شرح ألفاظ الأذان
كتاب ألفاظ الأذان شرح مختصر لمعاني ألفاظ الأذان بأسلوب يناسب غير المسلمين
Ufafanuzi wa matamshi ya Adhana
Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Kuhudumia Maudhui za Kiislamu kwa Lugha Mbalimbali.
Adhana ni Wito wa Mola Mlezi anaousikia Muislamu mara tano kila siku; ukimkumbusha ukuu wa Mwenyezi Mungu na kumuita kwenye kheri na mafanikio. Ni wakati wa mawasiliano baina ya mwanadamu na Muumba wake, ambapo hujitenga na kelele za dunia ili asimame akinong'ona na Mola wake Mlezi. Adhana haichukuliwi kuwa ni tangazo tu la kuingia kwa wakati wa swala, bali ni wito wa utulivu na imani, na wa kufanya upya uhusiano na Mwenyezi Mungu. Adhana hubeba maana tukufu zinazoanza kwa kumtukuza Mwenyezi Mungu na kuishia kwa wito wa swala, ambapo Muislamu hupata utulivu wake. Kila mara Adhana inapotangazwa, hunong’ona moyoni kwamba maisha ya kweli huanza kwa kuwa karibu na Mwenyezi Mungu.
Maneno ya adhana:
Allaahu Akbaru Allaahu Akbaru, Allaahu Akbaru Allaahu Akbaru. Yaani: Mwenyezi Mungu ni Mkubwa Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa Mwenyezi Mungu ni Mkubwa.
Mwenyezi Mungu ni Mkubwa
Jina la Utukufu: “Allah” maana yake ni Mwenye Uungu, yaani anayestahiki kuabudiwa peke yake; nalo ni jina la Mola Mlezi, Muumbaji, Mwenye utukufu mkubwa. Na majina yote ya Kiungu yamefungamana na jina hilo na ni maelezo ya sifa zake. Na Allah ndiye Mmoja, Mpweke, ambaye hakuzaa wala hakuzaliwa, na Yeye ndiye Muumbaji wa mbingu zote na ardhi.
Maana ya neno "Allahu Akbaru" ni Mwenyezi Mungu ni Mkubwa na Mtukufu kuliko kila kitu. Ni Mtukufu mno kiasi kwamba hafailii kuhusishwa na chochote kisichofailiana na Utukufu wake na Ukamilifu wake.
Kauli "Allaahu Akbaru".. inamkumbusha Muislamu kwamba hakuna kitu katika maisha haya kinachopaswa kumshughulisha na kumtenga na Muumba wake, na kwamba inampasa mwanadamu aende katika maisha yake kwa mujibu wa matashi ya Mwenyezi Mungu na Sheria yake, si kwa mujibu wa matamanio na matakwa yake; kwa maana Mwenyezi Mungu ni Mkubwa na Mtukufu kuliko kila kilichomo duniani.
Fundi anaposikia "Allahu Akbaru", husimamisha ufundi wake; naye mkulima husimamisha kulima kwake; naye mfanyabiashara hufunga duka lake; naye mwalimu husimamisha somo lake; kwa sababu Mwenyezi Mungu ni Mkubwa na Mtukufu kuliko kila shughuli na kazi. Na kusimama huku na kujielekeza katika ibada ni ushahidi kwamba Mwenyezi Mungu ni Mkubwa zaidi katika moyo wa Muumini kuliko kila starehe ya dunia. Mwenyezi Mungu ni Mkubwa kuliko kila balaa na msiba, na kuliko hali yoyote katika maisha. Na anayeamini hivyo, huziona tabu na misukosuko kuwa ndogo sana, na moyo wake hutulia kwa sababu yuko pamoja na Mwenyezi Mungu, ameridhia mapitisho yake na mipango yake, na ana imani na hekima yake na uendeshaji wake wa mambo.
Ash-hadu anlaa ilaaha illa llaahu, Ash-hadu anlaa ilaaha illa llaahu. Yaani: Ninashuhudia kuwa hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, ninashuhudia kuwa hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu.
Ash-hadu anlaa ilaaha illa llaahu. Yaani: Ninashuhudia kwamba hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu.
Hii ndiyo shahada ya kwanza, na maana yake ni kukiri na kuitakidi kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu, na Mola Mlezi na Mmiliki wake, na Mpangiliaji Mwendeshaji wa mambo yake; na kwamba Yeye ndiye anayepasa kuabudiwa peke yake bila yeyote mwingine; na kwamba hakuna muabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake; na kwamba Yeye ni Mmoja, hana mshirika, wala hana mwana, wala hana mfano wake; basi ibada isielekezwe kwa yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu, wala asiombwe yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
Na shahada hii ndiyo shahada kubwa na tukufu zaidi kuwahi kuwepo, nayo ndiyo asili ya imani katika jumbe zote za ki-Mungu. Kwani, Manabii wote, amani iwe juu yao, kama vile Nuhu, Ibrahim, Musa na Isa hadi Muhammad, waliwaita kaumu zao wakiri, wakubali na waamini kwamba hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake. Na ndiyo kauli ambayo kwa ajili yake Mwenyezi Mungu aliwaumba viumbe, akawatuma Mitume kuithibitisha, na akateremsha Vitabu kuibainisha. Na akaifanya Pepo kuwa malipo kwa yule atakayeileta kwa ikhlasi kutoka moyoni mwake, na akaufanya Moto kuwa haramu juu ya yule atakayekufa akiwa na yakini nayo.
Hii ndiyo ufunguo wa Imani, na ni mlango wa kusalimika, na ndiyo asili ya Dini, na msingi wa kumpwekesha Mwenyezi Mungu.
Kwa ajili ya neno hili watu watafufuliwa kutoka makaburini mwao, na wataulizwa juu ya matendo yao Siku ya Kiyama. Basi atakayekuwa ameishi kwa mujibu wa kauli hiyo na akahitimisha maisha yake kwa neno hilo, huyo amefaulu kwa ushindi mkubwa. Na atakayelikataa na asilitamke, basi atastahiki kudumu milele katika Jahannam.
Ash-hadu anna Muhammadan Rasuulullaah, Ash-hadu anna Muhammadan Rasuulullaah. Yaani: Ninashuhudia kwamba Muhammad ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu, ninashuhudia kuwa Muhammad ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu.
Ash-hadu anna Muhammadan Rasuulullaah. Yaani: Ninashuhudia kwamba Muhammad ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu.
Maana ya Shahada hii ni kwamba Muislamu ashuhudie kuwa Mwenyezi Mungu alimtuma Muhammad kuwa Mtume wake wa mwisho, ili awafikishie watu ujumbe wa Mola wao Mlezi, na kwamba Muislamu athibitishe kwa yakini kwamba hakuna njia ya kumuabudu Mwenyezi Mungu na kuzipata radhi zake ila kwa kumshuhudilia Mtume - rehema na amani ziwe juu yake - Utume wake, kumtii, kumfuata na kumuiga, na kumuabudu Mwenyezi Mungu kwa sheria aliyoifikisha Mtume Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake. Na kwamba kila ibada anayojikurubisha kwayo mtu ambayo Mtume hakuifikisha, basi hiyo ni ibada batili, na haimsaidii mwenye kuifanya duniani wala Akhera. Bali ataulizwa juu yake na ataadhibiwa, kwa sababu alimuabudu Mwenyezi Mungu pasina yale aliyoyafikisha Mtume wake - rehema na amani ziwe juu yake.
Na shahada hii inajumuisha kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ni mja wa Mwenyezi Mungu na ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote. Vile vile, inajumuisha kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ni wa mwisho katika Wajumbe wa Mwenyezi Mungu, na kwamba hakuna Nabii baada yake. Vile vile, inajumuisha kuamini miujiza yote aliyokuja nayo, na iliyo kubwa zaidi ni Qur’ani Tukufu, ambayo ni ujumbe wa mwisho kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na ambayo imebaki kuwepo katika lugha ile ile iliyoteremshwa kwayo, ikiwa imelindwa dhidi ya kuongezewa, kupunguzwa au kubadilishwa. Na kwamba Qur'ani Tukufu haina cha kufanana nayo katika ufasaha wake, hukumu zake, na muongozo wake. Mwenyezi Mungu aliwapa changamoto wanadamu walete hata sura moja mfano wake; wakashindwa miaka nenda miaka rudi, na mpaka leo hii wanadamu wameshindwa kufanya hivyo.
Na inajumuisha shahada ya kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alikuja ili kuwarejesha watu katika kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kama walivyofanya kabla yake Ibrahimu, Musa na Isa, amani iwe juu yao. Basi yeye ni Mtume wa Mola Mlezi wa walimwengu, ambaye aliifuata njia ile ile waliyoiendea Manabii wote katika kufikisha ujumbe wa Mola wao Mlezi. Tofauti tu iliyoko katika yake na wengineo ni kwamba hakuna nabii atakayekuja baada yake (kutoka kwa Mwenyezi Mungu).
Njooni kwenye swala, njooni kwenye swala.
Njooni kwenye swala.
Maana yake ni: Enyi Waumini, elekeeni katika ibada ya Mola wenu Mlezi, hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe, ni Mwenye kurehemu, anakubali toba, na anaachilia mbali madhambi.
Kwa hakika, ni utukufu mkubwa mno kwamba Mwenyezi Mungu humwamuru mtu, katika kila mahali palipo na kundi la Waislamu, atangaze Adhana, na awaite kila siku mara tano, akiwaambia: Njooni, elekeeni katika kumwabudu Mola wenu Mlezi.
Kwa hakika huu ni wito na ukumbusho kwa Waumini kwamba umefika wakati wao wa kumuabudu Mola wao Mlezi, na kwamba inawapasa waachane na yanayowashughulisha katika mambo ya dunia, na waelekee katika ibada. Waachane yaliyo mikononi mwao ya biashara au kilimo, na waelekee kwa Mwenyezi Mungu; na hili ni ushahidi wa ukweli wa imani, na kwamba hilo hutangulizwa juu ya kila starehe ya dunia.
Kwa hakika huo ni Wito unaowaita watu kwenda katika Swala, ambayo ni uhusiano wa moja kwa moja baina ya mja na Mola wake Mlezi. Hakika hiyo ni Ibada inayobomoa ubaguzi wa kitabaka na kuwafanya watu kuwa sawa mbele ya Mola wao Mlezi.
Njooni kwenye mafanikio, njooni kwenye mafanikio.
Njooni kwenye mafanikio
Kufanikiwa humaanisha radhi, kufuzu, usalama na kuokoka katika dunia na Akhera, pamoja na furaha ya milele na kuongolewa kuifikia njia iliyo sahihi.
Na miongoni mwa maana zake ni kufaulu kupata radhi za Mwenyezi Mungu, na kufaulu kupata Pepo na kuokoka kutokana na Moto. Kwani, yeyote aliyeamini na kuswali, basi amefaulu. Na mwenye kufaulu, basi ameokoka na amefaulu kupata kudumu milele katika Pepo.
Hakika muadhini huwakumbusha Waumini katika kila Swala kwamba njooni kwenye usalama na amani, utulivu wa moyo, usafi wa roho, na furaha ya dunia na Akhira.
Allahu Akbaru, Allahu Akbaru, laa ilaaha illa llah. Yaani, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa. Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu.
Kuhitimisha adhana kwa kumtukuza Mwenyezi Mungu (takbira) na kumpwekesha (tauhidi).
Adhana huhitimishwa kwa kurudiarudia kauli “Allahu Akbaru (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa)”, na kusisitiza “Laa ilaaha illa llahu (Hakuna mungu apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu)”. Kauli hizi mbili zinatilia mkazo maana zilizotangulia, nazo ndizo mhimili wa uwepo wa wanadamu. Na ukweli huu ndio uhakika wa kiulimwengu na uwepo ulio wa ukweli zaidi, iwe mwanadamu ameuelewa au hakuuelewa, ameujua au hajaujua; kwani mambo makubwa ya uhakika hayadhuriki kwa kutojuliwa na baadhi ya watu. Uhakika huu hauwezi kubadilika wala kugeuka hata muda ukirefuka namna gani, na hata matukio yakifuatana namna gani. Nao ni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mkubwa kuliko kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mungu wa haki, na kwamba Mwenyezi Mungu ndiye anayestahiki kuabudiwa peke yake, na kwamba kumuabudu asiyekuwa Yeye ni batili.
Ni wito wa kutukuza yale aliyoyatukuza Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kumshuhudilia Mwenyezi Mungu kwa yale ambayo alijishuhudilia mwenyewe; na Mitume, amani iwe juu yao, wakamshuhudilia hayo, na vile vile Waumini.
Hatimaye, Adhana si wito wa swala tu, bali ni wito wa kufuzu, ushindi na mafanikio. Ni ujumbe unaosikika katika misikiti mara tano kila siku, ili uamshe nyoyo; na kutukumbusha kuwa Mwenyezi Mungu yuko karibu, na kwamba utulivu wa moyo unawezekana, na kwamba njia ya kuelekea katika kufuzu huanza kwa swala na kwa kuimarisha uhusiano kati ya mja na Muumba wake.
Hivyo basi, rudia pamoja na Muadhini: Allahu Akbaru Allahu Akbaru (Mwenyezi Mungu ni Mkubwa, Mwenyezi Mungu ni Mkubwa), Laa ilaaha illa llahu (hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu). Rudia shahada ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu (tauhidi), na ushuhudie kwa yale aliyojishuhudilia Mwenyezi Mungu, na yale ya haki waliyokuja nayo Mitume wake, utakuwa miongoni mwa wenye kufaulu na Waislamu wanaompwekesha Mwenyezi Mungu.
Fungua moyo wako kwa ajili ya imani, na sema: “Ninashuhudia kuwa hapana mungu apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na ninashuhudia kwamba Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu”, utaingia katika rehema za Mwenyezi Mungu, na utapata furaha duniani, na utafaulu Akhera, na utafufuliwa Siku ya Kiyama katika kundi la Waumini.