الوسائل المفيدة للحياة السعيدة
كتاب "الوسائل المفيدة للحياة السعيدة" للشيخ عبد الرحمن بن ناصر السعدي، يتناول مفهوم السعادة الحقيقية التي يسعى لتحقيقها كل إنسان. الكتاب يوضح أن السعادة تتحقق بطاعة الله ورسوله، والعمل الصالح، والإيمان. ويُقسم السعادة إلى دنيوية مؤقتة وأخروية دائمة، ويربط بينهما بالرضا الإلهي للمؤمنين. يعتمد الكتاب على الأدلة الشرعية من القرآن والسنة لتقديم الأسباب المؤدية للسعادة وكيفية تحقيقها، مما يجعله دليلاً للمسلمين لتنظيم حياتهم على بصيرة وإيمان.
Njia zenye Faida kwa Maisha yenye Furaha
Mtunzi
Sheikh Abdur-Rahman bin Naasir As-Sa'adiy (Mwenyezi Mungu amrehemu)
Utangulizi
Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, ambaye sifa njema zote ni zake, na ninashuhudia kwamba hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu peke yake, asiye na mshirika, na ninashuhudia kwamba Muhammad ni mja wake na Mtume wake, na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na juu ya jamaa zake na Maswahaba wake.
Ama baada ya hayo: Kwa hakika Raha ya moyo, utulivu wake, furaha yake na kuondoka kwa msongo wa mawazo na huzuni, ndicho kitu ambacho kila mtu anakitafuta, na kwa hayo yanapatikana maisha mazuri, na inatimia furaha na bashasha kubwa. Hayo yana sababu za kidini, za kiasili, na za kimatendo. Hata hivyo, hayo yote hayawezi kukusanyika pamoja isipokuwa kwa Muumini. Ama kwa wengine wasiokuwa Waumini, ingawa wanaweza kupata baadhi yake kwa njia na sababu fulani, akili zao zinahusika katika hilo, bado wanakosa njia bora, thabiti, na nzuri zaidi kwa hali na matokeo mazuri.
Lakini nitataja katika makala hii kile nitakachokumbuka miongoni mwa sababu za hitajio hili la hali ya juu, hitajio ambalo kila mmoja analipupia.
Miongoni mwao, kuna ambao walifanikiwa katika mengi ya hayo, wakawa na maisha mazuri, wakaishi maisha yenye furaha. Na miongoni mwao, kuna ambao walishindwa kabisa, wakawa na maisha ya mahangaiko na taabu. Na miongoni mwao kuna wale walio katikati, kulingana na kile walichoweza kufanikisha. Na Mwenyezi Mungu ndiye Muwezeshaji, naye ndiye anayeombwa msaada wa kufikia kila heri na katika kuzuia kila shari.
Sehemu: Imani na matendo mema
Na sababu kubwa zaidi na msingi wa hilo ni kuwa na imani na kutenda mema. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenye kutenda mema, mwanamume au mwanamke, naye akawa ni Muumini, tutamhuisha maisha mema; na tutawapa ujira wao kwa bora ya waliyo kuwa wakiyatenda." [An Nahli: 97].
Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwapa habari na akawaahidi wale waliojumuisha imani na matendo mema kwamba watakuwa na maisha mema hapa duniani, na malipo mema katika nyumba hii na katika nyumba ya maisha ya milele.
Sababu yake iko wazi: Kwani wale wanaomwamini Mwenyezi Mungu imani iliyo sahihi, inayozalisha matendo mema yanayoboresha nyoyo na tabia, dunia na akhera, wanayo misingi ambayo wanapokea kwayo sababu zote za furaha na shangwe zinazowajia, na sababu za wasiwasi, majuto na huzuni.
Wanapokea mambo ya kupendeza na ya kufurahisha kwa kuyakubali, na kushukuru, na kuyatumia katika mambo yenye manufaa. Kwa hivyo wanapoyatumia kwa njia hii, yanawafanya kupata - kwa sababu ya kuyafurahia, na tamaa ya kudumu kwake na baraka zake, na kutarajia malipo ya wenye kushukuru - mambo makuu yanayozidi kwa mema yake na baraka zake mambo haya ya kufurahisha ambayo hayo ndiyo matokeo yake.
Na wanapopatana na shida, madhara, huzuni na majonzi, wanakabiliana na yale wanayoweza kukabiliana nayo, na kupunguza yale wanayoweza kupunguza, na kuwa na subira nzuri kwa yale wasioweza kuepuka. Kwa njia hii, wanapata matokeo mazuri kutokana na kukabiliana na shida, majaribio, na nguvu, na kutokana na subira na kutarajia malipo na thawabu, mambo makuu yanayofuta shida, na hufuatwa na furaha, matarajio mema, na matumaini katika neema ya Mwenyezi Mungu na malipo yake, kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika Hadithi sahihi: "Ni ajabu iliyoje ya jambo la Muumini. Hakika jambo lake lote ni heri. Akipatwa na jambo lenye kufurahisha, anashukuru na hilo linakuwa ni heri kwake. Na akipatwa na madhara, anasubiri na hilo linakuwa ni heri kwake. Na hayo hayamtokei yeyote ila Muumini." Imepokelewa na Imamu Muslim.
Kwa hivyo, Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akajulisha kwamba Muumini, kushinda kwake, heri yake na matunda ya matendo yake yanazidishwa katika kila kinachompata cha kufurahisha na cha kuchukiza. Ndiyo maana unakuta watu wawili wamefikwa na jambo la heri au ubaya, na wanatofautiana sana katika kulipokea kwao, na hilo ni kulingana na tofauti zao katika imani na matendo mema. Huyu ambaye ameelezewa kwa sifa hizi mbili anapokea kheri na shari kwa yale tuliyosema ya shukrani na uvumilivu na yale yanayofuata hayo. Hivyo atapata furaha na shangwe, kuondoka kwa huzuni na uchungu, wasiwasi, ugumu wa moyo, na uchungu wa maisha, na maisha yake yatakuwa mazuri hapa duniani. Naye huyo mwingine, hupokea neema kwa uovu mkubwa, kiburi na dhuluma. Kwa hivyo, maadili yake yanapotoka na anaupokea kama vile wanyama wanavyoupokea kwa uchoyo na hofu, na bado moyo wake hauna amani. Bali umetawanyika katika pande mbalimbali. Umetawanywa katika upande wa hofu yake juu ya kutoweka kwa vitu avipendavyo, na kwa sababu ya upinzani mwingi ambao mara nyingi hujitokeza kutokana nayo, na kwa upande wa kwamba nafsi hazisimami kwenye kikomo fulani, bali hubakia kuwa na shauku ya mambo mengine, ambayo yanaweza kutokea au yasitokee. Ikiwa yatatokea inavyotarajiwa na kukadiriwa, basi hilo pia ni wasiwasi tu kutokea zile pande zilizotajwa. Na hupokea matatizo kwa wasiwasi, hofu, na kulalamika. Kwa hivyo usiulize juu ya kile kinachompata cha maisha ya taabu, magonjwa ya akili na mishipa ya fahamu, na hofu ambayo inaweza kumpelekea kwenye hali mbaya zaidi, na mambo mabaya zaidi ya kumsumbua, kwa sababu hatarajii malipo yoyote, wala hana subira inayoweza kumfariji au kumrahisishia mambo hayo.
Yote haya yameshuhudiwa kwa uzoefu. Na mfano mmoja wa aina hii, ukiutafakari na kuutumia kwa hali za watu, utaona tofauti kubwa kati ya Muumini anayefanya matendo kwa mujibu wa imani yake, na yule asiyekuwa hivyo. Hilo ni kwa sababu dini inahimiza sana kutosheka na riziki ya Mwenyezi Mungu, na yale aliyowapa waja wake kutokana na fadhila na ukarimu wake mbalimbali.
Muumini anapojaribiwa na maradhi, ufukara au matatizo mengine miongoni mwa mambo ambayo yanampata kila mtu, basi yeye - kwa imani yake na kwa alicho nacho cha kutosheka na kuridhia kile ambacho Mwenyezi Mungu alichomgawia - anakuwa mwenye macho yaliyotulia, na hatafuti moyoni mwake jambo ambalo hakupangiwa, na anawatazama wale walio chini yake, wala hawatazami wale walio juu yake, na hata pengine furaha yake na bashasha yake inaweza kuzidi yule ambaye alipata mahitaji yote ya kidunia, iwapo hawajapata kuridhika na hali yao.
Pia utamkuta yule asiyetenda kulingana na imani, akijaribiwa na umasikini, au kupoteza baadhi ya matamanio ya kidunia, utamkuta akiwa katika hali ya huzuni na taabu kubwa.
Mfano mwengine ni kwamba zikitokea sababu za hofu, na mtu akapatwa na misukosuko, utamkuta mwenye imani thabiti ana moyo thabiti, nafsi iliyotulia, mwenye uwezo wa kulisimamia na kulielekeza jambo hili lililompata kwa yale aliyo nayo na uwezo juu yake kama vile kufikiria, kuzungumza na kutenda. Yeye tayari alishajizoesha masumbuko haya yanayomsumbua. Kwa hivyo, hali hizi humtuliza mtu na kuuimarisha moyo wake.
Pia utamkuta yule ambaye hana imani akiwa katika hali iliyo kinyume na hiyo. Anapopatwa na hofu, dhamiri yake inasumbuka sana kwa sababu yake, mishipa yake inakuwa na wasiwasi mwingi, mawazo yake yanatawanyika, na anahisi hofu ya nje na wasiwasi wa ndani ambao hawezi kuelezewa ilivyo hasa. Watu wa aina hii, ikiwa baadhi ya sababu za kiasili haziwatokei ambazo zinahitaji mazoezi mengi, nguvu zao zinaanguka na mishipa yao inakuwa na wasiwasi, kwa sababu hana imani ambayo husababisha subira haswa katika hali ngumu na hali ya kuhuzunisha na kusumbua.
Mtu mwema na mtu muovu, Muumini na kafiri, wanashiriki katika kupata ujasiri kwa njia ya kujifunza, na katika silika ambayo hupunguza na kurahisisha hofu. Hata hivyo, Muumini ni tofauti kwa nguvu ya imani yake, subira, kumuamini Mwenyezi Mungu na kumtegemea na kutaraji malipo yake - mambo ambayo yanamzidishia ujasiri, yanampunguzia makali ya hofu, na yanamsahilishia matatizo, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ikiwa mnaumia, basi nao pia wanaumia kama mnavyoumia nyinyi. Nanyi mnataraji kwa Mwenyezi Mungu wasioyataraji wao." [An Nisaai: 104]. Pia wanapata msaada maalumu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, usaidizi wa kipekee unaoondoa hofu zao. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na subirini. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wanaosubiri." [Al-Anfaal: 46].
Kuwafanyia wema viumbe kwa kauli na kwa vitendo. Na miongoni mwa sababu zinazoondoa huzuni, dhiki, na wasiwasi ni kuwatendea mema viumbe kwa kauli na vitendo, na aina zote za wema. Yote haya ni heri na wema. Na kwa kupitia hayo, Mwenyezi Mungu huondoa wasiwasi na dhiki (huzuni) kwa watu wema na watu waovu kulingana na kiwango cha wema wao. Lakini Muumini ana sehemu na fungu kamili zaidi katika hayo, naye ni tofauti kwa kuwa matendo yake mema yanatokana na kumkusudia Mwenyezi Mungu pekee na kutaraji malipo yake.
Hivyo basi, Mwenyezi Mungu humrahisishia kufanya mambo mema kwa sababu ya kheri anayotarajia, na humzuilia machukizo (matatizo) kwa sababu ya kukusudia kwake Mwenyezi Mungu pekee, na wema wake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakuna kheri katika mengi ya wanayoshauriana kwa siri, isipokuwa kwa yule anayeamrisha kutoa sadaka, au kutenda mema, au kupatanisha baina ya watu. Na mwenye kufanya hayo kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, basi tutakujakumpa ujira mkubwa." [An Nisaai: 114].
Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu alitoa habari kwamba mambo haya yote ni kheri kutoka kwa yule ambaye ameyatenda. Na wema huleta wema na huondoa uovu. Na kwamba Muumini anayetarajia malipo kwa Mwenyezi Mungu atapewa ujira mkubwa. Na miongoni mwa malipo hayo makubwa ni kuondolewa wasiwasi, huzuni, dhiki na mengineyo.
Sehemu: Kujishughulisha na matendo au elimu yenye manufaa
Na katika sababu za kuondoa wasiwasi unaotokana na mfadhaiko wa neva na kutetereka kwa neva, na kuushughulisha moyo na mambo yanayochafua ni: kuushughulika na matendo fulani au kujifunza elimu yoyote yenye manufaa. Hili linaupa moyo pumbao ili asiwe na mawazo juu ya jambo lililompa wasiwasi. Labda kwa sababu ya hayo anaweza kusahau sababu zilizomletea wasiwasi na huzuni hiyo, hivyo basi nafsi yake ikawa na furaha na ikazidi kuwa na ukakamavu. Na Muumini na wengineo wanashiriki katika sababu hii. Lakini Muumini anakuwa bora zaidi kwa imani yake, kukusudia kwake Mwenyezi Mungu peke yake na kutaraji malipo kwa sababu ya kujishughulisha kwake na elimu hiyo anayojifunza au anayowafundisha wengine, na kwa sababu ya matendo mema ambayo anayafanya. Ikiwa ni ibada, basi inakuwa ibada. Na kama ni shughuli ya kidunia au desturi fulani, anaiambatanisha na nia njema, na akakusudia kuitumia katika kujisaidia kumtii Mwenyezi Mungu. Ndiyo maana hilo lina athari ya ufanisi sana katika kuondoa wasiwasi, dhiki na huzuni. Ni watu wangapi wamepatwa na wasiwasi na dhiki za mara kwa mara, na akapatwa na magonjwa mbalimbali, basi ikawa dawa yake yenye ufanisi ni kusahau visababu vilivyowafadhaisha na kuwatia wasiwasi, na kujishughulisha na kazi miongoni mwa kazi zao muhimu.
Shughuli anayofanya inapaswa kuwa kitu ambacho nafsi hupata utulivu na kukitamani . Kwani, hilo lina uwezekano mkubwa zaidi wa kusababisha kufikia lengo hili lenye manufaa, na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.
Kuelekeza akili yake yote katika kufanya kazi ya siku ya leo Na katika mambo anayoweza kujizuilia kwayo mifadhaiko na wasiwasi ni kuelekeza akili yake yote katika kufanya kazi ya siku ya leo, na kutojishughulisha kabisa na mambo ya siku zijazo, na kutohuzunika juu ya mambo yaliyopita. Ndiyo maana Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akijikinga kutokana na wasiwasi na huzuni. Kwa sababu kuhuzunika juu ya mambo yaliyopita na ambayo haiwezekani kuyarudisha wala kuyafikia hakusaidii kitu. Na huzuni inayotokana na kuhofu mambo ya siku zijazo huenda ikawa na madhara kwa mtu. Hivyo mja anapaswa kuwa mwana wa siku yake, akikusanya juhudi na bidii yake katika kuboresha siku yake na wakati wake wa sasa. Kwa kukusanya moyo juu ya hili, itasababisha kukamilika kwa matendo, na itamfariji mja kutokana na huzuni na machungu. Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, anapoomba dua au kuuelekeza Umma wake kwenye dua fulani, hapo huwa anahimiza - pamoja na kuomba msaada wa Mwenyezi Mungu na kutaraji fadhila zake - juu ya kuichukulia kwa uzito na kufanya bidii katika kufikia anachokiomba. Na kuacha yale aliyokuwa akiyaomba yaondolewe, kwa sababu dua inafungamana na vitendo. Na mja anapaswa kujitahidi katika mambo yanayomnufaisha katika dini na dunia, na kumuomba Mola wake Mlezi kwamba afikie lengo lake, na atafute msaada wake katika hilo, kama alivyosema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Pupia yenye kukunufaisha, na utake msaada kwa Mwenyezi Mungu, wala usishindwe, na likikusibu jambo usiseme: Lau ningefanya kadha basi ingelikuwa kadha na kadha, lakini sema: Hii ni mipango ya Mwenyezi Mungu naye hufanya alitakalo, maana neno "Lau" linafungua matendo ya Shetani." Imepokelewa na Muslim. Hapa, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akakusanya kati ya amri ya kujitahidi katika mambo yenye manufaa kwa kila hali na kutafuta msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kutojiingiza katika kushindwa, ambako ni kufanya uvivu unaoleta madhara, na baina ya kujisalimisha kwa mambo yaliyopita na kutekelezeka, na kutii mipango ya Mwenyezi Mungu na hatima yake.
Na aligawanya mambo katika sehemu mbili: sehemu ambayo mja anaweza kujitahidi kupata au kupata anachoweza kutoka kwayo, au kuizuia au kuipunguza. Sehemu hii, mja anafaa kuonyesha juhudi yake na kutafuta msaada wa Mola wake Mlezi. Na kuna sehemu ambayo hawezi kufanya hivyo. Sehemu hii, mja anafaa kutulizana, kuridhia na kujisalimisha kwa Mwenyezi Mungu. Hapana shaka kwamba kuzingatia kanuni hii ni sababu ya furaha na kuondoka kwa wasiwasi na huzuni.
Sehemu: Kumtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi
Na katika sababu kubwa za kufunguka kwa moyo na utulivu wake ni kumtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi, kwani hilo lina athari ya ajabu katika kufunguka na utulivu wa moyo, na kuondoka kwa wasiwasi na huzuni yake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Hakika kwa kumkumbuka Mwenyezi Mungu ndio nyoyo hutua! [Ar-Ra'd: 28] Kumtaja Mwenyezi Mungu kuna athari kubwa katika kufikia lengo hili kutokana na sifa zake maalumu, na kwa sababu ya malipo na thawabu zake ambazo mja anazitarajia.
Kuzungumza kuhusu neema za Mwenyezi Mungu zilizo dhahiri na zilizofichika Vile vile, kuzungumzia neema za Mwenyezi Mungu za ndani na za nje. Kuzijua na kuzizungumzia kunachangia Mwenyezi Mungu kuondoa wasiwasi na huzuni, na kunamhimiza mja kushukuru, jambo ambalo ndilo daraja la juu kabisa na tukufu, hata kama mja yuko katika hali ya ufukara, magonjwa, au aina nyingine za misiba. Kwa maana ikiwa atalinganisha neema za Mwenyezi Mungu juu yake - ambazo hazihesabiki - na matatizo yaliyompata, basi matatizo hayo hayataweza kulinganishwa hata kidogo na neema hizo.
Bali Mwenyezi Mungu akimjaribu mja kwa matatizo na balaa, naye akatekeleza wajibu wa subira, kuridhika, na kujisalimisha, basi athari yake inakuwa nyepesi na mzigo wake unakuwa hafifu, na tumaini la mja la kupata malipo yake na thawabu zake na kumwabudu Mwenyezi Mungu kwa kutenda wajibu wa subira na kuridhika humfanya kuhisi vitu vichungu vitamu, na utamu wa malipo yake humfanya asahau uchungu wa subira yake.
Kutazama walio chini yetu Na katika mambo yenye manufaa makubwa zaidi katika hali hii ni kutumia yale aliyoelekeza Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika Hadithi Sahihi pale aliposema: "Watazameni wale walio chini yenu na msiwaangalie wale walio juu yenu. Kwani, kuna uwezekano mkubwa kwamba hamtadharau neema ya Mwenyezi Mungu juu yenu." Imepokelewa na Muslim. Ikiwa mja ataweka maono haya makubwa mbele ya macho yake, utamuona akishinda idadi kubwa ya watu katika kuwa salama na manufaa yanayoambatana na hilo, na katika riziki na yanayoambatana nayo, bila kujali ni kiwango gani hali yake imemfikisha, basi ukaondoka wasiwasi wake na huzuni yake, na furaha na bashasha yake vinazidi kwa sababu ya neema za Mwenyezi Mungu, ambazo aliwazidi kwazo wengine walio chini yake.
Na kila inavyozidi tafakuri ya mja neema za Mwenyezi Mungu za nje na za ndani, za kidini na za kidunia, ndivyo anavyoona zaidi kwamba Mola wake Mlezi amempa heri na kumuepusha na maovu mengi. Na hakuna shaka kwamba hilo linazuia wasiwasi na huzuni, na linaleta furaha na bashasha.
Sehemu: Kujitahidi kuondoa sababu zinazoleta wasiwasi, na kutafuta sababu zinazoleta furaha
Na miongoni mwa sababu ziletazo furaha na kuondoa wasiwasi na huzuni ni kujitahidi kuondoa sababu zinazoleta wasiwasi na kutafuta sababu zinazoleta furaha. Hilo linakuwa kwa kusahau shida zilizopita ambazo hangeweza kuziepuka, na kujua kwamba kuishughulisha akili yake katika hayo ni kazi bure na kitu kisichowezekana, na kwamba huo ni upumbavu na na jambo lisilowezekana. Kwa hivyo na apambane na moyo wake dhidi ya kufikiria juu yake, na pia apambane na moyo wake dhidi ya kuwa na wasiwasi juu ya mambo yajayo, ikiwa ni pamoja na umasikini, hofu au mambo mengineyo miongoni mwa machukizo ambayo anadhani kwamba yatampata katika maisha yake yajayo. Anapaswa kujua kwamba mambo yajayo hayajulikani ni nini kitakachotokea cha heri na shari, matumaini na machungu, na kwamba yamo mikononi mwa Mwenye nguvu, Mwenye hekima. Waja hawana uwezo juu yake isipokuwa kujitahidi kupata heri zake na kuzuia madhara yake. Na mja anapaswa pia kujua kwamba ikiwa atageuza mawazo yake kutoka kwenye wasiwasi wake kwa ajili ya maisha yake yajayo, na kumtegemea Mola wake Mlezi katika kuyafanya yatengenee, na akapata utulivu kwake katika mambo hayo, akifanya hayo moyo wake utatulia, hali zake zitakuwa bora na huzuni wake na wasiwasi utaondoka.
Matumizi ya dua Na miongoni mwa mambo yenye manufaa makubwa zaidi katika kutazama siku zijazo za mambo, ni kutumia dua hii ambayo Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akiomba kwayo: "Ewe Mwenyezi Mungu nirekebishie dini yangu ambayo ndiyo ngome ya jambo langu, na unirekebishie dunia yangu ambayo ndani yake kuna maisha yangu, na unirekebishie Akhera yangu ambayo ndiyo kuna marejeo yangu, na uyafanye maisha kwangu kuwa ni ziada katika kila kheri, na ukifanye kifo kwangu kuwa ni pumziko kutoka kwa kila shari." Imepokelewa na Muslim. Na pia kauli yake: "Ewe Mwenyezi Mungu, rehema zako ndizo ninazozitarajia; basi usiniache kujitegemea mwenyewe kwa kiasi cha mpepeso wa jicho, na unitengenezee vizuri mambo yangu yote. Hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Wewe." Imepokelewa na Abu Daawuud kwa msururu sahihi wa wasimulizi. Hivyo, ikiwa mja atasema dua hii ambayo ina manufaa ya maisha yake ya kijumla ya kidini na ya kidunia kwa moyo thabiti, na nia ya dhati, pamoja na juhudi yake katika kutimiza hayo, Mwenyezi Mungu atamjalia aliyoyaomba na alivyotarajia, na huzuni yake itageuka kuwa furaha na shangwe.
Sehemu: Kukadiria uwezekano mabaya zaidi
Na miongoni mwa sababu zenye manufaa zaidi za kuondoa wasiwasi na huzuni iwapo mja atapatwa na baadhi ya matatizo, ni kujitahidi kuyapunguza kwa kukadiria matokeo mabaya zaidi ambayo jambo hilo linaweza kufikia, na aizoeshe nafsi yake kwa hilo. Akifanya hivyo, basi na ajitahidi kupunguza yale yanayoweza kupunguzwa kiasi inavyowezekana. Kwa kujizoesha huku, na kwa juhudi hii yenye manufaa, utaondoka wasiwasi wake na huzuni yake, na atakuwa amefanya bidii hiyo katika kuleta manufaa na kuzuia madhara ambayo ni rahisi kwa mja.
Kwa hivyo, anapopatwa na sababu za hofu, sababu za maradhi, sababu za umasikini na ukosefu wa vitu mbalimbali anavyopenda, basi na ayapokee hayo kwa utulivu na kujizoesha juu yake. Bali anafaa kufanya hivyo juu ya lililo kali zaidi miongoni mwake. Kwani kuizoesha nafsi kustahimili matatizo, huyafanya yawe rahisi na huondoa ukali wake, haswa ikiwa atajishughulisha na kuyazuia kulingana na uwezo wake. Hapo yatakuwa yamekusanyika kwake kuizoesha nafsi pamoja na kufanya bidii yenye manufaa ambayo itamshughulisha mbali na kujali balaa hizo, na atajitahidi kufanya upya nguvu ya kuzuia balaa hizo, huku akimtegemea Mwenyezi Mungu katika hilo na kuwa na imani nzuri naye. Na hapana shaka kwamba mambo haya yana manufaa makubwa sana katika kuleta furaha na kufunguka kwa nyoyo, pamoja na yale anayoyatarajia mja ya malipo ya sasa na ya baadaye. Hili ni jambo ambalo limeshuhudiwa na kujaribiwa, na matukio yake kwa wale waliolijaribu ni mengi sana.
Sehemu: Nguvu ya moyo, na kutosumbuka kwake na kuathirika
Na miongoni mwa tiba kubwa zaidi ya magonjwa ya moyo ya neva, na hata kwa magonjwa ya kimwili, ni nguvu ya moyo na kutosumbukana, kuathirika na dhana na mawazo yanayoletwa na fikira mbaya. Hasira na kusumbuka ni miongoni mwa sababu zinazoumiza. Na mwenye kutarajia kutokea kwa machukizo na kutoweka kwa mambo anayoyapenda, hilo litamsababishia wasiwasi, huzuni na magonjwa ya kimoyo na ya kimwili, na kuzorota kwa neva, ambako kuna athari zake mbaya, ambazo watu wameshuhudia madhara yake mengi.
Kumtegemea Mwenyezi Mungu Pindi moyo unapomtegemea na kuyakabidhi mambo yake kwa Mwenyezi Mungu, na usijisalimishe kwa mawazo yasiyo ya kweli wala usimilikiwe na fikira mbaya, na ukawa na imani na Mwenyezi Mungu na ukatulizana juu ya fadhila zake, wasiwasi na huzuni wake zitawekwa mbali sana na yeye kwa sababu ya hayo na yatamwondoka maradhi mengi ya kimwili na kimoyo, na moyo wake utapata nguvu, utafunguka na atakuwa na furaha ambayo haiwezi kuelezeka. Je, ni hospitali ngapi zilizojaa wagonjwa wanaoteseka kutokana na msongo wa mawazo na fikira mbovu? Na je, ni wangapi miongoni mwa watu wenye nguvu walioathirika na mambo haya, mbali na watu wanyonge? Na ni mara ngapi mambo haya yemesababisha upumbavu na wazimu? Basi aliye salama ni yule ambaye Mwenyezi Mungu amempa salama, na akamuwezesha kupambana na nafsi yake ili kupata visababu vyenye manufaa, vya kuuimarisha moyo, vya kuzuia wasiwasi wake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu, basi Yeye humtosha." [Attwalaaq: 3] Yaani, atamtosheleza katika mambo yote ya dini yake na dunia yake yanayompa wasiwasi.
Anayemtegemea Mwenyezi Mungu ana moyo wenye nguvu, haathiriwi na mawazo yasiyo ya kweli, na hasumbuliwi na matukio, kwa sababu anajua kwamba hili ni katika udhaifu wa nafsi, na ni katika udhaifu na hofu ambayo haina uhakika, na anajua kwamba Mwenyezi Mungu amemdhaminia utoshelevu kamili yule anayemtegemea. Kwa hivyo anakuwa na imani na Mwenyezi Mungu na anatulizana juu ya ahadi yake, kwa hivyo unaisha huzuni wake na wasiwasi wake, kisha ugumu wake huo unabadilika kuwa wepesi, na huzuni wake unakuwa furaha, na hofu yake inakuwa amani. Kwa hivyo, tunamuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu salama, na atujaalie kutokana na fadhila zake, nguvu na uthabiti wa moyo, na kumtegemea kikamilifu ambako Mwenyezi Mungu amewahakikishia watu wake kwamba watapata kila heri, na wataepushwa kila machukizo na madhara.
Sehemu: Kuizoesha nafsi kustahimili aibu za watu wengine
Na katika kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Asichukie Muumini wa kiume tabia za Muumini wa kike. Akichukia tabia fulani, basi ataridhishwa na tabia nyingine." Imepokelewa na Muslim.
Kuna faida mbili kuu:
Faida ya kwanza: Mwongozo wa jinsi ya kuamiliana na mke, jamaa, rafiki, na mfanyakazi na kila mtu ambaye una uhusiano na mawasiliano naye, na kwamba unapaswa kuwa umetayarisha nafsi yako kwamba lazima atakuwa na kasoro au upungufu au kitu unachokichukia. Kwa hivyo, ukipata hicho, basi linganisha hiki na kile kinachotakiwa kwako au unachopaswa kufanya cha kuwa na mawasiliano ya nguvu na kudumisha upendo, kwa kukumbuka mazuri yake, na madhumuni mahususi na ya ujumla. Basi kwa kupuuza makosa hayo na kutambua mazuri yao, unadumu usuhuba na mawasiliano, na utapata utulivu na faraja.
Faida ya pili: Ni kuondoka kwa huzuni na wasiwasi, kubaki kwa upole, na kuendelea kutekeleza haki za lazima zilizopendekezwa, na kupatikana kwa faraja baina ya hizi pande mbili. Kwa hivyo, asiyechukua mwongozo huu alioutaja Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, badala yake akageuza jambo hili na akaangalia mabaya tu, na akapuuza mazuri, basi lazima atakuwa na wasiwasi, na lazima kutakuwa na mahusiano mabaya kati yake na mtu aliyekuwa ameunganishwa naye kwa upendo, na kutakuwa na kukatwa kwa haki nyingi ambazo kila mmoja wao anapaswa kuzihifadhi.
Na watu wengi wenye ari ya juu hujiandaa kiakili wakati wa majanga na shida kwa subira na utulivu. Lakini wakati wa mambo madogo na yasiyokuwa na maana, wanahisi wasiwasi, na furaha yao inakuwa na dhiki. Sababu ya hili ni kwamba walijizatiti mbele ya mambo makubwa, lakini walijisahau kwenye mambo madogo, na hivyo ikawaathiri na kuathiri faraja yao. Mtu mwenye busara hujiandaa kwa mambo yote, makubwa na madogo, na anamuomba Mwenyezi Mungu msaada juu yake, na kwamba asimwache peke yake hata kwa sekunde moja. Hivi ndivyo atakavyoweza kukabiliana na mambo madogo kwa urahisi, kama vile alivyoweza kushughulikia mambo makubwa. Kwa hivyo, anabaki akiwa ana utulivu wa nafsi, utulivu wa moyo na kuhisi faraja.
Sehemu: Kuacha kuendeleza mahangaiko
Mwenye busara anajua kuwa maisha yake bora ni maisha ya furaha na utulivu, na kwamba ni mafupi sana, basi hafai kuyafupisha kwa wasiwasi na kujitosa kwenye mahangaiko, kwani hiyo ni kinyume na maisha sahihi. Kwa hivyo, anajiweka mbali na maisha yake ili asikubali sehemu kubwa yake itumike na mawazo mabaya na huzuni. Katika hili, hakuna tofauti kati ya mtu mwema na muovu, lakini Muumini anasifika zaidi na sifa hii na ana fungu na sehemu kubwa zaidi yenye manufaa ya sasa na ya baadaye katika hilo.
Kulinganisha baina ya neema za Mwenyezi Mungu na yale yanayochukiwa yaliyompata Pia inafaa anapopatwa na msiba au ikiwa atauhofu, basi na alinganishe kati ya neema alizo nazo, ziwe ni za kidini au za kidunia, na kati ya msiba uliompata. Akilinganisha, zitakuwa wazi neema alizo ndani yake na utapotelea mbali msiba uliompata.
Vile vile, alinganishe kati ya madhara anayoyahofu kumtokea na uwezekano mwingi wa kuwa salama kutokana nayo. Hapo asiache uwezekano dhaifu kushinda uwezekano mwingi wenye nguvu, na utaondoka wasiwasi wake na hofu yake kwa ajili ya hilo. Na anafaa kukadiria uwezekano mkubwa zaidi unaoweza kumpata. Hali hiyo humuwezesha kujiandaa kwa ajili ya kitakachotokea, na pia hutafuta kuzuia kile kisichotokea na kuboresha au kupunguza kile kilichotokea.
Maudhi ya watu ni juu yao wenyewe ilimradi usijishughulishe nayo Na miongoni mwa mambo yanayofaa ni kujua kwamba madhara yatokanayo na watu kwako, hasa kwa maneno mabaya, hayakudhuru bali yanawadhuru wao wenyewe, isipokuwa ikiwa utajishughulisha nayo na kuyaruhusu yazimiliki hisia zako. Hapo ndipo yatakavyokudhuru kama yalivyowadhuru wao. Lakini ikiwa hutashughulika nayo, basi hayatakudhuru chochote.
Fanya maisha yako kuwa mazuri kwa fikira zenye manufaa Jua ya kwamba maisha yako yanategemea fikira zako. Ikiwa ni fikira zenye manufaa kwako katika dini au katika dunia hii, basi maisha yako yatakuwa mazuri na yenye furaha. Vinginevyo, basi yatakuwa kinyume chake.
Iwe muamala ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wala si kwa ajili ya viumbe Na miongoni mwa mambo yenye manufaa zaidi katika kuondoa wasiwasi, ni kujizoesha kutotafuta shukrani isipokuwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kwa hivyo, ukimfanyia wema mtu ambaye ana haki juu yako au asiyekuwa na haki juu yako, jua ya kwamba hapo unaamiliana na Mwenyezi Mungu. Basi usijali kuhusu shukrani za wale uliowafanyia wema, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu viumbe wake maalumu: "Hakika sisi tunakulisheni kwa sababu ya kutaka radhi za Mwenyezi Mungu. Hatutaki kwenu malipo wala shukrani." [Al Insan: 9].
Hili linasisitizwa zaidi katika kuamiliana na mke, watoto wako, na kwa sababu ya nguvu ya uhusiano wako nao. Kwa hivyo, pindi unapojizoesha kuwaondolea ubaya, basi utakuwa umeshajipumzisha. Miongoni mwa vyanzo vya utulivu ni kuchukua fadhila na kuzitekeleza kulingana na hamu ya ndani, bila kujilazimisha kwa jambo linalokusumbua, kwani hivyo unaweza kurudi nyuma ukiwa umeshindwa kupata fadhila, baada ya kuchukua njia ndefu isiyokuwa na manufaa. Hilo ni hekima. Pia unafaa kuchukua mambo safi na matamu kutoka kwa mambo mabaya, na kwa hilo utazidi usafi wa kidhati, na yataondoka mambo machafu.
Kujishughulisha na mambo yenye manufaa, pasi na mambo yenye madhara Weka mambo ya manufaa mbele ya macho yako na fanya juhudi kuyafikia, wala usiyageukie mambo ya madhara ili kujifurahisha nayo mbali na sababu zinazosababisha wasiwasi na huzuni. Tumia utulivu na umoja wa nafsi katika kutekeleza kazi muhimu.
Kufanya na kumaliza matendo ya sasa Miongoni mwa mambo ya manufaa ni kumaliza kazi kwa wakati, na kujitolea kwa kazi zijazo. Hii ni kwa sababu kazi ambazo hazikamiliki hujikusanya na kazi zingine zilizopita, na kuongezeka kwa kazi zijazo, na kufanya mzigo kuwa mzito. Lakini ikiwa utamaliza kila kitu kwa wakati, utakutana na kazi zijazo kwa nguvu ya mawazo na nguvu ya kutenda kazi.
Mpangilio wa vipaumbele pamoja na kuomba ushauri Unapaswa kuchagua vitendo vyenye manufaa; muhimu zaidi kisha muhimu zaidi, na upambanue kati ya kile ambacho nafsi yako inakielekea na kile unachotamani sana, kwa sababu kinyume chake husababisha kuchoshwa na huzuni. Tafuta msaada katika hili kwa kufikiri kisahihi na kushauriana. Kwani hatajuta kamwe mwenye kutafuta ushauri. Soma kwa uangalifu kile ambacho unataka kukifanya. Kwa hivyo, ikiwa kina masilahi, na ukakiazimia, basi mtegemee Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wanaomtegemea.
Na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.
Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya bwana wetu Muhammad, na juu ya familia yake na Maswahaba wake.