التحقيق والإيضاح لكثير من مسائل الحج والعمرة والزيارة على ضوء الكتاب والسنة
Uchambuzi na ufafanuzi wa masuala mengi ya Hija, Umra na Ziara kwa mujibu wa muongozo wa Qur'ani na Sunna
Uchambuzi na ufafanuzi wa masuala mengi ya Hija, Umra na Ziara kwa mujibu wa muongozo wa Qur'ani na Sunna
Cha Mheshimiwa, mwanachuoni,
Abdul-Aziz bin Abdillah bin Baz
Utangulizi wa Mwandishi
Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu
Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na mwisho bora ni wa wachamungu, na rehema na amani ziwe juu ya mja wake na Mtume wake, Muhammad na jamaa zake na Maswahaba wake wote.
Ama baada ya hayo:
Huu ni ujumbe mfupi kuhusu Hija, unaoeleza fadhila zake na adabu zake, na kinachompasa yule anayetaka kusafiri kwenda kuitekeleza, na kueleza masuala mengi muhimu ya Hija, Umra, na kuutembelea msikiti wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kwa njia ya ufupi na ubainifu. Nimejitahidi kuweka ndani yake yale yaliyoashiriwa na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, nikiwa nimekikusanya kwa ajili ya kuwanasihi Waislamu kwa kuitekeleza kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini." [2] [Dhariyat: 55]. Na kauli yake Mtukufu: "Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua ahadi na wale waliopewa Kitabu kuwa: Lazima mtawabainishia watu, wala hamtokificha." [3] [Al Imran: 187]. Hadi mwisho wa Aya. Na kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na saidianeni katika wema na ucha Mungu." [4] [Al-Maaida: 2].
Na kwa Hadithi sahihi kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Dini ni kunasihiana" Alisema hivyo mara tatu. Akaambiwa: 'Kwa nani, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?' Akasema: "Ni kwa Mwenyezi Mungu, na kwa Kitabu chake, na kwa Mtume wake, na kwa Maimamu wa Waislamu na watu wote kwa ujumla." [5] (1) Kaipokea Muslim kwa nambari 55.
Na amepokea At-Twabarani kutoka kwa Hudhaifa, ya kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: “Asiyejali mambo ya Waislamu, basi si miongoni mwao. Na asiyefika asubuhi na jioni akinasihi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na Mtume wake, na Kitabu chake, na Imamu wake, na Waislamu kwa ujumla, basi si miongoni mwao." [2]. [2] Ameipokea At-Twabarani katika Al-Awsat, nambari 7469.
Ninamuomba Mwenyezi Mungu anifaidishe mimi na Waislamu kwayo, na aifanye juhudi yangu iwe kwa ajili Yake peke Yake, na iwe sababu ya kufanikisha Pepo Yake ya milele. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuitika maombi. Yeye ndiye wa kututosheleza, na ndiye mbora wa kutegemewa.
Mlango:
Kuhusu ushahidi wa ulazima wa kufanya Hija na Umra na kuharakisha kuyatekeleza mawili hayo.
Ikiwa hilo limeshajulikana, basi jueni - Mwenyezi Mungu aniwezeshe mimi na nyinyi kujua haki na kuifuata - kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwajibisha juu ya waja wake kufanya Hija kwenye Nyumba yake tukufu, na akafanya hilo kuwa moja ya nguzo za Uislamu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezaye njia ya kuiendea. Na atakayekanusha, basi Mwenyezi Mungu si muhitaji kwa walimwengu." [7] [Al Imraan: 97].
Na katika vile vitabu viwili vya hadithi sahihi kutoka katika hadithi ya bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Uislamu umejengwa juu ya mambo matano: Kushuhudia kwamba hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kusimamisha Swala, na kutoa Zaka, na kufunga saumu katika Ramadhani, na kuhiji kwenye Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu." ([8]) [3] Kaipokea Bukhari, kwa nambari 8, na Muslim, kwa nambari 16.
Na imepokelewa na Sa'id katika Sunna yake, kutoka kwa Omari bin Khattwab, Mwenyezi Mungu amridhie, ya kwamba alisema: "Hakika nilikuwa nimeazimia mno kutuma watu katika miji hii wamtazame kila mtu ambaye ana uwezo [9] lakini hakufanya Hija ili wamtoze kodi (jizia). Wao sio Waislamu. Wao sio Waislamu." [10] [4] Yaani, mwenye kiasi kikubwa cha mali. [5] Aliinasibisha na Sunan Sa’id ibn Mansur katika Jami’ al-Ahadith kwa nambari 31221, lakini sikuipata katika nakala inayopatikana.
Na imesimuliwa kutoka kwa Ali, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alisema: "Yeyote mwenye uwezo wa kufanya Hija na akaacha kuifanya, basi hakuna ubaya kwamba afe Myahudi au Mkristo." [6]. [6] Ameipokea Tirmidhiy kwa nambari 812.
Na yeyote ambaye ana uwezo wa kufanya Hija, inamlazimu aharakishe kuhiji, kwa sababu ya yale yaliyosimuliwa kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Harakisheni kwenda kufanya Hija - akimaanisha Hija ya lazima - kwani mmoja wenu hajui ni nini kinaweza kumpata." ([10]) Imepokelewa na Ahmad. [7] Ameipokea Abu Daud kwa nambari 1732.
Na kwa sababu utekelezaji wa Hija ni lazima mara moja kwa yule anayeweza kupata njia ya kuiendea; kwa maana ya dhahiri ya kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezaye njia ya kuiendea. Na atakayekanusha, basi Mwenyezi Mungu si muhitaji kwa walimwengu." [13] [Al Imran: 97]. Na kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika hotuba yake: "Enyi watu, hakika Mwenyezi Mungu amekufaradhishieni Hija, basi fanyeni Hija." ([14]) [8] Kaipokea Muslim kwa nambari 1337.
Na zimekuja hadithi mbalimbali zinazoonyesha ulazima wa Umra, ikiwa ni pamoja na:
Miongoni mwake ni kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akimjibu Jibril alipomuuliza kuhusu Uislamu, akasema: "Uislamu ni ushuhudie kwamba hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na usimamishe Swala, na utoe Zaka, na ufanye Hija na Umra katika Nyumba, na uoge kutokana na Janaba, na utawadhe kikamilifu na ufunge saumu katika mwezi wa Ramadhani." ([15]) Imepokelewa na bin Khuzaima, na ad-Darqutni, kutoka katika Hadithi ya Omari bin Khattwab, Mwenyezi Mungu amridhie. Ad-Darqutni alisema: Mlolongo huu wa wasimulizi umethabiti na ni sahihi. [9] Ameipokea Ibn Khuzaima, nambari 1.
Na miongoni mwake ni Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je wanawake wanalazimika kufanya Jihadi?" Akasema: "Wanalazimika kufanya jihadi ambayo haina kupigana: Hija na Umra." ([16]) Imepokelewa na Ahmad, na bin Maaja kwa isnadi (mlolongo) sahihi wa wasimulizi. [10] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1520.
Hija na Umra sio lazima kufanya katika maisha isipokuwa mara moja tu; kwa mujibu wa maneno ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika hadithi sahihi: "Hija ni mara moja. Kwa hivyo, atakayezidisha, basi hiyo itakuwa ya kujitolea." ([17]) [11] Kaipokea An-Nasai, kwa nambari 2620.
Ni sunna kufanya Hija na Umra kwa wingi kwa hiari; kwa mujibu wa yale yaliyothibiti katika Sahihi mbili, kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Umra hadi Umra ni kafara kwa yale yaliyo baina yake. Na Hija iliyokubaliwa haina malipo isipokuwa Pepo." [18] [12] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1773, na Muslim kwa nambari 1349.
Mlango:
Kuhusu ulazima wa kutubu kutokana na maasi na kuachana na udhalimu
Muislamu anapokusudia kusafiri kwenda Hija au Umra, inapendekezwa awausie wana familia yake na jamaa zake kumcha Mwenyezi Mungu Mtukufu, yaani kufanya maamrisho yake na kujiepusha na makatazo yake.
Na anapaswa kuandika mali yake na madeni yaliyo juu yake, na awashuhudishe watu hilo. Pia ni lazima aharakishe kutubu toba ya kweli kutokana na maasi yote; kwa mujibu wa maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa." [19] [An-Nuur: 31].
Na uhakika wa toba ni kujivua kutokana na madhambi na kuachana nayo, kujutia yaliyopita, na azimio la kutoyarudia. Na ikiwa ana vitu alivyowafanyia watu dhuluma kama vile kuua, au kuchukua mali au kuvunja heshima, basi itamlazimu kukirejesha kwao au kuwaomba wamsamehe kabla ya safari yake; kwa mujibu wa hadithi sahihi kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Yeyote ambaye ana vitu alivyochukua kwa dhuluma kutoka kwa ndugu yake, kama vile mali, kuvunja heshima, basi na amuombe amsamehe leo kabla wakati ambapo hakutakuwa na dinari wala dirhamu. Ikiwa atakuwa na matendo mema, yatachukuliwa kutoka kwake kwa kiasi cha udhalimu wake. Na ikiwa hatakuwa na matendo mema, basi yatachukuliwa kutoka katika mabaya ya mwenzake huyo na abebeshwe yeye." [20] (13) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2449.
Na anapaswa kuichagulia Hija yake na Umra yake mali nzuri na ya halali kwa ajili ya matumizi yake; kwa mujibu wa yale yaliyosimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu ni mzuri na wala hakubali isipokuwa vilivyo vizuri." [21] [14] Kaipokea Muslim kwa nambari 1015.
Na At-Tabarani alipokea kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mtu anapotoka kwenda kufanya Hija kwa mali nzuri ya matumizi na akaweka mguu wake kwenye kikanyagio cha mguu, na akaita: 'Nimekuitikia, ewe Mwenyezi Mungu nimekuitikia.' Anaitwa na muitaji kutoka mbinguni: 'Nami nimekuitikia na nipo tayari kukutumikia kwa furaha. Chakula chako ni halali, kipando chako ni halali na Hija yako iwe ya kukubaliwa na isiyo na dhambi.' Na ikiwa mtu atatoka na mali chafu ya matumizi, akaweka mguu wake kwenye kikanyagio cha mguu na kuita: 'Nimekuitikia, ewe Mwenyezi Mungu nimekuitikia.' Muitaji kutoka mbinguni anamuita: 'Sijakuitikia na sipo tayari kukutumikia kwa furaha. Chakula chako ni haramu na mali yako ni haramu, basi Hija yako isikubaliwe." [22] (15) Ameipokea Twabraniy katika Al-Kabir kwa nambari 2989.
Na hujaji anapaswa kuachana na kile kilicho mikononi mwa watu na kujiepusha kuwaomba; kwa mujibu wa kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Na mwenye kujizuilia, Mwenyezi Mungu atamzuilia. Na mwenye kujitosheleza, Mwenyezi Mungu atamtosheleza." [23] (16) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1427, na Muslim kwa nambari 1035.
Na kauli yake Mtume rehema na amani zimshukie: "Mtu ataendelea kuwaomba watu hadi aje Siku ya Kiyama hali ya kuwa hakuna chembe ya nyama kwenye uso wake." [24] (17) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1474, na Muslim kwa nambari 4040.
Hujaji analazimika kuukusudia uso wa Mwenyezi Mungu kwa Hija yake na Umra yake na nyumba ya Akhera, na kumkaribia Mwenyezi Mungu kwa yale yanayomridhisha miongoni mwa maneno na matendo katika maeneo hayo matukufu, na atahadhari tahadhari yote kukusudia kwa Hija yake dunia na mambo yake ya kupita, au kujionyesha kwa watu, kutaka sifa na kujifaharisha kwa hilo. Kwani hayo ni katika makusudio mabaya zaidi na ni sababu ya kuharibika matendo na kutokubaliwa kwake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Yule ambaye anataka uhai wa dunia na mapambo yake, tutawalipa humo matendo yao kamili. Na wao humo hawatapunjwa. (15) "Hao ndio ambao hawana kitu katika Akhera isipokuwa Moto, na yataharibika yale waliyoyafanya humo, na yatabatilika yale waliyokuwa wakiyatenda." [25] [Hud: 15-16].
Na amesema Mtukufu: "Anayetaka yapitayo upesi upesi, tutafanya haraka kumletea hapa hapa tunayoyataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannamu, ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa." (18) "Na anayeitaka Akhera, na akayafanyia juhudi matendo yake, naye ni Muumini, basi hao juhudi yao itakuwa ni ya kushukuriwa." [26] [Al-Israa: 18-19].
Na imethibiti kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, amesema: "Mwenyezi Mungu Mtukufu alisema: 'Mimi ndiye niliyejitosheleza zaidi kuhitaji mshirika. Mwenye kutenda tendo akanishirikisha katika hilo na asiyekuwa Mimi, nitamuacha yeye na huyo mshirika wake." [27] [18] Ameipokea Muslim kwa nambari 2985.
Na anapaswa pia kuandamana na watu wazuri katika safari yake hiyo miongoni mwa watu wenye utiifu, ucha Mungu, ufahamu wa dini, na atahadhari kuandamana na wapumbavu na watu wavukao mipaka ya dini.
Na anapaswa kujifunza yale anayofaa kufanya katika Hija yake na Umra yake na kuyaelewa vyema, na kuuliza kile kinachomtatiza; ili awe na ufahamu mzuri. Kwa hivyo, anapopanda mnyama wake, au gari lake, au ndege, au vipando vinginevyo, ni vyema kwake kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu na kumsifu, na kisha atoe takbira mara tatu, na aseme: "Ametakasika aliyemfanya huyu atutumikie, na tusingeliweza kufanya haya wenyewe." (13) "Na hakika sisi tutarudi kwa Mola wetu Mlezi." [28] [Az-Zukhruf: 13-14].
"Ewe Mwenyezi Mungu, hakika sisi tunakuomba katika safari yetu hii wema na ucha Mungu, na katika matendo unayoyaridhia. Ewe Mwenyezi Mungu, ifanye nyepesi safari yetu hii, na utufupishie umbali wake. Ewe Mwenyezi Mungu, Wewe ndiye Mwenza katika safari hii, na Mchungaji wa familia yangu. Ewe Mwenyezi Mungu, hakika mimi najilinda kwako kutokana na ugumu wa safari, na ubaya wa mtizamo, na uovu wa kubadilikiwa katika mali na familia." ([29]) Kwa sababu, hili lilithibiti kwa usahihi kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na likapokelewa na Muslim kutoka katika hadithi ya Ibn Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao. [19] Kaipokea Muslim kwa nambari 1342.
Wakati wa safari yake hii na akithirishe kufanya dhikri, kuomba msamaha, kumuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu, kumnyenyekea, kuisoma Qur'ani na kutafakari maana zake. Na asimamishe swala zote katika jamaa na auzuie ulimi wake kutokana na kueneza mambao yaliyosemwa hivi na hivi, na kuzama katika mambo yasiyomuhusu na mzaha wa kupindukia. Pia na aulinde ulimi wake dhidi ya kusema uongo, kusengenya, kufitini na kuwakejeli marafiki zake na wasiokuwa hao miongoni mwa ndugu Waislamu.
Na anapaswa kuwatendea wema wenzake kwa wingi, na kuacha kuwadhuru, na kuwaamrisha mema na kuwakataza maovu kwa hekima na mawaidha mema kulingana na uwezo wake.
Mlango:
Kuhusu atakachofanya hujaji anapofika kwenye Miqat (kituo cha kutia nia ya Hija au Umra)
Anapofika kwenye Miqat (kituo cha kutia nia ya Hija au Umra), inapendekezwa aoge na kupaka manukato, kwa mujibu wa yale yaliyosimuliwa kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alivua nguo za kawaida alipokuwa anataka kuingia katika Ihram (nia ya Hija au Umra) na akaoga. Na kwa mujibu wa yale yaliyothibiti katika vile vitabu viwili vya hadithi sahihi kutoka katika hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba alisema: "Nilikuwa nikimpaka Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, manukato kwa ajili ya Ihram yake kabla hajaingia katika Ihram, na kwa ajili ya kutoka kwake katika Ihram kabla ya kuzunguka kando ya Al-Ka'aba." [30] Na akamuamrisha Aisha pindi alipopata hedhi na alikuwa amehirimia Umra kwamba aoge na ahirimie Hija. Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alimuamuru Asmaa binti Umaisi, alipojifungulia huko Dhul-Hulaifa, kwamba aoge, ajifunike kwa nguo (ukeni) na aingine katika Ihram ([31]). Basi hilo likaonyesha kuwa mwanamke anapofika kwenye Miqat hali ya kuwa ana hedhi au damu ya baada ya kuzaa, anafaa kuoga na kuhirimia kama watu wengine na afanye yale wanayofanya mahujaji isipokuwa kuzunguka kando ya Al-Ka'aba, kama Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alivyowaamrisha hayo Aisha na Asmaa. (20) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1539, na Muslim kwa nambari 1189. (21) Ameipokea Muslim kwa nambari 1218.
Na inapendekezwa kwa anayetaka kuhirimia, kupunguza masharubu yake, kucha zake, sehemu zake za siri na kwapa zake kiasi inavyohitajika; ili asije akahitaji kuzipunguza baada ya kuingia katika Ihram, kwani hilo ni haramu kwake. Na kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliwawekea Waislamu sheria ya kupunguza nywele hizi wakati wote, kama ilivyothibiti katika Sahihi mbili kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amridhie, kwamba amesema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Mambo ya maumbile ya asili ni matano: kutahiri, kunyoa nywele za sehemu za siri, kupunguza masharubu, kukata kucha na kung'oa nywele za kwapani." ([32]) (22) Kaipokea Bukhari kwa nambari 5891, na Muslim kwa nambari 257.
Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa Anas, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: "Tumeelekezwa kuhusu kupunguza masharubu, kukata kucha, kung'oa nywele za kwapani, na kunyoa sehemu za siri kwamba tusiziache kwa muda wa zaidi ya siku arobaini." ([33]) [23] Kaipokea Muslim kwa nambari 258.
Na ameipokea An-Nasaai kwa matamshi haya: "Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alituwekea wakati..." Na imepokelewa na Ahmad, Abu Daud na At-Tirmidhi kwa matamshi ya An-Nasai. Na ama kichwa, si katika sheria kupunguza chochote kwacho wakati wa kuingia katika Ihram, si kwa upande wa wanaume wala wanawake. (24) Kaipokea An-Nasai kwa nambari 14.
Ama ndevu, ni haramu kuzinyoa au kupunguza kitu chochote kwazo wakati wote, bali ni lazima kuziachilia zimee kwa wingi; kwa mujibu wa yale yaliyothibiti katika Sahihi mbili, kutoka kwa bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kwamba alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Nendeni kinyume na washirikina: Achilieni ndevu zimee kwa wingi na punguzeni masharubu." ([34]) Na imepokelewa na Muslim katika Sahihi yake kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Yakateni masharubu, na ziachilieni ndevu zimee, kwendeni kinyume na Majusi (watu wanaoabudu moto)." ([35]) (25) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2892, na Muslim kwa nambari 259. (26) Kaipokea Muslim kwa nambari 260.
Na kwa hakika msiba umekuwa mkubwa katika zama hizi kwa sababu ya watu wengi kwenda kinyume na Sunna hii na kupigana na ndevu, huku wakiridhia kufanana na makafiri na wanawake, hasa wale wanaojinasibisha na elimu na ufundishaji. Basi hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu na kwake tutarejea. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atuongoze sisi na Waislamu wote kufuata Sunna na kushikamana nayo, na kuilingania, hata kama wengi wataipuuza. Na Mwenyezi Mungu anatutosha na ndiye Mtegemewa bora, na hakuna uwezo wala nguvu ila kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mtukufu.
Kisha mwanaume avae kikoi na shuka, na inapendekezwa ziwe safi na nyeupe. Pia inapendekezwa aingie katika ihraam akiwa amevaa ndara mbili, kwa mujibu wa kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Mmoja wenu na aingie katika Ihram akiwa amevaa vazi la chini, la juu na ndara mbili. Lakini ikiwa hawezi kupata ndara mbili, basi na avae soksi za ngozi (khuff), na azikate mpaka ziwe chini ya vifundo vya miguu." ([36]) Imepokelewa na Imam Ahmad, Mwenyezi Mungu amrehemu. [27] Kaipokea Muslim kwa nambari 1177.
Na ama mwanamke, yeye anaruhusiwa kuingia katika ihram kwa kuvaa nguo za rangi yoyote anayotaka, iwe nyeusi, kijani au nyinginezo, lakini atahadhari kuwaiga wanaume katika mavazi yao. Hata hivyo, haruhusiwi kuvaa nikabu (kitambaa kinachofunika uso wote) au glovu wakati wa ihram. Lakini aufunike uso wake na viganja vyake kwa kitu kisichokuwa nikabu au glovu. Kwani Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alimkataza mwanamke aliye katika ihram kuvaa nikabu na glovu. Na ama baadhi ya watu wa kawaida kuainisha kuwa mwanamke anatakiwa kuingia katika ihram kwa kuvaa rangi ya kijani au nyeusi na siyo nyingine, hilo halina msingi wowote wa kisharia.
Kisha baada ya kumaliza kuoga, kujisafisha, na kuvaa mavazi ya ihraam, ataweka nia moyoni ya kuingia katika ibada anayoitaka, iwe ni Hija au Umra, kwa mujibu wa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika matendo yanategemea nia. Na hakika kila mtu atalipwa kulingana na alichokusudia." ([37]) [28] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1, na Muslim kwa nambari 1907.
Na inaruhusiwa kwake kutamka alichokusudia. Kwa hivyo, kama nia yake ilikuwa ni kutekeleza Umra, atasema: Labbaika 'umrah (Nimekuitikia kwa ajili ya kufanya Umra) au Allahumma labbaika 'umrah (Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa ajili ya kufanya Umra). Na kama nia yake ilikuwa ni kufanya Hija, atasema: Labbaika hajjan (Nimekuitikia kwa ajili ya kufanya Hija) au Allahumma labbaika hajjan (Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa ajili ya kufanya Hija). Hilo ni kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alifanya hivyo. Na kama atayakusudia yote, atayasema yote akisema: Allahumma labbaika 'umratan wa hajjan (Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa ajili ya kufanya Umra na Hija). Hata hivyo, ni bora kutamka hili baada ya kukaa sawasawa juu ya kipando chake sawa kiwe ni mnyama, gari, au vinginevyo. Kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alihirimia baada ya kukaa sawasawa juu ya kipando chake, kisha ngamia wake huyo akainuka juu huku yuko juu yake kwenye Miqat kwa ajili ya kuanza safari. Hii ndiyo kauli sahihi kabisa miongoni mwa kauli za wanazuoni.
Hairuhusiwi kutamka alichokusudia isipokuwa katika kuhirimia (Ihraam) peke yake; kwa sababu hilo lilisimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Ama kuhusu swala, na kuzunguka Al-Ka'aba na ibada nyinginezo, haifai kwa mtu kutamka nia kwa maneno yoyote, kwa mfano asiseme: 'Nimeweka nia ya kuswali hivi na hivi' wala 'Nimeweka nia ya kuzunguka Al-Ka'aba hivi.' Kutamka nia ni katika uzushi uliozushwa, na kutamka kwa sauti kubwa ni jambo baya zaidi na ni dhambi kubwa. Kama kutamka nia kungekuwa jambo linaloruhusiwa, basi Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, angelielezea jambo hilo kwa umma wake na kuweka wazi kitendo chake au kwa kauli yake, na tena watangulizi wetu wema wangetangulia kulifanya.
Basi kwa kuwa hilo halikupokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, wala kutoka kwa Maswahaba zake, radhi za Mwenyezi Mungu ziwashukie, ikajulikana kuwa hilo ni uzushi katika dini. Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie alisema: "Na jambo ovu zaidi ni mambo mapya yanayozuliwa (katika dini). Na kila uzushi ni upotofu." ([38]) Imepokelewa na Muslim katika Sahihi yake, Na amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Yeyote atakayezua katika jambo letu hili kitu ambacho hakimo, basi hicho kitakataliwa." ([39]) Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi. Na katika tamko la Muslim: "Mwenye kufanya tendo ambalo hatukuliamrisha, basi hilo litakataliwa." ([40]) (29) Kaipokea Muslim kwa nambari 867. (30) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2697, na Muslim kwa nambari 1718. (31) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2550, na Muslim kwa nambari 1718.
Mlango: Kuhusu Vituo vya kimahali vya Hija au Umra
Vituo vya kimahali ni vitano:
Cha kwanza: Dhul-Halaifa, ambacho ni kituo cha watu wa Madina, ambacho leo watu hukiita 'Abyaar Ali'.
Cha pili: Al-Juhfa, ambacho ni kituo cha watu wa Sham. Nacho ni kijiji kilichoharibika kilicho karibu na mji wa Raabigh, na watu leo wanahirimia huko Raabigh. Na mwenye kuhirimia Raabigh, basi atakuwa amehirimia katika Miqat; kwa sababu Raabigh iko kabla ya Al-Juhfa kwa masafa mafupi tu.
Cha tatu: Qarnul-Manaazil, ambacho ni kituo cha watu wa Najd, ambacho leo kinaitwa 'As-Sail'.
Cha nne: Yalamlam, ambacho ni kituo cha watu wa Yemen.
Cha tano: Dhaat 'Irq, ambacho ni kituo cha watu wa Iraq.
Vituo hivi aliviweka Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwa wale tuliowataja, na yeyote atakayepita hapo katika wale wasiokuwa watu wa hapo, miongoni mwa wale wanaotaka kufanya Hija au Umra.
Na la wajibu kwa wale wenye kupita hapo ni kuhirimia hapo, na ni haramu kwao kupita hapo bila ya kuhirimia ikiwa wanaenda Makka kwa ajili ya Hija au Umra, iwe wanapitia hapo kwa nchi kavu au angani; kwa sababu ya ujumla wa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipoweka vituo hivi: "Hivi ni vya watu wa hapa, na pia kwa mwenye kuvijia asiyekuwa katika watu wake, miongoni mwa wanaotaka kufanya Hija na Umra." ([41]) (32) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1524, na Muslim kwa nambari 1181.
Na anachofaa kufanya kisheria yule anayeelekea Makka kwa nia ya kuhiji au Umra kwa njia ya ndege ni kujiandaa kwa ajili ya hilo kwa kuoga na mfano wa hilo kabla ya kupanda ndege. Atakapoikaribia Miqat yake, atavaa shuka na kikoi, kisha atahirimia Umra ikiwa kuna muda wa kutosha wa Hija. Lakini kama muda hautakuwa wa kutosha, basi atahirimia Hija. Na ikiwa atavaa shuka lake la juu na la chini kabla ya kupanda au kabla ya kukaribia Miqat, basi hakuna ubaya wowote, lakini asikusudie kuingia katika ibada (ya Hija au Umra) isipokuwa atakapofika kiwango sawa na Miqat au atakapoikaribia; kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakuhirimia isipokuwa tu katika Miqat, na wajibu uliopo kwa umma ni kumfuata yeye, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika hilo, kama mambo mengineyo ya kidini; kwa mujibu wa maneno ya Mwenyezi Mungu aliyetakasika: "Hakika nyinyi mnayo ruwaza (kiigizo) chema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu." ([42]) [Al-Ahzab: 21]. Na kwa mujibu wa maneno ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika Hija ya kuaga: "Chukueni kutoka kwangu ibada zenu za Hija." ([43]) [33] Kaipokea Muslim kwa nambari 1297.
Ama yule anayeenda Makka bila ya kuwa na nia ya kufanya Hija au Umra, kama vile mfanya biashara, mkata kuni, au mpeleka ujumbe na mfano wao, basi si lazima kwake kuingia katika hali ya Ihram isipokuwa atake kufanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe. Hii ni kwa mujibu wa maneno ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika hadithi iliyotangulia alipotaja Mawaqiit (sehemu za kuwekea nia ya Ihram): "Hivi ni vya watu wa hapa, na pia kwa mwenye kuvijia asiyekuwa katika watu wake, miongoni mwa wanaotaka kufanya Hija na Umra." ([44]) Maana yake isiyo ya moja kwa moja ni kwamba yule anayepitia kwenye Mawaqiit (maeneo ya kuweka nia ya Ihram) hizi bila kuwa na nia ya kufanya Hija au Umra, basi si lazima kwake kuingia katika Ihram. [34] Imeshatangulia kuelezwa aliyeipokea.
Hili ni katika rehema ya Mwenyezi Mungu kwa waja wake na kuwarahisishia. Basi sifa njema zote na shukrani ni zake kwa hilo. Na hili linaungwa mkono ukweli wa kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alipofika Makka katika mwaka wa ufunguzi wake (Fat-hu Makkah), hakuwa katika hali ya Ihram, bali aliingia huku amevalia helmeti juu ya kichwa chake, kwa sababu wakati huo hakuwa na nia ya kufanya Hija au Umra, bali lengo lake lilikuwa ni kuifungua Makka na kuondoa ushirikina uliokuwemo.
Ama wale ambao makazi yao yako nje ya Miqat, kama vile wakazi wa Jeddah, Ummu As-Salam, Bahra, Ash-Sharaii, Badr, Mastuura na mengineyo, si lazima kwake aende kwenye Miqat yoyote kati ya hizo tano zilizotajwa. Bali makazi yake ndiyo Miqat yake, na hapo hapo atahirimia anachotaka sawa iwe ni Hija au Umra. Na ikiwa ana makazi mengine nje ya Miqat, basi ana uhuru wa kuchagua, kama atataka, atahirimia kwenye Miqat, na akitaka, anahirimia kwenye makazi yake ambayo yako karibu zaidi na Makka kuliko Miqat; kwa mujibu wa kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika hadithi ya bin Abbas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipotaja Miqat mbalimbali akasema: "Kwa hivyo, atakayekuwa ndani yake (Miqat hizi), basi mahali pake pa kuhirimia ni kwa familia yake, hata watu wa Makka watahirimia huko Makka." ([46]) Imepokelewa na Bukhari na Muslim. [35] Hapa alimaanisha kwamba mtu kama huyu atahirimia Hija hapo anapoishi. [36] Hii ni sehemu katika Hadithi iliyotangulia.
Lakini, ikiwa mtu anataka kufanya Umra akiwa katika eneo takatifu huko Makka, ni lazima atoke nje yake na aende kwenye eneo lisilo takatifu la karibu na ahirimie huko Umra; kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alipoombwa na Aisha kufanya Umra, akamuamuru kaka yake, Abdur-Rahman aende naye kwenye eneo lisilo takatifu na ahirimie kutokea huko. Hilo likaonyesha kwamba mtu anayefanya Umra hafai kuhirimia ndani ya eneo takatifu, bali inapaswa kutoka nje yake na kuhirimia huko.
Hadithi hii inaifanya hadithi ya bin Abbas iliyotangulia kuwa mahususi, na inaonyesha kuwa makusudio ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake, katika kauli yake: "Hata watu wa Makka watahirimia huko Makka." ([47]) Ni kuhirimia Hija siyo Umra. Kwani kama kuhirimia Umra ndani ya eneo takatifu la Makka kunaruhusiwa, basi angemkubalia Aisha, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kufanya hivyo pasipo kumlazimisha kutoka kwenda kwenye eneo lisilo takatifu la Makka. Hili ni jambo lililo wazi na ndiyo kauli ya wengi katika wanazuoni, Mwenyezi Mungu awarehemu, nayo ndiyo bora zaidi kwa Muumini; kwa sababu linahakikisha kuna kuzitumia hadithi zote mbili kwa pamoja. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuafikisha. [37] Imeshatangulia kuelezwa aliyeipokea.
Na ama yale ambayo baadhi ya watu wanafanya ya kufanya Umra kwa wingi baada ya Hija kutokea At-Tan’iim au Al-Ji'raanah au kwingineko, na walikuwa wameshafanya Umra kabla ya Hija, basi hakuna ushahidi kwamba hilo liko katika sheria. Bali ushahidi wote unaonyesha kuwa ni bora kuliacha. Kwa sababu Mtume, rehema za Mwenyezi Mungu na amani ziwe juu yake, na Maswahaba zake, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, hawakufanya Umra baada ya kumaliza Hija. Aisha tu ndiye aliyefanya Umra kutokea At-Tan’im kwa sababu hakuweza kufanya Umra pamoja na watu walipoingia Makka kutokana na hedhi. Kwa hivyo, akamuomba Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kumruhusu kufanya Umra badala ya ile aliyokuwa ameihirimia kutokea kwenye Miqat, na Mtume akakubali ombi lake. Na Aisha alipata Umra mbili hizo: Umra aliyofanya pamoja na Hija yake, na Umra hii ya pekee. Kwa hivyo, mtu ambaye yuko katika hali kama ya Aisha hana tatizo kufanya Umra baada ya kumaliza Hija, kwa kufanyia kazi hoja zote na kuwarahisishia Waislamu.
Hakuna shaka kwamba kujishughulisha kwa mahujaji na Umra nyingine baada ya kumaliza Hija, kando na Umra waliyoifanya walipokuwa wanaingia Makka, ni jambo gumu kwa wote, husababisha msongamano mkubwa na ajali, na pia kunaenda kinyume na muongozo wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake na Sunna yake. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuafikisha.
Mlango:
Kuhusu hukumu ya mtu anayefika kwenye Miqat katika miezi isiyo ya Hija
Jua ya kwamba mtu anayefika kwenye Miqat ana hali mbili:
Ya kwanza: Afike kwenye Miqat katika miezi isiyo ya Hija, kama vile Ramadhani au Shaaban. Basi Sunna kwa mtu huyu ni kuhirimia Umra, ambapo ataanza kwa kunuia moyoni mwake na kutamka kwa ulimi wake akisema: “Labbaika Umrah (Nimekuitikia kwa nia ya kufanya Umra)” au “Allahumma Labbaika Umrah (Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa nia ya kufanya Umra).” Kisha atasema talbiya ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nayo ni: "Labbaika llaahumma labbaika. Labbaika laa shariika laka labbaika. Innalhamda wanni'imata laka walmulk laa shariika laka (Nimekuitika ewe Mwenyezi Mungu nimekuitikia! Nimekuitikia hauna mshirika nimekuitikia. Hakika sifa njema na neema na ufalme ni vyako nimekuitikia huna mshirika!) ([48]) Na ataendelea kurudia talbiya hii mara nyingi pamoja na kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu hadi afike katika Al-Ka'aba. Anapofika Al-Ka'aba, atakomesha talbiya na atatufu Al-Ka'aba mara saba. Baada ya tawafu, ataswali rakaa mbili nyuma ya Maqam Ibrahim, kisha atatoka kuelekea As-Safa, ambapo atafanya sa'ayi (kukimbia) kati ya As-Safa na Al-Marwa mara saba. Baada ya hapo, atanyoa nywele za kichwa chake au kupunguza nywele zake. Kwa kufanya hivyo, Umra yake itakuwa imekamilika, na kila kitu kilichokuwa haramu kwake kwa sababu ya Ihraam kitakuwa halali tena. (38) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1549, na Muslim kwa nambari 1184.
Ya pili: Afike kwenye Miqat katika miezi ya Hija, ambayo ni: Shawwal, Dhul-Qa’dah, na siku kumi za mwanzo za Dhul-Hijjah.
Mtu kama huyo anapewa hiari kati ya mambo matatu: Hija peke yake, Umra peke yake, au kuchanganya yote mawili. Kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipofika kwenye Miqat katika mwezi wa Dhul-Qa’adah wakati wa Hija ya Kuaga, aliwapa Maswahaba wake chaguo kati ya ibada hizi tatu. Lakini sunna kwa mtu huyu pia, ikiwa hana mnyama wa kuchinja (hadiy), ni kuhirimia Umra na kufanya kama tulivyoeleza kuhusu mtu anayefika kwenye Miqat katika miezi isiyo ya Hija. Hii ni kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, aliwaamuru Maswahaba wake walipokaribia Makka wafanye Ihram yao (ya Hija) kuwa ya Umra, na akawasisitizia hilo walipofika Makka. Walitufu, wakafanya sa'ayi (kukimbia), wakapunguza nywele na wakatoka katika Ihram zao kwa kufuata amri ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Hata hivyo, kwa wale waliokuwa na hadyi (wanyama wanaopelekwa Makka kama zawadi), Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliwaamuru wabaki kwenye Ihraam zao hadi siku ya kuchinja wanyama wa hadyi, ambayo ni siku ya Nahr (siku ya Idi ya kuchinja). Na Sunna kwa mtu ambaye amesafirisha hadyi (wanyama wanaopelekwa Makka kama zawadi) ni kuhirimia Hija na Umra kwa pamoja, kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alifanya hivyo, na alikuwa amesafiri pamoja na mnyama wake. Kwa hivyo, akawaamuru wale waliosafiri pamoja na wanyama wao miongoni mwa Maswahaba wake huku wamehirimia Umra tu, kwamba wahirimie Hija pamoja na Umra yao, na kwamba wasitoke katika Ihram ya mambo mawili hayo mpaka watakatoka kwayo yote kwa pamoja siku ya Nahr (siku ya kuchinja). Na ikiwa mtu ambaye amesafiri pamoja na mnyama wake amehirimia Hija pekee, atabaki kwenye Ihram yake hadi atakapotoka ndani yake siku ya kuchinja, kama anavyofanya Al-Qaarin (yule ambaye amehirimia Hija na Umra kwa pamoja).
Na kutokana na hili, jua ya kwamba mtu ambaye amehirimia Hija pekee, au Hija na Umra lakini hana mnyama wa kuchinja (hadyi), haipaswi kubaki kwenye Ihram yake. Bali, lililo sunna kwake ni kubadilisha Ihram yake kuwa ya Umra, kisha atatufu, atafanya kukimbia (saa'yi), atapunguza nywele kisha atatoka katika Ihram yake, kama alivyowaamuru Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, Maswahaba wake ambao hawakusafiri pamoja na wanyama wao wa kuchinja. Hata hivyo, kama atahofia kupoteza fursa ya kufanya Hija kwa sababu amechelewa kufika, basi hakuna shida kubaki kwenye Ihram yake. Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.
Na ikiwa mtu aliyehirimia atahofia kwamba hataweza kutekeleza ibada zake kwa sababu ya ugonjwa au kumuogopa adui au hali nyingine yoyote, inashauriwa kwake kusema wakati wa kuhirimia: "Kama nitazuiliwa na kitu, basi sehemu yangu ya kutoka katika Ihraam ni pale ambapo nitazuiliwa." Kwa mujibu wa hadithi ya Dhuba’ah bint Zubair, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ninataka kuhiji na mimi ni mgonjwa." Akamwambia: "Hiji na uweke sharti kwamba mahali pangu pa kutoka katika Ihraam ni pale ambapo nitazuiliwa." ([49]) Bukhari na Muslim wamekubaliana juu ya usahihi wa hadithi hii. [47] Imeshatangulia kubainishwa aliyeipokea.
Faida ya sharti hili ni kwamba, ikiwa mtu aliyehirimia (muhrim) atakutana na kizuizi kinachomzuia kumaliza ibada zake kutokana na ugonjwa au kuingiliwa na adui, basi anaruhusiwa kutoka katika Ihram bila kuwa na dhambi yoyote.
Mlango:
Kuhusu hukumu ya Hija ya mtoto mdogo, je, itamtosheleza kwa Hija ya Uislamu?
Hija ya mvulana na msichana mdogo ni sahihi; kwa mujibu wa yale yaliyokuja katika Sahihi Muslim, kutoka kwa ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kwamba mwanamke mmoja alimleta mvulana mdogo kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je, huyu ana Hija?" Akasema: "Ndiyo, nawe utapata ujira."([50]) [40] Kaipokea Muslim kwa nambari 1336.
Na katika Sahihi Bukhari, kutoka kwa As-Saaib bin Yazid, Mwenyezi Mungu amridhie, alisema: "Baba yangu alihiji nami pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nilipokuwa na umri wa miaka saba." ([51]) Lakini Hija hii haiwatoshelezi kuwa Hija ya Uislamu. [41] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1858.
Vile vile, Hija ya mtumwa wa kiume na wa kike wanaomilikiwa ni sahihi lakini haiwatoshelezi Hija ya Uislamu; kwa mujibu wa yale yaliyothibiti kutoka katika hadithi ya bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mtoto yeyote ambaye atahiji kisha akabaleghe, basi ni lazima afanye Hija nyingine. Na mtumwa yeyote atakayehiji kisha akaachiliwa huru, basi ni lazima afanye Hija nyingine." ([52]) Imepokelewa na bin Abi Shaiba, na Al-Baihaqi kwa Isnadi Hasan (mlolongo wa mzuri wa wasimulizi). [42] Ameipokea Ibn Abi Shaiba, Juzuu ya 4/444.
Kisha, ikiwa kijana huyo bado hajaweza kupambanua mambo, basi mlezi wake atamhirimia, kisha atamvua nguo zake za kawaida, na amfanyie Talbiya. Na kwa hayo, mvulana huyo mdogo atakuwa ameshaingia katika Ihramu. basi atazuiliwa kile ambacho mtu mzima anazuiliwa katika ihramu. Na hivyo hivyo, msichana mdogo ambaye hajafikia utambuzi wa mambo atahirimiwa na mlezi wake, kisha atatoa talbiya kwa niaba yake na kwa hilo anakuwa ameshaingia katika ihramu. Kisha atazuiliwa yote anayozuiliwa mwanamke aliyehirimia. Wawili hao wanapaswa wawe safi katika mavazi na miili yao wakati wa kutufu kando ya Ka'aba, kwa sababu tawafu inafanana na swala, na usafi ni sharti la usahihi wake.
Na ikiwa mvulana au msichana mdogo wana utambuzi wataingia katika ihram kwa idhini ya walezi wao, na watafanya mambo yanayofanywa na mtu mzima wakati wa kuingia katika ihraam, kama vile kuoga, kutumia manukato, na mengineyo yanayofanana na hayo, basi mlezi wao ndiye atakayesimamia mambo yao na kuwatekelezea masilahi yao, iwe ni baba yao, mama yao, au mtu mwingine yeyote. Mlezi wao atawafanyia yale wasiyoweza kuyafanya kwa niaba yao, kama vile kurusha vijiwe na mengine yanayofanana na hilo, lakini wao wenyewe watatakiwa kufanya ibada zisizokuwa hizo, kama vile kusimama Arafa, kulala Mina na Muzdalifa, na kuzunguka Al-Ka'aba na kufanya sa'ayi. Na ikiwa watashindwa kuzunguka Ka'aba na kufanya sa'yi (kukimbia kati ya Safa na Marwa), basi watazungushwa na kufanyiwa sa'yi wakiwa wamebebwa. Inapendekezwa zaidi kwa yule anayewabeba kwamba asifanye tawafu na sa'yi kwa pamoja baina yake na wao. Badala yake, anapaswa kukusudia tawafu na sa'yi kwa ajili yao, kisha afanye tawafu na sa'yi kwa ajili yake mwenyewe akiwa peke yake, kwa ajili ya kuhifadhi ibada hii na kufuata mafundisho ya hadithi tukufu ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Acha kinachokutia shaka, nenda katika kile kisichokutia shaka." ([53]) Ikiwa aliyembeba atakusudia kufanya tawafu kwa niaba yake mwenyewe na kwa niaba ya yule aliyembeba, basi jambo hilo litatosheleza kwa mujibu wa kauli iliyo sahihi zaidi. Hii ni kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakumuamuru yule mwanamke aliyemuuliza kuhusu Hija ya mtoto kufanya tawafu kwa ajili ya mtoto peke yake. Na kama hilo lingekuwa la lazima, basi Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, angelibainisha. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuwezesha. [43] Ameipokea At-Tirmidhiy, nambari 2518.
Mtoto mvulana mwenye utambuzi na mtoto msichana mwenye utambuzi wataamrishwa kujisafisha kutokana na hadathi na kuondoa najisi kabla ya kuanza tawafu, kama ilivyo kwa mtu mzima aliye katika ihram. Kumhirimia mvulana na msichana mdogo ni lazima juu ya mlezi wake, bali ni ibada ya hiari kwao. Kwa hivyo, ikiwa mlezi wao atafanya hivyo, basi atapata malipo, na ikiwa ataliacha, basi hakuna dhambi yoyote juu yake. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi.
Mlango:
Kuhusu mambo yanayokatazwa katika Ihram na mambo anayoruhusiwa muhrim kufanya
Hairuhusiwi kwa mwenye ihram - awe mwanaume au mwanamke - kunyoa kitu chochote kutoka kwenye nywele zake au kucha zake, au kutumia manukato, baada ya kutamka nia ya ihram.
Na hairuhusiwi kwa mwanaume pekee kuvaa nguo za kawaida zilizoshonwa na kuvaliwa mwili mzima kama vile kanzu, au kwa sehemu fulani kama vile fulana, suruali, viatu vya ngozi (Khofu) au soksi. Hata hivyo, ikiwa hatapata kikoi, ataruhusiwa kuvaa suruali. Kadhalika mtu ambaye hawezi kupata ndara, inaruhusiwa kuvaa soksi za ngozi bila kuzikata. Kwa mujibu wa Hadithi ya bin Abbas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, ambayo imethibiti katika Sahihi mbili, kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alisema: "Yeyote asiyeweza kupata ndara mbili, basi na avae soksi za ngozi. Na yeyote asiyeweza kupata kikoi, basi na avae suruali." ([54]) [44] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1841, na Muslim kwa nambari 1179.
Ama kuhusu yaliyokuja katika hadithi ya Ibn Omar, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao, inayozungumzia amri ya kukata soksi za ngozi anapohitaji kuzivaa kwa sababu ya kukosa ndara mbili, hiyo ilifutwa; kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliagiza hivyo mjini Madina alipoulizwa kuhusu mavazi anayovaa hujaji, kisha alipowahutubia watu huko Arafa, akaruhusu kuvaa viatu vya ngozi wakati mtu hawezi kupata ndara mbili, lakini hakuamuru kuvikata. Hotuba hii ilihudhuriwa na wale ambao hawakusikia jibu lake huko Madina, na kuchelewesha maelezo zaidi ya wakati wa haja hairuhusiwi, kama inavyojulikana katika elimu mbili za kanuni za hadithi na Fiqhi. Kwa hivyo, ikathibiti kwa hilo ile amri ya kuzikata. Na kama hilo lingekuwa ni wajibu, basi Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake angelibainisha. Na Mwenyezi Mungu ndiye anayejua zaidi.
Na mtu aliyehirimia anaruhusiwa kuvaa soksi za ngozi zinazofika chini ya kongo mbili.
Na anaruhusiwa kufunga kikoi kwa uzi na mfano wake; kwa sababu hakuna ushahidi wa kukataza hilo.
Na anaruhusiwa pia kuoga, kuosha kichwa chake, na kukisugua anapohitaji kufanya hivyo, kwa upole na kwa urahisi. Ikiwa kitu kitakatika kutoka kichwani kwake kwa sababu ya hilo, basi hakuna ubaya juu yake.
Na ni haramu kwa mwanamke hujaji kuvaa nguo iliyoshonwa kwenye uso wake kama vile glovu; kwa sababu ya kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Mwanamke asivae nikabu wala glovu ([55])." Imepokelewa na Bukhari. Glovu hushonwa kutokana na kitambaa cha sufu au pamba au kitu mfano wake kwa kiasi cha kutosha kuvaliwa mikononi. (45) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1838.
Na inaruhusiwa kwa mwanamke kuvaa nguo zilizoshonwa kando na hizo; kama vile shati, suruali, viatu vya ngozi, soksi na mfano wa hizo.
Vilevile anaruhusiwa kushusha kitambaa chake cha kichwani kwenye uso wake ikiwa atahitaji kufanya hivyo bila ya kukifunga kwa mkanda, na ikiwa kitambaa chake hicho kitagusa uso wake, basi hakuna dhambi juu yake; kwa mujibu wa hadithi ya Aisha, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema: "Wapandaji (wasafiri) walikuwa wakitupita huku tuko pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, tukiwa katika hali ya Ihraam. Walipokuwa wanatufikia, mmoja wetu alikuwa akishusha kitambaa chake kutoka kichwani hadi kwenye uso wake, na wanapotupita, anakiondoa." ([56]) Imepokelewa na Abu Daud na Ibn Maja, na Ad-Darqutni akapokea mfano wake kutoka katika hadithi ya Ummu Salama. [46] Ameipokea Abu Daud kwa nambari 1833.
Vilevile, hakuna tatizo kwa mwanamke kufunika mikono yake kwa vazi lake au kitu kinginecho, na ni lazima kwake kufunika uso wake na mikono yake anapokuwa mbele ya wanaume wasio maharimu wake, kwa sababu ni uchi; kwa mujibu wa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao." ([57]) An-Nuur: 31. Hakuna shaka kwamba uso na mikono ni miongoni mwa mapambo makubwa.
Na uso ndio unaoshika nafasi kubwa zaidi, na alisema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mnapowauliza wakeze haja, waulizeni nyuma ya mapazia. Hivyo ndio usafi zaidi kwa nyoyo zenu na nyoyo zao." ([58]) [Al-Ahzab: 53].
Ama kuhusu kile ambacho wanawake wengi wamezoea kufanya cha kuweka mkanda chini ya kitambaa cha kichwani ili kukiinua kutoka kwenye uso wake, hilo halina msingi wowote katika sheria ya Kiislamu kwa kadiri tunavyojua. Na kama jambo hilo lingekuwa la kisheria, basi Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, angeliufundisha umma wake na asingeruhusiwa kukaa kimya kuhusiana na hilo.
Na inaruhusiwa kwa mwanamume au mwanamke aliye katika ihramu kufua nguo walizohirimia ndani yake ikiwa ni chafu au vinginevyo, na hata wanaruhusiwa kuzibadilisha na nguo nyinginezo.
Na hairuhusiwi kwake kuvaa vazi lolote lililoguswa na manukato ya zafarani au waris, kwani Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikataza hilo katika hadithi ya bin Omari radhi za Mwenyezi Mungu ziwashukie:
Na ni lazima kwa mtu aliye katika ihraam kuacha maneno machafu, kuvuka mipaka ya kidini na mabishano; kwa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hija ni miezi maalumu. Na anayekusudia kufanya Hija katika miezi hiyo, basi asiseme maneno machafu wala asifanye vitendo vichafu wala asibishane katika Hija." ([59]) [Al-Baqara: 197].
Imepokelewa kwa njia sahihi kutoka kwa Mtume, rehema na amani zimshukie, kwamba alisema: "Mwenye kuhiji kisha hakusema maneno machafu wala kufanya uovu, atarejea (akiwa msafi) kama siku aliyozaliwa na mama yake." ([60]) Neno ‘Rafath’ linamaanisha tendo la ndoa, pamoja na maneno na matendo machafu. Nalo ‘Fusuq’ ni maasi, na ‘Jidal’ ni kubishana katika batili au katika mambo yasiyo na manufaa. Ama mabishano kwa njia iliyo bora ili kubainisha haki na kupinga batili, hilo halina ubaya, bali limeamrishwa; kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hekima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora." ([61]) [An-Nahl: 125]. [47] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa nambari 1521, na Muslim kwa nambari 1350.
Na ni haramu kwa mwanaume aliye katika Ihram kufunika kichwa chake kwa kitu kinachogusana nacho moja kwa moja, kama vile kofia, kilemba cha kawaida, kilemba kinachozungushwa kwenye kichwa au vitu mfano wake. Vivyo hivyo, ni haramu kuufunika uso wake; kutokana na kauli ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuhusu mtu aliyedondoka kutoka juu ya mnyama wake wa kusafiria siku ya Arafa na akafariki: "Muosheni kwa maji na mkunazi, na mumvishe sanda kwa hizo nguo zake mbili, wala msifunike kichwa chake wala uso wake; kwani atafufuliwa Siku ya Kiyama akitoa talbiya (Akisema: Nimekuitikia ewe Mwenyezi Mungu nimekuitikia)." ([62]) Hadithi hii imepokelewa na Bukhari na Muslim, na matamshi haya ni ya Muslim. (48) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1521, na Muslim kwa nambari 1350.
Na ama kuhusu kutafuta kivuli kutoka katika paa la gari, mwavuli, au vitu kama hivyo, basi hakuna ubaya katika hilo, kama vile kutafuta kivuli kutoka katika hema au mti. Kwa sababu imethibiti katika vitabu vya Hadithi Sahihi kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alitengenezewa kivuli kwa nguo wakati alipokuwa anarusha vijiwe kwenye Jamratul-Aqaba. Na pia imepokelewa kwa usahihi kutoka kwake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisimamishiwa hema katika eneo la Namira, kisha akakaa ndani yake hadi jua lilipoondoka siku ya Arafa."
Ni haramu kwa mtu aliye katika Ihram, awe mwanamume au mwanamke, kuua wanyama wa porini, kusaidia katika hilo, au kuwafukuza kutoka katika makazi yao. Vilevile, ni haramu kufunga ndoa, na kushiriki tendo la ndoa, na kuposa, au kuwagusa wanawake kwa matamanio; kutokana na hadithi ya Othman radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Mtu aliye katika Ihraam asifunge ndoa, wala asifungishe ndoa wengine, wala asipose."([63]) Imepokelewa na Muslim. Imepokelewa na Imamu Muslim. [49] Kaipokea Muslim kwa nambari 1409.
Na ikiwa mtu aliye katika Ihraam atavaa nguo ya kawaida iliyoshonwa au akafunika kichwa chake au akajipaka manukato akiwa amesahau au akiwa hajui, basi hakutakuwa na fidia juu yake. Na atatakiwa kuvua hizo pindi atakapolikumbuka au kujua. Vivyo hivyo, ikiwa atanyoa nywele au kukata kucha zake akiwa amesahau au akiwa hajui, basi hakuna chochote kitakachomlazimu kulingana na maoni yaliyo sahihi.
Na ni haramu kwa Muislamu – awe katika Ihraam au la, mwanaume au mwanamke – kuua wanyama wa porini katika eneo takatifu huko Makka, au kusaidia katika kuuawa kwa kutumia silaha, ishara, au njia nyingine yoyote.
Pia imeharamishwa kumfukuza mnyama kutoka mahali pake. Imeharamishwa pia kukata miti ya eneo takatifu huko Makka, mimea yake ya kijani, na kuchukua vitu vyake vilivyodondoka isipokuwa kwa mwenye kuvitangaza; kwa kauli ya Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika nchi hii - akiwa anamaanisha Makka - ni tukufu kwa utukufu alioupa Mwenyezi Mungu hadi Siku ya Kiyama. Hairuhusiwi kukata miti yake ya miba, wala kufukuza wanyama wake wa porini, wala hakiwi halali kitu chake kilichodondoka kwa yeyote isipokuwa kwa yule atakayekitangaza, wala kungo'a nyasi zake." ([64]) Wamekubaliana juu yake Bukhari na Muslim. Bukhari na Muslim wamekubaliana juu ya usahihi wa hadithi hii. [50] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1834, na Muslim kwa nambari 1353.
Na 'al-munshid' ni yule mtu anayetangaza kitu kilichopotea kikapatikana, na 'al-khalaa' ni majani mabichi (nyasi), na Mina na Muzdalifa ni katika eneo takatifu la Makka. Ama Arafa, hiyo iko nje ya eneo takatifu la Makka.
Mlango:
Kile anachopasa kufanya hujaji wakati wa kuingia Makka, na kuelezea anachopaswa kufanya baada ya kuingia Msikiti Mtakatifu, ikiwa ni pamoja na kuzunguka Ka'aba na jinsi ya kufanya hivyo.
Basi, pindi mtu aliyekatika Ihram anapofika Makkah, inapendekezwa kwake kuoga kabla ya kuingia; kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alifanya hivyo. Kisha anapofika kwenye Msikiti Mtakatifu, ni sunna kwake kuingia kwa mguu wa kulia na kusema: "Kwa jina la Mwenyezi Mungu, na rehema na amani ziwe juu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu. Ninajilinda kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kwa uso wake mtukufu, na kwa utawala wake wa kale, kutokana na Shetani aliyelaaniwa. Ewe Mwenyezi Mungu, nifungulie milango ya rehema zako." Atayasema haya wakati wa kuingia katika misikiti mingine yote, na hakuna dua maalumu ya kuingia Msikiti Mtakatifu ambayo imethibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nijuavyo mimi.
Hivyo, anapofika kwenye Ka'aba, atakata talbiya kabla ya kuanza kuzunguka kama akiwa ni Mutamattii (mtu anayejistarehesha kwa kufanya Umra kwanza kisha akaishi maisha ya kawaida kisha akahirimia Hija katika siku za Hija), au anayefanya Umra. Kisha aende kwenye jiwe jeusi (Hajarul-Aswad) na alielekee. Kisha atalisalimia kwa mkono wa kulia, na kulibusu ikiwa itakuwa rahisi kufanya hivyo. Vinginevyo, haifai kumdhuru mtu mwingine kwa kuleta msongamano. Anapolisalimia, aseme: 'Bismillah, Allahu Akbar (kwa jina la Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu ni Mkubwa),' au aseme: 'Allahu Akbar (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa).' Na ikiwa itakuwa vigumu kulibusu, basi atalisalimia kwa mkono wake au fimbo au mfano wa hivyo, na kisha atabusu kile alicholisalimia kwacho. Na ikiwa ni vigumu kulisalimia, ataliashiria tu na aseme "Mwenyezi Mungu ni Mkubwa" lakini asibusu kile alichoashiria kwacho. Ni sharti ili kuzunguka Al-Ka'aaba kuwe sahihi, kwamba mtu anayezunguka awe safi kutokana hadathi ndogo na kubwa. Kwa sababu kutufu ni kama swala, isipokuwa ilihurusiwa kuzungumza ndani yake. Ataiweka Nyumba upande wake wa kushoto wakati wa kutufu. Akisema mwanzoni mwa tawafu yake: “Ewe Mwenyezi Mungu, haya ni kutokana na kukuamini, kusadiki Kitabu chako, kutimiza ahadi yako na kufuata Sunna ya Mtume wako Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, basi hilo ni zuri. Kwa sababu lilisimuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Na atazunguka Ka'aba mara saba, na atatembea haraka katika mizunguko mitatu ya kwanza ya tawafu ya kwanza, ambayo ni tawafu anayofanya anapofika Makkah, iwe anafanya Umra, mtu ajifurahishaye kwa Umra kabla ya Hija (Mutamatti), anayefanya Hija peke yake, au mtu anayefanya Hija pamoja na Umra kwa pamoja. Kisha atatembea kama kawaida katika mizunguko minne iliyobakia. Ataanza kila mzunguko kwenye lile Jiwe jeusi na kumalizia hapo.
Na 'ar-ramal' ni kwenda mwendo wa haraka kwa hatua za karibu karibu. Pia inapendekezwa afanye 'idhtwibaa' katika tawafu hii yote, na sio katika tawafu nyinginezo. Idhtwibaa: Inamaanisha kuweka sehemu ya katikati ya shuka yake chini ya bega lake la kulia na ncha zake kwenye bega lake la kushoto.
Na ikiwa atapata mashaka kuhusu idadi ya mizunguko aliyofanya, atajenga uhakika juu ya idadi aliyo na uhakika nayo, ambayo ni ya chini zaidi. Kwa hivyo, ikiwa atashuku kama ametufu mizunguko mitatu au minne, basi atachukua uamuzi kwamba amezunguka mitatu. Na atafanya vivyo hivyo katika sa'ayi.
Na baada ya kumaliza tawafu hii, atavaa shuka yake bila ya kuliacha bega lake wazi na ataziweka pande zake mbili kwenye kifua chake kabla ya kuswali rakaa mbili za baada ya tawafu.
Na kinachopaswa kukemewa kwa wanawake na kuwakataza ni kufanya tawafu wakiwa wamevaa mapambo na manukato mazuri, na kutojisitiri ilhali wao ni uchi. Kwa hivyo, inapaswa kujisitiri na kuacha mapambo wakati wa tawafu na katika hali nyinginezo wanazochanganyika na wanaume; kwa sababu wao ni uchi na ni fitina (majaribu). Uso wa mwanamke ndio sehemu ya mapambo yake ya wazi zaidi, kwa hivyo haifai kuufunua isipokuwa kwa maharimu wake tu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao." ([65]) [An-Nur: 31] Basi hawaruhusiwi kufunua uso wao wakati wanapolibusu jiwe jeusi (Hajarul-Aswad) ikiwa wanaume wanawaona. Na ikiwa haitakuwa rahisi kwao kupata nafasi ya kuligusa na kulibusu, basi hawafai kusongamana na wanaume; badala yake, watatufu kwa nyuma yao, na hilo ni bora kwao na litakalowapa thawabu kubwa zaidi kuliko kutufu karibu na Ka'aba huku wanasongamana na wanaume. Kuzidisha kasi katika kuzunguka Al-Ka'aba na kuwacha wazi bega la kulia hayaruhusiwi isipokuwa katika tawafu hii tu, wala hata katika Sa’ayi, wala kwa wanawake. Kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakufanya Ramal na Idhtwiba’ isipokuwa katika tawafu yake ya kwanza, aliyoifanya alipofika Makka. Na anapaswa kuwa safi kutokana na hadathi zote na machafu anapofanya tawafu, na amnyenyekee Mola wake Mlezi, na ajishushe chini kwa ajili yake.
Na inapendeza kwake kumtaja Mwenyezi Mungu kwa wingi na kuomba dua katika tawafu yake, na ikiwa atasoma ndani yake kitu chochote kutoka katika Qur'ani, basi ni bora. Na hakuna dhikri (uradi) maalumu wala dua maalumu katika tawafu hii wala tawafu nyingine yoyote, wala katika sa'ayi.
Na kuhusu kile kilichozushwa na baadhi ya watu cha kutoa dhikri maalumu au dua maalumu katika kila mzunguko wa kando ya Ka'aba au katika sa'ayi, hilo halina msingi wowote. Bali chochote kitakachokuwa rahisi katika dhikri na dua kitatosheleza. Na wakati anapofika usawa na ar-Rukn al-Yamani (kona ya Ka'aba inayoelekea Yemen), ataigusa kwa mkono wake wa kulia, na kusema: 'Bismillah, Allahu Akbar (kwa jina la Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu ni Mkubwa),' lakini asiibusu. Ikiwa itakuwa vigumu kwake kuigusa, basi ataachana nayo na aendelee na tawafu yake. Asiiashirie kwa mkono wala kusema takbira (Allahu Akbar) wakati anapokuwa sawa nayo; kwa sababu hayo hayakuthibiti kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwa kadiri tunavyojua. Na inapendekezwa aseme kati ya kona hiyo ya Yemen kulia na jiwe jeusi (Hajarul-Aswad): "Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema na akhera tupe mema na utukinge na adhabu ya moto." ([66]) [Al-Baqara: 201]. Kila wakati anapofika katika jiwe jeusi (al-Hajar al-Aswad), ataligusa na kulibusu, na kusema: 'Allahu Akbar.' Ikiwa haitakuwa rahisi kwake kuligusa na kulibusu, basi ataliashiria na kutoa takbira (Allahu Akbar) kila atakapolifikia.
Hakuna ubaya wowote kufanya tawafu nyuma ya kisima cha Zamzam na Maqam ibrahim, hasa wakati wa msongamano. Msikiti mzima ni sehemu ya kufanyia tawafu, na hata ikiwa atafanya tawafu katika sehemu za juu za msikiti, hilo litatoshelea. Hata hivyo, kufanya tawafu karibu na Kaa'bah ndio bora ikiwa hilo litakuwa rahisi.
Mara tu atakapomaliza tawafu, ataswali rakaa mbili nyuma ya Maqam Ibrahim ikiwa hilo litakuwa rahisi. Na ikiwa halitakuwa rahisi kwa sababu ya msongamano au sababu nyingine, ataswali rakaa mbili katika sehemu yoyote ya msikiti. Ni sunna asome ndani yake baada ya Al-Fatiha: "Sema: Enyi makafiri!" [Al-Kaafiruun: 1] katika rakaa ya pili, na: "Sema: 'Yeye Mwenyezi Mungu ni wa pekee." ([68]) [Al-Ikhlaas: 1] katika rakaa ya pili. Hili ndilo bora, lakini ikiwa atasoma nyinginezo zozote badala yake, basi hakuna ubaya wowote. Kisha, atajiandaa kwenda katika jiwe jeusi (Hajarul-Aswad) na kuligusa kwa mkono wake wa kulia ikiwa hilo litakuwa rahisi; kwa kumuiga Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika hilo.
Kisha atatoka kwenda Mlima Swafa kupitia mlango unaoelekea huko, aupande au asimame karibu nao. Kupanda kwenye Safa ndiyo bora ikiwa hilo litakuwa rahisi. Atasoma wakati wa kuanza mzunguko wa kwanza kati ya vilima hivyo kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika vilima vya Safa na Marwa ni katika alama za Mwenyezi Mungu." ([69]) [Al-Baqarah: 158].
Na inapendekezwa kwamba aelekee Kibla, amsifu na kumtukuza Mwenyezi Mungu, aseme: "Hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa. Hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika, ufalme ni wake na sifa njema ni zake, huhuisha na hufisha, naye ni Muweza wa kila kitu. Hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, alitimiza ahadi yake, akamnusuru mja wake na akashinda makundi ya maadui peke yake." Kisha ataomba dua kwa chochote kitakachokuwa chepesi huku ameinua mikono yake juu, na atairudia dhikri hii na dua (mara tatu). Kisha atashuka na kutembea kwenda Marwa hadi atakapofika kwenye alama (taa) ya kwanza, hapo mwanamume ataharakisha mwendo katika safari ya kwanza mpaka afikie alama (taa) ya pili. Ama mwanamke, yeye hajawekewa kuharakisha mwendo katika sheria kati ya alama mbili hizo, kwa sababu yeye ni uchi. Badala yake, inampasa kutembea katika sa'ayi yote. Kisha atatembea na kupanda Marwa au atasimama karibu nayo. Na kupanda juu yake ni bora ikiwa hilo litakuwa rahisi. Atasema na kufanya juu ya Marwa kama alivyosema na kufanya juu ya Safa, isipokuwa kusoma aya ile, ambayo ni kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika vilima vya Safa na Marwa ni katika alama za Mwenyezi Mungu." ([70]) [Al-Baqarah: 158], Hilo limewekwa tu wakati wa kupanda juu ya Safa katika mzunguko wa kwanza pekee; kwa kufuata mfano wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake. Kisha atashuka na kutembea mahali pa kutembea, na ataharakisha mahali pa kuharakisha mpaka afike Marwa. Atafanya hivyo mara saba, ambapo kwenda ni mzunguko mmoja na kurudi ni mzunguko nyingine; kwa sababu Mtume rehema na amani ziwe juu yake alifanya hivyo na akasema: "Chukueni kutoka kwangu ibada zenu za Hija." ([71]) Na inapendekezwa kwa hujaji kufanya dhikri na dua nyingi katika Sa'ayi yake kwa kiasi atakachoweza, na awe safi kutokana na hadathi kubwa na ndogo. Lakini hata kama atafanya sa'ayi huku hana twahara, hilo litamtosheleza tu. Vivyo hivyo, ikiwa mwanamke atapata hedhi au damu ya baada ya kuzaa baada ya tawafu, atafanya sa'ayi, na hiyo itamtosheleza; kwa sababu twahara si sharti katika sa'ayi, lakini ni jambo linalopendekezwa tu kama ilivyotangulia hapo awali. [51] Imeshatangulia kuelezwa aliyeipokea.
Basi atakapomaliza sa'ayi, atanyoa au kupunguza nywele, lakini kunyoa kwa mwanaume ndiyo bora. Ikiwa atapunguza na akaacha kunyoa kwa ajili ya Hija, hilo ndilo nzuri. Na ikiwa kuwasili kwake Makka ni karibu na wakati wa Hija, basi kupunguza nywele ndiko bora, ili anyoe sehemu ya nywele zake iliyobakia katika Hija; kwa sababu Mtume rehema na amani ziwe juu yake alipofika Makka yeye na Maswahaba wake katika siku ya nne ya Dhul-Hijja, aliamuru wale ambao hawakusafiri pamoja na vichinjwa vyao watoke katika ihraam na wapunguze nywele zao, na hakuwaamuru kunyoa. Wakati wa kufupisha nywele, ni lazima kufupisha kichwa kizima wala haitoshi kufupisha baadhi yake tu, kama vile kunyoa baadhi yake haitoshi kunyoa baadhi ya nywele tu. Mwanamke hajawekewa katika sheria isipokuwa kufupisha tu. Atapunguza katika kila mshiko wa nywele kiasi cha moja ya sehemu tatu za kidole au chini kidogo tu, na haruhusiwi kupunguza zaidi ya hivyo.
Basi, muhrim atakapofanya yale yaliyotajwa, basi Umra yake itakuwa imeshakamilika na hapo atakuwa ameruhusiwa kufanya kila kitu ambacho kilikuwa kimeharamishwa kwake kwa sababu ya ihraam, isipokuwa ikiwa alileta mnyama wake wa kichinjwa pamoja naye kutoka nje ya eneo takatifu. Hapo ataendelea kuwa katika ihraam hadi atakapomaliza Hija na Umra kwa pamoja.
Na ama yule aliyehirimia Hija peke yake, au alihirimia Hija na Umra zote kwa pamoja, huyo ni sunna kwake kuvunja ihraam yake na kuifanya kuwa Umra, na kufanya kile ambacho Mutamatti hufanya, isipokuwa kama alikuwa ameleta mnyama wa dhabihu; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake aliwaamuru Maswahaba wake kufanya hivyo, na akasema: "Laiti ingekuwa sijaleta mnyama wa dhabihu, basi ningetoka katika ihram pamoja nanyi." ([72]) (52) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1568.
Na ikiwa mwanamke atapata hedhi au damu ya baada ya kuzaa baada ya kuhirimia umra, hatakiwi kuzunguka Al-Kaaba wala kati ya Safa na Marwa hadi atakapokuwa safi. Atakapokuwa safi, atatufu, afanye sa'ayi, na atapunguza nywele za kichwa chake, na umra yake itakuwa imekamilika kwa hayo. Ikiwa hatakuwa safi kabla ya siku ya Tarwiya (siku ya nane), atahirimia Hija katika mahali anapokaa, na ataondoka pamoja na watu kwenda Mina, na kwa hilo atakuwa katika hali ya kuwa mtu aliyejumuisha Hija na Umra (Qarin). Atafanya yale yote ambayo hujaji hufanya, kama vile kusimama Arafa, maeneo matakatifu, kurusha vijiwe kwenye Jamaraat, kulala usiku Muzdalifa na Mina, kuchinja dhabihu wake na kupunguza nywele za kichwa. Na anapokuwa safi, atazunguka Al-Ka'aba, afanye sa'ayi kati ya Safa na Marwa. Tawafu yake itakuwa moja na pia sa'ayi moja, na hayo yatamtosheleza katika Hija na Umra vyote kwa pamoja; kwa sababu ya hadithi ya Aisha kwamba alikuwa katika hedhi baada ya kuhirimia umra, na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake akamwambia: "Fanya kama anavyofanya hujaji isipokuwa usizunguke nyumba (Al-Ka'aba) hadi utakapokuwa safi." ([73]) Bukhari na Muslim wamekubaliana juu ya usahihi wa hadithi hii. (53) Kaipokea Bukhari kwa nambari 305, na Muslim kwa nambari 1211.
Na mwanamke aliye katika hedhi au aliye na nifasi atakaporusha vijiwe kwenye Jamarat siku ya Idul Adh-haa na akapunguza nywele za kichwa chake, basi atakuwa ameshahalalishiwa kila kitu ambacho kilikuwa haramu kwake kutokana na ihraam, kama vile kutumia manukato na vinginevyo, isipokuwa kuingiliana na mume wake hadi atakapokamilisha Hija yake kama ilivyo kwa wanawake wengine walio safi. Basi wakati atakapomaliza kutufu na kufanya sa'ayi baada ya kusafika, ataruhusiwa kuingiliana na mume wake.
Mlango:
Kuhusu hukumu ya kuhirimia Hija siku ya nane ya Dhul-Hijjah na kutoka kwenda Mina
Inapokuwa ni siku ya Tarwiya, ambayo ni siku ya nane ya Dhul-Hijja, inapendekezwa kwa wale walioko Makkah na wote wanaotaka kwenda Hija miongoni mwa watu wake wahirimie Hija kutoka katika makazi yao; kwani Maswahaba wa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, walishukia na kukaa huko Al-Abtah na wakahirimia Hija kutokea hapo siku ya Tarwiya kwa amri ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, hakuwaamrisha waende kwenye Nyumba na wahirimie hapo wala kwenye mfereji wa maji. Vilevile, hakuwaamuru wafanye tawafu ya kuaga walipokuwa wanatoka kwenda Mina. Na kama hilo lingekuwa katika sheria, basi angeliwafundisha kuhusiana nalo. Na heri yote ipo katika kumfuata Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na Maswahaba zake, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao.
Pia inapendekezwa kuoga, kujisafisha na kupaka manukato wakati wa kuhirimia Hija, kama alivyofanya wakati alipohirimia kwenye Miqat. Baada ya kuhirimia Hija, ni sunna kwake aende Mina kabla au baada ya Adhuhuri ya siku ya Tarwiya (siku ya nane), na wafanye Talbiya kwa wingi hadi watakaporusha vijiwe kwenye Jamratul-Aqaba. Huko Mina wataswali swala ya Adhuhrui, na Lasiri, na Magharibi, na Ishaa na Alfajiri. Na sunna ni kwamba waswali kila swala katika wakati wake kwa kuifupisha, bila ya kuziunganisha pamoja, isipokuwa Magharibi na Alfajiri ambazo hazifupishwi.
Hakuna tofauti kati ya watu wa Makka na wengineo; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake aliwaswalisha watu wa Makka na wengineo huko Mina, Arafa na Muzdalifa kwa kuzifupisha, na hakuwaamuru watu wa Makka kukamilisha swala zao. Na kama lingekuwa ni jambo la lazima kwao, basi angewabainishia hilo.
Baada ya kuchomoza jua katika siku ya Arafa, hujaji atatoka Mina aelekee Arafa, na ni sunna kushukia huko Namira hadi adhuhuri, ikiwa hilo ni rahisi kwao; kwa sababu Mtume rehema na amani ziwe juu yake alifanya hivyo.
Wakati jua linapopita katikati ya mbingu, ni sunna kwa imam au naibu wake kuwatolea watu hotuba inayohusiana na hali yao, akieleza ndani yake yale anayopaswa hujaji kufanya katika siku hii na baada yake, akiwaamrisha ndani yake kumcha Mwenyezi Mungu, kumpwekesha na kumkusudia Yeye peke yake katika kila jambo, na kuwaonya dhidi ya mambo aliyoyaharamisha, akiwausia ndani yake kushikamana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna za Mtume rehema na amani ziwe juu yake, na kutoa hukumu kwa mujibu wake, na kuvirudia katika kila jambo; kwa kumfuata Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake katika mambo haya yote. Baada ya hotuba hiyo, wataswali swala ya Adhuhuri na Lasiri kwa kizifupisha na kwa kuziunganisha pamoja, kwa adhana moja na iqama mbili; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mweneyzi Mungu ziwe juu yake alifanya hivyo. Imepokelewa na Muslim kutoka kwa Jabir, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.
Kisha watu watasimama Arafa, na Arafa yote ni mahali pa kusimama isipokuwa bonde la 'Urana. Na inapendekezwa kuelekea Kibla na mlima Rahma ikiwa hilo litawezekana. Lakini ikiwa kuelekea huko hukuwezekani, ataeleka Kibla hata kama hataelekea mlima huo. Na inapendekezwa kwa hujaji katika mahali hapa kujitahidi katika kumtaja Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kumuomba, na kumnyenyekea na kuinua mikono yake juu wakati wa dua. Ikiwa atafanya Talbiya au kusoma kitu chochote cha Qur'ani, basi hilo ni vizuri. Pia inapendekezwa kusema sana: "La ilaaha illallah wahdahu laa shariika lahu, lahul-mulk walahul-hamd, yuhyi wa yumiitu wahuwa 'alaa kulli shay-in qadiir (hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika. Ufalme ni wake, na sifa njema zote ni zake. Yeye huhuisha na hufisha. Naye ni Muweza wa kila kitu)." Hili ni kwa mujibu wa kile kilichosimuliwa kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Dua bora ni dua ya siku ya Arafa. Na kitu bora zaidi nilichosema mimi na Manabii waliotangulia kabla yangu ni: La ilaaha illallah wahdahu laa shariika lahu, lahul-mulk walahul-hamd, yuhyi wa yumiitu wahuwa 'alaa kulli shay-in qadiir (hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika. Ufalme ni wake, na sifa njema zote ni zake. Yeye huhuisha na hufisha. Naye ni Muweza wa kila kitu)." ([74]) Na imethibiti kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema: "Maneno yanayopendeza zaidi kwa Mwenyezi Mungu ni manne: Sub-haanallah (ametakasika Mwenyezi Mungu), wal-hamdulillah (sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu), wa laa ilaaha illallah (hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu), wallahu Akbar (na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa)." ([75] [54] Ameipokea Tirmidhiy kwa namba 3585. (55) Kaipokea Muslim kwa nambari 2137.
Kwa hivyo, inapasa kusema dhikiri hii kwa wingi na kuirudia kwa unyenyekevu na uwepo wa moyo. Na inapasa pia kusema kwa wingi nyiradi na dua zilizokuja katika sheria katika kila wakati, na hasa katika mahali hapa na katika siku hii tukufu, na anafaa kuchagua dua na nyiradi fupi zenye maana pana.
* Sub-hana llahi wabihamdihi, Sub-haana llahil-'adhwimi (Utakasifu ni wa Mwenyezi Mungu na sifa ni zake. Utakasifu ni wa Mwenyezi Mungu Mkuu). "Laa ilaaha illa anta sub-haanaka innii kuntu minadhdhwaalimiin (Hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Wewe, utakasifu ni wako, hakika mimi nilikuwa miongoni mwa madhalimu)." ([76]) [Al-Anbiya: 87].
* Laa ilaha illallah, wala na'abudu ila iyaahu, lahun-ni'imata walahulfadhal walahuth-thanaaul-hasan. La ilaha illallah, mukhliswiina lahud-diin walau karihal-kaafiruun (Hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, wala hatumuabudu yeyote isipokuwa Yeye tu. Yeye ndiye mwenye neema, na Yeye ndiye mwenye fadhila, na Yeye ndiye mwenye sifa nzuri. Hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, tunamsafia Dini Yeye tu hata kama watachukia makafiri).
* La haula walaa quwwata illa billaah (Hakuna uwezo wala nguvu ila kwa Mwenyezi Mungu). ([77]) [56] Kaipokea Muslim kutoka kwa Ibn az-Zubayr, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 594.
"Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema na akhera tupe mema na utukinge na adhabu ya Moto." ([78]) [Al-Baqara: 201]
* Allaahumma aslih lii diinii alladhii huwa ‘ismatu amrii, wa aslih lii dunyaaya allati fiiha ma‘aashi, wa aslih lii aakhiratii allatii fiiha ma‘aadii, waj‘al al-hayaata ziyaadatan lii fii kulli khair, waj‘al al-mauta raahatan lii min kulli sharri: (Ewe Mwenyezi Mungu nitengenezee dini yangu ambayo ndiyo kinga ya jambo langu. Na nitengenezee dunia yangu ambayo kunapatikana maisha yangu. Na nitengenezee Akhera yangu ambako ndiko nitakakorudi. Na fanya uhai wangu uzidi kwenye kila lenye heri. Na kifanye kifo kuwa raha kwangu dhidi ya kila uovu). ([79]) [57] Imepokelewa na Muslim kutoka kwa Abu Hurairah, Mwenyezi amuwiye radhi, nambari 2720.
* A‘ūdhu billāh min jahd al-balā, wa darak ash-shaqā, wa sūal-qadhwā, wa shamātat al-a‘dā: (Ninakimbilia kwa Mwenyezi Mungu kutokana na balaa zito, na kupatwa na uovu, na hukumu mbaya, na furaha ya maadui (kwa maumivu yangu). ([80]) [58] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abu Hurairah, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa nambari 6347.
Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi ninataka hifadhi kwako kutokana na msongo wa mawazo na huzuni, na ninataka hifadhi kwako kutokana na kushindwa na uvivu, na ninataka hifadhi kwako kutokana na woga na ubahili, na kutokana na dhambi na kugharamika, na ninataka hifadhi kwako kutokana na kuelemewa na madeni na kutokana na kutenzwa nguvu na watu. ([81]) [59] Kwa maneno haya. Ameipokea Abuu Daud kutoka kwa Abu Umama Al-Answari bila ya maneno haya: "Na kutokana na madhambi na kugharimika", nambari 1554.
"Ewe Mwenyezi Mungu hakika Mimi najikinga kwako kutokana na ukoma, na wazimu, na mbaranga na kutokana na maradhi mabaya." ([82]) [60] Ameipokea Abu Daud kutoka kwa Anas, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa nambari 1554.
* Allāhumma inni as’aluka al-‘afw wal-‘āfiya fid-dunya wal-ākhirah (Ewe Mwenyezi Mungu, hakika mimi ninakuomba msamaha na salama katika dunia na akhera).
* Allāhumma inni as’aluka al-‘afw wal-‘āfiya fi dīnii wa dunyāy wa ahli wa māli (Ee Mwenyezi Mungu, ninakuomba msamaha na afya njema katika dini yangu, na dunia yangu, na familia yangu, na mali yangu).
* Allāhumma ustur ‘aurāti wa āmin raw‘āti. Allāhumma hfadhni min baini yadayya wa min khalfii wa ‘an yamīni wa ‘an shimāli wa min fawqi wa a‘ūdhu bi‘adhwamatika an ughtāla min tahti: (Ewe Mwenyezi Mungu, ficha uovu wangu na uitulize hofu yangu. Ewe Mwenyezi Mungu nilinde kutoka mbele yangu, na nyuma yangu, kuanzia upande wangu wa kulia na kushoto, na juu yangu, na najilinda na ukubwa wako nisishambuliwe kutoka chini yangu). ([83]) [61] Ameipokea Abuu Daud kutoka kwa Ibn Omari, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa nambari 5074.
* Allāhumma ighfirli jiddi wa hazli wa khata’i wa ‘amdi wa kullu dhalika ‘indi. Allāhumma ighfirli ma qaddamtu wa ma akhkhart, wa ma asrartu wa ma a‘lant, wa ma anta a‘lamu bihi minni. Anta al-muqaddimu wa anta al-mu’akhkhiru wa anta ‘ala kulli shay-in qadīr: (Ewe Mwenyezi Mungu, nisamehe vichekesho vyangu, na michezo yangu, na makosa yangu, na madhambi yangu, na yote hayo nimeyafanya mimi. Ewe Mwenyezi Mungu, nisamehe dhambi zangu za mbele na dhambi zangu za nyuma, na zile nilizofanya kwa siri na zile nilizofanya kwa dhahiri, na zile unazozijua zaidi kuliko mimi. Wewe ndiwe mwenye kutanguliza na mwenye kuchelewesha, na Wewe ni Muweza wa kila kitu). [62] Ni sehemu katika Hadithi iliyopokelewa na Muslim kutoka kwa Abuu Musa Al-Ash’ari, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 2719.
* Allāhumma inni as-aluka ath-thabāt fil-amr wa al-‘azeemah ‘ala ar-rushd wa as-aluka shukra ni‘imatika wa husna ‘ibādatika wa as-aluka qalban salīman wa lisānan sādiqan wa as-aluka min khayri ma ta‘alamu wa a‘ūdhu bika min sharri ma ta‘alam wa astaghfiruka lima ta‘alam, innaka ‘allāmu al-ghuyūb: (Ewe Mwenyezi Mungu, ninakuomba uthabiti katika jambo na maamuzi ya kuelekea kwenye haki, na ninakuomba kushukuru neema zako na ibada nzuri kwako, na ninakuomba moyo safi na ulimi wa kweli, na ninakuomba kutoka katika kila kheri unayojua, na naomba kujiepusha na shari yoyote unayoijua, na nakuomba msamaha kwa yale unayoyajua. Hakika Wewe ni Mjuzi wa yote yaliyofichikana). ([85]) [63] Ameipokea Tirmidhiy kutoka kwa Shaddad bin Aws, Mwenyezi Mungu amuwiey radhi, nambari 3407.
* Allāhumma rabban-nabiyyi Muhammadin ‘alayhi as-swalātu was-salām ighfirli dhanbi wa adh-hib ghaidha qalbi wa a‘jirnii min mudhwillāt al-fitani ma ahyaytanii: (Ewe Mwenyezi Mungu, Mlezi wa Nabii Muhammad rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, nisamehe dhambi zangu, ondoa hasira kutoka ndani ya moyo wangu, na niokoe kutokana na mitego, kwa muda wote utakaoniacha niendelee kubakia hai). [64] Ameipokea Ahmad kutoka kwa Hadithi ya Ummu Salama, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, Juzuu 6/301.
"Ewe Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa mbingu (saba) na Mola Mlezi wa ardhi, na Mola Mlezi wa Kitu cha Enzi kitukufu, Mola wetu Mlezi na Mola Mlezi wa kila kitu, mwenye kupasua mbegu na kokwa, na mwenye kuteremsha Taurati na Injili na Qur'ani, najikinga kwako kutokana na shari ya kila kitu wewe ni mwenye kukishika kwa nywele za utosi. Ewe Mwenyezi Mungu, wewe ndiye wa mwanzo, hakuna kitu kabla yako. Na wewe ndiye wa mwisho, hakuna kitu baada yako. Na wewe ni wa wazi (wa juu zaidi), hakuna kitu juu yako. Na wewe ndiye wa ndani, hakuna kitu chini yako. Tulipie madeni na ututosheleze kutokana na ufakiri." ([87]) [65] Imepokelewa na Muslim kutoka katika Hadithi ya Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 2713.
* Allāhumma i‘twi nafsi taqwāha wa zakkiha anta khairu man zakkāha anta waliyyuha wa mawlāha. Allāhumma inni a‘ūdhu bika min al-‘ajzi wal-kasal wa a‘ūdhu bika min al-jubni wal-haram wal-bukhl wa a‘ūdhu bika min ‘adhāb al-qabr: (Ewe Mwenyezi Mungu, ipe roho yangu ucha Mungu wake, na itakase, Wewe ni Mbora wa kuisafisha, Wewe ni Mfalme wake na Mola wake. Ewe Mwenyezi Mungu, naomba hifadhi kwako kutokana na kushindwa na kutokuwa na nguvu, naomba hifadhi kwako kutokana na uoga na uchovu, naomba hifadhi kwako kutokana na ubahili na adhabu ya kaburi). ([88]) [66] Imepokelewa na Muslim kutoka katika Hadithi ya Zaid bin Arqam, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 2722.
* Allāhumma laka aslamtu wa bika āmantu wa ‘alaika tawakkaltu wa ilaika anabtu wa bika khāswamtu. A‘ūdhu bi‘izzatika an tudhwillani, la ilāha illa ant, anta Al-Hayy al-ladhi la yamūtu wal-jinn wal-ins yamūtūn: (Ewe Mwenyezi Mungu kwa ajili yako nimejisalimisha, na kwako nimeamini, na juu yako nimetegemea, na kwako nimejisogeza, na kwa ajili yako napambana. Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi najikinga kwako kwa utukufu wako kutonipoteza, hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Wewe, Wewe ndiye uliye hai ambaye hafi, na majini na watu wanakufa). ([89]) [67] Imepokelewa na Muslim kutoka katika hadithi ya Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, nambari 2717.
* Allāhumma inni a‘ūdhu bika min ‘ilmin la yanfa‘, wa min qalbin la yakhsha‘, wa min nafsin la tashba‘, wa min da‘awatin la yustajābu laha: (Ewe Mwenyezi Mungu, naomba hifadhi kwako kutokana na elimu isiyo na manufaa, na moyo usiojaa hofu, na nafsi isiyoshiba, na dua isiyojibiwa). ([90]) [68] Hii ni sehemu katika Hadithi ya Zaid bin Arqam, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, ambayo imeshatagulia kuelezwa aliyeipokea kwa nambari 2722.
* Allāhumma jannibni munkarāt al-akhlāq wal-a‘māl wal-ahwā’ wal-adwā: (Ewe Mwenyezi Mungu, ninakuomba uniweke mbali na maadili maovu, matendo mabaya, na tamaa na magonjwa).([91]) [69] Ameipokea Tirmidhiy kutoka kwa Ziyad bin 'Alaqah kutoka kwa ami yake, nambari 3591.
* Allāhumma alhimni rushdi wa a‘idhni min sharri nafsii: (Ewe Mwenyezi Mungu nijaze uongofu, na unikinge na shari ya nafsi yangu). ([92]) [70] Ameipokea Tirmidhiy kutoka katika Hadithi ya Imran bin Huswein, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 3483.
* Allāhumma ikfini bihalālika ‘an harāmik waghnini bifadhlika ‘amman siwāka: (Ewe Mwenyezi Mungu nitosheleze kwa halali yako dhidi ya haramu yako, na unitajirishe kwa fadhila zako nisimhitaji yeyote asiyekuwa Wewe). ([93]) [71] Ameipokea Tirmidhiy kutoka katika Hadithi ya Ali, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa namba 3563.
* Allāhumma inni as-alukal-huda wa at-tuqa wal-‘afāfa wal-ghina: (Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba uongofu na ucha Mungu na kujizuia na machafu na kuwa ni mwenye kutosheka). ([94]) [72] Ameipokea Muslim kutoka katika Hadithi ya Abdullah bin Masud, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 2721.
* Allāhumma inni as-alukal-huda was-sadād: (Ewe Mwenyezi Mungu, ninakuomba uongofu na ufanisi). ([95]) [73] Ameipokea Muslim kutoka katika Hadithi ya Ali, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 2725.
Allāhumma inni as-aluka min al-khayri kullihi, ‘ājilihi wa ājilihi, ma ‘alimtu minhu wa ma lam a‘lam. Wa a‘ūdhu bika min sh-sharri kullihi, ‘ājilihi wa ājilihi, ma ‘alimtu minhu wa ma lam a‘lam. Wa as-aluka min khairi ma sa-alaka minhu ‘abduka wa nabiyyuka Muhammadun sallallāhu ‘alayhi wa sallam, wa a‘ūdhu bika min sharri masta‘ādha minhu ‘abduka wa nabiyyuka Muhammadun sallallāhu ‘alaihi wa sallam. Allāhumma inni as-aluka al-jannata wa ma qarraba ilaiha min qawlin aw ‘amal, wa a‘ūdhu bika min an-nār wa ma qarraba ilaiha min qawlin aw ‘amal. Wa as-aluka an taj‘al kulla qadhwā’ qadhwaytuhu li khairan: (Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba (unipe) kutoka katika heri zote: zile za haraka na za kuchelewa, kwa ninayoyajua na nisiyoyajua, na najikinga kwako kutokana na shari zote zinazokuja haraka na zinazochelewa, kwa ninayoyajua na nisiyoyajua. Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi nakuomba (unipe) miongoni mwa heri alizokuomba mja wako na nabii wako, na ninajikinga kwako (uniepushe) na shari alizojikinga kwako mja wako na nabii wako. Ewe Mwenyezi Mungu hakika mimi ninakuomba pepo, na yaliyo karibu yake miongoni mwa kauli au matendo, na ninajikinga kwako kutokana na moto na yaliyo karibu na moto miongoni mwa kauli au matendo, na ninakuomba ujaalie kila hukumu utakayohukumu kwangu iwe ni heri). ([96]) [74] Ameipokea Ibn Majah kutoka katika Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwa nambari 3846.
* La ilāha illallāh wahdahu la sharīka lah, lahu al-mulku wa lahu al-hamdu, yuhyi wa yumītu biyadihi al-khair wa huwa ‘ala kulli shay’in qadīr. Subhānallāh, wal-hamdulillāh, wa la ilāha illallāh, wallāhu akbar, wa la hawla wa la quwwata illa billāh al-‘aliyy al-‘adhwīm: (Hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika. Ni wake ufalme na ni zake sifa njema. Yeye huhuisha na hufisha. Heri yote iko mikononi mwake, naye ni Muweza wa kila kitu. Ametakasika Mwenyezi Mungu, na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu peke yake, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, na hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, aliye juu, Mkuu). ([97]) [75] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Hadithi ya 'Ubada bin Al-Swamit, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 1154.
Allahumma swalli 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa swallaita 'alaa Ibraahima wa 'alaa aali Ibraahim, innaka hamiidum-majid. Wabaarik 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa barakta 'alaa Ibraahima wa 'alaa aali Ibraahim, innaka hamiidum-majid: (Ewe Mwenyezi Mungu mshushie Muhammad rehema, na jamaa zake Muhammad, kama ulivyomshushia rehema Ibrahim na jamaa za Ibrahim. Hakika Wewe ni Msifiwa, Mtukufu. Na mbariki Muhammad na jamaa zake Muhammad, kama ulivyombariki Ibrahim na jamaa zake Ibrahim. Hakika Wewe ni Msifiwa, Mtukufu). ([98]) [76] Imepokelewa na Bukhari kutoka katika Hadithi ya Ka’b bin 'Ujrah, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, nambari 3370.
Rabbana aatina fid-dunya hasanah wafil-aakhirati hasanah waqinaa ‘adhaaban-naar: (Ewe Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema na akhera tupe mema na utukinge na adhabu ya moto). ([99]) [Al-Baqara: 201]
Na inapendekezwa katika mahali hapa patukufu kwamba hujaji arudie dhikri na dua zilizotangulia na dhikri na dua nyinginezo zenye maana sawa na hizo, na kumswalia Mtume rehema na amani za Mweneyzi Mungu ziwe juu yake. Anafaa kusisitiza sana katika kuomba dua na kumuomba Mola wake Mlezi heri za dunia na akhera. Mtume rehema na amani ziwe juu yake alikuwa anapoomba, anarudia dua mara tatu, basi inafaa kumfuata katika hilo, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Katika mahali hapa, Muislamu anafaa kuwa mnyenyekevu mbele ya Mola wake Mlezi, Mtukufu, akiwa amejishusha chini kwa ajili yake, akiwa amevunjika mno mbele yake, akitarajia rehema na msamaha wake, na akiwa na hofu ya adhabu na hasira zake. Anapaswa kujihesabu mwenyewe juu ya matendo yake na kufanya tena toba ya kweli, kwani hii ni siku tukufu na mkusanyiko mkubwa ambapo Mwenyezi Mungu anawapa waja kwa wingi ndani yake, na hujivunia wao mbele ya Malaika wake, na anawaacha huru kwa wingi kutokana na Moto. Hakuna siku ambayo Shetani anaonekana dhalili zaidi ndani yake, wala mdogo zaidi, wala duni zaidi kuliko siku ya Arafa, isipokuwa alivyoonekana siku ya vita vya Badri. Hilo ni kutokana na yale anayoyaona katika fadhila nyingi za Mwenyezi Mungu juu ya waja wake, na wema wake kwao, na kuokoa kwake kwa wingi kutokana na Moto, na msamaha wake mkubwa.
Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa Aisha radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Hakuna siku ambayo Mwenyezi Mungu huwatoa zaidi waja Motoni kuliko siku ya Arafa. Hakika siku hiyo Mwenyezi Mungu husogea karibu, kisha anajifaharisha kwao mbele ya Malaika. Basi husema: Hawa wanataka nini?" ([100]) [77] Kaipokea Muslim kutoka katika Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 1348.
Kwa hivyo inafaa kwa Waislamu kumuonyesha Mwenyezi heri katika nafsi zao, na kumdunisha adui yao Shetani na wampe hizaya kwa kufanya dhikri na dua kwa wingi, na kushikamana na kutubu na kuomba msamaha kutokana na dhambi na makosa yote. Mahujaji watasalia katika pahali hapa wakijishughulisha na dhikri, dua na kumnyenyekea Mwenyezi Mungu hadi jua lizame. Na litakapozama, wataondoka waende Muzdalifa kwa utulivu na unyenyekevu, na wafanye Talbiya kwa wingi, na wanapopata mahali ambapo kuna nafasi kubwa, wanakwenda haraka; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alifanya hivyo. Hairuhusiwi kuondoka Arafa kabla ya jua kuzama, kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisimama hapo hadi jua lilipozama, na akasema: Chukueni kutoka kwangu ibada zenu za Hija." ([101]) "Chukueni kutoka kwangu ibada zenu za Hija." [78] [78] Imeshatangulia kuelezwa aliyeipokea.
Watakapofika Muzdalifa, wataswali Magharibi rakaa tatu na Ishaa rakaa mbili kwa pamoja kwa adhana moja na iqama mbili pindi wanapofika huko; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alifanya hivyo. Hili ni sawa wafike Muzdalifa wakati wa Magharibi au baada ya kuingia wakati wa Ishaa.
Na kile wanachokifanya baadhi ya watu wa kawaida cha kuchukua vijiwe vya kurushia Jamaraat kabla ya swala pindi tu wanapofika Muzdalifa, na wengi wao kuamini ya kwamba hilo ni jambo la kisheria, hilo ni kosa ambalo halina msingi wowote. Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake hakuwahi kuamrisha kuchukua vijiwe vya kurushia Jamaraat isipokuwa baada ya kutoka kwake kwenye maeneo matakatifu (Muzdalifa) kwenda Mina. Na pahali popote pale wanapochukua vijiwe hivyo, hilo litawatosheleza. Si lazima kuvichukua vijiwe hivyo huko Muzdalifa tu, bali inaruhusiwa kuvichukua Mina. Na lililo sunna ni kuchukua vijiwe saba siku hii ili kuvirusha kwenye Jamrat Al-Aqaba; ili kumfuata Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Ama katika siku tatu hizo, atachukua vijiwe hivyo Mina. Atachukua kila siku vijiwe ishirini na moja ili avitumie kurusha kwenye zile Jamaraat tatu.
Haipendekezwi kuosha vijiwe hivyo, bali atavirusha hivyo bila kuviosha. Kwa sababu hilo halikupokelewa kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na Maswahaba wake, na hairuhusiwi kurusha kijiwe ambacho tayari kimeshatumika.
Mahujaji watakaa usiku huko Muzdalifa, na inaruhusiwa kwa wanawake dhaifu, watoto, na wengineo mfano wao kwenda Mina mwishoni mwa usiku. Kwa mujibu wa Hadithi ya Aisha, na Ummu Salama na wengineo. Ama mahujaji wengineo, inasisitizwa kwamba wasalie huko mpaka wamalize swala ya alfajiri, kisha wasimame kwenye maeneo matakatifu (al-mash'ar al-haram), wakielekea Kibla na wamtaje Mwenyezi Mungu kwa wingi, kumtukuza na kuomba dua mpaka kupambazuke kabisa. Na inapendekezwa kuinua mikono hapa wakati wa kuomba dua. Na popote watakaposimama huko Muzdalifa, hilo litawatosheleza. Si lazima wawe karibu al-mash'ar au kupapanda; kwa mujibu wa kauli ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Nimesimama hapa - akimaanisha kwenye al-mash'ar - na kila sehemu ya Jam'u (Muzdalifa) ni sehemu ya kusimama." ([102]) Imepokelewa na Muslim katika Sahihi yake, na maana ya "Jama'u " ni Muzdalifa. [79] Kaipokea Muslim kutoka katika Hadithi ya Jabir, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 1218.
Wakishaanza kuona mwanga mkubwa wa asubuhi, wataondoka na kuelekea Mina kabla ya kuchomoza jua, na watatoa Talbiya kwa wingi katika safari yao. Pindi wakifika mahali panapoitwa Muhassir, inapendekezwa kwamba waharakishe mwendo kidogo.
Wanapofika Mina, wataacha kufanya Talbiya kwenye Jamrat Al-Aqaba, kisha watairushia vijiwe saba kwa mfululizo wanapoifikia, kwa kuinua juu mikono yao kila wanapoirushia kijiwe, na kusema "Allahu Akbar (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa)." Na inapendekezwa kuirushia vijiwe kutokea upande wa ndani ya bonde, na waiweke Ka'aba upande wao wa kushoto, na Mina upande wao wa kulia, kwa sababu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alifanya hivyo. Ikiwa watairushia vijiwe kutokea pande nyinginezo za Jamrat hiyo, hilo litatosheleza ikiwa vijiwe hivyo vitaingia ndani ya shimo la kandoni mwa Jamarat. Si sharti kwamba kijiwe kisalie ndani ya shimo la kandoni mwa Jamarat baada ya kuanguka humo, bali ni muhimu tu kwamba kiingie ndani yake. Ikiwa kijiwe kitaingia ndani ya shimo la kandoni mwa Jamarat kisha kikatoka nje yake, hilo litatosheleza kulingana na kauli iliyo dhahiri ya wanazuoni. Miongoni mwa wale waliosema haya wazi wazi ni An-Nawawi, Mwenyezi Mungu amrehemu, katika "Sharh Al-Muhadhdhab." Vijiwe vya kurusha kwenye Jamarat ni kama vikokoto vya kurusha kwa kidole, lakini ni vikubwa kidogo kuliko mbaazi.
Kisha baada ya kurusha vijiwe, atamchinja dhabihu wake, na inapendekezwa kwamba aseme wakati wa kumdunga kooni au kumchinja: Bismillahi Allahu Akbar. Allahumma hadhā minka wa laka (Kwa jina la Mweneyezi Mungu. Mwenyezi Mungu ni Mkubwa. Ewe Mwenyezi Mungu, huyu ni kutoka kwako na kwa ajili yako). Na amuelekeze Kibla. Na Sunna ni kumdunga ngamia kooni huku amesimama na amefungwa mkono wake wa kushoto, na kuchinja ng'ombe, mbuzi na kondoo wakiwa wamelalia upande wa kushoto. Ingawa kama atamchinja kuelekea kando na Kibla, atakuwa ameacha Sunna, lakini dhabihu wake huyo itamtosheleza. Kwa sababu kuelekea Kibla wakati wa kuchinja ni Sunna na si faradhi. Ni bora ale katika dhabihu wake, na pia kutoa zawadi au kufanya sadaka, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi kuleni katika hao na mlisheni mwenye shida aliye fakiri." ([103]) [Al-Hajj: 28], Wakati wa kuchinja unaendelea hadi kuzama kwa jua katika siku ya tatu siku za Tashriiq, kwa kauli sahihi zaidi miongoni mwa kauli za wanazuoni. Kwa hivyo, unakuwa muda wa kuchinja ni siku ya Idul-Adh-ha pamoja na siku tatu baada yake, ambazo ni siku ya 11, 12, na 13 za Dhul-Hijjah.
Kisha, baada ya kumdunga dhabihu kooni au kumchinja mnyama wa dhabihu, atanyoa nywele za kichwa chake au kuzipunguza, na kunyoa ni bora zaidi. Kwa sababu Mtume rehema na amani ziwe juu yake aliwaombea rehema na msamaha mara tatu wale walionyoa nywele zao na akawaombea msamaha mara moja wale waliopunguza nywele zao. Na haitoshi kupunguza sehemu tu ya kichwa, bali ni lazima kupunguza kichwa chote, kama vile kunyoa. Mwanamke anapaswa kupunguza urefu wa ncha ya kidole au kidogo zaidi kutoka katika mshiko wa nywele zake.
Baada ya kuzirushia vijiwe Jamrat al-Aqabah na kunyoa au kupunguza nywele za kichwa chake, kila kitu kilichoharamishwa kwake katika ihram kinakuwa halali isipokuwa kuwaingilia wanawake. Na huku kunaitwa kutoka katika ihram kwa kwanza. Ni sunna kwake baada ya kutoka huku kupaka manukato na kwenda Makka, ili kufanya Tawaf al-Ifadhwa; kwa mujibu wa Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba alisema: "Nilikuwa nikimpaka Mtume, rehema na amani ziwe za Mwenyezi Mungu juu yake, manukato kwa ajili ya Ihram yake kabla hajaingia katika Ihram, na kwa ajili ya kutoka kwake katika Ihram kabla ya kuzunguka kando ya Al-Ka'aba." ([104]) Imepokelewa na Bukhari na Muslim. (80) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1539, na Muslim kwa nambari 1189.
Tawaf hii inaitwa Tawaf al-Ifadhwa na Tawaf az-Ziyara. Nayo ni nguzo miongoni mwa nguzo za Hija ambazo bila hiyo, Hija haikamiliki, na ndiyo iliyokusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kisha wajisafishe taka zao, na waondoe nadhiri zao, na waizunguke Nyumba ya Kale." ([105]) [Al-Hajj: 29].
Kisha, baada ya tawafu na kuswali rakaa mbili nyuma ya Maqam Ibrahim (masimamio ya Ibrahim), atatembea kati ya Safa na Marwa ikiwa anafanya Hajj tamattu, na hii ndiyo sa'ayi ya Hija yake, na ile ya kwanza ilikuwa kwa ajili ya Umra yake.
Sa'ayi moja haitoshi, kwa mujibu wa kauli sahihi zaidi ya wanazuoni; kwa mujibu wa Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: “Tulitoka pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake..." kisha akataja Hadithi hiyo, na akasema ndani yake: “Na yule ambaye ana mnyama wake wa dhabihu pamoja naye, basi na ahirimie Hija pamoja na Umra, kisha asitoke katika Ihram mpaka atakapotoka katika ihram ya zote mbili kwa pamoja.” Mpaka aliposema: “Basi wale waliokuwa wamehirimia Umra waliizunguka Nyumba, Safa na Marwa, kisha wakatoka katika ihram, kisha wakafanya tawafu nyingine baada ya kurejea kutoka Mina kwa ajili ya Hija yao." ([106]) Imepokelewa na Bukhari na Muslim. (81) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1556, na Muslim kwa nambari 1211.
Na kauli yake, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuhusu wale waliohirimia Umra - "Kisha wakafanya tawafu nyingine baada ya kurejea kutoka Mina kwa ajili ya Hija yao"; inamaanisha kuzunguka baina ya Safa na Marwa kwa mujibu wa kauli sahihi zaidi katika kufasiri Hadithi hii. Ama kauli ya wale waliosema: Alikusudia Tawaf al-Ifadhwa, si sahihi. Kwa sababu Tawaful-Ifadhwa ni nguzo kwa kila mtu, nao tayari walikuwa wameshaifanya, lakini maana yake ni: Kinachomhusu mtu anayefanya Tamattu peke yake, ambacho ni sa'ayi baina ya Safa na Marwa kwa mara ya pili baada ya kurejea kutoka Mina ili kukamilisha Hija yake. Hilo liko wazi, na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu, na hii ndiyo kauli ya wanazuoni wengi.
Na usahihi wa kauli hii unaonyeshwa pia na yale aliyoyapokea Bukhari katika Sahihi yake, kwa mlolongo wa wasimulizi usiofika kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akiwa na uhakika juu yake, kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kwamba: Aliulizwa kuhusu Hajj Tamattu (kujistarehesha kwa kuishi maisha ya kawaida baada ya Umra kabla ya Hija), akasema: “Muhajirina, na Answari, na wake za Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake walihirimia katika Hija ya kuaga nasi pia tukahirimia. Tulipofika Makka, Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake akasema: "Fanyeni kuhirimia kwenu Hija kuwe kwa ajili ya Umra, isipokuwa wale waliowavisha kamba wanyama wao wa dhabihu.' ([90]) Basi tukaizunguka Nyumba na katika Safa na Marwa, tukawajia wanawake wetu na tukavaa nguo za kawaida. Kisha akasema: "Yeyote aliyemvisha kamba mnyama wake wa dhabihu asitoke katika ihram mpaka mnyama huyo wa dhabihu afike mahala pake.' ([91]) Kisha katika usiku wa kuamkia siku ya Tarwiya, akatuamrisha kuhirimia Hija. Tulipomaliza ibada za Hija, tulikuja (Makka) na tukaizunguka Nyumba, Safa na Marwa." ([107]) Kusudi lake lililokusudiwa limekwisha, nayo hadithi hii iko wazi kwamba mtu anayefanya Hija ya tamattu anafanya sa'ayi mara mbili. Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi. [82] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1572.
Na ama yale aliyopokea imamu Muslim kutoka katika Hadithi ya Jabiri, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwamba: “Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, na Maswahaba zake hawakuzunguka baina ya Safa na Marwa isipokuwa mara moja tu.” ([108]). Hayo yanamaanisha wale walioleta wanyama wao wa dhabihu pamoja nao; kwa sababu walisalia katika Ihraam yao pamoja na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake mpaka walipomaliza Hija na Umra kwa pamoja, na Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alihirimia Hija na Umra kwa pamoja, na akamuamrisha yeyote aliyekuja pamoja na mnyama wake wa dhabihu kwamba ahirimie Hija na Umra, na asitoke katika ihraam mpaka amalize zote mbili. Na anayeunganisha kati ya Hija na Umra hana isipokuwa kufanya sa’ayi moja tu, kama ilivyoashiriwa na Hadithi ya Jabir iliyotajwa hapo juu na Hadithi nyinginezo sahihi. [83] Kaipokea Muslim kwa nambari 1215.
Vile vile, mwenye kuhirimia Hija peke yake na akasalia katika ihram mpaka siku ya kuchinja, yeye halazimiki isipokuwa kufanya sa'ayi moja tu. Kwa hivyo, ikiwa mwenye kuunganisha Hija na Umra na mwenye kufanya Hija peke yake watafanya sa'ayi binafsi baada ya Tawaful-Qudum, hilo litawatosheleza kufanya sa'ayi nyingine baada ya Tawaful-Ifadhwa. Huku ndiko kuunganisha kati ya Hadithi ya Aisha na ya bin Abbas, na Hadithi ya Jabir Mwenyezi Mungu awe radhi nao, iliyotajwa hapo juu, na kwa hilo kunaondoka kupingana kuliopo na inawezekana kuzifanyia kazi hadithi zote hizi.
Katika yale yanayounga mkono muunganisho huu ni kuwa Hadithi ya Aisha na bin Abbas ni Hadithi sahihi, nao wamethibitisha sa'ayi ya pili kuhusiana na mwenye kufanya tamattu', na maana ya dhahiri ya hadithi ya Jabir inakanusha hilo, na kilichothibitika ndicho kinachotangulizwa mbele ya kinachokanushwa, kama ilivyothibiti katika elimu ya misingi na istilahi za Hadithi. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye mwenye kuwezesha kufikia usahihi, na hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu.
Mlango:
Kuhusu kueleza ubora wa yale anayoyafanya mwenye kuhiji, siku ya Nahr (kuchinja).
Ni bora kwa mwenye kuhiji kupanga mambo haya manne katika Siku ya kuchinja (Nahr), kama ilivyotajwa: Ataanza kwa kupiga mawe Jamarat al-Aqaba, kisha kuchinja, kisha kunyoa au kupunguza nywele zake, kisha kuzunguka Al-Ka'aba na sa'ayi baada yake kwa hujaji anayefanya Tamattu', na vivyo hivyo kwa yule anayefanya Hija peke yake na vile vile yule anayefanya Hija na Umra bila ya kupumzika kati yake ikiwa hawakufanya tawafu walipoingia Makkah. Na ikiwa atatanguliza baadhi ya mambo haya mbele ya mengine, hilo litamtosheleza; kwa sababu kuna ruhusa iliyothibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika suala hili. Hili ni pamoja na kutanguliza Sa’ayi mbele ya Tawaf. Kwa sababu ni miongoni mwa mambo yanayofanywa siku ya kuchinja, basi yamejumuishwa katika kauli ya Swahaba: Basi hakuulizwa siku hiyo chochote kilichofanywa kabla au baadaye isipokuwa alisema: "Fanya na wala hakuna ubaya.” ([109]) Na kwa sababu hayo ni katika mambo yanayosahaulika na kutoyajua, basi ikawa ni lazima yajumuishwe katika ujumla huu. Kwa sababu ya urahisi na wepesi ulio ndani yake. (84) Kaipokea Bukhari kwa nambari 83, na Muslim kwa nambari 1306.
Na imethibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyez Mungu ziwe juu yake, kwamba: "Hakuna tatizo". ([110]) Imepokelewa na Abuu Daud, kutoka katika Hadithi ya Usama bin Sharik yenye mlolongo sahihi wa wasimulizi. Kwa hivyo, ikaonekana wazi kwa hilo kwamba linajumuishwa katika ujumla huu bila shaka. Na Mwenyezi Mungu, ndiye mwenye kuwezesha. (85) Ameipokea Abuu Daud kwa nambari 2015.
Kuna mambo matatu ambayo humuwezesha hujaji kutoka kabisa katika ihram, nayo ni: Kupiga Jamratul-Aqaba kwa mawe kunyoa au kupunguza nywele zake, na Tawaf al-Ifadhwa pamoja na sa’ayi baada yake kwa vilivyotajwa kabla ya muda mfupi. Atakapofanya matatu haya, kila kilichoharamishwa kwake wakati wa ihraam, wakiwemo wanawake, manukato, na vitu vinginevyo, vinakuwa halali kwake. Na mwenye kufanya mawili katika hayo, anahalalishiwa kila kitu alichoharamishiwa kwa sababu ya ihraam isipokuwa wanawake, na hali hii inaitwa: kutoka katika ihram kwa kwanza.
Na inapendekezwa kwa hujaji kunywa maji ya Zamzam na kunywa kutoka humo na kushiba sawasawa, na kuomba dua yoyote yenye manufaa anayoweza. Na "Maji ya Zamzam huwa kwa kile yalichonywewa kwa ajili yake."([111]) Kama ilivyopokewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake katika Sahihi Muslim kutoka kwa Abuu Dharri, kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alisema kuhusu maji ya Zamzam: "Hakika ni chakula cha kutosheleza." ([112]) Abu Daud aliongeza: "Na ni ponyo la ugonjwa." ([113]) [86] Imepokelewa na Ibn Maja kutoka kwa Jabir bin Abdullah, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 3062. (87) Kaipokea Muslim kwa nambari 2473. [88] Anamaanisha Abuu Daud At-Tayalisi. Aliipokea katika hadithi yenyewe ya kisa cha kusilimu kwa Abuu Dharri, Mwenyezi Mungu amuwie radhi. Tazama Musnad Abi Daud At-Tayalisi nambari 459.
Baada ya Tawaf Al-Ifadhwah na Sa'ayi ya wale wanaopaswa kufanya Sa'ayi nyingine, mahujaji wanapaswa kurejea Mina na kukaa huko kwa siku tatu mchana na usiku wakipiga mawe kwenye zile Jamaraat tatu katika kila siku miongoni mwa hizo siku tatu baada ya adhuhuri, na lazima wazitupie Jamarat hizo kwa utaratibu.
Anaanza na Jamrat ya kwanza: Ambayo ni ile iliyo karibu na Msikiti wa Al-Khaif. Atairushia vijiwe saba mfululizo, akiinua mkono wake kwenye kila kijiwe, na ni Sunna kusogea mbali kutoka hapo na kuiweka Jamrat kushoto kwake, akielekea Kibla, akinyanyua mikono yake juu, na aombe dua kwa unyevunyevu mwingi.
Kisha ataitupia vijiwe Jamrat ya pili kama ya kwanza, na ni Sunna kwake kusogea mbele kidogo baada ya kuitupia vijiwe na kuifanya kulia kwake, na aelekee Kibla, anyanyue mikono yake na kuomba dua kwa wingi.
Kisha ataipiga vijiwe Jamrat ya tatu na asisimame hapo.
Kisha atazipiga mawe Jamarat zote katika siku ya pili ya siku za Tashriiq baada ya Adhuhuri, kama alivyozipiga kwa mawe siku ya kwanza, na atafanya hivyo kwenye Jamrat ya kwanza na ya pili kama alivyofanya siku ya kwanza; kwa kumfuata Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.
Na kupiga mawe Jamarat katika siku mbili za mwanzo za siku za Tashriiq ni miongoni mwa wajibu za Hija, na vile vile kukaa usiku wa kwanza na wa pili huko Mina isipokuwa kwa wateka maji, wachungaji mifugo na mfano wao. Wao hilo si wajibu kwao.
Kisha, baada ya kuzipiga vijiwe katika siku mbili zilizotajwa, anayependa kuharakisha kutoka Mina anaruhusiwa kufanya hivyo, lakini aondoke kabla ya kuzama kwa jua. Na mwenye kusalia na akakesha usiku wa tatu na akazipiga vijiwe Jamarat siku ya tatu, basi hilo ndilo bora na lenye malipo makubwa zaidi, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika zile siku zinazohesabiwa. Lakini mwenye kufanya haraka katika siku mbili (akarejea), si dhambi juu yake; na mwenye kukawia pia si dhambi juu yake, kwa mwenye kumcha Mungu." ([114]) [Suratul-Baqara: 203] Na kwa sababu Mtume rehema na amani ziwe juu yake aliwapa watu ruhusa ya kuharakisha kutoka huko, lakini yeye hakufanya haraka, bali alikaa Mina mpaka alipozipiga vijiwe Jamarat siku ya kumi na tatu baada ya Adhuhuri, kisha akatoka kabla ya kuswali Dhuhuri.
Anaruhusiwa mlezi wa mtoto wa kiume ambaye hawezi kupiga mawe mwenyewe ampigie mawe Jamarat Al-Aqaba na Jamarat zilizobakia kwa niaba yake baada ya kujipigia mawe mwenyewe. Na vile vile, kwa msichana mdogo ambaye hawezi kujipigia mawe kwenye Jamaraat, mlezi wake anaweza kumrushia mawe hayo; kwa mujibu wa Hadithi ya Jabiri, Mwenyezi Mungu amwiye radhi, kwamba alisema: "Tulihiji pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na tulikuwa pamoja na wanawake na watoto. Kwa hivyo tukafanya talbiya kwa niaba ya watoto hao, na pia kuwatupia vijiwe kwenye Jamaraat." ([115]) Imepokelewa na bin Majah. [89] Kaipokea At-Tirmidhiy kwa nambari 927.
Na anaruhusiwa mtu asiyeweza kurusha vijiwe kwenye Jamaraat kwa sababu ya maradhi, uzee, au ujauzito kumteua mtu wa kumrushia vijiwe hivyo; kulingana na maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi mcheni Mwenyezi Mungu kadiri muwezavyo." ([116]) [At-Taghabun: 16] Na watu hawa hawawezi kusongamana pamoja na watu katika Jamaraat, na muda wa kurusha vijiwe unaweza pita na wala haikufaradhishwa kulifidia hilo kwa niaba yao, kwa hivyo wakaruhisiwa kumteua mtu kinyume na zisizokuwa hii miongoni mwa ibada nyinginezo za Hija. Hizo hujaji hairuhusiwi kumteua mtu wa kumfanyia mambo ya Hija, hata kama ni Hija ya hiari. Kwa sababu anayeingia katika Ihraam kwa ajili ya Hija au Umra - hata ikiwa ni kwa hiari - ni wajibu juu yake kuikamilisha. Kulingana na maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na timizeni Hija na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu." ([117]) [Al-Baqara: 196] Wakati wa tawaf na sa’ayi hauwezi kuisha, tofauti na wakati wa kupiga vijiwe kwenye Jamaraat.
Ama kusimama Arafa na kulala Muzdalifa na Mina, hakuna shaka kuwa muda wa hayo hautapita, lakini inawezekana kwa mtu asiye na uwezo kufanya hivyo katika sehemu hizi, hata kwa shida, tofauti na kurusha kwake vijiwe moja kwa moja na kwa sababu kurusha vijiwe ni jambo ambalo mtu anaweza kufanyiwa kama ilivyosimuliwa kutoka kwa waliotangulia wema kuhusiana na mtu mwenye udhuru, tofauti na ibada nyinginezo.
Ibada ni kama zilivyowekwa, na hakuna mtu yeyote anayeweza kuanzisha ibada yoyote isipokuwa kwa ushahidi. Mtu anayemfanyia mwingine matendo ya Hija au Umra anaruhusiwa kujirushia vijiwe mwenyewe, kisha amrushie yule ambaye anamuwakilisha anaporusha kijiwe kwenye Jamaraat tatu zote huku amesimama mahali pamoja, na si lazima kwake kujirushia vijiwe kwenye Jamaraat zote tatu kisha anarudi ndiyo aanze kumrushia yule anayemuwakilisha. Hili ni kulingana na kauli iliyo sahihi zaidi kati ya kauli mbili za wanazuoni. Kwa sababu hakuna ushahidi wowote unaolazimu hilo, na kwa sababu ya ugumu na uzito ulio katika hilo. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika Dini." ([118]) [Al-Hajj: 78]. Na amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: "Fanyeni wepesi na wala msifanye ugumu." ([119]) Na kwa sababu hilo halikusimuliwa kutoka kwa Maswahaba wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, waliporusha vijiwe kwa niaba ya watoto wao na wale wasiokuwa na uwezo miongoni mwao, na lau wangefanya hivyo, basi yangetufikia. Kwa sababu ni katika mambo ambayo watu wana hima kubwa ya kuyasimulia. Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi. [90] Imepokelewa na Bukhari kutoka katika Hadithi ya Anas, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 69.
Mlango:
Kuhusu wajibu wa kuchinja kwa yule aliyefanya Tamattu’ na anayefanya Qiran.
Iwapo hujaji anafanya Hija ya tamattu’ au qiran – na si miongoni mwa wale wanaoishi katika Msikiti Mtakatifu - basi atalazimika kuchinja kondoo, au subui (moja ya saba) ya ngamia, au subui ya ng’ombe. Hilo ni lazima liwe kutoka katika mali halali na mapato mazuri; kwa sababu Mwenyezi Mungu ni mzuri na hukubali isipokuwa yaliyo mazuri.
Muislamu anatakiwa ajiepushe na kuwaomba watu zawadi au kitu chochote kile, wawe ni wafalme au wengineo, ikiwa Mwenyezi Mungu alimpa wepesi katika mali yake wa kupata kitu anachoweza kupata mnyama wa dhabihu kwa ajili yake mwenyewe na kimtosheleze kuomba vile vilivyo mikononi mwa watu. Kwa sababu ya yale yaliyokuja katika hadithi nyingi kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake katika kukashifu kuombaomba watu na kukosoa hilo, na kuwasifu wale wanaoachana nalo.
Iwapo mwenye kufanya tamattu' na mwenye kufanya Qiraan hawezi kutoa mnyama wa dhabihu, ni lazima afunge siku tatu wakati wa Hija na saba atakaporudi kwa familia yake. Na ana hiari ya kufunga siku tatu hizo; akitaka, anazifunga kabla ya Siku ya kuchinja (siku ya Idi). Na akitaka, anazifunga katika zile siku tatu za Tashriiq. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra kisha ndio akahiji, basi achinje mnyama aliye mwepesi kumpata. Na asiyepata, afunge siku tatu katika Hija na siku saba mtakaporudi; hizi ni kumi kamili. Hayo ni kwa ajili ya yule ambaye watu wake hawako karibu na Msikiti Mtakatifu." ([120]) [Al-Baqara: 196] Mpaka mwisho wa Aya.
Na katika Sahihi Bukhari, kutoka kwa Aisha na bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, walisema: "Katika siku za Tashriiq (kubanika nyama), hakuruhusiwa yeyote kufunga saumu isipokuwa kwa wale ambao hawakupata mnyama wa dhabihu."([121]) Hadithi hii iko katika hukumu ya hadithi inayofika kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na ni bora kufunga siku tatu hizo kabla ya siku ya Arafa, ili siku ya Arafa afungue saumu; kwa sababu Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisimama siku ya Arafa bila kufunga, na akakataza kufunga siku ya Arafa mtu anapokuwa Arafa, na kwa sababu kutofunga siku hii kunamfanya kuwa na nguvu ya kufanya dhikri na kuomba dua. Inaruhusiwa kufunga hizo siku tatu zilizotajwa kwa mfululizo au kwa kutenganisha, na vile vile kufunga zile siku saba si wajibu kwake kuzifululiza, bali inajuzu kuzifunga zote kwa mfululizo na kwa kutenganisha. Kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu hakuweka sharti la kuzifunga kwa mfululizo, wala Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Na ni bora kuchelewesha kufunga hizo siku saba mpaka arejee kwa ahali zake. Kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: "Na siku saba mtakaporudi." ([122]) [Al-Baqara: 196] [91] Kaipokea Bukhari kwa nambari 1998.
Kufunga kwa mtu asiye na uwezo wa kutoa mnyama wa dhabihu ni bora kuliko kuwaomba wafalme na wengine mnyama wa kuchinja kwa ajili yake mwenyewe. Na anayepewa mnyama wa kuchinjwa au kitu kingine bila ya kuomba wala kufanya hima ya kupewa, basi hakuna ubaya kwake, hata akiwa anahiji kwa niaba ya mtu mwingine. Yaani, ikiwa yule ambaye anamuwakilisha hakumpa sharti la kununua mnyama wa dhabihu kutoka katika mali aliyopewa. Ama yale wanayofanya baadhi ya watu kama kuomba serikali au wengine wanyama wa dhabihu kwa majina ya watu wanaowataja ilhali ni waongo, bila shaka hilo ni haramu. Kwa sababu ni kula mali kwa njia ya uongo. Mwenyezi Mungu atulinde sisi na Waislamu kutokana na hilo.
Mlango:
Kuhusu ulazima wa mahujaji na wengineo kuamrisha mema
Moja ya faradhi kubwa kwa mahujaji na wengineo ni kuamrisha mema na kukataza maovu, na kusimamisha swala tano za kila siku kwa jamaa, kama alivyoamrisha Mwenyezi Mungu hayo katika Kitabu chake, na kwa ulimi wa Mtume wake, Mwenyezi Mungu amfikishie rehema na amani.
Ama yale wanayoyafanya watu wengi miongoni mwa wakazi wa Makka na kwingineko, kama vile kuswalia majumbani na kutoenda misikitini, hilo ni makosa na kinyume na sheria, hivyo ni lazima yakatazwe, na kuwaamrisha watu kudumisha swala misikitini. Kwa sababu imethibiti kwamba yeye, rehema na amani ziwe juu yake, alimwambia bin Ummi Maktum, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alipomuomba idhini ya kuswalia nyumbani kwake, kwa sababu alikuwa kipofu na nyumba yake ilikuwa mbali na msikiti: “Je, unasikia wito wa swala?" Akasema: 'Ndiyo.' Akasema: "Basi itikia." ([123]) Na katika riwaya nyingine: “Siwezi kukupatia ruhusa." ([124]) Na amesema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Hakika nimeazimia sana kuamrisha swala, kisha ikimiwe, kisha nimuamuru mwanaume awaongoze watu, kisha niondoke niende kwa wanaume ambao hawahudhurii kwenye swala, niwachomee majumbani mwao." ([125]) Na katika Sunan bin Majah na wengineo kwa mlolongo mzuri wa wasimulizi kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Yeyote atakayesikia wito wa swala na asifike, basi hana swala isipokuwa kwa udhuru." ([126]) Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa bin Masudi, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisema: “Atakayefurahishwa kwamba akutane na Mwenyezi Mungu kesho akiwa Muislamu, basi na adumishe kuziswalia swala hizo pale zinapoitiwa. Kwani Mwenyezi Mungu amemuwekea Mtume wenu nyendo za uongofu, nazo hakika ni katika nyendo za uongofu. Na lau mtaswalia majumbani mwenu , kama anavyoswali huyu aliyesalia nyuma nyumbani kwake, basi mtakuwa mmeacha nyendo za Mtume wenu. Na lau mtaacha nyendo za Mtume wenu, basi mtapotea. Na hakuna mwanamume anayejisafisha kwa uzuri kisha akaenda kwenye msikiti miongoni mwa misikiti hii isipokuwa Mwenyezi Mungu humuandikia kwa hilo jambo jema kwa kila hatua anayoipiga. Na Mwenyezi Mungu anamnyanyua daraja kwa hilo na atamuondoshea kitendo kiovu kwa hilo. Na tulijiona hakuna aliyekuwa akisalia nyuma yake isipokuwa mnafiki anayejulikana kwa unafiki wake. Na mtu angeletwa huku ameshikiliwa baina ya watu wawili mpaka asimamishwe kwenye safu.” ([127]). (92) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2420, na Muslim kwa nambari 651. [93] Imepokelewa na Muslim kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 653. [94] Ameipokea Abuu Daud kutoka kwa Abdullah bin Umm Maktum, nambari 552. (95) Kaipokea Muslim kwa nambari 654. [96] Ameipokea Abuu Daud kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili kwa nambari 551.
Inawalazimu mahujaji na wengine kujiepusha makatazo ya Mwenyezi Mungu Mtukufu na wawe waangalifu kutoyafanya, kama vile uzinzi, kulawiti, wizi, kula riba, kula mali ya yatima, kulaghai katika miamala, hiyana katika amana, kunywa vileo, kuvuta sigara, kuburuta nguo chini, kiburi, husuda, kujionyesha, kusengenya, kufitini, kuwakejeli Waislamu, na kutumia vyombo vya pumbao; kama vile kinanda na mazumari na vinginevyo, kusikiliza nyimbo na ala za muziki kama redio na vinginevyo, kucheza kete, chesi, - ambayo ni kucheza kamari - na kupiga picha za viumbe hai kama vile wanadamu na vinginevyo; na kuridhika na hayo, kwani yote hayo ni miongoni mwa maovu ambayo Mwenyezi Mungu ameyaharamisha kwa waja wake katika kila wakati na mahali. Kwa hivyo, mahujaji na wakazi wa Nyumba Takatifu ya Mwenyezi Mungu ni lazima wajihadhari nayo zaidi kuliko wengine. Kwa sababu madhambi katika Ardhi hii ni makubwa zaidi na adhabu yake ni kubwa zaidi.
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na anayekusudia kufanya upotofu humo kwa kudhulumu, tutamuonjesha adhabu iumizayo." ([128]) [Al-Hajj: 25], Ikiwa Mwenyezi Mungu aliwaahidi adhabu wale wanaotaka kufanya upotofu katika eneo takatifu kwa dhuluma, basi itakuwaje adhabu ya mwenye kuufanya hasa? Hapana shaka kuwa ni kubwa zaidi na kali zaidi. Kwa hivyo ni lazima mtu ajihadhari na hayo na madhambi mengine yote.
Mahujaji hawawezi kupata wema wa Hija na msamaha wa madhambi isipokuwa kwa kutahadhari na maasi hayo na mengineyo ambayo Mwenyezi Mungu amewaharamishia, kama ilivyo katika Hadithi kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Mwenye kuhiji kisha hakusema maneno machafu wala kufanya uovu, atarejea (akiwa msafi) kama siku aliyozaliwa na mama yake." ([129]) [97] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 1521, na Muslim, nambari 1350.
Na yaliyo mabaya zaidi na makubwa kuliko haya ni: kuwaomba wafu, kuwataka msaada, kuwawekea nadhiri, na kuchinja kwa ajili yao; kwa matumaini ya kwamba watafanya uombezi kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya wale wanaowaomba, au kuwaponya wagonjwa wao, au kumrudisha asiyekuwapo, na mfano wa hayo.
Hili ni katika ushirikina mkubwa aliouharamisha Mwenyezi Mungu, na ndio dini ya washirikina wa zama za kabla ya Uislamu. Na Mwenyezi Mungu alituma Mitume na akateremsha vitabu ili kuupinga na kuukataza.
Kwa hivyo ni wajibu kwa kila mmoja miongoni mwa mahujaji na wengineo kujihadhari nayo, na atubu kwa Mwenyezi Mungu kwa yale aliyoyafanya huko nyuma katika hilo ikiwa amefanya chochote huko nyuma, na arudie Hija mpya baada ya kutubia. Kwa sababu ushirikina mkubwa unabatilisha matendo yote, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na lau wangelimshirikisha, yangeliwaharibikia yale waliyokuwa wakiyatenda." [130] [Al-An'am: 88].
Na miongoni mwa aina za ushirikina mdogo ni kuapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu; kama vile kuapa kwa Mtume, na Al-Kaaba, na amana na mengineyo.
Na miongoni mwake ni kujionyesha na kutaka kusifiwa, na kusema: Mwenyezi Mungu akitaka na wewe ukitaka, na lau si Mwenyezi Mungu na wewe, na haya yanatoka kwa Mwenyezi Mungu na kutoka kwako, na mfano wa hayo.
Basi ni lazima tujihadhari na maovu haya ya kishirikina, na kuusiana kuyaacha; kwa sababu ya yale yaliyothibiti kuwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Atakayeapa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, basi hakika amekufuru au ameshirikisha.' [131] Imepokelewa na Ahmad, Abuu Daud na At-Tirmidhi kwa mlolongo sahihi wa wasimulizi. [98] Ameipokea Abuu Daud kwa nambari 3251.
Na katika Sahihi kutoka kwa Omari, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: “Mwenye kuapa, basi na aape kwa Mwenyezi Mungu au anyamaze.” ([132]) Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, pia alisema: "Atakayeapa kwa amana, basi huyo si miongoni mwetu." ([133]) Imepokelewa na Abuu Daud. [99] Ameipokea Abuu Daud kwa nambari 3253. [100] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abdullah, nambari 2679, na Muslim, nambari 1646.
Na pia amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Kitu ninachowahofia zaidi ni ushirikina mdogo." Akaulizwa kuhusu ushirikina mdogo, akasema: "Ni kujionyesha." ([134]) Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Msiseme: Mwenyezi Mungu akipenda, na fulani akipenda.' Lakini semeni: Mwenyezi Mungu akipenda, kisha fulani." [135] Imepokelewa na An-Nasaai kutoka kwa Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awawiye radhi wote wawili, kwamba mwanamume mmoja alisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, apendacho Mwenyezi Mungu na upendacho. Akasema: "Umenifanya kuwa sawa na Mwenyezi Mungu. Bali apendacho Mwenyezi Mungu peke yake."([136]) [101] Ameipokea Ahmad kwa namba 5/428. (102) Ameipokea Abuu Daud kwa namba 4980. [103] Ameipokea Ibn Majah kwa nambari 2117.
Hadithi hizi zinaashiria ulinzi wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, juu ya tauhidi, maonyo yake kwa Umma wake dhidi ya shirki kubwa na ndogo, na pupa yake kubwa juu ya usalama wa imani yao na kuokoka kwao kutokana na adhabu ya Mwenyezi Mungu, na sababu za ghadhabu yake. Basi Mwenyezi Mungu amlipe malipo bora kwa hilo, kwani alifikisha ujumbe na akaonya, na akanasihi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na waja wake, rehema na amani ziwe juu yake, rehema na amani za daima hadi Siku ya Kiyama.
Na la wajibu kwa watu wenye elimu, wakiwemo mahujaji na wakazi wa mji wa Mwenyezi Mungu wenye amani, na mji wa Mtume wake Mtukufu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ni kuwafundisha watu yale aliyowawekea Mwenyezi Mungu katika dini, na kuwahadharisha yale aliyowaharamishia miongoni mwa aina za ushirikina na maasi, na kuyaeleza hayo kwa ushahidi wake, na kuyafafanua kwa ufafanuzi wa kina. Ili kuwatoa watu kwa hayo katika kiza na kuwapeleka kwenye nuru, na ili kutimiza yale ambayo Mwenyezi Mungu aliwaamrisha ya kufikisha na kubainisha. Mwenyezi Mungu aliyetakasika alisema: "Na pale Mwenyezi Mungu alipochukua ahadi na wale waliopewa Kitabu kuwa: 'Lazima mtawabainishia watu, wala hamtokificha." ([137]) [Al Imran: 187].
Na makusudio ya hilo ni wanazuoni wa umma huu kuonya dhidi ya kushika njia ya watu madhalimu miongoni mwa watu wa Kitabu katika kuficha haki; kwa kuwa na tamaa ya maisha ya sasa kuliko yajayo, kama Mwenyezi Mungu alivyosema: "Hakika, wale wanaoficha tuliyoyateremsha, nazo ni hoja zilizo wazi na uongofu baada ya Sisi kuzibainisha kwa watu Kitabuni. Hao anawalaani Mwenyezi Mungu, na wanawalaani kila wenye kulaani." ([159]) "Isipokuwa wale waliotubu, wakatengeneza na wakabainisha. Basi hao nitapokea toba yao, na Mimi ni Mwenye kupokea toba na Mwenye kurehemu." ([138]) [Al-Baqara: 159-160]. Aya za Qur'ani Tukufu na Hadithi za Mtume ziliashiria kuwa kulingania kwa Mwenyezi Mungu na kuwaongoza waja wake kwenye yale waliyoumbiwa ni miongoni mwa mambo bora zaidi ya kujiweka kwayo karibu na Mwenyezi Mungu na wajibu muhimu zaidi, na kwamba ndiyo njia ya Mitume na wafuasi wao mpaka Siku ya Kiyama, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na ni nani mbora zaidi wa kusema kuliko aitaye kwa Mwenyezi Mungu na akatenda mema, na akasema: Hakika mimi ni katika Waislamu?" ([139]) [Fussilat: 33], Na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Hii ndiyo Njia yangu - ninalingania kwa Mwenyezi Mungu kwa ufahamu mzuri - mimi na wale wanaonifuata. Na ametakasika Mwenyezi Mungu! Wala mimi si katika washirikina." ([140]) [Yusuf: 108].
Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Mwenye kujulisha katika heri yoyote, basi atapata ujira sawa na mtendaji wake.” ([141]) “Hakika Mwenyezi Mungu kumuongoa mtu mmoja kupitia kwako ni bora kwako kuliko ngamia wekundu." ([142]) Na kuna aya na hadithi nyingi zenye maana hii. [104] Kaipokea Muslim kwa nambari 1893. (105) Kaipokea Bukhari kwa nambari 3009, na Muslim kwa nambari 2406.
Inafaa zaidi kwa watu wenye elimu na imani kuzidisha juhudi zao katika kulingania kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, kuwaongoza waja wake kwenye sababu za uokovu, na kuwaonya juu ya sababu za maangamizi, hasa katika zama hizi ambazo matamanio yamekuwa mengi, na zikaenea ndani yake kanuni na kauli mbiu za kupotosha, na wakapunguka ndani yake wanaolingania kwenye uongofu, na wakazidi ndani yake wanaolingania kwenye kumkana Mwenyezi Mungu na maadili machafu. Basi Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kuombwa msaada, na hakuna uwezo wala nguvu isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu aliye Mkuu.
Mlango:
Kuhusu kupendekezwa kuzidisha matendo ya utiifu
Inapendekezwa kwa mahujaji kumkumbuka Mwenyezi Mungu daima, kumtii, na kufanya matendo mema wakati wa kukaa kwao Makka, na kuswali kwa wingi na kuizunguka Al-Kaaba. Kwa sababu matendo mema ndani ya eneo takatifu yanazidishwa, na maovu ndani yake ni makubwa na makali. Pia inapendekezwa kwao kumuombea amani na rehema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake.
Na hujaji anapotaka kuondoka Makka, ni lazima aizunguke Al-Ka'aba kuzunguka kwa kuaga; ili hilo liwe ndilo jambo la mwisho hapo kwenye Nyumba, isipokuwa kwa wanawake wenye hedhi na wale walio katika nifasi, hao hawalazimiki kuzunguka mzunguko wa kuaga; kwa mujibu wa hadithi ya bin Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kwamba alisema: “Aliwaamrisha watu kwamba kuizunguka Nyumba kuwe ndiko jambo lao la mwisho hapo kwenye Nyumba, isipokuwa akamrahisishia mwanamke mwenye hedhi." ([143]) (106) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1755, na Muslim kwa nambari 1328.
Akimaliza kuiaga Nyumba na akataka kutoka msikitini, atatembea huku ameelekea nje mpaka atoke, na asitembee kinyumenyume; kwa sababu hilo halikupokewa kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake wala kutoka kwa Maswahaba wake. Bali ni miongoni mwa mambo mapya yaliyozushwa, na alisema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Yeyote atakayefanya jambo ambalo hatukuliamrisha, basi hilo litakataliwa." ([144]) Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Jihadharini na mambo mapya yaliyozushwa (katika dini), kwa kuwa kila jambo lililozuliwa ni uzushi, na kila uzushi ni upotofu." ([145]) [107] Imeshatangulia kuelezwa aliyeipokea. [108] Imepokelewa na Muslim kutoka kwa Jabir, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 867.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu tuendelee kuwa imara katika dini yake na kuwa salama kutokana na jambo lolote linalopingana nayo. Hakika Yeye ndiye Mpaji, Mtukufu, Mkarimu.
Mlango:
Kuhusu hukumu za kutembelea msikiti wa Madina na adabu zake
Ni Sunna kuzuru Msikiti wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake kabla au baada ya Hija; kwa sababu ya yale yaliyothibiti katika Sahihi Mbili kutoka kwa Abuu Huraira radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Alisema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Kusali ndani ya Msikiti wangu huu ni bora kuliko sala elfu moja zinazoswaliwa nje ya Msikiti huu isipokuwa Msikiti wa Makka." ([146]) Na imesimuliwa kutoka kwa bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: “Swala moja katika msikiti wangu huu ni bora kuliko Swala elfu moja katika misikiti mingineyo isipokuwa Msikiti Mtukufu." ([147]) Imepokelewa na Imamu Muslim. Na imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Al-Zubairi Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Swala moja katika msikiti wangu huu ni bora kuliko swala elfu moja katika misikiti mingineyo isipokuwa Msikiti Mtakatifu. Na swala katika Msikiti Mtakatifu ni bora kuliko swala mia moja katika msikiti wangu huu." ([148]) Imepokelewa na Ahmad, bin Khuzaima, na Ibn Hibban. (109) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1190, na Muslim kwa nambari 1394. [110] Kaipokea Muslim kwa nambari 1395. (111) Ameipokea Ahmad kwa namba 4/5.
Na imesimuliwa kutoka kwa Jabiri, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake alisema: "Swala moja katika msikiti wangu huu ni bora kuliko swala elfu moja katika msikiti mwingine wowote, isipokuwa Msikiti Mtukufu. Na swala moja katika Msikiti Mtakatifu ni bora kuliko swala laki moja katika msikiti wowote." ([149]) Imepokelewa na Ahmad na Ibn Majah, na kuna Hadithi nyingi katika maana hii. [112] Amepokea Ibn Majah, nambari 1406.
Basi mwenye kuzuru anapoufikia Msikiti Mtakatifu, inapendekezwa kwamba autangulize mguu wake wa kulia wakati wa kuingia na aseme: "Kwa jina la Mwenyezi Mungu, na rehema na amani ziwe juu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu. Najilinda kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kwa uso wake mtukufu, na kwa utawala wake wa kale, kutokana na Shetani aliyelaaniwa. Ewe Mwenyezi Mungu, nifungulie milango ya rehema zako."
Vile vile atasema hayo wakati wa kuingia katika misikiti mingineyo, na hakuna dhikri maalumu ya kuingia msikitini kwake, rehema na amani ziwe juu yake. Kisha ataswali rakaa mbili na kumuomba Mwenyezi Mungu ndani yake kwa chochote atakacho katika mambo mema ya dunia na akhera. Na akiziswalia katika Raudhwa tukufu, basi hilo ndilo bora zaidi; kwa sababu ya kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Nafasi iliyoko baina ya nyumba yangu na mimbari yangu (Raudhwa) ni bustani miongoni mwa bustani za Peponi." ([150]) Kisha, baada ya swala, atazuru kaburi la Mtume rehema na amani ziwe juu yake na makaburi ya Maswahaba wake wawili: Abubakari na Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao. Atasimama mbele ya kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake kwa adabu nzuri kwa sauti ya chini, kisha amsalimie Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akisema: “Amani iwe juu yako ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, na rehema za Mwenyezi Mungu na baraka zake.” Kwa sababu ya yale yaliyokuja katika Sunan Abu Daud kwa mlolongo mzuri wa wasimulizi, kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwamba alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: "Hakuna yeyote atakayenisalimia isipokuwa Mwenyezi Mungu hunirudishia roho yangu ili nimjibu salamu." Na ikiwa mwenye kuzuru atasema katika salamu yake: “Amani iwe juu yako, ewe Nabii wa Mwenyezi Mungu. Amani iwe juu yako, ewe kiumbe bora zaidi wa Mwenyezi Mungu. Amani iwe juu yako, ewe bwana wa Mitume na imamu wa wacha Mungu. Ninashuhudia kwamba hakika ulifikisha ujumbe, ukatimiza amana, ukanasihi umma na ukapambana kwa ajili ya Mwenyezi Mungu ukweli wa kupambana," basi hakuna ubaya wowote katika hilo. Kwa sababu haya yote ni katika sifa zake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake. Na atamswalia - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - na kumuombea dua; kwa sababu imethibiti katika sheria kwamba inaruhusiwa kuunganisha kati ya kumswalia na kumuombea amani; kwa mujibu wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Mwenyezi Mungu na Malaika wake wanamsalia Nabii. Enyi mlioamini! Msalieni na mumsalimu kwa salamu." ([152]) [Ahzaab: 56]. Kisha atawasalimia Abubakari na Omari, Mwenyezi Mungu awawie radhi, na atawaombea dua na kuwatakia radhi za Mwenyezi Mungu. [113] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abdullah bin Zaid Al-Mazini kwa nambari 1195, na Muslim kwa nambari 1390. [114] Ameipokea Abuu Daud kwa namba 2041.
Na bin Omari, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, alikuwa anapomsalimia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, pamoja na hao Maswahaba wake wawili, hazidishi juu ya kauli yake: “Amani iwe juu yako, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Amani iwe juu yako, ewe Abubakari. Amani iwe juu yako, ewe baba yangu." Kisha anaondoka.
Kuzuru huku kumewekewa wanaume tu. Ama wanawake, wao hawaruhusiwi kuzuru makaburi yoyote, kama ilivyothibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba alisema: "Wamelaaniwa wanawake wanaozuru makaburi na wanaojenga misikiti juu yake na wanaoweka taa juu yake." ([153]) (115) Ameipokea Abuu Daud kwa nambari 3236.
Ama kwenda Madina kwa ajili ya kuswalia katika Msikiti wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake na kuombea dua humo na mfano wa hayo katika yale yanayoruhusiwa katika misikiti yote, basi hilo limewekewa wote katika sheria; kwa sababu ya Hadithi zilizotangulia kuhusu hilo.
Ni Sunna kwa mwenye kuzuru kuswalia Swala tano za kila siku katika Msikiti wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake na kufanyia humo dhikri na dua kwa wingi na swala za hiari; ili kutumia fursa hii kupata malipo makubwa yaliyo katika hayo.
Na inapendekezwa kuswali swala nyingi za kujitolea katika Raudhwa tukufu. Kutokana na Hadithi sahihi iliyotajwa hapo juu kuhusu fadhila yake, nayo ni kauli ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Nafasi iliyoko baina ya nyumba yangu na mimbari yangu ni bustani miongoni mwa bustani za Peponi." ([154]) [116] Imeshatagulia kuelezwa aliyeipokea.
Ama swala ya faradhi, hiyo inampasa mwenye kuzuru na wengineo kuiendea na kudumisha kuiswalia katika safu ya kwanza kadiri awezavyo, hata ikiwa ni katika ziada ya swala ya Qabliya (sunna inayoswaliwa kabla ya swala ya faradhi); kwa sababu ya yale yaliyotajwa katika Hadithi sahihi kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, ya kuhimiza juu ya safu ya kwanza, kama vile kauli yake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kama watu wangejua kilicho katika Adhana na safu ya kwanza, kisha wakawa hawana budi ila kupiga kura juu yake, basi wangepiga kura." ([155]) Hadithi hii wamekubaliana juu yake Bukhari na Muslim. Na kama Mtume rehema na amani ziwe juu yake, alivyowaambia Maswahaba wake: “Songeni mbele na mnifuate, na wakufuateni nyinyi wale walio baada yenu. Na mtu ataendelea kuchelewesha swala mpaka Mwenyezi Mungu amcheleweshe." ([156]) Imepokelewa na Muslim. [117] Kaipokea Muslim kutoka kwa Abu Said Al-Khudri, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwa nambari 438. (118)Kaipokea Bukhari kwa nambari 615, na Muslim kwa nambari 437.
Na imepokelewa na Abu Daud kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kwa mlolongo mzuri wa wasimulizi, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mtu ataendelea kuchelewa kuwa katika safu ya mbele hadi Mwenyezi Mungu atamuweka nyuma katika Moto." ([157]) Na imethibiti kutoka kwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kwamba aliwaambia Maswahaba wake: “Je, hampangi safu kama Malaika wanavyojipanga safu mbele ya Mola wao Mlezi?" Wakasema: 'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Malaika wanajipangaje safu mbele ya Mola wao Mlezi?' Akasema: Wanakamilisha safu za kwanza, na wanasimama pamoja sawasawa katika safu." ([158]) Imepokelewa na Imamu Muslim. [119] Kaipokea Muslim kutoka kwa Jabir bin Samura kwa nambari 430. [120] Ameipokea Abu Daud, nambari 679 kwa matamshi haya: "Watu hawataacha kuchelewa kuifikia safu ya kwanza (ya swala) mpaka Mwenyezi Mungu atakapowachelewesha Motoni."
Na zipo Hadithi nyingi zenye maana hii, nazo zinauenea msikiti wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na misikiti mingineyo kabla na baada ya kuongezwa. Na imepokelewa kwa njia sahihi kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwamba alikuwa akiwahimiza Maswahaba wake kuwa upande wa kulia wa safu, na inajulikana kuwa upande wa kulia wa safu uko katika msikiti wake wa kwanza na nje ya Raudhwa, kwa hiyo ikajulikana kutokana na hili kwamba kuchunga safu za mwanzo na pande za kulia za safu kumepewa kipaumbele juu ya kufanya hima ya kuswalia katika Raudhwa, na hili liko wazi kwa yeyote anayezizingatia hadithi zilizokuja kuhusiana na mlango huu. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwezeshaji.
Na hairuhusiwi kwa mtu yeyote kujipangusa kwenye chumba cha Mtume rehema na amani ziwe juu yake, kukibusu au kukizunguka. Kwa sababu haya hayakusimuliwa kutoka kwa watangulizi wema. Bali ni uzushi mbaya.
Na hairuhusiwi kwa mtu yeyote kumuomba Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, atimize haja zake, aondoe dhiki zake, au amponye mgonjwa wake au mfano wa hayo. Kwa sababu haya yote haombwi isipokuwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika, na kuyaomba kutoka kwa wafu ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kumuabudu asiyekuwa Yeye, ilhali dini ya Kiislamu imejengwa juu ya misingi miwili:
Ya kwanza: Asiabudiwe isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake.
Ya pili: Asiabudiwe isipokuwa kwa yale ambayo Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, aliyaweka katika sheria.
Hii ndiyo maana ya kushuhudia kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu.
Vile vile, hairuhusiwi kwa yeyote kumuomba Mtume rehema na amani ziwe juu yake, uombezi; kwa sababu hilo ni miliki ya Mwenyezi Mungu, na hauombwi ila kutoka kwake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: Uombezi wote uko kwa Mwenyezi Mungu." ([159]) [Az-Zumar: 44], Kwa hiyo unafaa kusema: “Ewe Mwenyezi Mungu, mruhusu Mtume wako kunifanyia uombezi. Ewe Mwenyezi Mungu, waruhusu Malaika wako na waja wako waumini kunifanyia uombezi. Ewe Mwenyezi Mungu, waruhusu watoto wangu waliokufa utotoni kunifanyia uombezi;" na mfano wa hayo. Ama wafu, hao hawaombwi chochote, si uombezi wala kitu kingine chochote, sawa wawe ni Manabii au wasiokuwa Manabii. Kwa sababu hilo sio katika sheria, na kwa sababu maiti alishakatikiwa matendo isipokuwa yale ambayo sheria iliyatenga.
Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alisema kwamba: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake: “Mwanadamu anapokufa, yanakatika matendo yake isipokuwa matatu: Sadaka inayoendelea, elimu yenye manufaa au mtoto mwema atakayemuombea.” ([160]) [121] Imepokelewa na Muslim kutoka kwa Abuu Huraira, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, nambari 1631.
Iliruhusiwa kuomba uombezi kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake katika zama za uhai wake na Siku ya Kiyama peke yake; kwa sababu ya uwezo wake wa kufanya hivyo. Kwani anaweza kwenda na kumuomba Mola wake Mlezi kwa ajili ya yule aliyemuomba kufanya hivyo. Ama katika dunia, hili linajulikana, na hilo si mahususi kwake tu, bali ni jumla kwake na kwa wengineo. Kwa maana inaruhusiwa kwa Muislamu kumwambia ndugu yake: Nifanyie uombezi kwa Mola wangu Mlezi katika hiki na kile, akimaanisha: Niombee kwa Mwenyezi Mungu. Na inaruhusiwa kwa aliyeombwa kufanya hivyo kumuomba Mwenyezi Mungu na kumfanyia ndugu yake uombezi ikiwa ni katika mambo ambayo Mwenyezi Mungu ameruhusu kuomba.
Ama Siku ya Kiyama, hakuna atakayeweza kufanya uombezi isipokuwa baada ya idhini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ni nani huyo awezaye kuombea mbele yake isipokuwa kwa idhini yake?" ([161]) [Al-Baqara: 255].
Ama hali ya kifo, hiyo ni hali maalumu na hairuhusiwi kuambatanisha na hali ya mtu kabla ya kufa kwake au hali yake baada ya kufufuliwa, kwa sababu matendo ya maiti huwa yameshakatika naye huwa rehani kwa yale aliyotenda isipokuwa yale ambayo Mtungaji sheria aliyatoa katika hukumu hiyo, kwa hivyo hairuhusiwi kuyaambatanisha na hayo. Hapana shaka kuwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, baada ya kufa kwake, anaishi maisha ya Barazahi (Akhera) yaliyokamilika zaidi kuliko maisha ya wale waliouawa kwa ajili ya dini, lakini si ya aina sawa na maisha yake kabla ya kufa, wala ya aina sawa na maisha yake ya Siku ya Kiyama, bali ni maisha ambayo hajui uhakika wake na namna yake isipokuwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika peke yake. Na ndiyo maana ilishatangulia katika Hadithi tukufu kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakuna yeyote atakayenisalimia isipokuwa Mwenyezi Mungu hunirudishia roho yangu ili nimjibu salamu." ([162])
Hili likaashiria kuwa alikufa, na kwamba roho yake iliuacha mwili wake, lakini inarudishwa kwake anaposalimiwa. Na maandiko yanayoashiria kifo chake, rehema na amani ziwe juu yake, katika Qur'ani na Sunna yanajulikana, na ni jambo lililokubaliwa kati ya wanazuoni, lakini hilo halizuii maisha yake katika Barazahi (Akhera), kama vile kifo cha wale waliouawa kwa ajili ya dini hakikuzuia kuishi maisha ya Barazahi yaliyotajwa katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala kabisa usiwadhanie wale waliouliwa katika Njia ya Mwenyezi Mungu kuwa ni wafu. Bali hao wako hai kwa Mola wao Mlezi wanaruzukiwa." ([163]) [Al Imran: 169] [122] Ameipokea Abuu Daud kwa nambari 2041.
Tumepanua mazungumzo katika suala hili, kwa sababu ya haja kubwa ya kufanya hivyo kwa kuwa kuna idadi kubwa ya wanaochanganyikiwa katika suala hili, na wanalingania katika ushirikina na kuabudu wafu badala ya Mwenyezi Mungu. Basi tunamuomba Mwenyezi Mungu atulinde sisi na Waislamu wote kutokana na kila jambo linalopingana na sheria yake, na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.
Ama yale wanayofanya baadhi ya wenye kuzuru msikiti wa Mtume ya kuinua sauti zao kwenye kaburi lake, rehema na amani ziwe juu yake, na kusimama hapo kwa muda mrefu, hili ni kinyume na ilivyoamrishwa. Kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu amekataza umma huu kuinua sauti zao juu ya sauti ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake, na kusema naye kwa kelele kama wanavyosemezana wao kwa wao, na akawahimiza washushe sauti zao chini mbele yake katika kauli yake Mtukufu: "Enyi mlioamini! Msinyanyue sauti zenu kuliko sauti ya Nabii, wala msiseme naye kwa kelele kama mnavyosemezana nyinyi kwa nyinyi, visije vitendo vyenu vikaharibika, na hali hamtambui. (2) "Hakika wale wanaoziteremsha sauti zao chini mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, hao ni wale ambao Mwenyezi Mungu Amewatahini nyoyo zao na Akazitakasa kwa ucha Mungu wake, watapata msamaha wa dhambi zao kutoka kwa Mola wao na malipo mema mengi, nayo ni Pepo." ([164]) [Al Hujraat: 2-3].
Na kwa sababu ya kusimama kwa muda mrefu kaburini kwake, rehema na amani ziwe juu yake na kumtolea salamu kwa wingi kunasababisha msongamano, kelele nyingi, na sauti kubwa kwenye kaburi lake, rehema na amani ziwe juu yake, na hilo linakwenda kinyume na yale ambayo Mwenyezi Mungu amewawekea sheria Waislamu katika Aya hizi zenye maana ya wazi, na Mtume rehema na amani ziwe juu yake anaheshimika akiwa hai na maiti, kwa hivyo Muumini hafai kufanya mambo yanayokwenda kinyume na adabu za Kiislamu kwenye kaburi lake.
Na vile vile wanavyofanya baadhi ya wageni na wengineo, ya kutafuta tu kuombea dua kwenye kaburi lake huku wamelielekea kaburi na kunyanyua mikono yao juu wakiomba dua, haya yote ni kinyume na waliyokuwa wakifanya watangulizi wema, miongoni mwa Maswahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na wale waliowafuata kwa wema. Bali ni miongoni mwa mambo mapya yaliyozushwa, na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Shikamaneni na Sunna zangu na Sunna za mahalifa wanyoofu waongofu baada yangu. Zikamateni na kuzing'ata kwa magego. Na jihadharini na mambo mapya. Kwani kila jambo jipya (katika dini) ni uzushi, na kila uzushi ni upotofu." ([165]) [123] Ameipokea Abu Daud kutoka katika Hadithi ya Al-'Irbadh bin Sariya, nambari 4607.
Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie: "Yeyote atakayezua katika jambo letu hili kitu ambacho hakimo, basi hicho kitakataliwa." ([166]) "Yeyote atakayefanya jambo ambalo hatukuliamrisha, basi hilo litakataliwa." ([167]) [124] Imeshatagulia kuelezwa aliyeipokea. [125] Imeshatagulia kuelezwa aliyeipokea.
Ali bin Al-Hussein Zain Al-Abidin, Mwenyezi Mungu awawie radhi, alimuona mwanamume mmoja akiomba dua kwenye kaburi la Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, basi akamkataza kufanya hivyo na akasema: “Je, nisikuambie Hadithi niliyoisikia kutoka kwa baba yangu kutoka kwa babu yangu kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: “Msilifanye kaburi langu kuwa sikukuu (mahali pa kuja mara kwa mara), wala msizifanye nyumba zenu kuwa makaburi, na niombeeni rehema, kwani salamu zenu zinanifikia popote mlipo." ([168]) [126] Hii ni riwaya ya Zain Al-Abidin ambayo Sheikh aliinasibisha na Al-Hafidh Al-Maqdisi. Na aliipokea hadithi hii bila kisa hiki, na Ahmad pia katika Al-Musnad, nambari 2/367.
Vile vile yale wanayofanya baadhi ya wageni wakati wa kumsalimia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwa kuuweka mkono wake wa kulia juu ya mkono wake wa kushoto, juu au chini ya kifua chake, sawa na muonekano wa mtu anayeswali. Muonekano huu hauruhusiwi wala wakati wa kumsalimu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wala wakati kumsalimu mtu mwingine miongoni mwa wafalme, viongozi na wengineo. Kwa sababu ni aina ya muonekano wa kujidhalilisha, na kunyenyekea na ni ibada inayomfaa Mwenyezi Mungu tu, kama Al-Hafidh bin Hajari, Mwenyezi Mungu amrehemu, alivyopokea hilo katika Al-Fat-h kutoka kwa wanazuoni, na suala hili liko wazi peupe kwa wanaoitafakari hali hii na lengo lao likawa ni kufuata muongozo wa watangulizi wema.
Ama yule aliyetawaliwa na ushabiki wa kipofu, na matamanio, na kuiga kiupofu na kuwa na dhana mbaya juu ya kulingania kwenye uongofu wa watangulizi wema, basi jambo lake liko kwa Mwenyezi Mungu, na tunamuomba Mwenyezi Mungu atuongoze sisi na yeye na atuwezeshe kupendelea Haki kuliko kila kitu. Hakika Yeye aliyetakasika ndiye bora aombwaye.
Vile vile yale wanayofanya baadhi ya watu, kama vile kulielekea Kaburi Tukufu kwa mbali na kutikisa midomo yao kwa salamu au dua, hayo yote ni sawa na yale yaliyotangulia miongoni mwa mambo ya uzushi. Muislamu hatakiwi kuzua katika dini yake yale ambayo Mwenyezi Mungu hakumruhusu, naye kwa matendo haya anakuwa karibu zaidi na usugu kuliko kuwa mwaminifu na safi. Na Imam Malik, Mwenyezi Mungu amrehemu, alikataza kitendo hiki na vinginevyo vinavyofanana nacho na akasema: “Watu wa mwisho wa Umma huu hawatatengemaa isipokuwa kwa yale waliyotengemaa kwayo wa mwanzo wake.” [127] Ighaathatu Allahfaani fii Maswaa-id Ash-Shaitwani, nambari 1/363.
Na inajulikana kuwa kilichowafanya wa mwanzo wa umma huu kutengemaa ni kufuata njia ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na makhalifa wake waongofu, Maswahaba wake walioridhiwa na wale waliowafuata kwa wema. Na kamwe watu wa mwisho wa umma huu hawatatengemaa isipokuwa kwa kushikamana na hayo na kuyafuata.
Mwenyezi Mungu awawezeshe Waislamu kufikia yale yenye uokovu wao, furaha yao na utukufu wao hapa duniani na akhera. Hakika Yeye ndiye Mpaji, Mkarimu mno.
Tahadhari:
Hukumu ya kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake
Kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, si faradhi wala sharti la Hija, kama wanavyofikiri baadhi ya watu wa kawaida na mfano wao. Bali ni jambo linalopendekezwa tu kwa mwenye kuutembelea msikiti wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, au yule ambaye yuko karibu nao.
Ama mtu ambaye yuko mbali na Madina, yeye haruhusiwi kufunga safari kwenda kuzuru kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, lakini anaruhusiwa kufunga safari kwenda kuzuru Msikiti Mtukufu wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake. Anapoufikia, anaweza kulizuru kaburi lake tukufu na makaburi ya wale Maswahaba wake wawili. Kuzuru kwake kaburi la Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na makaburi ya wale Maswahaba wake wawili kuliingia na kufuata kuzuru kwake msikiti wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na hilo ni kwa mujibu wa yale yaliyothibiti katika Vitabu viwili Sahihi, kwamba amesema Mtume, rehema na amani ziwe juu yake: “Hazifungwi safari isipokuwa kwenda kwenye Misikiti mitatu: Msikiti Mtakatifu, Msikiti wangu huu na Msikiti wa Al-Aqsa." ([169]) [128] Kaipokea Bukhari kutoka kwa Abuu Huraira kwa nambari 1189, na Muslim kwa nambari 1397.
Lau kufunga safari ya kwenda kwenye kaburi lake, au kaburi la mtu mwingine kungeruhusiwa, basi Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, angewaelekeza umma wake kuhusiana na hilo na akawaongoza kwenye fadhila zake. Kwa sababu yeye ndiye mwenye kunasihi zaidi ya watu wote, ambaye anamjua zaidi Mwenyezi Mungu kuliko watu wote, na mchamungu zaidi wa Mwenyezi Mungu kuliko wote, na tayari alishafikisha kufikisha kwa wazi, na akauonyesha umma wake kwenye kila jambo la kheri, na akawaonya dhidi ya maovu yote, alipotahadharisha kufunga safari kwenda katika misikiti isiyokuwa ile mitatu, na akasema: "Msilifanye kaburi langu kuwa sikukuu (mahali pa kuja mara kwa mara), wala nyumba zenu kuwa makaburi, na nitakieni rehema, kwani dua zenu hunifikia popote mlipo." ([170]) [129] Imeshatagulia kuelezwa aliyeipokea.
Kauli ya kuwa inaruhusiwa kufunga safari kwenda kuzuru kaburi lake, rehema na amani ziwe juu yake, inapelekea kulifanya kaburi hilo kuwa mahali pa kwenda mara kwa mara, na kutokea kwa jambo lililotahadharishwa ambalo alilihofia Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kama vile kuvuka mipaka na kumsifu zaidi ya kiasi, kama watu wengi walivyoangukia katika hayo kwa sababu ya kuamini kwamba kufunga safari kwenda kuzuru kaburi lake rehema na amani ziwe juu yake, kunaruhusiwa.
Na ama Hadithi zilizopokewa katika mlango huu zinazotumiwa kama hoja na wale waliosema kwamba kufunga safari kwenda kwenye kaburi lake kunaruhusiwa, hizo ni Hadithi zenye mlolongo dhaifu wa wapokezi, bali zilitungwa tu na watu, kama walivyotanabahisha juu yake wanazuoni waliohifadhi sawasawa, kama vile Ad-Daraqutni, Al-Baihaqi, Al-Hafidh Ibn Hajar na wengineo. Kwa hivyo, hairuhusiwi kupinga kwazo Hadithi sahihi zinazoashiria uharamu wa kufunga kwenda katika misikiti isiyokuwa ile Misikiti mitatu.
Hapa ewe msomaji kuna baadhi ya Hadithi hizi zilizotungwa na watu katika mlango huu; ili uzijue na ujihadhari na kudanganyika nazo:
Ya kwanza: “Mwenye kuhiji na asinizuru, basi hakika atakuwa amenitupa.”
Ya pili: “Mwenye kunizuru baada ya kufa kwangu, ni kama amenizuru katika uhai wangu.”
Tatu: “Mwenye kunizuru na akamzuru baba yangu Ibrahim katika mwaka mmoja, basi ninamdhamini Pepo kwa Mwenyezi Mungu."
Ya nne: “Mwenye kuzuru kaburi langu, basi lazima atapata uombezi wangu.”
Hadithi hizi na zinazofanana na hizo hazijathibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake.
Al-Hafidh Ibn Hajar alisema katika At-Talkhiis - baada ya kutaja riwaya nyingi: Njia za Hadithi hizi zote ni dhaifu.
Na amesema Al-Hafidh Al-'Uqailiy: Hakuna kitu chochote sahihi katika mlango huu.
Na Sheikh Al-Islam Ibn Taimiyya, Mwenyezi Mungu amrehemu, alisema huku akiwa na uhakika mkubwa kuwa Hadithi zote hizi ni za kutungwa na watu. Basi inatosha tu kuzijua, kuzihifadhi na kuzisoma.
Lau kama kuna chochote katika hizo kingethibiti, basi Maswahaba, Mwenyezi Mungu awawie radhi, wangelikuwa watu wa kwanza kuzifanyia kazi, wakauelezea umma na kuwalingania kwazo. Kwa sababu wao ndio watu bora zaidi baada ya Manabii, na wajuzi zaidi wa mipaka ya Mwenyezi Mungu na yale aliyowawekea waja wake katika sheria, na wenye kunasihi zaidi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na viumbe vyake. Basi kwakuwa hakuna chochote kilichosimuliwa kutoka kwao kuhusiana na hizo, hilo linaashiria kwamba haliko katika sheria.
Ikiwa chochote kati ya hizo kingekuwa sahihi, basi maana yake ingekuwa kuzuru kwa kisheria ambako hakuna kufunga safari kwenda kuzuru kaburi peke yake; ili kujumuisha kati ya Hadithi zote. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye anayejua zaidi.
Mlango:
Inapendekezwa kutembelea Msikiti wa Quba na makaburi ya Al-Baqi'i
Inapendekezwa kwa mtu anayezuru mji wa Madina kutembelea Msikiti wa Quba na kuswalia humo. Kwa sababu ya Hadithi ya bin Omar,i Mwenyezi Mungu awawie radhi, katika Sahihi mbili, kwamba alisema: “Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akitembelea Msikiti wa Quba, huku amepanda na akitembea, na anaswalia humo rakaa mbili." ([171]) (130) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1193, na Muslim kwa nambari 1399.
Na imesimuliwa kutoka kwa Sahl bin Hanif, Mwenyezi Mungu amwiye radhi, kwamba alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenye kujitwaharisha nyumbani kwake kisha akaja Msikiti wa Quba na akaswali humo swala yoyote, basi atapata ujira wa Umra." ([172]) [131] Kaipokea Ibn Majah kwa nambari 1412.
Na ni Sunna kwake kuzuru makaburi ya Al-Baqi’i, makaburi ya wale waliouawa kwa ajili ya dini (mashahidi) na kaburi la Hamza, Mwenyezi Mungu amuwie radhi. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akiwatembelea na kuwaombea dua, na kwa sababu alisema: “Tembeleeni makaburi, kwani yanakukumbusheni Akhera." ([173]) Imepokelewa na Muslim. [132] Kaipokea Muslim kwa nambari 976.
Na Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikuwa akiwafundisha Maswahaba wake wanapotembelea makaburi kusema: "Amani iwe juu yenu, enyi watu wa makazi haya, miongoni mwa Waumini na Waislamu. Nasi Mwenyezi Mungu akipenda, tutakufuateni. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe salama sisi na nyinyi." ([174]) Imepokelewa na Muslim kutoka katika Hadithi ya Suleiman bin Buraidah kutoka kwa baba yake. (133) Kaipokea Muslim kwa nambari 975.
Imepokelewa na At-Tirmidhi kutoka kwa bin Abbas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba: Siku moja alipita Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, karibu na makaburi ya Madina, basi akawaelekea kwa uso wake na akasema: "Amani iwe juu yenu, enyi watu wa makaburini haya. Mwenyezi Mungu atusamehe sisi na nyinyi. Nyinyi ni watangulizi wetu, nasi tutakufuateni nyuma." ([175]) [134] Ameipokea Tirmidhiy kwa nambari 1035.
Na kutokana na Hadithi hizi, inajulikana kuwa kuzuru makaburi kwa njia ya kisheria kunakusudiwa kukumbuka maisha ya baada ya kifo, kuwafanyia wema wafu na kuwaombea dua na rehema.
Ama kuwazuru kwa ajili ya kuomba dua karibu na makaburi yao, au kukaa kwenye makaburi yao, au kuwataka watimize haja fulani, au kuwaponya wagonjwa, au kumuomba Mwenyezi Mungu kupitia wao, au kwa heshima zao, na mfano wa hayo, hayo ni uzushi ulioongezwa katika dini unaopaswa kukatazwa kwani Mwenyezi Mungu hakuamrisha hayo wala Mtume wake, wala hawakuyafanya watagulizi wema, Mwenyezi Mungu awawie radhi. Bali ni katika maneno mabaya ambayo Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikataza aliposema: “Tembeleeni makaburi, wala msiseme mambo mabaya." ([176]) [135] Kaipokea Muslim kutoka kwa Ibn Buraida kutoka kwa baba yake, kwa nambari 977.
Mambo haya yaliyotajwa yanakusanyika pamoja katika sifa ya uzushi, lakini yako katika viwango tofauti tofauti. Baadhi yake ni uzushi na sio ushirikina; kama vile kumuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu dua karibu na kaburini, na kumuomba kwa haki na cheo cha maiti, na mfano wa hayo. Lakini baadhi yake ni ushirikina mkubwa, kama vile kuwaomba dua wafu na kuwaomba msaada, na mfano wa hayo.
Haya yameshatangulia kubainishwa kwa undani. Basi kuwa macho na jihadhari, na muombe Mola wako Mlezi akuwezeshe na akuongoe kufikia haki, kwani Yeye, aliyetakasika ndiye Mwenye kuwezesha na Mwenye kuongoza, na hakuna mungu mwingine wala mola mlezi ila Yeye.
Huu ndio mwisho wa yale tuliyotaka kuandika, na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu mwanzoni na mwisho, na rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie mja wake, Mtume wake, na mbora wa viumbe vyake, Muhammad, na ahali zake na Maswahaba wake, na wote wanaowafuata kwa wema mpaka Siku ya Kiyama.