آداب السفر وأحكامه
Adabu za safari na hukumu zake Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na rehema na amani ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad, na watu wake na Maswahaba zake wote.
Adabu za safari na hukumu zake Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na rehema na amani ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad, na watu wake na Maswahaba zake wote.
Ama baada ya hayo:
Hii ni makala fupi kuhusu adabu za safari na hukumu zake. Tumepupia ndani yake kuweka wazi mambo ambayo aghalabu anayahitajia msafiri.
Na tunamuomba Mwenyezi Mungu aufanye ujumbe huu uwe kwa ajili ya kutafuta uso wake mtukufu, na awanufaishe kwao Waislamu wote.
Kamati ya Kisayansi ya Jumuia ya Huduma ya Maudhui za Kiislamu kwa Lugha mbalimbali.
Kwanza: Adabu za safari
Mwenye kusafiri kwenda Hija au safari nyingine ya kiibada anafaa kuzingatia yafuatayo:
1-Amuombe Mwenyezi Mungu Mtukufu amchagulie muda sahihi wa safari, kipando, rafiki wa kuendana naye, na muelekeo wa njia, ikiwa njia zitakuwa nyingi. Na awatake ushauri kuhusu safari hiyo watu wenye uzoefu na wale walio wema. Ama Hija na Umra, ibada hizo ni za heri na hakuna shaka katika hilo. Na namna ya kumuomba Mwenyezi Mungu amchagulie jambo ni: Aswali rakaa mbili, kisha aombe dua iliyopokelewa kutoka kwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Ni wajibu kwa mwenye kufanya ibada ya Hija na Umra akusudie katika Hija yake na Umra yake kutafuta uso wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kujiweka karibu naye, na ajihadhari na kukusudia starehe za kidunia au kujifaharisha au kupata umaarufu au kujionyesha au kutaka kusikiwa; kwani kufanya hivyo kunasababisha kuharibika kwa matendo na kutokubaliwa kwake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sema: 'Mimi ni mwanadamu tu kama nyinyi. Ninaletewa Wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Kwa hivyo, mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi, basi naatende vitendo vyema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi.'" [Suratul Kahf: 110]. Na katika Hadithi takatifu: "Mimi ndiye niliyejitosheleza zaidi kuhitaji mshirika. Atakayefanya jambo lolote akamshirikisha pamoja nami mwingine, nitamuacha yeye na shirki yake (au na mshirika wake)." [1] Ameipokea Muslim, kwa namba 2985.
3. Ni wajibu kwa mwenye kufanya ibada ya Hija na Umra kujifunza hukumu za Umra na Hija, na kujifunza hukumu za safari kabla ya kuanza safari; ili asije akawacha jambo la wajibu au akafanya jambo la haramu. Amesema Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Yule ambaye Mwenyezi Mungu anamtakia heri, humpa ufahamu katika dini." (2) Kaipokea Bukhari kwa nambari 3116, na Muslim kwa nambari 100.
4. Ni wajibu kwa mwenye kukusudia kufanya Hija au Umra achaguwe mali halali kwa ajili ya ibada yake ya Hija na Umra; kwa sababu Mwenyezi Mungu ni mzuri na hakubali isipokuwa kilicho kizuri; na kwa sababu mali haramu husababisha kutojibiwa maombi.
5. Kutubia madhambi yote na maasi, na ikiwa aliwadhulumu watu, atarudisha alichokidhulumu na kuwataka wamwachilie. Ni sawa dhuluma hiyo iwe ni kuhusiana na heshima, mali au haki nyingine.
6. Inapendekezwa kwa msafiri aandike wasia wake, na kuandika anachodai na anachodaiwa. Amesema Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu, ziwe juu yake: "Sio haki kwa Muislamu kulala usiku mbili ikiwa anacho cha kuwaachia wasia familia ila awe amekiandika."[3] Na auwekee wasia huo mashahidi, na alipe madeni anayodaiwa, na arudishe amana kwa wenyewe au awatake idhini ziendelee kubakia kwake. [3] Kaipokea Bukhari kwa nambari 2788, na Muslim kwa nambari 1627.
7. Inapendekezwa kwa msafiri ajitahidi kuchaguwa rafiki mwema na apupie kwamba yule amchaguaye ni miongoni mwa wanafunzi wenye kujifunza elimu ya sheria; kwani kufanya hivyo ni sababu ya kufanikiwa na kuepuka kuingia kwenye makosa katika safari yake na katika ibada yake ya Hija na Umra. Haya ni kwa ushahidi wa maneno ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mtu huwa katika mwenendo wa rafiki yake wa karibu, basi na aangalie mmoja wenu ni nani anayemfanya kuwa rafiki yake."(4) Na kwa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, "Usifuatane katika safari zako isipokuwa na Muumini na asile chakula chako isipokuwa mcha Mungu."[5] [4] Ameipokea Abuu Daud, kwa namba 4833. [5] Ameipokea Abuu Daud, kwa namba 4832, na Tirmidhiy, kwa namba 2395.
8. Inapendekezwa kwa msafiri kuwaaga watu wake, jamaa zake wa karibu, majirani zake na marafiki zake. Amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Yeyote mwenye kutaka kusafiri, basi amwambie anayewaacha: "Ninakuachieni Mwenyezi Mungu, ambaye havipotei alivyoachiwa kutunza."[6] Na alikuwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - akiwaaga maswahaba zake anapotaka mmoja wao kusafiri. Alikuwa akisema: "Astaudiullaaha diinaka, wa amaanataka, wa khawaatiima 'amalika (Ninamkabidhi Mwenyezi Mungu dini yako, na amana yako na mwisho wa matendo yako)."[7] Na alikuwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - akimwambia msafiri mwenye kumtaka Mtume ampe wasia: "Zawwadaka llaahut taqwa, waghafara dhambaka, wayassara lakal khaira haithu ma kunta (Mwenyezi Mungu akupe ucha Mungu, na akusamehe dhambi zako na aifanye kheri kuwa nyepesi kwako mahala popote utakapokuwa)."[8] Na alikuja mtu mmoja kwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - akitaka kusafiri na akasema: 'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, nipe wasia.' Akasema: "Ninakuusia kumcha Mwenyezi Mungu, na kuleta Takbiira kila unapofika sehemu ya muinuko." Alipoondoka, Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, akamuombea kwa kusema: "Ewe Mwenyezi Mungu, mkunjie ardhi na umfanyie safari yake kuwa nyepesi."[9] (6)Ameipokea Twabaraniy kwa namba 823. (7) Ameipokea Ahmad katika Musnad yake kwa namba 4524. (8) Ameipokea Tirmidhiy, kwa namba 3444. (9) Ameipokea Ahmad katika Musnad yake kwa namba 9724.
(9)Asiandamane na kengele wala gitaa wala mbwa katika safari; kwa ushahidi wa Hadithi ya Abuu Huraira - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Hawafuatani Malaika na jamaa ambao miongoni mwao kuna mbwa wala kengele".(10) (10) Ameipokea Muslim kwa namba 2113.
(10) Na akitaka kusafiri na mmoja kati ya wake zake, ikiwa ni mwenye mke zaidi ya mmoja, atawapigia kura, na mke yeyote atakeyeangukiwa na kura ndiye atakayesafiri naye, kwa ushahidi wa hadithi ya Aisha - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - kwamba alisema: (11) "Alikuwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - akitaka kusafiri, anapiga kura kati ya wake zake, na yeyote ambaye utatoka mshale wenye jina lake, basi huyo ndiye aliyekuwa akisafiri pamoja naye."[11] (11) Kaipokea Bukhari kwa nambari 2593, na Muslim kwa nambari 2770.
(11) Inapendekezwa kwa msafiri asafiri siku ya Alhamisi mwanzo wa mchana ikiwa ni wepesi kwake; kwa sababu Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake -alikuwa akifanya hivyo. Amesema Kaab ibnu Maalik - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Ni mara chache sana alikuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akitoka kwenda safarini isipokuwa angetoka siku ya Alhamisi."(12) (12) Kaipokea Bukhari, kwa nambari 2949.
(12) Inapendekezwa kwake aombe dua ya kutoka nyumbani wakati anapotoka kwa jili ya safari au kwa jambo lingine. Atasema wakati wa kutoka: "Bismillaahi tawakkaltu 'alallaahi walaa hawla wala quwwata illaa billaahi. Allaahumma innii a'udhu bika an adhwilla aw udhwalla, aw azilla aw uzalla, aw adhlima aw udhlama, aw ajhala aw yujhala 'alayya (Kwa jina la Mwenyezi Mungu, nimetegemea kwa Mwenyezi Mungu na hakuna hila (namna) wala nguvu isipokuwa kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu. Ewe Mola wangu wa haki, hakika mimi ninajikinga kwako ili nisipotee au kupotezwa, au kuteleza na kufanya kosa au kutelezeshwa na kufanya makosa, au kudhulumu au kudhulumiwa, au kufanya ujinga au kufanyiwa ujinga)."(13) (13) Ameipokea Abu Daud, kwa nambari 5094.
(13) Na ni Sunna kwake aombe dua ya safari, atakapopanda mnyama wake, au gari lake, au ndege, au kipando kingine miongoni mwa vipando. Atasema: "Allahu Akbaru, Allahu Akbaru, Allahu Akbaru. "Sub-haanalladhii sakhkhara lanaa haadhaa wamaa kunnaa lahuu muqriniina, wa innaa ilaa rabbinaa lamunqalibuun." (Surat Az-ukhrufu) Allaahumma inna nas-aluka fii safarina haadhaa albirra wattaqwaa waminal 'amali maa tardhwaa. Allaahumma hawwin 'alaynaa safaranaa haadhaa wat-wi 'annaa bu'dahu. Allaahumma antas-swaahibu fis-safari, wal-khaliifatu fil-ahli. Allaahumma innii a'udhubika min wa'athaais-safari, waka-aabatil mandhwari, wasuuil-munqalabi fil-maali wal-ahli" Maana yake: "Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa "Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliyetudhalilishia (kipando) hiki, na hatukuwa ni wenye uwezo juu yake. Na hakika sisi kwa Mola wetu Mlezi ni wenye kurejea." Ewe Mwenyezi Mungu, hakika sisi tunakuomba katika safari yetu hii wema na ucha Mungu, na katika matendo yale unayoyaridhia. Ewe Mwenyezi Mungu, turahisishie safari yetu hii na utupunguzie umbali wake. Ewe Mwenyezi Mungu, wewe ndiye mwenza katika safari, na ndiye msimamizi katika familia. Ewe Mwenyezi Mungu, hakika ninajilinda kwako kutokana na uchovu na ugumu wa safari, na mandhari mabaya, na kurejea kubaya katika mali na familia."(17) (14) Maana ya neno "Wa'athaais-safar" ni ugumu wa safari. Maana hii inapatikana kwenye kitabu kiitwacho Al-ifswaahu 'an Ma'aani As-swihaah 4/284. (15) Neno hili linamaanisha muonekano mbaya na mtu kuwa katika hali ya kuvunjika kutokana na huzuni. Al-ifswaahu 'an Ma'aani As-swihaah 4/284. (16) Neno "Al-munqalab" ni kurudi. Maana hii inapatikana katika kitabu kiitwacho Al-ifswaahu 'an Ma'aani As-swihaah 4/284. (17) Ameipokea Ahmad katika Musnad yake kwa namba 6374.
(14) Inapendekezwa kwa msafiri asisafiri peke yake pasina kuwa na mtu wa kufuatana naye; kwa maneno ya Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Lau wangetambuwa watu yaliyopo kwenye upweke ninavyotambuwa mimi, asingesafiri msafiri wakati wa usiku akiwa peke yake."(18) (18) Kaipokea Bukhari, kwa nambari 2998.
(15) Wasafiri wanafaa kumchagua moja wao kuwa kiongozi; ili iwe rahisi zaidi kukusanya jambo lao pamoja, na kuwafanya kukubaliana zaidi, na lenye nguvu zaidi katika kufikia malengo yao. Amesema Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Watakapotoka watu watatu kwenda katika safari yoyote, basi wamfanye mmoja wao kuwa kiongozi."(19) (19) Ameipokea Abuu Daud, kwa namba 2608.
(16) Awe na pupa ya kufanya yale ambayo Mwenyezi Mungu amemuwajibishia miongoni mwa ibada, na kujiepusha mbali na yaliyoharamishwa. Vile vile anapaswa kujipamba kwa tabia njema, na amsaidie mwenye kuhitajia msaada, na atoe elimu kwa mwenye kuitafuta na kuihitajia, na awe mkarimu kwa mali yake, kwa kuitoa katika masilahi yake mwenyewe na katika masilahi ya ndugu zake na kuwatekelezea mahitaji yao.
(17) Inafaa aongeze matumizi na vinavyohitajika safarini, kwa kuwa shida inaweza kumtokea na mambo yakaenda tofauti.
(18) Inafaa awe katika safari ni mwenye uso wa bashasha, roho safi, akijitahidi kuingiza furaha kwa anayesafiri pamoja naye, ili awazoee wengine na azoeleke.
(19) Anafaa kuwa na subira kwa kila kinachomkuta miongoni mwa muamala mgumu wa wenye kusafiri pamoja naye, na wanapokwenda tofauti na maoni yake, na aamiliane nao kwa namna iliyo nzuri zaidi, ili awe ni mwenye kuheshimiwa baina yao na mwenye kupewa taadhima nyoyoni mwao.
(20) Inapendekezwa kwa wasafiri wanapofika mahala pa kushukia, wakae pamoja. Kwa maana, baadhi ya Maswahaba wa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - walikuwa wanapofika sehemu ya kushukia, wanatawanyika kwenye njia za milimani na mabonde. Akasema Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kwa hakika kutawanyika kwenu kwenye njia mbalimbali na kwenye mabonde, kufanya kwenu hivyo kunatokana na Shetani."(20) Kwa hivyo, baada ya hapo wakawa wanakusanyika pamoja kiasi kwamba ingekunjuliwa nguo juu yao ingewatosheleza wote. (20) Ameipokea Ahmad katika Musnadi wake kwa nambari 17736.
(21) Inapendekezwa mtu anaposhuka mahali katika safari yake au mahali pengine popote, aombe dua iliyothibiti kutoka kwa mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "A'udhu bikalimaatillaahit-taammaati min sharri maa khalaqa (Ninajilinda kwa maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyokamilika, kutokana na shari ya alichokiumba."(21) Kwani hakika akiyasema maneno hayo, hatodhuriwa na kitu chochote mpaka atakapoondoka mahala pale. (21) Ameipokea Muslimu kwa nambari 2708.
(22) Na inapendekezwa kwake afanye takbira (yaani kusema: Allaah akbaru (Mwenyezi Mungu nu Mkubwa)) kwenye miinuko,na kufanya tas-biih (yaani kusema: Subhaanallah (Ametakasika Mwenyezi Mungu)) anapoteremka kwenye mabonde na majangwa. Amesema Jaabir, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, "Tulikuwa tukifika kwenye miinuko, tunafanya takbira, na kwenye miteremko tanafanya tas-biihi."(22) Na wala wasipaze sauti zao kwa kuleta Takbira. Amesema Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Enyi watu, zioneeni huruma nafsi zenu. Kwani nyinyi hamumuombi kiziwi wala aliye mbali. Hakika Yeye yu pamoja nanyi. Hakika Yeye ni Msikivu, aliye karibu."[23] (22) Ameipokea Bukhari kwa nambari 2994. (23) Ameipokea Bukhari, kwa nambari 2993.
(23) Na inapendekezwa kwake asafiri wakati wa usiku na haswa mwanzo wa usiku, kwa maneno yake Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - "Pendeleeni kusafiri usiku, kwa sababu ardhi hupunguzwa wakati wa usiku."(24) (24) Ameipokea Abudaudi, kwa nambari 2571.
(24) Inapendekezwa kwake azidishe dua awapo safarini; kwa maneno ya Mtume - rehema na amani ziwe juu yake: "Dua za aina tatu ni zenye kukubaliwa bila shaka. Katika dua hizo ni dua ya aliyedhulimiwa, dua ya msafiri na dua ya mzazi kwa mtoto wake."(25) (25) Ameipokea Ahmad katika Musnad yake kwa namba 10771.
***
Pili: Twahara (usafi) katika safari
Ni wajibu kwa msafiri atilie umuhimu usafi wake. Kwa hivyo, atachukuwa udhu kutokana na hadathi ndogo na ataoga kutokana na Janaba.
Na ikiwa hakupata maji, au ikiwa ana maji machache anayoyahitajia kwa ajili ya kupikia na kunywa, basi atafanya Tayammam.
Na namna ya kutayammamu ni: Aipige ardhi kwa mikono (kwa ndani ya mikono) yake miwili, na aupake uso wake na viganja vyake kwayo.
Twahara ya kutayammam ni twahara ya muda tu. Kwa hivyo, wakati wowote akipata maji, tayammamu yake inaharibika, na itamlazimu kuyatumia maji. Na ikiwa alifanya tayammamu kwa sababu ya kupata Janaba kisha akapata maji, basi itamlazimu kuoga. Na kama akitayammam kwa sababu ya kukidhi haja kubwa kisha akapata maji, basi itamlazimu atawadhe. Imekuja katika hadithi kwamba: "Udongo safi ni udhu wa Muislamu hata kama atakosa maji miaka kumi. Akiyapata maji, basi amche Mwenyezi Mungu na ayagusishe kwenye mwili wake."(26) (26) Ameipokea Al-bazzaar katika Musnad wake kwa nambari 10068.
Kupangusa juu ya khofu mbili ni jambo la kisheria katika Qur'ani na Sunnah na ni makubaliano ya Ahlussunnah.
Kuna masharti kadhaa kwa ajili ya kupangusa juu ya khofu mbili na chenye kufanana na nazo:
1. Khofu (viatu vya kitambaa kizito) mbili hizo au soksi mbili hizo zinapaswa kuwa Halali na ni safi.
2. Azivae hizo khofu (viatu vya kitambaa kizito) akiwa na twahara.
3. Ziwe ni zenye kufunika sehemu za faradhi.
4. Iwe kupangusa ni kutokana na kupatwa na hadathi ndogo. Hairuhusiki kupangusa kwa kupatwa na Janaba wala kwa jambo ambalo linalazimisha kuoga.
5. Iwe kupangusa ni ndani ya wakati uliowekwa kisheria, nao ni mchana na usiku kwa mkazi, na michana mitatu na masaa yake ya usiku kwa msafiri. Muda huu kulingana na kauli sahihi huanzia pale mtu alipangusa kwa mara ya kwanza ya baada ya kuharibika kwa udhu, na huisha kwa kutimia masaa 24 kwa mkazi, na kwa masaa 72 kwa msafiri.
Na kupangusaji juu ya khofu hubatilika kwa moja kati ya mambo haya matatu:
1. Na likitokea jambo linalolazimisha kuoga, kama vile janaba hubatilisha kupaka na ni lazima kuoga.
2. Ikiwa atazivua khofu baada ya kuwa amekwishapangusa juu yake.
3. Ikiwa muda unaozingatiwa kisheria utaisha, basi upangusaji utakuwa batili.
***
Tatu: Hukumu za kupunguza swala safarini
Kupunguza swala katika safari ni bora kuliko kuswali swala kamili; lakini kama msafiri atakamilisha swala rakaa nne, basi swala yake itakuwa ni sahihi lakini atakuwa amekwenda kinyume na kilicho bora.
Anapunguza swala msafiri atakapokuwa ametoka na kuziwacha kabisa nyumba zote za kijiji chake au mji wake, na huu ndio msimamo wa madhebu ya wengi wa maulamaa.
Ikiwa atasafiri baada ya kuingia wakati wa swala, ana haki ya kupunguza swala kwa sababu amesafiri kabla ya muda wake kwisha.
Ama kukusanya swala kati ya Adhuhuri na Alaasiri na kati ya Magharibi na Isha, hilo ni Sunna kwa msafiri anapohitajia kufanya hivyo. Itakapokuwa safari imeshika kasi na imeshaendelea, basi afanye litakalokuwa rahisi kwake kama vile kutanguliza au kuchelewesha.
Ama ikiwa msafiri hana hitajio la kukusanya swala, basi asikusanye, mfano awe ameshuka na kukaa mahala ambapo hataki kuondoka hapo mpaka ifike saa ya swala inayofuata, basi lililo bora kwake ni kutokusanya. Kwa sababu hahitaji kufanya hivyo. Na ndiyo maana Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - hakukusanya alipokuwa ameshuka na kukaa Mina katika Hija ya Kuaga kwa sababu hakuhitaji kufanya hivyo.
Ama swala za sunnah, ataziswali msafiri kwa namna anavyoziswali mkazi. Kwa hivyo ataswali swala ya Dhuha, Tahajjud, Witiri na zinginezo miongoni mwa swala za sunna isipokuwa sunna za kabla na baada ya swala ya Adhuhuri, Maghari na Isha. Sunnah katika hizo ni kuwacha kuziswali.
Ni sahihi kuswalia swala za sunnah juu ya kipando kama vike ndege, gari, meli na vyombo vinginevyo vya usafiri. Ama swala za Faradhi, hizo ni lazima kuteremka kwa ajili ya kuziswalia chini isipouwa itakaposhindikana.
Swala ya msafiri anayeswali nyuma ya mkazi ni sahihi, na atakamilisha msafiri kama swala ya imamu wake. Ni sawa ameikuta swala yote au amekuta rakaa moja au chini ya hivyo. Hata kama ataingia pamoja naye katika Tashahhud ya mwisho kabla ya kutoa salamu, basi atakamilisha swala hiyo bila kufupisha. Hivi ndiyo sahihi kutoka katika kauli za wanazuoni.
***
Nne: Adabu za kurudi kutoka katika ibada ya Hija, Umra au safari
Anapaswa afanye haraka kurudi na wala asikae muda mrefu katika safari pasina kuwa na haja ya kukaa muda mrefu; kwa maneno ya Mtume -rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: Safari ni kipande cha adhabu. Inamzuia mmoja wenu kula na kunywa na kulala kwake. Kwa hivyo, akimaliza mmoja wenu hitajio lake, basi na afanye haraka arudi kwa watu wake."(27) (27) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1804, na Muslim kwa nambari 1927.
Na akitaka kurudi kwenye mji wake, atasoma dua ya safari wakati wa kupanda kwake kipando chake na atazidisha kwa kusema: "Aayibuun, taaibuun, 'aabiduun, lirabbinaa haamiduun" yaani, tunarejea, tunatubia, tunamuabudu Mwenyezi Mungu na tunamsifu Mola wetu Mlezi."(28) (28) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1797, na Muslim kwa nambari 1342.
Inapendekezwa kwake aseme wakati wa kurudi kutoka katika safari yake kilichothibiti kutoka kwa mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - kuwa yeye alikuwa akirejea kutoka safari au vita, au Hijja au Umra, alikuwa akifanya takbira tatu kila alipopanda sehemu ya miinuko kisha anasema: "Laailaaha illa llaahu, wah-dahuu laa shariika lahuu, lahul-mulku, walahul-hamdu, wahuwa 'alaa kulli shay-in Qadiir. Aayibuuna, taaibuuna, 'aabiduuna, saajiduuna, lirabbinaa haamiduuna. Swadaqallaahu wa'adahuu, wanaswara 'abdahuu, wa hazamal-ahzaaba wah-dahuu." Yaani, "Hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirka. Ni wake ufalme, na sifa njema zote ni zake, na yeye ni Muweza wa kila kitu. Tunarejea, tunatubia, tunafanya ibada, tunasujudu na tunamsifu Mola wetu Mlezi. Mwenyezi Mungu alitimiza ahadi yake, akamnusuru mja wake na akashinda makundi ya maadui peke yake."(29) (29) Kaipokea Bukhari, kwa nambari 4116.
Inapendekezwa kwake pindi atakapouona mji wake, aseme: "Aayibuun, taaibuun, aabiduun, lirabbinaa haamiduun." Yaani, "Tunarejea, tunatubia, tunamuabudu Mwenyezi Mungu na tunamsifu Mola wetu Mlezi."(30) Na atarudiarudia maneno hayo mpaka atakapoingia katika mji wake; kwa kufanya kwake hivyo Mtume, rehema na amani ya mwenyezi mungu ziwe juu yake. (30) Kaipokea Bukhari kwa nambari 1797, na Muslim kwa nambari 1342.
Asije kwa familia yake usiku ikiwa alikaa mbali kwa muda mrefu pasina kuwa na haja ya kuja usiku, isipokuwa ikiwa aliwafikishia kuwa anakuja, na akawapa habari kwamba atafika usiku. Hii ni kwa sababu Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - alikataza hilo. Amesema Jaabir ibnu Abdillah - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao: "Alikataza Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - mwanamume kuwagongea wana familia yake wakati wa usiku (bila ya kuwapa taarifa ya kurudi kwake usiku)."(31) Na hekima ya kufanya hivyo imetafsiriwa na riwaya nyingine: "Mpaka awe amekwishachana matimtimu ya nywele zake (32) na amenyoa nywele za sehemu za siri."(33) Na katika riwaya nyingine: "Alikataza Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - mwanamume kuwagongea watu wa familia yake usiku ili kuchunguza kama wanamfanyia hiyana au kutafuta makosa yao."(34) (31) Kaipokea Muslim, kwa nambari 715. (32) Neno "Ash-shaa'tha" linamaanisha mwanamke mwenye nywele matimtimu ambazo hazijapakwa mafuta kwa muda mrefu. Na "Al-istihdaad" ni kutumia ala iliyotengenezwa kwa chuma kama vile wembe katika kunyoa sehemu za siri. Nalo neno "Al- maghiiba" ni mwanamke ambaye mume wake amekaa mbali naye kwa muda mrefu. Tazama At-Tahriir fii sharh Swahih Muslim, cha Al-Asbahaaniy uk. 292. (33) Kaipokea An-Nasai, kwa nambari 9099. (34) Kaipokea Muslim, kwa nambari 715.
Inapendekezwa kwa mwenye kutoka safarini aanzie msikiti ambao upo jirani naye na aswali humo rakaa mbili; kwa sababu Mtume -rehema na amani ya Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akifanya hivyo
Inapendekezwa kwa msafiri atakapofika kutoka safarini, awaonyeshe huruma watoto wa nyumbani kwake na majirani zake na awafanyie wema watakapompokea. Imepokelewa kutoka kwa Ibnu Abbas - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Alipofika Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika mji wa Makkah, walimpokea watoto wadogo wa Banii Abdul Mutwalib. Basi akambeba mtoto mmoja mbele yake na mwingine mgongoni kwake." Naye Abdullahi ibnu Jaafar - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - alisema: "Alikuwa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - anaporudi kutoka safarini, analakiwa pamoja nasi. Basi siku moja alilakiwa pamoja nami na Hassan au Hussein, na akambeba mmoja wetu mbele yake na mwingine nyuma yake mpaka tukaingia Madinah."(35) (35) Kaipokea Muslim, kwa nambari 2428.
Inapendekezwa kutoa zawadi, kwa kuwa kutoa zawadi kuna furahisha nyoyo na kuondoa chuki. Na inapendekezwa kuikubali zawadi na kulipa juu yake. Na inachukiza kuikataa pasina kuwepo kizuizi cha kisheria. Ndiyo maana amesema Mtume -rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Peaneni zawadi, mtapendana."(36) Na zawadi ni sababu miongoni mwa sababu za kuleta upendo baina ya Waislamu. (36) Ameipokea Baihakiy katika Sunanil Kubra, kwa nambari 11946.
Akifika msafiri katika mji wake, imependekezwa kukumbatiana, kwa sababu ya yale yaliyothibiti kutoka kwa Maswahaba wa Mtume - rehema na amani za Mwenyezi mungu ziwe juu yake - kama alivyosema Anas - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Walikuwa wanapokutana, wanasalimiana kwa mikono, na wanaporudi kutoka safarini, wanakumbatiana."(37) (37) Ameipokea Twabariy katika Al-awswat, kwa nambari 97.
Na mwisho tunaomba rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie Nabii wetu Muhammadi.