مخالفات الحج والعمرة والزيارة

مخالفات الحج والعمرة والزيارة

MAKOSA YANAYOFANYIKA KATIKA HIJA, UMRAH NA KUTEMBELEA MSIKITI WA MTUME

Language: lang_sw
Prepared by: Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Kuhudumia Maudhui za Kiislamu kwa Lugha Mbalimbali.
Version: 3.0
Translations 35
Amharic Assamese Bambara Bengali +31
Attachments 7
PDF
Audio
Video
+3

MAKOSA YANAYOFANYIKA KATIKA HIJA, UMRAH NA KUTEMBELEA MSIKITI WA MTUME

Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Kuhudumia Maudhui za Kiislamu kwa Lugha Mbalimbali.

Makosa na ukiukaji unaohusiana na Umra

Kwanza: Ukiukaji wa watu na makosa yao katika Ihram

1. Kuacha kufanya ihlaal, kwa kutoinua juu sauti yake mwanzoni mwa kuhirimia ibada aliyokusudia sawa iwe Hija au Umra.

Na Sunna: Ni kunyanyua sauti katika hilo.

2. Baadhi ya watu wanadhani kuwa Ihram ni vazi la Hija au Umra, yaani shuka na kikoi.

Ihram ni nia ya kuingia katika ibada ya Hija au Umra, na alama yake ni kuinua juu sauti wakati wa kufanya mwitikio (Talbiya). Kwa hivyo, mwenye kuinua juu sauti yake wakati anafanya mwitikio (Talbiya), huku amenuia Hija au Umra, basi atakuwa ameshahirimia.

3. Baadhi ya watu wanadhani kuwa ni wajibu kuoga kwa ajili ya ihramu.

Ni Sunna kufanya hivyo, na mwenye kuliacha, basi hakuna ubaya wowote juu yake.

4. Baadhi ya watu wanadhani kuwa ni wajibu kuswali rakaa mbili wakati wa kuingia kwenye ihram, au kwamba ni Sunna maalum ambayo lazima itekelezwe, hivyo wanaziswali kwa vyovyote vile.

Mtazamo sahihi ni kwamba inaruhusiwa kuswali kabla ya kuingia katika ihramu, lakini hakuna swala maalumu kwa ajili yake. Kwa hivyo, ikiwa ataswali swala ya faradhi au swala nyingine yoyote ile iliyo katika sheria, basi anaruhusiwa kuingia katika ihramu baada yake.

5. Baadhi ya watu wanadhani kuwa ni wajibu kusimama kwenye Miqat na kushuka msikitini.

Hili si jambo la faradhi, ikiwa mtu alikwishavaa vazi la ihram na akapita karibu na Miqat na akafanyia hapo Talbiyah au kwenye sehemu iliyo kiwango sawa na hapo huku yuko ndani ya gari lake, basi hilo litamtosheleza, kama vile mtu aliye ndani ya ndege anavyofanya Talbiyah anapofika kwenye Miqat au kwenye kiwango kilicho sawa nayo au hata kabla yake kidogo ili asiivuke Miqat.

6. Kupaka manukato katika mavazi ya ihram.

Jambo sahihi ni kuyapaka kwenye mwili tu.

7. Baadhi ya watu wanaona kuwa ni wajibu kunyoa nywele za sehemu ya siri, kupunguza kucha, na kunyoa makwapa wakati wa kuingia kwenye ihram, au wanadhani kuwa hii ni Sunna ya ihram.

Hayo yote ni Sunna ya ujumla inapohitajika wakati wowote.

8. Kuingia katika Ihram kabla ya kufika kwenye Miqat.

Hili ni kinyume na Sunna, lakini mtu aliye ndani ya ndege anaweza kuhirimia mapema kidogo ili asikosee sehemu iliyo sambamba na Miqat kwa sababu ya kasi kubwa ya ndege.

9. Mtu anayekusudia kufanya Hija au Umra kupita Miqat bila ya kuingia katika hali ya Ihramu, ima kwa ujinga, uzembe au kwa sababu yuko kwenye ndege.

Iwapo atavuka Miqat akiwa anataka kufanya Umra au Hija na wala hakuhirimia Miqat, basi ni lazima arudi kwenye Miqat na ahirimie kutokea huko. Vile vile mwenye kutua kwenye uwanja wa Ndege wa Jeddah na akawa hakuhirimia alipokuwa katika ndege kutokana na sababu yoyote ile, basi analazimika aende kwenye moja ya Miqat ili ahirimie kutokea huko. Anatolewa katika hukumu hii yule ambaye hapitii kwenye Miqat yoyote wala hafiki kwenye kiwango kilicho sambamba na Miqat, huyo atahirimia huko Jeddah, kama vile watu wa Sudan wanapofika hapo kwa ndege au meli. Isipokuwa ikiwa watajua kuwa wanapita kwenye Miqat ya Yalamlam au Miqat ya Al-Juhfah kwenye njia waliyopitia.

10. Kutokuelewa maana ya nguo zilizoshonwa kwa kufikiria kwamba ni kila kitu chenye uzi, basi mtu akaona ugumu kuvaa mkanda au kiatu ambacho kimeshonwa kwa uzi.

Hii si sahihi. Nguo zilizoshonwa ni chochote kilichoshonwa ili kivaliwe kwenye mwili mzima, kama vile nguo na suruali ikiwa zitavaliwa kwa njia yake ya kawaida.

11. Mwanamke kuvaa glovu, barakoa, nikabu au pazia kamili.

La wajibu kwake - ikiwa yuko mbele ya wanaume wasio maharimu wake - ni kwamba ajifunike uso na mikono yake kwa kitu kisichokuwa nikabu na glovu. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikataza kuvaa vitu hivyo kwa mwanamke aliye katika ihramu.

12. Baadhi ya watu hufikiri kuwa wanawake wana vazi maalumu kwa ajili ya ihram, ima jeusi, kijani kibichi au jeupe.

Hili si sahihi. Mwanamke aliye katika Ihramu anaweza kuvaa nguo yoyote anayotaka, bila ya kuonyesha mapambo yake.

13. Baadhi ya watu wanadhani kuwa hairuhusiwi kubadili au kuvua nguo ya ihramu.

Mtazamo sahihi ni kwamba mtu aliye katika Ihramu anaruhusiwa kubadilisha au kuiosha nguo yake kisha akaivaa tena.

Kuvaa lubega (Idhtwibaa') kuanzia mwanzo wa ihram hadi mwisho.

Mtazamo sahihi ni kwamba kuvaa lubega (idhtwibaa’) kumewekwa tu katika tawafu ya Umra au tawafu ya kufika Makka peke yake.

Kuivunja na kutoka katika ihramu bila ya sababu za kisheria za kufanya hivyo.

La wajibu kwa mtu aliyehirimia Hija au Umra ni abakie katika hali yake ya ihram mpaka amalize ibada zake, isipokuwa ikiwa atapata sababu ya kisheria ya kutoka ndani yake, ambayo ni kuzuiliwa. Basi katika hali hii, anaruhusiwa kutoka katika ihramu. Kama wakati alipoingia katika ihram aliweka sharti la kutoka katika ihramu, basi anaruhusiwa kutoka katika ihramu na hakuna ubaya wowote juu yake. Na kama hakuweka sharti, basi atalazimika kuchinja kondoo, kunyoa nywele au kuzipunguza kisha atatoka katika ihramu yake.

***

Pili: Ukiukaji wa watu na makosa yao wakati wa Tawafu

1. Kushikamana na dua ambazo hazikusimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wakati wa kuingia katika Msikiti Mtakatifu au wakati mtu anapoiona Al-Kaaba.

Sunna ni kusema yale yaliyokuja kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake tu.

2. Kutamka nia kabla ya kuanza Tawafu.

Nia mahali pake ni moyoni, kwa hivyo hairuhusiwi kuitamka.

3. Kufanya hima kubwa kuanzia tawafu kabla ya Jiwe Jeusi, ili kuchukua tahadhari kubwa ya kutoanzia mbele yake.

Huku ni kuwa na msimamo mkali na kuvuka kiwango bila haja ya kufanya hivyo.

4. Kuanzia tawafu baada ya kupita Jiwe Jeusi, na kuchukulia hilo kuwa ni mzunguko mzima.

Hili ni kosa, na mwenye kufanya hivyo, basi asihesabu mzunguko huo.

5. Kuinua mikono wakati mtu unapolingana na Jiwe Jeusi kama anavyoiinua katika swala, au kurudia kuinua mikono mara tatu.

Sunna ni kuliashiria Jiwe Jeusi kwa mkono wake wa kulia mara moja tu.

6. Kusimama kwa muda mrefu wakati mtu anapofika usawa wa Jiwe Jeusi.

Sunna sio kurefusha kisimamo.

7. Kuleta msongamano mkubwa ili kulifikia Jiwe Jeusi ili kulibusu.

Sunna sio kuleta msongamano. Akiweza kulifikia bila ya kuleta msongamano, basi na afanye. Vinginevyo, aliashirie tu kwa mkono.

8. Mtu kurudi nyuma ikiwa alipita kwenye Jiwe Jeusi bila na kusema Allah Akbaru (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa); ili aliashirie na atoe takabira, au mtu kutoa takbira baada ya kulipita.

Yote haya ni makosa, kwani hiyo ni Sunna ambayo umeshapita wakati wake, na haipendekezwi kurejea ili kuifanya, na hakuna ubaya kwa mwenye kusahau Takbira au aliyeiacha kwa makusudi.

9. Kuuwekea kila mzunguko dua maalumu.

Hakuna ushahidi kwa hili, bali Sunna ni kwamba mtu anayefanya tawafu aombe kwa chochote anachopenda katika mambo ya kheri ya dunia na Akhera [1], na amtaje Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa utajo wowote unaokubalika kisheria, kama vile kumtakasa (Tasbihi), kumsifu (himdi), kusema: Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu (tahliil), kumtukuza, au kusoma Qur’ani.

10. Kwenda kwa kasi kubwa (Ar-Ramal) katika mizunguko yote.

Sunna ni kwamba aende kwa kasi kubwa katika mizunguko mitatu ya mwanzo tu.

11. Kutoiweka Al-Kaaba upande wake wa kushoto wakati wa kufanya tawafu bila ya udhuru.

Sunna ni kuwa Al-Kaaba iwe upande wake wa kushoto. Kwa hivyo, asizembee kwa kwenda kinyume na hilo. Lakini ikiwa ana udhuru kwa sababu ya msongamano au mfano wa hilo, basi hakuna ubaya kwake.

12. Kubusu kona ya Yemeni, au kuiashiria wakati hawezi kuibusu.

Sunna ni kuigusa kwa mkono tu bila ya kuibusu, na ikiwa hawezi kuigusa, basi asiiashirie.

13. Kugusa na kubusu pembe zote za Al-Kaaba, au kuta zake, na kujipangusa kwazo.

Hili ni kinyume na Sunna, kwani hairuhusiwi isipokuwa kulibusu Jiwe Jeusi tu na kuigusa Pembe ya Yemen pekee.

14. Kudhani kwamba kugusa kona ya Yemeni na Jiwe Jeusi ni kwa ajili ya kutafuta baraka, na si kwa ajili ya kufanya ibada.

Yote haya ni ujinga na upotofu, kwani manufaa na madhara yako mikononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake. Imesimuliwa kutoka kwa Omari, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba aliliendea Jiwe Jeusi, kulibusu na kusema: “Hakika mimi ninajua kuwa wewe ni jiwe tu lisiloweza kudhuru wala kunufaisha, na lau nisingalimuona Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akikubusu, basi nisingelikubusu.” [1] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 1597.

15. Kuinua sauti juu katika kuomba dua kwa njia ambayo inasumbua wazungukaji.

Sunna ni kwamba mtu amtaje Mola wake Mlezi na kumuomba baina yake na nafsi yake; ili asiwasumbue wengine.

16. Kushughulika na kupiga picha au kuongea mazungumzo ya pembeni wakati wa Tawafu.

Mtu anayefanya tawafu anafaa kumtaja Mola wake Mlezi kwa unyenyekevu, udhalili na uwepo wa moyo.

17. Kumaliza tawafu kabla ya kuhakikisha umefika kwenye Jiwe Jeusi.

La wajibu ni mtu kumaliza mzunguko wa saba ili ahakikishe au awe na yakini au awe na uwezekano mkubwa kwamba amefika kwenye kiwango sawa na Jiwe Jeusi.

18. Kuamini kwamba rakaa mbili za baada ya tawafu ni lazima ziswaliwe moja kwa moja nyuma ya Maqam Ibrahim au karibu nayo, basi wakafanya hapo msongamano na kuwaudhi wale wanaozunguka Kaaba katika msimu wa Hija, na wanazuia kuzunguka kwa wale wanaofanya tawafu.

Dhana hii ni potofu, kwani rakaa mbili za baada ya tawafu zinatosha katika sehemu yoyote ya msikitini. Mwenye kuswali anaweza kuiweka Maqam Ibrahim baina yake na Ka’ba - hata akiwa mbali nayo - na akaswalia kwenye sahani la Al-kaaba au eneo la ua lenye paa, basi atakuwa amesalimika kutokana na kuwadhuru wengine, na ataweza kuswali kwa unyenyekevu na utulivu.

19. Kurefusha rakaa mbili za baada ya tawafu na kuomba dua baada yake.

Sunna ni kuzihafifisha, na kutoomba chochote baada yake; kwa sababu hayo hayakupokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.

20. Kuswali rakaa mbili za baada ya tawafu huku amevaa lubega.

Sunna ni kurudisha shuka lake kwenye bega lake mara tu baada ya kumaliza tawafu.

***

Tatu: Ukiukaji wa watu na makosa yao katika sa'yi

1. Kuvaa lubega wakati wa sa'yi.

Imeshatangulia hapo awali kwamba kuvaa lubega hakufanywi isipokuwa wakati wa tawafu peke yake.

2. Kutamka nia kabla ya kuanza sa’yi.

Imeshatangulia hapo awali kwamba mahali pa nia ni moyoni, na kuitamka kwa maneno si katika sheria.

3. Kuanzia kwenye Marwah wakati wa kufanya sa’yi.

Hili ni kosa, na yeyote atakayefanya hivyo, basi na asiuhesabu mzunguko huo.

4. Watu wengine kufikiri kwamba mzunguko mmoja ni safari ya kwenda na kurudi, hivyo akafanya sa'yi raundi kumi na nne.

Hili ni kosa, kwa sababu kutoka Safa kwenda Marwa ni mzunguko mmoja, na kutoka Marwa kwenda Safa ni mzunguko mwingine, na mtu anapaswa kuanzia Safa na kumalizia Marwa.

6. Kupanda juu kabisa ya kilima cha Safa akidhani kwamba ni jambo lisilobudi.

Hakuna ushahidi wowote kwamba hilo ni sharti.

7. Kuinua mikono juu na kuashiria kwayo kama anavyofanya katika takbira za swala.

Sahihi ni kwamba inatosha kukielekea Kibla tu na kuomba kwa yale yaliyokuja kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.

8. Mwanamke kufanya sa'yi kwa kasi kubwa kati ya zile taa mbili za kijani kibichi kama wanavyofanya wanaume.

Kilicho katika sheria kwa mwanamke ni kutembea tu, kwa mujibu wa makubaliano ya wanachuoni; ili kumhifadhi kutokana na kujifunua.

9. Kuuwekea kila mzunguko wa sa’yi dua maalumu.

Hakuna ushahidi wowote kwa hili. Bali anapaswa kuomba apendavyo bila kuweka chochote maalumu.

10. Kuinua sauti juu katika kufanya sa'yi kwa njia ambayo inawasumbua watu wengine.

Sunna ni kwamba mtu amtaje Mola wake Mlezi na kumuomba baina yake na nafsi yake; ili asiwasumbue wengine.

11. Kwenda kwa kasi kubwa katika kufanya sa'yi katika ya Safa na Marwa katika kila mzunguko.

Sunna ni kwenda kwa kasi kubwa baina ya zile taa mbili za kijani kibichi pekee.

12. Kuswali rakaa mbili baada ya kumaliza sa'yi.

Hakuna ushahidi kwa hili, kwa hivyo hairuhusiwi kufanya hivyo.

13. Kufanya sa'yi kwa hiari bila kuwa katika Hija wala Umra.

Kufanya sa'yi ya hiari si katika sheria.

***

Nne: Ukiukwaji na makosa ya watu katika kunyoa au kufupisha nywele zao

1. Kuzembea katika kunyoa kichwa chote au katika kufupisha nywele.

Sunna ni kunyoa au kupunguza nywele zote za kichwa.

2. Kunyolea au kupunguzia nywele ndani ya Msikiti Mtukufu, na kutupa nywele ndani yake.

La wajibu ni kuuheshimu Msikiti Mtukufu na kuhakikisha usafi wake.

3. Kuchelewesha sana kunyoa au kufupisha nywele kiasi cha kumsababishia kuisahau au kujishughulisha mbali na hilo.

Kilicho katika sheria ni kuharakisha kufanya hivyo mara tu baada ya kukamilisha tawafu na sa’yi.

4. Kufanya vitendo vilivyoharamishwa ndani ya ihram kabla ya kunyoa au kupunguza nywele.

La wajibu ni kutofanya lolote katika maharamisho ya ihramu isipokuwa baada ya kunyoa au kupunguza nywele.

***

Makosa na ukiukaji unaohusiana na Hija

Kwanza: Ukiukaji na makosa ya watu Siku ya Tarwiya (siku ya nane ya Dhul-Hijja)

1. Baadhi ya watu kudhani kwamba ni katika sheria kuingia katika Ihram Siku ya Tarwiya kutokea kwenye Msikiti Mtakatifu, au kutokea chini ya mfereji wa maji ya paa la Kaaba.

Sunna ni kuingia kwenye ihram kutokea mahali alipo; iwe ni Makkah au Mina.

2. Kuchelewesha kuingia katika Ihram mpaka baada ya swala ya Adhuhuri.

Sunna ni kuingia katika ihram ya Hija asubuhi kabla ya swala ya adhuhuri.

3. Kuacha kulala usiku huko Mina ilhali mtu anaweza kufanya hivyo.

Sunna kwa hujaji ni kulala usiku huko Mina madamu ana uwezo wa kufanya hivyo. Hili ni kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alifanya hivyo.

4. Kuunganisha swala huko Mina.

Sunna ni kuswalia swala zote huko Mina kwa kuzifupisha bila ya kuziunganisha; kwa kumfuata Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake katika hilo.

***

Pili: Ukiukaji na makosa ya watu Siku ya Arafa

1. Kusimama Arafa kwa baadhi ya masaa ya siku ya nane kama njia ya kuchukua tahadhari.

Huku ni kujisumbua na kupitiliza kiwango ambako kuliharamishwa.

2. Kwenda Arafa siku ya nane au usiku wa siku ya tisa na kulala huko.

Hili ni kinyume na sunna, na linapoteza sunna ya kulala Mina usiku.

3. Kusimama nje ya mipaka ya Arafa.

La wajibu kwa hujaji ni kufanya hima kusimama ndani ya mipaka ya Arafa.

4. Kudhani kwamba ni lazima kuswali pamoja na imamu katika Msikiti wa Namira na kuleta msongamano mkubwa kwa ajili ya kukaa humo.

Hili sio lazima, na kuleta msongamano hakuruhusiwi kwa sababu hii.

5. Kuelekea mlima (Ilal) wakati wa kuomba dua.

Sunna ni kuelekea Kibla.

6. Kuamini kwamba ni wajibu kupanda Mlima Ilaal, au kwamba ni miongoni mwa matendo ya Hija, au kwamba una fadhila au sifa maalumu kuliko sehemu zinginezo za Arafa.

Hakuna ushahidi juu ya hili, bali ni kinyume na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.

7. Kuuita Mlima Ilaal mlima wa rehema, au mlima wa dua.

Jina lake sahihi ni Ilal, na hakuna ushahidi kwamba unaitwa mlima wa rehema au wa dua.

8. Kuingia kwenye kuba la Mlima Arafa, na kuliita Kuba la Adam, na kuswalia humo na kulizunguka kama mtu anavyoizunguka Nyumba tukufu.

Yote haya ni uzushi ulioharamishwa, na unaweza kusababisha ushirikina.

9. Kutafuta baraka kutoka kwa nguzo iliyosimamishwa juu ya Mlima Arafa na kuandika majina juu yake.

Yote haya ni uzushi ulioharamishwa, na unaweza kusababisha ushirikina.

10. Kuweka pesa kwenye nyufa zilizoko kwenye Mlima Arafa au Mlima An-Nuur, au kuweka nywele, kucha, nguo na vinginevyo, na kuamini kwamba hilo itasababisha kurudi kwa wafanyao hivyo kwenye maeneo haya.

Yote haya ni uzushi ulioharamishwa, na unaweza kusababisha ushirikina.

11. Baadhi ya watu wanadhani kwamba ni wajibu kusimama katika nafasi aliyosimama Mtume, au kujisumbua kufanya hivyo.

Mtazamo sahihi ni kwamba si wajibu, na hairuhusiwi kujisumbua kufanya hivyo.

13. Kupoteza wakati, kupuuza dua na kumtaja Mwenyezi Mungu, na kujishughulisha na mambo ambayo hayana faida.

Kuchelewesha kuanza kuomba dua mpaka karibia kuzama kwa jua, au mwisho wa mchana.

13. Mtu kujisumbua kusimama kuomba dua, akidhani kuwa hilo ni sunna, au akifikiria kuwa maana ya kusimama Arafa ni kusimama kwa ajili ya kuomba dua.

Mtazamo sahihi ni kwamba kusimama Arafa ni kuwa pale kwa wakati huo, kwa kusimama, au kwa kukaa chini, kwa kupanda kipando au kwa kutembea.

14. Kundoka kutoka Arafa kabla ya jua kutua.

Hili ni haramu, kwa sababu ni kinyume na Sunna ya Mtume, Mwenyezi Mungu amfikishie rehema na amani.

15. Kuchelewa kuondoka Arafa baada ya jua kutua bila udhuru.

Sunna ni kuondoka mara tu baada ya kuzama kwa jua, isipokuwa kama kuna udhuru.

16. Baadhi ya watu wanaamini kuwa kusimama Arafa siku ya Ijumaa ni sawa na kuhiji mara sabini.

Hakuna ushahidi kwa hilo.

***

Tatu: Ukiukaji wa watu na makosa yao katika kwenda Muzdalifa na kulala huko usiku

1. Kukimbia wakati wa kutoka Arafa (kwenda Muzdalifa) na kusumbua watu kwa magari.

Sunna ni kutoka huko kwa utulivu na unyenyekevu na kutowaudhi watu.

2. Baadhi ya watu wanadhani kuwa ni (lazima) katika sheria kuoga ili kulala Muzdalifa usiku.

Hakuna ushahidi kwamba hili liko katika sheria.

3. Baadhi ya watu wanadhani kwamba inapendekezwa kwa mtu aliyepanda kipando kushuka chini ili aingie Muzdalifa kwa miguu.

Hakuna ushahidi kwamba hili liko katika sheria.

4. Kushukia katika mahali kabla ya kuhakikisha kuwa pako ndani ya mipaka ya Muzdalifa.

5. Kuacha kuharakisha kuswali mara mtu anapofika Muzdalifa.

Sunna ni kuharakisha kuswali mara baada ya kufika Muzdalifa.

6. Kujishughulisha na kukusanya vijiwe mara baada ya kufika hapo na kufanya hima juu ya hilo huko na kufikiria kuwa hilo liko katika sheria.

Hakuna ushahidi kwa hilo.

7. Kuchelewesha swala ya Magharibi na Ishaa mpaka muda wake upite, yaani usiku wa manane.

La wajibu ni kuswali swala ya Magharibi na Ishaa kabla ya usiku wa manane, hata ikiwa ni kabla ya kufika Muzdalifa.

8. Kuadhimisha usiku wa Muzdalifa kwa swala, ibada fulani, au furaha mambo ya pumbao na michezo.

Sunna ni kuchukua hatua ya kulala na kupumzika. Kwa kumfuata Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ili hilo limsaidie kutekeleza matendo ya siku ya Idi.

9. Wanyonge na wenzao kuondoka Muzdalifa kabla ya saa sita usiku.

Hawapaswi kuondoka hapo hadi baada ya saa sita usiku.

10. Kutoka kwa wale ambao sio dhaifu na ambao hawana watu dhaifu pamoja nao kabla ya alfajiri.

La wajibu ni kubaki Muzdalifa mpaka Alfajiri.

11. Kuchelewesha kuondoka Muzdalifa mpaka jua lichomoze.

Sunna ni kutoka huko kabla ya jua kuchomoza.

***

Nne: Ukiukaji wa watu na makosa yao katika matendo ya Siku ya kuchinja (siku ya Idi)

1. Baadhi yao wanadhani kuwa ni (lazima) katika sheria kuoga kwa ajili ya kurusha vijiwe kwenye Jamaraat.

Hakuna ushahidi kwamba hili liko katika sheria.

2. Kuosha vijiwe vya kurusha kwenye Jamaraat.

Hakuna ushahidi kwamba hili liko katika sheria.

3. Kuamini kwamba kurusha vijiwe hakuwi sahihi isipokuwa ikiwa vijiwe hivyo vitachukuliwa huko Muzdalifa.

Hakuna ushahidi wa hilo, na hivyo mtu anaweza kuvichukua kutoka mahali popote.

4. Kurusha visivyokuwa vijiwe kwenye Jamaraat, au kurusha mawe makubwa.

Hili ni kinyume na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.

5. Kuwa na hasira wakati wa kutupa vijiwe kwenye Jamaraat, na kuamini kuwa anayetupiwa vijiwe ni Shetani.

6. Kukusanyika pamoja na kushikamana katika vikundi wakati wa kwenda kurusha vijiwe kwenye Jamaraat, na kuwaudhi watu.

7. Kuongeza nyiradi zingine juu ya nyiradi zilizokuja katika sheria wakati wa kutupa vijiwe kwenye Jamaraat.

Lililo bora zaidi ni kufanya Takbira tu.

8. Kutupia Jamaraat vijiwe saba mara moja.

Katika hali hii, vijiwe hivyo vyote havinatoshelezi isipokuwa kijiwe kimoja tu, na la wajibu ni kutupa kila kimoja peke yake.

9. Kuweka vijiwe hivyo kwenye hodhi lililoko pembezoni mwa Jamaraat bila kuvirusha.

Hilo halitoshelezi kitu, na kile kilichowekwa katika sheria ni kuvirusha kwa njia yoyote inayoweza kuitwa kurusha.

10. Kufanya hima kubwa kuvirusha vijiwe kwenye sehemu ya juu zaidi ya ukuta wa Jamaraat na kufikiria kwamba huo ndio uliokusudiwa kimsingi.

Kilicho katika sheria ni kwamba kijiwe kianguke kwenye hodhi iliyoko pembezoni mwa Jamaraat hata kama hakitagonga ukuta mrefu wa Jamaraat.

11. Kutupa vijiwe kutokea mahala mbali, na bila kuhakikisha kuwa vijiwe vimeanguka ndani ya hodhi iliyoko pembezoni mwa Jamaraat.

12. Kusimama kwa ajili ya kuomba dua baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamarat Al-Aqaba.

Hili haliruhusiwi; kwa sababu hakuna ushahidi wa kwamba liko katika sheria.

13. Kuchinja mnyama wa dhabihu kwa ajili ya Hija ya Tamattu na Qiran kabla ya siku ya kuchinja.

Atakayefanya hivyo, basi hilo halitamtosheleza na itamlazimu arudie kuchinja katika wakati uliowekwa kisheria, ambao ni siku ya Idi mpaka siku ya mwisho katika siku za Tashriq (kubanika nyama).

14. Kukataa kuchinja na kuhiari kutoa thamani ya mnyama anayepaswa kuchinjwa.

Atakayefanya hivyo, hilo halitamtosheleza, na itamlazimu achinje.

15. Kunyoa au kupunguza sehemu tu katika kichwa.

Sunna ni kunyoa au kupunguza nywele zote za kichwa.

16. Kufanya Tawaful-Qudum peke yake badala ya kufanya Tawaful-Ifadhwa pia, au kuifanya Tawaful-Ifadhwa kabla ya kusimama Arafa na Muzdalifa.

Atakayefanya hivyo, hilo halitamtosheleza. Kwa sababu Tawaful-Ifadhwa ni moja ya nguzo za Hija, na Hija haiwi sahihi bila ya hiyo, na hairuhusiwi kuifanya isipokuwa baada ya kusimama Arafa na Muzdalifa.

***

Tano: Ukiukaji wa watu na makosa yao katika matendo ya siku za Mina (siku za Tashriq)

1. Kuzembea katika suala la uwakilishaji katika kurusha vijiwe.

Kanuni ya msingi ni kwamba mwenye kuhiji anatakiwa kurusha vijiwe mwenyewe, isipokuwa kama kuna udhuru wa kisheria unaozingatiwa na unaomruhusu kumteua mtu wa kufanya hivyo kwa niaba yake.

2. Mtu anayemuwakilisha mwingine katika kurusha vijiwe kuondoka kabla ya kumalizika kwa ibada na siku za Hija.

Hili ni kosa, na la wajibu kwake ni abakie Mina au mahali alipo hadi yakamilike matendo ya Hija, kisha afanye tawafu ya kuaga kisha aondoke.

3. Kurusha vijiwe katika siku za Tashriq kabla ya jua kupita katikati ya mbingu.

Sunna ni kurusha vijiwe baada ya jua kupita katikati ya mbingu.

4. Kutozipanga hizo Jamaraat tatu kwa mpangilio wa sawasawa.

La wajibu ni azipange mpangilio wa sawa sawa, kwa kuitupia vijiwe Jamrat ya kwanza, kisha Jamrat ya kati, kisha Jamrat kubwa, ambayo ni Jamratul-Aqaba. Mwenye kugeuza au kwenda kinyume, basi itamlazimu arudie kwa utaratibu wa sawasawa, akianza na Jamrat ndogo kisha azitupie Jamaraat za baada yake.

5. Kusimama kwa ajili ya kuomba dua baada ya kurusha vijiwe kwenye Jamrat al-Aqaba.

Sunna ni kuomba dua tu baada ya kuirushia vijiwe Jamrat ya kwanza na ya kati peke yake.

***

Sita: Ukiukaji wa watu na makosa yao wakati wa Tawafu ya Kuaga

1. Kutanguliza tawafu ya kuaga mbele ya kurusha vijiwe katika siku ya mwisho; ili asafiri mara baada ya kutupa vijiwe.

Hili ni kosa, na mwenye kulifanya, basi atakuwa amelifanya katika wakati usiofaa, kwa hivyo hilo halitamtosheleza, na itamlazimu airudie baada ya kurusha vijiwe.

2. Kumteua mtu wa kumrushia vijiwe, kisha yeye mwenyewe akafanya Tawafu ya kuaga kabla ya wakili wake hajarusha vijiwe.

Mtazamo sahihi ni kwamba asubiri mpaka arushiwe vijiwe ndipo afanye tawafu ya kuaga.

3. Kukusudia kutoipa mgongo Al-Kaaba, bali kuondoka kinyumenyume, kwa sababu ya kuiheshimu Al-Kaaba.

Hakuna ushahidi wa kwanba hilo liko katika sheria, na muongozo ulio bora zaidi ni muongozo wa Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake.

4. Kusimama ili kuomba dua wakati wa kutoka kwenye Msikiti Mtukufu.

Hakuna ushahidi kwa hilo.

5. Kukaa kwa muda mrefu Makka baada ya Tawafu ya Kuaga bila ya udhuru wa kisheria.

La wajibu ni kuharakisha kuondoka Makka baada ya kufanya Tawafu ya kuaga, na hakuna ubaya kusubiri marafiki au kununua vifaa vya safirini na mfano wa hayo.

Iwapo atakaa kwa muda mrefu bila kigezo, basi itamlazimu arudie kufanya Tawafu ya kuaga.

Makosa na ukiukwaji unaohusiana na kutembelea Msikiti wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake

1. Kujipangusa kwenye kuta na nguzo za chuma wakati wa kulizuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na kufunga nyuzi na mfano wake kwenye madirisha kwa kutafuta baraka.

Baraka ziko katika yale waliyoyaamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na si katika uzushi.

2. Kwenda kwenye mapango ya Mlima Uhud, na vile vile kwenye Pango la Hira na Pango la Thauri huko Makka, na kufunga matambara huko na kuomba dua ambazo Mwenyezi Mungu hakuziruhusu, na kuvumilia shida katika kufanya hivyo.

Yote haya ni uzushi usio na msingi katika sheria safi.

3. Kuzuru baadhi ya maeneo wanayodai kuwa ni mabaki ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kama vile mahali pa kupumzikia ngamia wake, kisima cha pete, au kisima cha Othman, na kuchukua udongo kutoka sehemu hizi kwa ajili ya kutafuta baraka.

4. Kuwaomba dua maiti wakati wa kuzuru Makaburi ya Baqi na makaburi ya mashahidi wa Uhud na kuwarushia pesa ili kujiweka karibu nao na kutafuta baraka kutoka kwao.

Hayo ni katika makosa makubwa, bali ni katika ushirikina mkubwa, kama walivyoyaelezea wanavyuoni, na kama yalivyoashiriwa na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtume Wake, rehema na amani ziwe juu yake. Kwani ibada ni ya Mwenyezi Mungu peke yake na wala hairuhusiwi kumfanyia yeyote chochote katika ibada kama vile dua, kuchinja, nadhiri na mfano wa hayo, kwa sababu ya kauli ya Mwenyezi Mungu: "Na hawakuamrishwa ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini." [Al-Bayyina: 5]

Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie Nabii wetu Muhammad.