المختصر في صفة العمرة وأحكامها
MUHTASARI WA NAMNA YA KUFANYA UMRAH NA HUKUMU ZAKE
MUHTASARI WA NAMNA YA KUFANYA UMRAH NA HUKUMU ZAKE
Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na rehema na amani ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad, na watu wake na Maswahaba zake wote.
Ama baada ya hayo:
Hii ni makala fupi juu ya namna ya kufanya Umra, hukumu zake na adabu zake. Tumejitahidi kubainisha ndani yake mengi katika yale anayohitaji mtu anayefanya ‘Umra.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu aifanye iwe kwa ajili ya uso wake mtukufu, na kwamba anufaishe kwayo Waislamu wote.
Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Huduma ya Maudhui za Kiislamu kwa Lugha mbalimbali.
Dibaji
Kwanza: Masharti ya kukubalika kwa ibada
Ibada haikubaliki kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu isipokuwa kwa masharti mawili:
Ikhlasi, ambayo ni kutafuta radhi na thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu na nyumba ya Akhera. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu". [1] [Al-Bayyina: 5] Yaani wamuelekee Yeye tu na wamuabudu Yeye tu, na wajiepushe na kila kisichokuwa Yeye. Tafsiri ya As-Sa'adi (uk. 538)
Amesema Mtume, rehehma na amani zimshukie: "Hakika matendo yote huzingatiwa nia, na hakika kila mtu atalipwa kwa lile alilolinuia." [2] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 1, na Muslim, kwa nambari 1907.
Kumfuata Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ndani yake kwa kauli na vitendo. Amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Yeyote atakayezua katika jambo letu hili kitu ambacho hakimo, basi hicho kitakataliwa." Na katika riwaya ya Muslim (1718): "Mwenye kufanya tendo ambalo hatukuliamrisha, basi hilo litakataliwa." [3] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 2697, na Muslim, kwa nambari 1718. [4] Kaipokea Muslim, kwa nambari 1718.
***
Pili: Hukumu ya kujifunza namna ya kufanya Umra na hukumu zake mbalimbali
Mwenye kutaka kumuabudu Mwenyezi Mungu kwa ibada yoyote ile anapaswa kujifunza uongofu wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kuhusiana na ibada hiyo; ili amali yake iwe kwa mujibu wa Sunna. Na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akiwahimiza watu kumfuata na kuongoka kwa muongozo wake. Imesimuliwa kutoka kwa Malik bin Al-Huwairith, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Swalini kama mlivyoniona nikiswali." [5] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 6008.
Na imesimuliwa kutoka kwa Jabiri, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: “Nilimuona Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akirusha vijiwe huku akiwa juu ya kipando chake siku ya kuchinja (siku ya Idi) huku akisema: "Chukueni ibada zenu (za Hija) kutoka kwangu. Kwani mimi sijui, huenda sitahiji baada ya Hija yangu hii." [6] Kaipokea Muslim, kwa nambari 1297.
***
Tatu: Ubora na Fadhila za ibada ya Umra
Umra ina fadhila mbili: Fadhila ya ujumla na fadhila maalumu.
Ama fadhila ya ujumla:
Imesimuliwa kutoka kwa Abu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Kwenda Umra mpaka Umra nyingine kunafanya mtu kusamehewa madhambi yanayofanyika baina ya Umra hizo mbili. Na Hija yenye kukubalika haina malipo isipokuwa Pepo." [7] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 1773, na Muslim, kwa nambari 1349.
Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Masudi, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Fuatisheni baina ya Hija na Umra; kwani viwili hivyo huondoa umasikini na madhambi kama vile kiriba [2] kinavyoondoa uchafu wa chuma, na dhahabu na fedha. Na Hija iliyokubaliwa haina malipo isipokuwa Pepo." Kiriba: Ni mahali pa moto wa mhunzi na mfua dhahabu. Rejea kitabu Attamhiid cha Ibn Abdil-Barr (15/102). [9] [9] Kaipokea At-Tirmidhiy, kwa nambari 810, na An-Nisaii, kwa nambari 2631.
Na fadhila maalumu katika mwezi wa Ramadhani: Imesimuliwa kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, ya kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake alisema: “Umra katika Ramadhani ni sawa na Hija pamoja nami."[3] Yaani, ni sawa na Hija ya pamoja na mimi, kama ilivyoelezwa katika riwaya nyingine.
***
Namna ya kufanya Umra
Kwanza: Hukumu za Mawaaqiit (Vituo vya kuhirimia(Nia) Umra)
Mawaaqiit: Ni sehemu alizozipanga Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ili wahirimie huko wale wanaotaka kuhiji au kufanya Umra.
Kwa hivyo, yeyote anayepita katika mojawapo ya hizo huku akiwa amekusudia kuhiji au kufanya Umra, basi ni lazima ahirimie huko, na wala hataruhusiwa kuzipita bila ya kuhirimia.
Na yeyote aliye karibu na Makka katika wakazi wa vituo hivi, basi kituo chake ni mahali anapoishi. Basi atahirimia papo hapo Hija na Umra.
Ama watu wa Makka na wote wanaokusudia kuhirimia kutokea huko Makka, basi watahirimia Hija kutokea Makka. Na ama wanapofanya Umra, basi watatoka nje ya eneo takatifu, kisha wahirimie huko, kama vile At-Tan’iim na mfano wake.
Na yeyote atakayekuwa ndani ya ndege, yeye atahirimia atakapofika usawa wa Miqat. Hivyo basi, anafaa kujiandaa na kuvaa nguo za ihram kabla ya kufika usawa wa Miqat. Atakapofikia usawa wake, basi papo hapo atahirimia, na wala haruhusiwi kuichelewesha mpaka atakapotua kwenye uwanja wa ndege. Pia anaweza kuchukua hadhari kabla ya kuifika, akafanya Talbiya (kuhirimia) kabla ya kuifikia Miqat kwa kuhofia asijepita mahali pa kuhirimia kwa sababu ya kasi kubwa ya ndege.
Pili: Jinsi ya kuhirimia na hukumu zake:
Anayetaka kuhirimia anaruhusiwa kufanya mambo yafuatayo:
Kuoga. Hili ni sunna iliyosisitizwa kwa wanaume na wanawake, hata wenye hedhi na nifasi (Damu ya uzazi).
Kujipaka manukato yaliyo bora zaidi kichwani na kwenye ndevu zake, sawa sawa yawe ni mafuta ya udi au mengineyo, na haimdhuru ikiwa yatabakia baada ya kuhirimia. Ama wanawake, wao hawaruhusiwi kutumia manukato yenye harufu; ili wanaume wasiokuwa maharimu wao wasiyanuse.
Kuvaa nguo za Ihram, ambazo ni kikoi na shuka. Sunna ni kwamba ziwe nyeupe na safi au mpya. Mwanamke anaweza kuvaa nguo zozote anazotaka bila ya kuonyesha mapambo yake, isipokuwa anapaswa kujiepusha na kuvaa nikabu na glovu, na kufunika uso wake na mikono yake kwa kitu kingine.
Inaruhusiwa kuhirimia baada ya swala, sawa iwe ni swala ya faradhi au ya sunna, lakini si lazima kwamba mtu ahirimie baada ya swala.
Atasema: “Labbaika allahumma umra (Nimekuitikia ewe Mwenyezi Mungu, kwa kufanya Umra)." Na ikiwa anafanya Umra kwa niaba ya mtu mwingine, atasema: “Labbaika allahumma umar 'an fulani (Nimekuitikia, ewe Mwenyezi Mungu, kwa kufanya Umra kwa niaba ya fulani)."
Iwapo mtu anayetaka kuhirimia Umra anahofia kizuizi kitakachomzuia kukamilisha ibada yake, basi na aweke sharti anapoingia katika Ihram, akisema: “Nimekuitikia ewe Mwenyezi Mungu kwa kufanya Umra. Na ikiwa nitazuiliwa na kizuizi chochote, basi mahali pangu pa kutoka katika ihramu ni pale kitakaponizuilia." Basi pindi atakapoweka sharti hili na akapatwa na cha kumzuia kukamilisha ibada yake ya Umra, basi atatoka katika ihramu na wala hakutakuwa na chochote juu yake.
Kisha atarudia kutoa Talbiyah mara kwa mara: (Nimekutikia, Ewe Mola, Nimekuitikia, mimi Nimekuitikia, huna mshirika, Nimekuitikia, sifa na baraka zote ni zako, na utawala, huna mshirika) [4] Mwanamume atainua juu sauti yake kwa hili, na mwanamke pia; Isipokuwa ikiwa mwanamke atakuwa kati ya wanaume wasiokuwa maharimu wake. Mtu huyu aliyehirimia Umra anafaa kurudia Talbiyah mara kwa mara, hasa pale hali na nyakati zinapobadilika, kama vile anapopanda mahali pa juu, au anaposhuka chini, au unapoingia usiku au mchana. Maana ya mtu kusema: “Labbaika” ni nimekutikia ewe Mola Mlezi mara baada ya mara. Hili linamaanisha kwamba mtu amemuitikia Mola wake Mlezi na akadumu katika kumtii. Innalhamda wanni'imata laka walmulk. Tafsiri: Alhamdu ni kumsifu anayesifiwa kwa ukamilifu pamoja na upendo na taadhima. Na anni'imat (neema) ni yale ambayo Mwenyezi Mungu huwapa waja wake kutokana na fadhila zake kwa kuwawezesha kupata kile wanachokitafuta na kuwazuilia wanachokichukia. Na kauli yake 'almulk' inamaanisha kwamba ufalme ni wako. Kwa hivyo Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka ndiye Mwenye kumiliki peke yake. Na kauli yake 'laa shariika lak' inamaanisha kwamba hakuna anayeshiriki nawe katika kile ambacho ni makhsusi kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika sifa zake kamili, ikiwa ni pamoja na upekee wake katika ufalme wake, kuumba, kuendesha mambo na uungu. (Mkusanyo wa Fatwa na makala za Al-'Uthaimiin (22/96)) kwa muhtasari.
Talbiya inaruhusiwa katika Umra kuanzia wakati wa kuhirimia mpaka mtu atakapoanza kuzunguka Al-Ka'aba.
Mtu aliyehirimia Umra analazimika kutahadhari asije akaangukia katika makatazo yoyote ya ihramu mpaka atakapotoka katika ihramu yake.
Tatu: Namna ya kuzunguka Al-Ka'aba
Mtu aliyehirimia Umra atakapoingia kwenye Msikiti Mtukufu, ni sunna kwake autangulize mguu wake wa kulia na aseme dua ya kuingia Msikitini. Miongoni mwa mambo yaliyo sahihi kabisa kuhusiana na hilo ni aseme: “Ewe Mwenyezi Mungu, nifungulie milango ya rehema zako.” Dua hii ataisema wakati wa kuingia msikiti wowote, na sio maalumu kwa Msikiti Mtukufu.
Anapotaka kuanza kuzunguka Al-Ka'aba, atakata Talbiyah, kisha atafanya idhtwibaa. Na namna ya kufanya Idhtwibaa ni kuweka katikati ya shuka yake chini ya kwapa lake la kulia na ncha zake mbili za juu kwenye bega lake la kushoto. Atakapomaliza kuzunguka Al-Ka'aba, atalirudisha shuka lake katika hali yake ya kabla ya kuzunguka Al-Ka'aba. Kwa sababu Idhtwibaa hufanywa katika tawafu peke yake.
Kisha ataliendea Jiwe jeusi na kuligusa kwa mkono wake wa kulia na kulibusu. Ikiwa hataweza kulibusu, ataligusa kwa mkono wake kisha aubusu mkono wake. Na ikiwa hataweza kuligusa kwa mkono wake, ataligusa kwa kitu alichonacho, kama vile fimbo au kitu kama hicho kisha akibusu. Na ikiwa hataweza kufanya hivyo, basi atalielekea Jiwe hilo na aliashirie kwa mkono wake lakini asiubusu. Kilicho bora zaidi ni kwamba asiwaudhi watu kwa kuleta msongamano.
Atakapoligusa Jiwe hilo au kuliashiria, atasema: ""Allahu Akbaru“Mwenyezi Mungu ni Mkubwa.”
Kisha atakwenda upande wa kulia na aiweke Al-Ka'aba upande wake wa kushoto. Atakapoifikia kona ianayoelekea upande wa Yemeni, ataigusa bila kuibusu. Na ikiwa hilo halitawezekana, basi asifanye msongamano hapo wala asiiashirie.
Atasema baina ya kona ya Yemen na Jiwe Jeusi: "Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema, na Akhera mema, na utulinde kutokana na adhabu ya Moto!"
Kila mara atakapolipita lile Jiwe Jeusi, ataliashiria kwa mkono wake na kusema: “Mwenyezi Mungu ni Mkubwa.”
Na mizunguko yake iliyosalia, atasema chochote anachopenda mingoni mwa dhikri, dua na kusoma Qur’ani.
Sunna ni kwamba afanye 'arramal'"kukimbia mtiti" katika mizunguko mitatu ya kwanza peke yake. Arramal ni kutembea kwa kasi lakini kwa hatua fupi fupi. Na ama mizunguko minne iliyosalia, hiyo haina arramal. Atatembea kama kawaida.
Atakapomaliza kuzunguka Al-Ka'aba, ataenda katika Maqam Ibrahim na atasoma: "Na alipokuwa akisimama Ibrahim pafanyeni pawe pa kusalia." [Al-Baqarah: 125] Kisha ataswali rakaa mbili nyuma yake ikiwezekana. Vinginevyo, ataswalia mahala popote pale Msikitini. Katika rakaa ya kwanza baada ya Fatiha atasoma: "Sema: 'Enyi makafiri'". [Al-Kaafiruun: 1] Na katika rakaa ya pili, baada ya Al-Fatihah, atasoma: "Sema: 'Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee". [Al-Ikhlaas: 1]
Nne: Namna ya kufanya sa'yi
Atakapomaliza kuzunguka Al-Ka'aba na akaswali rakaa mbili za baada yake, atatoka aende kwenye Mas’a (mahali pa kufanyia sa'yi), atakapokaribia Safa, atasoma: "Hakika vilima vya Safaa na Marwa ni katika alama za Mwenyezi Mungu". [Al-Baqara: 158] Kisha atasema: “Ninaanza kwa kile ambacho Mwenyezi Mungu alianza kwacho.” "Abda-u bimaa bada-allaahu bihi" Yaani, "Ninaanza kwa kile alichoanza kwacho Mwenyezi Mungu."[12] [12] Kaipokea Muslim, kwa nambari 1218.
Kisha atapanda juu ya Safa mpaka aweze kuiona Al-Ka'aba au muelekeo wake. Atampwekesha Mwenyezi Mungu na kumtukuza kwa kusema: “Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa. Hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu asiye na mshirika. Ufalme ni wake, na sifa njema ni zake, naye ni Muweza wa kila kitu. Hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu peke yake, aliitekeleza ahadi yake, na akamnusuru mja wake, na akayashinda makundi (ya maadui) peke yake." Atayarudia haya mara tatu, na ataomba dua kati yake. "Laa ilaaha illa llaahu wahdahuu laa shariika lahuu, lahul-mulku walahul-hamdu wahuwa alaa kulli shay-in Qadiir. Laa ilaaha illa llaahu, wahdahuu, anjaza wa'dahuu, wanaswara abdahuu, wa hazamal-ahzaaba wahdahuu", Yaani: Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, Yeye pekee asiye na mshirika. Ufalme ni wake, na sifa njema ni zake, naye ni Muweza wa kila kitu. Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, Yeye pekee. Alitimiza ahadi yake, na akamnusuru mja wake, na akayashinda makundi ya maadui peke yake." Kisha ataomba kati ya dua hiyo, na atasema namna hii mara tatu.[13] [13] Kaipokea Muslim, kwa nambari 1218.
Kisha atashuka kutoka Safa na aende hadi Marwa kwa miguu. Atakapoifikia alama (taa) ya rangi ya kijani kibichi, anatembea haraka. Na atakapoifikia alama (taa) ya rangi ya kijani kibichi ya pili, atatembea kama kawaida. Wanawake hawaruhusiwi kuharakisha mwendo katika kutembea wakati wa kufanya sa'yi.
Atakapofika Marwa, anaruhusiwa kufanya yale aliyoyafanya kwenye Safa (tazama kifungu cha 2).
Kisha atashuka kutoka kwenye Marwa kwenda Safa kwa kutembea kwa miguu. Atakapofika kwenye alama ya kijani, atatembea haraka. Na atakapoifikia alama (taa) ya rangi ya kijani kibichi ya pili, atatembea kama kawaida.
Ataendelea hivi hadi amalize mizunguko saba. Kutoka Safa hadi Marwa ni mzunguko mmoja, na kurudi kutoka Marwa hadi Safa ni mzunguko mwingine.
Na atasema katika sa'yi yake chochote anachopenda miongoni mwa dhikri, dua na kusoma Qur'ani.
Tano: Namna ya kunyoa nywele na kuzipunguza:
Mwenye kufanya Umra atakapomaliza kuzunguka Al-Ka'ba na kufanya sa’yi, itamlazimu anyoe kichwa chake au azipunguze ikiwa ni mwanaume. Sunna ni kunyoa au kufupisha kichwa chote.
Kunyoa nywele ni bora kuliko kupunguza, isipokuwa ikiwa wakati wa Hija umekaribia kiasi kwamba hakuna wakati wa kutosha wa kuota nywele za kichwa. Basi kilicho bora ni kuzipunguza tu.
Ama mwanamke, yeye atapunguza kwenye ncha za nywele zake kiasi cha ncha ya kidole au chini ya hivyo.
Makatazo ya Ihram
Makatazo ya Ihram ni:
Kunyoa nywele au kuzipunguza au kuzing'oa kutoka sehemu yoyote ile ya mwili.
Kukata kucha zote au baadhi yake kwenye miguu au mikono.
Kufunika kichwa kwa kitu kinachoshikamana nacho, kama vile kofia, kitambaa na kilemba, au kuweka shuka juu ya kichwa, au kuweka leso za mikononi, blanketi, boksi au kitu kingine chochote kinachoweza kutumika katika kufunika kichwa. Haya ni maalumu kwa wanaume, sio kwa wanawake.
Kuvaa mavazi ya kawaida yaliyoshonwa ili kuvaliwa kwenye mwili mzima, kwa njia ya kawaida, kama vile: Nguo iliyoshonwa, suruali, na shati, na soksi na glovu. Haya ni maalumu kwa wanaume tu, sio kwa wanawake. Ama wanawake, wao wanakatazwa tu:
Kuvaa nikabu, au barakoa, au pazia linalofanana na nikabu, lakini itamlazimu kufunika uso wake mbele ya wanaume wasiokuwa maharimu wake kwa kitu kinachotumika kwa kawaida katika kufunika uso; Hata kama kifuniko hicho kitaugusa uso wake, lakini haruhusiwi kutumia kizuizi au kitu kama hicho kwenye kichwa chake ili kuzuia kifuniko hicho kuugusa uso wake; Kwa sababu hakuna ushahidi wa kuruhusiwa kwa hilo.
Kuvaa glovu mikononi mwake, na itamlazimu kufunika mikono yake mbele ya wanaume wasio maharimu wake kwa kuiweka ndani ya abaya (buibui) yake.
Kujipaka manukato mwilini au katika nguo za ihramu.
Kuua viwindwa vya mwituni, au kuwawinda hata kama hatawauwa.
Kuposa au kumposea mtu mwingine.
Kufunga ndoa.
Kumpapasa mwanamke katika sehemu zisizokuwa tupu; kama vile kumbusu na kumgusa kwa matamanio.
Kujamiiana kwenye uke.
Muhutasari wa matendo ya Umra (uwekwe kwenye jalada au ukurasa wa mwisho)
1. Kuoga.
2- Kutumia manukato.
3. Kuvaa nguo za ihram.
4. Kuhirimia. Nako ni kuweka nia ya kuingia katika ibada ya Umra.
5. Kufanya Talbiyah.
6. Kuizunguka Al-Ka'aba.
7. Kuswali rakaa mbili nyuma ya Maqam Ibrahim.
8. Kufanya sa'yi kati ya Safa na Marwa.
9. Kunyoa nywele za kichwa au kupunguza. Mwenyezi Mungu ndiye anayejua zaidi, na Mwenyezi Mungu amfikishie rehema na amani Nabii wetu Muhammad.