فتاوى الحج والعمرة والزيارة
FATWA ZA HIJA, UMRA NA KUTEMBELEA MSIKITI WA MTUME
FATWA ZA HIJA, UMRA NA KUTEMBELEA MSIKITI WA MTUME
Kuhusu mambo ambayo watu wanaofanya Umrah wanayahitaji sana.[1] Ambayo yalichaguliwa kutoka katika Mkusanyiko wa Fatwa za Kamati ya Kudumu ya Fatwa katika Ufalme wa Saudi Arabia, huku maswali yakiwa yamefupishwa ili kuendana na kila hali.
Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Huduma ya Maudhui za Kiislamu kwa Lugha mbalimbali.
Kwanza: Majibu (Fatwa) ya kiujumla
Swali: Je, inaruhusiwa kwa baba yangu kufanya Umra kwa pesa alizokopa benki?
Jibu: Ni lazima kwa anayetaka kuhiji au kufanya Umra kwa niaba yake au kwa niaba ya mtu mwingine achague pesa nzuri kwa ajili ya matumizi katika Hija yake na Umra. Kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu ni mzuri na hakubali isipokuwa yaliyo mazuri tu.
Ama kuhusu kukopa kutoka kwenye benki au kutoka sehemu nyingineyo kwa riba, hilo haliruhusiwi. Kwa sababu hiyo ni riba, na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, amemlaani mwenye kula riba, mwenye kuilipa, mwenye kuiandika na mashahidi wake wawili, na akasema: “Wote ni sawa (katika dhambi).” Na kula kilichoharamishwa ni sababu ya kukataliwa dua na kutokubalika kwa matendo. Ama ikiwa si kwa riba, basi hakuna ubaya.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/353)
***
Swali: Je, ni kweli kwamba mtu ambaye amekuwa mbali na Makka kwa muda wa siku arobaini ni wajibu kwake kufanya Umra, hata kama alifanya Umra mara kadhaa?
Jibu: Umra ni wajibu mara moja tu katika maisha kwa mtu anayelazimishwa kisheria, aliye na uwezo wa kufanya hivyo, na chochote kinachozidi mara moja, basi hicho ni sunna. Zaidi ya hayo, Umra inaruhusiwa wakati wowote na haina muda maalumu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/20)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kufanya Umra wakati wowote wa mwaka?
Jibu: Inaruhusiwa kufanya Umra katika siku zote za mwaka, hata katika miezi ya Hija. Ikiwa mtu atataka kufanya Umra katika miezi ya Hija, kisha akafanya Hija baada ya hapo mwaka huo huo, basi atakuwa katika wale waitwao Mutamatti' (mtu aliyefanya Umra na akaishi maisha ya kawaida kabla ya kufanya Hija mwaka huo). Na akifanya Umra pamoja na Hija yake, basi atakuwa katika wale wanaoitwa Qaarin (mtu anayeunganisha Umra na Hija kwa safari moja). Inamlazimu Mutamatti na Qaarin kuchinja mnyama anayeweza kutosheleza kuchinjwa katika Idi ikiwa si katika wakazi wa Msikiti Mtakatifu. Na iwapo mwenye kuhiji ataitekeleza Umra katika Dhul-Hijja baada ya siku za Tashriiq (kubanika nyama), basi hilo pia linaruhusiwa, lakini hatalazimika kuchinja mnyama.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/316)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kufanya Umra kabla ya kuhiji Hija ya faradhi?
Jibu: Ndiyo, mtu anaruhusiwa kufanya Umra kabla ya kuhiji. Kwa sababu, Mtume, rehema na amani zimshukie, na Maswahaba wake walifanya Umra kabla ya kuhiji Hija ya faradhi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/318)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya kurudia Umra katika mwaka?
Jibu: Maoni sahihi ni kwamba inaruhusiwa kurudia Umra mara kadhaa kwa mwaka. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Kwenda Umra mpaka Umra nyingine kunafanya mtu kusamehewa madhambi yanayofanyika baina ya Umra hizo mbili. Na Hija iliyokubalika haina malipo isipokuwa Pepo." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/334)
***
Swali: Baadhi ya watu wanakuja kwa ajili ya Hija, na baada ya kumaliza Umra ya Tamattu’ wanataka kufanya Umra kwa niaba ya mmoja wa wazazi wake, basi atafanyaje?
Jibu: Yeyote atakayehirimia Umra, kisha akaishi maisha ya kawaida kabla ya Hija, basi baada ya kumaliza Umra yake, kilicho bora zaidi kwake ni kwamba akae Makka mpaka ufike wakati wa Hija, kisha aihirimie na wala asirudie Umra kabla ya Hija. Atakapomaliza Hija, basi hakuna ubaya kwake kufanya Umra baada yake kutokea At-Tan’im au katika sehemu nyingine miongoni mwa sehemu zilizoko nje ya eneo takatifu. Na ikiwa atafanya Umra nyingine kwa niaba ya baba yake aliyefariki au mama yake aliyekufa au ambao hawawezi kufanya hivyo kutokana na uzee au ugonjwa ambao hautarajiwi kupona, au ikiwa atawafanyia wengineo miongoni mwa wenye sifa hizi, basi hakuna ubaya juu yake. Hili ni kwa sababu ya ujumla wa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kwenda Umra mpaka Umra nyingine kunafanya mtu kusamehewa madhambi yanayofanyika baina ya Umra hizo mbili. Na Hija iliyokubalika haina malipo isipokuwa Pepo." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/117)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mwenye kufanya zaidi ya Umra moja? Na katika kila Umra anaenda Tan'im ili kuhirimia huko?
Jibu: Kurudia Umra kwa mtu aliyekuja Makkah katika muda mfupi haikuwa sehemu ya muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wala Maswahaba wake, Mwenyezi Mungu awawie radhi, hawakuwa wakifanya hivyo. Kama hilo lingekuwa ndilo bora, basi wangetangulia kufanya hivyo. Hivyo basi, lililo katika sheria kwa atakayekuja Makka na akamaliza ibada yake (ya Hija au Umra), ni afanye tawafu hasa kwa wingi, asome Qur'ani, aswali, atoe sadaka na mengineyo miongoni mwa ibada. Na kama atafanya Umra kwa ajili yake mwenyewe au kwa niaba ya mtu mwingine ambaye inaruhusiwa kumfanyia Umra, kama vile maiti, au asiyeweza kutokana na uzee au maradhi ambayo hayatarajiwi kupona, basi hakuna tatizo ikiwa haimsababishii ugumu wala kuwafanyia watu ugumu kama vile nyakati za msongamano wa watu. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Kwenda Umra mpaka Umra nyingine kunafanya mtu kusamehewa madhambi yanayofanyika baina ya Umra hizo mbili. Na Hija iliyokubalika haina malipo isipokuwa Pepo." Na kwa yale yaliyothibiti kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alimuamuru Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kufanya Umra kutokea At-Tan’im baada ya kumaliza Hija na Umra, alipomuomba ruhusa kufanya hivyo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/355)
***
Pili: Fatwa za vituo vya kuhirimia Hija na Umra (Miqat)
Swali: Mtu akitaka kuhiji au kufanya Umra, na ikamuwia vigumu kuhirimia ndani ya ndege, na wala hajui umbali wa Miqat, je anaweza kuchelewesha kuhirimia mpaka atakapofika Jeddah au la?
Jibu: Mtu anapotaka kuhiji au kufanya Umra huku yuko ndani ya ndege, basi anaweza kuoga nyumbani kwake na kuvaa shuka na kikoi, akipenda. Kisha atakapokua umbali mfupi kabla ya Miqat anaweza kuhirimia anachotaka, sawa sawa iwe ni Hija au Umra, kama hilo halina ugumu. Na kama hajui Miqat iko wapi, basi amuulize rubani wa ndege au yeyote anayemsaidia au muhudumu yeyote, au abiria wenzake miongoni mwa wale ambao ana imani nao katika watu wenye uzoefu katika jambo hilo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/153)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mtu anayetaka kufanya Umra huku anasafiri kwa ndege kwenda kuhirimia Umra bila ya kuvaa nguo za Ihram, kwa sababu anataka kufanya baadhi ya kazi zake katika mji wa Jeddah, na baada ya kumaliza kazi zake hizo, atahirimia huko huko Jeddah na kwenda kufanya Umra, au analazimika kufanya nini?
Jibu: Yeyote atakayefunga safari kwa ajili ya kuhiji au Umra, basi haruhusiwi kupita Miqat isipokuwa akiwa ameshahirimia kile alichokusudia kufanya, atavua nguo za kawaida na atajiepusha na makatazo ya ihramu.
Kwa hivyo, hauruhusiwi kufanya uliyoyataja katika swali lililotajwa; Kwa sababu linakiuka hukumu ya Kiislamu, lakini hakuna ubaya kwake kwenda Jeddah bila ya kuhirimia ili kutimiza mahitaji yake, kisha arudi kwenye Miqat ili ahirimie huko kwa ajili ya Hija yake au Umra.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/81)
***
Swali: Je, ni sahihi kwa mwenye kuhiji au kufanya Umra kuhirimia mahali paitwapo Abyaar Ali huko Madina, pamoja na kwamba alitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Jeddah, lakini alitangulia kusafiri kwenda Madina kisha akahirimia kutokea huko Abyaar Ali?
Jibu: Hujaji anapotua katika Uwanja wa Ndege wa Jeddah na akataka kutoka Jeddah kwenda Madinah kabla ya Hija, basi atakapomaliza ziara yake ya Madina na kisha akataka kurejea Makka kufanya Hija au Umra, atahirimia katika Miqat ya watu wa Madinah “Dhul-Hulaifah” ambayo kwa sasa inaitwa “Abyaar Ali”. Kwa sababu ataingia katika hukumu ya watu wa Madina. Hili ni kwa mujibu wa kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kuhusu Miqat: "Hivi ni vya watu wa hapa, na pia kwa mwenye kuvijia asiyekuwa katika watu wake, miongoni mwa wanaotaka kufanya Hija au Umra." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/94)
***
Swali: Ikiwa mtu atafanya Umra siku ya Ijumaa ya mwezi wowote, kisha akataka kwenda sehemu nyingine, na baada ya siku mbili au tatu akarejea Makka, na akataka kufanya Umra tena, je inaruhusiwa kufanya Umra hiyo bila kuvaa nguo za Ihramu?
Jibu: Yeyote anayetaka kufanya Umra lazima aingie kwenye Ihramu kutokea kwenye Miqat anayopitia akiwa njiani kuelekea Makka, na hairuhusiwi kwake kuivuka bila ya kuingia kwenye ihram. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alizibainisha Miqat hizi za kuingia katika Ihram kutokea hapo kwa wale wanaotaka kuhiji au kufanya Umra, iwe ni kwa mara ya kwanza au kwa Umra ya pili au zaidi. Ama wale walio ndani ya Miqat, wao wataingia kwenye Ihram kutokea sehemu ambayo wamekusudia kufanya Umra, isipokuwa wakiwa Makka, hapo watatakiwa watoke waende kwenye eneo lililo nje ya eneo takatifu na wahirimie Umra kutokea huko, kama alivyofanya Aisha, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwa amri ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/354)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mwenye kumfanyia baba yake Umra baada ya kujifanyia Umra, na akarudia kufanya Umra kwa niaba ya baba yake kutokea mahala pa kuhirimia huko Makka Al-Mukarramah (At-Tan’iim)?
Jibu: Ukijifanyia Umra na kisha ukaimaliza, na ukataka kumfanyia baba yako Umra ikiwa alikufa au hana uwezo, basi utatoka uende katika eneo lisilo takatifu kama vile At-Tan’iim, na uhirimie Umra kutokea huko, na hautakiwi kusafiri kwenda kwenye Miqat.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/135)
***
Tatu: Fatwa za Ihram na makatazo yake
Swali: Iwapo mtu atavaa nguo za ihram kwa ajili ya Umra au Hija, kisha akaitengua nia yake, ni nini kitakachomlazimu?
Jibu: Iwapo mtu atavaa kikoi na shuka lakini hado hajakusudia kuhiji au kufanya Umra, na bado hajafanya Talbiya, basi ana hiari: Akitaka, anaweza kuhiji au kufanya Umra, na akitaka, anaweza kuacha kufanya hivyo, na hakuna ubaya juu yake ikiwa alishawahi kufanya Hija na Umra ya Kiislamu (ya lazima).
Ama iwapo alikuwa ameshakusudia kuhiji au kufanya Umra, basi hawezi kuyavunjilia mbali hayo na kuachana nayo. Bali inamlazimu akamilishe alichohirimia kwa njia ya kisheria. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu aliyetakasika: "Wa-atimmulhajja wal-‘umrata lillaahi (Na timizeni Hija na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu)." (Suratul-Baqara: 196)
Kwa hayo, inakudhihirikia kwamba Muislamu akiingia katika Hija au Umra kwa nia, basi haruhusiwi kuachana nayo. Bali ni lazima akamilishe aliyoyaanza; kwa mujibu wa Aya tukufu iliyotajwa hapo juu, isipokuwa kama alikuwa ameweka sharti, kisha kizuizi alichohofia kikatokea, basi anaweza kujivua akaachana nayo. Hili ni kwa sababu ya kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alipomwambia Dhuba’ah bint Zubair pale aliposema: “Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ninataka kuhiji lakini mimi ni mgonjwa." Akasema: "Hiji na uweke sharti kwamba mahali pangu pa kutoka katika Ihramu ni pale utakaponizuilia." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/166)
***
Swali: Mwanamke anapohirimia Umra, kisha akapata hedhi kabla ya kufanya tawafu au sa’yi, kisha akarudi nyumbani kwake na akatoka katika ihramu yake, je, kuna lolote juu yake? Na kama hakutoka katika ihramu yake, je, kuna lolote juu yake?
Jibu: Ikiwa mwanamke atahirimia Umra kisha akapata hedhi na akatoka katika ihramu yake kabla ya kufanya tawafu na sa’yi, basi ikiwa hakujua hukumu ya hilo na mume wake hakujamiiana naye, basi itamlazimu akamilishe Umra yake baada ya hedhi yake kukatika na kuoga kutokana nayo kama anavyofanya kwa ajili ya janaba. Kisha atafanya tawafu na sa'yi na atatoka katika ihramu baada ya kupunguza nywele za kichwa chake, na wala hakutakuwa na chochote juu yake.
Na ikiwa atajamiiana, basi Umra yake itabatilika na itamlazimu kukamilisha tawafu, sa’yi na kupunguza nywele. Kisha itamlazimu afanye Umra nyingine badala yake kutokea kwenye Miqat aliyohirimia ile ya kwanza, na itamlazimu achinje mnyama: Ima kondoo mwenye umri wa miezi sita au zaidi, au mbuzi mwenye umri wa mwaka mmoja au zaidi. Atamchinjia Makka na aigawanye nyama yake kwa masikini wake.
Ama ikiwa hakuwa ametoka katika Umra yake, basi itamlazimu kukamilisha Umra yake kwa kufanya tawafu na sa’yi kisha atatoka katika Umra yake kwa kunyoa baadhi ya nywele zake, wala Umra yake haibatiliki kwa hedhi kwa hali yoyote ile.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/323)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mtu aliyehirimia (Hija au Umra) kutumia sabuni yenye manukato?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mtu aliye katika ihramu, awe mwanamume au mwanamke, kutumia manukato, ikiwa ni pamoja na kutumia sabuni yenye manukato. Na mwenye kugusa manukato kwa makusudi na kwa kujua, basi inamlazimu alipe fidia. Na kama alikuwa hajui hukumu ya hilo au alikuwa amesahau, basi hakuna chochote juu yake; kwa mujibu wa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Rabbanaa laa tu-aakhidhnaa in nasiinaa aw akhtwa-anaa (Mola wetu Mlezi! Usituchukulie ubaya tukisahau au tukikosea)." (Suratul-Baqara: 286) Na kwa kauli ya Mtume, rehema na amani zimshukie: "Umma wangu umesamehewa mambo waliyoyafanya kwa kukosea na kwa kusahau na yale waliyolazimishwa kufanya."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/137)
***
Swali: Kabla ya kuhirimia kwangu, nilikwenda chooni, basi nikajisahau na nikaweka shuka langu juu ya kichwa changu kwa muda mfupi, kisha nikakumbuka na nikaliondoa. Swali: Je, kinanilazimu chochote?
Jibu: Iwapo mtu aliyehirimia atasahau na kufanya jambo lolote lililoharamishwa wakati wa ihramu, basi la wajibu juu yake ni kuliacha pindi anapokumbuka, na wala hakuna dhambi yoyote juu yake wala fidia. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Rabbanaa laa tu-aakhidhnaa in nasiinaa aw akhtwa-anaa (Mola wetu Mlezi! Usituchukulie ubaya tukisahau au tukikosea)." (Suratul-Baqara: 286) Mwenyezi Mungu akasema, “Nimeshafanya.” kama ilivyothibiti kwa njia sahihi kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake. Vile vile, ilisimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake kwamba alisema: "Umma wangu umesamehewa mambo waliyoyafanya kwa kukosea, na kwa kusahau na yale waliyolazimishwa kufanya."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/149)
***
Swali: Mimi, mke wangu na dada yangu tulifanya Umra katika Ramadhani, lakini walivaa glovu kwa amri yangu wakati wa Umra kwa kutojua hukumu ya hilo. Sasa tunalazimika kufanya nini?
Jibu: Ikiwa mwanamke aliye katika ihramu atavaa glovu kwa kutojua hukumu yake, basi hakuna ubaya wowote juu yake. Hata hivyo, ikiwa atajua hukumu yake huku ameshahirimia, basi itamlazimu aivue glovu hiyo mara moja.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/156)
***
Swali: Mimi na mke wangu tulihirimia Umra, kisha mke wangu akapatwa na hedhi baada ya hapo, na kwa sababu sikujua hukumu yake, nilitoka katika ihram yangu na nikavua nguo za ihram na hatukumaliza tukaenda Makka. Kisha katika mwezi wa Ramadhani wa mwaka huu, mimi na mke wangu tukafanya Umra – kwa fadhila za Mwenyezi Mungu - na ninatumai kwamba utakuwa mkarimu kunielezea hukumu ya kisheria ya hayo. Pia nitapenda unielezee cha kufanya sasa?
Jibu: Mlipaswa kufanya Umra bila ya kuivunja. Kuvunjilia kwenu mbali nia ya Umra na kuvaa kwenu nguo za kawaida hakubadilishi uhalisia hata kidogo. Kwani Ihram ilibakia na wala haikufutiliwa mbali. Hivyo basi, ile Umra yenu ya pili inachukuliwa kuwa ni mwendelezo wa ile Umra yenu ya kwanza. Ikiwa mlijamiiana katika muda huo uliokuwepo kabla ya kufanya Umra ya pili, basi inawalazimu mfanye Umra nyingine ya kulipa ile Umra iliyoharibika kwa sababu ya kujamiiana kwenu. Mtaifanya kutokea kwenye Miqat mliyohirimia ile Umra ya kwanza, kisha mtalazimika kulipa fidia, ambayo ni kondoo mmoja kwa kila mmoja wenu. Atachinjiwa Makka na agawiwe masikini wa eneo takatifu (Haram).
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/384)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya kuvaa mkanda ikiwa umetengenezwa kwa ngozi, lakini pia umeshonwa kwa uzi na mashine, na pia kuvaa viatu vilivyoshonwa kwa uzi?
Jibu: Inaruhusiwa kwa aliyehirimia Hija au Umra kuvaa mkanda na viatu, hata kama vimeshonwa kwa uzi na mashine.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/170)
***
Swali: Nilipohirimia kutokea huko Abyaar Ali, na tukaendelea na safari yetu kuelekea Makka, nilipata shida kubwa njiani mpaka nikapatwa na homa kali. Kwa hiyvo, nikalala na kujifunika kichwa changu. Je, inanilazimu kufanya chochote?
Jibu: Inakulazimu kutoa fidia, ambayo ni kufunga siku tatu, au kulisha masikini sita, au kuchinja kondoo kwenye eneo takatifu la Makka (Haram).
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/181)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya kuvaa soksi miguuni na kufanyia tawafu ndani yake? Na je, soksi zinachukuliwa kuwa miongoni mwa vitu vilivyoshonwa kwa uzi?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mwanamume kuvaa soksi akiwa katika hali ya Ihram ya Hija au Umra. Ikiwa atahitaji kuzivaa kutokana na maradhi au mfano wa hilo, basi inaruhusiwa, lakini itamlazimu kutoa fidia, ambayo ni kufunga saumu siku tatu, au kulisha masikini sita, kila mmoja wao apokee nusu kibaba ya tende au mfano wake, au achinje kondoo mmoja.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/183)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mtu aliyehirimia kuosha mwili wake wote ili kupata ubaridi, na kwa nini?
Jibu: Inaruhusiwa kwa Muislamu kuosha mwili wake wote ili kupata ubaridi ikiwa anahisi joto. Hili litamfanya kuwa mkakamavu juu ya kufanya ibada hii, lakini anapaswa kuwa mwangalifu wakati wa kuuosha ili kisianguke chochote kutoka kwenye nywele zake au ngozi yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/184)
***
Swali: Iwapo mtu aliyehirimia Hija au Umra atakanyaga mti au nyasi kwa gari lake, je, kuna ubaya wowote juu yake katika hilo?
Jibu: Iwapo atavikanyaga ilhali hayuko katika eneo takatifu, basi hakuna chochote juu yake, isipokuwa ampe mmiliki wa kile alichokiharibu thamani yake ikiwa ni mali yake. Na ikiwa ataharibu chochote katika miti au nyasi za eneo takatifu la Makka ambacho ni mali ya mtu, basi atalazimika kulipa thamani yake kwa mmiliki wake. Na kama si miliki ya mtu yeyote, basi hakuna chochote juu yake, lakini haifai kukusudia kufanya hivyo, kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikataza hilo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/185)
***
Swali: Je, anaruhusiwa mwanamume au mwanamke aliyehirimia kubadilisha nguo yake ya ihramu kwa nguo nyingine ya ihramu sawa sawa iwe ni wakati wa Hija au Umra?
Jibu: Mtu aliyehirimia Hija au Umra anaruhusiwa kubadilisha nguo zake za ihramu kwa nguo nyingine za ihramu na kubadilisha huku hakutaathiri chochote katika ihramu yake ya Hija au Umra.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/185)
***
Swali: Nilipokuwa ninaomba dua huku nimegusana na Al-Kaaba Tukufu katika eneo la Al-Multazam, nilijikuta mkono wangu umegusa mafuta ya manukato ya Al-Kaaba Tukufu, na nikajipaka mwili wangu, nywele zangu na nguo zangu kwa manukato hayo. Je, ni ipi hukumu ya kujipaka huku manukato ya Al-Multazam, ambayo niliyagusa kwa bahati mbaya bila ya kukusudia kisha nikatawadha na kuyaondoa bila kuchelewa sana?
Jibu: Kugusa kwa mkono wako manukato yanayopatikana kwenye Al-Kaaba kwa bahati mbaya, kisha ukajipaka manukato hayo kwenye mwili wako, nywele zako na nguo zako, pamoja na kwamba umeharamishiwa, itakulazimu utoe fidia ambayo ni kufunga saumu siku tatu, au kulisha masikini sita kwa kumpa kila masikini nusu ya kibaba, au kuchinja kondoo mmoja, isipokuwa ikiwa ulikuwa hujui hukumu ya kisheria ya hilo, au ikiwa ulisahau, basi hutalazimika kufanya chochote.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/186)
***
Swali: Mwanamke alifanya Umra mara tatu, na alikuwa amevaa barakoa. Pia alikuwa amevaa kitambaa hafifu juu ya barakoa. Wakati mwingine alikuwa akikiweka juu ya barakoa hiyo na wakati mwingine alikuwa anakiondoa. Na hakuwa anajua hukumu ya kuvaa barakoa. Basi ni nini hukumu ya hilo ewe mheshimiwa Sheikh?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mwanamke aliyehirimia Hija au Umra kuvaa nikabu, ambayo ndiyo barakoa, lakini anapokuwa pamoja na wanaume wasiokuwa maharimu wake, basi anapaswa kukishusha kitambaa chake juu ya uso wake, kama walivyofanya hivyo wake wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yao, wakati wa Hija ya kuaga. Na maadamu mwanamke huyo aliyetajwa hapo juu alivaa nikabu kwa kutojua, basi hakuna ubaya wowote juu yake. Kwa sababu, anakubaliwa udhuru wake kwa sababu ya kutojua hilo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/194)
***
Nne: Fatwa za Tawafu
Swali: Nilifanya ibada za Umra... na kwa vile sikuwa nazifahamu ibada hizo sawa sawa, nilipoanza tawafu, sikuanzia kwenye Jiwe Jeusi, bali nilianzia kwenye kona ya Yemeni, kutokana na kutojua kwangu masharti na wajibu. Kisha nilikamilisha ibada zilizosalia kwa usahihi, Mwenyezi Mungu akipenda... kwa hivyo tunatumai kwamba utanifahamisha kile kinachotakiwa kwangu?
Jibu: Alichofanya muulizaji wakati wa tawafu cha kuanzia kwenye kona ya Yemeni, kinachukuliwa kuwa ni kosa. Kwa sababu mwanzo unafaa uwe kutokea kwenye Jiwe Jeusi, lakini kosa hili haliathiri usahihi wa tawafu yake. Kwa sababu, hilo linachukuliwa kuwa ni raundi ya ziada katika raundi ya kwanza, na haina madhara yoyote ikiwa alimalizia raundi ya saba vyema katika Jiwe Jeusi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/210)
***
Swali: Je, kuvaa lubega wakati wa Twawaf ni sunna? Na je, mtu aliyesahau kuvaa lubega afanye nini? Na je, kulibusu Jiwe Jeusi kunatosheleza badala ya kusema: "Bismillahi wallahu akbar (Kwa jina la Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa)?" Ni nini kilicho juu ya mwenye kuiacha kauli hii na akatosheka na kulibusu Jiwe Jeusi kwa kusahau, kisha akakumbuka ilhali yuko mbali na mahali pa Jiwe Jeusi, na kusema hayo huku anaenda kwenye Maqam Ibrahim?
Jibu: Idtiba’ (kuvaa lubega) ni pale mwenye kuhiji anapoweka katikati ya shuka yake chini ya kwapa lake la kulia na ncha zake juu ya bega lake la kushoto, ili bega lake la kulia na mkono wa juu viwe wazi. Hilo ni sunna katika tawafu ya kwanza mtu anapofika Makka. Hii ndiyo Tawafu ya Umra ya Hija ya Tamattu’, au Tawafu ya kufika Makka kwa mtu anayefanya Hija na Umra kwa pamoja bila ya kuwepo muda kati ya Umra na Hija, pia kwa yule anayefanya Hija peke yake. Mwenye kuiacha tawafu hii, hana kitu chochote juu yake.
Hakuna ubaya wowote kwa mtu anayeacha Takbira na kusema Bismillah mwanzoni mwa Tawafu. Kwa sababu Takbira, kumtaja Mwenyezi Mungu na kuomba dua wakati wa tawafu na sa’yi ni sunna na si wajibu. Bali lililo wajibu ni kuzunguka Kaaba na kufanya sa’yi kwa nia kutokea mwanzo hadi mwisho.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/210)
***
Swali: Wakati wa tawafu, mimi humbeba binti yangu mdogo, naye huwa amevaa nepi. Nilisisikia kwamba hairuhusiwi kufanya tawafu katika hali hii, kwa sababu mara nyingi nepi huwa na mkojo. Hivyo basi, tungependa kujua hukumu ya hilo kutoka kwenu weheshimiwa.
Jibu: Mtu anayefanya tawafu anaruhusiwa kumbeba mtoto, hata akiwa amevaa nepi maadamu mwenye kufanya tawafu hajapatwa na najisi kwenye mwili wake au nguo zake. Vile vile, inaruhusiwa kuswali naye katika hali hii.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/236)
***
Swali: Je, mwanamke mwenye hedhi anaruhusiwa kufanya Tawafu?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mwenye hedhi kuzunguka Nyumba mpaka asafike na aoge kutokana na hedhi yake. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimwambia Aisha alipokuwa katika hedhi: "Usiizunguke Nyumba mpaka uwe safi."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/249)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwanamke kufanya tawafu na Sa’yi huku mumewe au maharimu wake amemngoja mpaka amalize, na wala hayuko pamoja naye wakati wa tawafu na Sa’yi, bali amemngojea katika eneo takatifu la Makka, mpaka amalize Umra yake?
Jibu: Sio katika masharti ya kufanya Tawafu kuwa sahihi kwamba mwanamke aambatane na maharimu wake wakati wa Tawafu ya Umra au Hija. Bali maharimu anatakiwa kwa mwanamke katika safari ya Umra na safari nyinginezo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/353)
***
Swali: Mtu alikuwa akiizunguka Nyumba akiwa katika mzunguko wa tano, kwa mfano, na kabla hajamaliza mzunguko huo wa tano, swala ikakimiwa. Basi akaswali kisha akasimama ili kukamilisha tawafu yake. Je, atauhesabu mzunguko huo wa tano alioukata kwa ajili ya swala na aendelee kuanzia pale aliposimamia, au auvunje mzunguko huo wa tano na auanzishe tena kutokea kwenye Jiwe Jeusi?
Jibu: Mtazamo sahihi ni kwamba hafai kuufutilia mbali mzunguko huo katika hali kama hiyo. Bali ataukamilisha mzunguko huo kutokea pale ambapo aliukatizia kwa ajili ya kuswali pamoja na imamu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/230)
***
Swali: Je, Jiwe Jeusi lilishuka kutoka mbinguni? Au ni jiwe kama mawe mengine?
Jibu: Mwenyezi Mungu Mtukufu aliliteua Jiwe Jeusi kwa yale aliyotuwekea katika sheria ya kulibusu na kuligusa. Pia alitaka liwe kwenye kona ya Kaaba ambayo huwa tunaielekea katika swala zetu. Na aliwawekea mahujaji na wale wanaofanya Umra sheria ya kulibusu na kuligusa ikiwa hilo litawezekana. Lakini ikiwa haliwezekani, basi mtu ataliashiria anapofikia usawa wake huku akitoa Takbira. Kuna Hadithi iliyopokelewa na At-Tirmidhi na wengineo ikieleza kuwa lilishuka kutoka Peponi, lakini silsila (mlolongo) wa wapokezi wake ni dhaifu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/228)
***
Swali: Je, kubusu Al-Kaaba wakati wa ibada ya Hija au Umra kunaruhusiwa au ni haramu?
Jibu: Kile ambacho kiko katika sheria ni kulibusu Jiwe Jeusi. Imethibiti kuwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alilibusu Jiwe Jeusi na hakubusu sehemu nyingine yoyote ya Al-Kaaba Tukufu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/228)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwanamke kulibusu Jiwe Jeusi ilhali kuna wanaume wasiokuwa maharimu wake hapo karibu?
Jibu: Kubusu Jiwe Jeusi wakati wa Tawafu ni sunna iliyosisitizwa miongoni mwa sunna za Tawafu ikiwezekana kuifanya bila kuleta msongamano wala kumdhuru mtu yeyote kwa vitendo vyako, kwa kumfuata Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika hilo. Lakini ikiwa haiwezekani isipokuwa kwa msongamano na kuleta madhara, basi inalazimu kuliacha, na kutosheka na kuliashiria tu kwa mkono, hasa mwanamke; Kwa sababu wao ni uchi, na kwa sababu hata wanaume hawaruhusiwi kuleta msongamano, basi itafaa zaidi kwa wanawake kutofanya hivyo. Vile vile hairuhusiwi kwa mwanamke wakati wa kulibusu ikiwa hilo linawezekana kwake bila ya msongamano kuufunua uso wake huku akilibusu Jiwe Jeusi. Kwa sababu mahali hapo kuna wale ambao si maharimu wake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/229)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwenye kuhiji au mwenye kufanya Umra kuingilia kwenye Hijr Ismail wakati anapokuwa anafanya tawafu kwenye Nyumba?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mtu anayeizunguka Nyumba wakati wa Hija, Umra au yule anayefanya tawafu ya hiyari kuingia kupitia kwenye Hijr Ismail, na hilo haliwezi kumtosheleza ikiwa atafanya hivyo. Kwa sababu tawafu huwa kandoni mwa Nyumba, nayo Hijr Ismail ni sehemu katika Nyumba; kama alivyosema Mwenyezi Mungu aliyetakasika: "...wal-yuufuu nudhuurahum wal-yattwawwafuu bilbaytil-‘atiiq (...na waizunguke Nyumba ya Kale)." (Suratul-Hajj: 29). Na yale aliyoyasimulia imamu Muslim na wengineo kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: “Nilimuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuhusu Jiwe Jeusi, akasema: "Ni sehemu katika Nyumba." Na katika matamshi mengine, Aisha alisema: "Hakika niliweka nadhiri kuswalia katika Nyumba." Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akasema: "Swalia katika Al-Hijr. Kwa maana Al-Hijr ni katika Nyumba."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/233)
***
Tano: Fatwa za Sa’yi
Swali: Kuhusu wanawake kuzidisha kasi ya kutembea baina ya zile taa mbili za kijani kibichi wakati wa Sa’yi, sijawahi kupata katika usomaji wangu mdogo katika vitabu vya fiqhi katika mlango wa kueleza Hija na Umra kitu chochote kinachowazuia wanawake kufanya hivyo. Na siku moja niliwahi kusikia kutoka kwa mwanachuoni wa televisheni kwamba wanawake hawatakiwi kukimbia wakati wa Sa’yi, na kwamba hilo ni kwa wanaume peke yao, lakini hakutoa ushahidi wowote juu ya kauli yake hii. Basi nikasema: Ikiwa kweli hayo kayasema mwenyewe kutokana na jitihada zake, basi mtu kuongeza kasi katika kufanya Sa'yi ni jambo la sunna iliyoanzishwa na Hajar, Mwenyezi Mungu amuwie radhi. Lakini mimi ninaelewa maoni - na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu - kwamba dini haitokani na maoni ya watu, kama alivyosema kiongozi wa Waumini Ali, Mwenyezi Mungu amuwie radhi. Tafadhali tushaurini, Mwenyezi Mungu akubarikini.
Jibu: Amesema bin Mundhir: "Wanavyuoni walikubaliana kwamba wanawake hawatakiwi kuizunguka Nyumba tukufu kwa kasi kubwa, wala kuzidisha kasi baina ya Swafa na Marwa, na wala hawatakiwi kuvaa lubega katika tawafu. Hayo ni kwa sababu madhumuni ya awali ya yote mawili ni kudhihirisha ngozi, na hili halikusudiwi kwa wanawake. Kwa sababu wanawake wameamrishwa kujifunika, na katika kuzidisha kasi na kuvaa lubega kuna uwezekano mkubwa wa kujifunua.”
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/226)
***
Sita: Fatwa za kumaliza Umra
Swali: Iwapo mtu atanyoa kichwa chake katika Umra wiki hii kisha akafanya Umra wiki ijayo. Afanye nini? Kwani nywele zake huwa bado ni fupi sana, na labda huwa bado hazijaota.
Jibu: Mwenye kufanya Umra au Hija ni lazima anyoe kichwa chake au apunguze nywele zake. Ikiwa hakuna nywele juu ya kichwa chake, basi faradhi hii imeondolewa, na Hija yake au Umra bado ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/327)
***
Swali: Kundi la watu lilikwenda kufanya Umra, wakakamilisha ibada zao na mmoja wao akanyoa nywele za hao wenzake, kisha mmoja wao akamnyoa yeye na wakatoka katika ihramu zao kwa kufanya hivyo. Basi ni nini hukumu ya hilo?
Jibu: Ikiwa mtu aliye katika ihram atamnyoa kichwa mtu mwingine aliye katika ihram ambaye anataka kutoka katika ihramu, basi hakuna ubaya katika hilo. Kwa sababu huko ni kunyoa ambako kunaruhusiwa.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/146)
***
Swali: Tafadhali tufahamisheni kuhusu njia sahihi ya kunyoa wakati wa Hija na Umra. Je, ni kunyoa kwa wembe au kunyoa kwa mashine? Na je, kunyoa kwa wembe ni bora kuliko kunyoa kwa mashine, au yote mawili ni sawa?
Jibu: Jambo linalozingatiwa ni kwamba kunyoa au kupunguza nywele kufanyike kwa chombo chochote kile kinachotumiwa, pamoja na kujua kwamba kunyoa ni bora zaidi. Ilithibiti kuwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliwaombea msamaha na rehema mara tatu wale walionyoa nywele zao, na akawaombea mara moja wale waliopunguza tu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/201)
***
Swali: Iwapo mkazi wa Jeddah atafanya Umra na asinyoe kichwa chake mpaka anapokwisharudi Jeddah, ni ipi hukumu ya kitendo hiki?
Jibu: Hakuna ubaya kunyoa kichwa kwa ajili ya ibada ya Hija au Umra katika sehemu yoyote ile nje ya eneo takatifu la Makka au ndani yake. Hata hivyo, kwa yule anayefanya Umra, yeye hatatoka katika hali yake ya Ihramu mpaka anyoe au afupishe nywele za kichwa chake. Na katika Hija, ikiwa alikuwa ameshalirushia vijiwe Jamarat na kufanya Tawafu na Sa’yi, basi haruhusiwi kumuingilia mkewe mpaka anyoe nywele za kichwa chake au azipunguze.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/203)
***
Swali: Mtu mmoja alikuja Jeddah, kisha siku iliyofuata akaenda kufanya Umra ya kwanza katika maisha yake. Alienda pamoja na jamaa yake mmoja na akakamilisha Umra. Alipomaliza Sa'yi, nikamwambia: "Je, tunyoe nywele au tupunguze tu?" Akasema: "Tutanyolea nyumbani." Baada ya kurudi nyumbani, tulisahau kunyoa na tukavua nguo zetu za ihram. Basi tufanye nini, Mwenyezi Mungu akulipeni?
Jibu: Iwapo mtu atasahau kunyoa nywele zake au kuzifupisha, na alifanya tawafu na sa’yi, kisha akavaa nguo zake za kawaida kabla ya kunyoa au kupunguza nywele zake, basi la wajibu kwake ni avue nguo hizo mara tu anapokumbuka na avae nguo za ihram. Kisha anyoe au apunguze nywele zake, kisha avae nguo zake za kawaida na hakuna ubaya wowote juu yake kwa hilo, na wala hatapata dhambi kwani udhuru wake utakubalika kwa sababu alisahau.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/206)
***
Fatwa ambazo mahujaji mara nyingi huzihitajia [2] Ambazo zilichaguliwa kutoka katika Fatwa za Kamati ya Kudumu ya kutoa Fatwa katika Ufalme wa Saudi Arabia, huku maswali yakiwa yamefupishwa ili yaendane sawa na kila hali.
Hukumu ya Hija, hadhi yake na uwakilishi ndani yake
Swali: Ni upi umuhimu wa Makka kwa ulimwengu wa Kiislamu?
Jibu: Mwenyezi Mungu ameifanya Makka kuwa ni pahala pa kukusanyikia watu, mahali pa amani na eneo takatifu lenye usalama. Mahujaji na wanavyuoni hukusanyika huko kutekeleza ibada zao kwa raha na utulivu wa hali ya juu, wakitaraji malipo ya Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kuogopa adhabu yake. Pia Waislamu wanajuana huko, wakishauriana na kunasihiana juu ya yale yanayowahusu katika mambo ya dini yao na dunia yao, na huko swala zao na matendo yao mema huzidishwa.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/8)
***
Swali: Baba yangu alihiji mara moja kwa miguu takribani miaka 40 iliyopita, na alifanya Umra mara mbili, moja kati ya hizo ilikuwa miaka mitatu kabla ya kifo chake. Alikuwa ni mtu asiyejua kusoma wala kuandika, na sikujua jinsi alivyofanya Hija hii. Je inanilazimu nifanye Hija kwa niaba yake, na ni nini maoni yenu enyi waheshimiwa juu ya hilo?
Jibu: Hija ni wajibu mara moja tu katika maisha. Kanuni ya msingi katika kutekeleza ibada zote na ibada za Hija na Umra ni kwamba huwa ziko sahihi na hazina makosa. Kwa hivyo, hiyo Hija ya pili si wajibu, na ikiwa utamfanyia baba yako Hija, basi hiyo inakua ni kitendo cha kujitolea, na utapata wewe pamoja na yeye malipo makubwa kwa hilo ikiwa Mwenyezi Mungu ataikubali kutoka kwako.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/15)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mke kutoka kwenda kuhiji Hija ya faradhi bila idhini ya mumewe?
Jibu: Hija ya faradhi ni wajibu iwapo masharti ya uwezo yatapatikana, na ruhusa ya mume si miongoni mwa hayo. Haruhusiwi kumzuia kufanya hivyo. Bali ni katika sheria kwamba ashirikiane naye katika kutekeleza wajibu huu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/20)
***
Swali: Je, mwanamke aliyeolewa anaruhusiwa kwenda Hija bila ya ridhaa ya mumewe anapokuwa pamoja na jamaa zake ambao ni kaka zake?
Jibu: Mwanamke haruhusiwi kusafiri kwa ajili ya Hija bila ya idhini ya mumewe, isipokuwa ikiwa ni Hija ya faradhi. Kwa sababu mume wake hana haki ya kumzuia katika hilo ikiwa yuko pamoja na maharimu wake, na haruhusiwi kusafiri bila ya maharimu, si kwa ajili ya Hija wala kwa ajili ya kitu kingine chochote. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Si halali kwa mwanamke anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kusafiri isipokuwa ikiwa yuko pamoja na maharimu wake." Kundi la wanawake tu halitoshi kuchukua mahali pa maharimu. Na Hija ya faradhi na Hija nyingineyo ni sawa katika suala hili.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/40)
***
Swali: Nikitaka mdogo wangu ambaye bado hajabaleghe ahiji pamoja nami, je, nimvalishe nguo za Ihram na nimfanyie ibada zote za Hija kama vile kumfanyia Tawafu na mengineyo, au nimvalishe nguo zake za kawaida na nisifanye lolote kwa niaba yake maadamu bado ni mdogo ambaye halazimiki kuhiji?
Jibu: Iwapo mlezi wa mtoto mdogo ambaye bado hajabalehe lakini anapambanua mambo anataka kuhiji kwa niaba yake, anapaswa kumuamuru kuvaa nguo za Ihram na ajifanyie mwenyewe ibada zote za Hija, kuanzia kwenye Miqat mpaka kwenye ibada ya mwisho ya Hija. Mlezi wake atamrushia vijiwe ikiwa hataweza kuvirusha mwenyewe. Pia atamuamrisha kujizuilia makatazo ya ihramu atakapokuwa bado yuko katika ihram. Na ikiwa mtoto huyo atakuwa ni katika wale wasiokuwa na utambuzi wa mambo, basi mlezi wake atamtilia nia ya kufanya Hija au Umra, kisha atamfanyia Tawafu na Sa’yi pamoja naye, na pia atakuwa pamoja naye katika ibada zilizosalia na atarusha vijiwe kwa niaba yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/22)
***
Swali: Iwapo mvulana mdogo au msichana atahiji, je hiyo itatosheleza Hija ya faradhi au itachukuliwa kuwa ni jambo la hiari tu na malipo yake yanakwenda kwa wazazi wake?
Jibu: Umra au Hija ya mtoto ambaye hajabalehe inachukuliwa kuwa jambo la hiari, na haitoshelezi Hija au Umra ya Uislamu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/23)
***
Swali: Mama yangu alikwenda katika Ufalme wa Saudi Arabia na akaweza kuhiji kwa gharama ya programu ya mpango wa wageni. Anauliza kama Hija hii inatosheleza Hija ya Uislamu, kutokana na kuwa hakutumia mali yake yoyote katika Hija yake?
Jibu: Usahihi wa utekelezaji wake wa faradhi ya Hija hauathiriwi na suala kwamba hakutumia mali yake yoyote katika kuitekeleza, au kwa sababu alitumia kiasi kidogo cha mali na mtu mwingine akamlipia kiasi kikubwa cha gharama za Hija yake. Hivyo basi, kama Hija yake ilitimiza masharti, nguzo na wajibu zake, basi faradhi ya Hija inaondolewa kwake, hata kama mtu mwingine ndiye aliyelipa gharama zake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/34)
***
Swali: Anayetaka kuhiji hapa kwetu ... analazimika aweke kiasi cha laki moja na elfu ishirini na tano ... katika benki, kiasi ambacho ni kikubwa sana. Hili ni pamoja na kwamba benki hizo zinatoza riba, na hakuna njia nyingine ya kwendea Hija isipokuwa njia hii. Katika hali hii, je, Muislamu huyu mwenye uwezo analazimika kuhiji? Na je, Hija yake ni sahihi ikishajulikana kwamba alizisaidia benki zinazoamiliana na riba na pia akaisaidia nchi?
Jibu: Hija yake ni sahihi, na kilichotajwa hakizingatiwi kuwa ni kigezo cha kuichelewesha Hija ikiwa mtu huyo anayeitekeleza ana uwezo wa kufanya hivyo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/42)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mwenye kuhiji kwa mali ya haramu? Je, Hija yake inakubalika au hapana?
Jibu: Hija ya kutekelezwa kwa mali ya haramu haizuii Hija hiyo kuwa sahihi, lakini aliyeichukua kwa njia ya haramu anapata dhambi, na inapunguza malipo ya Hija, lakini haiibatilishi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/43)
***
Swali: Nilichukua kiasi fulani cha pesa kutoka benki ambacho hulipwa kwa awamu mbalimbali katika mwaka. Je, nina haki ya kuhiji wakati ninadaiwa na benki kiasi hiki cha pesa?
Jibu: Kuwa na uwezo wa kuhiji ni mojawapo ya masharti ya kufanya Hija iwe faradhi juu ya mtu. Ikiwa utaweza kuifanya na kulipa awamu zinazotakiwa kwako wakati wa Hija, basi inakulazimu uhiji. Lakini ikiwa yote mawili yatakutokea na huna uwezo wa kuyafanya yote mawili, basi tanguliza kulipa awamu ya mkopo ambayo unatakiwa kulipa na ucheleweshe Hija mpaka utakapoweza. Hili ni kwa mujibu wa maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Walillaahi ‘alannaasi hijjul-bayti manistatwaa’a ilayhi sabiilan (Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezaye njia ya kuiendea)." (Suratul-Baqara: 97)
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/45)
***
Swali: Iwapo mtu atahiji kwa niaba ya maiti au mzee, na yeye mwenyewe hajawahi kuhiji na hana mali isipokuwa mali ya yule anayemuwakilisha. Je, ahiji kwa niaba yake mwenyewe au kwa niaba ya aliyemtuma?
Jibu: Hairuhusiwi mtu kuhiji kwa niaba ya mtu mwingine kabla ya yeye mwenyewe kuhiji. Ushahidi wa hilo ni yale yaliyosimuliwa na bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kwamba: Mtume, rehema na amani ziwe juu yake alimsikia mtu akisema: ‘Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa niaba ya Shubruma.’ Akasema: "Je, wewe mwenyewe ulishahiji?" Akasema: ‘Hapana.’ Akasema: "Hiji kwa niaba yako, kisha kwa niaba ya Shubruma."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/50)
***
Swali: Je, anaruhusiwa Muislamu aliyetekeleza Hija ya faradhi yake kuhiji kwa niaba ya jamaa yake ikiwa hawezi kufika mahali pa kuhiji?
Jibu: Anaruhusiwa Muislamu ambaye ameshajitekelezea Hija ya faradhi kuhiji kwa niaba ya mtu mwingine ikiwa mtu mwingine huyo hawezi kuhiji mwenyewe kwa sababu ya uzee, ugonjwa usiotarajiwa kutibika au kifo. Hilo ni kwa mujibu wa Hadithi sahihi ambazo zimeripotiwa juu ya jambo hili. Ama ikiwa mtu anayefanyiwa Hija hawezi kufanya Hija kutokana na dharura inayotarajiwa kuondoka, kama vile ugonjwa unaotarajiwa kupona, udhuru wa kisiasa, ukosekanaji wa usalama wa njia na mfano wa hayo, basi kumhijia hakumtoshelezi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/51)
***
Swali: Je, nihiji kwa niaba ya wazazi wangu waliofariki na hawakuwajibikiwa kuhiji kutokana na umasikini wao, lakini mimi ndiye niliyetaka tu kuwahijia? Kwa hivyo ninaomba kujua hukumu ya kisheria ya hilo.
Jibu: Unaruhusiwa kuhiji kwa niaba ya wazazi wako mwenyewe, au kumteua mtu wa kuhiji kwa niaba yao ikiwa ulishajihijia, au ikiwa mtu anayehiji kwa niaba yao alishajihijia. Kwa sababu Abuu Daud alisimulia katika Sunan yake kutoka kwa Abdullah bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake alimsikia mwanamume mmoja akisema: “Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa niaba ya Shubruma.” Akasema: “Huyu Shubruma ndiye nani?" Akasema: 'Ni kaka yangu, au jamaa yangu. Imepokelewa na bin Majah. Al-Baihaqi alisema: Huu ni mlolongo wa upokezaji ulio sahihi, na hakuna kilicho sahihi zaidi yake katika mlango huu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/53)
***
Swali: Je, anaruhusiwa mtu kuhiji mara moja tu; akawa amejihijia, na kumhijia baba yake na mama yake?
Jibu: Inaruhusiwa kufanya Hija kwa niaba ya mtu aliyekufa au mtu ambaye yuko lakini hawezi kufanya Hija. Mtu haruhusiwi kujifanyia Hija katika safari moja na kufanya Hija hiyo iwe kwa niaba ya watu wawili. Hija hiyo haitatosheleza isipokuwa mtu mmoja tu. Na vile vile Umra. Lakini ikiwa atamhijia mtu mmoja na akafanya Umra kwa niaba ya mtu mwingine katika mwaka mmoja, basi hizo zitatosheleza ikiwa mwenye kufanya huyo alikuwa ameshajihijia na kujifanyia Umra.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/57)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mwenye kusafiri kwenda Hija na akakusudia kumfanyia Umra mama yake na Hija kwa niaba ya baba yake, na katika mwaka unaofuata akafanya kinyume cha hilo kwa kumhijia mama yake na kufanyia Umra baba yake. Je, hayo yanaruhusiwa?
Jibu: Hija na Umra ni ibada zinazojitegemea, Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alieleza jinsi ya kuzitekeleza, sawa sawa mtu awe Qiran (kuunganisha Umra na Hija bila kupumzika), Ifrad (kufanya Hija peke yake) au Tamattu’ (kuunganisha Umra na Hija pamoja na kupumzika baada ya kumaliza Umra). Kwa hivyo, atakayehirimia Umra kwa niaba ya mama yake kwa mfano, kisha akahirimia Hija baada ya kumaliza Umra kwa niaba ya baba yake, au kinyume cha hivyo, basi anakubaliwa kufanya hivyo. Na kama atahirimia moja ya ibada hizi mbili kwa ajili yake mwenyewe, kisha baada ya kumaliza, akahirimia kwa niaba ya baba yake, kwa mfano, basi hilo pia linaruhusiwa. Kwa sababu matendo yanahukumiwa kulingana na nia, na kila mtu atalipwa kulingana na alichokusudia.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/58)
***
Swali: Mume wangu, Mwenyezi Mungu amrehemu, alifariki dunia, na ninataka - Mwenyezi Mungu akipenda - nimteuwe mtu wa kumhijia mwaka huu. Je, anaruhusiwa huyo mwenye kumhijia kuchukua malipo kwa ajili ya juhudi yake zaidi ya mali anayochukua kama nauli ya usafiri, chakula na vinywaji, au hapana? Ninaomba mnishauri, Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Mtu anayeteuliwa kuhiji kwa niaba ya mtu mwingine anaruhusiwa kuchukua malipo aliyopewa kwa ajili ya kuhiji, hata kama ni zaidi ya kile alichotoa kwa usafiri, chakula, kinywaji na mfano wa hayo miongoni mwa mambo anayoyahitaji mtu mfano wake kwa ajili ya kuhiji. Mtu huyo anaruhusiwa kisheria kukusudia kushiriki katika heri na kufanya ibada atakazoweza katika Eneo Takatifu la Makka, na yasiwe makusudio yake ni mali tu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/60)
***
Swali: Tulihiji pamoja na kijana mdogo na tukamuwekea nia ya kuhiji kwa niaba ya mwanamke fulani aliyefariki. Kisha tukafanya tawafu na tukamaliza na kumtolea fidia kwa niaba ya mwanamke huyo aliyefariki. Ni nini hukumu ya hayo?
Jibu: Alichofanya mvulana huyo mdogo kinachukuliwa kuwa ni Hija ya hiari kwake, na hata halazimiki kujihijia achilia mbali kuhiji kwa niaba ya mtu mwingine, na Hija hiyo haitoshelezi Hija ya faradhi mpaka abaleghe.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/68) zenye marekebisho kidogo
***
Swali: Je, mtu inaruhusiwa (kugharamia gharama za) kuwapeleka wazazi wake kuhiji kabla ya yeye mwenyewe kwenda kuhiji?
Jibu: Hija ni faradhi kwa kila Muislamu aliye huru, mwenye akili timamu na mwenye uwezo wa kuitekeleza, mara moja katika maisha. Kuwafanyia wema wazazi na kuwasaidia kutekeleza majukumu ya wajibu kwao ni jambo lililo katika sheria kulingana na uwezo wa mtu. Hata hivyo, unapaswa kujihijia kwanza, kisha uwasaidie wazazi wako ikiwa haiwezekani kuchanganya Hija hizo zote. Hata hivyo, ikiwa utawatanguliza wazazi wako kuliko wewe mwenyewe, basi Hija yao bado ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/70)
***
Swali: Nina mama mzee ambaye ana umri usiopungua miaka mia moja na hawezi kutekeleza faradhi ya Hija. Kwa hivyo, nilimhijia na kumfanyia Umra mwaka jana kwa kutumia mali yake mwenyewe. Basi baadhi ya watu walisema: "Hija hiyo si sahihi ila baada ya kufa kwake, na Hija yako hiyo haina faida yoyote.” Hivyo basi, ni nini jibu lenu enyi waheshimiwa?
Jibu: Ikiwa mama yako hawezi kuhiji mwenyewe kwa sababu ya uzee wake, basi Hija yako na Umra yako kwa niaba yake ni sahihi, ikiwa umeshajihijia na kujifanyia Umra inavyotakiwa.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/71)
***
Swali: Je, ni mambo gani ambayo inaruhusiwa kumwakilisha mtu katika ibada za Hija, na ni wakati gani inaruhusiwa kuhiji kwa niaba ya mtu mwingine?
Jibu: Inaruhusiwa kuhiji na kufanya Umra kwa niaba ya Muislamu aliyefariki, au kwa niaba ya Muislamu aliye hai ambaye hawezi kuzitekeleza yeye mwenyewe; kwa sababu ya uzee au maradhi yasiyotarajiwa kupona. Pia inaruhusiwa kumfanyia mtu tendo la kurusha vijiwe kwenye Jamarat ikiwa hawezi kujirushia mwenyewe, kama vile mtoto mdogo, mgonjwa au mtu mzee, ikiwa yule anayemwakilisha ni mmoja wa mahujaji katika mwaka huo na tayari mwenyewe ameshajirushia vijiwe.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/76)
***
Swali: Muislamu alikufa katika nchi ya Kiislamu isiyokuwa Ufalme wa Saudi Arabia, na alikuwa hajahiji, na pia Hija ilikuwa tayari imeshakuwa wajibu kwake. Je, ninaruhusiwa kuhiji kwa niaba yake kutokea katika Ufalme wa Saudi Arabia kwa vile ninaishi huku? Na je, kuna tofauti kati ya malipo ya kuhiji kutokea nchi ya mbali au ya karibu?
Jibu: Unaruhusiwa kuhiji kutokea katika Ufalme wa Saudi Arabia kwa niaba ya Muislamu yeyote aliyefariki katika nchi yake au kwingineko, sawa sawa iwe alihiji au hapana, na tofauti ya umbali uliotajwa haina athari yoyote, bali malipo yatakuwa kwa mujibu wa ikhlasi, gharama, tabu na kufanyia hima mambo ya kisheria.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/77)
***
Swali: Mtu anayehiji kwa malipo kwa niaba ya maiti; Iwe ni mwanamume au mwanamke, au kwa niaba ya mtu asiyeweza kufanya Hija au Umra kwa sababu ya uzee au ugonjwa usiotarajiwa kupona, je, mtu huyu anayelipwa atapata thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu?
Jibu: Mwenye kuhiji au kufanya Umra kwa niaba ya mtu mwingine, kwa malipo au bila malipo, malipo ya Hija na Umra hiyo yanamfikia yule aliyeifanya kwa niaba yake, naye aliyeifanya pia anatarajiwa kupata malipo makubwa kulingana na ikhlasi yake na hima yake juu ya mambo ya kheri. Yeyote anayeufikia Msikiti Mtukufu na akafanyia humo ibada nyingi za hiari na mambo mbalimbali ya kumuweka karibu na Mwenyezi Mungu, basi anatarajiwa kupata kheri nyingi ikiwa atamkusudia Mwenyezi Mungu peke yake kwa matendo hayo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/77)
***
Swali: Mtu anaishi Afrika na anataka kumteuwa mtu mwingine kuhiji kwa niaba ya mama yake. Je, amlipe malipo ya mtu anayehiji kutokea Afrika kwenda Makka Tukufu? Na je, anaruhusiwa kuyapunguza malipo hayo?
Jibu: Mtu aliyetajwa hapo juu anaweza kumteua mtu kutoka Makka au kwingineko ambaye ni mwaminifu ili ahiji kwa niaba ya mama yake ikiwa amefariki au hawezi kuhiji mwenyewe; kwa sababu ya uzee au ugonjwa usiotarajiwa kupona, kwa malipo kidogo au mengi au bila malipo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/80)
***
Swali: Baba yangu alifariki bila ya kufanya faradhi ya kuhiji, na nikaelewa kuwa ilikuwa ni wajibu kwangu kuhiji kwa niaba yake. Hivyo basi, nilikubaliana na mtu amhijie, lakini aliponiuliza kuhusu jina la baba yangu na jina la mama yake aliyekufa, hatukujua majina yao. Je, jina la baba yangu linatosheleza badala ya jina la mama yake?
Jibu: Kumfanyia mtu Hija huwa tu kwa kuweka nia kwa niaba yake, na si lazima kutaja jina la mtu ambaye anafanyiwa Hija, si jina lake tu, wala jina lake na jina la baba yake au mama yake. Hata hivyo, ikiwa atatamka jina lake wakati wa kuhirimia, au wakati wa talbiya, au wakati wa kuchinja mnyama wa dhabihu ikiwa anafanya Hija ya Tamattu au ya Qiran, basi hilo pia ni zuri. Hilo ni kwa mujibu wa yale aliyosimulia Abuu Daud, na bin Majah na bin Hibban kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, ya kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimsikia mwanamume mmoja akisema: ‘Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa niaba ya Shubruma.’ Akasema: "Ni nani huyo Shubruma?’ Akasema: ‘Ni kaka yangu au jamaa yangu.’ Akasema: "Je, wewe mwenyewe ulishahiji?" Akasema: ‘Hapana.’ Akasema: "Jihijie, kisha uhiji kwa niaba ya Shubruma."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/81)
***
Swali: Mwanaume mmoja mwenye umri wa miaka 25 alifariki bila ya kuhiji. Je, tunaruhusiwa kuhiji kwa niaba yake. Na je, Hija tu inatosha bila ya kufanya Umra pamoja na kwamba ana mali?
Jibu: Iwapo mtu atatakiwa kuhiji na akafa kabla ya kuhiji, basi kitatolewa kutoka katika mali yake kiwango kinachotosha kutumiwa kuhiji na kufanya Umra kwa niaba yake. Pia inaruhusiwa kuhiji kwa niaba yake bila ya kutumia mali yake yoyote ikiwa atapata mtu wa kujitolea kumfanyia Hija. Ama Hija hiyo inajulikana kuwa ni moja ya nguzo za Uislamu, na haiwezi kuanguka kwa kifo cha yule ambaye ni wajibu kwake. Imam Bukhari, Mwenyezi Mungu amrehemu, alipokea katika Sahihi yake kwamba: “Mwanamke mmoja wa kutoka Juhaiyna alikuja kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na akasema: “Mama yangu aliweka nadhiri ya kuhiji, lakini hakuhiji mpaka akafa. Je, nihiji kwa niaba yake?” Akasema: "Ndiyo, hiji kwa niaba yake. Unaonaje ikiwa mama yako alikuwa na deni, je ungemlipia? Lipeni deni la Mwenyezi Mungu, kwani Mwenyezi Mungu anastahili zaidi kulipwa kikamilifu." Pia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, aliulizwa na mwanamke mmoja wa kutoka Khath'am: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika faradhi ya Mwenyezi Mungu juu ya waja wake katika Hija imemfikia baba yangu huku ni mzee ambaye hawezi kukaa imara juu ya kipando chake. Je, nifanye Hija kwa niaba yake?" Akasema: "Fanya Hija kwa niaba ya baba yako." Ama Umra, hiyo ni kwa sababu ya yale yaliyosimuliwa na wale wapokezi watano kutoka kwa Abu Razin Al-Uqaili kwamba alikuja kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Hakika baba yangu ni mzee ambaye hawezi kuhiji, kufanya Umra wala kusafiri juu ya kipando." Akasema: “Fanya Hija na Umra kwa niaba ya baba yako.”
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/87)
***
Swali: Je, mwanamke wa Kiislamu anaruhusiwa kuhiji pamoja na wanawake waaminifu, ikiwa hawezi kumchukua pamoja naye jamaa yake, au ikiwa baba yake alifariki? Je, mama yake anaruhusiwa kwenda pamoja naye ili kutekeleza faradhi hii ya Hija, au mama yake mdogo, au shangazi yake au mtu yeyote anayemchagua kuwa maharimu wake?
Jibu: Mtazamo sahihi ni kwamba haruhusiwi kusafiri kwa ajili ya Hija isipokuwa pamoja na mume wake au maharimu wa kiume. Hivyo basi, haruhusiwi kusafiri pamoja na wanawake waaminifu au wanaume waaminifu ambao si maharimu wake, au pamoja na shangazi yake, au mama yake mdogo, au mama yake mzazi. Bali ni lazima awe pamoja na mumewe au maharimu wa kiume. Ikiwa hataweza kumpata mmoja wao, basi Hija haiwi lazima kwake maadamu hii ndiyo hali yake. Hili ni kwa sababu hajatimiza sharti la kuwa na uwezo wa kisheria. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Walillaahi ‘alannaasi hijjul-bayti manistatwaa’a ilayhi sabiilan (Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezaye njia ya kuiendea)." (Suratul-Baqara: 97)
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/91)
***
Swali: Je, ni wajibu kwa mwanamke kuhiji ikiwa hawezi kumpata wa kuhiji pamoja naye kama vile mume wake au maharimu ilhali yeye mwenyewe ana uwezo wa kufanya Hija, au ikiwa yuko katika eda ya kufiwa na mumewe?
Jibu: Si wajibu kwa mwanamke kuhiji ikiwa hawezi kumpata maharimu wa kusafiri pamoja naye kwenda huko, na wala haruhusiwi kwenda kuhiji huku bado yuko katika eda ya kufiwa mumewe.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/94)
***
Swali: Mwanamke mmoja alihiji Hija ya faradhi bila ya maharimu lakini pamoja na kundi la wanawake wema. Je, hilo lilimuondolea ulazima wa kufanya Hija ya faradhi?
Jibu: Ikiwa hali halisi ni kama ilivyotajwa, basi Hija yake ni sahihi na hilo linamuondolea ulazima wa kufanya Hija ya faradhi, lakini anapata dhambi ya kusafiri bila maharimu, na inamlazimu atubie kwa Mwenyezi Mungu na kuomba msamaha.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/97)
***
Swali: Alikufa mwanamume mmoja bila ya kuhiji, na aliacha wosia kwamba ahijiwe kutoka katika mali yake, na waulizwe wanazuoni ikiwa Hija hiyo ni sahihi. Na je, Hija anayoifanya mtu mwingine ni sawa na ile anayojifanyia mtu mwenyewe?
Jibu: Iwapo Muislamu atafariki kabla ya kutekeleza wajibu wa Hija, na ametimiza masharti ya ulazima wa faradhi ya Hija, basi ni lazima ifanywe Hija kwa niaba yake kutoka katika mali yake aliyoiacha, sawa awe alitoa wosia lifanyike hilo au hapana. Hivyo, ikiwa mtu atafanya Hija kwa niaba yake, naye akawa alishajifanyia Hija ya faradhi, basi Hija ya yule anayemfanyia inakuwa sahihi na itatosheleza katika kumuondoshea ulazima wa kuhiji. Na ama kulinganisha Hija ya mtu mwenyewe ikiwa ni sawa na Hija anayofanyiwa na mtu mwingine au iko chini yake au juu yake kwa fadhila, hilo linamrudia Mwenyezi Mungu aliyetakasika, na hapana shaka kwamba la wajibu juu yake ni aharakishe kuhiji ikiwa ataweza kabla ya kufa. Hili ni kwa sababu ya ushahidi wa kisheria unaoonyesha hilo, na anahofiwa akichelewesha, atapata dhambi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/100)
***
Swali: Ikiwa mtu atabishana na baadhi ya marafiki zake wakati wa Hija, je, Hija yake hiyo itamtosheleza hata kama ni Hija ya faradhi?
Jibu: Hija yake ni sahihi, na inamtosheleza Hija ya faradhi, lakini malipo yake yatapunguzwa kwa kiasi cha kubishana kubaya alikofanya, na pia inamlazimu atubie kwa hilo. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Watuubuu ilallaahi jamii’an ayyuhal-mu-uminuuna la’allakum tuflihuun (Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa)." (Surat An-Nur: 31)
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/112)
***
Fatwa za Miqat (stesheni za kuhirimia Hija au Umra)
Swali: Je, inaruhusika kuhirimia kutokea huko Jeddah?
Jibu: Jeddah si Miqat ya Hija wala Umra isipokuwa kwa wale walio na makazi huko huko au wale wanaokaa tu huko kwa muda. Pia mwenye kufika huko kwa sababu ya haja fulani bila ya kukusudia kuhiji au kufanya Umra, kisha wakaamua kuhiji au kufanya Umra. Ama wale walio na Miqat yao kabla yake, kama vile Dhul-Hulaifa kwa watu wa Madina na wote waliyo nyuma yake, au wale walio kiwango sawa nayo kwenye nchi kavu au angani, na kama vile al-Juhfah kwa watu wake na wote walio kiwango sawa nayo anayewiana nayo kwenye nchi kavu au baharini au alipita hapo angani, na vivyo hivyo Yalamlam, basi inamlazimu kuhirimia katika Miqati yake au eneo lililo katika kiwango sawa nayo angani, baharini au kwenye nchi kavu.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/130)
***
Swali: Mwenye kuhiji anapotaka kuhirimia na akataka kujipaka manukato, je, ajipake manukato kabla ya kuoga au baada ya kuoga kwa ajili ya ihramu?
Jibu: Iwapo mtu anayetaka kuhiji au kufanya Umra anataka kutumia manukato wakati wa kuingia katika Ihram kabla ya kuhirimia Hija au Umra, basi anaweza kufanya hivyo, na ni bora zaidi iwe baada ya kuoga. Aisha, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, alisema: “Nilikuwa nikimtia manukato Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, kwa ajili ya Ihramu yake kabla ya kuingia katika Ihraamu, na kwa ajili ya kutoka katika ihramu kabla ya kuzunguka Nyumba". Bukhari na Muslim wamekubaliana kwamba ni Hadithi sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/168)
***
Swali: Kwa nini Mwenyezi Mungu aliwakataza mahujaji kuvaa nguo zilizoshonwa, na kuna hekima gani katika hilo?
Jibu: Kwanza: Mwenyezi Mungu ameifanya Hija kuwa lazima kwa mwenye uwezo wa kufanya hivyo, mara moja katika maisha, na akaifanya kuwa moja ya nguzo za Uislamu, kama inavyojulikana katika dini bila shaka yoyote. Basi ni juu ya Muislamu kutekeleza yale ambayo Mwenyezi Mungu alimfaradhishia ili kumridhisha Mwenyezi Mungu na kutii amri yake, kwa kutaraji malipo yake na kuogopa adhabu yake, kwa yakini kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye hekima katika sheria zake na vitendo vyake vyote, na ni mwenye huruma kwa waja wake. Kwa hivyo hawawekei sheria isipokuwa yenye masilahi kwao na yale yanayowaletea manufaa ya jumla duniani na akhera. Ni kwa Mola wetu Mlezi, Mfalme, Mwenye hekima, utakatifu ni wake, kuweka sheria, na ni juu ya mja kuitekeleza na kujisalimisha kwayo.
Pili: Kuna hekima nyingi kuhusiana na kuamrisha kutovaa nguo za kawaida zilizoshonwa wakati wa Hija na Umra, zikiwemo: kukumbuka hali za watu Siku ya Kiyama, kwani watafufuliwa Siku ya Kiyama wakiwa peku na uchi, kisha watavalishwa nguo. Kuna somo na mawaidha katika kukumbuka hali za Akhera, ikiwa ni pamoja na kuitisha nafsi na kuifanya kuhisi wajibu wa kunyenyekea na kuitakasa kutokana na uchafu wa kiburi. Pia miongoni mwa hekima zake ni kuifahamisha nafsi kanuni ya ukaribu wa Waislamu, usawa, ugumu, na kujiepusha na anasa za kuchukiza, na kuwahurumia masikini na mafukara... na malengo mengine ya Hija kwa utaratibu uliowekwa na Mwenyezi Mungu na kuelezwa na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/179)
***
Swali: Kwa nini mahujaji huvaa nguo hizo wakati wa Hija?
Jibu: Mwenyezi Mungu alituamrisha, kupitia ulimi wa Mtume Wake Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, kuvaa kikoi na shuka wakati wa Hija na Umra kwa sababu anayoijua Yeye, hivyo ni lazima tuitii, tukitaraji malipo, sawa sawa tujue hekima au tusijue. Miongoni mwa yale waliyoyataja wanachuoni kuhusu hili ni kuwakumbusha watu hali ya Siku ya Mkutano na Ufufuo Siku ya Kiyama, na kumfanya mwenye kuhiji ajisikie kuwa mnyenyekevu na kuwepo usawa baina ya tajiri na masikini. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atujaalie sisi na nyinyi tufanikiwe, tuongoke, na tuwe imara katika haki mpaka tukutane naye.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/171)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya Hija ya mwenye hedhi?
Jibu: Hedhi haimzuii mwanamke kuhiji. Ikiwa mwanamke aliye katika hedhi atahirimia, basi atekeleze ibada ya Hija, isipokuwa kuizunguka Nyumba tukufu isipokuwa hedhi yake itakapokatika na akaoga. Vile vile mwanamke mwenye damu ya baada ya kuzaa. Ikiwa atatekeleza nguzo za Hija, basi Hija yake ni sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/172)
***
Swali: Mwanamke mmoja alikwenda hapa katika Ufalme wa Saudi Arabia kuhiji kisha akapata hedhi kabla ya kufanya Tawafu al-Qudum (tawafu ya kuingia Makka). Ni ipi hukumu yake? Na je, anaweza kwenda Arafa wakati wa hedhi yake, na ni ipi hukumu ya hilo?
Jibu: Atabakia katika ihramu yake na atafanya kila anachofanya mwenye kuhiji, isipokuwa kuizunguka Nyumba tukufu mpaka asafike kwa kukatika damu ya hedhi, na akaoga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/173)
***
Swali: Je, anaruhusiwa mwanamume kukaa na kukata kucha zake anapoingia kwenye ihramu kwenye Miqat, au hairuhusiwi kufanya hivyo mpaka atakapochinja mnyama wa dhabihu?
Jibu: Akifanya hivyo kabla ya kuhirimia, basi hakuna ubaya katika hilo, isipokuwa ikiwa alitaka kuchinja mnyama wa dhabihu na mwezi wa Hija ukawa tayari umeshaanza, basi katika hali hiyo hataruhusiwa kufanya hivyo. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikataza kufanya hivyo. Ama kufanya hivyo baada ya kuhirimia, hilo haliruhusiwi kabisa. Kwa sababu mtu aliyehirimia Hija au Umra haruhusiwi kukata kucha zake au kupunguza chochote katika nywele zake mpaka atakapomaliza tawafu na sa’yi yake ya Umra. Hapo atatoka katika ihramu yake kwa kunyoa au kupunguza nywele zake. Na vile vile katika Hija, atakaporusha vijiwe kwenye Jamratul-‘Aqaba, basi ataruhusiwa kunyoa nywele zake au kuzipunguza, ila kuzinyoa ni bora zaidi. Kisha atatoka katika ihramu sawa sawa hilo liwe kabla au baada ya kuchinja mnyama wa dhabihu ila akifanya hivyo baada ya kuchinja ndiyo bora zaidi, ikiwa itawezekana.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/178)
***
Swali: Baba yangu alihiji mwaka jana, lakini alikuwa mgonjwa sana na hakuweza kuvaa nguo za ihramu. Je, wajibu wake ni upi?
Jibu: Mwenye kuhiji akiingia kwenye ihram akiwa amevaa nguo zake za kawaida kwa sababu anahitaji kufanya hivyo kutokana na baridi, maradhi na mfano wa hayo, basi anaruhusiwa kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria ya Kiislamu. Hapo, la wajibu juu yake kuhusiana na kuvaa nguo za kawaida zilizoshonwa ni kufunga siku tatu, au kulisha masikini sita, kila masikini apewe nusu ya kibaba cha chakula kikuu cha nchi hiyo, au kuchinja kondoo anayetosha kuchinjwa katika dhabihu wa Idi. Vivyo hivyo itakuwa hukumu ikiwa atafunika kichwa chake. Na kufunga kunamtosheleza mahali popote atakapofungia. Ama kulisha na kuchinja kondoo, hayo mahala pake ni kwenye Msikiti Mtakatifu ulioko Makka.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/180)
***
Swali: Hakika mimi ninataka sana kuhiji, Mwenyezi Mungu akipenda, lakini tatizo langu ni kwamba mimi ni mwanamume mwenye kipara, na ngozi yangu ni nyeti sana, na miale yoyote ya jua huathiri afya yangu, na kusababisha uvimbe mkubwa katika ngozi ya kichwa, na kuonekana kwa mishipa ya kichwa hasa kwenye uso kwa ujumla. Na kama unavyojua, miongoni mwa makatazo ya ihramu kwa mwanamume ni kufunika kichwa. Basi ninawaomba enyi waheshimiwa mnitolee fatwa kuhusiana na hali hii na vile vile mjue kwamba mimi ni mwanamume mfupi na siwezi kubeba mwavuli; kwa sababu inawadhuru wale walio karibu nami. Ni hayo tu, na Mwenyezi Mungu akulindeni na akuongozeni sawasawa katika hatua zenu.
Jibu: Ikiwa jambo ni kama ilivyotajwa, basi utafunika kichwa chako ukiwa katika hali ya Ihramu, na utatoa fidia kwa kuchinja kondoo na kuwalisha masikini wa huko Makka, au kuwalisha masikini sita katika eneo takatifu la Makka (Haram), kila masikini utampa nusu ya kibaba cha tende au chakula kingine kikuu cha nchi hiyo, au ufunge siku tatu. Hili linahusiana kuhirimia Hija. Ama ukihirimia Umra, basi utalazimika kulipa fidia nyingine.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/181)
***
Swali: Hujaji alifanya tendo lililoharamishwa, ambalo lilikuwa ni kumbusu mke wake na kumwaga manii nje ya uke kwa matamanio baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamarat al-Aqaba na kunyoa kichwa chake, lakini kabla ya kufanya Tawaf al-Ifadhwa. Huyo mkewe hakuwa anafanya Hija. Tafadhalini tupeni ushauri, na Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Hairuhusiwi kwa Muislamu ambaye amehirimia Hija au Umra au vyote viwili kufanya chochote kitakachoharibu ihram yake au kupunguza matendo yake. Kubusu ni haramu kwa mtu aliyehirimia Hija mpaka atoke kikamilifu katika ihram yake. Hilo huwa kwa kurusha vijiwe kwenye Jamarat al-Aqaba, kunyoa nywele za kichwa au kuzipunguza, kufanya Tawaful-ifadhwa, kufanya sa'yi ikiwa analazimika kufanya sa’yi. Kwa sababu bado yuko katika hukumu ya Ihram, ambayo humfanya kuharamishiwa wanawake. Hata hivyo, haiharibiki Hija ya mtu ambaye alimbusu mke wake na akashusha manii baada ya kutoka kwa kwanza katika ihramu, lakini analazimika kumuomba Mwenyezi Mungu msamaha na wala asifanye mfano wa kitendo hicho tena. Atafidia hilo kwa kuchinja kondoo anayeweza kutosha kuchinjwa kama dhabihu wa Idi kisha amgawanye kwa masikini wa eneo takatifu la Makka. Na la wajibu kwake ni aharakishe kufanya hivyo kiasi iwezekanavyo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/188)
***
Swali: Nilitekeleza wajibu wa kuhiji, na usiku mmoja nikiwa Mina, nililala na sikuweza kuoga. Je, ninalazimika kufanya chochote?
Jibu: Kushusha manii usingizini kwa mtu ambaye yuko katika hali ya ihramu ya Hija au Umra hakuathiri Hija yake au Umra. Haviwezi kubatilika kwa hilo. Kwa hivyo, atakayepatwa na hilo, basi atatakiwa kuoga kama vile anavyooga kwa kwa ajili ya janaba baada ya kuamka kutoka usingizini ikiwa ataona alama za manii, na hatalazimika kutoa fidia yoyote. Kwa sababu kushusha manii usingizini sio hiari yako.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/188)
***
Swali: Je, njiwa wa Makka na Madina wana sifa zozote maalumu?
Jibu: Hakuna sifa yoyote maalumu kwa njiwa wa Makka au Madina, isipokuwa kwamba hawawindwi wala hawaogopeshwi maadamu wako ndani ya mipaka ya eneo takatifu. Hili ni kwa ujumla wa Hadithi kwamba: “Hakika Mwenyezi Mungu ameifanya Makkah kuwa ni takatifu, na wala haikuwahi kuwa halali kwa yeyote kabla yangu, na haitawahi kuwa halali kwa yeyote baada yangu. Na ilihalalishwa kwa ajili yangu kwa muda wa masaa kadhaa tu ya mchana. Kwa hivyo, zising'olewe nyasi zake, wala isikatwe miti yake wala visiogopeshwe viwindo vyake. Hadithi hii imepokelewa na Bukhari. Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: “Hakika Ibrahim aliifanya Makka kuwa takatifu, nami hakika niliifanya Madina kuwa takatifu, na chochote kilichoko baina ya pande zake mbili zenye mawe na udongo mweusi. Isikatwe miti yake wala visiwindwe viwindo vyake." Imepokelewa na Muslim.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/202)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kuvua nguo za Ihramu baada ya kufanya Umra, ikiwa mimi ni katika wale wanoafanya Umra kisha wakaishi maisha ya kawaida kabla ya kufanya Hija mwaka huo huo (Mutamati’)?
Jibu: Inaruhusiwa kwa mtu anayehiji Hija ya Tamattu’ kutoka katika hali ya ihram baada ya kufanya Umra, kama vile kutufu, kufanya sa'yi, kunyoa au kupunguza nywele, na kuvaa nguo zake za kawaida, kama vile Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alivyowaamrisha Maswahaba wake kufanya hivyo, wale ambao hawakuwa wameleta wanyama wao wa dhabihu pamoja nao katika Hija ya Kuaga. Kisha inapofika siku ya nane, ahirimie Hija?
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/202)
***
Swali: Tafadhali niambieni ni mambo gani ambayo yanaruhusiwa kwa hujaji anayefanya Hija ya Tamattu’ wakati wa kutoka kwake katika Ihramu baada ya kufanya Umra?
Jibu: Mwenye kuhirimia Hija ya Tamattu', kisha akafanya ibada za Umra yake kama vile kuzunguka Kaaba, sa'yi, kunyoa au kupunguza nywele, basi atakuwa ameshatoka katika Umra yake na anaruhusiwa kufanya yale aliyoharamishiwa wakati wa Ihraamu, kama vile kunyoa, kukata kucha, kuvaa nguo za kawaida zilizoshonwa, kufunika kichwa, kupaka manukato, kuwinda mawindo ya nchi kavu, kufunga ndoa, kuingiliana na wanawake na yote yanayosababisha hilo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/204)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya Talbiya ya pamoja ya mahujaji? Ambapo mmoja wao anaanza kisha wengine wanarudia nyuma yake?
Jibu: Hilo haliruhusiwi. Kwa sababu haikupokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wala kutoka kwa Makhalifa wake waongofu, Mwenyezi Mungu awawie radhi, bali ni uzushi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/358)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya mwanamke anayepata hedhi wakati wa Hija? Je, atatekeleza ibada zote za Hija na je anatakiwa kuoga kwa ajili ya hilo? Au kuna ibada ambazo hawezi kufanya na atawezaje kuzilipiza? Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Mwanamke akipata hedhi huku amekusudia kuhiji, atahirimia na asalie katika ihramu yake na afanye anayoyafanya hujaji, kama vile kusimama Arafa, kulala Muzdalifa na Mina usiku, na kurusha vijiwe kwenye Jamarat, isipokuwa haruhusiwi kuizunguka Nyumba tukufu mpaka asafike na aoge.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/128)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwanamke kujipamba wakati wa kuhiji?
Jibu: Mwanamke haruhusiwi kuwa na pupa ya kuvaa mapambo wakati wa kufanya ibada za Hija, lakini ni lazima afunike mapambo yoyote au hina anayopaka wasiyaone wanaume, na wala hatakiwi kuyatoa mkononi kwake au kwenye sehemu nyinginezo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/144)
Swali: Nilihiji, na baada ya kuhirimia kwenye Miqati huku ninafanya Hija peke yake, nilisema: “Labbaykallahumma labbayk (Nimekuitikia ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia)." Baada ya hayo, nikasahau na nikasema: “Nimekuitikia ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa ajili ya Hija na Umra." Niambieni - Mwenyezi Mungu akulipeni heri - kuhusu kile kinachonipasa.
Jibu: Iwapo hicho ulichofanya cha kutamka ni kuteleza kwa ulimi ambacho hukukikusudia, basi hakuna ubaya wowote juu yako. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Rabbanaa laa tu-aakhidhnaa in nasiinaa aw akhtwa-anaa (Mola wetu Mlezi! Usituchukulie ubaya tukisahau au tukikosea)." (Suratul-Baqara: 286) Na amesema Mtume, rehema na amani zimshukie: "Hakika matendo ni kulingana na nia tu, na kila mtu atalipwa kulingana na kile alichokusudia."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/132)
***
Swali: Niliona baadhi ya mahujaji wakikata miswaki kutoka kwenye matawi ya miti na kuitumia kupiga mswaki. Ni ipi hukumu ya kukata miti huko Mina, na nini hukumu ya kukubali zawadi ya mswaki uliokatwa kutoka kwenye miti ya eneo takatifu la Makka (Al-Haram)?
Jibu: Hairuhusiwi kukata mti wowote wa eneo takatifu la Makka, si kwa mwenye kuhiji wala kwa mtu mwingine yeyote. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Haikatwi miti yake ya miba yake, wala haing'olewi miti yake." Imepokelewa na Muslim.
Basi yeyote anayefanya jambo kama hilo ni lazima atubu kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na asilifanye tena. Pia hairuhusiwi kuchukua zawadi ya mswaki ikiwa ulikatwa kutoka katika miti ya eneo takatifu la Makka; kwa sababu hilo ni kukiri na kusaidia katika yale yaliyokatazwa.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/166)
***
Kulala usiku huko Mina
Swali: Nilikwenda Hija kwa kampuni inayowapeleka watu Hija na tukalala huko Mina katika usiku wa tisa wa Dhul-Hijja, kisha tukaondoka hapo kuelekea Arafa kabla ya swala ya Alfajiri, ambapo tuliswalia huko swala ya Alfajiri kwa maana waandaaji wa kampuni hiyo walifanya hivi kwa kuogopa msongamano. Je, kuna chochote juu yetu?
Jibu: Hakuna chochote juu yenu, lakini ni bora kwa mwenye kuhiji kutoka Mina kwenda Arafa baada ya jua kuchomoza katika siku ya tisa ya mwezi wa Dhul-Hijja.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/210)
***
Swali: Nilihiji katika kampuni inayowapeleka watu Hija ya hapa ndani na malazi yetu yalikuwa nje ya Mina. Nililala katika usiku wa tarehe 9 Dhul-Hijja mahali hapo, lakini katika usiku wa siku za Tashriq nililala ndani ya Mina. Je, ni wajibu kulala usiku wa tarehe 9 Mina au ni Sunna? Na kama ni wajibu, basi nifanye nini? Mwenyezi Mungu akulipeni heri kwa niaba yangu, na kwa niaba ya Uislamu na Waislamu.
Jibu: Kulala huko Mina katika usiku wa tisa wa Dhul-Hijja kunapendekezwa kwa mwenye kuhiji, lakini si wajibu. Hivyo basi, hakuna chochote juu yako kwa sababu ya kutolala usiku huko, lakini ulikosa malipo ya kulala huko usiku.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/177)
***
Kusimama Arafa
Swali: Baadhi ya watu wanasema: Siku ya Arafa ikikutana na siku ya Ijumaa, kama vile mwaka huu, basi ni kama mtu amehiji mara saba. Je, kuna ushahidi wowote kutoka katika sunna juu ya hili?
Jibu: Hakuna ushahidi wowote sahihi kwa hilo. Baadhi ya watu wamedai tu kuwa ni sawa na Hija sabini, au Hija sabini na mbili, lakini hilo pia si sahihi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/211)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwenye kuhiji - baada ya kuswali swala ya Adhuhuri na Alasiri pamoja na imamu huko Arafa - kuswali swala za hiari mpaka kuzama kwa jua?
Jibu: Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, hakuswali swala ya hiari siku ya Arafa baada ya swala yake ya Adhuhuri na Alasiri huko Arafa. Lau hilo lingekuwa katika sheria, basi angelipupia zaidi kuliko sisi. Na heri yote kabisa ni katika kufuata mfano wake na sunna zake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/211)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya aliyetoka Arafa dakika moja kabla ya muda uliowekwa kwa ajili ya swala ya Magharib, kwa muda ulioandikwa kwenye kalenda, huku akijua kuwa abiria wa gari walisema kwamba jua lilikuwa limeshazama?
Jibu: Kanuni ya msingi ni kwamba mwenye kuhiji atasalia Arafa siku ya tisa, na hataondoka mpaka ahakikishe kuwa jua limeshazama. Haruhusiwi kutoka huko kabla ya hapo, kwa hivyo mazingatio ni kuzama kwa jua. Ikiwa alitoka huko baada ya kuwa na yakini ya kwamba jua limeshazama, basi amefanya lile lililotakiwa kwake na hakuna kitu juu yake katika hilo. Na ikiwa alitoka huko kabla ya kuzama kwa jua au hakuwa na yakini na hilo na hakurejea huko na kukaa huko mpaka kuzama kwa jua, au hakurudi huko hata kwa muda mfupi katika usiku, basi analazimika kuchinja kondoo; kwa sababu ya kuacha wajibu miongoni mwa wajibu za Hija.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/181)
***
Kulala usiku huko Muzdalifa
Swali: Nilihiji pamoja na familia ambazo zilikodi gari kutoka kwangu kwa ajili ya Hija katika usiku wa kwenda Arafa tulishukia huko Arafa saa tatu asubuhi, na tukafika Muzdalifa saa mbili usiku. Kwa kisingizio kwamba walikuwa pamoja na familia, na kwamba sheria iliwaruhusu kufanya hivyo, wakakataa kulala usiku huko Muzdalifa. Hatukuwa tumekaa Muzdalifa zaidi ya robo saa. Je, kuna chochote kinachonilazimu kutokana na hilo?
Jibu: Ikiwa hali yao ni kama ulivyotaja, kwamba wana familia pamoja nao ambao wanahofia kudhurika kwa kulala mpaka Alfajiri, basi hakuna kosa juu yako wewe au wao ikiwa mlitoka Muzdalifa saa nane usiku kulingana na majira ya kupinduka jua. Kwa sababu hilo lilikuwa baada ya usiku wa manane, na wameruhusiwa wanyonge na wanawake kufanya hivyo kwa kuwahurumia.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/212)
***
Swali: Kwa sababu ya msongamano mkubwa wa watu wakati wa Hija ya mwaka jana, baadhi ya mahujaji hawakuweza kulala usiku huko Muzdalifa kutokana na ugumu wa kufika huko, na hata baadhi yao walipotea njia ya kwenda huko. Kwa hivyo wafanye nini?
Jibu: Iwapo mtu hawezi kulala usiku huko Muzdalifa kwa sababu ya msongamano, basi hatakiwi kulala huko. Hata hivyo, ikiwa mtu atapotea njia ya kwenda huko na akalala mahali pengine, basi inamlazimu atoe kafara ya kuchinja kondoo. Kwa sababu anaweza kuuliza kuhusu palipo Muzdalifa na akaonyeshwa njia yake sahihi ya kufika huko. Hivyo basi huyo alipuuza wajibu kwa kutouliza juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/189)
***
Swali: Muulizaji anauliza kuhusu mtu ambaye amehiji kwenye Nyumba tukufu, kwamba alihama kutoka Muzdalifa karibia theluthi ya kwanza ya usiku, yaani karibia saa nne usiku, na udhuru wake ni kwamba alikuwa pamoja na wanawake. Basi ni nini kinachotakiwa kwake na wao, Mwenyezi Mungu akulipeni heri?
Jibu: Yeyote anayetoka Muzdalifa kabla ya saa sita usiku bila ya udhuru wa kisheria, kama vile ugonjwa, basi anakuwa hajatimiza wajibu wa kulala huko usiku na inamlazimu alipe fidia ya kuchinja kondoo huko Makka, ambaye anatosha kuwa dhabihu wa siku ya Idi. Kisha aigawe kwa masikini wa huko. Kwa sababu kiwango cha chini zaidi kinachohitajika kukaa huko usiku ni hadi usiku wa manane. Kwa sababu Mtume, rehema na amani zimshukie, hakuwaruhusu wanyonge kuondoka Muzdalifa isipokuwa baada ya saa sita usiku.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/194)
***
Matendo ya siku ya kuchinja
Swali: Iwapo watu na wale walio wanyonge wataondoka Muzdalifa kwenda Mina kabla ya Alfajiri ya siku ya kuchinja (siku ya Idi) lakini baada ya usiku wa manane, je wanaweza kurusha vijiwe kwenye Jamratul-Aqaba kabla ya Alfajiri kuingia? Na pia ikiwa wana muda wa kutosha kufanya Tawaful-Ifadhwa kabla ya Alfajiri kuingia, je wanaruhusiwa kufanya hivyo?
Jibu: Inaruhusiwa kwa wanawake dhaifu, wazee na wengineo kama wao kuondoka Muzdalifa baada ya usiku wa manane, na wanaruhusiwa kupiga vijiwe kwenye Jamarat, kufanya Tawaful-Ifadhwa na wanyoe nywele kabla ya Alfajiri kuingia. Kwa sababu hilo ndilo rahisi zaidi kwao.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/190)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwenye kuhiji kuchelewesha kurusha vijiwe kwenye Jamrat al-Aqaba (nguzo ya kwanza) mpaka siku ya pili au ya tatu ya Tashriq bila ya udhuru au hapana, na ni ipi hukumu ya mwenye kufanya hivyo?
Jibu: Hairuhusiwi kwa mwenye kuhiji kuchelewesha kurusha vijiwe kwenye Jamrat al-Aqaba mpaka siku ya pili au ya tatu ya Tashriq bila ya udhuru. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, aliirushia vijiwe katika siku ya Idi, na Maswahaba wake wakamfuata katika hilo na hawakuchelewesha mpaka siku za Tashriq bila ya udhuru. Alisema Mtume, rehma na amani zimshukie: "Chukueni ibada zenu za Hija kutoka kwangu." Atakayelichelewesha hilo mpaka siku za Tashriq bila ya udhuru, atakuwa ameenda kinyume na sunna na atanyimwa baadhi ya malipo ya ibada yake ya Hija, pia itamlazimu aombe msamaha kwa Mwenyezi Mungu kwa yale yaliyopita na apupie kutekeleza ibada yake ya Hija kwa njia ya kisheria katika siku zijazo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/217)
***
Swali: Tuliona wakati wa Hija baadhi ya watu wanapofupisha nywele zao kwa ajili ya Hija au Umra, wanazipunguza tu kutokea chini ya kichwa kwa umbo la duara, wakipita juu juu kutokea pande zote. Ama sehemu zilizosalia, hawakupunguza chochote kwazo. Tulipowaambia kwamba kufupisha ni lazima kufanyike kwenye sehemu zote za kichwa, walituambia: "Hilo ndilo linalohitajika. Basi ni kitendo gani kinachotakiwa?
Jibu: La wajibu ni kunyoa au kupunguza kichwa kizima wakati wa Hija au Umra, lakini si wajibu kupunguza kila moja ya nywele yenyewe. Na hicho alichokifanya huyo uliyemtaja hakitoshelezi kwa mujibu wa maoni sahihi zaidi ya wanachuoni, na wala si katika sunna ya Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/217)
***
Swali: Hujaji mmoja alisimama Arafa, akalala Muzdalifa, na akafika Mina asubuhi ya siku ya Idi. Akarusha vijiwe kwenye Jamrat Al-aqaba, akachinja dhabihu wake na akanyolea nywele zake huko Mina. Kisha baada ya hapo akaenda Makkah na akafanya Tawaf al-Ifadhwah? Je, hayo yanaruhusiwa kisheria? Hili ni kwa sababu mfanyakazi mmoja aliniambia kwamba hairuhusiwi kunyoa au kuvulia nguo za Ihramu huko Mina isipokuwa baada ya kufanya Tawaful-Ifadhwa.
Jibu: Inaruhusiwa kunyoa nywele kabla na baada ya Tawaful-Ifadhwa. Na hayo uliyoyafanya siku ya Idi ya kurusha vijiwe kwenye Jamrat kisha kuchinja, kisha kunyoa, kisha kufanya Tawafu, ni Sunna, na ndivyo alivyofanya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika Hija yake ya Kuaga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/218)
***
Swali: Tawaful-Ifadhwa inaisha wakati gani?
Jibu: Tawaful-Ifadhwa huanza baada ya usiku wa manane wa usiku wa kuchinja (Idi) kwa wale walio wanyonge na walio mfano wao. Hakuna muda maalumu wa mwisho wake, lakini ni bora zaidi kwa mwenye kuhiji kuharakisha kufanya Tawaful-Ifadhwa kiasi awezavyo, huku akifanya hima kujifanyia upole, na pia anafaa kuangalia nyakati ambazo sehemu ya kuzungukia Kaaba haina msongamano; ili asiwaudhi watu wala asiudhiwe.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/227)
***
Swali: Iwapo hujaji atafanya Tawaful-Ifadhwa na akasahau mojawapo ya mizunguko na akakosa kujua hilo mpaka baada ya kutoka katika Msikiti Mtukufu, ni nini hukumu ya hilo? Na ikiwa atajua hilo baada ya kujivua kutoka katika ihramu kwa mara ya kwanza, ikijengeka juu ya ukweli kwamba mzunguko huu ni mojawapo ya yale mambo mawili ambayo humfanya mtu kutoka katika ihramu yake kwa mara ya kwanza.
Jibu: Iwapo hujaji atafanya Tawaful-Ifadhwa na akasahau mojawapo ya mizunguko, na ukapita muda mrefu, basi ni lazima arudie Tawafu yote. Lakini ikiwa muda uliopita ni mfupi, basi ataufanya mzunguko huo aliousahau peke yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/253)
***
Swali: Ni nini hukumu ya mtu aliyefanya Tawaful-Ifadhwa na hakufanya Sa’yi mpaka kuzama kwa jua, baada ya siku ya mwisho ya Tashriq? Ni nini hukumu ya sa’yi yake ikiwa ataifanya baada ya kuzama kwa jua siku hiyo, au baada ya siku za Tashriq?
Jibu: Kufanya kwako Sa’yi katika siku za mwisho za Tashriq au baada ya siku za Tashriq ni sahihi, na hakuna kosa juu yako kuichelewesha. Kwa sababu sio katika masharti yake kwamba iunganishwe na kuzunguka Kaaba, lakini ili kuifanya iwe kamili ni vyema iwe baada ya kuzunguka Kaaba huku imeunganishwa na hilo; kwa kumfuata Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/262)
***
Swali: Je, ni wajibu kunyoa au kupunguza nywele za mtu katika kujitoa kukubwa katika ihramu baada ya kunyoa au kupunguza nywele katika kujitoa kudogo katika ihramu, yaani baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamaraat?
Jibu: Si wajibu wala haipendekezwi kunyoa au kupunguza nywele baada ya kujitoa kukubwa katika ihramu baada ya kunyoa au kupunguza nywele katika kujitoa kudogo katika ihramu, yaani baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamaraat. Kwa sababu hilo ni katika matendo ya Hija kwa hivyo ni ibada, na ibada zote zimejengeka juu ya wahyi. Haikuthibiti kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alinyoa au kupunguza nywele zake baada ya kujitoa kukubwa katika ihramu. Bali alifanya hivyo tu wakati wa kujitoa katika ihramu kudogo. Imethibiti kuwa alisema: "Chukueni ibada zenu za Hija kutoka kwangu."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/263)
***
Swali: Nilifanya ibada za Umra, na baada ya kuzitekeleza nikarudi katika mji wangu (bila kufanya Hija). Na kwa vile nimekusudia, Mwenyezi Mungu akipenda, kuhiji mwaka huu, je, ni lazima nitoe fidia au hapana? Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Wanachuoni wengi wanaona kwamba si lazima kutoa kafara. Kwa sababu hukujumuisha kati ya Umra na Hija katika safari moja, kama ulivyotaja kwamba ulirejea katika nchi yako baada ya kufanya Umra katika mwezi wa Shawwal ya mwaka wa 1395 Hijria, na hukukaa Makka ili ufanye Hija.
Na baadhi ya wanachuoni wanaona kwamba ni lazima utoe mnyama wa kuchinjwa Makka kama utahiji katika mwaka wako huu, hata kama ulirudi katika nchi yako au nchi iliyo mbali zaidi nayo. Kwa ujumla wa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "....Faman tamatta’a bil-‘umrati ilalhajji, famastaysara minalhadyi (basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra kisha ndiyo akahiji, basi achinje mnyama aliye mwepesi kumpata)." (Suratul-Baqara: 196). Hata hivyo, fatwa na matendo sahihi ni kulingana na maoini ya walio wengi miongoni mwa maulamaa kwamba kutoa kafara si wajibu katika suala hili.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/366)
***
Swali: Ni nini hukumu ya mtu aliyesahau kupunguza nywele zake baada ya kumaliza ibada ya Hija na hakukumbuka hilo mpaka muda mrefu baadaye?
Jibu: Kunyoa au kupunguza nywele za kichwa ni ibada ya faradhi katika Hija na Umra. Ikiwa mtu atasahau kufanya hivyo, basi ni lazima anyoe au apunguze nywele zake atakapokumbuka. Na ikiwa atafanya tendo la ndoa kabla ya kunyoa au kupunguza, basi ni lazima alipe fidia kwa ajili ya kujamiiana huko, nayo ni kondoo anayetosha kuchinjwa katika Idi. Atachinjwa Makka na wagawiwe masikini wa eneo takatifu la Makka. Kwa sababu katika Hija alikuwa hajamaliza kujitoa katika ihramu kwa mara ya kwanza, na kujamiiana kabla yake kunamlazimu mtu kutoa fidia, na vivyo hivyo katika Umra, anakuwa bado hajamaliza kujitoa katika ihramu kwa mara ya kwanza.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/204)
***
Swali: Iwapo hujaji atafanya tawafu ya kufika Makka, je inamlazimu tena kufanya tawaful-ifadhwa?
Jibu: Tawaful-Qudum haichukui nafasi ya Tawaful-Ifadhwa kwa hujaji anayefanya Hija na Umra bila kutenganisha (Qarin) au yule anayefanya Hija peke yake (Ifrad). Kwa sababu huu sio wakati wa Tawafu ya Ifadha. Kwa maana Tawaful-Ifadhwa ni moja ya nguzo za Hija, na haikamiliki bila ya hiyo, na wakati wake ni baada ya kusimama Arafa na kutoka Muzdalifa. Ama tawaful-qudum, hiyo ni sunna, akitaka anaifanya, na akitaka, anaweza kuiacha.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/217)
***
Swali: Je, ninaruhusiwa nimteuwe mtu wa kufanya Tawaful-Ifadhwa na Tawaf ya kuaga kwa niaba yangu ikiwa siwezi kurejea Makkah al-Mukarramah kutokana na uzee wangu na afya mbaya?
Jibu: Hairuhusiwi kumteua mtu kukufanyia tawaful-ifadhwa wala tawafu ya kuaga. Mtu ambaye hawezi kuifanya ataifanya huku amebebwa. Hivyo basi, ni lazima uje Makka kama ilivyotajwa kwenye fatwa hii, na Mwenyezi Mungu ndiye Muwezeshaji. Na rehema na amani ziwe juu ya Nabii wetu Muhammad, familia yake, na Maswahaba wake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/271)
***
Siku za Tashriq na kurusha vijiwe
Swali: Je, afanye nini mtu aliyerusha vijiwe asubuhi ya siku ya pili ya Idi, kisha akajua baadaye kuwa wakati wa kuvirusha ni baada ya Adhuhuri?
Jibu: Mwenye kurusha vijiwe siku ya pili ya Idul-Adh-ha kabla ya jua kupita katikati ya mbingu, basi analazimika kuvirusha baada ya jua kupita katikati ya mbingu siku hiyo. Ikiwa hatajua kosa lake mpaka siku ya tatu au ya nne, basi atarudia kuvirusha baada ya Adhuhuri ya siku ya tatu au ya nne baada ya jua kupita katikati ya mbingu, kabla ya kurusha vijiwe vya siku hiyo aliyokumbuka ndani yake. Na ikiwa hatajua mpaka baada ya kuzama kwa jua katika siku ya nne, basi na asirushe, na inamlazimu kuchinja kondoo huko Makka na awagawiye masikini wake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/273)
***
Swali: Ni nini maana ya kauli yake Mola Mtukufu: "Kwa hivyo, mwenye kufanya haraka katika siku mbili (akarejea), basi si dhambi juu yake.?” Pia ninaomba ufafanuzi wa kile ambacho Aya hii inaeleza.
Jibu: Mwenyezi Mungu aliyetakasika anasema: "Wadhkurullaha fii ayyaamim ma’aduudaat. Faman ta’ajjala fii yawmayni falaa ithma ‘alayhi waman ta-akhkhara falaa ithma ‘alayhi limanittaqaa (Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika zile siku zinazohisabiwa. Lakini mwenye kufanya haraka katika siku mbili (akarejea), si dhambi juu yake; na mwenye kukawia, pia si dhambi juu yake, kwa mwenye kumcha Mungu)." (Suratul-Baqara: 203) Hadi mwisho wa Aya. Hadi mwisho wa Aya. Maana ya "siku zinazohesabiwa" hapa ni zile siku tatu za Tashriq: siku ya kumi na moja, ya kumi na mbili, na ya kumi na tatu. Basi yeyote katika mahujaji atakayetoka baada ya kurusha vijiwe siku ya kumi na mbili baada ya Adhuhuri na kabla ya kuzama kwa jua, atakuwa ameharakisha. Na atakayebaki Mina mpaka akatupa vijiwe siku ya kumi na tatu, basi atakuwa amechelewa, na hilo ndilo bora kwa sababu linaafikiana na matendo ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/297)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kurusha vijiwe asubuhi kabla ya adhuhuri ya siku ya pili, au kuvirusha baada ya adhuhuri pamoja na kuvirusha kwa ajili ya siku inayofuata?
Jibu: Kurusha vijiwe katika siku za Tashriq hakufai ila baada ya jua kupita katikati ya mbingu, na hairuhusiwi wala haitoshelezi kufanya hivyo asubuhi. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, hakurusha vijiwe isipokuwa baada ya jua kupita katikati ya mbingu, na akasema: "Chukueni ibada zenu za Hija kutoka kwangu." Atakayekosa kurusha vijiwe siku moja, basi na avirushe siku inayofuata baada ya Adhuhuri, na anaanza na siku iliyompita kabla ya kurusha vijiwe vya siku inayofuata. Kisha atarudi baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamrat ya mwisho na kurusha vijiwe kwenye Jamarat zote tatu kwa ajili ya siku ya pili.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/189)
***
Swali: Nilihiji mwaka mmoja na kurusha vijiwe siku ya pili kabla ya Adhuhuri. Je, kuna chochote juu yangu ukishajua kwamba sikuwa na elimu ya hilo.
Jibu: Kurusha vijiwe kwenye Jamarat kabla ya Adhuhuri katika siku za Tashriq si sahihi. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, hakurusha vijiwe isipokuwa mpaka baada ya Adhuhuri na akasema: "Chukueni ibada zenu za Hija kutoka kwangu." Kwa hivyo, ni lazima ulipe fidia kwa sababu ya kurusha vijiwe kabla ya Adhuhuri, ambayo ni kuchinja kondoo anayetosha kuwa dhabihu wa Idi, utamchinjia huko Makka na kuwagawia masikini wa eneo takatifu la Makka (Al-Haram), lakini usile chochote kutoka kwake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/293)
***
Swali: Kuna mtu alisahau akabeba kijiwe cha kurusha kwenye Jamaraat alichochukua huko Mina, na akaambiwa kwamba yeyote anayechukua kijiwe Mina inamlazimu akirudishe Makka. Tufafanulieni suala hili.
Jibu: Ikiwa mtu atasalia na kijiwe cha kurusha kwenye Jamaraat, hatakiwi kukirudisha Mina, kwani hakuna ushahidi wa kuunga mkono hilo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/294)
***
Swali: Mtu mmoja alirusha vijiwe saba kwenye Jamarat Al-Aqaba wakati wa Hija kwa mrusho mmoja.
Jibu: Yeyote anayerusha vijiwe kwenye Jamarat kwa mrusho mmoja inamlazimu arushe vijiwe hivyo tena ndani ya siku zake. Kwa sababu ni wajibu kuvitupa kimoja baada ya kingine, na kuvitupa vyote kwa pamoja ni sawa na kurusha kijiwe kimoja. Kwa hivyo, ikiwa hatarudia kurusha, basi itamlazimu achinje mnyama kwa ajili ya hilo kwa sababu aliacha wajibu miongoni mwa wajibu za Hija. Naye ni kondoo anayetosheleza kuchinjwa siku ya Idi, na atachinjiwa Makka kisha agawiwe masikini wa eneo takatifu la Makka. Kama hataweza, basi na afunge siku kumi, sawa sawa zifuatane au zitengane.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/310)
***
Swali: Mama yangu mdogo alihiji mwaka jana, lakini alipotupa vijiwe, alisema kwamba wakati alipotupa, hakuweza kuona mahali ambapo vijiwe hivyo vilianguka kwa sababu ya msongamano wa watu. Je, vilianguka ndani ya hodhi la hapo au hapana? Hili ni pamoja na ukweli kwamba wakati mwingine alikuwa akiiona Jamrat wakati alipokuwa anarusha vijiwe hivyo. Tafadhali tushaurini, Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Moja ya masharti ya usahihi wa kurusha vijiwe ni kuhakikisha kwamba vinaanguka ndani ya hodhi vinamotupwa. Kwa hivyo, ikiwa ana uhakika kwamba vilianguka ndani ya hodhi hiyo wakati wa kuvirusha kisha akawa na shaka baada ya hapo, basi shaka hiyo haina athari, na kurusha kwake ni sahihi. Na ikiwa alipata shaka na hana uhakika kwamba kijiwe hicho kilianguka ndani ya hodhi, basi analazimika kutoa fidia kwa kuchinja kondoo ambaye atawagawia masikini wa eneo takatifu la Makka, na kama hawezi hilo, basi na afunge siku kumi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/311)
***
Swali: Baadhi ya mahujaji - Mwenyezi Mungu awaongoze - wanazirushia Jamarat chochote wanachokipata, kama vile viatu, chupa tupu za maji na vitu vinginevyo. Je, hili linabatilisha kurusha kwao kwa sababu ya hiki wanachokifanya, au hawachukuliwi makosa kwa sababu ya ujinga wao?
Jibu: Hairuhusiwi kurushia Jamarat viatu, chupa au mfano wa vitu hivi. Kwa sababu hilo haliko katika sheria, na tena linapingana na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake. Kwani, yeye alizirushia Jamarat vijiwe ambavyo ni vikubwa kidogo kuliko mbaazi, na akasema: "Chukueni ibada zenu za Hija kutoka kwangu." Kwa hivyo, wanapata dhambi kwa kufanya hivi, na mwenye kuwaona, anapaswa kuwakataza na kuwanasihi, lakini kitendo chao hiki hakibatilishi kurusha, ikiwa walirusha vijiwe vinavyoruhusiwa kisheria.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/324)
***
Swali: Ni ipi hukumu ya watu waliohiji, na zilipofika siku za Tashriq, wakataka kuharakisha na kuzitupia Jamarat tatu vijiwe katika siku ya kwanza na siku ya pili vile vile, kisha wakaenda Makka moja kwa moja kabla ya kuzama kwa jua siku ya pili, na wakalala huko usiku na hawakutupa vijiwe kwenye Jamarat katika siku ya tatu. Je, inawalazimu kuchinja kondoo au hapana?
Jibu: Mwenye kuzirushia Jamarat tatu vijiwe katika siku ya kumi na mbili ya Dhul-Hijja na akataka kuharakisha, basi aondoke Mina kabla ya kuzama kwa jua, na wala si lazima azitupie hizo Jamarat tatu vijiwe katika siku ya kumi na tatu, sawa sawa atakaa Makkah baada ya hapo au kwingineko.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/335)
***
Tawafu ya Kuaga
Swali: Ninaishi Jedda kwa muda na huwa ninaenda Makka tukufu mara kwa mara. Je, niiage Nyumba Tukufu baada ya Hija, au nicheleweshe mpaka wakati wa safari ya kwenda katika mji wangu? Je, kuna kafara ya kuchelewesha kuaga Nyumba tukufu?
Jibu: Ukihiji, usisafiri kwenda Jeddah baada ya Hija yako mpaka utekeleze tawafu ya kuaga. Na ukisafiri kabla ya tawafu ya kuaga, basi inakulazimu uchinjie mnyama huko kwenye Msikiti Mtukufu, lakini usile hata kidogo kwaye. Bali utawalisha masikini wa huko. Kwa sababu tawafu ya kuaga ni wajibu baada ya Hija; kwa ujumla wa Hadithi ya bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili: "Watu waliamrishwa kwamba jambo lao la mwisho Makka liwe ni kuzunguka Nyumba tukufu, isipokuwa wanawake wenye hedhi walirahisishiwa katika hilo." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi. Pia inakulazimu utubu kwa Mwenyezi Mungu kwa kuondoka kwenda Jeddah kabla ya kufanya tawafu ya kuaga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/303)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kwa mwenye kuhiji aende Taif katika masiku ya Mina kisha arejee kuaga baada ya siku ishirini kupita?
Jibu: Hairuhusiwi kwa aliyehiji Nyumba tukufu kusafiri mpaka akamilishe ibada za Hija ikiwemo tawafu ya kuaga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/307)
***
Swali: Je, wanawake walio katika hedhi na wenye damu ya baada ya kujifungua wanatakiwa kufanya tawafu ya kuaga, na vile vile walemavu na wagonjwa?
Jibu: Mwenye hedhi au mwenye kutokwa na damu ya baada ya kuzaa si lazima afanye tawafu ya kuaga. Ama asiye na uwezo, huyo atafanyishwa tawafu huku amebebwa, na vile vile mgonjwa. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Asitoke yeyote miongoni mwenu mpaka liwe jambo lake la mwisho ni kuzunguka Nyumba tukufu.” Na kwa yale yaliyothibiti katika Sahihi mbili kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: "Watu waliamrishwa kwamba jambo lao la mwisho Makka liwe ni kuzunguka Nyumba tukufu, isipokuwa wanawake wenye hedhi walirahisishiwa katika hilo." Kuna Hadithi nyingine inayoonyesha kuwa mwanamke anayetokwa na damu ya baada ya kuzaa ni sawa na mwanamke mwenye hedhi. Yeye pia halazimiki kufanya tawafu ya kuaga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/307)
***
Swali: Wakati wa kufanya tawafu ya kuaga, niliugua na nikaacha kufanya tawafu hiyo, lakini jamaa zangu waliosalia walimaliza kufanya tawafu hiyo. Walipomaliza, nilienda na mmoja wao kukamilisha mzunguko wangu uliosalia, lakini nikasahau mzunguko mmoja katika tawafu hiyo ya kuaga, na sikujua hilo isipokuwa baada ya kurudi katika nchi yangu. Je kuna fidia juu yangu au kitu chochote?
Jibu: Ikiwa una uhakika kwamba uliacha mzunguko katika tawafu ya kuaga, basi unalazimika ulipe fidia, ambayo ni kuchinja kondoo huko Makka kama kafara na kuwagawia masikini wa eneo takatifu la Makka. Na kama huwezi kulipa fidia, basi funga siku kumi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/126)
***
Swali: Nilihiji, na katika siku ya pili ya Tashriq nikafanya tawafu ya kuaga baada ya Alasiri, lakini nikakaa Makkah tukuku na sikusafiri kwenda Taif hadi asubuhi iliyofuata. Tafadhali nishaurini, je, tawafu yangu ya kuaga niliyoifanya mimi na familia yangu inatosha, au ninalazimika kutoa kafara, au ninalazimika kurudia tawafu yangu? Ninaomba unishauri, Mwenyezi Mungu akulipeni heri.
Jibu: Iwapo mtu atafanya tawafu ya kuaga kwa ajili ya Hija kisha akakaa Makka kwa muda mfupi baada ya tawafu, basi halazimiki kuirudia. Ama ikiwa atakaa muda mrefu baada ya tawafu ya kuaga, basi inamlazimu arudie tawafu hiyo. Na maadamu mlifanya tawafu ya kuaga baada ya swala ya Alasiri na hukusafiri isipokuwa asubuhi ya siku iliyofuata, na mkawa mlisafiri bila kurudia tawafu ya kuaga, basi kila mmoja wenu analazimika kuchinja mnyama anayetosha kuwa dhabihu wa Idi. Atamchinjia huko Makka na awagawie masikini wa eneo takatifu la Makka. Hata hivyo, ikiwa kulikuwa na mwanamke mwenye hedhi au mwenye damu ya baada ya kuzaa, basi hao hawalazimiki kufanya tawafu ya kuaga.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/337)
***
Swali: Mke wangu alihiji mwaka jana. Hija yake hiyo ilikuwa Hija ya tamattu (kujistarehesha baada ya Umra kabla ya kufanya Hija). Alifanya ibada zote za Hija isipokuwa tawafu ya kuaga kwa sababu alipatwa na damu ya hedhi. Baba yangu alimpeleka kwenye Msikiti Mtakatifu na akamwingiza humo. Akaangalia Kaaba tukufu. Ni nini hukumu ya hilo. Nielezeeni, Mwenyezi Mungu Mtukufu akulipeni heri.
Jibu: Tawafu ya kuaga haimlazimu mwanamke mwenye hedhi na wala hakuna chochote juu ya mke wako. Haya ni kwa sababu ya yale yaliyothibiti kwamba bin Abbas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisema kuwa: "Watu waliamrishwa kwamba jambo lao la mwisho Makka liwe ni kuzunguka Nyumba tukufu, isipokuwa wanawake wenye hedhi walirahisishiwa katika hilo." Na pia yale yaliyosimuliwa kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: "Safia binti Huyayyi alipata hedhi baada ya kumaliza Tawaful-Ifadhwah. Akasema: Basi nikamtajia hilo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Atatuzuia?" Nikasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, alikuwa ameshakamilisha Tawaful-Ifadhwa kisha akapata hedhi baada ya kumaliza Tawaful-Ifadhwa." Akasema: "Basi na aondoke."
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/342)
***
Swali: Iwapo mtu ataingia Makka bila ya kufanya Umra au Hija na akataka kutoka humo, je, anatakiwa kufanya tawafu ya kuaga? Na ikiwa mtu aliyefanya Umra atakaa siku moja au mbili au kitu kama hicho, je, kuna kitu kinachoitwa tawafu ya kuaga kilichosimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, au kila tawafu inaweza kuwa tawafu ya kuaga atakapotoka Makka baada ya hapo? Tafadhalini tushaurini, Mwenyezi Mungu akulipeni heri na asikunyimeni Pepo. Amin.
Jibu: Tawafu ya kuaga ni wajibu kwa mwenye kuhiji ikiwa anataka kusafiri kutoka Makka baada ya Hija. Kwa mujibu wa Hadithi ya bin Abbas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, amesema kwamba: "Watu waliamrishwa kwamba jambo lao ya mwisho Makka liwe ni kuzunguka Nyumba Tukufu, isipokuwa wanawake wenye hedhi, wao walirahisishiwa katika hilo." Hadithi hii wamekubaliana Bukhari na Muslim kwamba ni sahihi. Na mwanamke mwenye damu ya baada ya kuzaa ni hukumu hii hii. Ama mtu asiyekuwa hujaji, basi yeye halazimiki kulingana na kauli sahihi zaidi kufanya tawafu ya kuaga. Kwa sababu Mtume, rehema na amani zimshukie, hakuwaamrisha watu wanaofanya Umra kufanya hivyo. Kisha tawafu ya kuaga inamhitaji mtu kuweka nia, kwa sababu ni ibada na tendo. Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Hakika matendo yote hulipwa kulingana na nia, na kila mtu atalipwa kulingana na kile alichokusudia." Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/344)
***
Swali: Je, inaruhusiwa kununua baadhi ya mahitaji baada ya tawafu ya kuaga? Na mwenye kununua kitu baada ya tawafu ya kuaga, je kinamlazimu kitu chochote?
Jibu: La wajibu ni kwamba tawafu ya kuaga iwe ndiyo jambo la mwisho analofanya hujaji katika matendo ya Hija yake, kisha aondoke Makka baada ya hapo. Hata hivyo, ikiwa atasalia kwa muda mfupi kuwasubiri wenzake, kubeba vitu vyake, au kununua baadhi ya mahitaji yake, basi hakuna ubaya juu yake.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/345)
***
Swali: Mwanamume mmoja miongoni mwa mahujaji alifanya tawafu ya kuaga siku ya kumi na mbili, kisha akaenda Mina na kurusha vijiwe kwenye Jamarat. Je, tawafu yake ni sahihi ambapo alifanya tawafu kabla ya kurusha vijiwe? Basi mtu huyu afanye nini, naye ni katika watu wa Jeddah?
Jibu: Iwapo mtu atafanya tawafu ya kuaga kabla ya kurusha vijiwe, hilo halitoshelezi. Kwa sababu tawafu ya kuaga ndiyo kitu cha mwisho katika Hija. Na kwa kuwa alisafiri kabla ya kurudia tawafu ya kuaga baada ya kurusha vijiwe, bas inamlazimu achinje fidia huko Makka na kuwagawia masikini wa eneo takatifu la Makka, na asile chochote kwayo, na pia kichinjo hicho hakitoshelezi isipokuwa kiwe kama kile kinachochinjwa siku ya Idi. Hata hivyo, akishindwa kufanya hivyo, basi na afunge siku kumi.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/345)
***
Swali: Maji ya Zamzam yameelezwa kuwa yana sifa mahususi nyingi. Je, kuna Hadithi sahihi juu ya suala hili?
Jibu: Maji ya Zamzam ndiyo maji matukufu zaidi duniani, na riwaya iliyo sahihi zaidi kuhusu fadhila zake ni ile iliyothibiti katika Sahihi Muslim, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema kuhusu Zamzam: "Hakika yamebarikiwa na ni chakula kitamu." Abu Daud aliongeza kwa mlolongo sahihi wa wapokezaji: "Na ni uponyaji kwa ugonjwa." Imepokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Maji ya Zamzam huwa kwa kile yalichonywewa kwa ajili yake." Imepokelewa na Imam Ahmad, Ibn Majah na wengineo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Pili (10/168)
***
Fatwa zinazohusiana na kuzuru Madina
Swali: Nikiwa na nia ya kufanya Umra katika Ramadhani - Mwenyezi Mungu akipenda - na kuzuru mji wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, mnanielekeza nifanye nini?
Jibu: Inaruhusiwa kisheria kusafiri kwenda kuzuru Msikiti wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na si kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, au kaburi lolote lile. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Hazifungwi safari isipokuwa kwenda kwenye misikiti mitatu: Msikiti wangu huu, Msikiti Mtakatifu na Msikiti wa Al-Aqsa.” Lakini inaruhusiwa kwa mwenye kuzuru Msikiti wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kumsalimia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na Maswahaba zake wawili: Abu Bakar na Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao. Pia anaruhusiwa kuzuru makaburi ya Al-Baqi’ na mashahidi wa huko Uhud na kuwaombea dua, na kuwaombea rehema na kuwaswalia, kukumbuka mauti na yaliyo baada yake. Pia anaruhusiwa kwenda katika msikiti wa Quba na kuswali ndani yake. Hayo ni kwa mujibu wa Hadithi ambazo zimeripotiwa kuhusiana na hayo.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/78)
***
Swali: Je, mahujaji, wanaume na wanawake wanatakiwa kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, Al-Baqi’, Uhud na Quba, au ni wanaume tu?
Jibu: Mahujaji, wanaume au wanawake hawalazimiki kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wala Al-Baqi’. Bali ni haramu kabisa kusafiri kwa ajili ya kuzuru makaburi. Pia ni haramu kwa wanawake kufanya hivyo, hata bila ya kufunga safari. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Hazifungwi safari isipokuwa kwenda kwenye misikiti mitatu: Msikiti wangu huu, Msikiti Mtakatifu na Msikiti wa Al-Aqsa.” Hadithi hii wamekubaliana juu yake Bukhari na Muslim kwamba ni sahihi. Kwa sababu yeye, rehema na amani zimshukie, aliwalaani wanawake wanaozuru makaburi. Hivyo basi, inawatosha wanawake kuswalia tu katika Msikiti wa Mtume na kuzidisha kumuombea rehema Mtume wanapokuwa msikitini na kwingineko.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Kundi la Kwanza (11/362)
***
Swali: Nina kaka ambaye huwatembeza mahujaji na wafanyao Umra wanapotujia Madina. Yeye huwapeleka kwenye maeneo ambayo baadhi yake hayaruhusiwi kisheria, kisha anachukua malipo ya kifedha waliyokubaliana. Je, kazi yake hii inaruhusiwa kisheria?
Jibu: Kazi hii anayoifanya kaka yako ya kuwapeleka mahujaji na wafanyao Umra katika maeneo ya mjini ambayo hayaruhusiwi kuzuru, ni kazi iliyoharamishwa, na mali anayochukua kama malipo yake kwa hilo ni pato la haramu. Hivyo basi inakupasa kumshauri aache kazi hii.
Fatwa za Kamati ya Kudumu - Mukhtasari wa Kundi la Pili (10/390).
***