mwake ni ushahidi wa makafiri wa kikuraishi kuwa Qur'ani hii si katika maneno ya wanadamu, na kuwa ni tofauti na maneno yao. Imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, alisema kuwa: “Al-Walid bin Mughiira alikuja kwa Mtume rehema na amani zimshukie, akamsomea Qur'ani, akawa kana kwamba ameathirika nayo. Basi hilo likamfikia Abuu Jahali, akamjia na akasema: "Ewe Ami, hakika watu wako wameshauriana kuwa wakukusanyie mali". Akasema: "Kwa nini?" Akasema: "Ili wakupe mali hiyo. Kwani hakika wewe ulimjia Muhammad ili akupe alicho nacho." Akasema: "Hakika Makuraishi walikwishajua kuwa mimi ni katika watu wenye mali nyingi miongoni mwao." Akasema: "Basi sema juu yake jambo ambalo litawafikia watu wako kuwa wewe unamkataa, au kwamba unamchukia." Akasema: "Niseme nini?!" Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, hakuna mwanaume yeyote miongoni mwenu ajuaye aina mbalimbali za mashairi kuliko mimi, hata mashairi ya majini. Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, hayo anayoyasema hayafanani na chochote na haya. Na ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, kuwa hakika maneno anayosema ni matamu, na yana uzuri mkubwa, na hakika sehemu yake ya juu inazaa matunda, na ya chini yake ni yenye ukwasi; na hakika yanashinda wala hayashindwi, na hakika yanapondaponda yaliyo chini yake." (Imepokelewa na Hakim 3872, Al-Baihaqi katika Ash-Shu'ab 133, na katika Dalail An-Nubuwwa 2/198).
Na miongoni mwake ni kwamba Qur’ani hii tukufu inaafikiana na kile anachotaka Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kutoka kwa viumbe, amesema Mola Mtukufu: "Na kwa hakika hii ndiyo Njia yangu iliyonyooka. Basi ifuateni, wala msifuate njia nyinginezo, zikawatenga na Njia yake. Haya amewausia ili mpate kumchamungu." [Al-An'am: 153].
Na miongoni mwake ni kuwa yale yaliyo ndani ya Qur’ani miongoni mwa elimu ya kimungu, hukumu za kisheria, na adabu zinazopaswa kuzingatiwa, yote hayo ni katika yale yaliyothibiti katika maumbile asili ya mwanadamu. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Basi uelekeze uso wako sawa sawa kwenye Dini -ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo Dini iliyonyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui." [Ar-Rum: 30].
Na miongoni mwake ni kuwa Qur'ani tukufu inaafikiana na mambo yenye masilahi kwa viumbe. Na hilo ni kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye Muumba, kwa hivyo anajua kile ambacho waja wanahitajia, na anajua chenye kufanya dini zao kutengemaa, na miili yao, na mali zao, na majumba yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Asijue aliyeumba, naye ndiye Mjua siri, Mwenye habari?" [Al-Mulk: 14]. Wala hakuamrisha kitu isipokuwa ndani yake kuna masilahi makubwa kabisa. Na wala hakukataza kitu isipokuwa katika kukataza kwake huko kuna tahadhari na ulinzi wa hali ya juu.
Na miongoni mwake ni kwamba Qur’ani tukufu inaafikiana na yale yanayohitajiwa na akili, na ndiyo maana Mwenyezi Mungu alipotaja mambo ya msingi yaliyoharamishwa katika “Surat Al-An’am” akayahitimisha kwa kusema: "ili myatie akilini." Amesema Mtukufu: "Sema: Njooni niwasomee yale aliyowaharamishia Mola wenu Mlezi. Nayo ni kuwa, msimshirikishe Yeye na chochote. Na wazazi wenu wafanyieni wema. Wala msiwauwe watoto wenu kwa sababu ya umasikini. Sisi tunawaruzuku nyinyi na wao. Wala msikaribie mambo machafu, yanayo onekana, na yaliyo fichikana. Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharamisha kuiuwa, isipokuwa ikiwa ni kwa haki. Hayo amewausia ili myatie akilini." [Al-An'am: 151].
Na Qur’ani imewasemesha watu wenye akili kwa mara zisizohesabika, kama vile Mwenyezi Mungu mara nyingi huwataka waja wake kutafakari, kutazama, na kuzingatia yale anayoamrisha au kukataza.
Na miongoni mwake ni kwamba ushahidi ulioletwa na Qur'ani Tukufu ni ushahidi wenye ubainifu mkubwa mno, na wenye ufasaha, nguvu, ukaribu, na wepesi, ambao kila mtu anauelewa. Na hili halijulikani katika maneno ya mwanadamu yeyote yule, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye! Lakini madhalimu wamo katika upotovu ulio dhahiri." [Luqman: 11]. Na katika maneno yake Aliyetakasika na kutukuka: "Lau wangelikuwamo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu, basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeliharibika. Sub-haanallaah (Ametakasika Mwenyezi Mungu), Bwana wa 'Arshi (Kiti cha Enzi), na hayo wanayoyazua." [Al-Anbiya: 22] Kama vile ushahidi wake mbalimbali hauwezi - kwa hali yoyote ile - kuwa ushahidi juu ya batili. Na katika nguvu ya ushahidi wake ni kwamba ushahidi huu hauwezi kuvunjiliwa mbali wala kukataliwa. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na sema: Kweli imefika, na uongo umetoweka. Hakika uongo lazima utoweke!" [Al-Israa: 81].
Na miongoni mwake ni kwamba Qur’ani tukufu – ambayo ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote – imesahilishwa (imerahisishwa) kwa kila mtu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kufahamika. Lakini yupo anayekumbuka?" [Al-Qamar: 17]. Na si jambo la kawaida kwa wanadamu kuwa mmoja wao aandike kitabu, kisha kikawa rahisi kwa kila mtu, na kikamuhusu kila mtu. Hili halitokei isipokuwa kwa kitabu hiki kitukufu tu.
Na miongoni mwake ni kwamba Qur’ani tukufu imehifadhiwa kutokana na kugeuzwa na kubadilishwa. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Sisi ndio tulioteremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutakaoulinda." [Al-Hijr: 9]. Na Mwenyezi Mungu aliweka amri kuwa Qur'ani ni lazima ibakie na idumu hadi siku ya Kiyama. Na kubakia huku, na kudumu na kutobadilika kunaashiria kuwa ni uteremsho kutoka kwa Mwingi wa hekima, Msifiwa, amesema Mola wa Haki: "Hebu hawaizingatii hii Qur'ani? Na lau kuwa ingekuwa imetoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, bila ya shaka wangelikuta ndani yake kuhitilafiana kwingi." [An-Nisaa: 82]
Na pamoja na kubakia kwake huku, kudumu kwake, na kuhifadhiwa kwake, na pamoja na kutokea kwa elimu na fani mpya, na uvumbuzi mbalimbali, hatujawahi kupata kwamba kuna elimu iliyokuja na jambo kinyume na yale yaliyokuja katika Qur'ani. Bali elimu zote zinaafikiana na Qur'ani katika yale yaliyotajwa ndani yake, kama vile kuumbwa mbingu, kuumbwa mwanadamu, na mengineyo.
Na miongoni mwake ni kwamba Qur'ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka zaidi, inajumuisha heri yote. Inajumuisha habari juu ya Muumba na viumbe, dunia na Akhera, majini na wanadamu, maamrisho na makatazo, adabu na wajibu mbalimbali, Pepo na Moto. Kwa hivyo, inajumuisha imani, matendo na malipo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote." [Al-An'am: 38]. Na amesema Mtukufu: "Hakika hii Qur'ani inaongoa kwenye yale yaliyonyooka kabisa." [Al-Israa :9]
Na miongoni mwake ni kwamba Qur’ani tukufu ni ponya ya maradhi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Yamewajia mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha ya yaliyomo vifuani, na uongofu, na rehema kwa Waumini" [Yunus: 57] Na hayajawahi kujulikana maneno yoyote ya mwanadamu yenye tiba kwa maradhi ya nyoyo na miili, kama ilivyo katika Qur'ani tukufu, ambayo ni maneno ya Mola Mlezi wa walimwengu wote.
Na miongoni mwake ni kwamba Mwenyezi Mungu aliwapa changamoto watu na majini kuwa walete mfano wake, au sura kama hiyo, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, ndiyo wanasema ameizua? Sema: Hebu leteni sura moja mfano wake na muwaite (wa kuwasaidia) muwawezao, isiyekuwa Mwenyezi Mungu, ikiwa nyinyi ni wakweli." [Yunus: 38], Na alibainisha kwamba haina shaka yoyote ndani yake, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Na haiwezekani Qur'ani hii kuwa imetungwa na haitoki kwa Mwenyezi Mungu. Lakini hii inasidikisha yale yaliyotangulia, na ni ufafanuo wa kina wa Kitabu kisicho na shaka ndani yake, kutoka kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote." [Yunus: 37].
Na miongoni mwake ni kuwa Qur’ani hii inatusimulia habari za umma zilizopita kama zilivyotokea, na habari zao hizo hazikuwa zimeenea kwa watu wa Makka, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akatusimulia habari hizo, kama ilivyo katika maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sisi tunasimulia simulizi nzuri kwa kukufunulia Qur'ani hii. Ijapokuwa kabla ya haya ulikuwa miongoni mwa wasiojua." [Yusuf: 3]. Na hilo ni ushahidi kwamba uteremsho huu ulitoka kwa Mwenye hekima, Msifiwa.
Na miongoni mwake ni kuwa Qur’ani hii tukufu ambayo inajumuisha ubainisho mkubwa mno, na ufasaha, na habari za ghaibu, na sheria za kiungu, alikuja nayo Mtume asiyejua kusoma wala kuandika. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na wewe hukuwa kabla yake unasoma kitabu chochote, wala hukukiandika kwa mkono wako wa kulia. Ingelikuwa hivyo, wangelifanya shaka wana batili." [Al-Ankabut: 48], Na amesema Mtukufu: "Wale wanaomfuata Mtume huyo, Nabii, asiyesoma wala kuandika, wanayemkuta kaandikwa kwao katika Taurati na Injili." [Al-A'raf: 157]
Na miongoni mwake ni kwamba sura moja ya Qur'ani Tukufu iliteremshwa kwa nyakati tofauti na katika sehemu tofauti, lakini sura hiyo inasomwa kana kwamba iliteremka mara moja tu. Na ni kawaida kwamba watu wana uwezo tofauti tofauti, na njia zao hutofautiana wanapoandika vitabu katika nyakati tofauti tofauti.
Na miongoni mwake ni kwamba Mtume, rehema na amani zimshukie, alipewa Sunna na Mwenyezi Mungu kama alivyopewa Qur’ani. Amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika mimi nimepewa Kitabu, na mfano wake pamoja nacho." (Imesimuliwa na Abuu Daud 4604, Tirmidhi 2664, Ibn Abi Shaybah katika Al-Muswannaf 24816 na katika Al-Musnad 927, na Ahmad 17174).
Na miongoni mwake ni kuwa Qur’ani inajumuisha mambo ya kumuelekeza Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, juu ya kile kinachopaswa kuwa, au kile anachopaswa kufanya, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Lau isingelikuwa hukumu iliyokwishatangulia, kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ingeliwapata adhabu kubwa kwa vile mlivyochukua." [Al-Anfal: 68], Na maneno yake Mtukufu: "Ewe Nabii! Kwa nini unaharamisha alichokuhalalishia Mwenyezi Mungu? Unatafuta kuwaridhisha wake zako. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu." [At-Tahrim: 1], Na kauli yake Mtukufu: "Alikunja uso na akageuka * Kwa sababu alimjia kipofu! * Na nini kitakujulisha pengine yeye atatakasika? * Au atawaidhika, na mawaidha yamfae? * Ama ajionaye hana haja ya dini * Wewe ndio unamshugulikia? * Na si juu yako kama hakutakasika." ['Abasa: 1-7] Na kauli yake Mtukufu: "Na lau tusingekuweka imara, ungelikaribia kuwaelekea kidogo * Hapo basi bila ya shaka tungelikuonjesha adhabu maradufu ya uhai, na adhabu maradufu ya kifo. Kisha usingepata mtu wa kukunusuru nasi." [Al-Israa: 74, 75], Na lau kuwa Qur'ani hii ingekuwa inatoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, basi asingelijiandikia haya mwenyewe. Na pindi mfano wa maelekezo haya matukufu yalipotokea humo yakimwelekeza Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, yakaonyesha bila shaka yoyote kwamba haikutoka kwake, bali ni kutoka kwa Yule ajuaye zaidi, Mwenye hekima.
Kitabu cha Mitume na Manabii - amani iwe juu yao -
Muhtasari wa Kitabu
Na tunaamini kuwa kuamini Mitume, amani iwe juu yao, ni nguzo ya nne katika nguzo za kumuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Na tunaamini kwamba msingi wa wito wa Mitume, amani iwe juu yao, ni kumjua Mwenyezi Mungu Mtukufu, majina yake, sifa zake na vitendo vyake, na kwamba wote walitumilizwa na Tauhidi na wakalingania kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake na kuacha kumuabudu yeyote asiyekuwa yeye. Kwa hivyo, Manabii na Mitume ndio watu kamili zaidi katika tauhidi na imani, na wao ndio wajuzi zaidi katika viumbe kuhusu Muumba, Aliyetakasika na kutukuka, na yale anayopasa kufanyiwa, na yale yasiyowezekana kwake.
Na kila Nabii aliwalingania watu wake kwenye misingi miwili mikuu: Kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuamini Siku ya Mwisho na neema ambayo Mwenyezi Mungu aliwaandalia vipenzi wake huko na adhabu aliyowaandalia maadui zake.
Na tunaamini kwamba Mitume, amani iwe juu yao, wameafikiana katika misingi mikuu waliyokuwa wakiilingania. Wote walilingania kumwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake, na Mitume wake, na Siku ya Mwisho, na kuamini kadari; njema yake na mbaya yake. Nao wote walilingania ibada za kimsingi, kama vile swala, zaka, saumu, Hija, na maadili mema ya msingi, na wakakataza tabia mbaya zisizosifika. Kwa hivyo, Manabii rehema na amani ziwe juu yao walikubaliana juu ya misingi, ama sheria walizozilingania, hizo zilitofautiana katika hukumu zake na maelezo yake ya kina.
Na tunaamini kwamba ni lazima kuwaamini Manabii wote, amani iwe juu yao, na kuwasadikisha katika kila walichokieleza cha ghaibu na kuwatii katika yale waliyoamrisha, na kujiepusha na yale waliyokataza, kuwapenda, kuwaheshimu na kuwafuata, na kuwashuhudilia ya kwamba walifikisha ujumbe, na wakatekeleza amana, na wakawa waaminifu kwa Mwenyezi Mungu na wakawanasihi waja wake, na wakapigana Jihadi ajili ya Mwenyezi Mungu ukweli wa kumpigania. Na ni lazima kwa kila umma kufuata sheria ya mtume ambaye alitumwa kwao. Na ni lazima kwa umma huu - Umma wa Muhammad rehema na amani ziwe juu yake miongoni mwa majini na wanadamu, kufuata sheria ya wa mwisho wa Manabii na Mitume, Muhammad rehema na amani ziwe juu yake. Kwa sababu yeye alitumwa kwa viumbe wa aina mbili (majini na binadamu).
Na Manabii wote na Mitume, amani iwe juu yao, walikuja kuwatoa watu katika giza la ukafiri, ushirikina, na ujinga, hata kama walikuwa katika utukufu katika dunia, mamlaka, nguvu, mazao, na viwanda.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwatuma kama wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya Mitume.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alituma Mtume katika kila umma. Hivyo, yule tunayemjua kwa jina lake miongoni mwao, ni lazima tumwamini. Na yeyote ambaye hatujui jina lake miongoni mwao, tunamwamini kwa ujumla. Ni lazima juu ya kila Muislamu mwanaume na mwanamke kuwaamini Manabii na Mitume wote, amani iwe juu yao. Na mwenye kumkufuru Nabii mmoja, basi hakika amewakufuru Mitume wengineo wote, amani iwe juu yao.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu huwatuma Mitume wake kwa amtakaye katika waja wake kwa mujibu wa hekima yake, na hakuna wa kurekebisha hukumu yake. Yeye hufanya anachotaka na anachochagua.
Na tunaamini kuwa Unabii ni neema ya Mwenyezi Mungu na ni rehema ya Mola Mlezi ambayo humpa amtakaye katika waja wake. Kwani Mwenyezi Mungu huchagua Mitume miongoni mwa Malaika na miongoni mwa watu.
Na Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, wanatofautiana wao kwa wao, na walio bora wao zaidi ni wale wenye stahamala (uvumilivu) mkubwa, na walio bora zaidi katika hao wenye stahamala kubwa wale marafiki wandani wawili wa Mwenyezi Mungu: Ibrahim na Muhammad, amani iwe juu yao. Na Mtume, rehema na amani zimshukie, alikataza kuwapendelea Manabii na kuwafanya kuwa juu ya wengine ikiwa ni kwa njia ya ushabiki tu na dharau. Kama vile Mwenyezi Mungu alivyomchukua Ibrahim na Muhammad, amani iwe juu yao, kuwa marafiki wake wandani, basi pia alimchagua Musa, amani iwe juu yake, katika watu wote na akampa ujumbe wake na akamsemesha moja kwa moja. Na Nabii wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, alipata daraja kubwa zaidi ya urafiki wandani, na heshima kiasi kwamba Mola wake Mlezi alimsemesha kutokea nyuma ya pazia usiku aliopandishwa kwa Mwenyezi Mungu, kwa hivyo anakuwa Nabii wetu, rehema na amani zimshukie alipata urafiki wa ndani, na utukufu wa kusemeshwa.
Na tunaamini Manabii ndio wanadamu bora zaidi, na wala hakuna anayefikia daraja ya Nabii, si walii (kipenzi wa Mwenyezi Mungu) wala mtu mwingine yeyote, wala hairuhusiwi kumfadhilisha mwanadamu yeyote juu ya Mtume yeyote. Na unabii sio kitu cha kujitafutia, na wala mja hawezi kuupata kwa bidii ya utiifu, wala kwa kuitakasa nafsi yake, na kupambana, na kuusafisha moyo na kuuondolea uchafu, na kusafisha tabia.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakutuma isipokuwa wanaume tu, na tunajua kwamba Mitume na Manabii, amani iwe juu yao, ni wanadamu kama wanadamu wengine, na wao ndio wanadamu wakamilifu zaidi katika dini zao, akili zao na maadili yao, lakini wanateremshiwa ufunuo (wahyi), na wao wamehifadhiwa kutokana na kukosea katika yale wanayoyafikisha kuhusiana na amri ya Mwenyezi Mungu. Na ikiwa Nabii atajitahidi katika yale ambayo hayakuteremshwa kitu kuhusiana nayo lakini hakukipata kwa usahihi, basi Mwenyezi Mungu hakubaliani naye katika jitihada yake hiyo, bali humteremshia ufunuo (Wahyi) ili kumuweka sawa.
Na Mitume na Manabii, amani iwe juu yao, hawajimilikii manufaa yoyote wala madhara, licha ya kuwa wana hadhi ya juu, daraja za juu, na cheo chenye kusifiwa duniani na Akhera. Na ikiwa hawajimilikii manufaa yoyote wala madhara, basi hawawamilikii hayo watu wengine, kwa njia inayofaa zaidi. Na ikiwa hawajimilikii wenyewe wala wengine - katika uhai wao - manufaa wala madhara, basi kwa njia inayofaa zaidi hawammiliki mtu mwingine manufaa wala madhara baada ya kufa kwao.
Nao hawajui ghaibu isipokuwa kwa kiasi ambacho Mwenyezi Mungu amewajulisha na kuwapa idhini ya kufanya hivyo.
Na Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, wanamuabudu Mwenyezi Mungu kwa hofu na matumaini, na wanatafuta njia ya kumwendea, na wanajiweka karibu naye Yeye aliyetakasika na kutukuka.
Na tunaamini kwamba Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, wanakabiliwa na balaa na magonjwa ambayo wanadamu wanakabiliwa nayo, na pia wanakabiliwa na huzuni na kifo, na kwamba wana wake na dhuria (watoto), na kuwa wanakula chakula na wanatembea katika masoko, na tunajua kwamba Masihi, amani iwe juu yake, alinyanyuliwa na Mwenyezi Mungu ilhali yu hai wakati kaumu (watu) wake walipotaka kumuua.
Na tunashuhudia ya kwamba wao waliwanasihi viumbe, na wakatimiza amana zao, na wakafikisha jumbe za Mola wao Mlezi, na wala haiwadhuru kuwa wafuasi wao hawakuwaitikia, wala kuwa wakuu wa kaumu (Jamii) zao waliwafanyia kiburi.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alimpa kila Nabii ishara na hoja ambazo wanadamu wanaamini mfano wa hizo.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakumtuma Nabii yeyote, isipokuwa alikuwa na ishara inayoonyesha ukweli wake, sawa iwe tunazijua au hatuzijui. Na Mwenyezi Mungu alitutajia baadhi yake katika Qur'ani Tukufu. Na tunajua pia kuwa kuna ishara nyingi ambazo Mwenyezi Mungu aliwasaidia kwazo Mitume wake waliotangulia. Na Mwenyezi Mungu hakuzitaja kwetu. Lakini wakati mwingine Mwenyezi Mungu huzitaja ishara hizo zilizo wazi, na wakati mwingine hutaja hoja. Na tunajua kuwa ishara na hoja ambazo Mwenyezi Mungu aliwasaidia kwazo Mitume wake na Manabii wake, amani iwe juu yao, ni nyingi sana.
Na ushahidi mkubwa zaidi unaoonyesha ukweli wao ni kile wanachokilingania kama vile kumpwekesha Mwenyezi Mungu ambako ni jambo lililothibiti katika maumbile ya asili ya mwanadamu, ambako akili zote zinashuhudia kuwa ni jambo zuri. Na pia miongoni mwa ushahidi ni yale waliyokuja nayo ya elimu yenye manufaa, matendo mema, uongofu, na dini ya haki na mizani. Na pia ushahidi wa Mwenyezi Mungu kwa Mitume wake kwamba wao wako katika haki, na kwamba yale waliyokuja nayo ni haki. Na miongoni mwa ishara zao kubwa zaidi ni ufunuo (wahyi) unaowashukia kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na ufunuo (wahyi) mkubwa zaidi ni Qur'ani Tukufu, ambayo ni ishara ya Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie. Na hakuna mwanadamu anayeweza kuja na mfano wa ufunuo huu, kwa sababu ni maneno ya Mwenyezi Mungu na ufunuo wake, na kwa sababu una habari za ghaibu ndani yake, na kwa sababu una uongofu, nuru, rehema, na hekima.
Na miongoni mwa mambo ambayo Mwenyezi Mungu aliwasaidia kwayo Mitume wake, amani iwe juu yao, ni hoja za kiakili ambazo Mwenyezi Mungu huwapa, ambazo huwashinda makafiri na kuondoa batili zao.
Na miongoni mwa ishara zao kubwa zaidi ni kueleza kwao ghaibu ambayo Mwenyezi Mungu amewaruhusu kuwaeleza watu wengine. Na miongoni mwake ni kuwaokoa Manabii waliotangulia, amani iwe juu yao, na kuwaokoa wafuasi wao kutokana na njama za maadui zao, kuwaangamiza wakaidi wenye kiburi, na Mwenyezi Mungu kuwakumbusha wale wale wanaolinganiwa yale aliyowafanyia wale waliotangulia, na kuwa Sunna (utaratibu) wa Mwenyezi utaendelea. Na miongoni mwake ni ukamilifu wa sifa zao, tabia njema, matendo yao, mwenendo wao, na ukweli wa maneno yao, ambayo huwazuia kusema uongo. Na miongoni mwake ni simulizi nyingi za watu wengi zaidi katika kusimulia ishara za Manabii, na yale waliyokuja nayo ya elimu na uongofu, na dini ya haki, ushahidi ambao haiwezekani watu wote wakubaliane kusimulia uongo. Na miongoni mwake ni kuwa hawaombi malipo juu ya utume wao, wala hawatafuti ufalme. Na miongoni mwake ni kuwa hakuna anayeukashifu unabii wa Manabii hawa isipokuwa mtu mjinga ambaye haangalii yale waliyokuja nayo ya dini, elimu, na uongofu, au mtu mkaidi mwenye kiburi.
Na katika ishara zao kubwa zaidi ni hoja za kihisia zinazoonekana kwa macho, na akili zinajisalimisha kwazo, kama vile kuzama kwa watu wa Nuhu, ngamia wa Swaleh, na changamoto ya Hud kuwa watu wake wote wapange njama dhidi yake, na kuokoka kwa Ibrahim kutoka motoni, na ishara za Musa, ambazo miongoni mwake ni fimbo, nzige, chawa, vyura, damu, mafuriko, na kuzama kwa Firauni na watu wake, na miujiza ya Daudi, amani iwe juu yake, kama vile milima kumtakasa Mwenyezi Mungu na kulainisha chuma, na ishara za Sulaiman, amani iwe juu yake, kama vile kumtiishia upepo na majini, na kujua kwake mazungumzo ya ndege, na ishara za Masihi, amani iwe juu yake, kama vile kuponya wakoma, na vipofu wa tangu kuzaliwa na vipofu wa kawaida, na kuwafufua wafu, na kuwa alikuwa akiunda kwa udongo kama sura ya ndege. Kisha anampuliza na anakuwa ndege kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na ishara za Nabii wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, nazo ni nyingi hazihesabiki isipokuwa kwa tabu kubwa mno, kama vile kupasua mwezi, kusafiri usiku kisha kupandishwa mbinguni, na kufanya chakula kuwa kingi, na kuwaongelesha wanyama, na changarawe kumtakasa Mwenyezi Mungu, na kulia kwa shina la mtende, na Mwenyezi Mungu kumnusuru dhidi ya maadui zake.
Na miongoni mwa ishara za manabii ni hali ya Nabii anayelingania kwenye haki. Kwa maana watu hutofautisha kati ya mwenye kulingania kwenye haki kwa maneno yake, na mlinganiaji muongo katika maneno yake, na ishara nyinginezo.
Na ishara zote za Manabii zilikwishatoweka isipokuwa Qur'ani Tukufu na Sunna ya Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, kwa sababu viwili hivyo ni wahyi ambao Mwenyezi Mungu alichukua jukumu la kuuhifadhi, na ndani yake umo ushahidi mkubwa zaidi na hoja mbalimbali juu ya ukweli wa ujumbe wake, na ukweli wa Mtume, rehema na amani zimshukie.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu anawaunga mkono Mitume wake, amani iwe juu yao, kwa yale yanayohitajiwa na hekima yake kwa ishara mbali mbali na hoja za kiulimwengu na kisheria. Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu humuongoa amtakaye kwa fadhila zake, na humpoteza amtakaye kwa uadilifu wake, lakini mkaidi hazimzidishii ishara hizi isipokuwa ukaidi na kutakabari.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu angetaka, angewaongoa watu wote.
Na tunaamini kwamba ushahidi wa Manabii, na ishara walizoleta na uthibitisho ambao Mwenyezi Mungu aliwapa ni jambo lisilowezekana kwa mtu yeyote anayedai unabii, au hata mchawi, au muongo. Kwa sababu Mwenyezi Mungu alishapitisha kuwa mtu wa batili hawezi kuungwa mkono kwa ushahidi sahihi, na wala muongo hawezi kusadikishwa kwa uthibitisho wa kweli. Kwa sababu Yeye ndiye Mwenye hekima katika sheria yake na amri yake. Na hekima ya Mwenyezi Mungu na desturi zake zinazoendelea zinazuia hilo.
Na tunaamini kuwa Nabii wetu Muhammad bin Abdullah ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote, na ndiye mwisho wa Manabii na Mitume, na ndiye bwana wa wanadamu, naye ni rafiki mwandani wa Mola Mlezi wa walimwengu wote.
Na tunajua kwamba alipewa ishara ambazo hakupewa yeyote mfano wake miongoni mwa Mitume, amani iwe juu yao. Na ishara yake kubwa zaidi ni Qur'ani Tukufu. Na cha kwanza alichoanzishwa nacho Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake katika ufunuo, ni ndozo nzuri usingizini, alikuwa haoti ndoto yoyote isipokuwa inatokea wazi kama kupambazuka kwa Alfajiri. Na jambo la kwanza lililoteremshwa kwake ni mwanzo wa “Surat Al-Alaq”. Kisha baadaye akateremshiwa “Al-Muddaththir”. Kisha ufunuo ukashika kasi na ukafuatana. Na akakaa Makka kwa muda wa miaka kumi na tatu akilingania tauhidi, na akakaa Madina kwa muda wa miaka kumi akifafanua sheria za Mwenyezi Mungu, na akiilingania dini yake, na kupambana katika njia yake, mpaka Mwenyezi Mungu alipomfisha akiwa na umri wa miaka sitini na tatu (63). Rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, ninamfidia kwa baba na mama yangu.
Na tunajua kuwa katika ishara kubwa zaidi baada ya Qur'ani tukufu ni ile safari ya usiku kutoka Makka kisha kupandishwa mbinguni. Na miongoni mwa ishara zake, Mwenyezi Mungu amfikishie rehema na amani ni kupasuka kwa mwezi. Na pia Mwenyezi Mungu alimpa sifa nyingi mahususi kwake, ambazo wanazuoni walizitaja mara katika uandishi wao na mara nyingine waliziandika katika vitabu vya kujitegemea.
Na tunaamini kwamba ni wajibu kwa kila jini na mwanadamu amwamini, amsadikishe katika yale aliyoyaeleza, na amtii katika yale aliyoamrisha.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu hapaswi kuabudiwa isipokuwa kwa kile alichokiweka katika sheria. Na Mola wa Haki ilitahadharisha juu ya kuasi amri ya Mtume, rehema na amani zimshukie, na akaamrisha kumcha na kumpenda, na kuwa Mtume rehema na amani zimshukie ni lazima awe ndiye kipenzi zaidi kwa mtu kuliko nafsi yake mwenyewe, na baba yake, na mtoto wake na watu wote.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amefungamanisha utajo wa Nabii wetu Muhammad rehema na amani ziwe juu yake pamoja na utajo wake Yeye aliyetakasika, katika shahada mbili na katika adhana. Na utajo wake yeye rehema na amani zimshukie ametajwa sana katika vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyotangulia, na katika Qur’ani tukufu, na maimamu wa Uislamu wameandika vitabu mbalimbali vinavyoelezea Sunna zake, maisha yake, sifa zake, maadili yake, na vita vyake.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alimtuma kwa viumbe wote, kwani yeye ndiye Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa viumbe viwili vizito: Majini na watu. Na Mwenyezi Mungu alimpelekea kundi la majini limsikilize, ili wawe waonyaji wa wale walio nyuma yao, na ili hoja isimame juu yao. Na Mwenyezi Mungu alichukua agano kwa kila Nabii na Mtume, amani iwe juu yao: Ikiwa Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie atatumwa hali ya kuwa yupo hai, basi hakika atamwamini.
Na tunaamini kuwa Manabii waliwabashiria watu wao kuhusu Mtume Muhammad rehema na amani zimshukie, zikaja sifa zake na sifa za maswahaba zake, Mwenyezi Mungu awawie radhi, katika Taurati na Injili. Na Masihi amani iwe juu yake hasa aliwabashiria Wana wa Israeli juu yake, na Wana wa Israeli walikuwa wakimjua kama wanavyowajua watoto wao. Na katika ishara za unabii wake rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie zilizokuwa zikijulikana kwa Watu wa Kitabu (Mayahudi na Wakristo) ni muhuri wa unabii uliokuwa kwenye bega lake tukufu.
Na tunaamini kuwa ujumbe wake unaenea kwa watu wote, na ndiyo maana aliwaandikia barua wafalme na wakuu akiwalingania kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuuamini ujumbe wake yeye rehema na amani zimshukie na wamsadikishe.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alimkunjia Mtume wetu ardhi, akaona hadi pale ambapo umiliki wa watu wake utafikia.
Na miongoni mwa ushahidi wa kuwa ujumbe wake, yeye rehema na amani ziwe juu yake, ni kwa viumbe wote kwa ujumla ni kwamba, Wakristo wa Najran walikataa kuhusika katika kuapizana, na wakakubali kumpa jizya (kodi ya ulinzi) huku wakiwa wamenyenyekea; kwa sababu walijua kuwa yeye ni Nabii.
Na miongoni mwa ushahidi wa kwamba ujumbe wake, yeye rehema na amani ziwe juu yake, ni kwa viumbe wote kwa ujumla ni kusilimu kwa Makasisi wengi wa Kiyahudi na watawa wa Kikristo, bali maelfu na maelfu ya Watu wa Kitabu. Na miongoni mwa ushahidi wa ujumla wa ujumbe wake, ni kuwa alipigana vita na Warumi, na akawaamuru maswahaba wake kupigana vita dhidi ya Waajemi na Warumi baada yake.
Na miongoni mwa ushahidi unaoonyesha ujumla wa ujumbe wake, rehema na amani ziwe juu yake, ni kuwa alimuahidi Suraqa (bin Maliki) kwamba atavaa bangili za Kaisari (Mfalme wa Roma), na kweli akazivaa katika utawala wa Omari, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.
Na tunajua kwa yakini kabisa kuwa hekima ya Mwenyezi Mungu ilipelekea kumuongoa amtakaye kwa fadhila zake, na ampoteze amtakaye kwa uadilifu wake, kama vile hekima yake ilivyohitaji kwamba kila Nabii awe na adui, na kwamba kati ya maadui hawa pawepo wasia juu ya batili, na kuafikiana katika maneno yao. Kwa hivyo maneno ya wakuu katika kila umma yalikuwa yanafanana: Wakati mmoja walikuwa wakisema: Huyu ni mchawi au kuhani au muongo. Na wakati mwingine wanakataa kwamba hakuwajia na ushahidi wowote, na wakati mwingine wanadai kwamba anamzulia uongo Mwenyezi Mungu. Na wakati mwingine wanamuelezea kuwa ni kichaa, Mwenyezi Mungu apishe mbali hilo kwa Mitume wake, amani iwe juu yao - kwa maana wao ndio watu wenye akili kamilifu zaidi na nyoyo safi kabisa. Na wakati mwingine wanaona kwamba ni kikubwa mno kile anachowaitia cha kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na wakati mwingine wanaukataa wito wa Nabii kwa sababu ni binadamu kama wao, na wakati mwingine wanawaomba vitu ambavyo haviko katika uwezo wa kibinadam, lakini hicho ni kiburi na ukaidi. Walimuomba Mtume wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, atimbue chemchemi kutoka ardhini, au awe na kitalu, au aiangushe mbingu vipande vipande, au awaletee Mwenyezi Mungu na Malaika, au Nabii awe na nyumba ya mapambo, au apae mbinguni, na awateremshie kitabu. Na wakati mwingine wanamuomba Mtume awaletee yale anayowaahidi, na wakati mwingine wanaizuilia njia ya Mwenyezi Mungu na kuwaambia wafuasi wao: Msiisikilize Qur'ani hii, na timueni zogo. Wakati mwingine wanakabiliana na Mtume kwa kumuita muongo, au wanamshutumu Mtume wa Mungu amani iwe juu yake, kwamba anafundishwa tu na mwanadamu, na sio yule anayemjia kumletea kama wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na wakati mwingine wanamkadhibisha Mtume rehema na amani ziwe juu yake, au wanamtuhumu kwamba anafundishwa tu na mwanadamu, na hayo yanayomjia sio ufunuo kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Na wanaweza pia kumuacha Mtume na kutomfuata ati kwa sababu wale waliomfuata ni wanyonge. Na wakati mwingine wanawadhihaki na kuwafanyia kejeli Mitume. Na wakati mwingine wanamhadaa Mtume, na wanatamani ipo siku atajishusha chini akubaliane nao au kuwategemea. Na wakati mwingine mkaidi huyo anakosoa kwa kile ambacho anajuwa mwenyewe kwamba ni muongo katika hicho anachokisema, kama vile Firauni alivyomkosoa Musa kwa kusema kwamba yeye ni kafiri.
Na wakati mwingine wakuu wanamtishia Mtume kwamba watamfukuza kutoka katika nchi hiyo. Na Makafiri wa Kikuraishi walimzingira Mtume wetu Muhammad rehema na amani ziwe juu yake, na wale waliokuwa pamoja naye na Bani Hashim katika bonde kwa muda wa miaka mitatu, na wakamfukuza kutoka kwenye mji wake yeye, rehema na amani ziwe juu yake. Na watu wa Ibrahim, amani iwe juu yake, walijaribu kumteketeza kwa moto, lakini Mwenyezi Mungu akamuokoa. Nao Wana wa Israeli walijaribu kuwaua Manabii, na hata wakawaua wale walioweza kuwauwa miongoni mwao.
Huu ndio mwenendo wa wale wanaotakabari juu ya Mitume, na hii ndiyo desturi inayoendelea ambayo wakuu hawa wanaifuata na kuwafanyia wale wanaofanya mambo kutengemaa katika kila umma.
Mlango wa kuwaamini Mitume, rehema na amani ziwe juu yao
Kuwaamini Mitume, amani iwe juu yao, ni nguzo ya nne katika nguzo za imani, amesema Mola Mtukufu: "Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola Mlezi wake, na Waumini wote wamemuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake na Mitume wake; hatutofautishi baina ya yeyote katika Mitume wake." [Al-Baqara: 285] Na amesema Mola wa Haki, aliyetakasika na kutukuka: "Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi. Bali wema ni wa anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii." [Al-Baqara: 177] Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa amekaa nje kwa ajili ya watu, kisha mwanaume mmoja akamjia, na akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nini Imani?" Akasema: “Ni kwamba umwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Kitabu chake, na kukutana naye, na Mitume wake, na kuamini ufufuo wa mwisho.” (Imepokelewa na Bukhari 4777, Muslim 9, na Ibn Majah 64).
Na tunaamini kuwa msingi wa wito wa Mitume, amani iwe juu yao, ni kumjua Mwenyezi Mungu Mtukufu, majina yake, sifa zake na vitendo vyake, na kwamba wote walitumwa na Tauhidi na wakalingania kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake na kuacha kumuabudu yeyote asiyekuwa yeye, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia ya kwamba hapana mungu isipo kuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu." [Al-Anbiya: 25], Na kila Nabii aliwaambia watu wake: "Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna mungu isipokuwa Yeye. Basi je, hamumchi?" [Al-A'raf: 65]. Kwa hivyo, Manabii na Mitume ndio walio kamilika zaidi ya watu wote katika kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kumuamini, nao ndio viumbe wanaomjua Muumba, aliyetakasika na kutukuka na kile anachostahili, na yale anayopasa kufanyiwa, na yale yasiyowezekana kwake.
Na kila Nabii aliwalingania watu wake kwenye misingi miwili mikuu: Kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuamini Siku ya mwisho na neema ambayo Mwenyezi Mungu aliwaandalia vipenzi wake huko na adhabu aliyowaandalia maadui zake, amesema Mtukufu: "Hakika, tulimtuma Nuhu kwa kaumu yake, naye akasema: Enyi kaumu yangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu isipokuwa Yeye. Hakika mimi ninawahofia adhabu ya Siku iliyo kuu." [Al-A'raf: 59], Na amesema Mtukufu: "Na kwa watu wa Madiana tuliwatumia ndugu yao Shuaib. Akasema: Enyi watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu isipokuwa Yeye, wala msipunguze vipimo na mizani. Mimi ninawaona mmo katika hali njema, nami ninawahofia adhabu ya Siku kubwa hiyo itakayowazunguka." [Hud: 84], Na amesema Mwenyezi Mungu, aliyetakasika na kutukuka: "Na mtaje ndugu wa kina 'Adi, alipowaonya watu wake kwenye vilima vya mchanga. Na kwa yakini waonyaji wengi walitokea kabla yake na baada yake kuwaambia: Msimuabudu isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ninawahofia isijewapata adhabu ya siku iliyo kuu." [Al-Ahqaf: 21].
Na tunaamini kuwa Mitume, amani iwe juu yao, waliafikiana katika misingi mikuu waliyokuwa wakiilingania. Wote walilingania kumwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake, na Mitume wake, na Siku ya Mwisho, na kuamini kadari; njema yake na mbaya yake. Nao wote walilingania ibada kuu, kama vile swala, zaka, saumu, Hija, na msingi wa maadili, na wakakataza misingi ya tabia mbaya zisizopendeza, amesema Mtukufu: "Amewawekea sheria katika Dini yale aliyomuusia Nuhu na tuliyokufunulia wewe, na tuliyowausia Ibrahim na Musa na Isa, kwamba shikeni Dini wala msifarikiane kwayo." [Ash-Shura: 13]. Kwa hivyo, Manabii rehema na amani ziwe juu yao walikubaliana juu ya misingi, ama sheria walizozilingania, hizo zilitofautiana katika hukumu zake na maelezo yake ya kina, amesema Mola Mtukufu: "Na tumekuteremshia wewe, kwa haki, Kitabu hichi kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake katika Vitabu na kuyalinda. Basi hukumu baina yao kwa aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, wala usifuate matamanio yao ukaacha Haki iliyokujia. Kila mmoja katika nyinyi tumemuwekea sheria yake na njia yake." [Al-Ma'ida: 48].
Na tunaamini kwamba ni lazima kuwaamini Manabii wote, amani iwe juu yao, na kuwasadikisha katika kila walichokieleza cha ghaibu na kuwatii katika yale waliyoyaamrisha, na kujiepusha na yale waliyoyakataza, na kuwapenda, kuwaheshimu na kuwafuata, na kuwashuhudilia ya kwamba walifikisha ujumbe, na wakatekeleza amana, na wakawa waaminifu kwa Mwenyezi Mungu na wakawanasihi waja wake, na wakapigana Jihadi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu ukweli wa kumpigania. Na ni lazima kwa kila umma kufuata sheria ya mtume ambaye alitumwa kwao. Na ni lazima kwa umma huu - Umma wa Muhammad rehema na amani ziwe juu yake miongoni mwa majini na wanadamu, kufuata sheria ya wa mwisho wa Manabii na Mitume, Muhammad rehema na amani ziwe juu yake. Kwa sababu yeye alitumwa juu ya wazito wawili (majini na binadamu).
Na Manabii wote na Mitume, amani iwe juu yao, walikuja kuwatoa watu katika giza la ukafiri, ushirikina, na ujinga, hata kama walikuwa katika utukufu katika dunia, mamlaka, nguvu, mazao, na viwanda, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusiana na Musa, amani iwe juu yake: "Na hakika tulimtuma Musa pamoja na miujiza yetu, tukamwambia: Watoe watu wako kwenye giza uwapeleke kwenye mwangaza. Na uwakumbushe siku za Mwenyezi Mungu. Hakika katika hayo zipo ishara kwa kila mwenye kusubiri sana, akashukuru mno." [Ibrahim: 5], Na amesema Mtukufu: "Je, mnajenga juu ya kila mnyanyuko kumbusho la kufanyia upuuzi? * Na mnajenga majengo ya fahari kama kwamba mtaishi milele! * Na mnapotumia nguvu, mnatumia nguvu kwa ujabari. * [Ash-Shu'ara: 128-130] Na akasema Mtukufu: “Je, hawajatembea katika ardhi wakaona ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Nao walikuwa na nguvu zaidi kuliko wao, na wakaitimbua ardhi na wakaistawisha zaidi kuliko walivyoistawisha wao. Na Mitume wao wakawajia na ushahidi ulio wazi. Basi hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwadhulumu, lakini walikuwa wakijidhulumu nafsi zao wenyewe.” [Ar-Rum: 9].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwatuma kama wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya Mitume, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mitume hao ni wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya kuletewa Mitume. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima." [An-Nisa: 165].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alituma Mtume katika kila umma, amesema Mtukufu: “Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Taghut (Shetani na kila kinachoabudiwa kinyume na asiyekuwa Mwenyezi Mungu).” [An-Nahl: 36]. Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Wana wa Israeli walikuwa wakijiwa na Manabii mmoja baada ya mwingine. Kila alipokufa Nabii, Nabii mwingine alifuata baada yake. Na hakika hakuna nabii yeyote baada yangu." (Imepokelewa na Bukhari 3455, Muslim 1842, na Ibn Majah 2871). Bali Mwenyezi Mungu Mtukufu alitueleza kwamba alituma katika kijiji miongoni mwa vijiji vyao Manabii watatu katika wakati mmoja, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Tulipowatumia wawili, wakawakanusha. Basi tukawazidishia nguvu kwa mwingine wa tatu. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwenu." [Yasin: 14].
Kwa hivyo, yule tunayemjua kwa jina lake miongoni mwao, ni lazima tumwamini. Na yeyote ambaye hatujui jina lake miongoni mwao, tunamwamini kwa ujumla. Hivyo, ni lazima juu ya kila Muislamu mwanaume na mwanamke kuwaamini Manabii na Mitume wote, amani iwe juu yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mitume tuliokwishakukuhadithia kabla yake, na Mitume wengine hatukukuhadithia. Na Mwenyezi Mungu alinena na Musa kwa maneno." [An-Nisa: 164], Na akasema Mtukufu: "Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola Mlezi wake, na Waumini vile vile. Wote wamemuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake na Mitume wake. Hatutafautishi baina ya yeyote katika Mitume wake, na (Waumini) husema: Tumesikia na tumetii. Tunakutaka maghfira (msamaha) Mola Mlezi wetu! Na marejeo ni kwako." [Al-Baqara: 285] Na akasema Mtukufu: “Sema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu, na yale tuliyoteremshiwa sisi, na yale aliyoteremshiwa Ibrahim, na Ismail, na Is-haaka na Yaakub na wajukuu zao, na yale aliyopewa Musa na Isa na Manabii wengine kutoka kwa Mola wao Mlezi. Hatubagui baina yao hata mmoja, na sisi ni wenye kusilimu kwake." [Al-Imran: 84].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu hutuma Mitume wake kwa amtakaye miongoni mwa waja wake kwa mujibu wa matakwa ya hekima yake, amesema Mola Mtukufu: "Na tungelitaka, tungelipeleka katika kila mji Muonyaji." [Al-Furqan: 51], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kisha tukawatuma Mitume wetu, mmoja baada ya mmoja. Kila umma alipowafikia Mtume wao, walimkadhibisha. Kwa hivyo, tukawafuatanisha hawa baada ya hawa, na tukawafanya ni hadithi za kusimuliwa. Wakapotelea mbali watu wasioamini." [Al-Mu'minun: 44], Hivyo, hakuna wa kurekebisha hukumu yake. Yeye hufanya anachotaka na anachochagua, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mola wako Mlezi huumba na huteuwa atakavyo. Viumbe hawana hiari. Mwenyezi Mungu ametakasika na ametukuka mbali na hao wanaowashirikisha naye." [Al-Qasas: 68],
Na mwenye kumkufuru Nabii mmoja, basi hakika amewakufuru Manabii wengineo wote, amani iwe juu yao, na ndio maana alisema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kaumu ya Nuhu waliwakadhibisha Mitume." [Ash-Shu'ara: 105]. Na aya hii ni kama maneno yake Mtukufu: "Wote hao waliwakadhibisha Mitume, kwa hivyo onyo likathibitika juu yao." [Qaf: 14].
Na tunaamini kuwa Unabii ni neema ya Mwenyezi Mungu na ni rehema ya Mola Mlezi ambayo humpa amtakaye katika waja wake. Kwani Mwenyezi Mungu huchagua Mitume miongoni mwa Malaika na miongoni mwa watu, amesema Mtukufu: "Mwenyezi Mungu huteua Wajumbe miongoni mwa Malaika na miongoni mwa watu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona." [Al-Hajj: 75], Na Mola Mtukufu alisema: "Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi kuliko wote kujua wapi anaweka ujumbe wake." [Al-An'am: 124]. Na unabii sio kitu cha kujitafutia, na wala mja hawezi kuupata kwa bidii wala kwa utiifu, wala kwa kuitakasa nafsi yake, na kupambana, na kuusafisha moyo na kuuondolea uchafu, na kusafisha tabia.
Na tunaamini kwamba Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, wamezidiana ubora wao kwa wao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mitume hao tumewaboresha baadhi yao juu ya wengineo. Katika wao wapo ambao Mwenyezi Mungu alisema nao, na wengine akawapandisha vyeo. Na tukampa Isa mwana wa Mariyam hoja zilizo wazi, na tukamtia nguvu kwa Roho mtakatifu." [Al-Baqara: 253]. Na kwamba Manabii bora zaidi ni wale wenye uhimili (Uvumilivu) mkubwa, nao ni wale waliotajwa katika maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tulipochukua ahadi kwa Manabii na kwako wewe, na Nuhu na Ibrahim na Isa mwana wa Mariamu, na tulichukua kwao ahadi ngumu." [Al-Ahzab: 7], Na Mwenyezi Mungu aliwaashiria katika kauli yake Mtukufu: "Basi subiri, kama walivyosubiri Mitume wenye kuhimili (uvumilivu) mkubwa." [Al-Ahqaf: 35]. Na wabora wa Mitume wenye stahamala kubwa ni wale marafiki wandani wawili wa Mwenyezi Mungu: Ibrahim na Muhammad amani iwe juu yao. Mola Mtukufu amesema: "Na ni nani aliye bora zaidi kwa dini kuliko yule aliyeusilimisha uso wake kwa Mwenyezi Mungu, naye akawa mwema, na akafuata mila ya Ibrahim muongofu? Na Mwenyezi Mungu alimfanya Ibrahim kuwa ni rafiki mwandani." [An-Nisaa: 125]. Na imesimuliwa kutoka kwa Jundab, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisema: Nilimsikia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, siku tano kabla ya kufa kwake akisema: "Hakika mimi ninajiweka mbali kwa Mwenyezi Mungu na kumfanya yeyote miongoni mwenu kuwa ndiye rafiki mwandani wangu. Kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu alinifanya mimi kuwa rafiki mwandani wake kama vile alivyomfanya Ibrahim kuwa rafiki mwanani wake." (Imepokelewa na Muslim 532).
Na tunashuhudia kuwa Mtume wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, ndiye mbora wa Mitume na Manabii, anasema rehema na amani ziwe juu yake: "Mimi ndiye bwana wa wana wa Adam Siku ya Kiyama." (Imepokelewa na Muslim 2278 na Abu Daud 4673).
Na alikataza Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwapendelea Manabii juu ya wengine ikiwa ni kwa njia ya ushabiki tu na dharau. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Watu wawili, Muislamu na Myahudi, walitukanana. Muislamu akasema: "Ninaapa kwa Yule ambaye alimteua Muhammad juu ya walimwengu!" Na Myahudi akasema: "Ninaapa kwa Yule ambaye alimteua Musa juu ya walimwengu!" Hivyo, Muislam akainua mkono wake na akampiga yule Myahudi usoni. Yule Myahudi akamuendea Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akamwambia kuhusu kilichotokea kati yake na yule Muislam. Basi Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akamuita Muislam huyo na akamuuliza juu ya hilo, akamjibu kuhusu tukio hilo. Basi Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Msiniboreshe juu ya Musa, kwa sababu Siku ya Kiyama, watu wote watazimia, na mimi nitazimia pamoja nao, lakini nitakuwa wa kwanza wao kuzindukana, na ghafla nitamuona Musa amesimama hali ya kuwa amekamata kwa nguvu upande wa 'Arshi (ya Mwenyezi Mungu). Kwa hivyo sitaweza kujua ikiwa yeye pia alikuwa miongoni mwa wale waliozimia kisha akazinduka kabla yangu, au alikuwa miongoni mwa wale ambao Mwenyezi Mungu aliwaepusha (na kuzimia huko)." (Imepokelewa na Bukhari 2411, Muslim 2373, Abu Daud 4671, Tirmidhi 3245, na Ibn Majah 4274). Na katika maneno mengine: "Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akakasirika mpaka hasira ikaonekana usoni mwake, kisha akasema: "Msiniboreshe kati ya Manabii wa Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Muslim 2373).
Na kama vile Mwenyezi Mungu alivyomchukua Ibrahim na Muhammad, amani iwe juu yao, kuwa marafiki wake wandani, basi pia alimchagua Musa, amani iwe juu yake, juu ya watu na akampa ujumbe wake na akamuongelesha moja kwa moja. Na Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, alipata daraja kubwa zaidi ya urafiki wandani, na heshima kiasi kwamba Mola wake Mlezi alimuongelesha kutokea nyuma ya pazia usiku aliopandishwa mbinguni, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi (Mwenyezi Mungu) akamfunulia mja wake kile alichomfunulia." [An-Najm: 10], Basi Mtume wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, anakuwa kakusanya kati ya utukufu wa kufanywa kuwa rafiki mwandani na kuongeleshwa moja kwa moja na Mwenyezi Mungu.
Na tunaamini Manabii ndio wanadamu bora zaidi, na wala hakuna anayefikia daraja ya Nabii, si walii (kipenzi wa Mwenyezi Mungu) wala mwingine yeyote, wala hairuhusiwi kumfadhilisha mwanadamu yeyote juu ya Mtume yeyote. Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Haifai kwa yeyote kuwa bora kuliko Yunus bin Matta." (Imepokelewa na Bukhari 4804).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu hakutuma isipokuwa wanaume tu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kabla yako hatukuwatuma isipokuwa watu wanaume tuliowapa ufunuo (wahyi)." [Al-Anbiya: 7].
Na tunajua kwamba Mitume na Manabii, amani iwe juu yao, ndio watu wa hadhi ya juu zaidi miongoni mwa viumbe wote, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu huteuwa Wajumbe miongoni mwa Malaika na miongoni mwa watu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona." [Al-Hajj: 75]. Nao ndio wanadamu wakamilifu zaidi katika dini zao, akili zao na maadili yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Hakika, mimi ni mwanadamu tu kama nyinyi. Ninaletewa ufunuo (Wahyi)." [Al-Kahf: 110]. Kwa hivyo, wao ni wanadamu tu kama wanadamu wengineo, lakini wamehifadhiwa kutokana na kukosea katika yale wanayoyafikisha kuhusiana na amri ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema kuhusiana na Nabii wake na rafiki wake mwandani, Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake: "Wala hatamki kwa matamanio. * Hayakuwa haya isipokuwa ni ufunuo uliofunuliwa * Amemfundisha mwenye nguvu nyingi." [An-Najm: 3-5].
Na ikiwa Nabii atajitahidi katika yale ambayo hakuteremshiwa kitu kuhusiana nayo lakini hakuyapata kwa usahihi, basi Mwenyezi Mungu hakubaliani naye katika jitihada yake hiyo, bali humteremshia ufunuo (Wahyi) ili kumuweka sawa, kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Haimfalii Nabii yeyote kuwa na mateka mpaka awe ameshinda barabara katika nchi. Mnataka vitu vya dunia, na Mwenyezi Mungu anataka Akhera. Na Mwenyezi Mungu ni Mtukufu Mwenye nguvu Mwenye hekima." [Al-Anfal: 67]. Na kauli yake, Mwenye sifa tukufu: "Ewe Nabii! Kwa nini unaharamisha kile alichokuhalalishia Mwenyezi Mungu? Unatafuta kuwaridhisha wake zako. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu." [At-Tahrim: 1].
Pamoja nakuwa wana hadhi hii ya juu, na daraja za juu, na cheo chenye kusifiwa duniani na Akhera, hawajimilikii manufaa yoyote wala madhara, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Sijimilikii nafsi yangu shari wala heri isipokuwa apendavyo Mwenyezi Mungu. Kila umma una muda wao waliowekewa. Na ukifika muda wao, hawakawii hata saa moja wala hawatangulii." [Yunus: 49].
Na ikiwa hawajimilikii wenyewe manufaa wala madhara, basi kwa mtu mwingine ndio aula (bora) zaidi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu Nabii wake na rafiki yake mwandani, Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake: "Wewe huna lako jambo katika haya, ima atawahurumia au atawaadhibu, kwani hakika wao ni madhalimu." [Al-Imran: 128], Na akasema kuhusiana na Masihi, amani iwe juu yake: "Sema: Ni nani mwenye kumiliki chochote mbele ya Mwenyezi Mungu ikiwa Yeye angetaka kumuangamiza Masihi mwana wa Maryamu, na mama yake, na wote waliomo katika ardhi?" [Al-Ma'ida: 17].
Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema kumwambia shangazi yake, na binti yake Fatima, Mwenyezi Mungu awe radhi naye: "Enyi kundi la Makuraishi - au neno linalofanana na hilo -, jikomboeni wenyewe, mimi sitowasaidia kwa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Enyi Banu Abdi Manafi, mimi sitawasaidia kwa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Ewe 'Abbas bin Abdil-Muttwalib, mimi sitakusaidia kwa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Ewe Safia, shangazi yake Mtume wa Mwenyezi Mungu, mimi sitakusaidia kwa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Na ewe Fatima binti ya Muhammad, niombe chochote utakacho katika mali yangu (nitakupa, lakini) mimi sitakusaidia kwa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari 2753, Muslim 206, Tirmidhi 3185, na An-Nasai 3646). Na ikiwa hawajimilikii wao wenyewe wala wengine - katika uhai wao - manufaa wala madhara, basi hawammilikii mtu mwingine manufaa wala madhara baada ya kufa kwao.
Na tunaamini kwamba hawajui ghaibu isipokuwa kwa kiasi ambacho Mwenyezi Mungu amewajulisha na kuwapa idhini ya kufanya hivyo, amesema Mtukufu: "Sema: Mimi siwaambii kuwa ninazo hazina za Mwenyezi Mungu. Wala sijui mambo yaliyofichikana. Wala siwaambii kuwa mimi ni Malaika. Mimi sifuati isipokuwa yale yanayofunuliwa kwangu?" [Al-An'am: 50], Na akasema Mtukufu: "Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara, isipokuwa apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa ningekuwa ninayajua ya ghaibu, ningejizidishia mema mengi, wala ovu lisingenigusa. Mimi si chochote isipokuwa ni muonyaji na mbashiri kwa watu wanaoamini." [Al-A'araf: 188], Na akasema Mtukufu: "Yeye ndiye Mwenye kujua ya siri, wala hamdhihirishii yeyote siri yake. * Isipokuwa Mtume wake aliyemridhia. Naye huyo humwekea walinzi mbele yake na nyuma yake." [Al-Jinn: 26, 27].
Na Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, wanamuabudu Mwenyezi Mungu kwa hofu na matumaini, amesama Mtukufu: "Hakika wao walikuwa wepesi wa kutenda mema, na wakituomba kwa shauku na hofu. Nao walikuwa wakitunyenyekea." [Al-Anbiya: 90] Na wanatafuta njia ya kumwendea, na wanajiweka karibu naye Aliyetakasika, na kutukuka, amesema Mtukufu: "Hao wanaowaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kwendea kwa Mola wao Mlezi - hata miongoni mwao walio karibu mno - na wanataraji rehema zake na wanaihofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi yafaa kutahadhari nayo." [Al-Israa: 57].
Na Manabii na Mitume, amani iwe juu yao, pia wanakabiliwa na balaa, magonjwa na mauti ambayo wanadamu wanakabiliwa nayo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika wewe utakufa, nao kwa hakika watakufa." [Az-Zumar: 30], Na alisema Mtukufu akieleza kuhusu Ayub kuwa alipatwa na madhara: "Na Ayub, alipomuita Mola wake Mlezi, akasema: Mimi yamenipata madhara. Na Wewe ndiye unayerehemu kuliko wote wanaorehemu." [Al-Anbiya: 83] Na pia wana wake na dhuria (watoto). Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hakika Sisi tulikwishawatuma Mitume kabla yako, na tukajaalia wawe na wake na dhuria." [Ar-Ra'd: 38]. Na wanakula chakula na wanatembea katika masoko, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hatukuwatuma kabla yako Mitume wowote isipokuwa kwa hakika na yakini walikuwa wakila chakula, na wakitembea masokoni." [Al-Furqan: 20], Na pia wanakabiliwa na huzuni. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza kuhusu Ya'kub, amani iwe juu yake: "Naye akajitenga nao, na akasema: Ah! Masikini Yusuf! Na macho yake yakawa meupe kwa huzuni aliyokuwa akiizuia." [Yusuf: 84]. Na katika vitabu viwili vya hadithi sahihi, kuhusiana na habari ya kifo cha mtoto wa kiume wa binti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: Alipokaa, akanyanyuliwa akaletwa kwake, naye akamkalisha mapajani kwake, na mtoto akiwa tayari keshakuwa mzito (amefariki). Basi, macho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, yakabubujika machozi. Sa'di akasema: "Ni nini hicho ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema: "Hii ni rehema ambayo Mwenyezi Mungu huiweka ndani ya nyoyo za amtakaye miongoni mwa waja wake. Na hakika Mwenyezi Mungu huwarehemu wenye huruma miongoni mwa waja wake." (Imepokelewa na Bukhari 6655, Muslim 923, Abu Daud 3125, An-Nasai 1868, na Ibn Majah 1588). (Neno juitha: linamaanisha kuingiwa na hofu. Fat-hul-Bari 722/8, An-Nihaya fi Gharib Al-Hadith 1/ 232).
Na tunajua kwamba waliwanasihi viumbe, na wakatimiza amana zao, na wakafikisha jumbe za Mola wao Mlezi, na wala haiwadhuru kuwa wafuasi wao hawakuwaitikia, wala kwamba wakuu wa kaumu zao waliwafanyia kiburi, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Nilionyeshwa Umma mbele yangu; basi nikamuona Nabii ilhali ana kikundi kidogo cha watu pamoja naye. Na Nabii, akiwa na mwanaume mmoja na wanaume wawili. Na Nabii, akiwa hana mtu yeyote pamoja naye." (Imepokelewa na Bukhari 5705, Muslim 220, na Tirmidhi 2446).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu amemnyanyua juu Masihi, amani iwe juu yake, akiwa hai wakati watu wake walipotaka kumuua, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Isa alipohisi kuwa kati yao pana ukafiri, alisema: "Ni nani wasaidizi wangu kwa Mwenyezi Mungu?" Wanafunzi wake wakasema: "Sisi ni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu. Tumemuamini Mwenyezi Mungu, na shuhudia kwamba sisi hakika ni Waislamu * Mola wetu Mlezi! Tumeyaamini uliyoyateremsha, na tumemfuata huyu Mtume, basi tuandike pamoja na wanaoshuhudia * Na Makafiri walipanga mipango na Mwenyezi Mungu akapanga mipango, na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa wenye kupanga." [Al-Imran: 52-54] Na amesema Mtukufu: "Na kwa hakika yeye ni alama ya Saa ya Kiyama. Basi msiitilie shaka, na nifuateni. Hii ndiyo njia iliyonyooka." [Az-Zukhruf: 61] Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awawie radhi, Mujahid na Katada, kuwa maana yake ni: Kushuka kwa Isa bin Maryam, amani iwe juu yake. (Imepokelewa na At-Twabari katika Tafsir 20/631-633).
Na amesema Mtukufu: "Na hakuna yeyote katika Watu wa Kitabu isipokuwa atamuamini yeye bila shaka kabla ya kufa kwake. Naye Siku ya Kiyama atakuwa shahidi juu yao" [An-Nisaa: 159] Amesema bin Abbas Mwenyezi Mungu awe radhi naye: Maana ya "Kabla ya kufa kwake" Ni kabla ya kifo cha Isa bin Mariamu. (Tafsir Twabari: 9/380).
Na tunaamini kwamba katika zama za mwisho, atashuka hakimu muadilifu. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko mkono mwake! Kwa hakika amekaribia mno kuteremka kwenu (Waislamu) mwana wa Mariam, akiwa ni mtawala (kiongozi) mwadilifu. Atavunja msalaba, na kuwaua nguruwe na kukomesha ulipaji wa Jizia (kodi inayolipwa na wasiokuwa Waislamu, ambao wanaishi chini ya ulinzi wa serikali ya Kiislamu). Kisha kutakuwa na wingi wa mali hadi hakutakuwa na mtu yeyote atakayeikubali (kuchukuwa kama sadaka)." (Imepokelewa na Bukhari 2222, Muslim 155, Abu Daud 4324, Tirmidhi 2233, na Ibn Majah 4078).
Na katika habari za kushuka kwa Isa, amani imshukie, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Basi wakati atakapokuwa bado yuko hivyo, mara Mwenyezi Mungu atamtuma Masihi mwana wa Mariamu, naye atashukia kwenye mnara mweupe, mashariki mwa Damaskas (Syria), huku amevalia shuka mbili." (Neno "Mahrudatain" Linamaanisha atakuwa amevalia shuka mbili au nguo mbili zenye mapambo, au nguo iliyotiwa manukato ya Al-wars, kisha zafarani. An-Nihaya fi Gharibil-Hadith 5/258). Huku ameweka mikono yake juu ya mbawa za Malaika wawili, anapoinamisha kichwa chake matone ya maji yanadondoka, na anapokiinua zinatawanyika punje kama lulu kutoka kwake..." (Imepokelewa na Muslim 2937, Abu Daud 4321, Tirmidhi 2240, na Ibn Majah 4075).
Mlango wa ishara za Manabii na ushahidi wa unabii wao, amani iwe juu yao
Na tunajua kwamba Mwenyezi Mungu alimpa kila Nabii ishara na hoja ambazo wanadamu wanaamini mfano wa hizo. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakuna Nabii yeyote miongoni mwa Manabii isipokuwa alipewa miujiza ambayo kwa sababu yake, watu walimuamini au waliiamini. Na hakika kile nilichopewa (katika miujiza) ni ufunuo (Wahyi) ambao Mwenyezi Mungu alinifunulia. Kwa hivyo, ninatarajia kwamba nitakuwa na wafuasi wengi zaidi yao Siku ya Kiyama." (Imepokelewa na Bukhari 7274, na Muslim 152).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hakumtuma Nabii yeyote isipokuwa alikuwa na ishara zinayoonyesha ukweli wake, sawa iwe tunazijua au hatuzijui. Na Mwenyezi Mungu alitutajia baadhi yake katika Qur'ani tukufu. Na pia tunajua kuwa kuna ishara nyingi ambazo Mwenyezi Mungu aliwasaidia kwazo Mitume wake waliotangulia lakini hakuzitaja kwetu, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Na wale waliokufuru na wakazikadhibisha Ishara zetu, hao ndio watu wa Motoni." [Al-Maida: 10] Na maneno yake Mtukufu: "Kama ada ya watu wa Firauni na wale waliokuwa kabla yao, walizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu. Basi Mwenyezi Mungu akawashika kwa sababu ya madhambi yao. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu na mkali wa kuadhibu." [Al-Imran: 11]. Wakati mwingine, Mwenyezi Mungu hutaja ishara zilizo wazi, na wakati mwingine hutaja hoja, kama ilivyo katika kauli yake Mwenye sifa tukufu: "Na hakika tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na uthibitisho (hoja) zilizo wazi." [Hud: 96] Na kauli yake Mtukufu: "(Mwenyezi Mungu) akasema: Tutautia nguvu mkono wako kwa nduguyo, na tutawapa madaraka, hata wasikufikieni." [Al-Qasas: 35] Amesema Ikrima: "Chochote kilichotajwa ndani ya Qur'ani kwamba ni uthibitisho, hicho kinamaanisha hoja." (Tafsir Twabari 8/30 na 9/337).
Na tunajua kwamba ishara na hoja ambazo Mwenyezi Mungu aliwaunga mkono kwazo Mitume wake na Manabii wake, amani ziwashukie, ni nyingi sana. Na ishara kubwa zaidi inayoonyesha ukweli wao ni yale waliyokuja nayo katika ufunuo (wahyi). Na ufunuo wa Mwenyezi Mungu kwa Mitume wake na Manabii wake, amani iwe juu yao, ima ni ufunuo usiokuwa na yeyote wa kuufikisha, kama vile ndoto, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka akieleza kuhusu Ibrahim, amani iwe juu yake, kwamba alisema: "Basi alipofika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, akamwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja." [As-Saffat: 102], Au Mtume asikie maneno ya Mwenyezi Mungu moja kwa moja lakini kwa nyuma ya pazia, kama katika kauli yake Yeye mwenye sifa tukufu: "Na haikuwa kwa mwanadamu yeyote kwamba Mwenyezi Mungu amsemeshe isipokuwa kwa Ufunuo (Wahyi), au nyuma ya pazia." [Ash-Shura: 51], Na kama Mwenyezi Mungu alivyomuongelesha Musa, amani iwe juu yake, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "(Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Musa! Hakika mimi nimekuteua uende kwa watu na ujumbe wangu na maneno yangu. Basi chukua niliyokupa na uwe katika wanaoshukuru." [Al-A'raf:144], Au azungumzishwe na Malaika, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Au kumtuma Mjumbe. Naye humfunulia ayatakayo kwa idhini yake." [Ash-Shura: 51].
Na tunajua kwamba ushahidi mkubwa zaidi unaoonyesha ukweli wao ni kile wanachokilingania, kama vile kumpwekesha Mwenyezi Mungu ambako ni jambo lililothibiti katika maumbile ya asili ya mwanadamu, ambako akili zote zinashuhudia kuwa ni jambo zuri. Na pia miongoni mwa ushahidi ni yale waliyokuja nayo ya elimu yenye manufaa, matendo mema, uongofu, na dini ya haki na mizani (uadilifu). Imesimuliwa kutoka kwa Ubaidillah bin Abdallah, kwamba Abdallah bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, alimwambia akasema: Aliniambia Abuu Sufian kuwa: "Hirakil (Mfalme wa Roma) aliniambia: "Nilikuuliza anawaamuru nini (Huyo Mtume wenu?)? Ukasema kuwa anawaamuru kuswali, kusema ukweli, kuwa safi (kutokuwa washerati na mengineyo), kutimiza ahadi na kurejesha amana." Akasema: "Na hizi ndizo sifa za Manabii." (Imepokelewa na Bukhari 2681, Muslim 1773, na Tirmidhi 2717).
Na alisema Mfalme Najashi (wa Ethiopia) pale Jafari Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alipomsomea Suratu Maryam: "Hakika maneno haya na maneno aliyokuja nayo Musa yanatoka katika chanzo moja.” (Imepokelewa na Is-haq bin Rahwaih 1835, Ahmad 22498, Ibn Khuzaima 2260, Twahawi katika Sharh Mushkil Al-Aathaar 5598, na Abu Nu'aim katika Al-Hilya 1/115 na katika Dalail An-Nubuwwa 194).
Na miongoni mwake ni ushahidi wa Mwenyezi Mungu kwa Mitume wake kwamba wao wako katika haki, na kwamba yale waliyokuja nayo ni haki, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lakini Mwenyezi Mungu anayashuhudia yale aliyokuteremshia wewe. Ameyateremsha kwa kujua kwake - na Malaika pia wanashuhudia. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi." [An-Nisaa: 166], Na amesema Mtukufu: "Na wale waliokufuru wanasema: Wewe hukutumwa. Sema: Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi, na pia yule mwenye elimu ya Kitabu." [Ar-Ra'd: 43].
Na miongoni mwa ishara zao kubwa zaidi ni ufunuo (wahyi) unaowashukia kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na ufunuo (wahyi) mkubwa zaidi ni Qur'ani tukufu, ambao ni ishara ya Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie. Na hakuna mwanadamu anayeweza kuja na mfano wa ufunuo huu, kwa sababu ni maneno ya Mwenyezi Mungu na ufunuo wake, na pia kwa sababu una habari za ghaibu ndani yake, na kwa sababu una uongofu, nuru, rehema na hekima.
Na miongoni mwa ishara zao zilizo wazi ni hoja za kiakili ambazo Mwenyezi Mungu huwapa Mitume wake na Manabii wake, amani iwe juu yao, ambazo huwashinda makafiri na kuondoa batili yao, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyosema: "Je, hukumuona yule aliyehojiana na Ibrahim juu ya Mola wake Mlezi kwa sababu Mwenyezi Mungu alimpa ufalme? Ibrahim aliposema: Mola wangu Mlezi ni yule ambaye huhuisha na kufisha. Yeye akasema: Mimi pia ninahuisha na kufisha. Ibrahim akasema: Mwenyezi Mungu hulichomozesha jua Mashariki, basi wewe lichomozeshe Magharibi. Akafedheheka yule aliyekufuru; na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhalimu." [Al-Baqara: 258] Na kauli yake Mwenye sifa tukufu, na majina matakatifu: "Kwani hakika hao ni adui zangu, isipokuwa Mola Mlezi wa walimwengu wote * Ambaye ndiye aliniumba, na Yeye ndiye ananiongoa * Na ambaye ndiye ananilisha na kuninywesha * Na ninapougua, ni Yeye ndiye ananiponyesha * Na ambaye atanifisha, na kisha atanihuisha * Na ambaye ndiye ninamtumai kunisamehe makosa yangu Siku ya Malipo." [Ash-Shu'ara: 77-82] Na kauli yake kuhusu Musa, amani iwe juu yake, kuwa, alisema kumwambia Firauni: "Mola wetu Mlezi ni yule aliyekipa kila kitu umbo lake, kisha akakiongoa." [Twaha: 50], Na miongoni mwake ni kauli yake Mtukufu: "Lau wangelikuwamo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu, basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeliharibika. Ametakasika Mwenyezi Mungu, Bwana wa Kiti cha Enzi, na hayo wanayoyazua." [Al-Anbiya: 22] Na kauli yake Mwenye sifa tukufu: "Mwenyezi Mungu hana mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine. Ingekuwa hivyo, basi kila mungu angelichukua alivyoumba, na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa wanazomsifu." [Al-Mu'minun: 91]. Ushahidi huu ni mwingi sana. Tulitaja baadhi yake katika mlango wa umola na uungu. Na katika ishara zao kubwa zaidi, ni kujulisha kwao juu ya mambo ya ghaibu ambayo Mwenyezi Mungu anawaruhusu kuyasimulia.
Na miongoni mwa ishara zao za ajabu ni kuokolewa kwa Manabii waliotangulia, amani iwe juu yao, na wafuasi wao kutokana na njama za maadui zao, kuwaangamiza wakaidi wenye kiburi, na Mwenyezi Mungu kuwakumbusha wale wanaolinganiwa yale aliyowafanyia wale waliotangulia, na kwamba desturi ya Mwenyezi Mungu itaendelea. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema mwanzoni mwa suratul-Anbiyaa: "Kisha tukawatimizia miadi, na tukawaokoa wao na tuliowataka, na tukawateketeza waliovuka mipaka." [Al-Anbiya: 9] Na akasema katika kuihitimisha: "Na hakika tulikwisha andika katika Zaburi baada ya Kumbukumbu, ya kwamba ardhi watairithi waja wangu walio wema." [Al-Anbiya: 105] Na akasema Mtukufu: "Walizikadhibisha Ishara zetu zote, nasi tukawashika kama anavyoshika mwenye nguvu, mwenye uwezo * Je, makafiri wenu ni bora kuliko hao, au yameandikwa vitabuni kuwa nyinyi hamtiwi makosani?" [Al-Qamar: 42-43]. Na katika 'Surat Ash-Shu'ara', kila wakati Mwenyezi Mungu anapotaja kuokolewa kwa Manabii waliotangulia, amani iwe juu yao, na kuangamia kwa maadui zao, anaifuatisha kila habari miongoni mwa habari hizi haya maneno yake Mtukufu: "Hakika katika haya zipo Ishara (mazingatio), lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini." [Ash-Shu'ara: 67]. Amesema Mola wa Haki: "Basi wakipuuza, wewe sema: 'Ninawahadharisha adhabu mfano wa adhabu ya 'Adi na Thamudi." [Fussilat: 13], Na amesema Mola Mtukufu: "Je, hawatembei katika ardhi wakaona ulivyokuwa mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? Nao walikuwa na nguvu zaidi kuliko wao, na wakaitimbua ardhi na wakaistawisha zaidi kuliko walivyoistawisha wao. Na Mitume wao wakawajia na ishara zilizo wazi. Basi hakuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwadhulumu, lakini walikuwa wakijidhulumu nafsi zao." [Ar-Rum: 9].
Na miongoni mwa ishara zao zinazoashiria unabii wao ni ukamilifu wa sifa zao, tabia zao njema, matendo yao, mwenendo wao, na ukweli wa maneno yao, ambayo huwazuia kusema uongo. Mwenyezi Mungu alisema akieleza juu ya watu wa Swaleh, amani iwe juu yake, walisema kuwa: "Wakasema: Ewe Saleh! Hakika kabla ya haya ulikuwa unatarajiwa heri kwetu. Je, unatukataza tusiwaabudu waliyokuwa wakiwaabudu baba zetu? Na hakika sisi tuna shaka na wasiwasi kwa hayo unayotuitia." [Hud: 62] Na akasema Mtukufu: "Wakasema: Ewe Shuaibu! Ni swala zako ndizo zinazokuamrisha tuyaache yale waliyokuwa wakiyaabudu baba zetu, au tuache kufanya tupendavyo katika mali zetu? Ama hakika wewe ni mstahamilivu kweli na muongofu!" [Hud: 87].
Na alisema Mfalme Hirakli baada ya kumuuliza Abuu Sufian kuhusu Nabii wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Na nilikuuliza: Je, mliwahi kumtuhumu kwa kusema uongo kabla ya kusema kile alichosema? Wewe ukasema kwamba hamjawaji. Kwa hivyo, nikajua kwa hakika asingeweza kuacha kuwadanganya watu, kisha akasema uongo juu ya Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari 7, na Muslim 1773).
Na miongoni mwake ni simulizi nyingi za watu wengi zaidi katika kusimulia ishara za Manabii, na yale waliyokuja nayo ya elimu na uongofu, na dini ya haki, mambo ambayo haiwezekani watu wote kwa pamoja wakubaliane kusimulia uongo.
Na miongoni mwake ni kwamba hawaombi malipo juu ya utume wao, wala hawatafuti ufalme. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza kuhusu wengi katika Manabii wao kwamba kila mmoja wao aliwaambia watu wake: "Enyi watu wangu! Siwaombi ujira wowote kwa ajili ya haya. Haukuwa ujira wangu isipokuwa kwa Yule aliyeniumba. Basi hamtumii akili?" [Hud: 51].
Na miongoni mwake ni kwamba hakuna anayeukashifu unabii wa Manabii hawa isipokuwa mtu mjinga ambaye haangalii yale waliyokuja nayo ya dini, elimu, na uongofu, au mtu mkaidi mwenye kiburi, amesema Mtukufu: "Na wakazikataa kwa dhuluma na kujivuna, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo." [An-Naml: 14], Na amesema Mola wa Haki: "Tunajua ya kwamba yanakuhuzunisha hayo wanayoyasema. Basi hakika wao hawakukanushi wewe, lakini hao madhalimu wanazikataa Ishara za Mwenyezi Mungu." [Al-An'am: 33].
Na katika ishara zao kubwa zaidi ni hoja za kihisia zinazoonekana kwa macho, na akili zinajisalimisha kwazo, kama vile kuzama kwa watu wa Nuhu, ngamia wa Swaleh, na changamoto ya Hud kwa watu wake kwamba wote wampangie njama, na kuokoka kwa Ibrahim kutoka motoni. Na ishara za Musa ambazo miongoni mwake ni fimbo, nzige, chawa, vyura, damu, mafuriko, na kuzama kwa Firauni na watu wake. Na ishara za Daudi, amani iwe juu yake, kama vile milima kumtakasa Mwenyezi Mungu na kulainishiwa chuma. Na ishara za Sulaiman, amani iwe juu yake, kama vile kumtiishia upepo na majini, na kujua kwake mazungumzo ya ndege, na ishara za Masihi Issa, amani iwe juu yake, kama vile kuponya wakoma, na vipofu wa tangu kuzaliwa na vipofu wa kawaida, na kuwafufua wafu, na kwamba alikuwa akiunda kwa udongo kama sura ya ndege. Kisha anampuliza na anakuwa ndege kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na ishara za Nabii wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, nazo ni nyingi, na haziwezi kudhibitiwa isipokuwa kwa taabu kubwa mno, kama vile kupasua mwezi, kusafiri usiku kisha kupandishwa mbinguni, na kufanya chakula kuwa kingi, na kuwaongelesha wanyama, na changarawe kumtakasa Mwenyezi Mungu, na kulia kwa shina la mtende, na Mwenyezi Mungu kumnusuru dhidi ya maadui zake.
Na miongoni mwa ishara za Manabii ni hali ya Nabii anayelingania kwenye haki. Kwa maana watu hutofautisha kati ya mwenye kulingania kwenye haki kwa maneno yake, na mlinganiaji muongo katika maneno yake. Na ndiyo maana, akasema Abdallah bin Salam: "Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipofika Madina, watu walikwenda haraka kukutana naye, na ikasemwa: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, amefika. Basi nikaja pamoja na watu ili nimtazame. Nilipouona vyema uso wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, nikajua kwamba hakika uso wake haukuwa uso wa muongo." (Imepokelewa na Tirmidhi 2485, Ibn Majah 1334, Ibn Abī Shaiba 25898, Ahmad 23784, na 'Abd ibn Humaid 496). Na mengineyo yasiyo kuwa hayo yaliyotajwa miongoni mwa ishara mbalimbali.
Hakuna kilichobakia katika ishara za Manabii isipokuwa Qur'ani Tukufu na Sunna ya Mtume wetu Muhammad, amani imshukie, viwili hivyo vitabakia, kwa sababu ni wahyi ambao Mwenyezi Mungu alichukua jukumu la kuuhifadhi, amesema Mola Mtukufu: "Hakika Sisi ndio tuliouteremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutakaoulinda." [Al-Hijr: 9], Na ndani yake umo ushahidi mkubwa zaidi na hoja mbalimbali juu ya ukweli wa ujumbe wake, na ukweli wa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu anawaunga mkono Mitume wake, amani iwe juu yao, kwa yale yanayohitajiwa na hekima yake kwa ishara mbalimbali na hoja za kiulimwengu na za kisheria. Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu humuongoa amtakaye kwa fadhila zake, na humpoteza amtakaye kwa uadilifu wake, lakini mkaidi hazimzidishii ishara hizi isipokuwa ukaidi na kutakabari, amesema Mola wa Haki: "Na hakika tumekwisha bainisha katika Qur'ani hii ili wapate kukumbuka. Lakini haikuwazidisha isipokuwa kuwa mbali nayo." [Al-Israa: 41] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na hakika hayo ulioteremshiwa wewe kutokana na Mola wako Mlezi yatawazidishia wengi katika wao uasi na ukafiri." [Al-Maida: 68], Amesema Mtukufu: "Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu ukomo wa kuapa kwao, kwamba akiwajia muonyaji, bila ya shaka watakuwa waongofu zaidi kuliko taifa jingine lolote. Lakini alipowajia muonyaji, hakuwazidishia isipokuwa kuikimbia haki hiyo." [Fatwir: 42], Na akasema Mtukufu: "Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu kwa ukomo wa viapo vyao, kuwa ikiwafikia Ishara, bila ya shaka wataiamini. Sema: Ishara ziko kwa Mwenyezi Mungu. Na nyinyi hamjui kuwa zitakapokuja hawataamini." [Al-An'am: 109], Na akasema Mtukufu: "Na tuliwapa watu wa Thamudi ngamia jike kuwa ni Ishara iliyo dhahiri, lakini walidhulumu kwaye. Nasi hatutumi Ishara isipokuwa kwa ajili ya kuhadharisha." [Al-Israa: 59].
Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: "Watu wa Makka walimuomba Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, awafanyie mlima wa Swafa kuwa dhahabu, na kwamba awaondolee milima ili wafanye kilimo. Akamwambiwa: "Ukitaka unaweza kuendelea kuwangojea, na ukitaka, tutawatumia hicho walichoomba, lakini wakikufuru, wataangamizwa kama nilivyowaangamiza wale waliokuwa kabla yao." Akasema: "Hapana, nitawangojea." Hivyo Mwenyezi Mungu akateremsha aya hii: "Na hapana kinachotuzuia kutuma miujiza isipokuwa ni kuwa watu wa zamani waliikadhibisha. Na tuliwapa watu wa Thamudi ngamia jike kuwa ni Ishara iliyo dhahiri." [Al-Israa: 59]. (Imepokelewa na Ahmad 2333, Al-Bazzar 5036, An-Nasai katika Al-Kubra 11226, Al-Hakim 3437, na Al-Baihaqi katika Dalail An-Nubuwwa 605).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu angetaka, angewaongoa watu wote, amesema Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu angelitaka, kwa yakini angeliwafanya muwe umma mmoja. Lakini anampoteza anayemtaka, na anamuongoa amtakaye." [An-Nahl: 93]. Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angependa, angeliwakusanya kwenye uongofu. Basi usiwe miongoni mwa wasiojua." [Al-An'am: 35].
Na tunaamini kwamba ushahidi wa Manabii, na ishara walizoleta na uthibitisho ambao Mwenyezi Mungu aliwapa ni jambo lisilowezekana kwa mtu yeyote anayedai unabii, au hata mchawi, au muongo. Kwa sababu Mwenyezi Mungu alishapitisha kwamba mtu wa batili hawezi kuungwa mkono kwa ushahidi sahihi, na wala muongo hawezi kusadikiwa kwa uthibitisho wa kweli. Kwa sababu Yeye ndiye Mwenye hekima katika sheria yake na amri yake. Na hekima ya Mwenyezi Mungu na desturi zake zinazoendelea zinazuia hilo. aAmesema Mola Mtukufu: "Na lau kama angetuzulia baadhi ya maneno tu * Bila ya shaka tungelimshika kwa mkono wa kulia * Kisha kwa hakika tungelimkata mshipa mkubwa wa moyo!" [Al-Haqqa: 44-46].
Mlango wa unabii wa Nabii wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie
Na tunaamini kuwa Nabii wetu Muhammad bin Abdallah ni Mtume wa Mola wa walimwengu wote, na ndiye mwisho wa Manabii na Mitume, amesema Mtukufu: "Muhammad si baba wa yeyote katika wanaume wenu, bali ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na Mwisho wa Manabii." [Al-Ahzab: 40]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika mfano wangu kwa kulinganisha na Manabii waliokuwa kabla yangu, ni kama mtu aliyejenga nyumba vizuri na akairemba, isipokuwa mahali pa tofali moja kwenye kona. Basi watu wakawa wanaizunguka na wanashangazwa na uzuri wake, lakini wanasema: "Lau kama tu tofali hili lingewekwa mahali pake (basi nyumba hii ingekuwa nzuri kiasi gani)!" Akasema: "Kwa hivyo, mimi ndiye tofali hilo, na mimi ndiye mwisho wa Manabii." (Imepokelewa na Bukhari 3535, na Muslim 2286).
Naye ndiye bwana wa wanadam. Amesema rehema na amani ziwe juu yake: "Mimi ndiye bwana wa wanadam Siku ya Kiyama, na nitakuwa wa kwanza ambaye kaburi litamfungukia, na wa kwanza kufanya uombezi, na wa kwanza kukubaliwa uombezi wake." (Imepokelewa na Muslim 2278 na Abuu Daud 4673). Yeye ndiye rafiki mwandani wa Mola Mlezi wa viumbe vyote, anasema rehema na amani ziwe juu yake: "Lau ningemchagua rafiki mwandani katika umma wangu, basi ningelimchagua Abubakari, lakini ni ndugu yangu na swahaba wangu.” (Imepokelewa na Bukhari 3656).
Na tunajua kwamba alipewa Ishara ambazo hakupewa yeyote mfano wake miongoni mwa Mitume, amani iwe juu yao. Na ishara yake kubwa zaidi ni Qur'ani Tukufu. Na cha kwanza alichoteremshiwa ni mwanzo wa “Suratul-Alaq”, kama ilivyothibiti katika hadithi hii: Imesimuliwa kutoka kwa Aisha mama wa Waumini kuwa alisema: Cha kwanza alichoanzishwa nacho Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake katika ufunuo (wahyi) kilikuwa ndoto nzuri katika usingizi. Hivyo, akawa haoni ndoto yoyoye isipokuwa ilikuwa inakuja mfano wa mwanga wa asubuhi. Kisha, alifanywa kupenda kukaa peke yake. Kwa hivyo, akawa anakaa peke yake ndani ya pango la Hiraa na anafanya ibada humo kwa siku zenye idadi maalumu kabla ya kurudi kuiona familia yake na kuchukua chakula kingine tena kwa sababu ya hilo. Kisha anarudi kwa Khadija (bint Khuwailid) na anachukua chakula cha muda kama huo. Mpaka alipojiwa na haki hali ya kuwa yuko ndani ya pango la Hiraa. Malaika akamjia na akasema: "Soma!". (Mtume) akasema: "Mimi sijui kusoma." (Mtume) Akasema: " Hivyo, (Malaika huyo) akanichukua na akanifinya kwa nguvu mpaka akanimaliza nguvu kabisa. Kisha akaniachilia na akasema: “Soma!” Nikasema: "Mimi sijui kusoma." (Malaika huyo) akanichukua kwa mara ya pili na akanifinya kwa nguvu mpaka akanimaliza nguvu kabisa. Kisha akaniachilia na akasema: “Soma!” Nikasema: "Mimi sijui kusoma." (Malaika huyo) akanichukua na akanifinya kwa mara ya tatu. Kisha akaniachilia na akasema: "Soma kwa Jina la Mola wako Mlezi, aliyeumba. Alimuumba mwanadam kutokana na pande la nyama. Soma, na Mola wako Mezi ndiye Mkarimu mno." (Qur'ani, Suratul-Alaq: 1-3).” Kisha, Mtume rehema na amani ziwe juu yake akarudi (nyumbani) na hayo (aliyoambiwa) huku moyo wake unatetemeka (kwa hofu)." (Imepokelewa na Bukhari 3, Muslim 160, na Tirmidhi 3632). Kisha baada ya Aya hizo zikateremshwa "Al-Muddathir". Imesimuliwa kutoka kwa Jabir bin Abdallah, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alimsikia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akizungumzia kipindi cha kukatika kwa wahyi: "Nilipokuwa ninatembea, tazama! Nilisikia sauti kutoka mbinguni, hivyo nikainua macho yangu juu kuelekea mbinguni, na tazama! Nikamuona Malaika yule aliyenijia katika pango la Hiraa hali ya kuwa ameketi juu ya kiti kati ya mbingu na ardhi, hivyo nikamuogopa sana kiasi kwamba nilianguka chini. Basi nikaenda kwa mke wangu (Khadija), na nikasema: "Nifunikeni! Nifunikeni! Nifunikeni!", Basi, Mwenyezi Mungu aliyetukuka akateremsha: "Ewe uliyejigubika! Simama uonye!"(Muddathir: 1,2) hadi kauli yake: "Na yaliyo machafu yahame!" Abuu Salama anasema: 'Rijz: Inamaanisha vyote vinavyoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu. Baada ya hapo, ufunuo (wa Mwenyezi Mungu) ulianza kuja kwa kasi ukifuatana." (Imepokelewa na Bukhari 4926, Muslim 161, na Tirmidhi 3325).
Na imesimuliwa kutoka kwa Aisha mama ya waumini, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Al-Harith bin Hisham, Mwenyezi Mungu amridhie, alimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Je wahyi unakujia namna gani? Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Wakati mwingine, unanijia kama sauti ya kengele, na huu ndio wakati mgumu zaidi juu yangu kuliko zote, kisha unaondolewa kwangu hali ya kuwa tayari nimeshafahamu kutoka kwake (yani Malaika) kile alichosema." Amesema Aisha: “Na hakika, nilimuona (Mtume) akiwa katika hali ya kuteremkiwa na wahyi katika siku yenye baridi kali, kisha hali hiyo ikamuondokea, na kwa hakika paji la uso wake lilikuwa likitiririka jasho.” (Imepokelewa na Bukhari 2, Muslim 2333, Tirmidhi 3634, na An-Nasai 933).
Na kuwa alikaa Makka kwa muda wa miaka kumi na tatu akilingania tauhidi, na akakaa Madina kwa muda wa miaka kumi akifafanua sheria za Mwenyezi Mungu, na akilingania dini yake, na kupambana katika njia yake, mpaka Mwenyezi Mungu alipomfisha akiwa na umri wa miaka sitini na tatu. Rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, ninamfidia kwa baba na mama yangu.
Na tunajua kwamba katika ishara kubwa zaidi baada ya Qur'ani tukufu ni ile safari ya usiku kutoka Makka kisha kupandishwa mbinguni, amesema Mtukufu: "Ametakasika Yule aliyemchukua mja wake usiku mmoja kutoka Msikiti mtukufu mpaka Msikiti wa mbali, ambao tumevibariki vilivyouzunguka, ili tumuonyeshe baadhi ya Ishara zetu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia na Mwenye kuona." [Al-Israa: 1].
Na imesimuliwa kutoka kwa Anas Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Nililetewa Buraq, naye ni mnyama mweupe, mrefu, mkubwa zaidi ya punda lakini mdogo kuliko nyumbu, ambaye alikuwa akiziweka kwato zake kwenye sehemu ya mwisho yanapofikia macho yake -. Anasema: nikampanda mpaka nilipofika katika Baitul-Maqdis (huko Yerusalemu, Palestina). Kisha nikamfunga kwenye kigingi ambacho Manabii walikuwa wakitumia kufunga wanyama wao." Akasema: Kisha nikaingia ndani ya msikiti na nikaswali humo rakaa mbili, kisha nikatoka nje. Jibril akaniletea chombo chenye pombe na chombo kingine chenye maziwa, nikachagua maziwa, Jibril akasema: "Umechagua umbile la asili." Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya chini. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaulizwa: "Wewe ni nani?" Akajibu: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Hivyo, tukafunguliwa (mlango). Ghafla! Nikamuona Adam, akanikaribisha na akaniombea heri. Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya pili. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaambiwa: "Wewe ni nani?" Akajibu: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Hivyo, tukafunguliwa (mlango). Na tazama! Nikawaona watoto wawili wa mama zangu wakubwa; Isa bin Maryam na Yahya bin Zakaria, amani iwe juu yao, hivyo, wakanipokea na wakaniombea heri. Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya tatu. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaambiwa: "Wewe ni nani?" Akasema: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad" Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Hivyo, tukafunguliwa (mlango). tazama! Nikamuona Yusuf, amani iwe juu yake, basi alikuwa kapewa nusu ya uzuri. Akanikaribisha na akaniombea heri. Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya nne. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaulizwa: "Wewe ni nani?" Akasema: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Basi, tukafunguliwa (mlango). Na tazama! Nikamuona Idrisa. Basi, akanikaribisha na akaniombea heri. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema: "Na tulimuinua (Idrisa) daraja ya juu." ( Maryam 19:57). Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya tano. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaulizwa: "Wewe ni nani?" Akasema: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Basi, tukafunguliwa (mlango). Na tazama! Nikamuona Harun, amani iwe juu yake. Basi, akanikaribisha na akaniombea heri. Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya sita. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaulizwa, "Wewe ni nani?" Akasema: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaambiwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndio) Amekwisha pewa utume." Kwa hivyo, tukafunguliwa (mlango). Na tazama! Nikamuona Musa, amani iwe juu yake. Basi, akanikaribisha na akaniombea heri. Kisha akapanda pamoja nami mpaka mbingu ya saba. Jibril akaomba ruhusa ya kuingia. Akaambiwa: "Wewe ni nani?" Akasema: "Jibril." Akaulizwa: "Ni nani aliye pamoja nawe?" Akasema: "Muhammad." Akaulizwa: "Je, amekwisha pewa utume?" Jibril akasema: "(Ndiyo) Amekwisha pewa utume." Kwa hivyo, tukafunguliwa (mlango). Na tazama! Nikamuona Ibrahim, amani iwe juu yake, hali ya kuwa ameegemea na amekaa katika Baitul-Ma'muri (Msikiti ulioko Mbinguni), na tazama! Ulikuwa unaingiwa na Malaika elfu sabini (70,000) kila siku, na wala hawarejei tena humo. Kisha akaenda pamoja nami mpaka katika Mti wa Mkunazi ulioko mwisho kabisa (Sidratul-Muntaha ), Tazama! Majani yake yalikuwa kama masikio ya tembo, na matunda yake yalikuwa kama vyungu vikubwa. Wakati ulipofunikwa (mti huo) na kile kilichoufunika katika mambo ya Mwenyezi Mungu, ukabadilika, na hakuna hata mmoja katika viumbe wa Mwenyezi Mungu anayeweza kuusifia kwa uzuri wake. Kisha Mwenyezi Mungu akanifunulia kile alichonifunulia, kisha akanifaradhishia swala hamsini (50) kwa mchana na usiku. Kisha nikateremka mpaka kwa Musa, amani iwe juu yake, akasema: "Mola wako Mlezi amekufaradhishia nini juu ya umma wako?" Nikasema: "Swala hamsini (50)." Akasema: "Rudi kwa Mola wako Mlezi na umuombe akupunguzie (idadi ya swala hizo), kwa sababu umma wako hautaweza hilo. Kwani mimi kwa hakika, niliwajaribu Wana wa Israel na kuwapa mitihani." (Mtume) akasema: "Basi, nikarudi kwa Mola wangu Mlezi na nikasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Wapunguzie umma wangu." Basi, (Mwenyezi Mungu) akanipunguzia swala tano. Basi, nikarudi kwa Musa nikamwambia: "(Mwenyezi Mungu) amenipunguzia swala tano. Akasema: "Hakika umma wako hautaweza hilo. Rudi kwa Mola wako Mlezi na umuombe akupunguzie." Basi, nikaendelea kurudi kati ya Mola wangu Mlezi Aliyetakasika na kutukuka, na Musa amani iwe juu yake, mpaka aliposema (Mola wangu Mlezi), "Ewe Muhammad! Hakika, ni swala tano kila mchana na usiku, na kila swala itahesabika kama (swala) kumi. Na swala hizo kwa hilo ni swala hamsini (50). Na yeyote yule atakayetaka kufanya wema wowote, kisha asiufanye (wema huo), basi ataandikiwa hilo kama tendo jema moja. Na kama ataufanya, basi ataandikiwa hilo mara kumi. Na yeyote yule atakayetaka kufanya tendo ovu (baya), lakini asilifanye, basi hilo halitaandikwa kitu chochote. Na kama atalifanya, basi litaandikwa kama ovu (baya) moja." Kisha nikateremka mpaka nilipofika kwa Musa na nikamwambia. Akasema: "Rudi kwa Mola wako Mlezi umuombe akupunguzie." Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema: "Tayari nimesharudi kwa Mola wangu Mlezi mpaka ninamstahi." (Imepokelewa na Bukhari: 7517, Muslim: 162, Tirmidhi: 3131, An-Nasai: 450, na Ibn Maja: 1399).
Na miongoni mwa ishara zake, Mwenyezi Mungu amfikishie rehema na amani, ni kupasuka kwa mwezi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Saa imekaribia, na mwezi umepasuka!" [Al-Qamar:1] Na imesimuliwa kutoka kwa bin Masud, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, mwezi ulipasuka vipande viwili; kipande kimoja kilikuwa juu ya mlima, na kingine chini ya mlima. Basi, Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Shuhudieni (hili)." (Imepokelewa na Bukhari: 4864, Muslim: 2800, na Tirmidhi: 3285).
Na Mwenyezi Mungu alimpa yeye tu mambo maalumu mengi, kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Nimefanywa kuwa bora juu ya Manabii wote kwa mambo sita: Nimepewa maneno mafupi yenye maana pana, na nimenusuriwa na hofu (inayotiwa ndani ya mioyo ya adui zangu), na nimehalalishiwa ngawira, na nimefanyiwa ardhi yote kuwa safi na mahali pa kuswalia, na nimetumwa kwa viumbe wote, na mimi ndiye mwisho wa Manabii." (Imepokelewa na Muslim: 523 na Tirmidhi: 1553). Sifa zake hizi maalumu wanazuoni walizitaja mwanzoni mwa tunzi zao wakati mwingine, na wakati mwingine waliziandika katika vitabu vya kujitegemea.
Na tunaamini kwamba ni wajibu kwa kila Muumini wa kiume na Muumini wa kike amwamini, amsadikishe katika yale aliyoyaeleza, na amtii katika yale aliyoamrisha, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ili mumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na mumsaidie, na mumheshimu, na mumtakase asubuhi na jioni." [Al-Fath: 9] Na amesema Mwenye Nguvu, na Mwenye majina matukufu: "Basi muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na Nuru tuliyoiteremsha. Na Mwenyezi Mungu anazo habari za mnayoyatenda." [At-Taghabun: 8]
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu hapaswi kuabudiwa isipokuwa kwa yale aliyoyaweka Mtume wetu katika sheria, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na anachowapa Mtume, chukueni. Na anachowakataza, jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu." [Al-Hashir: 7] Na alitahadharisha Mola wa Haki juu ya kuasi amri ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, akasema Mtukufu: "Basi na watahadhari wale wanaoihalifu amri yake, usije ukawapata msiba au ikawapata adhabu chungu." [An-Nur: 63]
Ni lazima kumheshimu na kumpenda. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Sema: Ikiwa nyinyi mnampenda Mwenyezi Mungu, basi nifuateni mimi, Mwenyezi Mungu atawapenda na atawafutia madhambi yenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta madhambi na Mwenye kurehemu." [Al-Imran: 31]
Na kumpenda Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ni miongoni mwa misingi ya imani. Na Mwenyezi Mungu ameliunganisha hilo na kumpenda Yeye, na akaahidi adhabu mwenye kutanguliza mbele yake chochote katika mambo yanayopendwa kwa mujibu wa maumbile ya asili, kama vile jamaa, mali, nchi na vitu vinginevyo. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Sema: Ikiwa baba zenu, na wenenu, na ndugu zenu, na wake zenu, na jamaa zenu, na mali mlizozichuma, na biashara mnazoogopa kuharibika, na majumba mnayoyapenda, ni vipenzi zaidi kwenu kuliko Mwenyezi Mungu na Mtume wake na Jihadi katika Njia yake, basi ngojeni mpaka Mwenyezi Mungu alete amri yake. Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wavukao mipaka." [At-Tauba: 24]
Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, anapaswa kuwa ndiye mpendwa zaidi kwa Muumini kuliko yeye mwenyewe, baba yake, watoto wake na watu wote. Imesimuliwa kutoka kwa Abdallah bin Hisham kuwa alisema: Tulikuwa pamoja na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, hali ya kuwa amemshika Omari bin Khattwab kwa mkono wake. Omari akamwambia: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Hakika wewe, ni mpendwa zaidi kwangu kuliko kila kitu isipokuwa kuliko nafsi yangu." Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasema: "Hapana, ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko mkononi mwake! (huwezi kuwa na imani kamili) mpaka niwe mpendwa zaidi kwako kuliko nafsi yako." Basi, Omari akamwambia: "Basi, sasa wallahi! Hakika wewe ni mpendwa zaidi kwangu hata kuliko nafsi yangu." Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasema: "Sasa, ewe Omari (umesema ipasavyo)." (Imepokelewa na Bukhari: 6632).
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu ameunganisha utajo wa Nabii wetu Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, pamoja na utajo wake, Yeye aliyetakasika, katika shahada mbili na katika adhana. Na Mtume, rehema na amani zimshukie ametajwa sana katika vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyotangulia, na katika Qur’ani tukufu, na maimamu wa Uislamu wameandika vitabu mbalimbali vinavyoelezea Sunna zake, maisha yake, sifa zake, maadili yake, na vita vyake. Na hapa tutataja tu yale ambayo ni wajibu kuyaitakidi kuhusiana na unabii wake.
Amesema Kadhi Iyadh Mwenyezi Mungu amrehemu : "Ikiwa sifa za ukamilifu na utukufu ndizo tulizozitaja, na tukamuona mmoja wetu anaheshimika na moja kati yazo, au mbili ikiwa atabaki nazo katika kila zama: Ima kutokana na nasaba, uzuri, nguvu, ustahamilimu, ujasiri, au uvumilivu, utangamano bora na watu wote na apate hadhi nzuri, umaarufu, na upendo wa kipekee katika mioyo ya watu kutokana na tabia yake, hata huenda alikufa zamani sana; kwa hivyo unafikiria nini kuhusu yule ambaye zimekusanyika sifa zote hizi kwake kwa njia ambayo haiwezi kupimwa, kuonyeshwa kwa maneno, au kupatikana kwa juhudi au njia maalumu? Isipokuwa kwa kuteuliwa na Mola Mtukufu Mkubwa, kwa kupewa ubora wa unabii, utume, urafiki mwandani, upendo, kuchaguliwa, kupelekwa katika safari ya Israa, na kumuona Mwenyezi Mungu Mtukufu. (Suala la Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kumuona Mwenyezi Mungu usiku wa Israa ni jambo ambalo lina kauli tofauti za wanachuoni juu yake, lakini kauli sahihi ni kwamba Mtume wetu, rehema na amani zimshukie, hakumuona Mola wake Mlezi katika usiku wa Israa.) Na kuwa karibu (na Mwenyezi Mungu), na ufunuo, na uombezi, kutafuta njia ya kumfikia Mwenyezi, na hadhi kubwa, na daraja la juu, na mahali panaposifiwa, na Buraq, na kupanda mbinguni, na kutumwa kufikisha ujumbe kwa watu wekundu na weusi, na kuwaswalisha Manabii, kushuhudia kati ya Manabii na umma zao, na ubwana wake juu ya wanadam wote, na bendera ya kumsifu Mwenyezi Mungu, na bishara njema, na kuaonya watu, na kuwa na cheo kwa Mwenye Kiti cha Enzi, na kutiiwa huko, na uaminifu, na uongofu, na rehema kwa walimwengu wote, na kuridhiwa na kupewa aombacho, na Kauthari (Mto), na kusikiliza yanayosemwa, na kukamilishiwa neema, na kusamehewa yaliyotangulia na yatakayokuja, na kukunjuliwa kifua, na kuondolewa mizigo, na kunyanyuliwa katika utajo, na nusura kubwa, na kushuka utulivu, na kusaidiwa na Malaika, na kupewa Kitabu na hekima, na aya saba zinazosomwa kwa kurudiwarudiwa, na Qur'ani tukufu, na kuwatakasa umma, na kumuomba dua Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu na Malaika kumuombea, na kuhukumu baina ya watu kwa yale aliyoonyeshwa na Mwenyezi Mungu, na kuwaondolewa mizigo na minyororo, na kuapa kwa jina lake, na kuitikia dua yake, na kuviongelesha na vitu visivyo na uhai na watu wasiojua lugha yake... na kuwasikilizisha viziwi, na chemchemi ya maji kutoka baina ya vidole vyake, kukithirisha chakula kichache, na kupasuka mwezi, na kulirejesha jua, na kupindua vitu kutoka katika hali yake ya kawaida, na kunusuriwa kwa hofu, na yale yote ambayo mshereheshaji hawezi kuyahifadhi, na wala hawezi kuidhibiti elimu yake isipokuwa yule aliyempa hayo, na akamboresha kwayo ambaye hapana mungu isipokuwa yeye, pamoja na yale aliyomtayarishia Akhera kama vile mashukio ya heshima, daraja za utukufu, viwango vya furaha, wema, na kuongezewa ambako akili haziwezi kukufikia, na hata mawazo hayawezi kujua kwa hali yake ya uhalisia. (Ash-Shifa bita'riif Huquuqul-Mustwafaa 1/55-57).
Mlango wa kuenea utume wake, amani iwe juu yake kwa viumbe wote
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alimtuma Mtume wake Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, kwa viumbe wote, amesema Mtukufu: "Sema: Enyi watu! Hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu nyinyi nyote. Yeye ambaye ni wake ufalme wa mbingu na ardhi. Hapana mungu isipokuwa Yeye anayehuisha na anayefisha. Basi muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake asiyejua kusoma na kuandika, ambaye anamuamini Mwenyezi Mungu na maneno yake. Na mfuateni yeye ili mpate kuongoka." [Al-A'raf: 158], Na amesema Mola Mtukufu: "Na hatukukutuma isipokuwa kwa watu wote, uwe mbashiri (mtoa habari njema), na muonyaji. Lakini watu wengi hawajui." [Saba': 28]
Na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, amesema: "Nimepewa vitu vitano ambavyo havikupewa kwa mtu mwingine miongoni mwa Manabii kabla yangu. Nimenusuriwa na hofu kwa umbali wa safari ya mwezi mmoja. Na nimefanyiwa ardhi kuwa mahali pa kuswalia na ni twahara (safi). Hivyo, yeyote katika umma wangu atakapopatwa na swala, basi na aswali (popote). Na nimehalalishiwa ngawira. Na kila Nabii alikuwa akitumwa kwa umma wake tu, lakini mimi nimetumwa kwa watu wote. Na nimepewa uombezi (Siku ya Kiyama).” (Imepokelewa na Bukhari: 438, Muslim: 521, na An-Nasai: 432).
Na Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, alitumwa na Mwenyezi Mungu kwa vizito viwili: Wanadamu na majini kwa na hili wamekubaliana juu yake Waislamu wote. Na majini walisikiliza Qur'ani na wakarudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya, Mwenyezi Mungu akamueleza Mtume wake hilo katika Qur'ani katika kauli yake: "Na wakati tulipowaleta kundi la majini kuja kwako kusikiliza Qur'ani. Basi walipoihudhuria, walisema: Sikilizeni! Na ilipokwishasomwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya * Wakasema: Enyi kaumu yetu! Hakika sisi tumesikia Kitabu kilichoteremshwa baada ya Musa, kinachosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na kinachoongoza kwenye Haki na kwenye Njia iliyonyooka * Enyi kaumu yetu! Muitikieni Mwenye kuitia kwa Mwenyezi Mungu, na muaminini, Mwenyezi Mungu atawasamehe, na atawakinga kutokana na adhabu chungu * Na wasiomuitikia Mwitaji wa Mwenyezi Mungu, basi hao hawatashinda katika ardhi, wala hawatakuwa na walinzi mbele yake. Hao wamo katika upotovu ulio dhahiri." [Al-Ahqaf: 29- 32].
Na Mwenyezi Mungu alichukua agano kwa kila Nabii na Mtume, amani iwe juu yao: Ikiwa Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie atatumwa hali ya kuwa yupo hai, basi hakika atamwamini, amesema Mola Mtukufu: "Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua ahadi kwa Manabii: Nikishawapa Kitabu na hekima, kisha akawajia Mtume mwenye kusadikisha mliyo nayo, ni juu yenu mumuamini na mumsaidie. Akasema: Je, mmekiri na mmekubali kushika agizo langu juu ya hayo? Wakasema: Tumekubali. Akasema: Basi shuhudieni, na Mimi ni pamoja nanyi katika wanaoshuhudia." [Al-Imran: 81]. Ali bin Abi Twalib, Mwenyezi Mungu awe radhi naye alisema: "Mwenyezi Mungu Mtukufu hakumtuma Nabii, kuanzia kwa Adam wala yeyote baada yake, isipokuwa alichukua agano kutoka kwake kuhusiana na Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba ikiwa atatumwa - ilhali yu hai - basi hakika atamwamini na atamnusuru, na pia anamwamrisha na anachukua agano kutoka kwa kaumu yake. Akasema: "Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua ahadi kwa Manabii: Nikishawapa Kitabu na hekima." hadi mwisho wa Aya" [Al Imran: 81]. (Imepokelewa na At-Twabari katika Tafsir: 5/540).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "(Mimi natokana) na dua ya baba yangu, Ibrahim, na bishara njema ya Isa kwa kaumu yake, na ndoto ya mama yangu ambaye aliona kuwa ametokwa na nuru ambayo ilimuangazia makasri ya Sham." (Imepokelewa na Ahmad: 17163, Othman bin Sa'id Ad-Darmi katika Ar-Raddu alal-Jahmiyya: 261, Ibn Abi 'Asim katika As-Sunna: 418, Abdallah bin Ahmad katika As-Sunnah: 865, Ibn Hibban 6404, na At-Twabrani katika Musnad Al-Shamiyyin 1455). Na amesema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mimi ni dua ya baba yangu Ibrahim." Anakusudia kwa hiyo yale aliyotueleza Mola Mtukufu kuhusiana na dua ya Ibrahim, amani iwe juu yake, ambayo ni kauli yake: "Ewe Mola Mlezi wetu! Watumie Mtume anayetokana na wao, awasomee Aya zako, na awafundishe Kitabu na hekima na awatakase. Hakika Wewe ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hekima." [Al-Baqara: 129].
Na tunaamini kuwa Manabii walizibashiria kaumu zao kuhusu Mtume Muhammad, rehema na amani zimshukie, na zikaja sifa zake na sifa za Maswahaba zake, Mwenyezi Mungu awawie radhi, katika Taurati na Injili. Amesema aliyetakasika na kutukuka: "Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na wale walio pamoja naye wana nguvu mbele ya makafiri, na wanahurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama na kusujudu wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Alama zao ni katika nyuso zao, kwa athari ya kusujudu. Huu ndio mfano wao katika Taurati. Na mfano wao katika Injili ni kama mmea uliotoa chipukizi lake, kisha ukalitia nguvu, ukawa mnene, ukasimama sawa juu ya ubuwa wake, ukawafurahisha wakulima, ili kuwakasirisha kwa ajili yao makafiri. Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walioamini na wakatenda mema katika wao msamaha na ujira mkubwa." [Al-Fath: 29], Na amesema Mola Mtukufu: "Wale ambao wanamfuata Mtume huyo, Nabii, asiyesoma wala kuandika, wanayemkuta kaandikwa kwao katika Taurati na Injili, anayewaamrisha mema na anawakanya maovu, na anawahalalishia vizuri, na anawaharamishia viovu, na anawaondolea mizigo yao na minyororo iliyokuwa juu yao. Basi wale waliomuamini yeye, na wakamheshimu, na wakamsaidia, na wakaifuata nuru iliyoteremshwa pamoja naye - hao ndio wenye kufanikiwa." [Al-A'araf: 157]. Na Masihi amani iwe juu yake aliwabashiria Wana wa Israeli juu yake, amesema Mtukufu akieleza juu yake kuwa alisema: "Enyi Wana wa Israeli! Hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu, ninayethibitisha yale yaliyokuwa kabla yangu katika Taurati, na mwenye kubashiria kuja Mtume atakayekuja baada yangu; jina lake ni Ahmad! Lakini alipowaletea hoja zilizo wazi, walisema: Huu ni uchawi ulio dhahiri!" [As-Saff: 6]. Na Watu wa Kitabu walikuwa wakimjua kama wanavyowajua watoto wao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wale tuliowapa Kitabu wanayajua haya kama wanavyowajua watoto wao; na kuna kikundi katika wao huificha haki na hali wanajua." [Baqara: 146].
Na katika ishara za unabii wake rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie zilizokuwa zikijulikana kwa watu wa Kitabu ni muhuri wa unabii uliokuwa kwenye bega lake tukufu. Imesimuliwa kutoka kwa As-Saib bin Yazid radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kuwa alisema: "Kisha nilisimama nyuma ya mgongo wake na nikauona muhuri wa unabii kati ya mabega yake mawili, na ulikuwa kama kishikizo cha hema dogo linalotengenezwa kwa nguo, (au mithili ya yai la njiwa.)" (Imepokelewa na Bukhari: 190, Muslim: 2345, na Tirmidhi: 3643).
Na imesimuliwa kutoka kwa Jabir bin Samura, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: "Niliuona muhuri kwenye mabega yake ulikuwa mfano wa yai la njiwa, huku ukifanana na mwili wake." (Imepokelewa na Muslim: 2344, Tirmidhi: 3644, na An-Nasai: 5114).
Na tunaamini kwamba ujumbe wake unawaenea watu wote, na ndiyo maana aliwaandikia barua wafalme na wakuu akiwalingania kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na kuuamini ujumbe wake yeye rehema na amani zimshukie na wausadikishe. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Burda kutoka kwa baba yake radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema: Alituamrisha Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kwenda katika nchi ya Mfalme Najashi (Ethiopia)- na akasimulia kisa chake hicho - Najashi alisema: Ninashuhudia kuwa, hakika huyo ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, na yeye ndiye ambaye Isa bin Maryamu alimbashiria. Na lau kama nisingekuwa mfalme, basi ningemjia mpaka nikazibeba ndara zake." (Imepokelewa na Abu Daud: 3205, Ibn Abi Shaiba: 37795, ʻAbd ibn Ḥumaid: 550, Ibn Abi 'Asim katika Al-Aahaad Wal-Mathanii: 366, Ar-Rawyānī 502, na Al-Ḥākim: 3268).
Na Mfalme Hirakli alisema baada ya kupokea barua ya Mtume wa Mwenyezi Mungu: "Hakika nilikuwa najua kwamba angetokea, lakini sikudhania kuwa angekuwa kutoka miongoni mwenu. Na ikiwa hayo uliyosema ni kweli, basi imekaribia mno atamiliki mahali hapa palipo chini ya miguu yangu hii. Na kama ningejua kuwa nitamfikia, basi ningekwenda mara moja kukutana naye. Na lau kama ningekuwa pamoja naye, basi bila shaka ningeiosha miguu yake." (Imepokelewa na Bukhari: 2941, na Abuu Daud: 5136).
Imesimuliwa kutoka kwa Hudhaifa, Mwenyezi Mungu amridhie, amesema: Al-'Aqib na Sayyid, watawala wa Najran, walimjia Mtume wa Mwenyezi Mungu hali ya kuwa wanataka kumfanyia laana. Mmoja wao akamwambia mwenzake, "Usilaaniane naye. Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu! Ikiwa yeye ni Nabii (wa kweli), kisha tukalaaniana naye, hatutafaulu, wala watoto wetu baada yetu." Kisha wote wawili wakasema (wakimwambia Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakika sisi tutakupa kile ulichotuomba, lakini umtume mtu mwaminifu pamoja nasi, wala usitume mtu yeyote pamoja nasi isipokuwa (mtu) mwaminifu." Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, akasema: "Hakika nitamtuma mwanaume mwaminifu mwenye kutegemewa pamoja nanyi." Kisha kila mmoja wa Maswahaba wa Mtume wa Allah rehema na amani zimshukie akatamani awe ni mwanaume huyo. Kisha Mtume akasema: "Simama, ewe Abuu 'Ubaida bin Jarrah." Aliposimama, Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie akasema: "Huyu ndiye mtu mwaminifu zaidi wa umma huu." (Imepokelewa na Bukhari: 4380, Muslim: 2420, Tirmidhi: 3796, na Ibn Majah: 135).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alimkunjia ardhi Mtume wetu, rehema na amani ziwe juu yake, na akaona hadi pale ambapo umiliki wa watu wake utafikia. Amesema rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika, Mwenyezi Mungu alinikunjia ardhi na nikaona Mashariki yake na Magharibi yake, na kwamba utawala wa umma wangu utafika pale nilipokunjiwa kwayo." (Imepokelewa na Muslim: 2889, Abuu Daud: 4252, Tirmidhi: 2176, na Ibn Maja 3952).
Na miongoni mwa ushahidi wa kuenea kwa ujumbe wake, rehema na amani ziwe juu yake, ni kusilimu kwa makasisi wengi wa Kiyahudi na watawa wa Kikristo, bali maelfu na maelfu ya Watu wa Kitabu (Mayahudi na Wakristo).
Na pia alipigana vita na Warumi, na akawaamuru Maswahaba wake kupigana vita dhidi ya Waajemi (Wairani) na Warumi baada yake.
Mlango wa maneno ya wapinzani wa utume na Mitume, amani iwe juu yao
Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na kadhalika tumemfanyia kila Nabii maadui mashetani wa kibinadam, na kijini, wakifundishana wao kwa wao maneno ya kupamba-pamba, kwa udanganyifu. Na angelipenda Mola wako Mlezi, wasingelifanya hayo. Basi waache na wanayoyazua." [Al-An'am: 112] Na amesema Mwenyezi Mungu Mwenye utajo mtukufu na majina matakatifu: "Na vivi hivi tumemfanyia kila Nabii adui miongoni mwa wakosefu, na Mola wako Mlezi anatosha kuwa Mwenye kuongoa na Mwenye kunusuru." [Al-Furqan: 31]
Na hekima ya Mwenyezi Mungu ilihitaji kwamba amuongoe amtakaye kwa fadhila zake, na ampoteze amtakaye kwa uadilifu wake, kama vile hekima yake ilivyohitaji kwamba kila Nabii awe na adui, na kwamba kati ya maadui hawa pawepo wasia juu ya batili, na kuafikiana katika maneno yao. Amesema Mtukufu: "Huambiwi ila yale yale waliyoambiwa Mitume wa kabla yako. Hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ni Mwenye maghfira, na ni Mwenye adhabu chungu." [Fusswilat:43] Kwa hivyo maneno ya wakuu katika kila umma yalikuwa yanafanana: Kuna wakati walikuwa wakisema: Huyu ni mchawi au kuhani au muongo, kama Firauni alivyomwambia Musa, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza juu yake katika maneno yake: "Na kwa yakini tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na uthibitisho ulio wazi * Kumwendea Firauni na Hamana na Qaruni, wakasema: Huyu ni mchawi, muongo mkubwa." [Ghafir: 23, 24] Wakati mwingine wanakanusha kuwa hakuwajia na ishara, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wakasema: Ewe Hud! Hujatuletea dalili ya wazi. Wala sisi hatuiachi miungu yetu kwa kufuata kauli yako. Na wala sisi hatukuamini wewe." [Hud: 53] Wakati mwingine wanadai kwamba anamzulia uongo Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu alisema akieleza juu ya maneno yao maovu: "Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi, wanasema: Huyu si chochote isipokuwa ni mtu anayetaka kuwazuia na yale waliyokuwa wakiabudu baba zenu. Na wakasema: Haya si chochote isipokuwa ni uongo uliozuliwa. Na wale waliokufuru waliiambia Haki ilipowajia: Haya si chochote isipokuwa ni uchawi ulio dhahiri." [Saba: 43]
Na wakati mwingine wanampa sifa za kuwa ni kichaa, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na walisema: Ewe uliyeteremshiwa Ukumbusho! Hakika wewe ni mwendawazimu." [Al-Hijr: 6] Mwenyezi Mungu aliyetakasika alisema akieleza kuhusu maneno yao: "(Firauni) akasema: Hakika huyu Mtume wenu aliyetumwa kwenu ni mwendawazimu." [Ash-Shu'ara: 27]. Na lipishwe mbali hilo na Mitume wa Mwenyezi Mungu, amani iwe juu yao, kwa kuwa wao ndio watu kamili kabisa katika akili, na wenye nyoyo safi zaidi.
Na wakati mwingine wanaona kuwa ni jambo kubwa mno kile anachowaitia Nabii wao, kama vile kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, amesema Mwenyezi Mungu akieleza juu ya maneno yao kuwa walisema: "Wakasema: Je, umetujia ili tumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na tuyaache yale waliyokuwa wakiyaabudu baba zetu? Basi tuletee hayo unayotuahidi, ikiwa wewe ni miongoni mwa wakweli." [Al-A'raf: 70] Na walisema: "Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu." [Swad: 5]
Na wakati mwingine wanaukataa wito wa Nabii; kwa sababu yeye ni binadamu kama wao. Amesema Mtukufu: "Na wakasema wakuu waliokufuru katika watu wake: Hatukuoni wewe isipokuwa ni mtu tu kama sisi." [Hud: 27] Na amesema Mtukufu: "Zimeghafilika nyoyo zao. Na wale waliodhulumu hunong'onezana kwa siri: Ni nani ati huyu isipokuwa ni binadamu tu kama nyinyi! Mnauwendea uchawi hali nanyi mnaona?" [Al-Anbiya: 3]
Na wakati mwingine wanawaomba vitu ambavyo haviko katika uwezo wa kiumbe, lakini hicho ni kiburi na ukaidi. Walimuomba Nabii wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, atibue chemchemi kutoka ardhini, au awe na kitalu, au aiangushe mbingu vipande vipande, au awaletee Mwenyezi Mungu na Malaika, au Nabii awe na nyumba ya mapambo, au apae mbinguni, na awateremshie kitabu, kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Na walisema: Hatutakuamini mpaka ututimbulie chemchem katika ardhi hii * Au uwe na kitalu cha mitende na mizabibu, na utupitishie mito kati yake ikimiminika * Au utuangushie mbingu vipande vipande kama ulivyodai; au utuletee Mwenyezi Mungu na Malaika uso kwa uso * Au uwe na nyumba ya dhahabu, au upae mbinguni. Wala hatutaamini kupaa kwako mpaka ututeremshie kitabu tukisome. Sema: Sub-haana Rabbi (Ametakasika Mola wangu Mlezi)! Kwani mimi ni nani isipokuwa ni mwanadamu na Mtume? * Na ni nini kilichowazuilia watu kuamini ulipowajia uongofu isipokuwa walisema: Je, Mwenyezi Mungu humtuma mwanadamu kuwa ni Mtume? * Sema: Ingelikuwa duniani wapo Malaika wanatembea kwa utulivu wao, basi bila ya shaka tungeliwateremshia Malaika kuwa ni Mtume wao." [Al-Israa: 90-95]
Na wakati mwingine wanamuomba Mtume awaletee kile anachowaahidi cha adhabu, Mwenyezi Mungu anasema: "Wakasema: Je, umetujia ili tumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na tuyaache yale waliyokuwa wakiyaabudu baba zetu? Basi tuletee hayo unayotuahidi, ikiwa wewe ni miongoni mwa wakweli." [Al-A'araf: 179], Na amesema Mtukufu: "Na wakamuuwa yule ngamia, na wakaasi amri ya Mola Mlezi wao, na wakasema: Ewe Saleh! Tuletee hayo unayotuahidi ikiwa wewe ni miongoni mwa Mitume." [Al-A'araf: 77].
Na wakati mwingine wanamshutumu Mtume kwa upotevu au upumbavu, kama katika kauli yao, ambayo Mwenyezi Mungu alitusimulia katika kauli yake Yeye Mwenye hekima: "Wakasema watukufu wa wale waliokufuru katika kaumu yake: Sisi tunakuona umo katika upumbavu, na hakika sisi tunakufikiria kuwa wewe ni katika waongo." [Al-A'araf: 66]
Na wakati mwingine wanaizuilia njia ya Mwenyezi Mungu na kuwaambia wafuasi wao: Msiisikilize Qur'ani hii, na timueni zogo ndani yake. Mwenyezi Mungu amesema: "Na wale waliokufuru walisema: Msiisikilize Qur'ani hii, na timueni zogo ndani yake, huenda mkashinda." [Fussilat: 6]
Na wakati mwingine wanamkadhibisha Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyoeleza juu ya hilo kuwa walisema: "Na hakika sisi tunakufikiria kuwa wewe ni katika waongo." Au wanamtuhumu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba anafundishwa tu na mwanadamu, na hayo yanayomjia sio ufunuo kutoka kwa Mwenyezi Mungu, anasema Mola Mtukufu: "Na Sisi hakika tunajua kwamba wanasema: Yuko mtu anayemfundisha. Lugha ya yule wanayemuelekezea ni ya kigeni, na hii ni lugha ya Kiarabu iliyo wazi." [An-Nahl: 103]
Na wanaweza pia kumuacha Mtume na kutomfuata ati kwa sababu wale waliomfuata ni wanyonge, kama katika kauli yake Mtukufu alipoeleza kuhusu kaumu ya Nuhu: "Na wakasema wakuu waliokufuru katika kaumu yake: Hatukuoni wewe isipokuwa ni mtu tu kama sisi, wala hatukuoni wamekufuata isipokuwa wale waliokuwa kwetu watu duni, wasio kuwa na akili. Wala hatukuoneni kuwa mna ubora wowote kutushinda sisi. Bali tuna hakika nyinyi ni waongo." [Hud: 27] Mfalme Hirakli alimwambia Abuu Sufian: “Na ni kakuuliza: Je, watu watukufu ndio wanamfuata yeye au wale walio dhaifu?” Wewe ukasema kwamba ni wanyonge miongoni mwao walimfuata, na wao ndio wafuasi wa Mitume." (Imepokelewa na Bukhari: 6227, na Muslim: 2841).
Na wakati mwingine huwafanyia Mitume masihara na kejeli, kama katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Mlikuwa mkimfanyia masihara Mwenyezi Mungu na Ishara zake na Mtume wake?" [At-Tauba: 65] Na kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na akawa anaunda jahazi, na kila wakipita wakuu wa kaumu yake wakimkejeli. Yeye akasema: Ikiwa nyinyi mnatukejeli, na sisi tunakukejelini kama mnavyotukejeli." [Hud: 38] Na wakati mwingine wanamhadaa Mtume, na wanatamani kwamba atajishusha chini akubaliane nao au kuwategemea, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyosema: "Wanatamani lau ungelainisha ili nao wakulainishie." [Al-Qalam: 9] Na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na lau kuwa hatukukuweka imara, hakika ungelikaribia kuwaelekea kidogo." [Al-Israa: 74]
Na wakati mwingine wanamkosoa na kumtia dosari Nabii, kama vile Firauni alivyomuambia Musa, amani iwe juu yake: "Au mimi si bora kuliko huyu aliye mnyonge, wala hawezi kusema waziwazi?" [Az-Zukhruf: 52]
Na kauli ya Abuu Sufian akiwaambia marafiki zake alipokuwa nao huko Sham kuhusiana na Mtume wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Basi nikawaambia marafiki zangu tulipotoka nje: Hakika jambo la bin Abi Kabsha limepata nguvu, kiasi kwamba hata mfalme wa Banu Asfar anamuogopa." (Imepokelewa na Bukhari: 4553, Muslim: 1773, na Tirmidhi: 2717).
Na wakati mwingine wakuu wanamtishia Mtume kwamba watamfukuza kutoka katika nchi hiyo, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusiana na kaumu ya Shuaib: "Wakasema wakuu waliotakabari katika kaumu yake wakasema: kuwaambia wale waliodhaifu wenye kuamini miongoni mwao.Je mtaitakidi ya kwamba Salehe ametumwa na mola wake? Hakika tunayaamini yale aliyotumwa kuyafikisha" [Al-A'araf: 75]
Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na wale waliokufuru wakawaambia Mitume wao: Tutawatoa katika nchi yetu, au lazima mrudi katika mila yetu." [Ibrahim: 13] Na watu wa Luti wakamwambia Luti na wale walioamini pamoja naye, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza kuhusu wao: "Wafukuzeni katika mji wenu, maana hao ni watu wanaojitakasa." [Al-A'araf: 82] Na makafiri wa Kikuraishi walimzingira Mtume wetu Muhammad rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na wale waliokuwa pamoja naye na Bani Hashim katika bonde kwa muda wa miaka mitatu, na wakamfukuza kutoka katika mji wake rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Imesimuliwa kutoka kwa bin Mas'ud, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipogawanya ngawira za (vita vya) Hunain, mwanaume mmoja miongoni mwa Maanswari alisema: "Hakutaka (yani Mtume) uso wa Mwenyezi Mungu katika ugawanyaji huu." Basi, nilimjia Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake nikamwambia habari hiyo, basi rangi ya uso wake ikabadilika, kisha akasema: "Mwenyezi Mungu amrehemu (Nabii) Musa. Kwa hakika, aliudhiwa kwa mengi zaidi ya haya, lakini akavumilia." (Imepokelewa na Bukhari: 4335, Muslim: 1062, na Tirmidhi: 3896).
Na watu wa Ibrahim, amani iwe juu yake, walijaribu kumchoma moto, lakini Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka akamuokoa, amesema Mola Mtukufu: "Basi halikuwa jawabu la watu wake isipokuwa ni kusema: Muuweni au mchomeni moto!" [Al-'Ankabut: 24] Na Mwenyezi Mungu amesema akieleza kuhusu kitendo cha wana wa Israeli walichowafanyia Manabii wao: "Basi kila mlipofikiwa na Mitume kwa yale ambayo hayapendwi na nafsi zenu, mlijivuna; wengine mkawakanusha, na wengine mkawauwa." [Al-Baqara: 87]
Huu ndio mwenendo wa watu wanaotakabari kwa Mitume wao, na huu ni utaratibu unaoendelea wanaoufuata wakuu wa watu katika kila umma wanavyowafanyia watu wanaotengeneza mambo.
Na Sunna (Utaratibu) wa Mwenyezi Mungu unaendelea kwa kuwanusuru Mitume na Manabii wake, rehema na amani ziwe juu yao. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Hakika bila ya shaka Sisi tunawanusuru Mitume wetu na wale walioamini katika uhai wa duniani na siku wataposimama Mashahidi." [Ghafir: 51] Na amesema Mtukufu: "Kisha tukawatimizia miadi, na tukawaokoa wao na tulio wataka, na tukawateketeza walio pita mipaka." [Al-Anbiya: 9]
Kitabu cha Siku ya Mwisho
Muhtasari wa Kitabu
Na tunaamini Siku ya Mwisho, na kuwa ni nguzo miongoni mwa nguzo sita za imani. Na imeitwa Siku ya Mwisho; kwa sababu ndiyo siku ya mwisho ya dunia hii, na hakuna siku nyingine (ya kidunia) baada yake. Na pia ina majina mengi, miongoni mwake ni: Siku ya Kiyama, Siku ya Ufufuo, Siku ya Hesabu, Siku ya Malipo, Siku ya Balaa kubwa, siku ya Tukio la haki, na Tukio, na (siku ya) Ukelele, (siku ya) msiba wa kufudikiza. Mwenyezi Mungu ametaja Siku ya Mwisho katika sehemu nyingi katika kitabu chake kitukufu.
Na katika kuamini Siku ya Mwisho ni kuamini ishara zake, yaani: Dalili za Kiyama, na pia kuamini kinachotokea baada ya kifo. Na tutaanza kuzungumza juu ya ishara za Kiyama, kisha yale yanayotokea baada ya kifo; kwa sababu hayo yanatokea kabla ya Siku ya Mwisho.
Alama za Kiyama ni ishara zinazoonyesha ukaribu wa Siku ya Mwisho, nazo ni katika ghaibu ambayo tuliamrishwa kuiamini.
Nazo ni sehemu tatu:
Ya kwanza: Ni dalili za Kiyama zilizokwishatokea na zikaisha, nazo ni nyingi mno.
Ya pili: Ni dalili za Kiyama zilizotokea, lakini hazijaisha, bado zinaendelea.
Ya tatu: Ni dalili ambazo bado hazijatokea, ambazo zitatokea kabla ya Kiyama na zitakuwa karibu nayo.
Na katika kuamini Siku ya Mwisho ni kuamini kwamba kila kitu kitaangamia isipokuwa uso wake Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, na kuwa Malaika wa kifo hutoa roho, na pia kuamini yote yatakayotokea baada ya kifo kama vile maiti kuulizwa maswali, na adhabu za kaburini na neema zake.
Na tunaamini kuwa wakati Mwenyezi Mungu atakapotoa idhini ya kuondoka kwa dunia hii na kuisha kwake, Mwenyezi Mungu atamuamrisha Malaika, naye atapuliza baragumu mpulizo wa kwanza, na kila aliye mbinguni na ardhini atazimia, isipokuwa amtakaye Mwenyezi Mungu. Kisha Mwenyezi Mungu atateremsha mvua ambayo kwayo miili ya viumbe itaota, kisha Mwenyezi Mungu atampa idhini Malaika atapuliza baragumu mpulizo wa pili, kisha watafufuliwa kutoka makaburini mwao, na watu watasimama mbele ya Mola Mlezi wa walimwengu wote. Na wa kwanza ambaye ardhi itapasuka atoke ni Nabii wetu, rehema na amani zimshukie. Na wa kwanza atakayezinduka ni Nabii wetu, rehema na amani zimshukie. Na wa kwanza atakayevishwa nguo ni Nabii wa Mwenyezi Mungu, Ibrahim rafiki mwandani wa Mwingi wa rehema. Na watu watakusanywa pekupeku, uchi, bila kutahiriwa, na ardhi ya kukusanywa viumbe juu yake itakuwa nyeupe.
Na tunaamini uombezi wa Mtume wetu, rehema na amani ziwe juu yake, na tunaamini kuonyeshwa matendo, hesabu na malipo, na kwamba yeye Aliyetakasika na kutukuka, ni mwepesi wa hesabu. Hesabu ya Mwenyezi Mungu kwa waja wake ina viwango na hali tofauti, miongoni mwa waja kuna wale watakaohesabiwa hesabu ngumu, na miongoni mwao wapo watakaohesabiwa hesabu nyepesi, na miongoni mwa waumini wapo watakaoingia Peponi bila ya kuhesabiwa.
Hakuna atakayedhulumiwa siku hiyo, na wa kwanza kuhesabiwa siku ya Kiyama ni umma wa Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, na la kwanza kuhukumiwa kati ya watu ni umwagaji damu.
Na tunaamini kwamba siku hii wataletwa mashahidi, na Malaika watashuhudia, na ardhi itashuhudia waliyoyafanya waja juu yake, na pia viungo vitashuhudia.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu ataweka mizani ya kweli kwa ajili ya kupima matendo ya waja.
Na tunaamini kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie ana hodhi (birika kubwa) ambalo umma wake watakunywa humo, kisha waja watapelekwa ima Peponi au Motoni – Mwenyezi Mungu atuepushe mbali na hilo – na daraja litawekwa juu ya Jahannam, na kutakuwa na ndoana mfano wa miiba ya mti wa Saadan. Miba hiyo itawakamata watu kulingana na matendo yao, na wa kwanza kuvuka daraja hilo ni Mtume wetu Muhammad rehema na amani ziwe juu yake.
Kitabu cha Uthibitisho wa kuamini Siku ya Mwisho
Na tunaamini Siku ya Mwisho, ambayo ni moja ya nguzo sita za imani zilizotajwa katika maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sio wema kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa Mashariki na Magharibi. Bali wema ni wa anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho." [Al-Baqara: 177] Na kwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lakini waliobobea katika elimu miongoni mwao, na Waumini, wanayaamini uliyoteremshiwa wewe, na yaliyoteremshwa kabla yako. Na wanaoshika Swala, na wakatoa Zaka, na wanaomuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, hao tutawapa malipo makubwa." [An-Nisa: 162]
Na hilo linaashiriwa na hadithi ya Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa amekaa nje kwa ajili ya watu, kisha mwanaume mmoja akamjia, na akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nini Imani?" Akasema: "Ni umuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Kitabu chake, na kukutana naye, na Mitume wake, na kuamini ufufuo wa mwisho.” Imepokelewa na Bukhari: 4777, Muslim: 9, na Ibn Majah: 64).
Na zimejulisha juu ya hilo dalili za kiakili, kama kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo atakayeihuisha mifupa nayo imekwishamung'unyika? * Sema: Ataihuisha huyo huyo aliyeiumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba." [Yasin: 78, 79], Na katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu! Ikiwa nyinyi mna shaka ya kufufuliwa, basi kwa hakika Sisi tuliwaumba kutokana na udongo, kisha kutokana na manii, kisha kutokana na kipande cha damu iliogandana, kisha kutokana na kipande cha nyama chenye umbo na kisichokuwa na umbo, ili tuwabainishie. Nasi tunakiweka katika matumbo ya uzazi tunachokitaka mpaka muda uliowekwa. Kisha tunawatoa kwa hali ya mtoto mchanga, kisha mfikie kutimia akili. Na wapo katika nyinyi wanaokufa, na wapo katika nyinyi wanaorudishwa kwenye umri wa unyonge kabisa, hata mtu awe hajui kitu baada ya kuwa anakijua. Na unaiona ardhi imetulia kimya, lakini tunapoyateremsha maji juu yake, husisimka na kututumka, na kumea kila namna ya mimea mizuri." [Al-Hajj: 5], Na kauli yake Mola wa kweli Mtukufu, Mwenye majina matakatifu: "Je, ni vigumu zaidi kuwaumba nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliyeijenga!" [An-Nazi'at: 27]. Na kauli yake Aliyetakasika na kutukuka: "Na katika Ishara zake ni kwamba unaiona ardhi nyonge, lakini tunapoiteremshia maji, mara unaiona inataharaki na kuumuka. Bila ya shaka yule aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu. Hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu." [Fussilat: 39]. Na kauli yake Mtukufu, Mwenye majina Matukufu: "Na Yeye ndiye anayeanzisha uumbaji, kisha ataurudisha mara nyingine. Na jambo hili ni jepesi zaidi kwake." [Ar-Rum: 27]. Na kauli yake Mwenyezi Mungu Aliyetukuka: "Kama tulivyoanza umbo la mwanzo, tutalirudisha tena. Ni ahadi iliyo juu yetu. Hakika Sisi ni watendao." [Al-Anbiya: 104].
Na imeitwa Siku ya Mwisho; kwa sababu ndiyo siku ya mwisho ya dunia hii, na hakuna siku nyingine (ya kidunia) baada yake. Na pia ina majina mengi. Na miongoni mwa majina yake ni Siku ya Kiyama, Siku ya Ufufuo, Siku ya Hesabu, Siku ya Malipo, Siku ya Balaa kubwa, siku ya Tukio la haki, na Tukio, na (siku ya) Ukelele, (siku ya) msiba wa kufudikiza. Mwenyezi Mungu ametaja Siku ya Mwisho katika sehemu nyingi katika kitabu chake kitukufu. Kama kauli yake Mtukufu: "Siku watakapomsimamia watu Mola Mlezi wa walimwengu wote?" [Al-Mutaffifin: 6]. Na kauli yake Mwenye sifa tukufu: "Siku watakapotoka makaburini upesi kana kwamba wanakimbilia mfundo (bendera)." [Al-Ma'arij: 43], Na kauli yake Mwenye sifa tukufu: "Basi itakapofika hiyo balaa kubwa." [An-Nazi'at: 34]. Na kauli yake: "Basi utakapokuja ukelele * Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye * Na mamaye na babaye * Na mkewe na wanawe * Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha." [Abasa: 33-37], Na kauli yake: "Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi, hakika tetemeko la ardhi ni jambo kubwa * Siku mtakapoiona, kila mwenye kunyonyesha atamsahau amnyonyeshaye, na kila mwenye mimba ataharibu mimba yake. Na utaona watu wamelewa, na kumbe hawakulewa. Lakini adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali." [Al-Hajj: 1, 2]. Na kauli yake Mwenye utukufu mkubwa, Mwenye mamlaka makubwa: "Siku atakayowakusanya kwa ajili ya Siku ya Mkusanyiko; hiyo ni siku ya kupunjana." [At-Taghabun: 9].
Mlango wa kuamini dalili za Kiyama
Na katika kuamini Siku ya Mwisho ni kuamini ishara zake ambazo ni ishara zinazoonyesha ukaribu wa Siku ya Mwisho, kama alivyosema Aliyetakasika na kutukuka: "Kwani wanangojea jengine isipokuwa iwafikie Saa (ya Kiyama) kwa ghafla? Na hakika alama zake zimekwishakuja?" [Muhammad: 18] Nazo ni katika ghaibu ambayo tuliamrishwa kuziamini.
Na miongoni mwa ishara za Saa ya Kiyama ni zile ambazo zilidhihiri na kumalizika, nazo ni nyingi sana, na miongoni mwazo ni kauli yake Mtume rehema na amani zimshukie: "Nimetumwa mimi ilhali Saa (ya Kiyama) ni kama hiki kutoka kwa hiki - au - ni kama viwili hivi." Na akaunganisha baina ya kidole cha shahada na kidole cha kati. (Imepokelewa na Bukhari: 6227, na Muslim: 2841). Na kauli yake Mtume rehema na amani zimshukie: "Hesabu mambo sita kabla ya Saa (ya Kiyama): Kufa kwangu, kisha kuifungua Baitul-Maqdis, kisha vifo vingi vitakavyotokea miongoni mwenu kama vile magonjwa yanayowasibu na kuwauwa kondoo, na mali itamiminika kwa wingi mpaka mtu atapewa dinari mia moja, naye atashinda amekasirika." (Imepokelewa na Bukhari: 3176, na Ibn Majah: 4042). Na kauli yake rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Saa (ya Kiyama) haitasimama mpaka makundi mawili makubwa yapigane na kutakuwa na mauaji mengi baina yao, na dini yao itakuwa ni moja, na (haitasimama) mpaka watakapotokea waongo wakubwa karibia thelathini (30), na kila mmoja wao atadai kuwa yeye ni mtume wa Mwenyezi Mungu, na (haitasimama) mpaka elimu itakapoondolewa (kwa kufa wanazuoni wa kidini) na matetemeko ya ardhi yatakithiri, na nyakati zitakaribiana, majaribio yatadhihirika, mauaji yatakuwa mengi, na mpaka mali itakapokithiri miongoni mwenu na imiminike mpaka mtu mwenye mali apatwe na wasiwasi mkubwa kwamba hakuna mtu atakayekubali sadaka yake, na mpaka atakapompelekea, naye huyo aliyepewa atasema: Mimi sina haja nayo. na mpaka watu watakaposhindana katika kujenga majengo marefu." (Imepokelewa na Bukhari: 7121, Muslim: 157, na Tirmidhi: 2218).
Na miongoni mwa ishara za Kiyama ni zile zilizotokea, lakini hazijaisha, bado zinaendelea. Na miongoni mwa hizo ni kutokea kwa (Fitina) majaribio katika umma. (Kuna hadithi nyingi katika vitabu viwili vya hadithi sahihi kuhusu fitina, lakini sio moja kwa moja kwamba fitina ni miongoni mwa alama za Kiyama. Ndiyo maana tukataja Hadithi mbili zifuatazo kutoka katika Sunan: Kwa sababu zote mbili zimetaja hilo moja kwa moja.) Nazo ni nyingi, amesema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika kabla ya Kiyama kuna majaribio makubwa kama vile vipande vya usiku wa giza, mtu atakuwa Muumini asubuhi na anafika jioni akiwa ni kafiri, na atafika jioni ni Muumini na anafika asubuhi akiwa ni kafiri. Mwenye kuketi chini ndani ya wakati huo ni bora kuliko mwenye kusimama. Na mwenye kutembea ndani yake ni bora kuliko mwenye kukimbia. Basi vunjeni pinde zenu, na kateni kamba za pinde zenu, na zipigeni panga zenu juu ya mawe, na mmoja wenu akiingiliwa - na majaribio hayo -, basi na awe kama yule mbora wa wale wana wawili wa Adam.” (Imepokelewa na Abuu Daud: 4259, Tirmidhi: 2204, Ibn Majah: 3961, Ibn Abī Shaiba: 30978, Ahmad: 19662, na Ar-Rawyānī: 585).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Kutakuwa na fitina kabla ya Kiyama kama vipande vya usiku wa giza. Mtu atafika asubuhi ndani yake akiwa ni Muumini na anafika jioni akiwa ni kafiri. Na atafika jioni akiwa ni Muumini na anafika asubuhi akiwa ni kafiri. Watu watauza dini yao kwa ajili ya pumbao tu ya kidunia." (Imepokelewa na Tirmidhi: 2197, Ibn Abī Shaiba katika Al-Muṣwannaf: 31053 na katika Al-Iman: 64, na Al-Faryabi katika Swifatun-Nifaa wa-dhammil-Munafiqiin 97).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakitosimama Kiyama mpaka watumwe waongo wakubwa karibia thelathini, kila mmoja wao akidai kuwa yeye ni Mtume wa Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari: 7121, Muslim: 157, na Tirmidhi: 2218).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Wakati mmoja Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa katika mkusanyiko mmoja akiwahadithia kaumu fulani, bedui mmoja alimjia na akasema: "Saa ya Kiyama itakuwa lini?" Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake akaendelea tu kuzungumza. Basi baadhi ya watu wakasema: "(Mtume) amesikia alichosema na akakichukia hicho alichosema." Na baadhi yao wakasema: "Bali (Mtume) hakusikia." Mpaka (Mtume) alipomaliza mazungumzo yake, akasema: "Yuko wapi - ninaona alisema - aliyeuliza juu ya Saa ya Kiyama?" (bedui huyo) Akasema: "Mimi hapa, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu!" (Mtume) akasema: "Uaminifu utakapopotezwa, basi ingonjee Saa." (bedui) akasema: "Je, utapotezwaje?" (Mtume) akasema: "Wakati uongozi utakapopewa wasioustahili, basi ingojee Saa." (Imepokelewa na Bukhari: 3191).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakika, miongoni mwa alama za Saa ya Kiyama ni elimu kuondolewa, na ujinga kuwa thabiti, na pombe kunywewa, na kudhihiri zinaa.” (Imepokelewa na Bukhari: 80, Muslim: 2671, Tirmidhi: 2205, na Ibn Majah: 4045).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakika, karibu na kusimama kwa Saa ya Kiyama, kutakuwa na siku ambazo ujinga utaenea, na elimu itanyanyuliwa, na mauaji yatakithiri ndani yake." (Imepokelewa na Bukhari: 7062, Muslim: 2672, Tirmidhi: 2200, na Ibn Majah: 3959, 4050).
Na miongoni mwa alama za Kiyama ni zile ambazo bado hazijatokea, ambazo zitatokea kabla tu ya Saa ya Kiyama na zitakuwa karibu nayo. Miongoni mwake ni kushuka kwa Masihi Isa bin Maryam, amani iwe juu yake, amesema Mwenyezi Mungu tukufu: "Na hakuna yeyote katika Watu wa Kitabu isipokuwa hakika atamuamini yeye kabla ya kufa kwake. Naye Siku ya Kiyama atakuwa shahidi juu yao." [An-Nisa: 159] Na kutokea kwa Ya'juju na Maajuju. Amesema Mtukufu: "Mpaka watapo funguliwa Ya'juju na Ma'ajuju wakawa wanateremka kutoka kila mlima." [Al-Anbiya: 96] Na kutokea kwa mnyama, amesema Mtukufu: "Na itakapowaangukia kauli juu yao, tutawatolea mnyama katika ardhi atakayewasemesha, ya kuwa watu walikuwa hawana yakini na Ishara zetu." [An-Naml: 82]
Imesimuliwa kutoka katika hadithi ya Hudhaifa bin Usaid Al-Ghifarii kuwa alisema: Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alituangalia (siku moja) hali ya kuwa tunakumbushana. Akasema: "Mnakumbushana nini?" Wakasema: "Tunakumbushana Saa ya Kiyama." Akasema: "Hakika, saa haitasimama mpaka muone kabla yake ishara kumi." Kisha, akataja moshi, Dajjal, mnyama, jua kuchomozea Magharibi yake, kushuka kwa Isa bin Mariam, amani iwe juu yake, Yaajuju na Ma'ajuju, mitetemeko mitatu ya ardhi: mtetemeko mmoja huko Mashariki, na mtetemeko mmoja huko Magharibi, na mtetemeko mmoja katika Bara la Arabu, na ya mwisho wa ishara hizo ni moto utakaotokea Yemen ambao utawafukuza watu kwenda katika mahali pao ya kukusanyika (huko Sham)." (Imepokelewa na Muslim: 2901, Abuu Daud 4311, Tirmidhi: 2183, na Ibn Majah: 4041).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakitosimama Kiyama mpaka jua litakapochomozea Magharibi mwake. Litakapochomozea Magharibi mwake, watu wote kwa pamoja wataamini, na siku hiyo ndiyo "kuamini hapo hakutomfaa mtu kitu, ikiwa hakuwa ameamini kabla yake." [Al-An'am: 158] (Imepokelewa na Bukhari: 4635, Muslim: 157, Abuu Daud: 4312, na Ibn Majah: 4068).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Ninaapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mikono mwake! Kwa hakika mwana wa Mariam (yani Nabii Isa) amekaribia mno kuteremka kwenu nyinyi (Waislamu) huku akiwa ni mtawala (kiongozi) muadilifu. Atavunja msalaba na kuwaua nguruwe na kukomesha ulipaji wa Jizia (kodi inayolipwa na wasiokuwa Waislamu, ambao wanaishi chini ya ulinzi wa serikali ya Kiislamu). Kisha kutakuwa na wingi wa mali hadi hakutakuwa na mtu yeyote atakayekubali (kuchukuwa kama sadaka)." (Imepokelewa na Bukhari: 2222, Muslim: 155, Abuu Daud: 4324, Tirmidhi: 2233, na Ibn Majah: 4078).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Mwenyezi Mungu hakumtuma Nabii yeyote isipokuwa alionya kaumu yake dhidi ya yule muongo mkubwa ambaye ni chongo (yani Dajjal). Hakika yeye ni chongo, na Mola wenu Mlezi si chongo, na imeandikwa kati ya macho yake mawili 'Kafiri (yani kafiri)'." (Imepokelewa na Bukhari: 7408, Muslim 2933, Abuu Daud: 4316, na Tirmidhi: 2245).
Mlango wa kuamini yale yatakayotokea baada ya kifo
Na tunaamini kwamba katika kuamini Siku ya Mwisho ni kuamini kuwa kila kitu kitaangamia isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, yeye Aliyetakasika, na kutukuka, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyosema: "Kila kitu kitaangamia isipo kuwa Yeye." [Al-Qasas: 88] Na amesema Mola Mtukufu: "Kila kilichoko juu yake kitatoweka * Na atabakia Mwenyewe Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu." [Ar-Rahman: 26, 27], Na kuwa Malaika wa mauti atatoa roho, amesema Mola wa haki, Mtukufu: "Sema: Atawafisha Malaika wa mauti aliyewakilishwa juu yenu; kisha mtarejeshwa kwa Mola wenu Mlezi." [As-Sajda:11]
Na tunaamini kile kitakachotokea baada ya kifo, kama vile maiti kuulizwa maswali, na adhabu ya kaburini na furaha yake, kama ilivyo katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wanaonyeshwa Moto asubuhi na jioni. Na itakapofika Saa ya Kiyama, patasemwa: Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali kabisa!" [Ghafir: 46], Na kauli yake Mtukufu: "Tutawaadhibu mara mbili, kisha watarudishwa kwenye adhabu kubwa." [At-Tauba: 101] Na kauli yake Mtukufu: "Na laiti ungeliona Malaika wanapowafisha wale waliokufuru, wakiwapiga nyuso zao na migongo yao, na kuwaambia: Ionjeni adhabu ya Moto wenye kuunguza! * Hayo ni kwa sababu ya yale yaliyokwishatangulizwa na mikono yenu, na hakika Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja." [Al-Anfal: 50,51] Na kauli yake Mtukufu: "Na lau ungeliwaona madhalimu wanavyokuwa katika mahangaiko ya mauti, na Malaika wamewanyooshea mikono wakiwambia: Zitoeni roho zenu! Leo mtalipwa adhabu ya fedheha kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyasema juu ya Mwenyezi Mungu yasiyo ya haki, na mlivyokuwa mkizifanyia kiburi Ishara zake." [Al-An'am: 93] Na kauli yake Mtukufu: "Na hakika wale waliodhulumu watapata adhabu nyingine isiyokuwa hii." [At-Tur: 47]
Imesimuliwa kutoka Al-Baraa bin ‘Azib kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: "Mwenyezi Mungu huwatia imara wenye kuamini kwa kauli imara." [Ibrahim: 27] Akasema: Ilishuka kuhusiana na adhabu ya kaburi. (Maiti) Ataambiwa: "Ni nani Mola wako Mlezi?" Atasema: "Mola wangu Mlezi ni Mwenyezi Mungu, na Nabii wangu ni Muhammad." Na hiyo ndiyo kauli yake Mwenyezi Mungu Mwenye Nguvu, Mtukufu: "Mwenyezi Mungu huwatia imara wenye kuamini kwa kauli imara katika maisha ya dunia na katika Akhera." [Ibrahim: 27]. (Imepokelewa na Bukhari: 1369, Muslim: 2871 na matamshi haya ni yake, Tirmidhi 3120, An-Nasai: 2056, 2057 na Ibn Majah: 4269, 4750).
Na imesimuliwa na bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akiwafundisha dua hii kama alivyokuwa akiwafundisha sura ya Qur'ani. Alikuwa akisema: "Semeni, "Allahumma innaa na'udhu bika min 'adhabi Jahannam, wa 'audhu bika min 'adhabil-qabri, wa 'audhu bika min fitnatil-masihid-Dajjal, wa 'audhu bika min fitnatil-mahyaa wal-mamaat (Ewe Mwenyezi Mungu! Hakika sisi, tunajikinga kwako kutokana na adhabu ya Jahannam, na ninajikinga kwako kutokana na adhabu ya kaburi, na ninajikinga kwako kutokana na fitina ya Masihi Dajjal, na ninajikinga kwako kutokana na fitina ya uhai na mauti)." (Imepokelewa na Muslim: 590, Abu Daud 1542, Tirmidhi: 3494, An-Nasai: 2063, na Ibn Majah: 3840).
Na imesimuliwa kutoka bin Abbas kuwa alisema: Siku moja, Mtume rehema na amani za Allah zimshukie, alipokuwa anapita katika moja ya maeneo ya makaburi ya Madina, alisikia sauti za watu wawili ambao walikuwa wanaadhibiwa ndani ya makaburi yao. Mtume, rehema na amani za Allah zimshukie, akasema: "Hakika watu hawa wawili wanaadhibiwa, nao hawaadhibiwi kwa sababu ya dhambi kubwa. Nalo kwa hakika ni dhambi kubwa. Mmoja wao alikuwa hajihifadhi kutokana na mkojo wake, na mwingine alikuwa akieneza fitina." Kisha Mtume rehema na amani za Allah zimshukie, akaomba shina la mitende na akalivunja vipande viwili na kuweka kwenye kila kaburi kipande kimoja, na akasema: "Nina matumaini kwamba watapunguziwa adhabu zao kabla havijakauka." (Imepokelewa na Bukhari: 6055, Muslim: 292, Abu Daud: 20, Tirmidhi: 70, An-Nasai: 31, na Ibn Majah: 347).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Sa'id, alisema: Nilisimuliwa na Zaidi bin Thabit, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: (Siku moja) Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipokuwa ndani ya bustani moja ya Banu Najjar, akiwa juu ya nyumbu wake hali ya kuwa tuko pamoja naye, tazama! (nyumbu huyo) alijipinda kutoka kwenye njia na akawa karibu kumtupa chini. Na tazama! Kulikuwa na makaburi sita, au matano au manne. (Ibn 'Ulayyah) Alisema: "Hivyo ndivyo (Sa'id) Al-Jurairii alivyokuwa akisema." (Mtume) Akasema: "Ni nani anawajua wenye haya makaburi?" Mwanaume mmoja akasema: "Mimi." (Mtume) Akasema: "Je, hawa walikufa lini?" Akasema: "Walikufa katika (zama za) ushirikina." Akasema: "Hakika, huu umma utapewa mitihani ndani ya makaburi yao. Na lau tu si kwamba hamtazikana, basi ningemuomba Mwenyezi Mungu awasikizishe katika adhabu ya kile ambacho ninasikia kutoka humo (makaburini)." Kisha, akatuelekea kwa uso wake na akasema: "Jilindeni kwa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya Moto." Wakasema: "Tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya Moto." Akasema: "Jilindeni kwa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya kaburi." Wakasema: "Tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na adhabu ya kaburi." Akasema: "Jilindeni kwa Mwenyezi Mungu kutokana na majaribio yake ya dhahiri na ya siri yake." Wakasema: "Tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na majaribio yake ya dhahiri na ya siri." Akasema: "Jilindeni kwa Mwenyezi Mungu kutokana na majaribio ya Dajjal." Wakasema: "Tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na majaribio ya Dajjal." (Imepokelewa na Muslim: 2203).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Ayub kuwa alisema: Siku moja Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alitoka baada ya jua kuzama na akasikia sauti (ya kutisha) akasema: "(Hao ni) Mayahudi wanaoadhibiwa ndani ya makaburi yao." (Imepokelewa na Bukhari: 1375, Muslim: 2869, na An-Nasai: 2059).
Na imesimuliwa kutoka kwa 'Aisha, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Wanawake wawili ajuza miongoni mwa maajuza wa Kiyahudi wa Madina waliingia kwangu na wakaniambia: "Hakika watu wa makaburini huadhibiwa ndani ya makaburi yao." Mimi nikawapinga, na halikunifurahisha kuwasadikisha. Walipotoka, Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akaingia kwangu nikasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Hakika wanawake wawili ajuza (wazee)...." na nikamwambia hadithi hiyo yote. Akasema: "Wawili hao wamesema kweli. Hakika wafu huadhibiwa adhabu ambayo wanyama wote huisikia." Tangu wakati huo sikuwahi kumuona katika swala isipokuwa anajilinda (kwa Mwenyezi Mungu) kutokana na adhabu ya kaburini. (Imepokelewa na Bukhari: 6366, Muslim: 586, na An-Nasai: 2067).
Na kama vile kafiri, mnafiki, na baadhi ya Waislamu wanaofanya madhambi wataadhibiwa makaburini mwao, vivyo hivyo Muumini ataneemeshwa kaburini. Imesimuliwa kutoka kwa Anas bin Malik, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba aliwahadithia kuwa: Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: “Hakika mja anapowekwa kaburini mwake, na marafiki zake wakarudi, basi husikia sauti ya viatu vyao, Malaika wawili humjia na kumketisha, kisha wanamwambia: "Ulikuwa ukisema nini kuhusu huyu mtu" - Yaani: Muhammad? Ama Muumini, atasema: "Ninashuhudia kuwa yeye ni mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake." Kisha wanamwambia: "Angalia mahali pako Motoni, Mwenyezi Mungu amekupa nafasi nyingine badala yake Peponi." Basi, anaziona sehemu zake zote mbili." Akasema: "Ama mnafiki au kafiri, ataambiwa: "Je, ulikuwa ukisema nini kuhusu mtu huyu- yaani Muhammad?" Atasema: "Sijui. Lakini nilikuwa nikisema walichokuwa wakisema watu." Basi, ataambiwa: "Haukujua wala hukufuata." Kisha atapigwa kipigo kimoja kwa nyundo za chuma, na atapiga kelele ambayo kila kitu kilichoko karibu naye kitasikia, isipokuwa majini na wanadamu." (Imepokelewa na Bukhari: 1374, na Muslim: 1374).
Mlango wa kuamini ufufuo na kitakachotokea baada yake
Na tunaamini kuwa wakati Mwenyezi Mungu atakapotoa idhini ya kuondoka kwa dunia hii na kuisha kwake, Mwenyezi Mungu atamwamrisha Malaika, naye atapuliza baragumu, na kila aliye mbinguni na ardhini atazimia, isipokuwa amtakaye Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na litapulizwa barugumu, wazimie waliomo mbinguni na waliomo katika ardhi, isipokuwa aliyemtaka Mwenyezi Mungu. Kisha litapulizwa mara nyingine. Hapo, watainuka wawe wanangojea." [Az-Zumar: 68]. Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Kisha, litapulizwa baragumu na hakuna (mtu) yeyote atakayelisikia isipokuwa ataangukia upande mmoja wa shingo lake na ainue upande wake mwingine wa shingo lake." Amesema: "Na wa kwanza kuisikia ni mtu mmoja atakayekuwa analishughulikia hodhi la ngamia wake. Kisha, atazimika, kisha watu wote watazimika." (Imepokelewa na Muslim: 2940). (Neno (rafa' laitan) linamaanisha kuwa ataangukia upande mmoja wa shingo yake na ainue upande wake mwingine wa shingo yake. An-Nihayat fii Gharib al-Hadith (3/33).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "... Na hakika Saa itasimama hali ya kuwa wanaume wawili wanataka kuuziana nguo zao, lakini hawatauziana wala kuzikunja (kabla ya Saa kusimama). Na hakika Saa itasimama hali ya kuwa mtu mmoja ameshaondoka na maziwa ya ngamia wake, lakini wala hatayaonja. Na hakika Saa itasimama hali ya kuwa analitengeneza hodhi lake, lakini hatawanywesha humo. Na hakika Saa itasimama hali ya kuwa mmoja wenu amekiinua chakula chake hadi mdomoni mwake, lakini hatokila."
Hivyo Mwenyezi Mungu atamwangamiza amtakaye katika viumbe vyake, kwa wale walioandikiwa kutoweka na kuangamia, mpaka kisibaki chochote isipokuwa Yeye wa Haki, aliyetakasika, na kutukuka. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kila kilichoko juu yake kitatoweka * "Na atabakia Mwenyewe Mola wako Mlezi Mwenye utukufu na ukarimu." [Surat Ar-Rahman: 26, 27], Na amesema Mtukufu: "Wala usimuombe pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwinginewe. Hapana mungu isipokuwa Yeye. Kila kitu kitaangamia isipokuwa Yeye. Hukumu iko kwake, na kwake mtarejeshwa." [Suratul-Qasas: 88], Na amesema Mtukufu: "Siku watakayodhihiri wao. Hapana kitachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu Mmoja Mshindi." [Surat Ghafir: 16].
Kisha Mwenyezi Mungu atateremsha mvua ambayo kutokana na mvua hiyo miili ya viumbe itachipuka, kama alivyosema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Kisha Mwenyezi Mungu atatuma - au alisema: atateremsha - mvua kama umande - au: kivuli - Nuuman (ambaye ni mmoja wa wapokezi wa Hadithi hii ndiye alikuwa na shaka hii). kwa hivyo miili ya watu itaota kutokana na mvua hiyo. Kisha litapulizwa tena, na tazama, watainuka wawe wanangojea..." (Imepokelewa na Muslim: 2940).
Kisha Mwenyezi Mungu atamwamuru Malaika, naye atapuliza baragumu kupuliza kwa mara ya pili, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyosema: "Kisha litapulizwa mara nyingine. Hapo, watainuka wawe wanangojea." [Suratul Az-Zumar:68]
Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alibainisha muda ulio kati ya kupulizwa kwa mabaragumu hayo mawili. Na kutoka kwa Abuu Huraira radhi za Allah ziwe juu yake amesema: Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Kati ya kupulizwa kwa kwanza na kwa pili kwa baragumu kutakuwa na (miaka) arobaini. Kisha akasema: "Kila kitu cha mwili wa mwanadamu kitaoza isipokuwa kifandugu (kifupa cha mwisho cha uti wa mgongo) chake, na kutokana na hicho, Mwenyezi Mungu atauunganisha mwili wake." (Imepokelewa na Bukhari: 4814, na Muslim: 2955).
Na tunayaamini yale aliyotueleza Nabii wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, kuhusu hali ya mbingu na ardhi siku ya Kiyama, kama ilivyo katika Hadithi ya bin Mas'ud, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mwalimu mmoja miongoni mwa walimu wa Kiyahudi alimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, na akasema: "Ewe Muhammad! Hakika sisi tunajifunza kwamba Mwenyezi Mungu ataziweka mbingu zote juu ya kidole kimoja, na ardhi zote juu ya kidole kimoja, na miti juu ya kidole kimoja, na maji na mchanga juu ya kidole kimoja, na vitu vingine vyote vilivyoumbwa juu ya kidole kimoja, kisha atasema: "Mimi ndiye Mfalme." Basi, Mtume rehema na amani zimshukie, akatabasamu kiasi kwamba magego yake yakaonekana katika hali ya kuyasadikisha maneno ya huyo mwalimu wa Kiyahudi. Kisha Mtume rehema na amani zimshukie akasoma: "Na wala hawakumheshimu Mwenyezi Mungu kama anavyostahiki kadiri yake. Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume. Sub-hanahu wa Taa'la (Ametakasika na Ametukuka) na hayo wanayomshirikisha nayo." [Az-Zumar: 67]. (Imepokelewa na Bukhari: 4811, Muslim: 2786, na Tirmidhi: 3238).
Na tunaamini kwamba watu watafufuliwa kutoka makaburini mwao, kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu atawahuisha wafu litakapopulizwa baragumu kwa mara ya pili. Kisha watu watasimama mbele ya Mola Mlezi wa walimwengu wote, kama alivyosema Mwenyezi mungu Mtukufu: "Kisha hakika nyinyi baada ya hayo mtakufa * "Kisha hakika nyinyi Siku ya Kiyama mtafufuliwa." [Al-Muminun:15,16] Na amesema Mtukufu: "Na litapulizwa baragumu, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao Mlezi * Watasema: Ole wetu! Ni nani aliyetufufua kwenye malazi yetu? Haya ndiyo aliyoyaahidi Mwingi wa Rehema na Mitume wakasema ukweli* Haitakuwa isipokuwa ukelele mmoja tu, mara wote watahudhuruishwa mbele yetu." [Yasin: 51-53].
Na amesema Mtukufu: "Na Sisi ndio tunaohuisha na tunaofisha. Na Sisi ndio Warithi * Na tunawajua wale waliotangulia katika nyinyi, na tunawajua waliochelewa) * Na hakika Mola wako Mlezi ndiye atakayewakusanya. Hakika Yeye ni Mwenye hekima na Mjuzi." [Al-Hijr: 23-25]
Na amesema Mtukufu: "Na walisema: Je, tutakapokuwa mifupa na mapande yaliyovurugika, tutafufuliwa kwa umbo jipya? * Sema: Kuweni hata mawe au chuma * Au umbo lolote mnalo liona kubwa katika vifua vyenu. Watasema: Ni nani atakayeturudisha tena? Sema: Yule yule aliyewaumba mara ya kwanza! Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Lini hayo? Sema: 'Asaa (nataraji) yakawa karibu! * Siku atakapowaita, na nyinyi mkamuitikia kwa kumshukuru, na mkadhani kuwa hamkukaa isipokuwa muda mdogo tu." [Al-Israa:49-52] Na amesema Mtukufu: "Na anayemuongoza Mwenyezi Mungu, basi huyo ndiye aliyeongoka. Na anaowapotoa, basi hutowapatia walinzi badala yake. Na tutawakusanya Siku ya Kiyama hali wakikokotwa juu ya nyuso zao, nao ni vipofu na mabubu na viziwi. Na makaazi yao ni Jahannamu. Kila moto ukifanya kusinzia, tutazidi kuuchochea uwake kwa nguvu * Hayo ni malipo yao kwa sababu walizikataa ishara zetu, na wakasema: Hivyo tukishakuwa mifupa na mapande yaliyovurugika, tutafufuliwa kwa umbo jipya? * Kwani hawakuona ya kwamba Mwenyezi Mungu aliyeumba mbingu na ardhi ni Mwenye kuweza kuumba mfano wao? Na Yeye amewawekea muda usio na shaka yoyote. Lakini madhalimu hawataki isipokuwa ukafiri." [Al-Israa: 97-99] Na amesema Mtukufu: "Itakapokuja ahadi ya Akhera, tutawaleta nyote pamoja." [Al-Israa :104] Na Aya tukufu zinazothibitisha kufufuliwa na kutawanyika ni nyingi sana.
Na mtu wa kwanza ambaye ardhi itafunguka atoke ni Mtume wetu, rehema na amani zimshukie. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kuwa, hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Mimi ndiye bwana wa watoto wa Adam Siku ya Kiyama, na wa kwanza ambaye atafungukiwa na kaburi, na muombezi wa kwanza, na wa kwanza atakayekubaliwa uombezi wake." (Imepokelewa na Muslim: 2278 na Abu Daud 4673).
Na wa kwanza kuzinduka ni Nabii wetu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Msiniboreshe juu ya Musa, kwa sababu Siku ya Kiyama, watu wote watazimia, na mimi nitazimia pamoja nao, lakini nitakuwa wa kwanza wao kuzinduka, na ghafla nitamuona Musa amesimama hali ya kuwa amekamata kwa nguvu upande wa 'Arshi (ya Mwenyezi Mungu). Hivyo sitaweza kujua ikiwa yeye pia alikuwa miongoni mwa wale waliozimia kisha akazinduka kabla yangu, au alikuwa miongoni mwa wale ambao Mwenyezi Mungu aliwaepusha (na kuzimia huko)." (Imepokelewa na Bukhari: 2441, na Muslim: 2373).
Na wa kwanza atakayevishwa nguo ni Nabii wa Mwenyezi Mungu, Ibrahim rafiki mwandani wa Mwingi wa rehema, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Wa kwanza kuvalishwa Siku ya Kiyama atakuwa Ibrahim." (Imepokelewa na Bukhari: 3349, Muslim: 2860, Tirmidhi: 2423, na An-Nasai: 2082).
Na watu watakusanywa pekupeku, uchi, bila kutahiriwa, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Siku ya Kiyama watu watakusanywa bila viatu, uchi, na wakiwa hawajatahiriwa." (Imepokelewa na Bukhari: 6527, Muslim: 2859, An-Nasai 2083, Ibn Majah: 4276).
Na tunaamini kuwa ardhi watakayokusanywa waja ni ardhi isiyokuwa hii, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Siku itakapogeuzwa ardhi iwe ardhi nyingine, na mbingu pia. Nao watahudhuria mbele ya Mwenyezi Mungu Mmoja, Mshindi." [Ibrahim: 48]
Na ardhi ya Siku ya Kiyama itakuwa nyeupe. Amesema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Watu watakusanywa Siku ya Kiyama juu ya ardhi nyeupe, nyekundu kama mkate safi." (Imepokelewa na Bukhari: 6521, na Muslim: 2790).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Sa'id Al-Khudri, kuwa alisema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Siku ya Kiyama, ardhi hii itakuwa mkate mmoja, naye afanyaye atakavyo (yani Mwenyezi Mungu) ataipindua kwa mkono wake kama vile mmoja wenu anavyoupindua mkate wake kwa mikono yake wakati (wa kuandaa mkate) wa safari." (Imepokelewa na Bukhari: 6520, na Muslim: 2792).
Hadithi sahihi zilikuja zikieleza ni wapi watu watakuwa wakati wa mabadiliko hayo: Imesimuliwa kutoka kwa Thauban mtumwa huru wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie, kwamba mwanasheria wa Kiyahudi alimjia Mtume wa Mwenyezi Mungu ili kumuuliza mambo, na miongoni mwake: Alisema mwanasheria huyo: "Watu watakuwa wapi Siku itakapogeuzwa ardhi iwe ardhi nyingine, na mbingu (pia)?" Mtume rehema na amani zimshukie akasema: "Watakuwa katika giza pasina daraja." (Imepokelewa na Muslim: 315).
Na imesimuliwa kutoka kwa Aisha Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Nilimuuliza Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuhusu (maana ya) maneno yake Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu, Mtukufu: "Siku itakapogeuzwa ardhi iwe ardhi nyingine, na mbingu pia." Watu watakuwa wapi siku hiyo, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema: "Juu ya Swirat (daraja ) (Imepokelewa na Muslim: 2791).
Na tunajua kuwa siku hii ni siku kubwa mno, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwani hawadhani hao kwamba watafufuliwa * Katika Siku iliyo kuu." [Al-Mutaffifin: 4, 5] Na amesema Mtukufu: "Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi. Hakika tetemeko la Saa (ya Kiyama) ni jambo kuu." [Al-Hajj: 1]
Muda wake ni miaka elfu hamsini (50,000), kama zilivyokuja habari sahihi kuhusiana na hilo. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Hakuna mmiliki yeyote wa hazina ambaye hatoi zaka yake..." hadi aliposema: "Mpaka Mwenyezi Mungu ahukumu baina ya waja wake katika siku ambayo muda wake ni miaka elfu hamsini (50,000) kama mnavyohesabu nyinyi. Kisha ataonyeshwa njia yake: Ima katika Pepo na ima katika Moto." (Imepokelewa na Bukhari: 2371, Muslim: 987, Abu Daud: 1658, Tirmidhi: 1636, An-Nasai: 3563, na Ibn Majah: 2788)
Na ndani yake jua litakaribia kwenye ardhi. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Umama, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie alisema: "Jua litasogezwa karibu na viumbe Siku ya Kiyama mpaka liwe karibu nao umbali wa maili moja." Sulaim bin 'Amir amesema: "Ninaapwa kwa Mwenyezi Mungu, sijui (kiwango) alimaanisha nini kwa "maili"? Je, ni umbali katika ardhi au ni kile kijiti kinachotumiwa kupaka wanja wa manga kwenye jicho." (Mtume) Akasema: "Kisha, watu watakuwa ndani ya jasho yao kulingana na matendo yao. Miongoni mwao, kuna ambaye litakuwa hadi kwenye vifundo viwili vya miguu yake. Na miongoni mwao, kuna ambaye litakuwa hadi kwenye magoti yake mawili. Na miongoni mwao, kuna ambaye litakuwa hadi kwenye nyonga zake mbili. Na miongoni mwao, kuna ambaye jasho (lake) litammeza kabisa." (Imepokelewa na Muslim: 2864, na Tirmidhi: 2421).
Waumini watajikinga kutokana na joto la jua hilo kwa metendo yao mazuri waliyoyafanya hapo awali. Miongoni mwao kuna watakaokuwa katika kivuli cha 'Arshi, kama alivyosema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Watu saba Mwenyezi Mungu atawaweka katika kivuli chake, siku ambayo hakutakuwa na kivuli isipokuwa kivuli chake.” (Imepokelewa na Bukhari: 660, na Muslim: 1031).
Na miongoni mwao wapo watakaofanyiwa kivuli na suratul "Baqara" na "Al-Imran", na zitamtetea. Amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Someni Qur'ani, kwani, itakuja Siku ya Kiyama kama muombezi kwa sahibu wake. Zisomeni Az-Zahraawaini: Al-Baqara na Surat Al-Imran. Kwani, zitakuja Siku ya Kiyama kana kwamba ni mawingu mawili au Ghayayatani (kitu chenye kumpa kivuli mtu kwa juu ya kichwa chake), au kana kwamba ni makundi mawili ya ndege walio katika safu, (sura hizo mbili) zikiwatetea wasomaji wake. Isomeni Surat Al-Baqara. Kwani kuichukua (kuisoma) ni baraka, na kuiacha ni majuto, na wala wachawi hawaiwezi." (Imepokelewa na Muslim: 804). Na miongoni mwao kuna watakaokuwa chini ya vivuli vya sadaka zao. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Kila mtu atakuwa katika kivuli cha sadaka zake mpaka itakapohukumiwa baina ya watu." (Ahmad: 17333, Abu Ya'la: 1766, Ibn Khuzaima: 2431, Ibn Hibban: 3310, na Ibn Khuzaima na Ibn Hibban walisema kwamba ni hadithi sahihi.)
Mlango wa uombezi Siku ya Kiyama, na kuja kwa Mola Mlezi, na kufika kwake ili kutenganisha na kuhukumu kati ya waja wake
Na tunaamini kuwa uombezi ni wa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika kutukuka, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Sema: Uombezi wote uko kwa Mwenyezi Mungu. Ni wake Yeye tu ufalme wa mbingu na ardhi. Kisha mtarejeshwa kwake." [Az-Zumar: 44].
Na tunaamini kwamba hakuna mtu anayeweza kufanya uombezi kwake isipokuwa kwa idhini yake, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Ni nani huyo awezaye kuombea mbele yake bila ya idhini yake?" [Al-Baqara: 255]. Waombezi hawawezi kumfanyia yeyote uombezi isipokuwa yule ambaye Mwingi wa rehema ataridhia kauli yake na kitendo chake, amesema Mola Mtukufu: "Wala hawamuombei yeyote isipokuwa yule anayemridhia Yeye, nao kwa sababu ya kumuogopa wananyenyekea." [Al-Anbiya: 28] Na amesema Mtukufu: "Siku hiyo uombezi hautafaa kitu, isipokuwa wa aliyemruhusu Mwingi wa rehema na akamridhia kusema." [Twaha: 109].
Na tunaamini kuwa watu watakaofurahia zaidi kufanyiwa uombezi na waombezi ni wale wanaomkusudia Mwenyezi Mungu peke yake na wanaompwekesha. Imekuja katika hadithi ya Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: Palisemwa: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, ni nani atakuwa mtu wa bahati kubwa zaidi kupata uombezi wako Siku ya Kiyama? Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ewe Abuu Huraira! Mimi kwa hakika nilijua kuwa hakuna mtu yeyote atakayeniuliza kuhusu hilo kabla yako kwa kuwa niliona hamu yako kubwa juu ya elimu ya Hadithi. Mtu mwenye bahati kubwa zaidi ambaye atakuwa na uombezi wangu Siku ya Kiyama ni yule atakayesema: “Laa ilaha illa Allah (Hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu)." akimkusudia Mwenyezi Mungu tu kwa hilo kutoka ndani ya moyo wake au nafsi yake." (Imepokelewa na Bukhari: 99, 6570).
Na tunaamini kwamba makafiri hawatopata uombezi wa waombezi. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Basi hautawafaa kitu uombezi wa waombezi." [Al-Muddathhir:48]
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu atamruhusu amtakaye katika waja wake kufanya uombezi, kwa ajili ya kumtukuza muombezi huyo na kwa kumhurumia mwenye kufanyiwa uombezi. Na tunajua kuwa muombezi mkubwa zaidi siku ya Kiyama atakuwa ni Mtume wetu Muhammad rehema na amani zimshukie, na atafanya uombezi kwa njia nyingi, mkubwa na mtukufu zaidi ni uombezi kwa watu wote katika hali ya kisimamo chao, ili ihukumiwe baina yao, na hicho ndicho cheo chenye kuhimidiwa, na hicho ndicho alichokitaja Mwenyezi Mungu katika Kitabu chake, amesema Mtukufu: "Na amka usiku kwa ibada; ni ziada ya sunna hasa kwako wewe. Huenda Mola wako Mlezi akakunyanyua cheo kinachosifika." [Al-Israa:79] Na katika Hadithi ya bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, katika (sahih) Bukhari: "...basi atawafanyia uombezi (kwa Mwenyezi Mungu) ili ihukumiwe kati ya viumbe. Kisha ataenda mpaka atakapokishika kishikio cha mlango (wa Pepo). Na hapo Mwenyezi Mungu atampandisha kwenye kituo chenye kusifika, ambapo watu wa mkusanyiko huo wote watakisifu." (Imepokelewa na Bukhari: 1475). Alitaja katika hadithi hii kufanya uombezi wa kukata hukumu, na Yeye wa Haki, Aliyatakasika na kutukuka akaeleza kuwa atafanya ukarimu wa kuhukumu (kati ya viumbe), kama ilivyo katika kauli yake Mtukufu: "Je wanangoja mpaka Mwenyezi Mungu awajie katika vivuli vya mawingu pamoja na Malaika, na hukumu iwe imekwishatolewa? Na kwa Mwenyezi Mungu ndio hurejeshwa mambo yote." [Al-Baqara: 210] Na kauli yake Mtukufu: "Na akaja Mola wako Mlezi na Malaika safu safu." [Al-Fajr: 22] Na kauli yake Mtukufu: "Je, wanangoja jengine isipokuwa Malaika wawajie, au awajie Mola wako Mlezi, au ziwajie baadhi ya Ishara za Mola wako Mlezi? Siku zitakapowajia baadhi ya Ishara za Mola wako Mlezi." Al-An'am: 158]
Kisha uombezi kwa watu wa Peponi waingie Peponi. Na uombezi huu umeashiriwa na Hadithi nyingi zilizosimuliwa kwa njia isiyo na shaka yoyote, kama vile Hadithi mashuhuri ya Anas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: "Itakapokuwa Siku ya Kiyama, watu watasongamana wao kwa wao, kisha watamuendea Adam na watasema: "Tufanyie uombezi kwa Mola wako Mlezi." Atasema: "Mimi sifai kwa hilo, lakini muendeeni Ibrahim, kwani yeye rafiki mwandani wa Ar-Rahman." Basi, watamuendea Ibrahim, naye atasema: "Mimi sifai kwa hilo, lakini muendeeni Musa, kwani, yeye alizungumzishwa na Mwenyezi Mungu moja kwa moja." Kwa hivyo, watamuendea Musa, naye atasema: "Mimi sifai kwa hilo, lakini muendeeni Isa, kwani, yeye ni roho wa Mwenyezi Mungu, na neno lake." Basi, watamuendea Isa, naye atasema: "Mimi sifai kwa hilo, lakini muendeeni Muhammad." Hivyo, watanijia, nami nitasema: "Mimi ninafaa kwa hilo." Kisha nitaomba ruhusa kwa Mola wangu Mlezi, na nitaidhinishwa. Kisha atanifahamisha sifa ambazo nitamsifu kwazo ambazo sizijui sasa. Basi, nitamsifu kwa sifa hizo, na nitaanguka nimsujudie. Kisha nitaambiwa: "Ewe Muhammad! Nyanyua kichwa chako, na sema, utasikilizwa, na omba utapewa ombi lako, na fanya uombezi utakubaliwa uombezi wako ." Basi, nitasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Umma wangu. Umma wangu." Hivyo, nitaambiwa: "Nenda, na yeyote yule atakayekuwa ana imani sawa na uzito wa mbegu ya shairi (ngano), basi muondoe kutoka humo." Basi, nitakwenda na kufanya hivyo. Kisha nitarudi na kumsifu kwa sifa hizo. Kisha nitaanguka nimsujudie. Kisha nitaambiwa: "Ewe Muhammad! Nyanyua kichwa chako, na sema, utasikilizwa, na omba, utapewa ombi lako, na fanya uombezi, utakubaliwa uombezi wako." Kwa hivyo, nitasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Umma wangu. Umma wangu." Basi, nitaambiwa: "Nenda, na yeyote yule atakayekuwa ana imani sawa na uzito wa mdudu chungu au mbegu ya haradali (ulezi), basi muondoe kutoka humo." Basi, nitakwenda na kufanya hivyo." Kisha nitarudi (kwa Mola wangu Mlezi) na nimsifu kwa sifa hizo. Kisha nitaanguka nimsujudie. Kisha nitaambiwa: "Ewe Muhammad! Nyanyua kichwa chako, na sema, utasikilizwa, na omba, utapewa ombi lako, na fanya uombezi, utakubaliwa uombezi wako ." Basi, nitasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Umma wangu. Umma wangu." Hivyo, nitaambiwa: "Nenda, na yeyote yule atakayekuwa na imani ambayo ni ya chini ya chini ya chini zaidi ya uzito wa mbegu ya haradali (ulezi), basi muondoe kutoka Motoni." Basi, nitakwenda na kufanya hivyo." (Ma'bad anasema) Tulipotoka kwa Anas, niliwaambia baadhi ya jamaa zetu, "Lau tutampitia Al-Hasan ambaye alikuwa amejificha katika nyumba ya Abuu Khalifa, tukamuombe atusimulie kile alichotusimulia Anas bin Malik." (Ma'bad bin Hilal) akasema: "Basi, tulimjia na tukamsalimia na akaturuhusu kuingia. Tukamwambia: "Ewe Abuu Sa'id! Tumekujia kutoka kwa ndugu yako, Anas bin Malik, na hatujawahi kusikia Hadithi kama ile aliyotusimulia (Anasi) kuhusiana na uombezi." Akasema: "Isimulie." Basi, tukamsimulia hadithi hiyo, na tukasema: "Alisimamia hapa." Akasema: "Isimulie (bado)." Tukasema: "Hakutuongeza juu ya haya." Akasema: "Hakika, (Anasi) alinisimulia hadithi hiyo kabla ya miaka ishirini (20) hali ya kuwa bado ana afya nzuri. Hivyo, sijui ikiwa aliyasahau au hakupenda kuwasimulia nanyi mkayategemea hayo tu (na kuacha kufanya matendo mema)." Tulimwambia: "Ewe Abuu Sa'd! Basi tusimulie hadithi hiyo." Basi, alicheka na akasema: "Mwanadamu ameumbwa na haraka. Sikuwatajia haya isipokuwa nilitaka niwahadithie (juu yake). Alinihadithia namna alivyowahadithia, na akasema (Anas), "(Mtume alisema) Kisha nitarudi (kwa Mola wangu Mlezi) kwa mara ya nne, na nitamsifu kwa sifa hizo, kisha nitaanguka nimsujudie, na nitaambiwa: "Ewe Muhammad! Nyanyua kichwa chako, na sema, utasikilizwa, na omba, utapewa ombi lako, na fanya utetezi (uombezi), uombezi wako utakubaliwa." Hivyo, nitasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Nipe ruhusa katika wale waliosema, Laa ilaaha illa llah (hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu)." (Allah) Atasema: "Ninaapa kwa Nguvu zangu, na Utukufu wangu, na Ukubwa wangu, na Ukuu wangu! Bila shaka, nitamtoa kutoka humo yeyote yule aliyesema, 'Laa ilaaha illa llah (Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu)." (Imepokelewa na Bukhari: 7510, Muslim: 193, na Ibn Majah: 4312).
Na miongoni mwake ni Hadithi ya Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, ambayo ni sawa na Hadithi ya Anasi, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, na akasema katika mwisho wake: "...Nendeni kwa Muhammad." Basi, watanijia, na watasema: "Ewe Mahammad! Wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na wa mwisho wa mitume. Mwenyezi Mungu alikwishakusamehe dhambi zako za zamani na za baadaye. Tutetee kwa Mola wako Mlezi. Je, huoni kile ambacho sisi tumo? Je, huoni ni yapi yaliyotufika?" Hivyo, nitaondoka na nije mpaka chini ya 'Arshi (Kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu), na nitaanguka chini nimsujudie. Kisha Mwenyezi Mungu atanifungulia na anifahamishe katika sifa zake na katika kumtukuza kwa uzuri mambo ambayo hakumfungulia yeyote kabla yangu. Kisha atasema: "Ewe Muhammad! Nyanyua kichwa chako, na omba, utapewa ombi lako, na fanya uombezi, uombezi wako utakubaliwa." Basi, nitainua kichwa changu, na nitasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Umma wangu! Umma wangu!" Basi, kutasemwa: "Ewe Muhammad! Ingiza Peponi katika umma wako mtu ambaye hana hesabu yoyote (juu ya matendo yake) kupitia katika mlango wa kulia katika milango ya Pepo. Na watawashiriki watu wengine katika milango yote isipokuwa mlango huo miongoni mwa milango (huo ni wao tu)." Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ninaapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad iko katika mkono wake! Hakika umbali ulioko kati ya pande mbili za milango ya Pepo, ni kama (umbali wa) kati ya Makka na Hajar (Mji wa Ahsaa kwa sasa -uko nchini Saudia, ni kilomita 1000 takriban), au kati ya Makka na Basra (Iraq)." (Imepokelewa na Bukhari: 3340, na Muslim: 194).
Na miongoni mwake ni Hadithi ya Anas bin Malik, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi kuwa: Amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Mimi nitakuwa muombezi wa kwanza katika Pepo, na hakuna Nabii yeyote miongoni mwa manabii aliyewahi kusadikishwa (na idadi kubwa ya watu) kama nilivyosadikishwa. Na hakika miongoni mwa Manabii, kuna Nabii ambaye hakusadikishwa katika Umma wake isipokuwa na mwanaume mmoja tu." (Imepokelewa na Muslim: 196, na Ad-Darmi: 52).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Kila Nabii ana dua maalumu ambayo aliomba kwayo na akajibiwa, lakini mimi niliiweka dua yangu (maalumu) ili kuwaombea umma wangu Siku ya Kiyama." (Imepokelewa na Bukhari: 6305). Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Kila Nabii ana dua maalum yenye kukubalika ambayo anamuomba Mwenyezi Mungu, na ninataka kuificha dua yangu ili niweze kuwafanyia umma wangu uombezi kule Akhera." (Imepokelewa na Bukhari: 6304, Muslim: 199, Tirmidhi: 3602, na Ibn Majah: 4307).
Na tunaamini kuwa kama ambavyo Mwenyezi Mungu alimkirimu Nabii wetu kwa uombezi, ndivyo atakavyowakirimu Manabii, Malaika na Waumini. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Sa'id Al-Khudri, kuwa alisema: "...Kisha Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu, Mtukufu atasema: "Malaika wameshafanya uombezi, na Manabii (pia) wameshafanya uombezi, na Waumini wameshafanya uombezi, na hajabakia isipokuwa Mbora wa kurehemu kuliko wenye kurehemu wote)" Kisha atachota mchoto mmoja katika Moto, na atawatoa humo watu ambao hawakuwahi kamwe kufanya heri." (Imepokelewa na Bukhari: 7439, na Muslim: 183).
Mlango wa kuonyeshwa matendo, kufanyiwa hesabu, na kupewa nyaraka za matendo
Na tunaamini kuwa kila mtu atapewa kitabu chake, kwa hivyo kuna yule atakayechukua kitabu chake kwa mkono wake wa kulia. Amesema Mola wa Haki, na kauli yake ni ya haki: "Basi ama atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, atasema: Haya someni kitabu changu!" [Al-Haqqa: 19].
Na kuna yule atakayechukua kitabu chake kwa mkono wa kushoto, amesema Mtukufu: "Na ama atakayepewa kitabu chake katika mkono wake wa kushoto, basi atasema: Laiti nisingelipewa kitabu changu!" [Al-Haqqa: 25] Na kuna yule atakayekichukua kwa nyuma ya mgongo wake, amesema Mola Mtukufu: "Na ama atakayepewa daftari lake kwa nyuma ya mgongo wake." [Al-Inshiqaq: 10] ِِِِِِAtaambiwa: "Soma kitabu chako! Nafsi yako inakutosha leo kukuhesabu." [Al-Israa: 14] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na kitawekwa kitabu. Basi utawaona wahalifu wanavyoogopa kwa yale yaliyomo humo. Na watasema: Ole wetu! Kitabu hichi kina nini! Hakiachi dogo wala kubwa isipokuwa huliandika? Na watayakuta yote waliyoyatenda yamehudhuria hapo. Na Mola wako Mlezi hamdhulumu yeyote." [Al-Kahf: 49]
Na tunaamini kwamba watu wataonyeshwa matendo yao, amesema Mola wa Haki - na kauli Yake ni ya haki: "Siku hiyo mtahudhurishwa - haitafichika siri yoyote yenu." [Al-Haqqa: 18] Na amesema Mtukufu: "Na wakahudhurishwa mbele ya Mola wako Mlezi kwa safu (wakaambiwa): Mmetujia kama tulivyowaumba mara ya kwanza! Bali mlidai kwamba hatutawawekea miadi." [Al-Kahf: 48] Imesimuiwa kutoka kwa 'Adiy bin Hatim kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie: "Hakuna yeyote miongoni mwenu, isipokuwa ataongeleshwa na Mwenyezi Mungu siku ya Kiyama bila ya kuwapo na mkalimani yeyote kati yake na Yeye (Allah). Atatazama kuliani kwake, na wala hataona kitu chochote isipokuwa matendo yake aliyotanguliza. Kisha ataangalia kushotoni kwake, na wala hataona kitu chochote isipokuwa matendo yake aliyotanguliza. Na ataangalia mbele yake, na hataona isipokuwa Moto mbele ya uso wake. Basi uepukeni Moto hata kama ni kwa nusu ya tende." (Imepokelewa na Bukhari: 6539, na Muslim: 1016).
Na tunaamini kuhesabiwa, na kwamba Mwenyezi Mungu atawahesabu waja wake. Amesema Mola Mtukufu: "Hakika ni kwetu Sisi ndio marejeo yao * Kisha hakika ni juu yetu Sisi hesabu yao!" [Al-Ghashiya: 25-26] Kwa hivyo, mwenye kupata heri, basi na amsifu Mwenyezi Mungu. Na mwenye kupata yasiyokuwa hayo, asimlaumu yeyote isipokuwa nafsi yake, kama yalivyothibiti hayo katika hadithi sahihi kutoka kwa Mtume rehema na amani zimshukie: "... Enyi waja wangu, bila shaka hayo ni matendo yenu, ninawakusanyia, kisha nitawalipa kwa ukamilifu. Kwa hivyo, mwenye kupata heri, basi na amsifu Mwenyezi Mungu. Na mwenye kupata yasiyokuwa hayo, asilaumu isipokuwa nafsi yake." (Imepokelewa na Muslim: 2577).
Naye Aliyetakasika ni mwepesi wa kuhesabu, amesema Mtukufu: "Leo kila nafsi italipwa kwa iliyochuma. Hapana dhulma yoyote leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhesabu." [Ghafir: 17].
Na tunaamini kwamba baadhi ya waumini wataingia Peponi bila ya hesabu, amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Wataingia Peponi katika umma wangu watu elfu sabini (70,000) bila ya kuhesabiwa....". (Imepokelewa na Bukhari: 5811, Muslim: 216 na lafudhi ya hadithi hii ni yake).
Hesabu ya Mwenyezi Mungu kwa waja wake ina viwango na hali tofauti, miongoni mwa waja kuna wale watakaohesabiwa hesabu ngumu, na miongoni mwao wapo watakaohesabiwa hesabu nyepesi. Amesema Mtukufu: "Ama yule atakayepewa daftari lake kwa mkono wa kulia * Basi huyo atahesabiwa hesabu nyepesi." [Al-Inshiqaq: 7-8]
Imehadithiwa kutoka kwa Aisha radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Hakuna yeyote atakayehesabiwa matendo yake Siku ya Kiyama isipokuwa ataangamia." (Imepokelewa na Bukhari: 6537, na Muslim: 2876). Nikasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu hakusema: "Ama yule atakayepewa daftari lake kwa mkono wa kulia * Basi huyo atahesabiwa hesabu nyepesi." [Al-Inshiqaq: 7-8] Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Hiyo ni kuonyeshwa matendo yake, na hakuna yeyote atakayejadiliwa kuhusu matendo yake Siku ya Kiyama isipokuwa ataadhibiwa." (Imepokelewa na Bukhari: 6537). Hatodhulumiwa yeyote siku hiyo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa kwa ukamilifu ilichochuma. Nao hawatadhulumiwa." [Al-Baqara: 281]
Na wa kwanza kuhesabiwa Siku ya Kiyama ni umma wa Muhammad, kwa kauli yake rehema na amani ziwe juu yake: "...Sisi (Waislamu) ni wa mwisho katika wakazi wa dunia na wa kwanza siku ya Kiyama. Na wa kwanza kuhukumiwa kabla ya viumbe wote." (Imepokelewa na Muslim 856).
Na la kwanza kuhukumiwa kati ya watu ni umwagaji damu, kwa kauli ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Cha kwanza kabisa kitakachohukumiwa baina ya watu (Siku ya Kiyama) itakuwa kuhusiana na damu (zilizomwagwa)." (Imepokelewa na Bukhari: 6864, na Muslim: 1678).
Na tunaamini kwamba siku hiyo wataletwa mashahidi; hivyo Malaika watashuhudia, na ardhi itashuhudia waliyoyafanya waja juu yake, na pia viungo vitashuhudia. Amesema Mtukufu: "Hakika bila ya shaka Sisi tunawanusuru Mitume wetu na wale walioamini katika uhai wa duniani na siku wataposimama Mashahidi." [Ghafir: 51] Amesema Mola wa Haki: "Na ardhi itang'ara kwa Nuru ya Mola wake Mlezi, na Kitabu kitawekwa, na wataletwa Manabii na mashahidi, na patahukumiwa baina yao kwa haki, wala hawatadhulumiwa." [Az-Zumar: 69] Na amesema Mola Mtukufu: "Siku hiyo itahadithia habari zake." [Al-Zilzala: 4] Na amesema Mola Mtukufu: "Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyokuwa wakiyachuma." [Ya-Sin: 65]
Na katika "sahihi" hadithi ya Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, imetajwa kwamba viungo vitashuhudia juu ya waja, na ndani yake kuna: "...kisha ataambiwa: Sasa tunawaleta mashahidi wetu juu yako." Naye atafikiria katika nafsi yake: "Ni nani huyo atakayekuwa shahidi juu yangu?" Kisha atafungwa mdomo wake na litaambiwa paja lake na nyama zake na mifupa yake: "Tamkeni." Kisha, paja lake na nyama zake na mifupa yake vitatamka matendo yake. Na hilo, ili asiweze kujipa udhuru wowote yeye mwenyewe. Na huyo ndiye mnafiki. Na huyo ndiye ambaye Mwenyezi Mungu atamkasirikia." (Imepokelewa na Muslim: 2968).
Imesimuliwa kutoka kwa Anas bin Malik kuwa alisema: Tulikuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akatabasamu. Kisha, akasema: "Je, mnajua ni kwa nini nimetabasamu?" Tukasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanajua zaidi." Akasema: "Ni kwa sababu ya vile mja atakavyozungumza na Mola wake Mlezi (Siku ya Kiyama). Atasema: "Ewe Mola (wangu) Mlezi! Je, haukuniahidi kwamba sitadhulumiwa?" Akasema: Atasema: "Bali (nilikuahidi)." Akasema: Kisha, (mja huyo) atasema: "Basi, mimi kwa hakika, sitamkubali shahidi yeyote juu ya nafsi yangu isipokuwa shahidi atokaye kwangu." Akasema: Basi, atasema: "Nafsi yako inakutosha leo kuwa shahidi [dhidi yako], na (pia) waandishi wenye heshima watashuhudia." Akasema: Kisha, atafungwa mdomo wake na vitaambiwa viungo vyake: "Tamkeni!" Akasema: Kisha vitatamka matendo yake (yote). Akasema: Kisha ataachwa azungumze. Akasema: Atasema: "Nendeni mbali sana na mimi. Ni kwa ajili yenu nilikuwa nikipambana." (Imepokelewa na Muslim: 2969).
Mlango wa kuamini Mizani
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu ataweka mizani ya kupima matendo ya waja wake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Nasi tutaweka mizani za uadilifu kwa Siku ya Kiyama. Basi nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu chochote. Hata ikiwa ni uzito wa chembe ya haradali (ulezi), tutaileta. Nasi tunatosha kuwa washika hesabu." [Al-Anbiyaa: 47] Na amesema Mtukufu: "Na Siku hiyo kipimo kitakuwa kwa Haki. Basi watakaokuwa na uzani mzito, hao ndio watakaofanikiwa * Na watakaokuwa na uzani hafifu, basi hao ndio waliozitia hasarani nafsi zao kwa sababu ya kuzipinga Ishara zetu." [Al-A'raf: 8, 9], Nayo ni mizani ya kweli yenye pande mbili na sehemu ya katikati zinapokutania pande hizo mbili, na kwayo yatapimwa matendo ya waja.
Na tunaamini kuwa matendo yatawekwa katika mizani hiyo, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Maneno mawili mepesi sana katika ulimi, ni mazito sana katika mizani, na yapendwa sana kwa Mwingi wa Rehema: Sub-haanallaah wa bihamdihi, Sub-haanaallahil-'Adhwiim (Ametakasika Mwenyezi Mungu na Sifa njema zote ni zake, na Ametakasika Mwenyezi Mungu Mtukufu)." (Imepokelewa na Bukhari: 6682, Muslim: 2694, Tirmidhi: 3467, na Ibn Majah: 3806).
Na pia amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Twahara (Usafi) ni nusu ya imani, na Al-Hamdulillaah (Sifa njema zote ni za Allah) hujaza mizani." (Imepokelewa na Muslim: 223, Tirmidhi: 3517, An-Nasai 2437, na Ibn Majah: 280).
Na tunajua kwamba mtendaji wa matendo atawekwa katika mizani pamoja na matendo yake. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kutoka kwa Mtume rehema na amani zimshukie kuwa alisema: "Hakika, Siku ya Kiyama, atakuja mtu mkubwa mnene lakini hatakuwa na uzito wowote wa kulingana na uzito wa bawa la mbu kwa Mwenyezi Mungu." Na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie aliongeza: "Someni, (kauli ya Allah)": "Na wala Siku ya Kiyama hatutawathamini kitu." (Al-Kahf: 105) (Imepokelewa na Bukhari: 4729, na Muslim: 2785). Vile vile, vitabu vya matendo vitawekwa kwenye mizani, kama lilivyoonyeshwa hilo na Hadithi ya kadi. (Imepokelewa na Tirmidhi: 2639, Ibn Majah 4300, Ibn Al-Mubarak katika Al-Musnad 100, katika Az-Zahd 2/109, na Ahmad 6994).
Mlango wa kuamini hodhi la Mtume
Na tunaamini kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie ana hodhi ambalo umma wake watakunywa humo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika tumekupa heri nyingi." [Al-Kauthar: 1].
Imesimuliwa kutoka kwa Anas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwa alisema: Siku moja, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa ameketi miongoni mwetu, na tazama! Alilala usingizi mfupi. Kisha akainua kichwa chake hali ya kuwa anatabasamu. Tukasema: "Ni kitu gani kinakufanya kutabasamu ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema: "Ni Sura ambayo imeteremshwa juu yangu muda mfupi uliopita, kisha akasoma: "Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu * Hakika, tumekupa (Mto wa) Kauthar. * Basi swali na uchinje kwa ajili ya Mola wako Mlezi. * Hakika, anaye kuchukia ndiye aliye mpungufu (amekatikiwa)." [Al-Kauthar: 1-3]. Kisha akasema: "Je, mnajua ni nini Kauthar?" Tukasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanajua zaidi." Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "(Kauthar) Ni mto ambao Mola wangu Mlezi, Mwenye Nguvu, Mtukufu aliniahidi, nao una heri nyingi sana. Nao ni hodhi ambayo Umma wangu wataijia (ili kunywa maji) Siku ya Kiyama, na vyombo vyake ni (vingi) kama idadi ya nyota. Atavutwa mja miongoni mwao, na nitasema: "Ewe Mola Mlezi, hakika huyo ni miongoni mwa Umma wangu." (Mola wangu Mlezi) Atasema: "Hujui yale waliyozua baada yako." (Imepokelewa na Muslim: 400).
Na amesema rehema na amani zimshukie: "(Ukubwa wa) Hodhi yangu ni safari ya mwezi mzima. Maji yake ni meupe kuliko maziwa, na harufu yake ni nzuri kuliko (manukato ya) miski, na vikombe vyake ni kama (idadi ya) nyota za mbinguni, na yeyote atakayekunywa humo, basi kamwe hatapatwa na kiu." (Imepokelewa na Bukhari: 6579, na Muslim: 2292).
Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Hakika, hodhi yangu ni mbali (ndefu) kuliko umbali ulioko kati ya Aila (Sham) na Aden (Yemen), na hakika maji yake ni meupe zaidi kuliko theluji (barafu) na ni matamu zaidi kuliko asali iliyochanganywa na maziwa, na hakika vikombe vyake ni vingi zaidi kuliko idadi ya nyota. Nami hakika nitawazuia watu kutoka hapo (kwenye hodhi) kama vile mtu anavyowazuia ngamia wa watu kutoka kwenye hodhi (chemchemi) yake." Wakasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Je, utatutambua siku hiyo?" Akasema: "Ndiyo, mtakuwa na alama ambazo hazitakuwa kwa yeyote katika Umma zingine. Mtanijia ili kunywa maji yake hali ya kuwa mnang'aa mapaji ya nyuso zenu, mikono yenu na miguu yenu kutokana na athari za udhu." (Imepokelewa na Muslim: 247).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Nilipokuwa nimesimama, mara nikaona kundi (la umma wangu) lilikuwa hapo (karibu nami), na nilipowajua, mwanaume mmoja (yani Malaika) alitokezea kati yangu na wao, kisha akasema: (akiwaambia) "Njooni." Nikauliza: "(Kwenda) Wapi?" Akasema: "Kwenda Motoni, ninaapa kwa Mwenyezi Mungu!" Nikauliza: "Kwani wana nini?" Akasema: "Hakika wao walirejea kinyumenyume baada yako (yani waliritadi)." Kisha tazama! kulikuwa na kundi jingine (karibu nami), na nilipokwishawajua, mwanaume mmoja alitokezea kati yangu na wao, na akasema: (akiwaambia), "Njooni!" Nikauliza: "(Kwenda) Wapi?" Akasema: "Kwenda Motoni, ninaapa kwa Mwenyezi Mungu!" Nikauliza: "Kwani wana nini?" Akasema: "Hakika wao walirejea kinyumenyume baada yako (yani waliritadi)." Basi, sikuweza kuona yeyote miongoni mwao akiokoka miongoni mwao isipokuwa wachache tu ambao walikuwa kama ngamia wasio na mchungaji." (Imepokelewa na Bukhari: 6587).
Imesimuliwa kutoka kwa Anas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kuwa alisema: Alipopandishwa Mtume rehema na amani zimshukie kwenda mbinguni, akasema (baada ya kurudi): "Nikaufikia mto (ndani ya pepo) ambao kingo zake zilikuwa zimetengenezwa kwa mahema ya lulu zilizo tupu ndani." Nilimuuliza Jibril: "Hii ni nini, ewe Jibril?" Akasema: "Hii ni Kauthar." (Imepokelewa na Bukhari: 4964).
Mlango wa Sirat (Daraja) na malipo
Na tunaamini kuwa Sirat (daraja) litawekwa juu ya mgongo wa Jahannam, nalo ni daraja linaloteleza, na waja watalivuka kulingana na matendo yao. Na lina ndoano mfano wa miiba ya mti wa Sa'daan. (Ndoano) Hizo zitawanyakuwa watu kulingana na matendo yao. Na wa kwanza kulivuka daraja hilo ni Mtume wetu rehema na amani zimshukie. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie alisema: "...Siku ya Kiyama, watu watakusanywa na atasema (Mola Mlezi): "Na wafuate watu walichokuwa wakiabudu." Basi miongoni mwao, kuna wale watakaolifuata jua, na miongoni mwao kuna wale watakaoufuata mwezi, na wengine watawafuata Matwaaghuti (kila kilichoabudiwa kinyume au pamoja na Mwenyezi Mungu hali ya kuwa kimeridhia), na umma huu utabakia hali ya kuwa bado kuna wanafiki wake ndani yake. Basi Mwenyezi Mungu atawajia na kusema: "Mimi ni Mola wenu Mlezi.' Watasema: "Tutakaa hapa mpaka Mola wetu Mlezi atujie, na atakapokuja Mola wetu Mlezi, sisi tutamtambua." Kisha Mwenyezi Mungu atawajia tena na kusema: "Mimi ni Mola wenu Mlezi." Watasema: "Wewe ni Mola wetu Mlezi." Kisha Mwenyezi Mungu atawaita, na Sirat (daraja nyembamba mno na yenye miba kama vile mti wa Sa'adan) itawekwa juu ya Jahannam, na mimi (Muhammad) nitakuwa wa kwanza kati ya Mitume kuivuka pamoja na umma wangu. Siku hiyo, hakuna yeyote atakayeweza kuzungumza isipokuwa Mitume. Nao watasema: "Ewe Mwenyezi Mungu! Tuokoe, tuokoe." (Imepokelewa na Bukhari: 806, Muslim: 182, Abu Daud: 4730, Tirmidhi: 2554, na Ibn Majah: 178).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Sa'id Al-Khudri, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: "...Kisha daraja litaletwa na kuwekwa juu ya Jahannam." Tukasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Daraja ndio nini?' Akasema: "Ni daraja lenye kuyumbisha, lenye kuteleza, na lina ndoano kali, na vyuma vyenye ncha kali vilivyopinda, na vyuma vilivyochongeka vipana, na lina miba iliyopinda, mfano wa miba ya Najidi, iitwayo Saadan, (ilikuwa maarufu kwa zama hizo), muumini atapita hapo (kwa kasi) mithili ya kupepesa jicho, na mwingine kama umeme, na mwingine kama upepo, na mwingine atapita kama Farasi waendao kwa kasi, na mwingine mfano wa msafiri, hapo atakayeokoka basi huyo kasalimika, na mwingine atasalimika lakini kwa kuchubuka sana, na kuna atakaye viringishwa na kutupwa ndani ya Jahannam, itakwenda hivyo mpaka atapita wa mwisho wao akiburutwa kwa nguvu." (Imepokelewa na Bukhari: 7439).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "... Na pembezoni mwa daraja hilo, kuna ndoana zilizotundikwa zilizoamrishwa kumchukua yeyote zitakayeamrishwa. Kwa hivyo kuna atakayekwaruzwa kisha aokoke, na kuna atakayeanguka Motoni." (Imepokelewa na Muslim: 195).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Zubair kuwa alimsikia Jabir bin 'Abdallah, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juuu yake, hali ya kuwa anaulizwa juu ya Al-Wuruud (kupita katika daraja la Jahannam). Akasema: "Tutakuja Siku ya Kiyama hivi na vile." - Angalia! ni kipi kilicho juu ya watu -(Msimulizi) akasema: "Kisha watu wataitwa pamoja na sanamu zao walizokuwa wakiabudu, wa kwanza, kisha anayefuata (hivyo hivyo). Kisha Mola wetu Mlezi atatujia na atasema: "Mnamsubiri nani?" Watasema: "Tunamsubiri Mola wetu Mlezi." Atasema: "Mimi ni Mola wenu Mlezi." Watasema: "Mpaka tukutazame." Basi, atajitokeza wazi hali ya kuwa anacheka. Akasema: Kisha ataenda pamoja nao hali ya kuwa wanamfuata. Na kila mtu, sawa awe Muumini au mnafiki atapewa nuru. Kisha watamfuata, na juu ya daraja la Jahannam kutakuwa na ndoana na miba inayomkamata yule ambaye Mwenyezi Mungu anamtaka. Kisha zitazimwa nuru za wanafiki, kisha waumini wataokoka..." (Imepokelewa na Muslim: 191).
Na waumini watakapookoka katika daraja hilo, watafanyiwa hesabu kwenye kivuko (daraja), sehemu iliyo baina ya Pepo na Moto. Imesimulia kutoka kwa Abuu Saidi Al-Khudri, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie: "Waumini wataokoka kutokana na Moto, kisha watafanyiwa hesabu kwenye kivuko kilicho baina ya Pepo na Moto, hivyo watalipizana kisasi wao kwa wao kuhusiana na makosa waliyokuwa wakifanyiana duniani. Na watakapokuwa wameshasafishwa na kutakaswa, watapewa idhini ya kuingia ndani ya Pepo. Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi ya Muhammad iko mkononi mwake! kila mmoja wao atayajua makao yake katika Pepo vizuri kuliko alivyoyajua makao yake duniani." (Imepokelewa na Bukhari: 6535).
Mlango wa Pepo na Moto
Na tunaamini kuwa Pepo na Moto ndiyo makao ya malipo. Imekuja sifa ya wakazi wa Peponi na Motoni katika Qur’ani na Sunna, na yakatajwa makazi yao, vinywaji vyao, vyakula vyao na mavazi yao.
Na tunaamini kwamba viwili hivyo vimeumbwa sasa, na kwamba Adam amani iwe juu yake, alikuwa katika Pepo ya Milele, amesema Mtukufu: "Na wewe, Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani hii, na kuleni humo mpendapo. Wala msiukaribie mti huu, mkawa katika wale waliodhulumu." [Al-A'araf: 19]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema: "Adam na Musa walijadiliana. Musa akamwambia Adam: "Ewe Adam! Wewe ndiye baba yetu ambaye alituvunja moyo na akatuondoa Peponi?" Adam akamwambia: "Ewe Musa! Mwenyezi Mungu alikuchagua kwa maneno yake (aliponena nawe moja kwa moja), na akakuandikia kwa mkono wake mwenyewe. Je, unanilaumu kwa kitu nilichokwishaandikwa na Mwenyezi Mungu miaka arobaini kabla sijaumbwa?" Kwa hivyo, Adam akamshinda Musa. Adam akamshinda Musa." Alisema hilo mara tatu. (Imepokelewa na Bukhari: 6614, Muslim: 2652, Abuu Daud: 4701, Tirmidhi: 2134, na Ibn Majah: 80).
Na Pepo ndiyo makazi ya neema ya kudumu. Amesema Mola wa haki Mtukufu: "Hao malipo yao ni msamaha kutoka kwa Mola wao Mlezi, na Bustani zipitazo mito kati yake. Humo watadumu, na mwema mno ujira wa watendao." [Al-I-Imran: 136] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu, akihimiza juu ya neema iliyomo ndani yake: "Nafsi yoyote haijui waliyofichiwa katika hayo yanayofurahisha macho, ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyatenda." [As-Sajda: 17]
Na tunaamini kuwa neema kubwa ya Peponi ni kuutazama uso wa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika bustani za neema, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Zipo nyuso siku hiyo zitakazong'ara * Zinamwangalia Mola wao Mlezi." [Al-Qiyama: 22-23] Na akasema: "Hasha! Hakika hao siku hiyo bila ya shaka watazuiliwa na neema za Mola wao Mlezi." [Al-Mutaffifin: 15] Imehadithiwa kutoka kwa Suhaib Ar-Rumi, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie alisema: "Wakati wakazi wa Peponi watakapoingia Peponi, Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, atasema: "Je, mnataka kitu chochote niwazidishie?" Watasema: "Je, hukuziangaza nyuso zetu? Je, hukutuingiza Peponi, na ukatuokoa kutokana na Moto?" Kisha (Mwenyezi Mungu) atainua pazia, basi, hawatapewa kitu chochote kinachopendwa zaidi kwao kuliko kumwangalia Mola wao Mlezi Mwenye Nguvu, Mtukufu." (Imepokelewa na Muslim: 181).
Na tunaamini kuwa Pepo ina viwango, alitueleza rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, juu ya hadhi ya mkazi wa chini zaidi, na yule wa juu kabisa miongoni mwao, amesema rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Musa alimuuliza Mola wake Mlezi: "Ni nani kati ya wakazi wa Peponi mwenye cheo cha chini zaidi?" (Mwenyezi Mungu) akasema: "Ni mtu atakayekuja baada ya wakazi wa Peponi kuingizwa Peponi, na ataambiwa: "Ingia Peponi." Atasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Vipi na tayari watu wameshaingia katika makazi yao na wameshakuchukua migao yao?" Ataambiwa: "Je, unaridhia kwamba uwe wako mfano wa ufalme wa mfalme mmoja katika wafalme wa duniani?" Atasema: "Nimeridhia, ewe Mola wangu Mlezi." (Mwenyezi Mungu) atasema: "Hivyo ni vyako na mfano wake, na mfano wake, na mfano wake, na mfano wake." Na akasema katika mara ya tano: "Nimeridhia, ewe Mola wangu Mlezi!" (Mwenyezi Mungu ) atasema: "Hivyo ni vyako na mara kumi mfano wake. Na ni chako chochote ambacho nafsi yako inatamani na jicho lako linafurahia." Atasema: "Nimeridhia, ewe Mola wangu Mlezi" (Musa) akasema: "Ewe Mola Mlezi, na wa juu yao zaidi katika cheo?" (Mwenyezi Mungu) akasema: "Hao ndio niliowataka. Niliupanda utukufu wao kwa mkono wangu mwenyewe, kisha nikaufunika sawasawa. Kwa hivyo, hakuna jicho lolote lililowahi kuuona, na hakuna sikio lolote lililowahi kuusikia, na haukuwahi kupita katika moyo wa mwanadamu yeyote." Akasema: Na cha kusadikisha hilo kiko katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mtukufu, "Nafsi yoyote haijui waliyofichiwa katika hayo yanayofurahisha macho." (As-Sajda: 17) hadi mwisho wa aya. (Imepokelewa na Muslim: 189).
Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika, mwenye kiwango cha chini zaidi kati yenu katika Pepo ni kwamba ataambiwa: "Tamani!" Basi atatamani na atamani, na ataambiwa: "Je umeshatamani?" Atasema: "Nidyo." Ataambiwa: "Ni vyako vyote ulivyotamani, na mfano wake pamoja navyo." (Imepokelewa na Muslim: 182).
Na tunajua kuwa milango ya peponi ni minane, amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie: "Yeyote yule atakayeshuhudia kuwa: Hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, peke yake hana mshirika, na kuwa Muhammad ni mja wake na ni Mtume wake, na kwamba Isa ni mja Mwenyezi Mungu na mtume wake, na neno lake tu alilompelekea Mariam, na ni roho iliyotoka kwake, na kwamba Pepo ni kweli, na kwamba Moto ni kweli, basi Mwenyezi Mungu atamuingiza peponi kupitia mlango wowote katika milango ya Pepo minane atakaotaka." (Imepokelewa na Bukhari: 3435, na Muslim: 28).
Na tunaamini kwamba nyumba ya neema ni Pepo mbalimbali, kama alivyosema Mtukufu: "Na mwenye kuogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi atapata Bustani mbili." [Ar-Rahman: 46] Na amesema Mtukufu: "Na zaidi ya hizo zipo Bustani nyingine mbili." [Ar-Rahman: 62] Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Pepo mbili za fedha, vyombo vyake na vyote vilivyomo ndani yake, na Pepo (zingine) mbili za dhahabu, vyombo vyake na vilivyomo ndani yake, na hakutakuwa na chochote kitakachowazuia wakazi wa Pepo ya milele kumuona Mola wao Mlezi isipokuwa pazia la ukubwa lililoko kwenye uso wake."
Na tunaamini kuwa neema ya Peponi ni ya kudumu na haikatiki. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema: "Atakayeingia Peponi, atapata neema (starehe). Hatapata shida yoyote. Nguo zake hazitachakaa, na wala ujana wake hautaisha."
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Atanadi mwenye kunadi: "Hakika, mtapata afya nzuri na wala hamtougua abadani (milele). Na hakika, mtakuwa vijana na wala hamtazeeka abadani. Na hakika, mtastareheka na wala hamtapata shida yoyote abadani." Na hayo ndiyo kauli yake Mwenye Nguvu, Mtukufu: "Na watanadiwa kwamba: Hiyo ndiyo Pepo mliyorithishwa kwa sababu ya yale mliyokuwa mkiyafanya." [Al-A'raf: 43].
Na Mwenyezi Mungu alieleza kuhusu Moto na adhabu na mateso yaliyo ndani yake, akasema Mtukufu: "Hakika Sisi tumewaandalia wenye kudhulumu Moto ambao utawazunguka kama hema. Na wakiomba msaada, watasaidiwa kwa kupewa maji kama mafuta yaliyotibuka. Yatakayowababua nyuso zao. Kinywaji hicho ni kiovu mno! Na matandiko hayo ya kupumzikia ni mabaya mno!" [Al-Kahf: 9] Na amesema Mola wa Haki, aliyetakasika: "Kwa maji hayo vitayeyushwa vilivyomo matumboni mwao, na ngozi zao pia * Na kwa ajili yao yatakuwapo marungu ya chuma." [Al-Hajj: 20-21] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika wale waliozikufuru Ishara zetu, tutawaingiza Motoni. Kila zitakapoiva ngozi zao, tutawabadilishia ngozi nyingine ili waionje adhabu hiyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu na Mwenye hekima." [An-Nisaa: 56]
Na tunaamini kwamba Moto una daraja tofauti tofauti. Na Mola wa haki ameshabainisha kwamba wanafiki watakuwa katika tabaka za Jahiim, amesema Mtukufu: "Hakika wanafiki watakuwa katika tabaka ya chini kabisa Motoni, wala hutompata yeyote wa kuwanusuru." [An-Nisaa: 145] Imekuja ndani ya Qur’ani tukufu kwamba Moto una milango saba, amesema Mola wa haki, Mtukufu: "Ina milango saba; na kwa kila mlango iko sehemu waliyotengewa." [Al-Hijr: 44]. Na Jahannam ni makao ya adhabu ya milele, amesema Mola wa Haki: “Hakika wale waliokufuru na wakadhulumu, Mwenyezi Mungu hawi mwenye kuwasamehe wala kuwaongoa njia * Isipokuwa njia ya Jahannamu. Humo watadumu milele. Na hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi." [An-Nisaa: 168, 169].
Kitabu cha kuamini Kadari (Mipango) ya Mwenyezi Mungu
Muhtasari wa Kitabu
Na tunaamini mapitisho na Kadari za Mwenyezi Mungu, na tunajua kwa yakini kwamba kuamini mapitisho na Kadari za Mwenyezi Mungu ni nguzo ya sita ya imani, kwani kuamini Kadari ni katika kumuamini Mwenyezi Mungu; kwa sababu Kadari ni katika elimu ya Mwenyezi Mungu na makadirio yake na mipangilio yake na matashi yake na uumbaji wake.
Na Waislamu wamekubaliana kuwa kuamini Kadari ni moja katika nguzo za imani.
Na tunajua kwamba kuamini mapitisho na Kadari kunaambatana na kuamini elimu ya Mwenyezi Mungu iliyoenea na kukizunguka kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kwa elimu yake, na kuwa elimu yake imeyazunguka mambo makuu na matukufu, na makubwa na madogo, na hakuna chochote katika vilivyopo au vitakavyokuwepo, ambavyo bado havijakuwepo, isipokuwa vipo katika ubao uliohifadhiwa, hayo yote yameandikwa humo, kwa idadi yake, kiasi chake, na wakati wake ambao yatatokea, na hali ambayo yataishia.
Na kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu alijua yaliyokuwa, na yatakayokuwa, na yale ambayo lau yatatokea yatatokea vipi, na kwamba Mwenyezi Mungu aliandika Kadari ya viumbe miaka elfu hamsini kabla ya kuumba mbingu na ardhi, na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliandika kila kitu kitakachotokea katika kitabu kilichohifadhiwa.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu anaandika anachotaka, anafuta anachotaka na huthibitisha, na asili ya hukumu zote iko kwake.
Na tunaamini kuwa hakiwezi kutokea kitu isipokuwa kwa amri na kadari ya Mwenyezi Mungu, na amri haiwezi kuzuiwa isipokuwa na hukumu ya Mwenyezi Mungu na kadari yake. Kwa hivyo, alichopitisha Mwenyezi Mungu hakuna budi lazima kitokee, na alichokizuia, hakuna anayeweza kukifanya kitendeke, viumbe wote hawawezi kufanya chochote ambacho Mwenyezi Mungu hakuandika, wala kuzuia kile ambacho Mwenyezi Mungu Mtukufu alikiandika, kwa hivyo, kile ambacho kimemkosa mja, hakikuwa ni cha kumfika, na kilichomfika, hakikuwa ni cha kumkosa.
Na tunaamini kuwa alichokitaka Mwenyezi Mungu kinakuwa, na asichokitaka hakiwi, na kuwa matashi yake yamekamilika, na uwezo wake unatendeka, wala hakuna kinachoweza kuwa katika ufalme wake isipokuwa kile anachokitaka, na tunaamini kuwa waja wana matashi kihakika, lakini yanafuata matashi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alimuongoa aliyemtaka kwa fadhila zake, na akamuacha aliyemtaka kwa uadilifu wake Yeye Aliyetakasika na Kutukuka, wala haulizwi juu ya anachokifanya, lakini wao wanaulizwa, na kila utiifu wa mwenye kutii ni kutokana na kuwezeshwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kila maasi ya mwenye kuasi basi hutokana na kuachwa na Mwenyezi Mungu na yeye mwenyewe pia kumuacha Mwenyezi Mungu, na mwenye furaha ni yule iliyetangulia amri ya Mwenyezi Mungu kuwa atakuwa na furaha, na mwenye tabu ni yule iliyetangulia amri ya Mwenyezi Mungu kuwa ni mtu wa mashakani, na matendo ya waja ya heri na shari ni matendo yao wenyewe, wao ni viumbe wa Muumba wao.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu anapenda utiifu na wanaomtii, na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu anachukia kutoka nje ya sheria na wale wanaotoka nje ya sheria, na Mwenyezi Mungu anapomtakia heri mja wake, anamuwezesha kupenda mambo anayopenda na mambo ya utii, na yale anayoyaridhia kutoka kwake, na yule anayemtakia yasiyokuwa hayo, basi humsimamishia hoja, kisha humuadhibu bila ya kuwa amemdhulumu.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu haamrishi machafu, wala haridhii kufuru kwa waja wake.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa vitu vyote, na kwamba Mwenyezi Mungu aliumba waja wake, na akaumba matendo yao, na hakuna yeyote anayeshirikiana naye katika uumbaji wake, wala hakuna yeyote anayeshirikiana naye katika ufalme wake. Na Mwenyezi Mungu aliwasimamishia hoja waja kwamba Yeye peke yake ndiye Muumbaji, na yeyote mwenye kupwekeka kwa uumbaji, basi haifai kwa yeyote kudai kuwa anashirikiana naye katika uumbaji.
Na tunaamini kuwa hakuna mgongano kati ya Sheria, amri na uumbaji. Mwenyezi Mungu Mtukufu ana uumbaji, na ana amri, na kama ambavyo anafanya anavyotaka, na haulizwi kwa anachokifanya, basi anaamuru, na wala hakuna wa kurudisha hukumu yake, wala wa kurekebisa amri yake.
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alipanga mapema kadari za viumbe miaka elfu hamsini kabla ya kuumba mbingu na ardhi, lakini pamoja na hayo aliamuru atiiwe pamoja na kutiiwa Mitume wake na Manabii wake, na akakataza kumuasi na kuwaasi Mitume wake na Manabii wake, kwa hivyo, Yeye Mtukufu aliunganisha katika Kitabu chake kati ya kueleza kuhusu kupangilia kwake, na kati ya kuamrisha kufuata ufunuo wake na amri yake. Na akabainisha Mola wa Haki kuwa ni lazima kufuata uongofu, na kwamba ulimuongoa aliyemtaka kwa fadhila zake, na akampoteza aliyemtaka kwa uadilifu wake. Naye Mola wa Haki uliunganisha kati ya habari juu ya matashi yake ya jumla, na kati ya kuwatisha kwake wale wanaokwenda kinyume, na kuwaamrisha kwake waja wake waumini kumuabudu na kumtegemea, na kukusanya pamoja kati ya kuamini kadari na kuifanyia kazi sheria kunawezekana. Na Mola Mtukufu alibainisha kwamba nafsi yoyote ile haibebeshwi jambo isipokuwa kwa kadiri ya uwezo wake.
Na tunaamini kuwa kama vile hakuna kupingana kati ya uumbaji, amri, na sheria, basi hakuna kupingana kati ya sheria, amri, na akili, kwa hivyo, kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu na Mtume wake rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, walikiamrisha au kila ambacho Mwenyezi Mungu na Mtume wake walikikataza, au Mwenyezi Mungu alikipitisha, au alijulisha juu yake, basi hakiwezi kupingana na akili, bali hivyo ndivyo akili inavyoamrisha, na ndicho kilele cha hekima.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu, na akawatuma Mitume, amani iwe juu yao, ili hoja iweze kusimama juu ya viumbe. Na Sheria, na amri, na kadari vyote vinakamilishana vyenyewe kwa vyenyewe, na hilo liko katika kilele cha uzuri, bali hakuna kilicho kizuri zaidi ya hilo.
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alisifu kitabu chake, ambacho alikielezea kwamba ni Hadithi nzuri zaidi ambayo ilijumuisha sheria na amri. Kwa hivyo, kile ambacho Mwenyezi Mungu amekifanya kuwa sheria au amekipitisha, basi kiko katika kilele cha ukamilifu na uzuri; sawa akili zilifahamu au zishindwe kulifahamu, na wala hatuwezi kuzifanya akili zetu na maoni yetu kuwa hakimu juu ya sheria ya Mwenyezi Mungu na kadari zake, mara nyingine kwa kuiona ni nzuri, na mara nyingine kwa kuiona ni mbaya. Bali kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu ameamrisha na akakifanya kuwa sheria, basi hicho kimetimia katika uzuri na ukamilifu.
Na tunaamini kuwa sheria na kadari zote ni heri, na Mwenyezi Mungu hapitishi kadari mbaya halisi, lakini ubaya huingia ndani ya kile kilichokadiriwa kwa ujumla, na inatajwa katika Qur'ani huku imefungamanishwa na yule aliyeifanya, na katika heshima ni kutofungamanisha shari na Mwenyezi Mungu Mtukufu moja kwa moja.
Na tunaamini kuwa kufanya sababu za kitu hakupingani na kuamini kadari, lakini badala yake kutekeleza sababu za kitu ni katika kuamini kadari kikamilifu na mapitisho ya Mwenyezi Mungu. Na Mola wetu Mlezi aliamrisha kufanya sababu za kitu, na moja ya sababu kubwa zaidi ni dua, ndiyo akatuamrisha tuombe dua, hali yakuwa alikwishapitisha maamuzi ya mambo yote.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka anaamrisha uadilifu na anahukumu kupitia uadilifu huo sheria, makadirio, na malipo, na alijikanushia kufanya dhulma yoyote, na akathibitisha uadilifu kamili.
Na tunaamini kuwa kutangulia kwa kadari hakulazimu kwamba anawadhulumu waja; kwa sababu Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu, na akatuma Mitume; ili watu wasiwe na hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu baada ya Mitume, na akaifanya kadari kuwa siri iliyofichwa, na akawafanya waja kuwa na utashi na hiari. Kwa hivyo mwenye kuongoka, basi ni kwa faida yake mwenyewe, na mwenye kupotea ni kwa hasara yake pia.
Na tunaamini kuwa hairuhusiwi kutumia kadari kama hoja ya kufanya dhambi au kuacha ibada, na kwamba washirikina waliotumia kadari kama ndiyo iliyowafanya kufanya ushirikina, Mwenyezi Mungu alibainisha uongo wao, na akawaonjesha adhabu yake. Na kama kadari ingekuwa hoja kwao dhidi juu ya ushirikina wao huo, basi Mwenyezi Mungu asingeliwaonjesha adhabu yake.
Na tunaamini kuwa inaruhusiwa kwa mja kutumia kadari kama hoja juu ya dhambi baada ya kutubu, na pia kutumia kadari kuwa ni hoja wakati wa masaibu.
Na tunaamini kwamba ikiwa muumini atasalimisha jambo lake kwa Mwenyezi Mungu, na akarudi na kusema kwamba tutarudi sote kwa Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu humuandikia mambo matatu mazuri: Baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na rehema, na kuwezeshwa kufikia njia ya uongofu.
Mlango wa ulazima wa kuamini Kadari
Na tunaamini mapitisho na kadari za Mwenyezi Mungu, kwani Yeye Aliyetakasika na kutukuka alijua yaliyokuwa, na yale yatakayokuwa, na akayaandika hayo yote, na akataka yawepo, na akayaumba, na akayapangilia sawa sawa.
Na tunajuwa kwa elimu ya yakini kwamba kuamini hukumu na kadari na mipango ya Mwenyezi Mungu ni nguzo ya sita katika nguzo za imani, Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo." [Al-Qamar: 49] Na amesema Yeye wa Haki Mtukufu: "Na amri ya Mwenyezi Mungu ni kudura iliyokwishakadiriwa." [Al-Ahzab: 38] Na Mola Mtukufu alisema: "Na akaumba kila kitu na akakikadiria kwa kipimo." [Al-Furqan: 2] Na Mola Mtukufu alisema: "Mtume ameamini yaliyo teremshwa kwake kutoka kwa Mola Mlezi wake, na Waumini vile vile. Wote wamemuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake." [Al-Baqarah: 285] Kwa hivyo kuamini kadari ni sehemu ya kumuamini Mwenyezi Mungu, kwa sababu kadari ni sehemu katika elimu ya Mwenyezi Mungu, na mipangilio yake, na uendeshaji wake.
Na amesema Mtukufu: "Yeye ndiye anayehuisha na anayefisha akihukumu jambo liwe, basi huliambia: Kuwa! Na linakuwa." [Ghafir: 68] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ziko kwake funguo za ghaibu; hakuna azijuaye ila Yeye tu, na Yeye anajua kilichoko nchi kavu na baharini, na halidondoki jani ila analijua, wala punje katika giza la ardhi, wala kinyevu, wala kikavu ila kimo katika Kitabu kinachobainisha." [Al-An 'am: 59].
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, katika hadithi ya Jibrili amani imshukie, akasema: Basi nieleze kuhusu imani, akasema: "Ni kumwamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na vitabu vyake, na Mitume wake, na Siku ya Mwisho, na kuamini kadari kheri yake na shari yake." Akasema: Umesema ukweli. (Imepokelewa na Muslim 8, Abuu Daud 4695, Tirmidhi 2610, An-Nasai 4990, na Ibn Majah 63).
Waislamu wamekubaliana kwa kauli moja kwamba kuamini kadari ni moja ya nguzo za imani, amesema Al-Hafidh Abul-Qasim Al-Lalakaii: "Ikiwa kuna makubaliano katika dunia hii ambayo yameenea bila ya kupingwa, basi ni katika jambo hili, (yaani kuamini kadari), Kwa hivyo, itakayekwenda kinyume kauli yake na hilo, basi atakuwa mkaidi na mpinzani, na atafikiwa na ahadi ya adhabu, na ataingia ndani ya kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na anayempinga Mtume baada ya kumdhihirikia uongofu, na akafuata njia isiyokuwa ya Waumini, tutamuelekeza alikoelekea, na tutamuingiza katika Jahannamu. Na hayo ni marejeo maovu." [An-Nisaa: 115]. (Sharhu Usuulu Itiqadi Ahlus-Sunna wal-Jamaa 4/726).
Na imesimuliwa kutoka kwa 'Amri bin Shu'aib, kutoka kwa baba yake kutoka kwa babu yake yakuwa: Watu fulani walikuwa wamekaa mlangoni kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, baadhi yao wakasema: 'Je, Mwenyezi Mungu hakusema hivi na hivi?' Na baadhi yao wakasema: 'Je, Mwenyezi Mungu hakusema hivi na hivi?' Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasikia hayo, akatoka nje kana kwamba katupiwa usoni punje ya komamanga, akasema: "Hivi ndivyo mlivyoamrishwa?" Au "Mlitumwa kufanya hivi? Kukipiganisha Kitabu cha Mwenyezi Mungu chenyewe kwa chenyewe? Hakika, walipotea umma waliokuwa kabla yenu katika jambo kama hili. Hapa hamzungumzi juu ya chochote chenye manufaa kwenu. Kwa hivyo, angalieni yale mliyoamrishwa, basi yafanyeni, na yale mliyokatazwa, basi muachane nayo." (Imepokelewa na Ibn Majah 85, Ahmad 6845 na matamshi haya ni yake, na Al-Harith bin Abi Usama katika Al-Musnad - kama ilivyo katika Bughyat Al-Baahith 735, na Ibn Abi Asim katika As-Sunna 406).
Na imesimuliwa kutoka kwa 'Abdul-Malik - ikimaanisha Ibn Juraiji - kutoka kwa 'Atwa bin Abi Rabah, kuwa alisema: 'Nilikuja kwa Ibn Abbas, naye alikuwa anavuta maji kutoka katika Zamzam, huku sehemu ya chini ya nguo yake imelowa, nikamwambia: 'Limeshazungumziwa suala la kadari.' Akasema: 'Je, wamefanya hivyo?' Nikasema: 'Ndiyo.' Akasema: 'Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, aya hii haikuteremka isipokuwa kuhusiana nao: "Onjeni mguso wa Jahannamu!* Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo." [Al-Qamar: 48, 49]. Msiwatembelee wagonjwa wao, na msiwaombee wafu wao, na ukinionyesha mmoja wao, nitalitoboa jicho lake.'' (Sharhu Usuulu Itiqad Ahlus-Sunna wal-Jamaa' 3/597).
Na Ubada bin Swamit, Mwenyezi Mungu amridhie, alimwambia mwanawe: Ewe mwanangu, hakika wewe hutapata ladha ya uhakika wa imani mpaka ujue kuwa kilichokupata hakikuwa cha kukukosa, na kilichokukosa hakikuwa cha kukupata. Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akisema: "Hakika hapo mwanzo Mwenyezi Mungu aliumba kalamu. Akaiambia: "Andika." Ikasema: "Ewe Mola Mlezi, niandike nini?" Akasema: "Andika makadirio ya kila kitu mpaka Kiyama kitakapo simama." Ewe mwanangu, hakika mimi nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akisema: "Atakayekufa hali yakuwa haamini hivi, basi si miongoni mwangu." (Imepokelewa na Abuu Daud katika Sunani yake 4700, na pia ipo katika Sunnah, cha Ibn Abi 'Asim 1/51).
Na imesimuliwa kutoka kwa Yahya bin Ya'mara kuwa alisema: "Aliyekuwa wa kwanza kuzungumza kuhusiana na Kadari huko Basra ni Ma'bad Al-Juhani. Kwa hivyo nikaondoka mimi pamoja na Humaid bin Abdir-Rahman Al-Himyari kwa ajili ya kufanya Hija - au alisema: kwa ajili ya kufanya Umra - Tukasema: 'Tunatamani tukutane na mmoja katika Maswahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, tumuulize kuhusu haya wanayosema hawa kuhusiana na kadari.' Basi tukawezeshwa kukutana na Abdullah bin Omari bin Khattwab akiwa anaingia msikitini, tukasimama katika pande zake mbili mimi na huyo mwenzangu, mmoja wetu alikuwa kulia kwake na mwingine kushoto kwake. Nilidhani kwamba mwenzangu huyo ataniachia mimi nizungumze. Nikasema: 'Ewe Abuu Abdur-Rahman, hakika wametokea kwetu watu fulani wanaosoma Qur'ani, na wanatafuta elimu. Na akataja mambo yao mengine, na kwamba wanadai kuwa hakuna kitu kiitwacho kadari, na kwamba mambo yote ni mapya tu.' Akasema: "Utakapokutana nao, waambie kwamba mimi kwa hakika niko mbali nao, nao wako mbali nami. Na ninaapa kwa yule ambaye Abdullah bin Omari anaapa kwake, lau kama mmoja wao angelikuwa na dhahabu mfano wa mlima Uhudi, kisha akaitoa yote, basi Mwenyezi Mungu asingeikubali toka kwake hadi aamini kadari." (Imepokelewa na Muslim katika Muqaddimat Sahihi (8), na katika Sheria, cha Al-Aajuri 2/851).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abu Harun al-Abli - na alikuwa mmoja wa wale waliokuwa pamoja na Sahl bin Abdullah - na alikuwa mwanaume mwema, na alikuwa akitusomea Qur'ani msikitini, alisema: Sahl bin Abdullah aliulizwa kuhusu kadari, akasema: "Kuamini kadari ni lazima, na kuikadhibisha ni ukafiri, na kuizungumzia ni uzushi, na kuinyamazia ndiyo Sunna." (Sharhu usuulu Itikadi Ahlus-Sunna wal-Jamaa' 4/786).
Na imesimuliwa kutoka kwa Hasan Al-Basri, kuwa alisema: "Kalamu imekwishakauka, na hukumu imekwishapitishwa, na kadari ikatimia kwa kutimia kwa andiko na kuwasadikisha Mitume, na furaha kwa mwenye kutenda mazuri na akamcha Mwenyezi Mungu, na uovu kwa mwenye kudhulumu na akavuka mipaka, na kwa urafiki mkubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa waumini, na kujiweka mbali kwa Mwenyezi Mungu na washirikina." (Sheria cha Al-Aajurri 2/881).
Amesema bin Batta al-Akbari: "Kisha baada ya hapo, ni kuamini Kadari; njema yake na mbaya yake, na tamu yake na chungu yake, na kidogo yake na nyingi yake kwamba yote hayo yamekadiriwa na ni lazima yatokee kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa waja wake, na kwa wakati anaotaka yatokee, na wala hayatangulii, wala hayachelewi kulingana na namna ambayo imetangulia elimu ya Mwenyezi Mungu, na kuwa kinachompata mja hakikuwa cha kumkosa. Na kilichomkosa, hakikuwa cha kumpata. Na kilichotangulia, hakikuwa cha kuchelewa. Na kilichochelewa hakikuwa cha kutangulia. Kuamini hivi ni haki ya lazima, na ni wajibu kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu juu ya viumbe wake. Kwa hivo, mwenye kukiuka hilo, au kutoka nje yake, au akalitia dosari kwa kutomthibitishie Mwenyezi Mungu Mtukufu Kadari (Upangaji wa mambo), na kuyafungamanisha naye, basi huyo ndiye mpotofu wa kwanza." (Ash-sharhu wal ibana Alaa Usuulis sunna wad-diyaana, cha Ibn Batta uk. 213-216).
Mlango wa mambo yanayoambatana na kuamini Kadari
Na tunaamini kwamba kuamini Kadari kunaambatana na kuamini kujua kwa Mwenyezi Mungu kunakokienea kila kitu, na kunakozunguka kila kitu, na kwamba Yeye Aliyetakasika na kutukuka anajua vilivyomo mbinguni na vilivyomo duniani, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, hujui kwamba Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na katika ardhi? Hakika hayo yamo Kitabuni. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi." [Al-Hajj: 70] Na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kwa elimu yake, amesema Mola Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ni yule ambaye ameziumba mbingu saba, na ardhi kwa mfano wa hizo. Amri zake zinashuka baina yake, ili mjue kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza juu ya kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kwa kukijua vilivyo kwa elimu yake." [Talaq: 12].
Na kwamba elimu yake imezunguka mambo makuu na matukufu, na makubwa na madogo, amesema Mola Mtukufu: "Na ziko kwake funguo za ghaibu; hakuna azijuaye ila Yeye tu. Na Yeye anajua kilichoko nchi kavu na baharini. Na halidondoki jani ila analijua. Wala punje katika giza la ardhi, wala kinyevu, wala kikavu ila kimo katika Kitabu kinachobainisha." [Al-An'am: 59]. Amesema bin Jariri, Mwenyezi Mungu amrehemu, wakati wa kutafsiri aya hii: "Na hakuna kitu chochote kilichopo, au kitakachokuwepo na ambacho hakijakuwepo bado, isipokuwa kimewekwa sawa sawa katika ubao uliohifadhiwa, ambao hayo yameandikwa ndani yake pamoja na idadi yake na kiasi chake, na wakati ambapo yatatokea, na hali ambayo yataishia. Na anamaanisha, kwa kauli yake, "kinachobainisha" Yaani: Kinabainisha usahihi wa yale yaliyo ndani yake kulingana na namna yalivyoandikwa." (Tafsir Tabari: 11/403).
Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Anajua yanayoingia katika ardhi na yanayo toka humo, na yanayo teremka kutoka mbinguni, na yanayo panda huko. Na Yeye ni Mwenye kurehemu, Mwenye kusamehe * Na walisema wale waliokufuru: Haitatufikia Saa (ya Kiyama). Sema: Kwani? Hapana shaka itakufikieni, naapa kwa haki ya Mola wangu Mlezi, Mwenye kujua ya ghaibu! Hapana kinachofichikana kwake hata chenye uzito wa chembe tu, si katika mbingu wala katika ardhi, wala kilicho kidogo kuliko hivyo, wala kikubwa zaidi; ila vyote hivyo vimo katika Kitabu chake chenye kubainisha. [Saba: 2,3].
Na imesimuliwa kutoka kwa Imran bin Huswain, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Wakati mmoja nilikuwa pamoja na Mtume rehema na amani zimshukie, na tazama, alijiwa na watu kutoka katika kabila la Banu Tamim, akasema: "Ikubalini bishara njema enyi Banu Tamim." Wakasema: "Umetubashiria, basi tupe." Kisha watu fulani kutoka Yemen wakaingia, akasema: "Ikubalini bishara njema enyi watu wa Yemen, kwa maana Banu Tamim hawakuikubali." Wakasema: "Tumeikubali. Tumekujia ili tuifahamu dini yetu, na kukuuliza kuhusu jambo hili (Ulimwengu) ulianza lini?" Akasema: "Mwenyezi Mungu alikuwako, na hakikuwepo kitu kabla yake, na Kiti chake cha Enzi kilikuwa juu ya maji, kisha akaumba mbingu na dunia, na akaandika katika kumbukumbu kila kitu." Kisha mtu mmoja akanijia, akasema: "Ewe Imran, Ngamia wako katoroka" Basi, nikaenda kumtafuta, ghafla nikaona mazingazi yakitandaa pembezoni mwake, ninaapa kwa Mwenyezi Mungu, nilitamani lau yangetoweka, nami nisingesimama. (Imepokewa na Bukhari: 7418, na Tirmidhi: 3951).
Na Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka alikwishajua yaliyokuwapo, na yatakayokuja kuwapo, na yale ambayo lau kuwa yangetokea, yangetokea vipi. Mwenyezi Mungu alisema - akieleza juu ya wanafiki kuwa lau wangetoka pamoja na waumini, wasingewaongezea isipokuwa mchafuko, nao hawakutoka pamoja nao-: "Lau wangelitoka pamoja nanyi, wasingeliwazidishia ila mchafuko, na wangetangatanga kati yenu kuwatakia majaribio. Na miongoni mwenu wapo wanaowasikiliza. Na Mwenyezi Mungu anawajua vyema madhalimu." [Tauba: 47].
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu watu wa Motoni: "Na unge ona watakapo simamishwa kwenye Moto, wakawa wanasema: Laiti tungeli rudishwa, wala hatutakanusha tena Ishara za Mola wetu Mlezi, na tutakuwa miongoni mwa Waumini. Bali yamewadhihirikia yale waliyokuwa wakiyaficha zamani. Na kama wangelirudishwa, bila ya shaka wangeyarejea yale yale waliyokatazwa. Na hakika hao ni waongo." [Al-An'am: 27, 28]. Basi akawa ametaja kwamba ikiwa wangerejeshwa katika dunia hii, wangerejea katika ukafiri wao, ilhali bado hawajaingizwa Motoni. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na walisema walio kufuru: Haitatufikia Saa (ya Kiyama). Sema: Kwani? Hapana shaka itakufikieni, naapa kwa haki ya Mola wangu Mlezi, Mwenye kujua ya ghaibu! Hapana kinacho fichikana kwake hata chenye uzito wa chembe tu, si katika mbingu wala katika ardhi, wala kilicho kidogo kuliko hivyo, wala kikubwa zaidi; ila vyote hivyo vimo katika Kitabu chake chenye kubainisha." [Saba': 3].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliandika kila kitu kitakachokuja kuwepo katika kitabu kilichohifadhiwa, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na huwi katika jambo lolote, wala husomi sehemu yoyote katika Qur'ani, wala hamtendi kitendo chochote ila Sisi huwa ni mashahidi juu yenu mnapo shughulika nayo. Na hakifichikani kwa Mola wako Mlezi chenye uzito hata wa chembe katika ardhi na katika mbingu, wala kidogo kuliko hicho wala kikubwa ila kimo katika Kitabu kilicho wazi." [Yunus: 61] Na amesema Mtukufu: "Je, hujui kwamba Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na katika ardhi? Hakika hayo yamo Kitabuni. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi." [Al-Hajj: 70] Na amesema Mtukufu: "Hautokei msiba katika ardhi wala katika nafsi zenu ila umekwisha andikwa katika Kitabu kabla hatujauumba. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi." [Al-Hadid: 22].
Na imepokelewa na Abdallah bin Amr bin Aaswi, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akisema: "Mwenyezi Mungu aliandika Kadari ya viumbe kabla ya kuumba mbingu na dunia kwa miaka elfu hamsini (50,000). Akasema: Na kiti chake cha enzi kilikuwa juu ya maji." (Imepokelewa na Muslim: 2653, na Tirmidhi: 2156).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika mwanzo Mwenyezi Mungu alipoiumba kalamu, aliiambia: "Andika." Ikasema: "Niandike nini?" Akasema: "Andika makadirio ya yale yaliyokuwa kabla, na yale yatayokuwa hadi milele." (Imepokelewa na Abuu Daud: 4700, Tirmidhi: 2155, 3319, At-Tayyalisi: 578, Ahmad: 22705, 22707, na Ibn Abi Asim katika As-Sunna: 115).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake amesema: "Mwenyezi Mungu alipomaliza uumbaji, aliandika kitabu alicho nacho: "Huruma yangu imeshinda ghadhabu yangu." Au alisema, "Rehema yangu imetangulia ghadhabu yangu." Nacho kiko kwake juu ya Kiti cha Enzi." Imepokelewa na Bukhari: 7553, Muslim: 2751, Tirmidhi: 3543, na Ibn Majah: 189).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu anaandika anachotaka na anafuta anachotaka na anathibitisha, na anacho kitabu cha asili, amesema Mola wa Haki- na kuali yake ni ya haki: "Mwenyezi Mungu hufuta na huthibitisha ayatakayo. Na asili ya hukumu zote iko kwake." [Ra'd: 39].
Na tunaamini kuwa kitu hakiwezekani isipokuwa kwa hukumu na makadirio yake Mwenyezi Mungu, na haiwezekani kuzuia amri isipokuwa hukumu na kadari ya Mwenyezi Mungu. Kwa hivyo, alichopitisha Mwenyezi Mungu, lazima kitokee hakuna budi. Na alichokiondoa, hakuna yeyote anayeweza kukifanya kitendeke. Viumbe wote hawawezi kufanya chochote ambacho Mwenyezi Mungu hakuandika, wala kuzuia kile ambacho Mwenyezi Mungu Mtukufu alikiandika. Hivyo, kilichomkosa mja hakikuwa ni cha kumfika. Na kilichomfika, hakikuwa ni cha kumkosa. Imesimuliwa kutoka kwa Abdallah bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: Nilikuwa nyuma ya Mtume wa Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ewe kijana, hakika mimi ninakufundisha maneno haya: Mhifadhi Mwenyezi Mungu, yeye pia atakuhifadhi. Mhifadhi Mwenyezi Mungu, utampata mbele yako. Unapoomba, muombe Mwenyezi Mungu. Na ukitafuta msaada, tafuta msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na jua kwamba ikiwa umma wote lau watakusanyika pamoja, ili wakunufaishe kwa kitu, hawawezi kukunufaisha isipokuwa kwa kitu ambacho Mwenyezi Mungu alikwishakuandikia. Na lau kuwa watakusanyika ili wakudhuru kwa kitu, hawawezi kukudhuru isipokuwa kwa kitu ambacho Mwenyezi Mungu alikiandika juu yako. Kalamu zimeshainuliwa, na vitabu vikakauka." (Imepokelewa na Tirmidhi: 2516, Ibn Wahab fi Al-Qadr 28, Ahmad: 2669, na Abdul-Hamid: 636).
Na tunaamini kuwa kile anachokitaka Mwenyezi Mungu kinakuwa. Na asichokitaka hakiwezi kuwa, na kuwa matashi yake ni timilifu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mola wako Mlezi huumba na huteuwa atakavyo. Viumbe hawana khiari. Mwenyezi Mungu ametukuka na ametakasika na hao wanao washirikisha naye." [Al-Qasas: 68] Na amesema Mtukufu: "Wala nyinyi hamtataka isipokuwa atake Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote." [At-Takwir: 29]. Na uwezo wake unatekelezeka, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hapana kitu kinacho weza kumshinda Mwenyezi Mungu mbinguni wala katika ardhi. Hakika Yeye ni Mwenye kujua, Mwenye uwezo." [Faatir: 44] Na amesema Mtukufu: "Na angelipenda Mola wako Mlezi wasingeli fanya hayo. Basi waache na wanayoyazua." [Al-An'am: 112].
Na hakuna kitu kinachoweza kuwa katika ufalme wake isipokuwa kile anachotaka, amesema Mola wa Haki: "Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angelipenda wasingeli pigana walio kuwa baada yao baada ya kuwajia hoja zilizo wazi. Lakini walikhitilafiana. Basi wapo kati yao walioamini, na wengine kati yao walio kufuru. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angelipenda wasingeli pigana. Lakini Mwenyezi Mungu hutenda atakavyo." [Al-Baqarah: 253].
Na tunaamini kuwa waja pia wana matashi ya hakika, lakini yanafuatana na matashi ya Mwenyezi Mungu, amesema Mola Mtukufu: "Wala hamuwezi kutaka ila atakapo Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye elimu, Mwenye hekima." [Al-Insaan: 30] Na alisema Mola wa Haki, Mtukufu: "Kwa yule miongoni mwenu anayetaka kwenda sawa * Wala nyinyi hamtataka isipokuwa atake Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote." [At-Takwir: 28, 29] Na amesema Mtukufu: "Hakika haya ni mawaidha; basi anayetaka atashika Njia ya kwenda kwa Mola wake Mlezi." [Al-Insaan: 29]. Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Hiyo ndiyo Siku ya haki. Basi anayetaka na ashike njia arejee kwa Mola wake Mlezi." [Al-Nabaa: 39].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu amemuongoa amtakaye kwa fadhila zake, na akamuachilia mbali amtakaye kwa uadilifu wake. Haulizwi atendalo, nao wanaulizwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na waliokanusha Ishara zetu ni viziwi na mabubu waliomo gizani. Mwenyezi Mungu humwachia kupotea amtakaye, na humweka katika Njia iliyo nyooka amtakaye." [Al-An'am: 39] Na amesema Mtukufu: "Basi yule ambaye Mwenyezi Mungu anataka kumuongoa humfungulia kifua chake kwa Uislamu. Na anayetaka apotee hukifanya kifua chake kina dhiki, kimebana, kana kwamba anapanda mbinguni. Namna hivi Mwenyezi Mungu anajaalia uchafu juu ya wasioamini." [Al-An'am: 125] Na amesema Mola wa Haki: "Na lau tungelitaka tungempa kila mtu uongofu wake. Lakini imekwisha kuwa kauli iliyo toka kwangu: Kwa yakini nitaijaza Jahannamu kwa wote hawa, majini na watu." [Sajdah: 13].
Imesimuliwa kutoka kwa Abubakari Al-Mirwadhi, alisema kuwa: "Nilimsikia Abu Abdallah - Yaani Ahmad bin Hanbal - akisema: Walimuuliza Abdur-Rahman bin Mahdi kuhusu Kadari, akawaambia: Heri na shari hutokea kwa Kadari." (Al-Ibana Al-Kubra, cha Ibn Batta: 4/261).
Na alisema Abubakari bin Abi Asim: "Uliuliza kuhusu Sunna, ni nini? Sunna ni jina linalojumuisha maana nyingi katika hukumu mbalimbali na mengineyo. Na katika yale ambayo wasomi walikubaliana juu yake kwamba yanahusiana na Sunna ni: kauli ya kuthibitisha Kadari, na kuamini Kadari njema yake na mbaya yake, tamu yake na chungu yake. Na kila utiifu wa mwenye kutii ni kutokana na kuwezeshwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu. Na kila uasi wa mwenye kuasi, basi ni kutokana na kuachwa na Mwenyezi Mungu na yeye pia kumuacha Mwenyezi Mungu. Na mwenye furaha ni yule ambaye ilitangulia kadari kuwa ni mwenye furaha, na muovu ni yule ambaye ilitangulia Kadari kuwa ni muovu. Na matendo ya waja ya heri na shari ni matendo yao wenyewe, na yameumbwa na Muumba wao." (Sunna, Ibn Abi Asim 2/645).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu anapenda utiifu na watiifu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lakini Mwenyezi Mungu amekupendezeeni Imani, na akaipamba katika nyoyo zenu, na amekufanyeni muuchukie ukafiri, na upotovu, na uasi. Hao ndio walioongoka." [Al-Hujurat: 7] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume, hao wa pamoja na wale alio waneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa Manabii, na Masiddiqi, na Mashahidi, na Watu wema. Na uzuri ulioje kuwa pamoja na watu hao!" [An-Nisaa: 69] Na amesema Mtukufu: "Na fanyeni wema. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema." [Al-Baqarah: 195] Na amesema Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wanao tubu na huwapenda wanaojisafisha." [Al-Baqara: 222] Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika Mwenyezi Mungu anapenda upigaji chafya, na anachukia upigaji wa miayo." (Imepokelewa na Bukhari 6223, Muslim 2994, Abuu Daud 5028, Tirmidhi 2746, na Ibn Maja 968).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Mwenyezi Mungu anapompenda mja, humuita Jibril: Hakika Mwenyezi Mungu anapenda fulani, kwa hivyo mpende..." (Imepokelewa na Bukhari 6040, na Muslim 2637, na Tirmidhi 3161).
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu anachukia kuvuka mipaka na wavukao mipaka, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Enyi mlio amini! Wanaume wasiwadharau wanaume wenzao, wala wanawake wasiwadharau wanawake wenzao. Huenda hao wakawa bora kuliko wao. Wala msivunjiane heshima, wala msiitane kwa majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya kwisha amini. Na wasio tubu, hao ndio wenye kudhulumu." [Al-Hujurat: 11] Amesema Mtukufu: "Kwani Mwenyezi Mungu hawapendi waanzao uadui" [Baqara: 190] Na amesema Mola Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu hapendi uharibifu" [Baqara: 205].
Na imesimuliwa kutoka kwa Othman Al-Batti, kuwa alisema: Niliingia kwa bin Siirin, akaniambia: "Watu wanasema nini kuhusu kadari?" Akasema (Othman): Sijui nilichomjibu." Kisha akasema: "Akainua kitu kutoka ardhini, kisha akasema, hakuna kitakachozidi katika yale nitakayokueleza isipokuwa mfano wa hiki, (Kuna mengi zaidi katika kitabu cha 'Sheria' cha Al-Aajurri kuliko hayo 2/887). Hakika Mwenyezi Mungu anapomtakia heri mja wake humuwezesha kupenda mambo anayoyapenda na mambo ya utiifu, na yale anayoyaridhia kutoka kwake. Na mwenye kumtakia yasiyokuwa hayo, basi humsimamishia hoja, kisha humuadhibu bila ya kuwa amemdhulumu". (Al-Qadar, cha Faryabi uk. 263).
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu haamrishi machafu, wala haridhii kufuru kwa waja wake, amesema Mwenyezi Mungu: "Hakika Mwenyezi Mungu haamrishi mambo machafu." [Al-A'raaf: 28] Na amesema Mwenyezi Mungu aliyetukuka mamlaka yake: "Lakini haridhii kufuru kwa waja wake. Na mkishukuru Yeye hufurahika nanyi." [Az-Zumar: 7].
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye muumba wa vitu vyote, amesema Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu." [Az-Zumar: 62] Na kwamba Mwenyezi Mungu aliwaumba waja wake, na akaumba matendo yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba nyinyi na hivyo mnavyovifanya!" [As-Saffat: 96] Hakuna yeyote anayeshirikiana naye katika uumbaji wake, kama ambavyo hakuna yeyote anayeshirikiana naye katika ufalme wake, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Ambaye ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, wala hakuwa na mwana, wala hakuwa na mshirika katika ufalme, na akaumba kila kitu na akakikadiria kwa kipimo." [Al-Furqan: 2]
Na Mwenyezi Mungu alisimamisha hoja juu ya viumbe kwamba Yeye pekee ndiye Muumba, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sisi tumewaumba nyinyi; basi hamsadiki? (Hamuamini?)* Je, mnaiona mbegu ya uzazi mnayoidondokeza?* Je, mnaiumba nyinyi, au ni Sisi ndio Waumbaji?" [Al-Waqi'a: 57-59]. Nao, hata kama ni uthibitisho juu ya ufufuo, ni ushahidi juu ya upekee wake - Aliyetakasika - katika uumbaji, Mwingi wa baraka, Mtukufu.
Mlango wa Hakuna mgongano kati ya amri, sheria, uumbaji na akili
Na tunaamini kuwa hakuna mgongano kati ya sheria, amri na uumbaji, uumbaji ni wa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, na anayo amri. Na kama vile Yeye hufanya anavyotaka, na haulizwi kwa anachofanya, basi pia huamrisha, na wala hakuna wa kuzuia hukumu yake, wala wa kurekebisha amri yake, amesema Mola wa haki Mtukufu: "Hakika Mola Mlezi wenu ni Mwenyezi Mungu aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Kisha akatulizana juu ya Kiti cha Enzi. Huufunika usiku kwa mchana, ufuatao upesi upesi. Na jua, na mwezi, na nyota zinazotumika kwa amri yake. Fahamuni! Kuumba na amri ni zake. Ametukuka kabisa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-A'araf: 54]
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alikadiria mapema kadari za viumbe miaka elfu hamsini kabla ya kuumba mbingu na dunia. Lakini pamoja na hilo, aliamuru atiiwe na watiiwe Mitume wake na Manabii wake, na akakataza kumuasi na kuwaasi Mitume wake na Manabii wake, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu akikupatisha madhara, basi hapana wa kukuondolea ila Yeye. Na akikutakia kheri, basi hapana awezaye kurudisha fadhila yake. Huifikisha kwa amtakaye katika waja wake, na Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwingi wa kurehemu * Sema: Enyi watu! Haki imekwisha kukujieni kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Basi anaye ongoka anaongoka kwa faida ya nafsi yake, na anaye potea anapotea kwa hasara ya nafsi yake. Na mimi si mwakilishi juu yenu * Na wewe fuata yanayo funuliwa kwako kwa wahyi. Na vumilia mpaka Mwenyezi Mungu ahukumu, na Yeye ndiye mbora wa mahakimu." [Yunus: 107-109]. Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu akaunganisha katika aya hii kati ya kueleza kuwa alikwishapangilia mambo, na akaamrisha kufuata ufunuo wake na amri yake, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Fuata yale uliyofunuliwa kutoka kwa Mola wako Mlezi. Hapana mungu ila Yeye. Na jitenge mbali na washirikina * Na lau Mwenyezi Mungu angelipenda, wasingelishirikisha (vitu vingine). Na Sisi hatukukufanya wewe uwe mtunzaji wao. Wala wewe si mlinzi juu yao." [Al-An'am: 106-107] Kwa hivyo, Mola wa Haki akabainisha kwamba la wajibu ni kufuata uongofu, na kwamba alimuongoa amtakaye kwa sababu ya fadhila zake, na akampotosha amtakaye kwa uadilifu wake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mola wako Mlezi angelipenda angewafanya watu wote wakawa umma mmoja. Lakini hawaachi kuhitilafiana * Isipokuwa wale ambao Mola wako Mlezi amewarehemu; na kwa hiyo ndio Mwenyezi Mungu amewaumba. Na litatimia neno la Mola wako Mlezi: Kweli kweli nitaijaza Jahannam kwa majini na watu pamoja * Na yote tunayokusimulia katika khabari za Mitume ni ya kukupa nguvu moyo wako. Na katika haya imekujia haki na mawaidha na ukumbusho kwa Waumini * Na waambie wale wasio amini: Fanyeni muwezavyo, nasi pia tunafanya* Na ngojeni, na sisi tunangoja* Na ni vya Mwenyezi Mungu tu vyote vilivyo fichikana katika ardhi na mbingu, na mambo yote yatarejezwa kwake. Basi muabudu Yeye na umtegemee Yeye. Na Mola wako Mlezi haghafiliki na yale mnayoyatenda." [Hud: 118-123]. Katika aya hizi pia Mwenyezi Mungu aliunganisha kati ya kueleza juu ya utashi wake wa jumla, na kuwaahidi adhabu wale wanaokwenda kinyume, na kati ya kuwaamuru waja wake waumini wamuabudu na kumtegemea.
Na kuunganisha kati ya kuamini kadari na kufanya matendo kulingana na Sheria ni kitu kinachowezekana na kiko ndani ya uwezo; Na ndiyo maana, Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema: "Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kiasi iwezavyo" [Al-Baqara: 286] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Na hatuilazimishi nafsi ila kwa kiasi ya uwezo wake." [Al-Muminun: 62].
Na Mwenyezi Mungu alituamuru tuwe wavumilivu juu ya kadari zake zenye kuumiza, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hapana shaka tutakujaribuni kwa chembe ya hofu, na njaa, na upungufu wa mali na watu na matunda. Na wabashirie wanaosubiri." [Al-Baqarah: 155] Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Hakika wenye subira watapewa ujira wao bila ya hesabu." [Az-Zumar: 10].
Na amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika watu wenye majaribio makubwa zaidi ya watu wote ni Manabii, kisha wale wanaowafuata, kisha wale wanaowafuata, kisha wale wanaowafuata." (Imepokelewa na Ishaq bin Rahawaihi 2413, Ahmad katika Al-Musnad 27079, Ibn Abi Duniah katika Al-maradh wal kaffaraati 6, na An-Nasai katika Al-Kubra 7440).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amridhie kuwa alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Majaribio hayaachi kumpata muumini wa kiume na muumini wa kike katika nafsi yake, na watoto wake, na mali yake mpaka atakapokutana na Mwenyezi Mungu ilhali hana dhambi hata moja." (Imepokelewa na Tirmidhi 7859, Ibn Abi Shaiba 10916, Ahmad katika Al-Musnad 7859), na Hannad ibn As-Sari katika Az-Zuhd 402).
Na Imepokelewa na Ally Mwenyezi Mungu amridhie, alisema kuwa: Tulikuwa kwenye mazishi huko Baqi Al-gharqad, kisha Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akatujia na akaketi nasi pia tukaketi kandoni mwake. Na alikuwa ameshika kijiti, basi akaangalia chini, na akaanza kukwaruza ardhi kwa kijiti hicho. Kisha akasema: "Hakuna yeyote miongoni mwenu, hakuna nafsi yoyote isipokuwa ameandikiwa mahali pake Peponi na Motoni, isipokuwa imeshaandikiwa kuwa ni ya mashakani au ya furahani." Basi, mtu mmoja akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, basi si tuache tu kufanya matendo? Ili atakayekuwa miongoni mwetu ni katika watu wa furaha, basi ataishia kufanya matendo ya watu wa furaha. Na atakayekuwa miongoni mwetu ni katika watu wa mashakani, basi ataishia kufanya matendo ya watu wa mashakani." Mtume akasema: "(Hapana msiache) Ama watu wa furaha, watarahisishiwa kufanya matendo ya furaha. Na ama watu wa mashakani, wao watarahisishiwa kufanya matendo ya mashakani." Kisha akasoma: "Ama mwenye kutoa na akamchamungu. Na akaliwafiki lilio jema." hadi mwisho wa aya [Al-Lail: 6]." (Imepokelewa na Bukhari (362, Muslim 2647, Abuu Daud 4694, na Tirmidhi 3344).
Na imesimuliwa kutoka kwa Imran bin Huswain, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa mwanaume mmoja alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je watu wa Peponi na wa Motoni wanajulikana tayari?" Akasema: "Ndiyo," Akasema: Kwa nini watu wafanye matendo?" Akasema: "Kila mmoja wao anafanya aliyoumbiwa kuyafanya." au "anafanya aliyorahisishiwa kufanya." (Imepokelewa na Bukhari 6596, Muslim 2649, na Abuu Daud 4709).
Na imepokelewa na Jabir Mwenyezi Mungu amridhie, alisema kuwa: Alikuja Suraqa bin Malik bin Ju'shum akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu tubainishie dini yetu kana kwamba tumeumbwa sasa, ni kwa matendo gani tunayoyafanya leo? Je, ni yale ambayo kalamu zilikwishayaandika na zikakauka na yakaamuliwa tayari, au ni katika yale yajayo mbeleni?" Akasema: "Hapana, ni katika yale ambayo kalamu zilikwishayaandika na zikakauka na yakaamuliwa tayari." Akasema: "Basi kwa nini tutende matendo?" Zuhair akasema: Kisha Abuu Zubair akasema kitu ambacho sikuelewa. Nikauliza: Amesema nini? Akasema: "Nyinyi fanyeni matendo. Kila mtu amerahisishiwa (Kuyatenda aliyoandikiwa)." (Imepokelewa na Muslim 2648).
Na imesimuliwa kutoka kwa Sahl bin Sa'ad As-Saaidi, Mwenyezi Mungu amridhie, amesema, amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika mja anawezakufanya jambo - katika yale wanayoyaona watu - kuwa ni matendo ya watu wa Peponi, hali yakuwa ni miongoni mwa watu wa Motoni. Na anawezakufanya jambo - katika yale wanayoyaona watu kuwa - ni matendo ya watu wa Motoni, hali yakuwa ni miongoni mwa watu wa Peponi. Na hakika matendo huzingatiwa mwisho wake." (Imepokelewa na Bukhari 6493, na Muslim 112)
Amesema imam Al-Aajurri akieleza kuhusu Mwenyezi Mungu yakwamba yeye: "Alipenda utiifu kutoka kwa waja wake na akaamuru watii, hivyo hilo likatokea kwa wanaomtii kwa kuwawezesha kwake. Na akakataza kumuasi, na akataka yatokee, si kwamba anayapenda, wala anayaamsrisha, Mwenyezi Mungu ametukuka na kuamrisha machafu, au kuyapenda. Na Mwenyezi Mungu ni Mtukufu mno hakifanyiki kitu katika ufalme wake ambacho hakutaka kifanyike, au kitu ambacho hakukijuwa kabla ya kutokea kwake. Naye alikwishajuwa yale ambayo viumbe watatenda kabla ya kuwaumba, na baada ya kuwaumba, na kabla ya wao kuyafanya matendo hayo, aliyajua fika kulingana na kadari waliyoandikiwa, kwa maana tayari kalamu ilikwisha andika kwa amri ya Mwenyezi Mungu katika ubao uliohifadhiwa kuhusiana na yatakavyokuwa, kama mema na maovu. Naye huwasifu wale wanaomtii katika waja wake, na anafungamanisha matendo na aliyeyatenda hasa, na anawaahidi malipo makubwa juu yake, na lau kuwa si Yeye kuwawezesha, basi wasingeweza kufanya hayo ambayo yamewasababishia kupata thawabu. "Hiyo ndiyo fadhila ya Mwenyezi Mungu, humpa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kuu." (Al-Hadid: 21) Na vile vile aliwakashifu watu wanaomuasi, na akawaahidi adhabu juu yake, na akafungamanisha matendo hayo na wao, kulingana na walivyoandikiwa. Anampoteza amtakaye, na anamuongoa amtakaye." (Kitabu As sharia, cha Al-Aajurri 2/702).
Na tunaamini kwamba kama vile hakuna kupingana kati ya uumbaji, amri, na sheria, basi hakuna kupingana kati ya sheria, amri, na akili. Kwa hivyo, kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, walikiamuru, au kila ambacho Mwenyezi Mungu na Mtume wake walikataza, au Mwenyezi Mungu alikipitisha, au alikieleza, basi vyote hivyo haviwezi kupingana na akili, bali hivyo ndivyo zinavyoamrisha akili, na ndicho kilele cha hekima. Mwenyezi Mungu Mwenye hekima, Ajuaye zaidi anasema: "Hayo ni katika hekima alizokufunulia Mola wako Mlezi. Wala usimuweke pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwingine, ukaja kutupwa katika Jahannamu ukilaumiwa na kufurushwa." [Al-Israa: 39] Na amesema Mtukufu: "Hekima ya hali ya juu; lakini maonyo hayafai kitu!" [Al-Qamar: 5] Na amesema Mola wa Haki: "Na Mwenyezi Mungu amekuteremshia Kitabu na hekima." [An-Nisaa: 113] Na kwa hayo ndiyo hoja inasimama juu ya viumbe, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Basi Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye hoja ya kukata. Na kama angelipenda angeliwaongoa nyote." [Al-An'am: 149]. Na sheria na amri na kadari hii, yote hayo yako katika kilele cha uzuri, bali hakuna kilicho kizuri kuliko hayo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, wao wanataka hukumu za Kijahiliya? Na nani aliye mwema zaidi katika kuhukumu kuliko Mwenyezi Mungu kwa watu wenye yakini?" [Al-Maida: 50].
Na imesimuliwa kutoka kwa bin Dailami alisema kuwa: "Nilimjia Ubay bin Ka'ab, nikamwambia; Ninahisi kitu katika nafsi yangu kuhusiana na suala la kadari. Kwa hivyo, niambie kitu ambacho huenda Mwenyezi Mungu akaiondoa hisia hii moyoni mwangu. Akasema: "Lau kuwa Mwenyezi Mungu angewaadhibu wakazi wa mbingu zake zote na wakazi wa ardhi yake, angekuwa amewaadhibu bila ya kuwadhulumu. Na lau kuwa angewarehemu, basi ingekuwa rehema yake hiyo ni heri kwao kuliko matendo yao. Na lau kuwa ungetoa dhahabu mfano wa (Mlima) Uhud katika njia ya Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu asingeikubali kutoka kwako mpaka uamini kadari, na ujue kwamba yaliyokupata, hayakuwa ni ya kukukosa. Na yaliyokukosa, hayakuwa ni ya kukupata, na kama ungekufa kwa imani isiyokuwa hii, basi ungeingia Motoni. Akasema: Kisha nikamwendea Abdallah bin Mas'ud, naye pia akasema hivyo hivyo. Akasema: Kisha nikamwendea Hudhaifa bin Al-Yaman, naye akasema hivyo hivyo. Akasema: Kisha nikamwendea Zaidi bin Thabit, naye akanisimulia hivyo hivyo kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake." (Imepokelewa na Abuu Daud 4699, Ibn Majah 77, Ahmad 21589, 'Abd ibn Humaid 247, na al-Fariyabi katika al-Qadar 190, na Sherhu Usuulu iitiqaadi Ahlus-Sunna wal- Jama'ah 4/676).
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akikisifu kitabu chake, ambacho kinajumuisha sheria na amri kwamba ndiyo hadithi bora zaidi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ameteremsha hadithi nzuri kabisa, Kitabu chenye kufanana na kukaririwa" [Az-Zumar: 23]. Kile alichokifanya Mwenyezi Mungu kuwa sheria au kadari yake, hayo yako katika kilele cha ukamilifu na uzuri; sawa ziwe akili zinakifahamu au ziwe zimeshindwa kukifahamu, na hatufai kuzifanya akili zetu na maoni yetu kuwa ndiyo yanahukumu juu ya sheria ya Mwenyezi Mungu na kadari yake; mara kwa kuona kwamba ni mazuri, na mara kwa kuona kuwa ni mabaya. Bali kila kitu ambacho Mwenyezi Mungu amekipitisha na kukifanya kuwa sheria basi ni kikamilifu katika uzuri na ukamilifu.
Na tunaamini kuwa sheria na kadari vyote viwili ni heri. Na Mwenyezi Mungu hapitishi uovu mtupu, amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Na heri yote iko mikononi mwako, na uovu haufungamanishwi na Wewe." (Imepokelewa na Muslim 771, Abuu Daud 761, Tirmidhi 266, na An-Nasai 897).
Uovu unaingia ndani ya ujumla wa kadari, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kadari (kipimo)." [Al-Qamar: 49] Na uovu unatajwa katika Qur'ani huku umefungamanishwa na wale walioufanya haswa, amesema Mwenyezi Mungu: "Sema: Ninajikinga kwa Mola Mlezi wa mapambazuko * Na kutokana na shari ya alivyoviumba." [Al-Falaq: 1, 2].
Na ni sehemu ya kuwa na adabu mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwa maovu yasifungamanishwe na naye, amesema Mola Mtukufu akieleza juu ya majini kwamba walisema: "Nasi hatujui kama wanatakiwa shari wale wanao kaa kwenye ardhi au Mola wao Mlezi anawatakia uongofu." [Al-Jinn: 10] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu Ibrahim amani imshukie, kuwa alisema: "Na ninapougua, ni Yeye ndiye anayeniponesha." [Ashu'araa: 80] Hapa akawa amefungamanisha ugonjwa na yeye mwenyewe, na akafungamanisha uponyaji na Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu ukubwa.
Mlango wa; kufanya sababu ni katika kadari
Na tunaamini kwamba kufanya sababu hakupingani na kuamini kadari, bali kuzifanya sababu ni katika kuamini kadari kikamilifu. Na Mola wetu Mlezi aliamrisha kuomba riziki, na alitueleza kuwa tayari alikwishatuandikia riziki, amesema Mola wa haki: "Yeye ndiye aliye idhalilisha ardhi kwa faida yenu, basi tembeeni katika pande zake, na kuleni katika riziki zake. Na kwake Yeye ndio kufufuliwa." [Al-Mulk: 15].
Na amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Na itakapo kwisha Swala, tawanyikeni katika nchi (Ardhi) mtafute katika fadhila za Mwenyezi Mungu, na mtajeni Mwenyezi Mungu kwa wingi ili mpate kufaulu." [Al-Jumu'a: 10].
Na amesema Mwenyezi Mungu akieleza kuhusu Yakub kwamba aliwaambia wanawe: "Msiingilie mlango mmoja, bali ingieni kwa milango mbali mbali. Wala mimi siwafai kitu mbele ya Mwenyezi Mungu. Hukumu haiko ila kwa Mwenyezi Mungu tu. Juu yake Yeye mimi nimetegemea, na juu yake Yeye na wategemee wanaotegemea." [Yusuf: 67]. Na imesimuliwa kutoka kwa As-Saib bin Yazid: "Hakika Mtume rehema na amani ziwe juu yake alichukua ngao mbili siku ya vita vya Uhudi, kana kwamba alizivaa kwa kuziunganisha." (Imepokelewa na Ibn Maja 2806, Said bin Mansur 2858, Ahmad 15722, na An-Nasai katika Al-Kubra 8529). Na Mwenyezi Mungu alimwamuru Nuhu, amani iwe juu yake, kutengeneza safina, na pia alimwamuru Musa, amani iwe juu yake, kuipiga bahari kwa fimbo, na akamwamuru Mariamu, amani iwe juu yake, atikise shina la mtende ili umuangushie tende mbivu, na mengineyo ambayo Mwenyezi Mungu aliwaamuru waja wake kufanya sababu za jambo fulani.
Na miongoni mwa sababu kubwa zaidi ni dua. Imesimuliwa kutoka kwa Nu'man bin Bashir, kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuhusiana na kauli yake Mtukufu: "Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni, nitawaitikia." Akasema: "Dua ndiyo ibada" Na akasoma: "Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni, nitawaitikia." [Ghafir: 60] hadi kauli yake: "wadhalilike." (Imepokelewa na Abuu Daud 1479, Tirmidhi 2969, na Ibn Majah 3828).
Na miongoni mwa sababu ni dawa na kufanya Ruqya Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Khizama, kutoka kwa baba yake Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Nilimuuliza Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nikasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, unaonaje Ruqya tunazofanya, na madawa tunayotumia, na kinga tunazojikinga kwazo. Je, hayo yanazuia chochote katika kadari ya Mwenyezi Mungu? Akasema: "Hayo ni katika kadari ya Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Tirmidhi 2065, Ibn Majah 3437, Ibn Wahab katika Al-Jaamii cha Hadithi 699, Ahmad 15472 na Ibn Abi Asim katika Al-Aahaad Wal-Mathani 2610).
Mlango wa kwamba kadari haipingani na uadilifu
Tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu anaamuru uadilifu, na anahukumu kwao kisheria, kikadari, na kimalipo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha kufanya uadilifu na hisani." [An-Nahl: 90] Na amesema Mola Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu anapiga mfano wa watu wawili. Mmoja wao ni bubu, hawezi chochote, naye ni mzigo kwa bwana wake. Popote anapo muelekeza haleti kheri. Je, huyo anaweza kuwa sawa na yule anayeamrisha uadilifu, naye yuko juu ya Njia iliyoyooka?" [An-Nahl: 76] Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Dharri, Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, katika yale aliyoyasimulia kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwingi wa baraka, kwamba alisema: “Enyi waja wangu, hakika Mimi nimejiharamishia dhuluma na nikaiharamisha baina yenu, kwa hivyo msidhulumiane.” (Imepokelewa na Muslim 2577, na Tirmidhi 2495).
Na aliikanusha dhuluma kwake, akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Anaye tenda mema basi anajitendea mwenyewe nafsi yake, na mwenye kutenda uovu basi ni juu ya nafsi yake vile vile; wala Mola wako Mlezi si mwenye kuwadhulumu waja." [Fusswilat: 46] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hadhulumu hata uzito wa chembe moja. Na ikiwa ni jambo jema basi Yeye hulizidisha." [An-Nisaa: 40] Na amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Na anaye fanya mema, akiwa mwanamume au mwanamke, naye ni Muumini - basi hao wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa hata kadiri ya tundu ya kokwa ya tende." [An-Nisaa: 124] Na amesema Mola Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hawadhulumu watu kitu chochote; lakini watu wenyewe wanajidhulumu nafsi zao." [Yunus: 44] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Afanyae wema atalipwa mfano wake mara kumi. na afanyae ubaya hatalipwa ila sawa nao tu. Na wao hawatadhulumiwa." [Al-An'am: 160]. Na aya nyinginezo zinazoonyesha ukamilifu wa uadilifu wake, na kujikanushia udhalimu.
Na tunaamini kuwa kadari iliyokwishatangulia haina maana kuwa anawadhulumu waja; kwa sababu Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu, na akatuma Mitume; ili watu wasiwe na hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu baada ya Mitume, amesema Mwenyezi Mungu: "Mitume hao ni wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya kuletewa Mitume. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima." [An-Nisaa: 165].
Na aliifanya kadari kuwa siri, amesema Mwenyezi Mungu: "Yeye ndiye Mwenye kujua ya siri, wala hamdhihirishii yeyote siri yake." [Al-Jinn: 26] Na aliwapa waja wake utashi na hiari, amesema Mola Mtukufu: "Na sema: Hii ni kweli itokayo kwa Mola wako Mlezi. Basi atakaye, aamini. Na atakaye, akufuru." [Al-Kahf: 29] Na amesema Mtukufu: "Hakika Sisi tumembainishia Njia. Ima (awe) ni mwenye kushukuru, au (awe) mwenye kukufuru." [Al-Insaan: 3] Na amesema Mola wa Haki: "Kisha akaifahamisha uovu wake na wema wake." [Ash-Shams: 8].
Mlango wa kutumia kadari kuwa ndiyo hoja
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu alituma Mitume, na akateremsha vitabu; ili watu wasije wakawa na hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mitume hao ni wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya kuletewa Mitume. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima." [An-Nisaa: 165]. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza juu ya washirikina kwamba walitumia kadari kuwa ndiyo hoja yao ya kufanya ushirikina, Mwenyezi Mungu akabainisha uongo wao huo, na akawaonjesha adhabu yake, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Watasema walio shirikisha (kingine pamoja na Mwenyezi Mungu): Lau kama Mwenyezi Mungu angetaka tusingeli shirikisha sisi, wala baba zetu; wala tusingeli haramisha kitu chochote. Vivi hivi walikanusha walio kuwa kabla yao mpaka walipo onja adhabu yetu. Sema: Je, nyinyi mnayo elimu mtutolee? Nyinyi hamfuati ila dhana. Wala hamsemi ila uongo tu." [Al-An'am: 148]. Na lau kama kadari ingelikuwa ni hoja kwao juu ya kufanya ushirikina wao huo, basi Mwenyezi Mungu asingeliwaonjesha adhabu yake.
Na imesimuliwa kutoka kwa Ally Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Tulikuwa tumekaa pamoja na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akiwa na kijiti akikwaruza ardhi kwacho, akasema: "Hakuna yeyote miongoni mwenu isipokuwa ameshaandikiwa mahali pake Motoni au Peponi." Basi, mwanaume mmoja miongoni mwa watu hao akasema: "Je, si tuache tu kufanya matendo na tutegemee kadari iliyoandikwa, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Akasema: "Hapana. Fanyeni matendo. Kwa maana kila mmoja amerahisishiwa." Kisha akasoma: "Ama mwenye kutoa na akamchamungu." [Al-Layl: 5] hadi mwisho wa aya. (Imepokelewa na Bukhari 6605, Muslim 2647, Tirmidhi 2136, na Ibn Majah 78). Kwa hivyo, Mtume rehema na amani ziwe juu yake akawa amewaamrisha watu wafanye matendo, na akakataza kutegemea kadari iliyoandikwa.
Na tunaamini kwamba inaruhusiwa kwa mja kutumia kadari kuwa ndiyo hoja juu ya kufanya kwake dhambi, lakini baada ya kutubu akaiacha. Imesimuliwa kutoka kwa Humaid bin ʻAbdur-Raḥman kuwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amridhie alisema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Adam na Musa walipingana. Musa akamuambia: "Wewe ndiye Adam ambaye dhambi lako lilikutoa katika Bustani ya mbinguni." Adam akamwambia: "Wewe ndiye Musa ambaye Mwenyezi Mungu alikuchagua kwa ajili ya ujumbe wake na akakuongelesha moja kwa moja, kisha unanilaumu kwa kitu ambacho nilikuwa nimeandikiwa kabla sijaumbwa?" Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: “Adam akamshinda Musa kwa hoja." Akalisema hilo mara mbili. (Imepokelewa na Bukhari 6614, Muslim 2652, Abu Daud 4701, Tirmidhi 2134, na Ibn Majah 80).
Na amesema Mutwarrif bin Abdallah bin Ash-Shikhir, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Hatukuachiwa katika Qur'ani kuendeshwa na kadari na tumeambiwa katika Qur'ani kwamba tutaishia huko." (As-Sunnah, cha Abdullah bin Ahmad 2/412). Na amesema Muhammad bin Sirin Mwenyezi Mungu amrehemu: "Ikiwa watu wa kadari si miongoni mwa wale wanaozama katika aya za Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, na Mtukufu, basi sijui ni akina nani." (As-Sunnah, cha Abdullah bin Ahmad 2/432, na Sharhu Usuulu itikadi Ahlus-Sunna Wal-Jama'ah 4/696).
Amesema Ibn Wahab na wengineo: "Maliki aliulizwa kuhusu watu wanaopinga kadari: Je, tuache kuongea nao? Akasema: "Ndiyo, ikiwa anajua anachofanya." Akasema: "Na amuamrishe mema na amkataze maovu, na awaeleze kuhusu kwenda kwao kinyume, wala asiwalainishie kauli, wala asiwaswalie, wala asihudhurie mazishi yao, na sioni kuwa inafaa kuwaozesha." Akaongeza katika riwaya ya wengine: Mwenyezi Mungu amesema: "Na mja mwema muumini ni bora (kumuozesha) kuliko mshirikina." [Al-Baqarah: 221]. Na alisema katika riwaya ya Ash-hab: Na haifai kuswali nyuma yao, wala kuchukua hadithi kutoka kwao, na mkiwakuta katika ngome basi watoeni." (Tartibul-Madarik wa Taqribul-Masalik 1/91).
Na tunaamini kuwa mja anaruhusiwa kutumia kadari kuwa ni hoja juu ya masaibu, imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Muumini mwenye nguvu ni bora na mpendwa zaidi kwa Mwenyezi Mungu kuliko muumini dhaifu, na katika kila heri. Pupia yenye kukunufaisha, na utafute msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu, wala usishindwe. Na kitu kikikusibu, usiseme: Lau ningelifanya hivi, ingelikuwa hivi. Lakini sema: Mwenyezi Mungu alishapitisha kadari yake, naye hufanya alitakalo. Kwa maana, kusema: Lau kunafungua matendo ya shetani." (Imepokelewa na Muslim 2664, na Ibn Majah 79).
Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kauli yake katika tafsiri ya maneno ya Mwenyezi Mungu: "Wale ambao ukiwasibu msiba, husema: Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na hakika kwake Yeye tutarejea." [Al-Baqarah: 156]: Alisema: Mwenyezi Mungu alieleza kuwa Muumini anapomkabidhi Mwenyezi Mungu jambo hilo na akarudi na akajua kwamba atarudi kwa Mwenyezi Mungu, wakati wa msiba, anaandikiwa sifa tatu za heri: Kuswaliwa (kutukuzwa) na Mwenyezi Mungu, kurehemewa, na kufikia njia ya uongofu." Na amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Atakayejua kwamba atarudi kwa Mwenyezi Mungu wakati anapopatwa na msiba, basi Mwenyezi Mungu atamlipa kwa msiba wake huo, na atamfanyia mwisho mzuri, na atampa njia mbadala nzuri ambayo atairidhia." (Imepokelewa na Twabari katika Tafsir 2/707, 3/223, Ibn Abi Hatim katika Tafsir 1421, Twabarani katika Al-Kabir 13027, na Al-Baihaqi katika Ash-Shu'ab 9240).
Mlango wa Ibada
Muhtasari wa Mlango
Tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliumba viumbe ili wamuabudu, na ibada ambayo Mwenyezi Mungu aliamuru ni ile ya uongofu, nayo ni mila ya Ibrahim, amani iwe juu yake, na ni ile ile ambayo Mwenyezi Mungu aliamuru vizito viwili (watu na majini). Na ibada ina aina nyingi, wala hairuhusiwi kumfanyia yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu chochote katika ibada hizo. Na miongoni mwa aina zake ni dua, kumtegemea Mwenyezi Mungu, kunyenyekea, kuhofu, kutumaini, kujilinda kwa Mwenyezi Mungu, kuchinja, kutafuta msaada, na kutafuta kuokolewa.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliumba viumbe ili wamuabudu, na tunajua kuwa amri ya kwanza iliyotajwa katika Qur'ani ni amri ya kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na si kitu kingine chochote. Na kila Nabii aliwaambia watu wake: "Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu yeyote isipokuwa Yeye." [Al-A'araf: 65].
Na tunajua kuwa ibada haikubaliki mpaka iwe imekusudiwa Mwenyezi Mungu tu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, kwa mujibu wa muongozo wa bwana wa Mitume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Na ni lazima awe yule anayekusudiwa kwa ibada ni Mwenyezi Mungu peke yake, ambaye hana mshirika yeyote, naye aliyetakasika na kutukuka alionya dhidi ya ushirikina wote, mkubwa wake na mdogo wake. kwa hivyo, mwenye kutenda matendo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, lakini yakawa hayakubaliani na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, basi atarudishiwa matendo yake hayo. Na mwenye kufanya matendo yanayokubaliana na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, lakini yakawa si kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake, basi hayo pia yatarudishwa kwake.
Na tunajua kuwa misingi ya ibada ni mitatu: Upendo kamili, matumaini kamili, na hofu kamili, na kuwa Manabii na Mitume walifaulu katika hayo kwa fungu kubwa mno.
Na tumaini kubwa zaidi la Waumini ni kuuona uso wa Mwenyezi Mungu wenye utukufu, ambayo ndiyo neema kubwa zaidi ya wakazi wa Peponi. Bali hilo ni nyongeza ya neema juu ya neema. Na wakazi wa Peponi watakapoingia humo, Mwenyezi Mungu atawaongezea waumini juu yao utukufu na ukarimu juu ya ukarimu wake kutoka na fadhila zake na ukarimu atakapowapa idhini ya kumtazama. Na kitu kikubwa zaidi wanachokihofu watu wenye Imani ni kunyimwa neema hii ambayo atawapa vipenzi wake tu waliomuamini, na atawanyima maadui zake, na atawazuia maadui wake wote wasimtazame kama vile washirikina, Mayahudi, Wakristo, Majusi (watu wanaoabudu moto) na wanafiki.
Na njia ni kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kufanya kila yanayompendeza, ya wajibu au yale yasiyo ya wajibu. (Na neno 'Al-Wasila' linaweza kuwa na maana nyingine - pia - ambayo imetajwa katika maneno yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake, "Niombeeni kwa Mwenyezi Mungu Al-wasila (daraja la juu)."
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaamuru waja wake kuomba dua, na akawaahidi kuwaitikia, na tunajua kuwa njia sahihi ya kumfikia Mwenyezi Mungu ni kupitia majina yake mazuri zaidi na sifa zake za juu, na ndiyo sababu dua nyingi za Manabii na Mitume zilikuwa kwa kutumia majina mazuri zaidi ya Mwenyezi Mungu. Na miongoni mwa maeneo ya kuomba dua ni mwisho wa swala, na katika theluthi ya mwisho ya usiku, na wakati wa kufungua saumu, na katika Tawaf, na juu ya Safa na Marwa, na huko 'Arafah na Muzdalifa, na baada ya kutupa vijiwe huko Mina.
Kama vile kumfikia Mwenyezi Mungu kunakuwa kwa kumuamini, pia kunakuwa kwa kutenda matendo mema ya kila aina ya ibada. Na kumfikia Mwenyezi Mungu pia kunakuwa kwa kutaja hali, na kuonyesha uhitaji juu ya Mwenyezi Mungu, na kuwa mja anahitaji msaada na rehema ya Mwenyezi Mungu, na kumfikia Mwenyezi Mungu pia kunakuwa wakati Muislamu anamuomba mtu mwema aliye hai, aliye pamoja naye kuwa amuombee, kama vile ndugu zake Yusuf walivyomuomba baba yao awaombee msamaha, na maswahaba wa Mtume, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, waliacha kumuomba Mwenyezi Mungu kuteremsha mvua kupitia kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, baada ya kifo chake na wakawa wanamfikia Mwenyezi Mungu kupitia Al-'Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye; kwa sababu walijua kuwa hili ni katika kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia njia zinazoruhusiwa.
Hairuhusiwi kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia njia ambazo haziko katika sheria, kwani watu zama za ujinga walikuwa wakijiweka karibu na Mwenyezi Mungu kwa kupitia masanamu yao na miungu yao.
Mlango wa: Maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Nami sikuwaumba majini na watu isipokuwa waniabudu Mimi.”
Tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliumba vizito viwili (watu na majini) ili wamuabudu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Nami sikuwaumba majini na watu isipokuwa waniabudu Mimi." [Dhariyat: 56]. Yaani: Hawakuamrishwa isipokuwa wamuabudu Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote. Na ibada aliyoiamrisha Mwenyezi Mungu ni ile ya uongofu, ambayo ni mila ya Ibrahim, amani imshukie, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Kwa hakika mimi Mola wangu Mlezi ameniongoa kwenye Njia iliyonyooka, Dini iliyo sawa kabisa, ambayo ndiyo mila ya Ibrahim aliyekuwa muongofu, wala hakuwa miongoni mwa washirikina." [Al-An'am: 161].
Na ibada aliyoiamrisha Mwenyezi Mungu ina aina nyingi, wala hairuhusiwi kumfanya yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu chochote katika hizo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu, basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu." [Al-Jinn: 18].
Na miongoni mwa aina zake ni dua, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na anayemuomba - pamoja na Mwenyezi Mungu - mungu mwinginewe, hana ushahidi wowote wa hili; basi bila ya shaka hesabu yake iko kwa Mola wake Mlezi. Kwa hakika makafiri hawafanikiwi." [Al-Mu'minun: 117] Na amesema Mtukufu: "Na Mola wenu Mlezi alisema: Niombeni, nitawaitikia. Kwa hakika, wale wanaojivuna wasiniabudu Mimi, wataingia Jahannamu wadhalilike." [Ghafir: 60].
Na miongoni mwake ni kumtegemea Mwenyezi Mungu, amesema Mtukufu: "Na mtegemeeni Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni Waumini." [Al-Ma'ida: 23] Na amesema Mtukufu: "Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu, basi Yeye humtosha." [At-Talaq: 3].
Na miongoni mwake ni kuogopa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi msiwaogope wao, lakini niogopeni Mimi" [Al-Baqara: 150].
Na miongoni mwake ni hofu, amesema Mola wa haki Mtukufu: "Basi msiwahofu, bali nihofuni Mimi ikiwa nyinyi ni Waumini." [Al-Imran: 175].
Na miongoni mwake ni kutarajia, amesema Mola wa Haki, Mwenye sifa nyingi: "Hao wanaowaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kwendea kwa Mola wao Mlezi - hata miongoni mwao walio karibu mno - nao wanataraji rehema zake na wanaihofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi yafaa kutahadhariwa." [Al-Israa: 57] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Sema: Hakika mimi ni mwanadamu tu kama nyinyi. Ninaletewa Wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja. Kwa hivyo, mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi, basi na atende matendo mema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi." [Al-Kahf: 110].
Na miongoni mwake ni kujilinda na Mwenyezi Mungu, amesema Mola wa haki Mwenye sifa nyingi: "Sema: Ninajikinga kwa Mola Mlezi wa wanadamu." [An-Nas: 1].
Na miongoni mwake ni kuchinja, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Sema: Hakika Swala yangu, na ibada zangu, na uhai wangu, na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-An'am: 162].
Na miongoni mwake ni kutafuta msaada, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wewe tu tunakuabudu, na Wewe tu tunakuomba msaada." [Al-Fatiha: 5].
Na miongoni mwake ni kuomba kuokolewa, amesema Mola wa Haki Mwenye Utukufu: "Mlipokuwa mkimuomba msaada Mola wenu Mlezi, naye akawaitikia kuwa: Kwa yakini Mimi nitawasaidia kwa Malaika elfu moja wanaofuatana mfululizo." [Al-Anfal: 9].
Na tunajua kuwa amri ya kwanza iliyotajwa katika Qur'an ni amri ya kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake na si kitu kingine chochote, amesema Mwenye sifa nyingi, na majina matakatifu: "Enyi watu! Muabuduni Mola wenu Mlezi aliyewaumba nyinyi na wale wa kabla yenu, ili mpate kuwa wachamungu." [Al-Baqara: 21]. Na kila Nabii alikuwa akiwaambia watu wake: "Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu isipokuwa Yeye." Kama alivyosema Mwenyezi Mungu kuhusiana na Mitume wa kwanza, amani iwe juu yao: "Hakika, tulimtuma Nuhu kwa kaumu yake, naye akasema: Enyi kaumu yangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu yeyote isipokuwa Yeye. Hakika mimi ninawahofia adhabu ya Siku iliyo kuu." [Al-A'raf: 59] Na Mwenyezi Mungu alisema akieleza kuhusu wa mwisho wao, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba aliwaambia watu wake: "Na muabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na chochote." [An-Nisaa: 36] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Taghut (Shetani, na vyote vinavyoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu).” [An-Nahl: 36].
Na tunajua kwamba ibada haikubaliki mpaka iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu tu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, kwa mujibu wa muongozo wa bwana wa Mitume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema Mtukufu: "Kwa hivyo, mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi, basi naatende matendo mema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi." [Al-Kahf: 110].
Na tunajua kuwa ibada inapasa kukusudiwa Mwenyezi Mungu peke yake asiye na mshirika yeyote, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika matendo yanategemea nia. Na hakika kila mtu atalipwa kulingana na kile alichokusudia. Kwa hivyo, yule ambaye kuhama kwake kulikuwa ni kwenda kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi kuhama kwake huko kweli kulikuwa ni kwenda kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na yule ambaye kuhama kwake kulikuwa ni kuliendea jambo fulani la kidunia alilotaka kulipata au mwanamke fulani aliyetaka kumuoa, basi kuhama kwake huko kulikuwa kwenda kwa alichohama kwa ajili yake." (Imepokelewa na Bukhari 6689, Muslim 1907, Abu Daud 2201, Tirmidhi 1647, An-Nasai 75, na Ibn Majah 4227).
Na Mwenyezi Aliyetakasika na kutukuka alitahadharisha dhidi ya ushirikina wote, mkubwa wake na mdogo wake, akasema Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, na Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hasamehe kushirikishwa, na husamehe dhambi isyokuwa shirki kwa amtakaye. Na anayemshirikisha Mwenyezi Mungu, basi hakika amezua dhambi kubwa." [An-Nisaa: 48]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie amesema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Amesema Mwenyezi Mungu, Mwingi wa baraka, na Mtukufu: Mimi ndiye nisiyehitaji zaidi mshirika kati ya washirika wote. Kwa hivyo, yeyote anayefanya tendo lolote na akanishirikisha ndani yake na mwingine, nitamuacha na mshirika wake huyo." (Imepokelewa na Muslim 2985).
Kwa hivyo, mwenye kufanya jambo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, lakini likawa halikubaliani na muongozo wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake basi atarudishiwa jambo lake hilo, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika nyinyi mna kiigizo chema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa anayemtaraji Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, na akamkumbuka Mwenyezi Mungu sana." [Al-Ahzab: 21]. Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Yeyote atakayefanya jambo ambalo hatukuliamrisha, hilo atarudishiwa." (Imepokelewa na Muslim 1718). Na amesema Mtukufu: "Basi nawatahadhari wale wanaohalifu amri yake, usije ukawapata msiba au ikawapata adhabu chungu." [An-Nur: 63] Na amesema Mtukufu: "Sema: Ikiwa nyinyi mnampenda Mwenyezi Mungu, basi nifuateni mimi, Mwenyezi Mungu atawapenda na atawafutia madhambi yenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta madhambi na Mwenye kurehemu." [Al-Imran: 31].
Na tunajua kuwa misingi ya ibada ni mitatu: Mapenzi kamili, matumaini kamili, na hofu kamili. Na Manabii na Mitume walifaulu katika hayo kwa fungu na kiwango kikubwa mno, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza juu ya hali yao: "Hakika wao walikuwa wepesi wa kutenda mema, na wakituomba kwa shauku na hofu. Nao walikuwa wakitunyenyekea." [Al-Anbiya: 90] Na amesema Mtukufu: "Na wale ambao wanatoa Zaka na Sadaka waliyopewa na hali nyoyo zao zinaogopa kwa kuwa watarejea kwa Mola wao Mlezi * Basi wote hao ndio wanaokimbilia katika mambo ya heri, na ndio watakaotangulia kuyafikia." [Al-Mu'minun: 60, 61] Na akasema Aliyetakasika na kutukuka: "Mbavu zao zinaachana na malazi kwa kumuomba Mola wao Mlezi kwa hofu na kutumaini, na hutoa kutokana na vile tulivyowaruzuku." [As-Sajda: 16] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Je, afanyae ibada nyakati za usiku kwa kusujudu na kusimama akitahadhari na Akhera, na akitaraji rehema za Mola wake Mlezi." [Az-Zumar: 9].
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie amesema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenyezi Mungu anasema: "Mimi niko pamoja na dhana ya mja wangu kwangu. Na mimi nipo naye anaponitaja. Atakaponitaja kwenye nafsi yake, nitamtaja kwenye nafsi yangu. Na atakaponitaja kwenye mkusanyiko, nitamtaja kwenye mkusanyiko bora kuliko wao. Na akijiweka karibu yangu kwa kiasi cha shibri moja (sent 8), nitakuwa karibu yake kwa kiasi cha dhiraa moja (sent 18). Na akijiweka karibu yangu kwa kiasi cha dhiraa moja, nitakuwa karibu yake kiasi cha baa moja (mita 2). Na akinijia kwa kutembea, nitamuendea kwa kukimbia". (Imepokelewa na Bukhari 7405), Muslim 2675, Tirmidhi 3603, na Ibn Majah 3822).
Na amesema Mola wa Haki, Mtukufu: "Na katika watu wapo wanaofanya waungu wasiokuwa Mwenyezi Mungu. Wanawapenda kama kumpenda Mwenyezi Mungu. Lakini wale walioamini wanampenda Mwenyezi Mungu zaidi sana." [Al-Baqara: 165] Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Mambo matatu yatakapokuwa kwa mtu, basi atapata kwa mambo hayo utamu wa imani: Kwamba awe Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio vipenzi zaidi kwake kuliko yeyote asiyekuwa wao, na ampende mtu si kumpenda kwa lolote isipokuwa ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na achukie kurudi katika ukafiri kama anavyochukia kutupwa motoni." (Imepokelewa na Bukhari 16, Muslim 43, Tirmidhi 2624, An-Nasai 4987, na Ibn Majah 4033).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie amesema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko mkononi mwake, hataamini mmoja wenu mpaka niwe mpendwa zaidi kwake kuliko baba yake na mwanawe." (Imepokelewa na Bukhari 14, na An-Nasai 5015). Na mja hawezi kupata upendo wa Mwenyezi Mungu mpaka amfuate Mtume rehema na amani ziwe juu yake, amesema Mola wa Haki, Mtukufu: "Sema: Ikiwa nyinyi mnampenda Mwenyezi Mungu, basi nifuateni mimi, Mwenyezi Mungu atawapenda na atawafutia madhambi yenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kufuta madhambi na Mwenye kurehemu." [Al-Imran: 31].
Na tumaini kubwa zaidi la Waumini ni kuuona uso wa Mwenyezi Mungu wenye utukufu, amesema Mtukufu: "Zipo nyuso siku hiyo zitakazong'ara * Zinamwangalia Mola wao Mlezi" [Al-Qiyama: 22, 23].
Na kumuona Mwenyezi Mungu ndiyo neema kubwa zaidi kwa wakazi wa Peponi, bali ni kuongezewa neema juu ya neema zao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa wale wafanyao wema ni wema na zaidi. Wala vumbi halitawafunika nyuso zao, wala madhila. Hao ndio watu wa Bustani ya mbinguni. Humo watadumu." [Yunus: 26].
Na imesimuliwa kutoka kwa Suhaib Mwenyezi Mungu amridhie, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Watakapoingia watu wa peponi, peponi atasema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka: "Je, kuna kitu mnataka niwaongezee?" Watasema: Kwani hukuzing'arisha nyuso zetu? Kwani hukutuingiza peponi na ukatuokoa na Moto?' Akasema: Hapo ataliondoa pazia, basi hakuna kitu walichowahi kupewa wanachokipenda zaidi kuliko kumtazama Mola wao Mlezi, Mtukufu." (Imepokelewa na Muslim 181, Tirmidhi 2552, na Ibn Majah 187).
Mlango wa kutafuta njia ya kumfikia Mwenyezi Mungu
Al-Wasila: Ni kumkaribia Mwenyezi Mungu kwa kila anachokiridhia miongoni mwa mambo ya wajibu au yasiyo ya wajibu.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaamrisha waja wake kuomba dua, na akawaahidi kuwaitikia, amesema Mtukufu: "Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni, nitawaitikia." [Ghafir: 60]. Na amesema Mwenye sifa tukufu kubwa na majina matakatifu: "Na watakapokuuliza waja wangu kuhusu Mimi; basi Mimi nipo karibu. Naitika maombi ya muombaji anaponiomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka." [Al-Baqara: 186].
Na tunajua kuwa kutafuta njia ya kumfikia Mwenyezi Mungu kunakuwa kupitia majina yake mazuri zaidi na sifa zake za juu zaidi kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri kabisa, basi muombeni kwa hayo. Na waacheni wale wanaoharibu utakatifu wa majina yake. Hao watakujalipwa yale waliyokuwa wakiyatenda." [Al-A'raf: 180] Na akasema Mtukufu: "Sema: Muombeni Allah (Mwenyezi Mungu), au muombeni Rahman (Mwingi wa rehema), kwa jina lolote mnalomuita. Kwani Yeye ana majina mazuri mazuri zaidi. Wala usitangaze Swala yako kwa sauti kubwa, wala usiifiche kwa sauti ndogo, bali shika njia ya kati na kati ya hizo." [Al-Israa: 110].
Na ndiyo sababu dua nyingi za Manabii na Mitume zilikuwa kwa kutumia majina mazuri zaidi ya Mwenyezi Mungu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu Adam na mkewe kwamba walisema: "Wakasema: Mola wetu Mlezi! Tumejidhulumu nafsi zetu, na kama hutusamehi na kuturehemu, hakika tutakuwa katika wenye kuhasirika." [Al-A'raf: 23] Na amesema Khalil (Ibrahim), amani iwe juu yake: "Mola wangu Mlezi! Nijaalie niwe mwenye kushika Swala, na katika dhuria (kizazi) changu pia. Ewe Mola wetu Mlezi, na ikubali dua yangu." [Ibrahim: 40] Na alisema Musa, amani iwe juu yake: "(Musa) akasema: Mola Mlezi wangu! Nisamehe mimi na ndugu yangu, na ututie katika rehema yako. Nawe ni Mwenye kurehemu kushinda wote wenye kurehemu." [Al-A'raf: 151].
Na kumfikia Mwenyezi Mungu pia kunakuwa kwa kumuamini Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mola wetu Mlezi! Tumeyaamini uliyoyateremsha, na tumemfuata huyu Mtume, basi tuandike pamoja na wanaoshuhudia." [Al-Imran: 53].
Na kumfikia Mwenyezi Mungu pia kunakuwa kwa matendo mema, kama ilivyo katika kisa cha wale watu watatu ambao walifungiwa ndani ya pango, Imesimuliwa na Abdallah bin Omar Mwenyezi Mungu awe radhi nao kuwa: Nilimsikia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Watu watatu kati ya wale waliokuwa kabla yenu, walitoka pamoja mpaka walipolifikia pango fulani usiku na wakaingia ndani yake. Jiwe kubwa liliporomoka kutoka kwenye mlima huo na likaufunga mlango wa pango hilo. Wakasema: 'Hakika hakuna kitu kinachoweza kuwaokoa kutokana na jiwe hili isipokuwa kumuomba Mwenyezi Mungu kwa matendo yenu yaliyo bora zaidi.' Kwa hivyo, mmoja wao akasema: "Ewe Mwenyezi Mungu! Nilikuwa na wazazi wangu wawili wazee, na sikuwahi kuinywesha familia yangu (mke, watoto, watumwa) wala mali yangu maziwa kabla yao. Siku moja, nilikwenda kutafuta kitu na nikachelewa kwa hivyo nikarudi (usiku) hali ya kuwa wameshalala. Niliwakamia (kondoo) maziwa yao lakini nilipowajia, niliwakuta wameshalala, na nikachukia kuinywesha familia yangu au mali yangu maziwa kabla yao. Kwa hivyo, nilisubiri huku bakuli hilo la maziwa liko mkononi mwangu nikiwangoja waamke. Niliendelea kuwangoja mpaka walipoamka asubuhi na wakanywa maziwa hayo. Ewe Mwenyezi Mungu! Ikiwa nilifanya hivyo kwa kutafuta radhi zako tu, basi tufariji kutokana na hali yetu hii iliyosababishwa na jiwe hili. Kwa hivyo, jiwe likasogea kidogo kiasi wasichoweza kutoka nje." Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Wa pili wao akasema: 'Ewe Mwenyezi Mungu! Nilikuwa na binti ya ami yangu ambaye alikuwa mpendwa zaidi kwangu kuliko watu wote, na nilitaka kujamiiana naye pasina yeye kutaka, lakini akakataa. Baadaye, alipatwa na ugumu wa maisha katika moja ya miaka ya njaa. Hivyo basi, alinijia na nikampa dinari mia moja na ishirini kwa sharti kwamba anikubalie kujamiiana naye, na akakubali. Nilipokuwa nimeshamkamata sawasawa, akasema: "Si halali kwako kuuvunja ubikira wangu isipokuwa kwa haki yake (ya kufunga ndoa ya halali). Kwa hivyo, niliona kwamba ni dhambi kuingiliana naye, na nikamuacha ingawa alikuwa mpendwa zaidi kwangu kuliko watu wote, na pia nilimuachia dhahabu ile ambayo nilikuwa nimempa. Ewe Mwenyezi Mungu! Ikiwa nilifanya hivyo kwa kutaka radhi zako tu, basi tufariji kutokana na hali yetu hii. Kwa hivyo, jiwe hilo likasogea kidogo kiasi kwamba hawakuweza kutoka hapo." Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Kisha wa tatu wao akasema: Ewe Mwenyezi Mungu! Hakika mimi, niliwaajiri wafanyakazi na nikawalipa mishahara yao isipokuwa mwanaume mmoja ambaye aliuacha mshahara wake na akaondoka nami nikaikuza mali yake hiyo hadi ikawa nyingi. Baadaye alinijia na akaniambia: Ewe mja wa Mwenyezi Mungu! Nilipe mshahara wangu.' Nikamwambia: Ngamia wote hawa unaowaona, na ng'ombe, na kondoo na watumwa ni katika ule ujira wako. Akasema: Ewe mja wa Mwenyezi Mungu! Usinifanyie masihara. Nikasema: Hakika mimi sikufanyii masihara. Kwa hivyo, akawachukua wote na akaenda nao, na hakuacha chochote katika mali hiyo. Ewe Mwenyezi Mungu! Ikiwa nilifanya hivyo kwa kutaka uso wako tu, basi tufariji kutokana na hali yetu hii. Basi, jiwe hilo likafunguka kabisa, na wakatoka nje wakitembea." (Imepokelewa na Bukhari 2272, na Muslim 2743).
Na kumfikia Mwenyezi Mungu kunakuwa kwa kila aina ya ibada, ambayo ibada muhimu zaidi ni dua, kama alivyosema Mwenye sifa nyingi kuhusiana na Manabii wake: "Hakika wao walikuwa wepesi wa kutenda mema, na wakituomba kwa shauku na hofu. Nao walikuwa wakitunyenyekea." [Al-Anbiya: 90] Na miongoni mwa maeneo ya kuomba dua ni mwisho wa swala, na katika theluthi ya mwisho ya usiku, na wakati wa kufungua saumu, na katika Tawaf, na juu ya Swafa na Marwa, na huko 'Arafa na Muzdalifa, na baada ya kutupa vijiwe huko Mina.
Na kunakuwa kumfikia Mwenyezi Mungu kwa kuitaja hali, na kuonyesha uhitaji kwa Mwenyezi Mungu, na kwamba mja anahitaji msaada na rehema ya Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu Musa, amani imshukie, kwamba alisema: "Mola wangu Mlezi! Hakika mimi ni mhitaji wa heri utakayoniteremshia." [Al-Qasas: 24] Na amesema Mwenye sifa nyingi kuhusiana na Nabii wa Mwenyezi Mungu, Ayub, amani iwe juu yake, kwamba aliomba akisema: "Na Ayub, alipomuita Mola wake Mlezi, akasema: Hakika mimi yamenipata madhara. Na Wewe ndiye unayerehemu kuliko wote wanaorehemu." [Al-Anbiya: 83].
Na kumfikia Mwenyezi Mungu pia kunakuwa wakati Muislamu anamuomba mtu mwema, aliye hai, aliyepo kwamba amuombee, kama vile ndugu zake Yusuf walivyomuomba baba yao, amani iwe juu yao, kwamba awaombee msamaha. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza kuhusu hilo: "Wakasema: Ewe baba yetu! Tuombee msamaha kwa dhambi zetu. Hapana shaka sisi tulikuwa na makosa." [Yusuf: 97] Na akasema Mtukufu: "Na lau pale walipojidhulumu nafsi zao wangelikujia, wakamuomba Mwenyezi Mungu msamaha, na Mtume akawaombea msamaha, hapana shaka wangelimkuta Mwenyezi Mungu ni Mwenye kupokea toba mno, Mwenye kurehemu zaidi." [An-Nisaa: 64]. Imesimuliwa na Anas bin Malik kutoka kwa Ummu Haraam bint Milhan alisema: "Siku moja, Mtume rehema na amani zimshukie, alilala karibu na mimi ndani ya nyumba yangu, kisha akaamka hali ya kuwa anatabasamu. Nikasema: "Ni nini kinachokufanya kutabasamu?" Akasema: "Watu fulani katika umma wangu nimeonyeshwa (katika ndoto) hali ya kuwa wanasafiri katika bahari hii ya kijani kibichi kama wafalme juu ya viti vya enzi." Akasema: "Niombee Mwenyezi Mungu anifanye kuwa miongoni mwao." Basi Mtume rehema na amani zimshukie, akamuombea na akarudi kulala mara ya pili, kisha akafanya kama alivyofanya mara ya kwanza, na Ummu Haram akarudia maneno yake yale, naye akamjibu na jibu lile lile. (Ummu Haram) Akasema: "Niombee Mwenyezi Mungu anifanye miongoni mwao." Akasema: "Wewe ni katika wa kwanza wao." (Imepokelewa na Bukhari 2799, Muslim 1912, Abuu Daud 2490, An-Nasai 3172, na Ibn Majah 2776).
Na alipofasiri Mtume rehema na amani ziwe juu yake sifa za wale watu elfu sabini ambao wataingia Peponi bila ya hesabu, Ukasha Mwenyezi Mungu awe radhi naye alinyanyuka na akasema: "Muombe Mwenyezi Mungu anifanye kuwa miongoni mwao." (Imepokelewa na Muslim 218).
Na imesimuliwa kutoka kwa Anas Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwamba Omari bin Khattab, Mwenyezi Mungu awe radhi naye alikuwa wanapopatwa na ukame, anaomba mvua kutoka kwa Mwenyezi Mungu kupitia kwa Al-Abbas bin Abdil-Muttwalib, na anasema: "Ewe Mwenyezi Mungu, hakika sisi tulikuwa tukitafuta njia ya kukufikia kupitia kwa Nabii wetu, na sasa kwa hakika tunatafuta njia ya kukufikia kupitia ami (baba mdogo) wa Nabii wetu, basi tuteremshie mvua." Basi wananyeshelezewa. (Imepokelewa na Bukhari 1010). Basi Maswahaba, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, wakaacha kuomba kunyeshelezewa mvua na kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, - kwa sababu alikufa - na wakaanza kumfikia Mwenyezi Mungu kwa dua ya Al-Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye; kwa sababu walijua kuwa huku ni kumfikia Mwenyezi Mungu kunakoruhusiwa. Basi Omari Mwenyezi Mungu awe radhi naye, alikusudia kumfikia Mwenyezi Mungu kwa dua ya Al-Abbas, na sio kwa Al-Abbas mwenyewe; kwa sababu kama angekusudia kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia Al-Abbas mwenyewe, basi Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, angekuwa ndiye anayefaa zaidi kwa hilo.
Na hairuhusiwi kumfikia Mwenyezi Mungu kupitia mambo ambayo hayako katika sheria yake, kwani watu wa zama za ujinga walikuwa wakijiweka karibu na Mwenyezi Mungu kupitia masanamu yao na miungu yao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza juu ya ubaya mkubwa wa kitendo chao hicho: "Na wale wanaowafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: Sisi hatuwaabudu isipokuwa ili wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu." [Az-Zumar: 3].
Kitabu cha: Yenye kupingana na imani ya msingi, au yanayopingana na ukamilifu wake
Muhtasari wa Kitabu
Na tunajua kwamba miongoni mwa yale yanayopingana na kumuamini Mwenyezi Mungu ni kumkufuru Mwenyezi Mungu.
Na kukufuru kunaweza kuwa kukubwa na kudogo, kukufuru kukubwa kunamtoa mtu katika Dini, na wala Mwenyezi Mungu hakubali kutoka kwake amali njema wala fidia (ya kujikomboa na adhabu). Na kufuru hii inaharibu matendo yote, na kafiri atadumu milele katika Moto. Ama kufuru ndogo, hiyo inapingana tu na ukamilifu wa imani.
Na tunajua kuwa kufuru kubwa ina aina mbalimbali, ambazo Mwenyezi Mungu alizieleza katika kitabu chake, na akaeleza kuwa kukufuru kwa makafiri kunakuwa kwa kukanusha, na wakati mwingine kunakuwa kwa kukataa na kuifanyia kiburi haki, na wakati mwingine kunakuwa kwa kukadhibisha. Na hakuna tofauti kati ya kukadhibisha kwa ulimi na kukadhibisha kwa moyo. Na wakati mwingine kunakuwa kwa kuwa na shaka na kusitasita, mtu akawa anasitasita katika jambo la haki na akatia shaka suala la kufufuliwa na kukutana na Mwenyezi Mungu. Na wakati mwingine kunakuwa kwa kutukana na kukejeli. Na wakati mwingine kunakuwa kwa kupuuza na kuziba njia ya Mwenyezi Mungu. Na wakati mwingine kunakuwa kwa kuichukia haki.
Na tunajua kuwa kuna kukufuru ambako siyo kukufuru kukubwa, yaani kukufuru kudogo, ambako hakupingani na imani ya msingi, lakini kunapingana tu na ukamilifu wake, huko hakumfanyi mfanyaji wake kudumu milele Motoni, wala hakuharibu matendo yote, na kufuru hii ina aina nyingi:
Na miongoni mwake ni kupigana na Muislamu, kwani huku ni kukufuru ambako hakumtoi mtu katika dini, wala mfanyaji hatobakia milele Motoni, kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwaita Waumini wanaopigana kuwa ni ndugu, na akawaita kuwa ni Waumini ilhali wanapigana.
Na tunajua kuwa miongoni mwa mambo yanayopingana na kumuamini Mwenyezi Mungu ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu - na hiyo ndiyo dhuluma kubwa mno. Na shirki inabatilisha matendo yote, na wala Mwenyezi Mungu haisamehi ikiwa mfanyaji wake atakufa bila ya kutubu. Na mshirikina akifa ilhali hakutubu, basi ni haramu kwake kuingia Peponi, na makazi yake ni Jahannamu, humo atadumu milele.
Mwenyezi Mungu ameifutilia mbali shirki, na akawashutumu washirikina kwa ushirikina wao, na akaeleza uharibifu wao wa kumfanyia wenza, na kwamba hao hawanufaishi, wala hawadhuru. Wakati mwingine anabainisha kuwa washirika hao hawasikii, na hata wangesikia wasingewaitikia wale waliowaomba. Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kwamba washirika hao hawafaidishi wala hawadhuru, na hawamiliki kifo wala uhai. Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kwamba hao wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu ni wapungufu zaidi hata kuliko wale wanaowaabudu. Kwani hawatembei, wala hawakamati kitu, wala hawasikii, wala hawaoni. Na wakati mwingine Mola Mtukufu anaeleza kutoweza kwa waabudiwa hawa na udhaifu wao. Na wakati mwingine Mola Mtukufu huwahukumu kwa umasikini na uhaba wa walivyo navyo, na kwamba hawamiliki uzito wa chembe mbinguni wala ardhini umiliki kamili, na wala hawamiliki kwa njia ya ushirikiano chochote katika hivyo, na wala hakuna yeyote miongoni mwao anayemsaidia Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, wala muombezi kwake. Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kwamba haiwezekani kuwepo miungu wengine pamoja na Mwenyezi Mungu kiulimwengu, na ni batili kisheria.
Na tunajua kuwa shirki kubwa ina aina nyingi:
Miongoni mwake ni kumfanyia Mwenyezi Mungu mshirika katika ubwana wake, uumbaji wake, umiliki wake, kuruzuku kwake, kuendesha kwake mambo. Na Mola wa Haki alibainisha kuwa Yeye Aliyetakasika ndiye wa Pekee katika uumbaji na amri.
Na miongoni mwake ni mja kumfanyia Mwenyezi Mungu mwana - Mwenyezi Mungu ametukuka sana juu ya hilo.
Na miongoni mwake ni kuamini sayari na kuziabudu, na pia kutafuta kunyeshewa mvua kupitia nyota, na kuitakidi kwamba zinaleta riziki.
Na miongoni mwake ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu katika majina yake na sifa zake, ametakasika na kutukuka, kama anayedai kuwa kuna mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayejua ghaibu (mambo yaliyofichikana). Na ahadi ya adhabu kali imekuja kwa wale wanaojiita wenyewe, au kuwaita wengine kwa moja wapo ya majina ya Mwenyezi Mungu ambayo hayamstahiki yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee, kama vile neno la ukuu “Allah,” au “Mwingi wa rehema.”
Na miongoni mwake ni kuitakidi kuwa yeyote katika viumbe ana sifa ya ukamilifu wa kimungu, au kuwa ana uwezo juu ya vitu vyote?! Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka amebainisha kutoweza kabisa kwa wale wanaoabudu na wale wanaoabudiwa badala yake.
Na miongoni mwake ni Mwenyezi Mungu kufanyiwa miungu mingine pamoja naye.
Na miongoni mwake ni kumfanyia ibada au baadhi ya ibada asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
Na miongoni mwake ni kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kama njia ya kujiweka karibu, kama vile anayechinja kwa ajili ya masanamu au wafu ili kujiweka karibu nao.
Na miongoni mwake ni kuweka nadhiri kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kwani kuweka nadhiri ni kumuabudu Mwenyezi Mungu na haifai kumfanyia yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Ndiyo maana Mwenyezi Mungu akawasifu waumini wanaotekeleza nadhiri.
Na miongoni mwake ni kujilinda kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
Na miongoni mwake ni kutafuta kuokolewa na kutaka msaada kutoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu katika yale ambayo Mwenyezi Mungu peke yake ndiye anaweza kuyafanya, au kumuomba dua asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Na miongoni mwake ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu kwa kumtii asiyekuwa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu alieleza kuwa Watu wa Kitabu waliwachukua makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu, wakawa wanawawekea sheria, na kuwaharamishia yale aliyowahalalishia Mwenyezi Mungu.
Na miongoni mwake ni kushirikisha (kitu kingine) wakati wa kuswali, kurukuu, kusujudu, na kutawadha; Haya ni kwa sababu ibada hizi na mifano yake haziruhusiwi kumfanyia yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu alimuamuru rafiki yake mwandani (Ibrahim), amani iwe juu yake, kuitakasa nyumba yake kwa ajili ya wanaoizunguka, na wanaokaa humo kwa ajili ya ibada na wanaorukuu na kusujudu. Na Mwenyezi Mungu alieleza kuwa ni wenye kiburi tu ndio wanaona uvunjifu kumuabudu Mwenyezi Mungu, na akataja kwamba viumbe wote wanamsujudia.
Na miongoni mwake ni kuhukumu kwa yale ambayo hayakuteremshwa na Mwenyezi Mungu, na kutafuta hukumu ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kama vile walivyofanya Watu wa Kitabu na wengineo. Pale ambapo walimfanyia Mwenyezi Mungu washirika wanaowawekea sheria. Na hili linaweza kuwa kufuru, na wakati mwingine linaweza kuwa dhuluma, na linaweza kuwa ni kutoka nje ya mipaka.
Na miongoni mwake ni kufanya shirki katika mapenzi. Na hili ni mtu kumpenda kiumbe upendo unaoambatana na kudhalilika, kutukuza, na kunyenyekea.
Na miongoni mwake ni shirki ya hofu na kunyenyekea. Na hili ni kuhofu au kuogopa kiumbe hofu inayoambatana na kunyenyekea, kudhalilika na kutukuza, kama vile kuogopa kuwa atamfikishia msiba, au kumzuia heri fulani, au kuacha jambo la wajibu kwa ajili yake, au kufanya jambo lililoharamishwa kwa ajili yake kwa njia ya kujikurubisha kwake. Mwenyezi Mungu Mtukufu alibainisha kuwa vipenzi wake hawamuogopi yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka tu.
Na miongoni mwake ni shirki katika matumaini, na hilo ni kama vile mtu kutarajia kutoka kwa kiumbe kilicho hai, kilichopo au kisichokuwepo, kitu ambacho Mwenyezi Mungu pekee ndiye anaweza kukifanya, au kutarajia kutoka kwa wafu ili waondoe dhiki, kutimiza mahitaji, na kufanya uombezi Siku ya Kiyama.
Na miongoni mwake ni uchawi.
Na miongoni mwake ni ukuhani na kupiga ramli (uaguzi); kwa sababu mwenye kudai hayo anadai kuwa anajua elimu ya ghaibu.
Na tunajua kuwa katika shirki ni shirki ndogo ambayo haimtoi mtu katika dini, na wala haipingani na msingi wa imani, lakini inapingana na ukamilifu wake, na hiyo haimfanyi mfanyaji wake kubaki milele Motoni, wala haiharibu matendo yake yote, nayo ina aina nyingi.
Na miongoni mwake ni kuamini mikosi (kuathiriwa na ndege), na uhakika wake - kama ilivyo katika Hadithi - ni kile kinachokufanya kutenda jambo au kukuzuia kulifanya.
Na miongoni mwake ni kufunga au kutundika hirizi.
Na miongoni mwake ni riyaa (kujionyesha) kidogo. Ama ikiwa moyo wake utajaa kujionyesha, na akawa anafanya matendo mema bila ya nia, imani, wala hofu, basi huyo ni mnafiki halisi, na matendo yake ni batili na yakataliwa wala hayatakubaliwa. Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alieleza kuwa ni shirki ya kisiri (haionekani), na akaeleza kuwa kujionyesha ni jambo lililofichika sana, na kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akiuhofia umma wake zaidi hilo kuliko hofu yake kwao juu ya Masihi Dajali.
Na miongoni mwake ni mtu kufanya matendo yake huku akitaka dunia kwayo. Na hili liko kati ya kuwa shirki kubwa na kuwa ndogo kulingana na yaliyomo moyoni mwa mja.
Na miongoni mwake ni unajimu (Utabiri wa Nyota). Nao unaweza kuwa shirki kubwa, au unaweza kuwa shirki ndogo, kulingana na kile kilichomo moyoni.
Na miongoni mwake ni mtu kusema: “Atakavyo Mwenyezi Mungu, na utakavyo,” na mfano wa maneno kama hayo.
Na miongoni mwake ni kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
Na tunajua kuwa katika yale yanayopingana na imani ya Mwenyezi Mungu ni unafiki. Na hilo ni kuudhihirisha Uislamu na kuficha ukafiri. Nao unaweza kuwa unafiki mkubwa na mdogo. Na unafiki ni ukafiri ikiwa atamkufuru Mwenyezi Mungu na kumuabudu mtu mwingine, na akaudhihirisha Uislamu hadharani kama wale wanafiki waliokuwa katika zama za Mtume rehema na amani ziwe juu yake. Na unafiki mkubwa unamtoa mtu katika Uislamu. Na tunashuhudia kwa ushahidi wa Mwenyezi Mungu kwamba wanafiki ni waongo katika madai yao kuwa ni waumini.
Na Mwenyezi Mungu hakubali jambo jema wala fidia kutoka kwa mnafiki, na mwisho wa mnafiki - ikiwa atafia katika unafiki - ni kudumu milele Motoni.
Na tunajua kuwa unafiki mkubwa unakuwa kwa kuichukia haki, na unakuwa kwa kufurahia kushindwa kwa Uislamu na watu wake, na majuto makubwa ikiwa wataona Uislamu umeshinda. Na unakuwa kwa kukufuru baada ya kuamini, na kukataa kukubali kuhukumu kwa mujibu wa Sheria ya Mwenyezi Mungu. Na unakuwa kwa kumdhania mabaya Mwenyezi Mungu kwamba hatamnusuru Mtume wake rehema na amani ziwe juu yake, na dini yake. Na unakuwa kwa kuidhihaki haki na watu wake, na kuwatukana na kuwafanyia kejeli, na pia kuwavunjia heshima Waislamu - na unakuwa kwa kuwahadaa waumini, na kujionyesha kwa matendo.
Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na Waumini wafanye jihadi dhidi ya wanafiki.
Na tunajua kuwa unafiki mdogo haumtoi mtu katika dini, na wala haupingani na msingi wa imani, lakini unapingana na ukamilifu wake, na kwamba unafiki una aina nne, ambazo ikiwa ziko kwa mtu basi atakuwa mnafiki. Na ambaye sifa moja katika hizi itakuwa ndani ya moyo wake, basi atakuwa na sifa ya unafiki mpaka aiache: Anapozungumza husema uongo, na anapoahidi huvunja ahadi, na anapofanya makubaliano hufanya hiana, na anapogombana huvuka mipaka.
*Na uzushi wote ni upotofu.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alitukamilishia Dini na akatukamilishia neema zake juu yetu. Na miongoni mwa mambo yanayopingana na ukamilifu wa imani ni uzushi katika dini. Na tunajua kuwa Mwenyezi Mungu amekataza mifarakano na kutofautiana.
Na tunajua kuwa katika uzushi ni kuyapa taadhima makaburi, na kuyajengea juu yake, na huenda hilo likafikia kumshirikisha Mwenyezi Mungu. Na katika uzushi ni kuwapiga picha watu wema kwa matumaini ya kuwaiga baada ya kufa kwao.
Na tunajua kuwa miongoni mwa mambo ya uzushi ya kupingwa ni sherehe za uzushi, na kushirikiana na makafiri katika sikukuu zao.
Na tunajua kuwa miongoni mwa mambo ya uzushi ya kupingwa ni kutafuta baraka kutoka katika kitu ambacho Mwenyezi Mungu hakukifanya kuwa sababu ya baraka. Na hili linaweza kuwa ni sababu ya kufanya ushirikina.
Mlango wa kumkufuru Mwenyezi Mungu
Tunajua kuwa miongoni mwa mambo yanayopingana na kumuamini Mwenyezi Mungu ni kumkufuru Mwenyezi Mungu. Nalo ni kukufuru kudogo na kukubwa. Na kukufuru kukubwa kunapingana na msingi wa imani, ilhali kukufuru kudogo kunapingana na ukamilifu wake. Kukufuru kukubwa kunamtoa mtu katika dini, na Mwenyezi Mungu hatamkubalia mtu huyo amali nzuri wala fidia, amesema Mtukufu: "Na anayetafuta dini isiyokuwa Uislamu, haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa miongoni mwa wenye kupata hasara." [Al-Imran: 85], Na amesema Mtukufu: "Hakika wale waliokufuru, na wakafa hali ya kuwa ni makafiri, kamwe haitakubaliwa kutoka kwa yeyote miongoni mwao, fidia ya dhahabu ya kujaza dunia nzima lau wangeliitoa. Hao watapata adhabu chungu, wala hawatakuwa na wa kuwanusuru." [Al-Imran: 91], Na amesema Mola wa Haki: "Na iogopeni Siku ambayo mtu hatamfaa mtu kwa lolote, wala hayatakubaliwa kwake maombezi, wala hakitapokelewa kikomboleo kwake; wala hawatanusuriwa." [Al-Baqara: 48]. Na ukafiri huharibu matendo yote, amesema Mtukufu: "Na anayekufuru kuamini, basi hakika matendo yake yameharibika, naye Akhera atakuwa miongoni mwa wenye hasara." [Al-Ma’idah: 5], Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas Mwenyezi Mungu awawie radhi wote wawili, kuhusu maneno yake: "Na anayekufuru kuamini, basi hakika matendo yake yameharibika." Akasema: “Mwenyezi Mungu aliyetakasika alieleza kwamba imani ndiyo kamba madhubuti, na kuwa hayakubaliki matendo yoyote bila hiyo, wala haiharamishwi Pepo isipokuwa kwa mwenye kuiacha." (Tafsir Twabari 3/113 na 9/593, Ibn Abi Hatim aliipokea katika Tafsir 1307, lakini katika tafsiri ya maneno yake, "Basi wakiamini kama mnavyo amini nyinyi)
Kafiri atadumu milele katika Moto, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika wale waliokufuru na wakadhulumu, hawi Mwenyezi Mungu mwenye kuwasamehe wala kuwaongoa njia. Isipokuwa njia ya Jahannamu. Humo watadumu milele. Na hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi." [An-Nisaa:168,169].
Na ukafiri mkubwa una aina mbalimbali, kama Mwenyezi Mungu alivyoeleza katika kitabu chake, na akaeleza kuwa ukafiri wa makafiri wakati mwingine unakuwa kwa kukataa tu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Tunajua ya kwamba yanakuhuzunisha hayo wanayoyasema. Basi hakika wao hawakukadhibishi wewe, lakini hao madhalimu wanazikataa Ishara za Mwenyezi Mungu." [Al-An'am: 33] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Wala hazikanushi Ishara zetu isipokuwa kila aliye haini kafiri mkubwa." [Luqman: 32], Na amesema Mtukufu: "Na wakazikataa kwa dhuluma na kujivuna, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa waharibifu!" [An-Naml: 14].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kuikataa na kutia kiburi katika haki, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu Ibilisi - ambaye ni imamu wa makafiri: "Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam, wakamsujudia wote isipokuwa Ibilisi, alikataa na akajivuna na akawa katika makafiri." [Al-Baqara: 34]. Na Nuhu alisema: "Na hakika mimi kila nilipowaita ili upate kuwaghufiria, walijiziba masikio yao kwa vidole vyao, na wakajigubika nguo zao, na wakakamia, na wakatakabari vikubwa mno." [Nuh: 7].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kukadhibisha, kama Mwenyezi Mungu alivyosema kuhusu umma zilizotangulia: "Kama yaliyowapata watu wa Firauni na wale waliokuwa kabla yao. Walikanusha Ishara zetu, basi Mwenyezi Mungu aliwashika kwa madhambi yao; na Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu." [Al-Imran: 11], Na akasema Mtukufu: "Bali wale waliokufuru wanakanusha tu." [Al-Inshiqaq: 22]. Na hakuna tofauti baina ya kukadhibisha kwa ulimi na kwa moyo, amesema Mola wa Haki kuhusu wanafiki: "Je, huwaoni wale wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao waliokufuru katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa, na sisi lazima tutatoka pamoja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu. Na mkipigwa vita, lazima tutawasaidia. Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo." [Al-Hashr: 11], Na amesema Mtukufu: "Wanapokujia wanafiki husema: Tunashuhudia ya kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anajua kuwa wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu anashuhudia ya kuwa hakika wanafiki ni waongo." [Al-Munafiqun: 1].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kuwa na shaka na dhana, mtu akawa anasitasita juu ya jambo la haki, akishuku ufufuo na kukutana na Mwenyezi Mungu, amesema Mtukufu akieleza kuhusu yule mwenye bustani kwamba alisema: "Wala sidhani kuwa hiyo Saa (ya Kiyama) itatokea. Na ikiwa nitarudishwa kwa Mola wangu Mlezi, bila ya shaka nitapata marejeo bora zaidi kuliko haya." [Al-Kahf: 36], Basi yule mwenzake muumini akamwambia: "Je, unamkufuru yule aliyekuumba kutokana na udongo, tena kutokana na tone la manii, kisha akakufanya mtu kamili?" [Al-Kahf: 37].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kutukana na kudhihaki, kama alivyosema Mola Mtukufu akieleza kuhusu makafiri: "Na hakika Mitume waliokuwa kabla yako walifanyiwa kejeli, lakini wale waliowafanyia kejeli wakaja kuzungukwa na yale yale waliyokuwa wakiyafanyia kejeli." [Al-An'am: 10], Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu, akitueleza kuhusu watu wa Nuhu na kumdhihaki kwao: "Na akawa anaunda jahazi, na kila wakipita wakuu wa kaumu yake wakimkejeli. Yeye anasema: Ikiwa nyinyi mnatukejeli na sisi tunawakejeli kama mnavyotukejeli." [Hud: 38].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kupuuza na kuzuia njia ya Mwenyezi Mungu, amesema Mtukufu akitueleza kuhusu kupuuza kwa makafiri: "Au wanawaabudu miungu mingine badala yake? Sema: Leteni ushahidi wenu! Haya ni ukumbusho wa hawa walio nami, na ukumbusho wa wale walio kabla yangu. Lakini wengi wao hawaijui kweli, na kwa hivyo wanapuuza." [Al-Anbiya: 24], Na amesema Mtukufu, Mwenye majina matakatifu: "Hatukuziumba mbingu na ardhi wala yaliyomo baina yake isipokuwa kwa haki na kwa muda maalumu. Na wale waliokufuru wanayapuuza yale wanayoonywa." [Al-Ahqaf: 3].
Na wakati mwingine ukafiri unakuwa kwa kuchukia haki, amesema Mtukufu Mwenye Nguvu: "Hayo ni kwa sababu waliyachukia yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, basi akaviharibu vitendo vyao." [Muhammad: 9].
Na tunajua kuwa katika ukafiri kuna ukafiri ulio chini ya ukafiri mkubwa, nao ni ukafiri mdogo. Na huo haupingani na msingi wa imani, bali unapingana na ukamilifu wake tu, na mfanyaji wake hatabakia Motoni milele, na wala haubatilishi matendo yake yote, nao una aina nyingi.
Na miongoni mwake ni maneno yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Kumtukana Muislamu ni ufasiki (kutoka nje ya mipaka), na kupigana naye ni ukafiri." (Imepokelewa na Bukhari 48, Muslim 64, Tirmidhi 1983, An-Nasai 4108, na bin Majah 69). Na miongoni mwake ni maneno yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "(Mambo) Mawili katika watu, hayo kwao ni (mambo ya) ukafiri: Kuutweza uzao wa mtu na kumuomboleza maiti kwa sauti kubwa." (Imepokelewa na Muslim 67). Na maneno ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Msirejee baada yangu mkawa makafiri, mkawa mnauwana nyinyi kwa nyinyi." (Imepokelewa na Bukhari 121, Muslim 65, An-Nasai 4131, na Ibn Majah 3942).
Ukafiri huu haumtoi mtu katika dini, wala mfanyaji wake hatabakia Motoni milele, kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwaita waumini wanaopigana kuwa ni ndugu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ikiwa makundi mawili katika Waumini yanapigana, basi yapatanisheni." [Al-Hujurat: 9], Basi akawaita Waumini ilhali wanapigana. Na alisema Imamu wa watu wa sunna, Imam Ahmad, Mwenyezi Mungu amrehemu, - baada ya kusimulia idadi ya hadithi hizi na zinazofanana na hizo: “Hadithi hizi zilizokuja kwa tamko la: Mambo matatu yatakapokuwa ndani ya mtu, basi atakuwa ni mnafiki." Hii ni kuonyesha ubaya mkubwa wa mambo hayo. Tunazisimulia jinsi zilivyokuja, na hatuzifasiri (kwa maana tofauti) .. na pia Hadithi zinazofanana na hizo ambazo zimesahihishwa na kuhifadhiwa, sisi tunajisalimisha kwazo, hata ikiwa tafsiri yake haijulikani, wala hazizungumziwi, wala hazijadiliwi, Wala hazifasiriwi Hadithi hizi isipokuwa kwa namna zilivyokuja. (Sharh usul i'tikad Ahlus-sunna Wal-jamaa 1/182).
Mlango wa kumshirikisha Mwenyezi Mungu
Na tunajua kuwa katika yale yanayopingana na kumuamini Mwenyezi Mungu ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kuna shirki kubwa na ndogo. Na shirki kubwa inapingana na msingi wa imani, na shirki ndogo inapingana tu na ukamilifu wake. Ushirikina mkubwa ndiyo dhuluma kubwa zaidi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Luqman alipomwambia mwanawe kwa kumpa mawaidha: Ewe mwanangu! Usimshirikishe Mwenyezi Mungu. Kwani hakika ushirikina bila ya shaka ni dhuluma iliyo kubwa." [Luqman: 13]. Ushirikina mkubwa unaharibu matendo yote, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwa yakini yamefunuliwa kwako na kwa wale waliokuwa kabla yako: Bila ya shaka ukimshirikisha Mwenyezi Mungu, matendo yako yataharibika, na lazima utakuwa miongoni mwa wenye kupata hasara." [Az-Zumar: 65], Na amesema Mtukufu: "Huo ni uongofu wa Mwenyezi Mungu. Kwa uongofu huo humuongoa amtakaye katika waja wake. Na lau wangelimshirikisha, yangeliwaharibikia waliyokuwa wakiyatenda." [Al-An'am: 88].
Mwenyezi Mungu hawezi kumsamehe mwenye kufanya shirki kubwa, ikiwa atakufa bila ya kutubia, amesema Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hasamehi kushirikishwa, na husamehe madhambi yasiyokuwa shirki kwa amtakaye. Na anayemshirikisha Mwenyezi Mungu, basi hakika amezua dhambi kubwa." [An-Nisaa: 48]. Na mshirikina akifa ilhali hakutubu, basi ni haramu kwake kuingia Peponi, na makazi yake ni Jahannamu, humo atadumu milele, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwani anayemshirikisha Mwenyezi Mungu, hakika Mwenyezi Mungu atamharamishia Pepo, na mahala pake ni Motoni. Na waliodhulumu hawatakuwa na wa kuwanusuru." [Al-Ma’idah: 72].
Na imesimuliwa kutoka kwa Jabiri kuwa alisema: Mwanaume mmoja alimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni mambo gani mawili yanayowezesha kabisa (kuingia Peponi au Motoni)?" Akasema: "Yeyote yule atakayekufa hali ya kuwa hamshirikishi Mwenyezi Mungu na kitu chochote, ataingia Peponi. Na yeyote yule atakayekufa hali ya kuwa anamshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu chochote, ataingia Motoni." (Imepokelewa na Muslim 93).
Na Mwenyezi Mungu ameifutilia mbali shirki, na akawashutumu washirikina kwa ushirikina wao, na akaeleza uharibifu wao wa kumfanyia wenza, na kwamba hao hawanufaishi, wala hawadhuru. Wakati mwingine, anabainisha kuwa washirika hao hawasikii, na hata wangesikia, wasingewaitikia wale waliowaomba, amesema Mtukufu: "Na hao mnaowaomba badala yake hawamiliki hata ngozi ya kokwa ya tende * Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu; na hata wakisikia, hawawezi kuwajibu. Na Siku ya Kiyama watakataa ushirikina wenu." [Fatir: 13,14]. Basi Mola wa haki akabainisha kuwa hawamiliki chochote, wala hawamsikii mwenye kuwaomba dua, na Siku ya Kiyama wataukana ushirikina wao huo.
Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kuwa washirika hao hawafaidishi wala hawadhuru, na hawamiliki kifo wala uhai, kama alivyosema Mtukufu: "Na wamechukua badala yake miungu ambayo haiumbi chochote, bali hiyo inaumbwa, haijimilikii nafsi zao madhara wala manufaa, wala haimiliki mauti, wala uhai, wala kufufuka." [Al-Furqan: 3], Na amesema Mtukufu: "Akasema: Je, yanawasikia mnapoyaita?* Au yanawafaa au yanawadhuru?" [Ash-Shu’ara: 72, 73].
Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kuwa hao wanaoabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu ni wapungufu zaidi hata kuliko wale wanaowaabudu. Kwani hawatembei, wala hawakamati kitu, wala hawasikii, wala haoni. Hao hawana chochote katika haya ambayo kwayo inawezekana kuleta manufaa na kuzuia madhara. (Tafsir Twabari 13/322). Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Je, wao wanayo miguu ya kwendea? Au wanayo mikono ya kutetea? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio ya kusikilizia? Sema: Ieteni hio miungu yenu ya ushirikina. Kisha nifanyieni mimi vitimbi, wala msinipe muhula." [Al-A'raf: 195].
Na wakati mwingine Mola Mtukufu anaeleza kutoweza kwa waabudiwa hawa na udhaifu wao, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Enyi watu! Unapigwa mfano, basi usikilizeni. Hakika wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu, hawatoumba hata nzi hata kama watajumuika kwa hilo. Na nzi akiwapokonya kitu hawawezi kukipata kutoka kwake. Amedhoofika kweli huyo mwenye kutaka (msaada) na mwenye kutakwa (msaada)." [Al-Hajj: 73], Na amesema Mtukufu: "Na hao mnaowaomba asiyekuwa Mwenyezi hawawezi kuwanusuru, wala hawajinusuru wenyewe." [Al-A'raf: 197].
Na wakati mwingine Mola Mtukufu huwahukumu kwa umasikini na uhaba wa walivyo navyo, na kwamba hawamiliki uzito wa chembe mbinguni wala ardhini umiliki kamili, na hata hawamiliki kwa njia ya ushirikiano chochote katika hivyo, na wala hakuna yeyote miongoni mwao anayemsaidia Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, wala muombezi kwake. Amesema Mtukufu: "Sema: Waiteni mnaowadaia kuwa ni badala ya Mwenyezi Mungu. Hawamiliki hata uzito wa chembe ndogo katika mbingu wala ardhi. Wala hawana ushirika wowote humo. Wala Yeye hana msaidizi miongoni mwao. * Wala uombezi mbele yake hautafaa kitu, isipokuwa kwa yule aliyempa idhini." [Saba: 22, 23].
Na wakati mwingine Mola wa Haki anabainisha kuwa haiwezekani kuwepo miungu wengine pamoja na Mwenyezi Mungu kiulimwengu, na ni batili kisheria. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Lau wangelikuwamo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu, basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeliharibika. Sub-haana Llah (Ametakasika Mwenyezi Mungu), Bwana wa 'Arshi (Kiti cha Enzi), na hayo wanayoyazua." [Al-Anbiya: 22] Na amesema Mwenye Nguvu, Mwenye utukufu mkubwa, na ufalme: "Sema: Lau kuwa wangelikuwa pamoja naye miungu mingine kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Kiti cha Enzi." [Al-Israa: 42]. Na amesema Mtukufu: "Mwenyezi Mungu hakujifanyia mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine. Ingekuwa hivyo, basi kila mungu angelichukua alivyoumba, na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa hizo wanazomsifu kwazo." [Al-Mu’minun: 91].
Na tunajua kuwa shirki kubwa ina aina nyingi:
Na miongoni mwa aina zake ni kumfanyia Mwenyezi Mungu mshirika katika ubwana wake, uumbaji wake, umiliki wake, kuruzuku kwake, kuendesha kwake mambo. Amesema Mola wa Haki akieleza kuhusu ushirikina wao huo: "Au wamemfanyia Mwenyezi Mungu washirika walioumba kama alivyoumba Yeye, na viumbe hivyo vikawafanania sawa? Sema: Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu. Na Yeye ni Mmoja, Mshindi!" [Ar-Ra'd:16], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akimkemea yule anayemfanyia Mwenyezi Mungu mshirika katika viumbe, na hali yeye ni kiumbe ambaye hawezi kuumba: "Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye! Lakini madhalimu wamo katika upotovu uliyo dhahiri." [Luqman: 11], Na Mola wa Haki alibainisha kuwa Yeye Aliyetakasika ndiye wa Pekee katika uumbaji na amri, amesema Mtukufu: "Hakika Mola Mlezi wenu ni Mwenyezi Mungu aliyeziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Kisha akatulizana juu ya Kiti cha Enzi. Huufunika usiku kwa mchana, ufuatao upesi upesi. Na jua, na mwezi, na nyota zilizotiishwa kwa amri yake. Fahamuni! Kuumba ni kwake, na amri (ni yake). Ametukuka kabisa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-A'araf: 54]
Na miongoni mwa aina zake ni kumfanyia mwana Mwenyezi Mungu - Mwenyezi Mungu ametukuka sana juu ya hilo. Amesema Mola Mtukufu: "Na Mayahudi wanasema: Uzeir ni mwana wa Mungu. Na Wakristo wanasema: Masihi ni mwana wa Mungu. Hiyo ndiyo kauli yao kwa vinywa vyao. Wanayaiga maneno ya wale waliokufuru kabla yao. Mwenyezi Mungu awaangamize! Wanageuzwa namna gani hawa!" [At-Taubah: 30], Na amesema Mtukufu: "Bado wamemfanyia Mwenyezi Mungu majini kuwa washirika wake, na hali Yeye ndiye aliyewaumba. Na wakamzulia, bila ya ujuzi wowote, kuwa ana wana wa kiume na wa kike. Sub-hanahu (Ametakasika) na ametukuka juu ya hayo wanayombandikiza nayo!" [Al-An'am: 100], Na amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Na wanamfanyia katika waja wake fungu. Kwa hakika mwanadamu ni mwenye kukufuru mno aliye dhahiri * Au amejifanyia watoto wanawake katika vile alivyoviumba, na akawateulia nyinyi watoto wanaume?" [Az-Zukhruf: 15, 16].
Na miongoni mwa aina zake ni kuamini sayari na kuziabudu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu Ibrahim Al-Khalil (mwandani), amani iwe juu yake, kwamba alijadiliana na watu wake kuhusu kuziabudu sayari: "Na vivyo hivyo tulimuonyesha Ibrahim ufalme wa mbingu na ardhi, na ili awe miongoni mwa wenye yakini * Na ulipomuingilia usiku, akaona nyota, akasema: Huyu ni Mola wangu Mlezi. Ilipotua, akasema: Siwapendi wanaotua * Alipouona Mwezi unachomoza, alisema: Huyu ndiye Mola wangu Mlezi. Ulipotua, akasema: Kama Mola Mlezi wangu hakuniongoa, nitakuwa katika kaumu ya waliopotea. * Na alipoliona Jua linachomoza, akasema: Huyu ndiye Mola wangu Mlezi. Huyu mkubwa kuliko wote. Lilipotua, alisema: Enyi watu wangu! Hakika mimi niko mbali na hayo mnayofanyia ushirikina * Hakika mimi nimeuelekeza uso wangu sawa sawa kwa aliyeziumba mbingu na ardhi, wala mimi si miongoni mwa washirikina * Na watu wake wakamhoji. Akasema: Je, mnanihoji juu ya Mwenyezi Mungu, na hali Yeye ameniongoa? Wala siogopi hao mnaowashirikisha naye, isipokuwa Mola wangu Mlezi akipenda kitu. Mola wangu Mlezi amekusanya elimu ya kila kitu. Basi je, hamkumbuki? * Na vipi nivihofu hivyo mnavyovishirikisha, na hali nyinyi hamhofu kuwa nyinyi mmemshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu ambacho hakukiteremshia uthibitisho wowote. Basi ni kundi gani katika mawili haya lina haki zaidi ya kupata amani, kama nyinyi mnajua?" [Al-An'am: 75-81].
Na miongoni mwa hayo - pia ni kutafuta kunyeshelezewa mvua kupitia nyota, na kuitakidi kwamba zinaleta riziki, amesema Mtukufu: "Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu mnafanya kuwa mnakadhibisha?" [Al-Waqi’ah: 82]. Na imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa alisema: Watu waliteremshiwa mvua katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie. Basi Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Kuna watu walioshukuru miongoni mwa watu, na kuna wale waliokufuru miongoni mwao." Waliosema: "Hii ni rehema (baraka) ya Mwenyezi Mungu" Na wengine wao wakasema: "Hakika nyota kadhaa na kadhaa imesadiki." Basi, aya hii ikateremka "Basi ninaapa kwa maanguko ya nyota" mpaka... "Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu, mnafanya kuwa mnakadhibisha?" [Al-Waqi'ah: 82] (Imepokelewa na Muslim 73, na Twabari katika Tafsir 23/154).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "(Mambo) manne katika umma wangu ni katika mambo ya zama za ujinga; hawatayaacha: Kujifaharisha na vyeo mbalimbali (vya baba zao), kutweza uzao (wa watu wengine), kuomba mvua kunyesha kupitia nyota, na kuomboleza maiti kwa sauti kubwa." (Imepokelewa na Muslim 934, na Ibn Majah 1581).
Na imesimuliwa kutoka kwa Zaid bin Khalid al-Juhani kuwa alisema: Alituswalisha Mtume rehema na amani ziwe juu yake swala ya Alfajiri huko Hudaibia baada usiku wa mvua. Baada ya kukamilisha swala, aliwaelekea watu na akasema: "Je, mnajua Mola wenu Mlezi amesema nini?" (Watu) wakasema: "Mwenyezi Mungu na Mtume wake ndio wanajua zaidi." Akasema: "Asubuhi ya leo, baadhi ya waja wangu wameniamini na wengine wamekufuru. Ama aliyesema kuwa: Tuliteremshiwa mvua kutokana na fadhila za Mwenyezi Mungu na rehema zake, basi huyo ndiye aliyeniamini na akaikufuru (imani ya) nyota. Na ama aliyesema: Tuliteremshiwa mvua kwa sababu ya nyota fulani na fulani, basi huyo ndiye aliyenikufuru na akaiamini nyota." (Imepokelewa na Bukhari 846, Muslim 71, Abu Daud 3906, na An-Nasai 1525).
Na miongoni mwa aina zake ni kumfanyia Mwenyezi Mungu mshirika katika majina yake na sifa zake, ametakasika na kutukuka, kama vile anayedai kuwa kuna mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayejua ghaibu, Mwenyezi Mungu alimuamrisha Mtume wake rehema na amani ziwe juu yake aseme kuwa: "Sema: Mimi siwaambii kuwa ninazo hazina za Mwenyezi Mungu. Wala sijui mambo yaliyofichikana. Wala siwaambii kuwa mimi ni Malaika. Mimi sifuati isipokuwa yale yanayofunuliwa kwangu. Sema: Je, wanakuwa sawa, kipofu na mwenye kuona. Basi hamtafakari?" [Al-An'am: 50], Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Hakika mambo ya ghaibu ni ya Mwenyezi Mungu tu." [Yunus: 20]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake alisema: “Mwenye kumjia kuhani – Musa akasema katika hadithi yake – na akamsadikisha katika mambo anayoyasema – au mwenye kumuingilia mwanamke aliye katika hedhi, au mwenye kumuingilia katika tupu yake ya nyuma, basi yuko mbali mno na yale yaliyoteremshwa kwa Muhammad (katenda dhambi kubwa).” (Imepokelewa na Abuu Daud 3904, Tirmidhi 135, Ibn Majah 639, Al-Fadhl ibn Dakin katika Swala 15, Ishaq ibn Rahawaihi 482, na Ahmad 9536). Na ahadi ya adhabu kali ilikuja kwa wale wanaojiita wenyewe, au kuwaita wengine mojawapo ya majina ya Mwenyezi Mungu ambayo hayamstahiki yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee, kama vile neno la ukuu “Allah,” au “Mwingi wa rehema.” Amesema Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri kabisa, basi muombeni kwa hayo. Na waacheni wale wanaoharibu utakatifu wa majina yake. Hao watakujalipwa yale waliyokuwa wakiyatenda." [Al-A'raf: 180] Na amesema Mola Mtukufu: "Mwenyezi Mungu! Hapana mungu isipokuwa Yeye. Yeye ana majina mazuri kabisa." [Twaha: 8], Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Jina ovu zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama ni la mwanaume aliyejiita Mfalme wa wafalme" (Imepokelewa na Bukhari 6205, Muslim 2143, Abu Daud 4961, na Tirmidhi 2837).
Na amesema Abuu Ubaid Mwenyezi Mungu amrehemu: "Sufian bin Uyaina alikuwa akifafanua kauli yake: "Mfalme wa wafalme" Akisema: Ni kama wanavyosema: Shahan Shah, yaani, mfalme wa wafalme. Na wasiokuwa Sufian walisema: Bali ni mtu kujiita kwa majina ya Mwenyezi Mungu, kama vile kusema: Mwingi wa rehema, Mfanya atakalo, Mwenye nguvu. Akasema: Mwenyezi Mungu ndiye Mfalme wa wafalme, na hairuhusiwi kwa yeyote asiyekuwa Yeye kujiita kwa jina hili. (Gharib al-Hadith, cha Al-Qasim bin Salam 2/18).
Na katika aina zake ni kuitakidi kwamba yeyote katika viumbe ana sifa ya ukamilifu wa kimungu, au kwamba ana uwezo juu ya vitu vyote?! Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Wala hana anayefanana naye hata mmoja." [Al-Ikhlaas: 4], Na akasema Aliyetakasika na kutukuka: "Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake. Basi muabudu Yeye tu, na udumu katika ibada yake. Je, mnamjua mwenye jina kama lake?" [Maryam: 65], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu ukamilifu wa uwezo wake: "Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye uwezo juu ya kila kitu." [Al-Baqara: 148], Amesema Mola Mtukufu: "Na hapana kitu kinachoweza kumshinda Mwenyezi Mungu mbinguni wala katika ardhi. Hakika Yeye ni Mwenye kujua, Mwenye uwezo." [Fatwir: 44], Na Mwenyezi Mungu aliyetakasika alibainisha kutoweza kabisa kwa wale wanaoabudu na wale wanaoabudiwa badala yake, akasema aliyetukuka, mwenye mamlaka makuu: "Enyi watu! Unapigwa mfano, basi usikilizeni. Hakika wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu, hawawezi kuumba hata nzi ijapokuwa watajumuika kwa hilo. Na nzi akiwapokonya kitu, hawawezi kukipata kutoka kwake. Amedhoofika kweli huyo mwenye kutaka na mwenye kutakiwa." [Al-Hajj: 73],
Na miongoni mwa aina zake ni kumfanyia Mwenyezi Mungu miungu mingine, kama alivyoeleza Mwenyezi Mungu kuhusu watu wa Ibrahim, amani iwe juu yake, kwamba walichukua miungu badala ya Mwenyezi Mungu, akasema Mtukufu: "Na pale Ibrahim alipomwambia baba yake, Azar: Unayafanya masanamu kuwa ni miungu? Hakika mimi ninakuona wewe na watu wako mmo katika upotofu ulio wazi." [Al-An'am: 74], Pia Mola wa Haki alitueleza kuhusu wale watu wa pangoni kwamba walijitenga mbali na watu wao; kwa sababu walijifanyia miungu wengine badala ya Mwenyezi Mungu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu Aliyetakasika: "Hawa watu wetu wameshika miungu mingine badala yake Yeye. Kwa nini basi hawawatolei uthibitisho ulio dhahiri? Na ni nani aliye dhalimu zaidi kuliko anayemzulia uongo Mwenyezi Mungu?" [Al-Kahf: 15], Na amesema Aliyetakasika kuhusu watu wa Musa, amani iwe juu yake, kwamba walimuomba Musa awafanyie mungu kama washirikina walivyokuwa na miungu. "Na tukawavusha bahari Wana wa Israeli, wakafika kwa watu wanaoabudu masanamu yao. Wakasema: Ewe Musa! Hebu tufanyie na sisi miungu kama hawa walivyokuwa na miungu. Musa akasema: Hakika nyinyi ni watu msiojua kitu. * Hakika haya waliyo nayo watu hawa yatakuja angamia, na hayo waliyokuwa wakiyafanya yamepotea bure." [Al-A'raf: 138, 139] Na amesema Mtukufu akibatilisha kuabudiwa kila mungu asiyekuwa Mwenyezi Mungu: "Mwenyezi Mungu hakujifanyia mwana yeyote, wala hanaye mungu mwingine. Ingekuwa hivyo, basi kila mungu angelichukua alivyoumba, na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa hizo wanazomsifu kwazo." [Al-Mu’minun: 91].
Na miongoni mwa aina zake ni kumfanyia ibada au sehemu katika ibada yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Amesema aliyetukuka akielezea hali ya washirikina: "Na wamemuwekea sehemu Mwenyezi Mungu katika mimea na wanyama alioumba, nao husema: Hii ni sehemu ya Mwenyezi Mungu - kwa madai yao - na hii ni ya miungu tunaowashirikisha. Basi vile walivyowakusudia miungu yao, havimfikii Mwenyezi Mungu, na vile vilivyokuwa vya Mwenyezi Mungu, huwafikia miungu yao. Ni uovu kabisa hayo wanayoyahukumu." [Al-An'am:136], Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Amesema Mwenyezi Mungu, Aliyetakasika na kutukuka: "Mimi ndiye nisiyehitaji mshirika kabisa. Atakayefanya jambo lolote na akanishirikisha mimi na mwingine ndani yake, nitamuacha pamoja na mshirika wake huyo." (Imepokelewa na Muslim 2985).
Na miongoni mwa aina zake ni kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu kama njia ya kujiweka karibu na kitu hicho, kama vile mwenye kuchinjia masanamu au wafu ili kujiweka karibu nao, amesema Mola Mtukufu akibainisha kwamba kuchinja hakupasi kuwa isipokuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, aliyetakasika na kutukuka: "Sema: Hakika Swala yangu, na ibada zangu, na uhai wangu, na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-An'am: 162]. Na amesema Mtukufu: "Hakika amewaharamishia nyamafu, na damu, na nyama ya nguruwe, na mnyama aliyechinjwa kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Lakini anayelazimishwa bila ya kuasi, wala kuruka mipaka, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu." [An-Nahl: 115]. Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Tufail ('Amir bin Wathila) kuwa alisema: Tulimuuliza Ally (bin Abii Twalib): Je, tuambie kuhusu kitu ambacho Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alikuambia kwa siri. Akasema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, hakuniambia chochote kwa siri ambacho hakuwaambia watu wote, isipokuwa nilimsikia akisema: "Mwenyezi Mungu amemlaani mwenye kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Muslim 1978, na An-Nasai 4422). Kwa sababu jambo hili ni kubwa sana, Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikataza kuchinjia katika sehemu ambayo huchinjwa kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Imesimuliwa kutoka kwa Thabit bin Adh-Dhwahak, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Mtu mmoja aliweka nadhiri katika zama za Mtume rehema na amani ziwe juu yake ya kuchinja ngamia huko Buwana – ambapo ni mahali tambarare nyuma ya Yanbu, karibu na pwani ya bahari - basi akamjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: Niliweka nadhiri kuwa nitamchija ngamia huko Buwana. Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: “Je, kulikuwa na sanamu miongoni mwa masanamu yaliyokuwa yakiabudiwa katika zama za ujinga?" Wakasema: Hapana. Akasema: “Je, hapo kulikuwa na sikukuu miongoni mwa sikukuu zao?” Wakasema: Hapana. Akasema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Itimize nadhiri yako. Kwani hakuna kutimiza nadhiri katika kumuasi Mwenyezi Mungu, wala katika kile asichokiweza mwanadamu." (Imepokelewa na Abu Daud 3313).
Na miongoni mwa aina zake ni kumuwekea nadhiri asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Kwani kuweka nadhiri ni kumuabudu Mwenyezi Mungu, na wala hairuhusiwi kuiweka kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Ndiyo maana Mwenyezi Mungu akawasifu waumini wanaotekeleza nadhiri. Amesema Mtukufu: "Wanatimiza nadhiri zao, na wanaiogopa siku ambayo shari yake itaenea sana." [Al-Insan: 7], Na akasema Mtukufu: "Na chochote mnachotoa au nadhiri mnazoweka, basi hakika Mwenyezi Mungu anajua. Na wale waliodhulumu hawana wa kuwanusuru." [Al-Baqara: 270]. Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenye kuweka nadhiri ya kumtii Mwenyezi Mungu, basi na amtii. Na anayeweka nadhiri ya kumuasi, basi asimuasi." (Imepokelewa na Bukhari 6696, Abu Daud 3289, Tirmidhi 1526, An-Nasai 3806, na Ibn Majah 2126).
Miongoni mwa aina zake ni kujilinda kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa alisema: "Walikuwapo wanaume fulani miongoni mwa watu ambapo mmoja wao alikuwa akikesha usiku kwenye bonde katika zama za ujinga, na alikuwa akisema: Ninajikinga kwa mtukufu wa bonde hili, na hilo likawazidishia dhambi." (Imepokelewa na Twabari katika Tafsiri 23/322). Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu akieleza kuhusu hali ya watu wa zama za ujinga: "Na hakika walikuwako wanaume katika watu waliokuwa wakitafuta kujikinga kwa wanaume wa kijini; kwa hivyo wakawazidisha madhambi." [Al-Jinn: 6]. Na alitueleza Mtume rehema na amani ziwe juu yake kwamba atakayeshuka mahali popote na akasema: "A'udhu bikalimatillahit-tammati min sharri ma khalaqa (Ninajilinda kwa maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyotimia kutokana na shari ya alichokiumba)." basi hakitamdhuri kitu chochote mpaka aondoke kutoka mahali pake hapo." (Imepokelewa na Muslim 2708, Tirmidhi 3437, na Ibn Majah 3547).
Na miongoni mwa aina zake ni kutafuta kuokolewa na kupata msaada kutoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu katika yale ambayo Mwenyezi Mungu peke yake ndiye anaweza kuyafanya, au kumuomba dua asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Amesema Mtukufu: "Na hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu, basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu." [Al-Jinn: 18]. Na akasema Mtukufu: "Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu; na hata wakisikia hawawezi kuwajibu. Na Siku ya Kiyama watakataa ushirikina wenu. Na hapana atakayekupa habari vilivyo kama Yeye Mwenye habari." [Fatwir: 14], Na amesema Mola Mtukufu akieleza kuwa washirikina yanapowapata madhara hutafuta msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kisha wanarejea katika ushirikina wao pindi Mwenyezi Mungu anapowaokoa. "Na wanapopanda katika merikebu, humuomba Mwenyezi Mungu kwa kumsafia utiifu. Lakini anapowavusha wakafika nchi kavu, mara wanamshirikisha." [Al-Ankabut: 65], Na amesema Aliyetukuka: "Na ni nani mpotofu mkubwa kuliko wenye kuomba badala ya Mwenyezi Mungu wale ambao hawatawaitikia mpaka Siku ya Kiyama, na wala hawatambui maombi yao." [Al-Ahqaf: 5], Na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu, akieleza kuwa Yeye ndiye anayewapa nafuu wenye dhiki na kuwaondolea madhara. "Au ni nani yule anayemjibu mwenye shida pale anapomuomba, na akaiondoa dhiki, na akawafanya nyinyi warithi wa ardhi? Je, yupo mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ni machache mnayoyazingatia." [An-Naml: 62].
Na miongoni mwa aina zake ni kumshirikisha katika kumtii asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema akieleza kuhusu Watu wa Kitabu kwamba waliwachukua makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu, wakawa wanawawekea sheria, na kuwaharamishia yale aliyowahalalishia Mwenyezi Mungu: "Wamewafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu, na pia Masihi bin Maryamu. Na wala hawakuamrishwa isipokuwa wamuabudu Mungu Mmoja, hapana mungu isipokuwa Yeye. Sub-haanahu (Ametakasika) na hayo wanayomshirikisha nayo." [At-Tawba: 31], Na akasema Mtukufu: "Au hao wana miungu ya kishirikina waliowatungia dini asiyoitolea idhini Mwenyezi Mungu?" [Ash-Shura: 21]. Na Mwenyezi Mungu aliwaamrisha waja wake kumwamini na kuhukumu kwa sheria yake, na akabainisha kwamba Shetani anataka watafute hukumu kwa Taghut. Amesema Mtukufu: "Huwaoni wale wanaodai kwamba wameamini yale yaliyoteremshwa kwako na yaliyoteremshwa kabla yako? Wanataka wakahukumiwe kwa njia ya upotofu, na hali wameamrishwa wakatae hayo! Na Shetani anataka kuwapotezelea mbali." [An-Nisaa: 60]. Imesimuliwa kutoka kwa 'Adi bin Hatim, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Nilimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, hali ya kuwa kuna msalaba wa dhahabu shingoni mwangu. Akasema: "Ewe 'Adi! Jiondolee sanamu hili." Na nikamsikia akisoma Suratu Baraa "Wamewafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu." [At-Tawba : 31]. Akasema: "Ama hakika, wao hawakuwa wakiabudiwa, lakini walikuwa wakiwahalalishia kitu, wao pia wanakihalalisha. Na wakiwaharamishia kitu, wao pia wanakiharamisha.” (Imepokelewa na Tirmidhi 3095, Ibn Saad 6/219, Ibn Abi Hatim katika Tafsiri 10057, na Twabrani katika Al-Kabir 17/92/218).
Na miongoni mwa aina zake ni kumshirikisha katika kuswali, kurukuu, kusujudu, na kuzunguka Al-Ka'ba. Na hilo ni kwa sababu ibada hizi na mifano yake haziruhusiwi kumfanyia yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu alimuamuru rafiki yake mwandani (Ibrahim), amani iwe juu yake, kuitakasa nyumba yake kwa ajili ya wanaoizunguka, wanaokaa humo kwa ajili ya ibada na wanaorukuu na kusujudu. Amesema Mtukufu: "Na pale tulipomuweka Ibrahim pahala penye ile Nyumba tukamwambia: Usinishirikishe na chochote; na isafishe Nyumba yangu kwa ajili ya wanaoizunguka kwa kutufu, na wanaokaa hapo kwa ajili ya ibada, na wanaorukuu, na wanaosujudu." [Al-Hajj: 26], Na aliamrisha Mola wa Haki kuwa asujudiwe Yeye peke yake, Aliyetakasika na kutukuka, amesema Mtukufu: "Na katika Ishara zake ni usiku na mchana, na jua na mwezi. Basi msilisujudie jua wala mwezi, bali msujudieni Mwenyezi Mungu aliyeviumba, ikiwa nyinyi mnamuabudu Yeye tu." [Fusswilat: 37]. Na wala hawaoni uvunjifu katika kumuabudu Mwenyezi Mungu isipokuwa wenye kiburi, amesema Mola wa Haki Aliyetakasika na kutukuka: "Ewe Ibilisi! Ni kipi kilichokuzuia kumsujudia yule niliyemuumba kwa mikono yangu? Je, umetakabari, au umekuwa katika wakuu kweli?" [Swad: 75], Na Mwenyezi Mungu ametaja kwamba viumbe wote wanamsujudia, amesema Mtukufu: "Na vyote vilivyo katika mbingu na katika ardhi, kuanzia wanyama mpaka Malaika, vinamsujudia Mwenyezi Mungu, na wala havitakabari." [An-Nahl: 49] Na katika kisa cha Ja'fari Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, alipoingia alimokuwa An-Najashi, Ja'fari akasema: “Mimi ndiye nitawazungumzia leo.” Basi wakamfuata mpaka wakaingia alimokuwa Mfalme Najashi, lakini hawakumsujudia. Akasema: Mna nini hamumsujudii mfalme?' Akasema: Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu ametutumia Nabii wake, rehema na amani ziwe juu yake, na akatuamrisha kuwa tusimsujudie yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu. (Imepokelewa na Twayalasi 344, Said bin Mansur 2481, Ahmad 4400, Luwain kwa Juz-u 4, na Twahawi katika Alhkamul-Qur'an 418).
Na miongoni mwa aina zake ni kuhukumu kwa yale ambayo hakuyateremsha Mwenyezi Mungu, na kutafuta hukumu kutoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka alibainisha hukumu ya mwenye kuhukumu kwa yale ambayo hakuyateremsha Mwenyezi Mungu, akasema yeye mwenye sifa tukufu, na majina matakatifu: "Na wasiohukumu kwa yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio makafiri." [Al-Ma’idah: 44]. Na akasema Mola wa Haki Mtukufu: "Na wasiohukumu kwa yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio madhalimu." [Al-Ma’idah: 45]. Na amesema Mola Mtukufu: "Na wasiohukumu kwa yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio wavukao mipaka." [Al-Ma’idah: 47]; Hilo ni kwa sababu amri zote ni za Mwenyezi Mungu, amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Fahamuni! Kuumba ni kwake na amri. Ametukuka kabisa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote." [Al-A'araf: 54], Na amesema Mtukufu: "Na washirikina wanasema: Mwenyezi Mungu angelitaka, tusingeliabudu chochote badala yake, sisi wala baba zetu, wala tusingeliharamisha chochote bila ya Yeye. Kama hivyo walifanya wale waliokuwa kabla yao. Basi lipo lolote juu ya Mitume isipokuwa kufikisha kwa wazi?" [An-Nahl: 35].
Na Mwenyezi Mungu amewakemea watu wa kitabu kwa kuwafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa miungu wanaowawekea sheria. Amesema Mtukufu: "Wamewafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu, na pia Masihi bin Maryamu. Na wala hawakuamrishwa isipokuwa wamuabudu Mungu Mmoja, hapana mungu isipokuwa Yeye. Sub-hanahu (Ametakasika) na hayo wanayomshirikisha nayo." [At-Tawbah: 31]. Na amesema Mola wa Haki Aliyetukuka: "Au hao wana miungu ya kishirikina waliowatungia dini asiyoitolea idhini Mwenyezi Mungu?" [ASh-Shura: 21]. Imesimuliwa kutoka kwa 'Adi bin Hatim, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Nilimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, hali ya kuwa kuna msalaba wa dhahabu shingoni mwangu. Akasema: "Ewe 'Adiyu! Jiondolee sanamu hili." Na nikamsikia akisoma Suratu Bara’a: "Wamewafanya makuhani wao na makasisi wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu." [At-Tawba : 31]. Akasema: “Ama hakika, wao hawakuwa wakiwaabudu, lakini walikuwa wakiwahalalishia kitu, wao pia wanakihalalisha. Na wakiwaharamishia kitu, wao pia wanakiharamisha.” (Imepokelewa na Tirmidhi 3095, Ibn Sa'ad 6/219, Ibn Abi Hatim katika Tafsir 10057, na Twabrani katika Al-Kabir 17/92/218).
Watu wa Kitabu wanajifananisha na washirikina katika hilo, ambao Mwenyezi Mungu alisema juu yao: "Na washirikina wanasema: Mwenyezi Mungu angelitaka, tusingeliabudu chochote badala yake, sisi wala baba zetu, wala tusingeliharamisha chochote bila ya Yeye. Kama hivyo walifanya wale waliokuwa kabla yao. Basi lipo lolote juu ya Mitume isipokuwa kufikisha kwa wazi?" [An-Nahl: 35].
Na amesema Mtukufu: " La! Ninaapa kwa Mola wako Mlezi! Hawataamini mpaka wakufanye wewe ndiye muamuzi katika yale wanayohitilafiana, kisha wasione uzito wowote katika nyoyo zao juu ya hukumu utakayotoa, na wanyenyekee kabisa." [An-Nisaa: 65]. Amesema aliyetukuka: "Au hao wana miungu ya kishirikina waliowatungia dini asiyoitolea idhini Mwenyezi Mungu?" [Ash-Shura: 21]. Na amesema Mtukufu: "Je, wao wanataka hukumu za Kijahiliya? Na ni nani aliye mwema zaidi katika kuhukumu kuliko Mwenyezi Mungu kwa watu wenye yakini?" [Al-Ma’idah: 50].
Na miongoni mwa aina zake ni kufanya shirki katika mapenzi, na hili ni mtu kumpenda kiumbe upendo unaoambatana na kudhalilika, kutukuza, na kunyenyekea. Amesema Mtukufu kuhusu mapenzi ya washirikina kwa masanamu yao. "Na katika watu wapo wanaochukua waungu wasiokuwa Mwenyezi Mungu. Wanawapenda kama kumpenda Mwenyezi Mungu." [Al-Baqara: 165], Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa alisema: Nilimuuliza Mtume rehema na amani ziwe juu yake: Ni dhambi gani kubwa zaidi? Akasema: "Ni kumfanyia Mwenyezi Mungu mwenza ilhali Yeye ndiye aliyekuumba." (Imepokelewa na Bukhari 4477, Muslim 86, Abu Daud 2310, Tirmidhi 3182, na An-Nasai 4013).
Na miongoni mwa aina zake ni shirki ya hofu na kunyenyekea. Na hili ni kuhofu au kuogopa kiumbe hofu inayoambatana na kunyenyekea, kudhalilika na kutukuza, kama vile kuogopa kwamba kitamfikishia msiba, au kumzuia heri fulani, au kuacha jambo la wajibu kwa ajili yake, au kufanya jambo lililoharamishwa kwa ajili yake kwa njia ya kujikurubisha kwake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika huyo ni Shetani anawatia hofu marafiki zake. Basi msiwaogope, bali niogopeni Mimi ikiwa nyinyi ni Waumini." [Al-Imran: 175]. Na washirikina wanaitakidi kuwa miungu yao inadhuru na kunufaisha; ndiyo maana wakadhania kuwa miungu yao ilimtia balaa Nabii wa Mwenyezi Mungu Hud, amani iwe juu yake, waliposema: "Hatusemi ila kuwa baadhi ya miungu yetu imekutia kwenye tabu na balaa: Akasema: Hakika mimi ninamshuhudisha Mwenyezi Mungu, na nyinyi shuhudieni, ya kwamba mimi ninajitenga mbali na hao mnaowafanya washirika." [Hud: 54]. Amesema Mujahid: "Baadhi ya miungu yetu imekusababishia balaa” Akasema: Inamaanisha kwamba masanamu yamekupatisha uwendawazimu." (Tafsir Twabari 15/361). Na amesema Mola wa Haki kuhusu mwenye dini nyoofu, amani iwe juu yake (yaani Ibrahim): "Na vipi nivihofu hivyo mnavyovishirikisha, hali nyinyi hamhofu kuwa nyinyi mmemshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu ambacho hakukiteremshia uthibitisho. Basi kundi gani katika mawili haya lina haki zaidi kupata amani, kama nyinyi mnajua?" [Al-An'am: 81].
Na watu wa zama za ujinga walikuwa wakijikinga kwa mabwana wa kijini kwa sababu ya kuwaogopa wapumbavu wao. Amesema Mtukufu: "Na hakika walikuwako wanaume katika watu waliokuwa wakitafuta kujikinga kwa wanaume wa kijini; kwa hivyo wakawazidisha madhambi." [Al-Jinn: 6].
Na amesema Mtukufu: "Na walipoamrishwa kupigana vita, mara kundi moja kati yao liliwahofu watu kama kumhofu Mwenyezi Mungu, au kwa hofu kubwa zaidi." [An-Nisaa: 77]. Na alibainisha Mola wa Haki kuwa vipenzi wake hawamhofu isipokuwa Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka kama alivyosema Mtukufu: "(Hao wa zamani) waliokuwa wakifikisha jumbe za Mwenyezi Mungu na wanamhofu Yeye, na wala hawamhofu yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ndiye atoshaye kuhesabu." [Al-Ahzab: 39], Na alisema pia: "Hakika wanaoimarisha misikiti ya Mwenyezi Mungu ni wale wanaomuamini Mwenyezi Mungu, na Siku ya Mwisho, na wakashika Swala, na wakatoa Zaka, na wala hawamchi isipokuwa Mwenyezi Mungu. Basi huenda hao wakawa katika waongofu." [At-Tawba: 18]. Na alieleza kwamba wale wachawi (katika zama za Nabii Musa), baada ya kuamini kwao, walipendelea kumcha Mwenyezi Mungu kuliko kumcha Firauni na ukandamizaji wake. Amesema Mtukufu akieleza kuhusu maneno yao: "Wakasema: Hatutokukhiari wewe kuliko ishara waziwazi zilizo tujia, na kuliko yule aliye tuumba. Basi hukumu utakavyo hukumu; kwani wewe unahukumu haya ya maisha ya duniani tu * "Hakika sisi tumemuamini Mola wetu Mlezi ili atusamehe makosa yetu na uchawi uliotulazimisha kuufanya. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mbora na Mwenye kudumu zaidi." [Twaha: 72, 73].
Na miongoni mwa aina zake ni kushirikisha katika matumaini. Na hilo ni kama vile mtu kutarajia kutoka kwa kiumbe kilicho hai, kilichopo au kisichokuwepo, kitu ambacho Mwenyezi Mungu pekee ndiye anaweza kukifanya, au kutarajia kutoka kwa wafu ili waondoe dhiki, kutimiza mahitaji, na kufanya uombezi Siku ya Kiyama. Amesema Mola wa Haki akieleza juu ya sababu iliyowafanya washirikina kuabudu miungu yao: "Sisi hatuwaabudu isipokuwa ili wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu." [Az-Zumar: 3]. Na amesema Mtukufu: "Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu; na hata wakisikia, hawawezi kuwajibu. Na Siku ya Kiyama watakataa ushirikina wenu. Na hapana atakayekupa habari vilivyo kama Yeye Mwenye habari." [Fatwir: 14], Na Mwenyezi Mungu alibainisha kwamba washirika hawa hawamiliki kitu chochote. Amesema Mtukufu: "Sema: Mnawaona hawa miungu wenu wa kishirikina mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu! Nionyesheni wameumba sehemu gani katika ardhi? Au wana ushirika wowote katika mbingu? Au tumewapa Kitabu nao kwa hicho wakawa na hoja zilizo wazi? Lakini madhalimu hawaahidiani wao kwa wao isipokuwa udanganyifu tu." [Fatwir: 40], Na amesema Mtukufu kuhusu wafuasi kwamba wataambiwa Siku ya Kiyama: "Waiteni hao miungu wa kishirikina wenu! Basi watawaita, lakini hawatawaitikia, na wataiona adhabu; laiti wangelikuwa wameongoka!" [Al-Qasas: 64]. Kila kitu kilichokuja katika Qur’ani kikitaja suala la washirikina kuwaomba miungu wao ni ushahidi juu ya ushirikina wao katika matumaini. "Bila ya shaka mnayeniitia kumuabudu hastahiki wito duniani wala Akhera. Na hakika marejeo yetu ni kwa Mwenyezi Mungu. Na wanaopindukia mipaka ndio watu wa Motoni!" [Ghafir: 43]. Lau kuwa hawakuwa wakiitakidi kwamba wanaweza kuwaitikia, basi yule Muumini wa familia ya Firauni asingeliwakanusha.
Na miongoni mwa aina zake ni uchawi. "Bali mashetani ndio waliokufuru, wakiwafundisha watu uchawi, na yale yaliyoteremshwa kwa Malaika wawili, Haaruta na Maaruta katika (mji wa) Babeli. Wala hao hawakumfundisha yeyote mpaka wamwambie: Hakika sisi ni mtihani; basi usikufuru." [Al-Baqara: 102]. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: Jiepusheni madhambi saba makuu yenye kuangamiza." Watu wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni yapi hayo Akasema: "Kumshirikisha Mwenyezi Mungu, uchawi, kuua nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameiharamisha, isipokuwa tu kwa haki, kula riba, kula mali ya yatima, kukimbia mnapokutana na adui katika jihadi, na kuwasingizia uongo wanawake waliotakasika Waumini wasiojua (maovo)." (Imepokelewa na Bukhari 2766, Muslim 89, Abu Daud 2874, na An-Nasai 3671).
Na imesimuliwa kutoka kwa Amri bin Dinar, ambaye alimsikia Bajaala akimhadithia Amri bin Aws na Abuu Sha'athaa, alisema: Nilikuwa mwandishi wa Juz bin Muawia, ami yake Al-Ahnaf bin Qaisi, na tazama ikatufikia barua ya Omari mwaka mmoja kabla ya kifo chake: “Waueni wachawi wote...” (Imepokelewa na Abu Daud 3043, Abdur-Razzaq 9972, Sa'id bin Mansur 2180, na Ahmad 1657).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Atakayechukua sehemu katika elimu ya nyota, atakuwa kachukua sehemu ya uchawi, utaongezeka (uchawi huo) kila anapoongeza (elimu hiyo)." (Imepokelewa na Abuu Daud 3905, Ibn Majah 3726, Ibn Abī Shaiba 26159, Ahmad 2000, na 'Abd ibn Humaid 714).
Na miongoni mwa aina zake ni ukuhani na kupiga ramli (uaguzi); kwa sababu mwenye kudai hayo, anadai kuwa anajua elimu ya ghaibu. "Yeye ndiye Mwenye kujua ya siri, wala hamdhihirishii yeyote siri yake * Isipokuwa Mtume wake aliyemridhia. Naye huyo humwekea walinzi mbele yake na nyuma yake." [Al-Jinn: 26, 27]. Imesimuliwa kutoka kwa Swafia, kutoka kwa baadhi ya wake wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Yeyote atakayemwendea kuhani na akamuuliza juu ya kitu, hazitakubaliwa Swala zake kwa siku arobaini." Imepokelewa na Muslim 2230).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira na Al-Hasan, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: “Atakayemjia kuhani au mtabiri kisha akamuamini katika kile anachosema, basi hakika ameshakufuru yale yaliyoteremshwa kwa Muhammad.” (Imepokelewa na Ahmad 9536 kutoka kwa Abuu Huraira, na Al-Hasan, na Imepokelewa na Abuu Daud 3904, Tirmidhi 135, Ibn Majah 639, Ibn Abi Shaiba 17077, Ishaq bin Rahawaihi 482, na Ahmad 9290 kutoka katika hadithi ya Abuu Huraira.
Na tunajua kwamba katika shirki ni shirki ndogo ambayo haimtoi mtu katika dini, wala haimfanyi mfanyaji wake kubakia milele Motoni, wala haiharibu matendo yake yote, nayo ina aina nyingi:
Na miongoni mwake ni kuamini mikosi ya ndege, na uhakika wake - kama ilivyo katika Hadithi - ni kile kinachokufanya kutenda jambo au kukuzuia kulifanya. Amesema Mtukufu: "Likiwafika jema, wanasema: Haya ni haki yetu. Na likiwafika ovu, husema: Musa na wale walio pamoja naye ni wakorofi. Hakika ukorofi wao huo unaowafikia unatoka kwa Mwenyezi Mungu. Lakini wengi wao hawajui." [Al-A'raf: 131] Na amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Wakasema: Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je, ni kwa kuwa mnakumbushwa? Ama nyinyi ni watu waliopindukia mipaka." [Yasin: 19]. Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakuna kuenea kwa ugonjwa (bila amri ya Mwenyezi Mungu), wala hakuna mkosi unaoweza kusababishwa na ndege, wala hakuna mkosi unaosababishwa na bundi" (Imepokelewa na Bukhari 5707, Muslim 2220, na Abuu Daud 3911).
Na imesimuliwa kutoka kwa 'Urwa bin 'Aamir Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Ilitajwa mikosi ya Ndege mbele ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: “Kilicho bora ni kuwa na matumaini, na wala hilo halipaswi kumrudisha Muislamu. Kwa hivyo mmoja wenu akiona jambo analolichukia, basi na aseme: Ewe Mwenyezi Mungu, hakuna aletaye mazuri isipokuwa wewe, na wala hakuna azuiaye mabaya isipokuwa wewe, na hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwako Wewe." (Imepokelewa na Abuu Daud 3919, na Ibn Abī Shaiba katika Muṣannaf 26920 na katika Al-Adab 162, na Al-Khallal katika 1405).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Amri Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Mwenye kurudishwa kwa sababu ya kuamini mkosi wa ndege asitekeleze mahitaji yake, basi hakika amefanya shirki." Wakasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kafara ya hilo ni nini? Akasema: “Ni mmoja wao aseme: Ewe Mwenyezi Mungu, hakuna heri isipokuwa heri yako, na hakuna kuamini mikosi ya ndege isipokuwa athari zote hutoka kwako, na hakuna mungu isipokuwa wewe." (Imepokelewa na Ibn Wahab katika Al-Jami' 658, na Ahmad 7045, na matamshi ya hadithi hii ni yake, na Twabrani katika Al-Kabir 14622, na Ibn Sunni katika 'Amalul-Yaum Wal-Layla 292).
Na miongoni mwake ni kufunga au kutundika hirizi. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Bashir Al-Answari, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi kuwa: “Alikuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, katika baadhi ya safari zake, Abdullah akasema: Nilidhania kuwa alisema: Na watu walikuwa kwenye makazi yao. Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake akamtuma mjumbe kuwa: Kamwe usibakie mkufu wa kamba ya upinde au mkufu wowote ule katika shingo za ngamia isipokuwa ukatwe.” (Imepokelewa na Bukhari 3005, Muslim 2115, na Abuu Daud 2552).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Nilimsikia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akisema: “Hakika kombe za kishirikina, na hirizi, na limbwata (uchawi unaofanywa kumfanya mtu kupendwa na mpenzi wake) ni ushirikina.” (Imepokelewa na Abuu Daud 3883, Ibn Majah 3530, Muammar katika Al-Jami' 20343, Ibn Abī Shaiba 23924, na Ahmad 3615).
Amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Mwenye kufungamana na kitu chochote (cha kishirikina), basi atakabidhiwa kwa hicho." (Imepokelewa na Tirmidhi 2072, na Ibn Abī Shaiba katika Al-Muṣannaf 23923, na katika Al-Musnad 786, na Ahmad 18781).
Na miongoni mwake ni riyaa chache (kujionyesha). Ama ikiwa moyo wake utajaa kujionyesha, na akawa anafanya matendo mema bila ya nia, imani, wala hofu, basi huyo ni mnafiki halisi, na matendo yake ni batili na yatakataliwa wala hayatakubaliwa. Amesema Mtukufu: "Kwa hivyo, mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi, basi na atende vitendo vyema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi." [Al-Kahf: 110], Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Amesema Mwenyezi Mungu, Mwingi wa baraka, Mtukufu: Mimi ndiye nisiyehitaji zaidi mshirika kati ya washirika wote. Kwa hivyo, yeyote atayefanya jambo lolote na akanishirikisha ndani yake na mwingine, nitamuacha na mshirika wake huyo." (Imepokelewa na Muslim 2985).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika mtu wa kwanza kuhukumiwa siku ya Kiyama, ni mwanaume aliyeuawa shahidi. Ataletwa, na (Mwenyezi Mungu) atamjulisha neema zake, naye atazijua. (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Ulifanya nini kwazo?" Atasema: "Nilipigana kwa ajili yako mpaka nikauawa shahidi." (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Umedanganya, bali wewe ulipigana ili isemwe: "(wewe ni) jasiri" na tayari ilishasemwa." Kisha, itatolewa amri juu yake, na atavutwa juu ya uso wake mpaka utupwe ndani ya Moto. Na mwanaume aliyesoma elimu na akaifunza (kwa wengine), na akasoma Qur'ani. Kwa hivyo, ataletwa, na (Mwenyezi Mungu) atamuonyesha neema zake (juu yake), naye atazijua. (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Ulifanya nini kwazo?" Atasema: "Nilisoma elimu na nikasoma Qur'ani kwa ajili yako." (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Umedanganya. Bali wewe ulisoma elimu ili isemwe: "Mwanachuoni". Na ukasoma Qur'ani ili isemwe "Yeye ni msomaji (mzuri wa Qur'ani)" na tayari ilishasemwa." Kisha itatolewa amri juu yake na atabururwa juu ya uso wake mpaka atupwe ndani ya Moto. Na mwanaume ambaye Mwenyezi Mungu alimkunjulia na akampa kila aina ya mali. Basi, ataletwa na (Mwenyezi Mungu) atamjulisha neema zake (juu yake), naye atazijua. (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Ulifanya nini kwazo?" Atasema: "Sikuacha njia yoyote unayoipenda kwamba itolewe mali katika njia hiyo isipokuwa nilitoa mali katika njia hiyo kwa ajili yako." (Mwenyezi Mungu) Atasema: "Umedanganya. Bali wewe ulifanya (hivyo) ili isemwe "huyu ni mkarimu" na tayari ilishasemwa." Kisha, itatolewa amri juu yake na atabururwa juu ya uso wake mpaka atupwe ndani ya Moto." (Imepokelewa na Muslim 1905, Tirmidhi 2382, na An-Nasai 3137).
Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Mwenye kuwasikilizisha watu (matendo yake mema kwa makusudi ili wamsifu), basi Mwenyezi Mungu atawafanya watu kujua nia yake halisi (Siku ya Kiyama ili amdhalilishe). Na mwenye kujionyesha, Mwenyezi Mungu atawaonyesha watu matendo yake halisi." (Imepokelewa na Bukhari 6499, Muslim 2987, na Ibn Majah 4207).
Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Omari Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mwenye kuwasikilizisha watu matendo yake, Mwenyezi Mungu atawasikilizisha habari zake wote wanaosikia katika viumbe wake, na atafanya adharaulike na kudunishwa." (Imepokelewa na Ibn al-Mubarak katika Az-Zuhd 141, Ibn Abī Shaiba 36448, Hannād katika Az-Zuhd 872, Ahmad 6509) na katika Az-Zuhd 238).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Musa kuwa: Mwanaume mmoja alimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni nini kupigana katika njia ya Mwenyezi Mungu? Kwani, mmoja wetu anapigana kwa sababu ya hasira, na baadhi yetu ni kwa sababu ya ushabiki mpofu tu." Basi Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akainua kichwa chake akamuelekea. (Msimulizi) alisema: Na wala hakuinua kichwa chake kumuelekea isipokuwa (muulizaji) alikuwa amesimama. Akasema: "Mwenye kupigana ili neno la Mwenyezi Mungu (Uislamu) liwe juu zaidi, basi huyo yuko katika njia ya Mwenyezi Mungu Mwenye Nguvu, aliyetukuka." (Imepokelewa na Bukhari 123, Muslim 1904, Abuu Daud 2517, Tirmidhi 1646, An-Nasai 3136, na Ibn Majah 2783).
Na tunajua kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake aliiita shirki ya siri, Imesimuliwa kutoka kwa Mahmud bin Labid kuwa amesema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Jihadharini, tena jihadharini na shirki ya siri." Wakasema: “Ni nini shirki ya siri?" Akasema: "Ni mmoja wenu kusimama na akaanza kuipamba swala yake kwa kutia juhudi kubwa; ili watu wamuangalie. Hiyo ndiyo shirki ya siri.” (Imepokelewa na Ibn Abī Shaiba 8489, Ibn Khuzaima 937, Twabarani katika Al-Kabīr 4301, Al-Baihaqī katika As-Sunan Al-Kubra 3629, na katika Ash-Shu'ab 2872).
Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alibainisha kwamba kujionyesha ni jambo lililofichika sana, na kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akilihofia hilo kwa umma wake zaidi kuliko hofu yake kwao juu ya Masihi Dajal, kama alivyosema: “Je, nisiwaambie ninayowahofia zaidi kuliko Misihi Dajali?" Akasema: Tukasema: Ndiyo. Akasema: “Shirki iliyofichika ni mtu kunyanyuka akiswali na akaipamba Swala yake kwa sababu ya anavyoona kuwa kuna mtu anamtazama.” (Imepokelewa na Ibn Majah 4204, Ahmad 11252, Hanbal ibn Ishaq katika Al-Fitan 30, na Twabari katika Tahdhib Al-Aathaar 1117).
Na miongoni mwa shirki ndogo ni mtu kufanya matendo yake huku akiitaka dunia kwayo. Amesema Mtukufu: "Mwenye kutaka mavuno ya Akhera, tutamzidishia katika mavuno yake. Na mwenye kutaka mavuno ya duniani, tutampa katika hayo, lakini katika Akhera hana fungu lolote." [Ash-Shura: 20], Na amesema Mwenyezi Mungu mwenye utukufu mkubwa: "Wanaotaka maisha ya dunia na pumbao lake, tutawalipa humo vitendo vyao kamili. Na wao humo hawatopunjwa." [Hud: 15]. Na hili liko kati ya kuwa shirki kubwa na kuwa ndogo kulingana na yaliyomo moyoni mwa mja. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Anayetaka starehe hii ya dunia ipitayo upesi upesi, tutafanya haraka kumletea hapa hapa tunayoyataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannamu; ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa." [Al-Israa: 18].
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Musa, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Mwanaume mmoja alimjia Mtume rehema na amani zimshukie akasema: "Mtu anapigana vita kwa ajili ya kupata ngawira, na mwingine anapigana vita ili awe na umaarufu, na mwingine anapigana vita ili kujionyesha cheo chake. Basi ni nani (kati yao) yuko katika njia ya Mwenyezi Mungu?" (Mtume) Akasema: "Mwenye kupigana vita ili neno la Mwenyezi Mungu liwe ndilo la juu zaidi, basi huyo ndiye aliye katika njia ya Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari 2810, Muslim 1904, Abuu Daud 2517, na An-Nasai 3136). Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimuapiza yule ambaye dunia hii ndiyo hamu yake kubwa, na lengo lake. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa amesema: Alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Ameangamia mtumwa wa Dinari na Dirhamu na mavazi na mapambo (yani pesa na nguo za kifahari). Kwani, akipewa, anaridhia (anafurahi), na akinyimwa haridhii!" (Imepokelewa na Bukhari 2886, na Ibn Majah 4135).
Na miongoni mwake ni mtu kusema: Atakavyo Mwenyezi Mungu, na utakavyo.” na maneno kama hayo. Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kuwa alisema: Mwanaume mmoja alimwambia Mtume rehema na amani ziwe juu yake: Atakavyo Mwenyezi Mungu, na utakacho wewe. Mtume rehema na amani ziwe juu yake akamwambia: "Umenifanya kuwa sawa na Mwenyezi Mungu. Bali sema tu: Atakacho Mwenyezi Mungu peke yake. (Imepokelewa na Ibn Abī Shaiba 27227, Ahmad 1839, Bukhari katika Al-Adab Al-Mufrad 783, Ibn Abī Dunia katika As-Swamt 342, na al-Baaghandī katika Amaali 36). Maneno haya yanafanana na maneno yao: Haya yametoka kwa Mwenyezi Mungu na kutoka kwako. Na, "lau kuwa si Mwenyezi Mungu na fulani, basi yasingekuwa hivi.
Na miongoni mwake ni kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Anayetaka kuapa, basi na asiape isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu tu." Na Makureshi walikuwa wakiapa kwa baba zao, basi (Mtume) akasema: "Msiape kwa baba zenu." (Imepokelewa na Bukhari 3836, Muslim 1646, na An-Nasai 3764). Imesimuliwa kutoka kwa Ibn Omari Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake, alisema: “Mwenye kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, basi hakika amekufuru au ameshirikisha.” (Imepokelewa na Tirmidhi 1535, Ahmad 6072, Abu 'Awana 6401, na Al-Hakim 7895).
Mlango wa unafiki
Na miongoni mwa mambo ambayo yanapingana na kumuamini Mwenyezi Mungu ni unafiki. Na hilo ni kuudhihirisha Uislamu na kuficha ukafiri. Nao unaweza kuwa unafiki mkubwa na mdogo. Unafiki mkubwa unapingana na msingi wa imani, lakini unafiki mdogo unapingana tu na ukamilifu wake. Imam Ahmad alisema katika Usuulus-Sunna: “Unafiki ni ukafiri, pale mtu anapomkufuru Mwenyezi Mungu, na akamuabudu mwingine, na akaonyesha Uislamu kwa dhahiri tu, kama vile walivyokuwa wanafiki katika zama za Mtume rehema na amani ziwe juu yake." (Usul as-Sunna, uk. 55). Na unafiki mkubwa unamtoa mtu katika Uislamu.
Na tunashuhudia kwa ushahidi wa Mwenyezi Mungu kwamba wanafiki ni waongo katika madai yao kuwa ni waumini. Amesema Mwenye nguvu, Mwenye mamlaka makubwa: "Na wapo waliojenga msikiti kwa ajili ya madhara na ukafiri na kuwafarikisha Waumini, na pa kuvizia kwa waliompiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake hapo kabla. Na bila ya shaka wataapa kwamba: Hatukukusudia isipokuwa wema tu. Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo." [At-Tawba: 107]. Na amesema Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu anashuhudia ya kuwa hakika wanafiki ni waongo."
Mwenyezi Mungu hakubali amali njema wala fidia kutoka kwa mnafiki. Amesema Mtukufu: "Sema: Toeni mkipenda msipende. Hakitopokelewa kitu kwenu, kwani nyinyi ni watu wapotovu * "Na hawakuzuiliwa kukubaliwa michango yao isipokuwa kwa kuwa walimkataa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala hawaji kwenye Swala isipokuwa kwa uvivu, wala hawatoi michango isipokuwa nao wamechukia." [At-Tauba: 53, 54].
Na maishio ya mnafiki - ikiwa atakufa ilhali bado ana unafiki - ni kudumu milele katika Jahannamu. Amesema Mtukufu: "Hakika wanafiki watakuwa katika tabaka ya chini kabisa Motoni, wala hutampata yeyote wa kuwanusuru." [An-Nisaa: 145]. Na akasema Mtukufu: "Mwenyezi Mungu amewaahidi wanafiki wanaume na wanafiki wanawake na makafiri Moto wa Jahannamu kudumu humo. Hayo yanawatosha, na Mwenyezi Mungu amewalaani; nao wana adhabu ya milele." [At-Tauba: 68].
Na tunajua kuwa unafiki mkubwa unakuwa kwa kuichukia haki, amesema Mtukufu akieleza kuhusu hali ya wanafiki: "Hayo ni kwa sababu wao waliyafuata yaliyomchukiza Mwenyezi Mungu na wakachukia yanayomridhisha, basi akaviharibu vitendo vyao * Je, wenye maradhi nyoyoni mwao wanadhani kwamba Mwenyezi Mungu hatazidhihirisha chuki zao? * Na tungelipenda, tungelikuonyesha hao na ungeliwatambua kwa alama zao; lakini bila ya shaka utawajuwa kwa namna ya msemo wao. Na Mwenyezi Mungu anavijua vitendo vyenu." [Muhammad: 28-30].
Na unakuwa kwa kufurahia kushindwa kwa Uislamu na watu wake, na majuto makubwa ikiwa wataona Uislamu umeshinda. Amesema Mola wa Haki Mtukufu aliye juu zaidi, akibainisha yaliyomo ndani ya nyoyo zao: "Ukikupata uzuri, unawachukiza. Na ukikusibu msiba, wao husema, Sisi tuliangalia mambo yetu vizuri tangu mwanzo. Na hugeuka kwenda zao nao wamefurahi" [At-Tauba: 50].
Na unakuwa kwa kukufuru baada ya kuamini, na kukataa kuhukumu kwa mujibu wa Sheria ya Mwenyezi Mungu. Amesema Mtukufu: "Na wanasema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu na Mtume, na tumetii. Kisha kikundi katika hao hugeuka baada ya hayo. Wala hao si Waumini * Na wanapoitwa kumuendea Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili ahukumu baina yao, kipo kikundi katika wao kinakataa" [An-Nur: 47, 48].
Na unakuwa kwa kumdhania mabaya Mwenyezi Mungu kuwa hatamnusuru Mtume wake rehema na amani ziwe juu yake, na dini yake. Amesema Mola wa Haki Mtukufu, Aliye juu zaidi: "Na waliposema wanafiki, na wale wenye maradhi katika nyoyo zao: Mwenyezi Mungu na Mtume wake hawakutuahidi isipokuwa udanganyifu tu." [Al-Ahzab: 12].
Na unakuwa kwa kuidhihaki haki na watu wake, na kuwatukana na kuwakejeli. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Wanafiki wanaogopa isijeteremshwa Sura itakayowatajia yaliyomo katika nyoyo zao. Sema: Fanyeni mzaha! Hakika Mwenyezi Mungu atayatoa nje hayo mnayoyaogopa * Na ukiwauliza, wanasema: Sisi tulikuwa tukipiga porojo na kucheza tu. Sema: Mlikuwa mkimfanyia maskhara Mwenyezi Mungu na Ishara zake na Mtume wake?" [At-Tawba: 64, 65].
Na unakuwa kwa kuwabeza Waislamu. Amesema Mtukufu: "Wale wanaowabeuwa Waumini wanaotoa sadaka nyingi na wasio nacho cha kutoa isipokuwa kwa kiwango cha juhudi yao, basi huwakejeli. Mwenyezi Mungu atawakejeli wao! Nao watapata adhabu chungu!" [At-Tauba: 79].
Na unakuwa kwa kuwahadaa waumini, na kujionyesha kwa matendo. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu Aliyetakasika: "Wanatafuta kumdanganya Mwenyezi Mungu na wale walioamini, lakini hawadanganyi isipokuwa nafsi zao; nao hawatambui." [Al-Baqara: 9], Na alisema pia: "Hakika wanafiki wanamhadaa Mwenyezi Mungu, na hali ni Yeye ndiye mwenye kuwahadaa wao. Na wanapoinuka kuswali, huinuka kwa kivivu, wanajionyesha kwa watu tu, wala hawamdhukuru Mwenyezi Mungu isipokuwa kidogo tu." [An-Nisaa: 142]. Imesimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: “Hiyo ndiyo swala ya mnafiki; anakaa akingojea jua mpaka wakati linapokuwa baina ya pembe mbili za Shetani, anainuka na kuidonoa (hiyo swala) rakaa nne, hamtaji Mwenyezi Mungu ndani yake isipokuwa kidogo tu." (Imepokelewa na Muslim 622, Abuu Daud 413, Tirmidhi 160, na An-Nasai 511).
Na amesema Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu amridhie: "Kwa hakika, tulijiona kuwa asiyehudhuria swala huyo ni mnafiki ambaye unafiki wake umeshajulikana." (Imepokelewa na Muslim 654, Abuu Daud 550, An-Nasai 849, na Ibn Majah 777).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira Mwenyezi Mungu amridhie, kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Basi ninaapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mkononi wake! Hamtapata shida yoyote katika kumuona Mola wenu Mlezi siku hiyo, kama ambavyo hampati shida yoyote katika kuona moja ya hivyo viwili." Akasema: "Kisha (Mwenyezi Mungu) atakutana na mja mmoja na atasema: "... mpaka aliposema: "Kisha atakutana na wa tatu na atamwambia mfano wa hayo. Naye atasema: "Ewe Mola wangu Mlezi! Nilikuamini Wewe, na kitabu chako, na Mitume wako, na niliswali, nikafunga na nikatoa sadaka." na atajisifu kwa mema kiasi atakavyoweza. Kisha, (Mwenyezi Mungu) atasema: "Basi, (simama) hapa hapa." Akasema: Ataambiwa: "Sasa tutawaleta mashahidi wetu juu yako." naye atafikiria katika nafsi yake: "Ni nani huyo atakayekuwa shahidi juu yangu?" Kisha atafungwa mdomo wake na litaambiwa paja lake na nyama zake na mifupa yake: "Tamka." Kisha, paja lake na nyama zake na mifupa yake vitatamka juu ya amali zake. Na hilo, ili asiweze kujipa udhuru wowote mwenyewe. Na huyo ndiye mnafiki. Na huyo ndiye Mwenyezi Mungu atamkasirikia." (Imepokelewa na Muslim 2968).
Na Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na Waumini kupigana jihadi dhidi yao. Mwenye nguvu amesema: "Ewe Nabii! Pambana na makafiri na wanafiki, na wakazanie. Na makazi yao ni Jahannamu, na huo ndio mwisho mbaya * Wanaapa kwa Mwenyezi Mungu kuwa hawakusema; nao wamekwishasema neno la ukafiri, na wakakufuru baada ya kusilimu kwao. Na wakajihimu kufanya ambayo hawakuweza kuyafikia. Na hawakuchukia isipokuwa ni kwakuwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake amewatajirisha kutokana na fadhila zake. Wakitubu, itakuwa heri kwao. Na wakigeuka, Mwenyezi Mungu atawaadhibu adhabu chungu duniani na Akhera. Na wala hawana katika ardhi mlinzi wala wa kuwanusuru." [At-Tawba: 73, 74].
Na tunajua kwamba unafiki mdogo haumtoi mtu katika dini, wala haubatilishi matendo, wala mfanyaji wake hatabakia milele Motoni, na kwamba unafiki una aina mbalimbali. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mambo manne yatakayekuwa ndani yake basi atakuwa ni mnafiki halisi. Na atakayekuwa na moja katika hayo, basi kutakuwa ndani yake na sifa ya unafiki mpaka aliache: Akiaminiwa, anahaini, na anapozungumza, anadanganya, na anapofanya agano analivunja, na anapogombana anakataa haki wazi wazi." (Imepokelewa na Bukhari 34, Muslim 58, Abu Daud 4688, Tirmidhi 2632, na An-Nasai 5020).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Musa, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kuwa alisema: "Muumini ambaye husoma Qur'ani na kuifanyia kazi, ni kama balungi (chenza); ladha yake ni tamu, na harufu yake ni nzuri. Na mfano wa Muumini ambaye haisomi Qur'ani, lakini anaifanyia kazi, ni kama tende; ladha yake ni tamu, lakini haina harufu yoyote. Na mfano wa mnafiki ambaye husoma Qur'ani, ni kama maua ya Mrehani; harufu yake ni nzuri na ladha yake ni chungu. Na mfano wa mnafiki ambaye haisomi Qur'ani, ni kama shubiri; ladha yake ni chungu, na harufu yake ni mbaya." (Imepokelewa na Bukhari 5059, Muslim 797, Tirmidhi 2865, An-Nasai 5038, na Ibn Majah 214).
Mlango wa Bad'a (uzushi)
Na tunajua kwamba kuna baadhi ya mambo ya uzushi ambayo yanapingana na msingi wa imani, na baadhi yake yanapingana na ukamilifu wa imani. Uzushi wa kishirikina na wa kikafiri unapingana na msingi wa imani, lakini uzushi ambao haufikii kiwango cha ushirikina na ukafiri unapingana tu na ukamilifu wa imani.
Na tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alitukamilishia Dini na akatukamilishia neema zake juu yetu. Amesema Mola wa Haki Mtukufu: "Leo nimewakamilishia Dini yenu, na nimewatimizia neema yangu, na nimewapendelea Uislamu uwe ndiyo Dini." [Al-Ma’idah: 3]. Amesema Mtume, rehema na amani zimshukie: “Mwenye kuzua katika jambo letu hili, jambo ambalo halimo ndani yake, basi hilo litakataliwa.” (Imepokelewa na Bukhari 2697, Muslim 1718, Abu Daud 4606, na Ibn Majah 14).
Na tunajua kuwa miongoni mwa mambo yanayopingana na ukamilifu wa imani ni uzushi katika dini. Amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Na jihadharini na mambo mapya (katika dini); Kwani kila mambo mapya ni uzushi, na kila uzushi ni upotofu.” (Imepokelewa na Abuu Daud 4607, Tirmidhi 2676, Ibn Majah 42, Ahmad 17144, Ibn Abi 'Asim katika As-Sunna 26, na Ibn Wadhaah katika Al-Bida' 54).
Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Atakayeita kwenye uongofu, atapata malipo mfano wa malipo ya atakayeufuata, na hilo halitapunguza kitu katika malipo yao. Na atakayeita kwenye upotofu, atapata madhambi mfano wa madhambi ya atakayeufuata, na hilo halitapunguza kitu katika madhambi yao." (Imepokelewa na Muslim 2674, Abuu Daud 4609, Tirmidhi 2674, na Ibn Majah 206).
Na Bukhari, Mwenyezi Mungu amrehemu, aliandika mlango katika "Sahihi yake" na akasema: “Mlango wa dhambi ya mwenye kulingania kwenye upotofu, au aliyeanzisha nyendo mbaya.” kisha akataja kauli yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakuna nafsi yoyote itakayouawa kwa dhuluma, isipokuwa linakuwa fungu juu ya mwana wa kwanza wa Adam" - na wakati mwingine Sufian alisema - ".. katika damu yake. Kwa sababu, yeye ndiye mtu wa kwanza kuua." (Imepokelewa na Bukhari 7321, Muslim 1677, Tirmidhi 2673, An-Nasai 3985, na Ibn Majah 2616).
Na imesimuliwa kutoka kwa Abuu Said, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika, mtazifuata nyendo za wale waliokuwa kabla yenu shibri (kiganja) kwa shibri (kiganja), na dhiraa kwa dhiraa kiasi kwamba hata kama wataingia ndani ya shimo la kenge, basi nyinyi pia mtaliingia." Tukasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Je, unamaanisha Mayahudi na Wakristo?" Akasema: "Nani mwingine (kama si hao)?" (Imepokelewa na Bukhari 3456, na Muslim 2669).
Na tunajua kuwa Mwenyezi Mungu amekataza mifarakano na kutofautiana. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu, mwenye majina matakatifu: "Wala msiwe kama wale waliofarakiana na kuhitilafiana baada ya kuwafikia hoja zilizo wazi. Na hao ndio watakaokuwa na adhabu kubwa." [Al-Imran: 105], Na amesema Mtukufu: "Basi nawatahadhari wale wanaohalifu (kwenda kinyume na) amri yake, usije ukawapata msiba au ikawapata adhabu chungu." [An-Nur: 63].
Na tunajua kuwa katika uzushi ni kuyapa makaburi taadhima, kuyajengea juu yake, na huenda hilo likafikia kumshirikisha Mwenyezi Mungu. Na katika uzushi ni kuwapiga picha watu wema kwa matumaini ya kuwaiga baada ya kufa kwao. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “...Sikilizeni! Hakika wale waliokuwa kabla yenu walikuwa wakiyafanya makaburi ya Manabii wao na watu wema kuwa ni sehemu za ibada. Sikilizeni! Nyinyi msiyafanye makaburi kuwa ni misikiti. Hakika mimi ninawakataza hilo. (Imepokelewa na Muslim 532).
Na imesimuliwa kutoka kwa Aisha Mwenyezi Mungu amridhie kuwa: Ummu Habiba na Ummu Salama walielezea kuhusu kanisa waliloliona huko Uhabeshi (Ethiopia) ambamo kulikuwa na picha. Basi wakamwambia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, juu ya hilo, akasema: "Hakika hao watu anapokuwa miongoni mwao mtu mwema kisha akafa, wanajenga kwenye kaburi lake mahali pa ibada na kutengeneza picha hizi ndani yake. Basi hao ndio waovu wa viumbe wote kwa Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama." (Imepokelewa na Bukhari 427, Muslim 528, na An-Nasai 704).
Na aliamrisha Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuharibu masanamu na kuyasawazisha makaburi. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Hayaj Al-Asadi kuwa alisema: Ali [bin Abi Twalib], Mwenyezi Mungu awe radhi naye, aliniambia: "Je, nisikutume katika yale aliyonituma kwayo Mtume rehema na amani ziwe juu yake? Kwamba usiliache sanamu lolote isipokuwa uliharibu, wala kaburi lolote lililoinuka, isipokuwa ulisawazishe." (Imepokelewa na Muslim 969, Abuu Daud 3218, Tirmidhi 1049, na An-Nasai 2031).
Na tunajua kuwa miongoni mwa mambo ya uzushi ya kupingwa ni sherehe za uzushi na kushirikiana na makafiri katika sikukuu zao. Imesimuliwa kutoka kwa Anas bin Malik, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa amesema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake alikuja Madina na walikuwa na siku mbili za kucheza, basi akasema: “Hizi ni siku mbili gani?" Wakasema: Tulikuwa tunacheza katika siku mbili hizi katika zama za ujinga. Akasema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Hakika, Mwenyezi Mungu amewabadilishia zilizo bora kuliko mbili hizo: Siku ya Idul-Adha na Siku ya Idul-Fitr.i” (Imepokelewa na Abuu Daud 1134, An-Nasai 1556, na Ismail bin Jaafar katika hadithi na Ali Ibn Hujr 62, Ahmad 12827, na Abd l bin Humaid 1392).
Na amesema Mwenyezi Mungu Mwenye sifa tukufu: "Kwa kila umma tumeuwekea ibada ambazo wao huzishika. Basi wasizozane nawe katika jambo hili. Na waite watu kwenda kwa Mola wako Mlezi. Hakika wewe uko katika uongofu ulionyooka." [Al-Hajj: 67]. Na imesimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuhusiana na kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa kila umma tumeuwekea ibada ambazo wao huzishika." Akasema: Ni sikukuu." (Tafsir Twabari 18/679, na Ibn Abi Hatim katika Tafsir 14718). Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Hakika kila kaumu ina sikukuu yake. Na hii ni Idi (siku kuu) yetu." (Imepokelewa na Bukhari 952, Muslim 892, Abu Daud 1593, na Ibn Majah 1898).
Na tunajua kwamba miongoni mwa mambo ya uzushi ya kupingwa ni kutafuta baraka kutoka kwa kitu ambacho Mwenyezi Mungu hakukifanya kuwa sababu ya baraka. Na hili linaweza kuwa ni sababu ya kufanya ushirikina. Imesimuliwa kutoka kwa Abuu Waqid Al-Laithi, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alipotoka kwenda huko Hunain, alipita karibu na mti mmoja wa washirikina unaoitwa Dhatu Anwat, ambao walikuwa wakitundika silaha zao juu yake. (Watu) wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tufanyie Dhat Anwat kama walivyo na Dhat Anwat. Basi Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Mwenyezi Mungu ametakasika! Hivi ndivyo walivyosema watu wa Musa: “Tufanyie mungu kama walivyo na miungu” [Al-A’raf: 138] “Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu imo mkononi mwake, bila shaka mtafuata nyendo za wale waliokuwa kabla yenu.” (Imepokelewa na Tirmidhi 2180, Muammar katika Al-Jami' 20763, Abdur-Razzaq katika Tafsir 931, na Ibn Abī Shaiba 38530).
Mlango wa madhambi makubwa
Tunajua kwamba kuna madhambi makubwa na madogo. Amesema Mwenye Nguvu Mtukufu: "Ambao wanajiepusha na madhambi makubwa na vitendo vichafu, isipokuwa makosa hafifu." [An-Najm: 32], Na amesema Mwenye Nguvu, Mtukufu: "Mkiyaepuka makubwa mnayokatazwa, tutawafutia makosa yenu madogo, na tutawaingiza mahali patukufu." [An-Nisaa: 31].
Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Mwanaume mmoja alisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni dhambi gani iliyo kubwa zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu? Akasema: “Ni kumuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu ilhali yeye ndiye aliyekuumba." Akasema: Kisha dhambi gani? Akasema: Ni kumuua mwanao kwa kuogopa kuwa atakujakula pamoja nawe." Akasema: Kisha lipi? Akasema: "Ni kuzini na mke wa jirani yako.” Basi Mwenyezi Mungu akateremsha uthibitisho wake: "Na wale wasiomuomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaui nafsi aliyoiharamisha Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa haki, wala hawazini." (Imepokelewa na Bukhari 6001 na Muslim 86).
Na tunajua kwamba imani inaongezeka na inapungua. Amesema Mtukufu: "Na inapoteremshwa Sura, wapo miongoni mwao wasemao: Ni nani miongoni mwenu Sura hii imemzidishia Imani? Ama wale walioamini, inawazidishia Imani, nao wanafurahi." [At-Tauba: 124]. Mambo ya utiifu huongeza imani na kuiimarisha, na madhambi hupunguza imani na kuidhoofisha. Kwa hivyo, maasi - ambayo ni madogo kuliko ukafiri na ushirikina - hupingana tu na ukamilifu wa imani, na mwenye kufanya dhambi kubwa haondolewa imani kamili, lakini pia hasifiwi kuwa ana imani kamili, kwa sababu alifanya jambo ambalo linapunguza imani yake, na ndiyo maana Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Hazini mwenye kuzini wakati anapozini hali ya kuwa ni Muumini, na wala hanywi pombe wakati anapokunywa hali ya kuwa ni Muumini, na wala mwizi haibi wakati anapoiba hali ya kuwa ni Muumini, na wala hanyang'anyi anachonyang'anya watu wakimwangalia kwa macho yao kwa sababu ya hilo wakati anaponyang'anya hali ya kuwa ni Muumini." (Imepokelewa na Bukhari 2475, na Muslim 57). Na amesema Mtume rehema na amani zimshukie: "Atakayeona miongoni mwenu maovu, basi na ayazuie kwa mkono wake, na kama hawezi, basi kwa ulimi wake, na kama hawezi, basi kwa moyo wake, na hiyo ndiyo imani dhaifu mno." (Imepokelewa na Muslim 49). Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akieleza kuhusu yale yatakayotokea Siku ya Kiyama: "...Kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu atasema: Nendeni, na yeyote mtakayepata ndani ya moyo wake kuna imani sawa na uzito wa nusu ya dinari moja, basi muondoeni kutoka humo." (Imepokelewa na Bukhari 7439, na Muslim 183). Hivyo basi, hadithi hizi zikaonyesha kuwa madhambi hudhoofisha imani.
Mwenye kufanya dhambi kubwa ameahidiwa kuadhibiwa kwa dhambi yake kubwa hiyo maadamu hakutubia akaiacha, au akatekelezewa adhabu maalumu ya kisheria - ikiwa dhambi kubwa hiyo imewekewa adhabu maalumu, au Mwenyezi Mungu amsamehe kupitia sababu mojawapo ya msamaha ambazo ni nyingi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu hasamehi kushirikishwa, na husamehe madhambi yasiyokuwa shirki kwa amtakaye." [An-Nisaa: 48].
Kitabu cha Maswahaba na uimamu
Mlango wa Maswahaba na ali (jamaa au familia) yake Mtume, Mwenyezi Mungu awe radhi nao
Tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwateua Maswahaba wa Nabii wake, rehema na amani ziwe juu yake, na akawafanya kuwa ndio bora zaidi katika viumbe wake baada ya Manabii, amani iwe juu yao, na akataja sifa zao na akawasifu katika Taurati na Injili. Amesema Mtukufu: "Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na wale walio pamoja naye wana nguvu mbele ya makafiri, na wanahurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama na kusujudu wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Alama zao zi katika nyuso zao, kwa athari ya kusujudu. Huu ndio mfano wao katika Taurati. Na mfano wao katika Injili ni kama mmea uliotoa chipukizi lake, kisha ukalitia nguvu, ukawa mnene, ukasimama sawa juu ya Buwa lake, ukawafurahisha wakulima, ili kuwakasirisha kwa ajili yao makafiri. Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walioamini na wakatenda mema katika wao msamaha na ujira mkubwa." [Al-Fath: 29], Na ametaja Mola wa Haki kuwa ameridhika nao, amesema Mtukufu: "Na wale waliotangulia, wa kwanza, katika Wahajiri (Walio hama) na Answari (watu wa Madina), na wale waliowafuata kwa wema, Mwenyezi Mungu amewaridhia, na wao wamemridhia; na amewaandalia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele. Huko ndiko kufuzu kukubwa." [At-Tawba: 100].
Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake. alibainisha kuwa Maswahaba wake watukufu ndio kizazi bora kuliko vizazi vyote. Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah kuwa alisema: Aliulizwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Ni akina nani watu bora zaidi?" Akasema: "Watu wa kizazi changu, kisha wale watakaofuata, na kisha wale watakaofuata." (Imepokelewa na Bukhari 6658, Muslim 2533, Tirmidhi 3859, na Ibn Majah 2362).
Na tunaamini kuwa Wahajiri (walio hama) ni bora kuliko Answari (walio wapokea), Mwenyezi Mungu awe radhi nao. Ndiyo maana Mwenyezi Mungu akawataja kwanza katika Kitabu chake madhubuti, kama ilivyo katika Aya iliyotangulia ya “Surat Tauba”. Mwenyezi Mungu Mtukufu aliye juu akawasifu wahajiri, akasema: "Wapewe mafukara Wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Hao ndio wakweli." [Al-Hashr: 8].
Amesema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka kuhusiana na Manswari: "Na wale walio na maskani zao na Imani yao kabla yao, wanawapenda wale waliohamia kwao, wala hawaoni choyo katika vifua vyao kwa walivyopewa (Wahajiri), bali wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji. Na mwenye kuepushwa uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufanikiwa." [Al-Hashr: 9].
Na tunaamini kuwa mbora wa Umma huu baada ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake, ni Abubakari kisha Omari kisha Othman, kisha Ali, Mwenyezi Mungu awawie radhi. Kwa hivyo utaratibu wao katika ubora ni sawa na utaratibu wao katika ukhalifa.
Na tunawashuhudia wale kumi walioahidiwa Pepo, kuwa ni watu wa peponi, kama alivyowashuhudia Mtume rehema na amani ziwe juu yake, ambapo Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie, alisema: “Abubakari ataingia Peponi, Omari ataingia Peponi, Othman yuko Peponi, Ali ataingia Peponi, Twalha ataingia Peponi, Az-Zubair ataingia Peponi, Abdur-Rahman bin 'Auf ataingia Peponi, Sa'd ataingia Peponi, Sa'id atakuwa Peponi, na Abu Ubaida bin Al-Jarraah atakuwa Peponi.” (Imepokelewa na Tirmidhi 3747, Ahmad katika Al-Musnad 1675, na katika Fadhila za Maswahaba 278, na Ibn Abī 'Āṣim katika Al-Aahaad wal-Mathani 232).
Na tunaamini kuwa watu wa Badri, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, walikuwa na fadhila ambazo hakuna mtu mwingine yeyote alikuwa nazo. Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema katika Hadithi: "...na ni nini kitakachokujulisha, labda Mwenyezi Mungu tayari ameshawaangalia wapiganaji wa Badri na akasema: Fanyeni mtakavyo, kwa maana nimeshakusameheeni." (Imepokelewa na Bukhari 3007, Muslim 2494, Abu Daud 2650, na Tirmidhi 3305).
Imesimuliwa kutoka kwa Mu'adh bin Rifa'a Az-Zuraki kutoka kwa babake - ambaye alikuwa mmoja wa wapiganaji wa (vita vya) Badri - kuwa: Jibril alimjia Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Mnawaonaje wapiganaji wa (vita vya) Badri miongoni mwenu?" Mtume rehema na amani ziwe juu yake akasema: "Ni miongoni mwa wabora zaidi kuliko wote." au alisema maneno kama hayo. Basi, Jibril akasema: "Na vilevile wale walioshiriki miongoni mwa Malaika katika (vita vya) Badri". (Imepokelewa na Bukhari 3992).
Na tunashuhudia yale aliyoyashuhudia Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake kwa watu wa kiapo cha utii cha Ar-Ridhwan; ambapo Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: “Hataingia Motoni yeyote miongoni mwa wale waliotoa ahadi ya utiifu (kwa Mtume) chini ya Mti.” (Imepokelewa na Abuu Daud 4653, Tirmidhi 3860, Abu Al-Jahm katika Juz-u 1, Ahmad (14778, na An-Nasai katika Al-Kubra 11444). Na kwamba walifuzu kwa sababu ya kiapo chao hiki, mpaka Mwenyezi Mungu akasema juu yao: "Bila ya shaka wale wanaofungamana nawe, kwa hakika wanafungamana na Mwenyezi Mungu. Mkono wa Mwenyezi Mungu uko juu ya mikono yao." [Al-Fath: 10]. Na tunajua kwamba Mwenyezi Mungu amewaridhia, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Aliyetakasika katika Qur'ani yake : "Kwa hakika Mwenyezi Mungu amewapa radhi Waumini walipofungamana nawe chini ya mti, na alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao, na akawalipa kwa Ushindi wa karibu." [Al-Fath: 18].
Na tunaamini kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu alie juu ameipa fadhila familia ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake na haki maalumu, kwa hivyo ni lazima kuwapenda, kuwafanya vipenzi na kutekeleza haki zao. Miongoni mwa haki zao ni kuwa Mwenyezi Mungu amewapa haki ya moja ya tano (ya ngawira), na ya Fay' (mali wanayopata waislamu bila ya kupigana vita), na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, aliamrisha waombewe na pia aombewe yeye, akasema rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Semeni: Ewe Mwenyezi Mungu, mswalie Muhammad na ali za Muhammad, kama ulivyowaswalia ali za Ibrahimu. Hakika wewe ni Msifiwa, Mtukufu. Na mbariki Muhammad na ali za Muhammad kama ulivyowabariki ali za Ibrahim. Hakika wewe ni Msifiwa, Mtukufu.
Na miongoni mwa fadhila zao ni yale aliyoyataja Mwenyezi Mungu mwenye sifa tukufu katika kauli yake: "Enyi wake wa Nabii! Nyinyi si kama yeyote katika wanawake wengine. Kama mnamcha Mungu basi msilegeze sauti zenu, akaingia tamaa mwenye maradhi katika moyo wake. Na semeni maneno mema * Na kaeni majumbani kwenu, wala msionyeshe mapambo yenu kwa walivyokuwa wakionyesha mapambo yao zama za kizamani. Na shikeni Swala, na toeni Zaka, na mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Hakika Mwenyezi Mungu anataka kukuondoleeni uchafu, enyi Watu wa Nyumba ya Mtume, na kukusafisheni barabara." [Al-Ahzab: 32, 33]. Na amesema Mtukufu: "Nabii ni bora zaidi kwa Waumini kuliko nafsi zao. Na wake zake ni mama zao." [Al-Ahzab: 6].
Imesimuliwa kutoka kwa Aisha Mwenyezi Mungu amridhie kwamba alisema: Mtume rehema na amani ziwe juu yake alitoka asubuhi moja hali ya kuwa amevaa shuka la manyoya lenye mistari mieusi, kisha akaja Hasan bin Ali akamuingiza (ndani yake). Kisha Husain akaja naye akamuingiza (ndani yake). Kisha, Fatima akaja, na akamuingiza (ndani yake). Kisha, Ali akaja, akamuingiza (ndani yake). Kisha, akasoma: “Hakika, Mwenyezi Mungu anataka tu akuondoleeni uchafu, enyi Watu wa Nyumba ya Mtume, na akusafisheni barabara." (Imepokelewa na Muslim 2424).
Na imesimuliwa kutoka kwa Wathila bin Al-Asqai’ Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kuwa alisema: Nilimsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake akisema: “Hakika Mwenyezi Mungu alimteuwa Kinana katika kizazi cha Ismail, na akawateuwa Makuraishi kutoka kwa Kinana, na akawateuwa Banu Hashim kutoka kwa Makuraishi, na akanichagua mimi kutoka kwa Banu Hashim." (Imepokelewa na Muslim 2276).
Na imesimuliwa kutoka kwa Zaid bin Ar-Qam, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kuwa alisema: Siku moja, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisimama miongoni mwetu akihutubu mahali penye maji paitwapo Khumm, kati ya Makka na Madina. Alimhimidi Mwenyezi Mungu, akamsifu, akawaidhi na akakumbusha. Kisha, akasema: "Ama baada ya hayo, sikilizeni! Enyi watu! Hakika, mimi ni mwanadamu tu, na anakaribia mjumbe Mola wangu Mlezi kunijia na nikamuitikia (yani Malaika wa kifo). Nami nimeacha kati yenu (vitu) vizito viwili. Cha kwanza kati ya hivyo viwili ni Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Ndani yake kuna uongofu na nuru. Kwa hivyo, kichukueni Kitabu cha Mwenyezi Mungu na mshikamane nacho." Kisha, akahimiza kuhusiana na (kukishikilia) Kitabu cha Mwenyezi Mungu na akalihimiza hilo. Kisha, akasema: "Na watu wa nyumba yangu. Ninawakumbusha kwa Mwenyezi Mungu kuhusu watu wa nyumba yangu. Ninawakumbusha kwa Mwenyezi Mungu kuhusu watu wa nyumba yangu. Ninawakumbusha kwa Mwenyezi Mungu kuhusu watu wa nyumba yangu." (Imepokelewa na Muslim 2408).
Na Maswahaba wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, waliwapa jamaa wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, haki zao na fadhila zao, kiasi kwamba Abubakari Mwenyezi Mungu amuwiye radhi akamwambia Ali, Mwenyezi Mungu awe radhi naye: "Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu iko katika mkono wake! Hakika, kuunga jamaa za Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, ni pendwa zaidi kwangu kuliko kuunga jamaa zangu." (Imepokelewa na Bukhari 3508, na Muslim 1759).
Na alikataza Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuwalaani Maswahaba wake, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, akasema: "Msiwatukane Maswahaba wangu, kwa sababu, lau kama yeyote kati yenu atatoa dhahabu sawa na (mlima) Uhud (katika njia ya Mwenyezi Mungu), basi haiwezi kuwa sawa na theluthi mbili ya kilo ya mmoja wao wala nusu yake." (Imepokelewa na Bukhari 3673, Muslim 2541, Abu Daud 4658, na Tirmidhi 3861). Na alibainisha Mtume mtukufu rehema na amani ziwe juu yake, kuwa kuwapenda Answari ni alama ya imani, na kuwachukia ni alama ya unafiki. Amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Alama ya imani ni kuwapenda Answari, na alama ya unafiki ni kuwachukia Answari." (Imepokelewa na Bukhari 17, Muslim 74, na An-Nasai 5019).
Na amesema Sa'id bin Zaid bin 'Amr bin Nufail, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi : “Mmoja wao kuwa tu pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, ukafunikwa uso wake kwa mavumbi wakati huo, ni bora kuliko matendo ya mmoja wenu ya maisha yake yote, hata kama atapewa muda wa maisha ya Nuhu.” (Imepokelewa na Abuu Daud 4650).
Mlango wa ulazima wa kuwatii wenye mamlaka
Tunajua kuwa ni wajibu kuwasikiliza na kuwatii watawala wa Waislamu, kwa sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi mlioamini! Mtiini Mwenyezi Mungu, na mtiini Mtume na wenye madaraka katika nyinyi." [An-Nisaa: 59] Na kwa mujibu wa maneno ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Ni lazima kwa mtu kusikiliza na kutii (maagizo ya kiongozi) maadamu hakuamurishwa kufanya maasi. Lakini ikiwa ataamrishwa kufanya maasi, basi kamwe hapaswi kusikiliza wala kutii." (Imepokelewa na Bukhari 2955, na Muslim 1839).
Na katika Sahihi mbili, kutoka kwa Ubada bin As-Swamit, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, alisema: "Tulimpa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, ahadi ya utii juu ya kusikiliza na kutii katika wakati mwepesi na wakati mgumu, na wakati tunapokuwa na nguvu na wakati tunapokuwa tumechoka, na kuwapendelea viongozi wetu kuliko sisi, na kuwa tusipigane dhidi yao juu ya jambo lao hili (la uongozi), na kwamba tuseme haki popote tutakapokuwa, wala tusiogope lawama ya mwenye kulaumu, kwa ajili ya Mwenyezi Mungu." (Imepokelewa na Bukhari 7055, na Muslim 1709).
Amesema Abuu Zur'a Mwenyezi Mungu amrehemu: “... na tunapaswa kutekeleza faradhi ya jihadi na Hija pamoja na maimamu wa Waislamu katika kila zama na nyakati, na wala hatuungi mkono suala la kupigana dhidi ya maimamu au kupigana katika nyakati za fitina, na tunawasikiliza na kuwatii wale ambao Mwenyezi Mungu Mtukufu amewapa mamlaka juu yetu, wala hatufai kutowatii hata kidogo, na kuwa ni lazima tufuate Sunna na mwenendo wa Maswahaba wa Mtume". (Sharh usul I'tikad Ahlis-Sunna wal-Jama, cha Imam Lalakaii, 1/175).
Kuwatii watawala ni wajibu katika mambo mema tu na ni haramu katika maasi, kwa mujibu wa maneno ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake - kama ilivyo katika hadithi iliyotangulia ya Ibn Omari Mwenyezi Mungu amuwiye radhi: "...maadamu hakuamrishwa kufanya maasi. Lakini ikiwa ataamrishwa kufanya maasi, basi kamwe hapaswi kusikiliza wala kutii." Na maneno yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakuna utii wowote katika maasi. Utii unakuwa tu katika (mambo) mema." (Imepokelewa na Bukhari 7257, na Muslim 1840).
Amesema Imam Abu Ibrahim Al-Muzani: “Na kuwatii wenye mamlaka kunakuwa tu katika yale yanayomridhisha Mwenyezi Mungu, na kujiepusha na yale yanayomchukiza Mwenyezi Mungu, na kuacha kupigana nao wanapofanya dhuluma na ukandamizaji, na kutubia kwa Mwenyezi Mungu, ili awafanye wawe wapole kwa wale walio chini ya uchungaji wao." (Saharhu Sunna, cha Al-Muzani, uk. 84).
Hitimisho
Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, ambaye kwa neema yake matendo mema yanatimia, na tunamtakia rehema na amani yule aliyetumwa kuwa rehema kwa walimwengu wote, na tunamshukuru Mola Mtukufu kwa yale aliyotuneemesha kwayo ya kukamilisha kitabu hiki kikubwa na chenye baraka, na tunasema kama watakavyosema watu wa peponi: "Alhamdulillahi Rabbil A'lamiin (Kuhimidiwa kote ni kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote)." [Yunus: 10]. Na kama alivyotuamrisha Mola wetu Mlezi, Mtukufu: "Sema: Alhamdu Lillahi (kuhimidiwa ni kwa Mwenyezi Mungu)! Na amani ishuke juu ya waja wake aliowateuwa. Je, Mwenyezi Mungu ni bora, au wale wanaowashirikisha naye?" [An-Naml: 59].
Na tunamuomba aifanye kazi hii kuwa imekusudiwa radhi zake Mtukufu tu, iwe inaafikiana na muongozo wa bwana wa Mitume rehema na amani ziwe juu yake, yenye manufaa kwa waja wake, yenye kutufanyia uombezi siku tutakayokutana Naye.
Na tunajua kuwa hata tukijitahidi kiasi gani, hatuwezi kudhibiti kikamilifu mada hii tukufu. Hilo ni kwa sababu ni mazungumzo juu ya Mwenyezi Mungu, Malaika wake, Vitabu vyake, Mitume wake, Siku ya Mwisho, na mipango ya Mwenyezi Mungu na kadari yake, lakini tunakihitimisha kitabu hiki kwa maneno yake Mola wa Haki, Mwenye mamlaka matukufu: "Na wala hawakumheshimu Mwenyezi Mungu haki ya kumheshimu. Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kiume. Sub-hanahu wa Taa'la (ametakasika na ametukuka) mbali na hayo wanayomshirikisha nayo." [Az-Zumar: 67].