يومي الأول في الإسلام
SIKU YANGU YA KWANZA KATIKA UISLAMU
SIKU YANGU YA KWANZA KATIKA UISLAMU
Kwa Jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu:
Utangulizi
Kila sifa njema zinamstahiki Mwenyezi Mungu aliyemtuma Nabii wake Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- kuwa ni huruma kwa walimwengu wote, na ninashuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, yeye pekee asiye na mshirika wake, Mola mlezi wa mwanzo na wa mwisho, na ninashuhudia kuwa Muhammadi ni mja wake na ni Mtume wake, ndiye wa mwisho katika manabii na Mitume, Rehema na Amani ziwe juu yake, na salamu nyingi mpaka siku ya kiyama, Ama baada ya hayo:
Watu wote wanatafuta furaha; yuko miongoni mwao anayedhani kuwa furaha iko katika kukusanya mali, na yuko anaye utafuta chini ya mwanga wa umaarufu, na yuko anaye iona furaha kuwa iko katika kupata vyeo vya juu, au mengineyo katika starehe za uhai wa dunia, lakini uhalisia unashuhudia kuwa watu wengi waliovipata vitu hivi bado hawajaifikia furaha wanayoitaka.
Hakika furaha hii haiwezekani kwetu sisi kuipata isipokuwa pale tutakapo ongoka katika dini ya kweli ambayo alituchagulia muumba wa watu wote, na tuitumie kama mfumo wa maisha, na tuishi kwa mujibu wa mafundisho yake, kwa hili pekee tutaipata furaha ya maisha mazuri duniani, na furaha ya milele katika maisha baada ya dunia (Akhera), anasema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka:
"Hakika ataingia Peponi mwenye kumtakasa Mwenyezi Mungu peke yake asiye na mshirika na akawa ni mwenye kumfuata Mtume Muhammad, rehema na amani zimshukie, katika maneno yake yote na vitendo vyake vyote. Basi mwenye kufanya hayo atakuwa na thawabu ya matendo yake mbele ya Mola wake huko Akhera, nayo ni kuingia Peponi, hali ya kuwa wao, hao wenye kuingia Peponi, hawaogopi mambo ya Akhera yanayowakabili mbele yao, wala hawahuzuniki juu ya hadhi za ulimwengu zilizowapita".
[Al Baqara: 112],
Na anasema:
"Mwenye kufanya tendo zuri, akiwa ni mwanamume au ni mwanamke, na huku ni mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake , basi tutampa maisha mema yenye utulivu duniani hata kama ni mchache wa mali, na tutawalipa huko Akhera thawabu zao kwa uzuri zaidi ya walivyofanya duniani."
[An Nahli: 97].
Na wewe kwa kuingia kwako katika uislamu -Ndugu yangu kipenzi- unakuwa tayari umeuweka mguu wako katika njia ya uongofu na mwangaza, na furaha na amani, unatakiwa kuwa na uhakika kuwa siku ya kusilimu kwako haifanani na siku yoyote katika maisha yako, kwani hiyo ni siku ya kuzaliwa upya kwako!
Ikiwa siku uliyozaliwa ulitoka katika giza la mfuko wa uzazi wa mama yako na mahala penye dhiki ukaja katika mwangaza wa dunia na upana wake, basi na wewe leo unatoka katika giza la ukafiri kuja katika mwangaza wa imani, na kutoka katika dhiki ya upotovu kuja katika upana wa uongofu, anasema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka:
"Je, yule ambaye amekufa katika upotofu, ameangamia na ameshangaa, tukaufufua moyo wake kwa Imani, tukamuongoza kwenye Imani na tukamuafikia (tukamuwezesha) kuwafuata Mitume wake, akawa anaishi kwenye miangaza ya uongofu, atakuwa ni kama mfano wa yule aliye ndani ya ujinga, matamanio ya moyo na namna mbalimbali za upotevu, asiye ongokewa kwenye sehemu yoyote ya kupenya na hana wa kumuokoa na yale ambayo yumo ndani yake? Hao wawili hawalingani. Na kama nilivyomuachilia kafiri huyu anayebishana na nyinyi, enyi Waumini, nikampambia vitendo vyake viovu akaviona ni vyema, vilevile nimewapambia wenye kukanusha vitendo vyao viovu ili wapaswe, kwa hilo, kupata adhabu".
[Al An'am: 122]
Karibu sana katika uwanja mpana wa uislamu, na chukua kitabu hiki ambacho kimekusanya mambo muhimu, na misingi mikubwa, ambayo unatakiwa kuifahamu katika siku ya kwanza ya kusilimu kwako.
Mwanzo:
UISLAMU NDIO DINI YA KWELI:
Dini ya uislamu ndiyo dini ya kweli aliyoichagua Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa watu wote, na ndiyo dini ambayo pekee haikubaliwi dini nyingine mbele ya Mwenyezi Mungu, na anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Hakika dini ya kweli mbele ya Mwenyezi Mungu ni uislamu"
[Al-Imran: 19].
Na anasema aliyetakasika na kutukuka:
"Na Mwenye kutafuta dini isiyokuwa dini ya Kiislamu, ambayo ni kujisalimisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kumpwekesha na kumfuata kwa kumtii na kumdhalilikia, na kwa Mtume wake aliye Nabii wa mwisho Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, kwa kumuamini na kumfuata na kumpenda kwa dhahiri na kwa siri, basi hiyo haitakubaliwa kwake, na yeye Akhera atakuwa ni miongoni mwa wenye kupata hasara ambao walizifanyia ubahili nafsi zao kwa kuzinyima mambo yenye kuzinufaisha".
[Al-Imran: 85].
Na mwenye kuikubali dini ya uislamu na akashikamana nayo, basi huyu atatembea katika njia ya mwangaza na uongofu; njia iliyonyooka wazi wazi ambayo inamfikisha mtu kwa Mwenyezi Mungu aliyemuumba mwanadamu na akamleta katika uhai huu.
Na imekuja dini ya uislamu kurekebisha hali ya mwanadamu na utulivu wake na furaha yake katika maisha yake ya dunia, na vile vile furaha yake na mafanikio yake katika maisha ya akhera baada ya kifo, wakati Mwenyezi Mungu atamuingiza peponi akastarehe kwa yale yaliyomo miongoni mwa neema za milele.
Ni wajibu kwa kila mwanadamu atafute dini ya kweli ambayo ni uislamu, na aisome aijue, na aingie ndani yake akiwa ni muumini, na ashikamane na mafundisho yake na hukumu zake, ili apate mazuri ya dunia na akhera.
NI NAMNA GANI MTU ANAWEZA KUINGIA KATIKA UISLAMU?
Mtu anaingia katika uislamu atakaposema: (Ash-hadu an laa ilaaha illa llaahu, wa ash-hadu anna Muhammadan Rasuulullah), Yaani: Nashuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kwamba Muhammadi ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Aseme hivyo kwa kuamini kweli na kwa yakini (kwa uhakika kweli) na kwa kujua maana ya neno hilo, atakayesema neno hilo kwa kulijua maana yake na akawa ni mkweli katika kauli yake akiwa na uhakika tena kwa utiifu juu ya yale anayokusudiwa katika neno hilo, basi huyo atakuwa kaingia katika uislamu, kisha anatakiwa ajifunze matendo mengine yaliyobakia katika matendo ya uislamu, na ayafanyie kazi kwa kadiri ya nafasi yake, na kila inapozidi elimu yake inazidi imani yake na malipo yake yanakuwa makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Maana ya shahada mbili: Nashuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ispokuwa Mwenyezi Mungu peke yake na Muhammad ni mtume wa Mwenyezi Mungu:
Tayari umekwisha kuingia katika uislamu kwa kauli yako ya (Ash-hadu An laa ilaaha illa llaah, wa anna Muhammadan Rasuulullaah), ukiwa na imani na neno hilo na kwa kusadikisha, Je wajua uhalisia wa maana yake?
Maana ya kushuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu: Ni kuitakidi kuwa hakuna mahala popote mungu mwenye kustahiki kuabudiwa na kutiiwa isipokuwa mungu mmoja tu, naye ni Allah aliyetakasika na kutukuka, muumba wa ulimwengu na mpangiliaji wa mambo yake.
Na maana ya kushuhudia kuwa Muhammadi ni mtume wa Mwenyezi Mungu: Ni kuitakidi na kukiri kuwa Muhammadi ni mja wa Mwenyezi Mungu na ni Mtume wake wa mwisho, aliyetumwa kwa watu wote, na kuyafanyia kazi yale yanayohitajika katika hilo; kwa kumtii katika yale aliyoyaamrisha na kumsadikisha katika yale aliyoyaeleza, na kuyaepuka yale aliyoyakataza na kuyakemea, na kuwa asiabudiwe Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa sheria alizoziweka.
HABARI NJEMA KWAKO KWA UISLAMU:
Ndugu yangu kipenzi, hakika siku yako ya kwanza kuingia katika uislamu ndiyo siku yako bora kwa ujumla, na imethibiti kuwa Nabii Muhammadi Rehema na Amani ziwe juu yake amesema:
"Uislamu unabomoa yaliyokuwa kabla yake"
Imepokelewa na Imamu Muslim,
Yaani nikuwa uislamu unafuta yote yaliyotokea kwako kabla ya kusilimu kwako; miongoni mwa ukafiri na shari na makosa na madhambi, basi jipe habari njema ya kupata msamaha wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, wewe leo hii unasafishwa kutokana na makosa yako, na unafungua ukurasa mweupe katika maisha yako, ili urudi kuwa msafi kama siku aliyokuzaa mama yako, na unaanza maisha mapya yaliyojaa kheri, na utatembea katika njia ya uongofu na mwangaza na furaha na amani.
KUFURAHIA NEEMA YA MWENYEZI MUNGU:
Hakika furaha kubwa uliyoihisi wakati wa kuingia kwako katika uislamu inatakiwa iendelee kuwa pamoja nawe maisha yako yote, neema ya uongofu ni katika neema tukufu, na ni katika neema kubwa anazo waneemesha Mwenyezi Mungu waja wake, ni neema kubwa kuliko neema ya hewa na maji na chakula na vinywaji, na ni kubwa kuliko mali na uongozi na vyeo, ni neema kubwa kwa ujumla, Ni kwanini tusiifurahikie? Anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Sema, ewe Mtume, kuwaambia watu wote, «Kwa wema wa Mwenyezi Mungu na rehema yake, basi na wawe na furaha.» Wema wa Mwenyezi Mungu na rehema yake ni Uislamu ambao ni uongofu na ni Dini ya haki aliyokuja nayo Mtume, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kwani Uislamu ambao Mwenyezi Mungu amewaita wao waufuate, na Qur’ani ambayo aliiteremsha kwa Muhammad, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie ni bora kuliko taka za ulimwengu wanazozikusanya na anasa zilizomo ndani yake zenye kutoweka na kuondoka."
[Yunus: 59].
Ni lazima uhisi fadhila za Mwenyezi Mungu juu yako, kwa kukuchagua wewe kati ya mamilioni ya watu ili uingie katika uislamu, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Mtu yeyote ambaye Allah hutaka kumuongoza basi hufungua kifua chake kwa ajili ya uislamu"
[Al An'am: 125],
Na neema hii kubwa na tukufu inahitaji kushukuru sana, hivyo unatakiwa kukithirisha kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumhimidi na kumsifu yeye aliyetakasika na kutukuka kwa kukuongoza katika dini sahihi.
MISINGI YA LAZIMA KUIFAHAMU:
Unapoingia katika uislamu kuna mambo ni lazima kwako kuyafahamu, na miongoni mwake ni kujua majibu ya maswali matatu muhimu ambayo ataulizwa kila mwanadamu baada ya kifo, na ambayo yatakayoweka kikomo cha maisha yake ya milele; ima aingie peponi au ima aingie motoni, nayo ni:
Ni nani Mola wako?
Ni ipi dini yako?
Ni nani Nabii wako?
Msingi wa kwanza: Ni nani mola wako?
Mola wangu ni Mwenyezi Mungu.
Muislamu anaamini kuwa mola wake mlezi ni Allah aliyeumba ulimwengu huu kwa kila kilichomo, na akamuumba mwanadamu.
Na sisi tunapotafakari katika huu ulimwengu mkubwa na vile vilivyomo miongoni mwa miujiza ya kutisha, na vile unavyovikusanya miongoni mwa mabilioni ya Sayari na Nyota, na tukiitafakari ardhi hii ambayo tunaishi juu yake na yale yaliyomo miongoni mwa viwanja vipana na Milima, na vitu vikavu na Mabahari na Mito, na vile vilivyomo miongoni mwa maajabu ya viumbe vilivyoko katika kina kirefu cha bahari na majangwa na mapori, basi hakika kufikiri kwetu kutatufikisha katika matokeo ambayo hayana namna zaidi ya kukubali; kuwa ni lazima awepo muumbaji mtukufu mjuzi muweza mwenye hekima; aliyeumba ulimwengu huu kwa umahiri, haiwezekani kupatikana viumbe hivi bila kuwepo mola muumba aliyeviumba, na akapangilia mambo yake, na akaufanya vizuri ufundi wake kwa namna inayozishangaza akili, na jambo hili kalibainisha Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kwa uwazi kwa kila mwenye akili pale aliposema:
"Je, wameumbwa hawa washirikina bila kuwako mwenye kuwaumba na kuwafanya wawepo au wao wamejiumba wenyewe? Na yote mambo mawili haya yametanguka na hayawezekani. Na kwa hivyo, inalazimika kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba, na yeye peke yake ndiye ambaye hakuna anayepasa kuabudiwa, wala kufaa kuabudiwa, isipokuwa yeye".
[Attur: 35]
Haviwezekani viumbe vyote hivyo kujileta vyenyewe, na wala haiwezekani kuwepo bila mletaji wake, hili haliwezekani kwa watu wenye akili!
MWENYEZI MUNGU NDIYE MWENYE KUSTAHIKI KUABUDIWA PEKEE:
Na huyu Mlezi ndiye Mola mwenye kustahiki kuabudiwa peke yake; kwa sababu yeye ndiye muumba mpangiliaji wa yote yaliyoko katika ulimwengu huu, na mgawaji wa riziki kwa vyote vilivyomo ndani yake; yeye ndiye aliyeumba watu wote na akawaleta katika ardhi hii, na akawapa sababu za kuishi, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Huyo, enyi washirikina, Ndiye Mola wenu, hapana Mwenye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye; Mwenye kuumba kila kitu. Basi mfuateni na mumnyenyekee kwa kumtii na kumuabudu. Na yeye ni Mlinzi wa kila kitu".
[Al An'am: 102].
Hivyo ni wajibu kwa wanadamu amuabudu Mwenyezi Mungu peke yake na wala asishirikishe kitu chochote katika ibada zake, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
(Enyi watu muabuduni Mola wenu ambaye amekuumbeni na amewaumba walio kabla yenu ili mpate kuwa wachamungu)
[Al Baqara: 21].
Na anasema Mtukufu:
"Na muabuduni Mwenyezi Mungu na msimshirikishe na chochote"
[An Nisaai: 36].
UJUMBE WA MANABII KATIKA KUMPWEKESHA MWENYEZI MUNGU MTUKUFU:
Pamoja na uwazi wa jambo hili, isipokuwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kwa fadhila zake na karama zake, na kwa huruma yake kwetu, hakutuumba na akatutelekeza (akatuacha bure) tukizagaa zagaa tu katika maisha, bali alitutumia mitume na akateremsha pamoja nao vitabu wakitufundisha kuhusu yeye na wakituelekeza kwake, kama alivyosema Mtukufu:
"Hakika sisi tumekutuma kwa haki, nayo ni kumuamini Mwenyezi Mungu na Sheria za Dini, hali ya kuwapa bishara ya Pepo wale wenye kukuamini na wakaufuata uongofu wako kivitendo, na hali ya kuwaonya Moto wale waliokukanusha na wakakuasi. Na hakuna taifa lolote la watu isipokuwa limejiwa na muonyaji wa kuwaonya mwisho mbaya wa ukafiri wao na upotevu wao."
{Surat Faatir: 24}
Na baba wa binadamu Adamu amani iwe juu yake, na Manabii wote, na miongoni mwao Nuhu na Ibrahimu na Musa na Issa na wengineo katika Manabii, mpaka mwisho kwa Nabii wetu Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- wote walikubaliana katika msingi mkuu; nao ni kuwaita watu kuja kumuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kumpwekesha na kumfanya wa pekee kwa ibada, na kuacha kumuabudu asiyekuwa yeye miongoni mwa vinavyoabudiwa; miongoni mwa mawe na miti na nyota na sayari na vinginevyo, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
{Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Shetani}.
[An Nahli: 36].
Na anasema aliyetakasika na kutukuka:
"Na hatukupata kutuma kabla yako, ewe Mtume, mjumbe yeyote isipokuwa tunampatia wahyi kwamba hapana mwenye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu. Basi mtakasieni ibada yeye peke yake".
[Al Anbiyaa: 25].
KATIKA MAJINA YA MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE:
Mwenyezi Mungu Mtukufu ana majina mazuri mno na sifa za hali ya juu mno, wakati tunapozifahamu tunazidisha kumuelewa Mola wetu aliyetakata na mtukufu, na tunazidisha kumpenda, na kumuogopa, na kutarajia fadhila zake na karama zake, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu.
"Mwenyezi Mungu ambaye hakuna muabudiwa kwa haki isipokuwa yeye, ni yake peke yake majina yaliyokamilika katika uzuri."
[Twaha: 8].
Na majina yake yenye kujulisha sifa zake ni mengi, miongoni mwa majina ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
Mwingi wa Rehema na Mwenye kurehemu: Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na Mola wenu, enyi watu, ni Mola Mmoja aliyepwekeka katika dhati yake, majina yake, sifa zake na vitendo vyake na uja wa viumbe vyake kwake. Hapana apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye, Mwingi wa rehema, Mwenye kusifika kwa sifa ya rehema katika dhati yake, vitendo vyake kwa waja wake wote, na Mwenye kuwarehemu Waumini."
[Al Baqara: 163]
Yeye ni mwenye huruma pana kubwa ambayo imekienea kila kitu, na imewaenea viumbe wote, na imewakusanya huruma yake katika dunia viumbe wake wote; kuanzia wanyama binadamu na wasiokuwa waislamu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na rehema yangu imekienea kila kitu".
[Al A'raf: 156],
Yeye anawaruzuku wote na anawapa afya na chakula na watoto na mengineyo, na ama huruma yake katika akhera haitokuwa isipokuwa kwa waumini miongoni mwa waja wake, waliowafuata Manabii wake na Mitume wake, hawa ndio watakaokuwa na huruma kamilifu itakayowafikisha katika furaha ya milele.
MUUMBA: Amesema Mtukufu:
{Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu},
[Azzumar: 62],
Yeye ndiye aliyeumba mbingu na ardhi na vyote vilivyo kati yake, na akaumba kila kitu kutoka katika punje mpaka kufikia umbile kubwa mfano wa mkusanyiko wa nyota, au zaidi ya hapo, na kuumba kwake pia kulikuwa ni kwa hekima kubwa, na kwa uweza, na kwa wema, huwezi kuona mapungufu katika uumbaji wake au kuharibika.
Msamehevu (Al ghafuur): Mwenye kusamehe madhambi yote kwa mwenye kutubia kikweli kweli, kwa namna yoyote atakavyokuja na matendo mabaya yaliyopita, bali anaweza kuyasamehe mengine mengi kutoka kwa waja wake ikiwa ni ukarimu kutoka katika nafsi yake- kasoro shirki katika ibada za Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwani hii haisameheki ila kwa kufanya toba, na Mwenyezi Mungu amefungua milango kwa viumbe wake wote kwa ajili ya kuupata msamaha wake; kwa kuomba toba, na kutaka msamaha, na kwa imani, na matendo mema, na kufanya wema kwa viumbe wa Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na mimi ni Mwingi wa kusamehe kwa anayetubia kutokana na dhambi zake na ukanushaji wake, akaniamini mimi na akafanya matendo mema kisha akaongoka kufuata njia ya ukweli na akasimama imara juu yake."
[Twaha: 82].
Mgawaji wa riziki (Arrazzaq): Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye Mfalme ambaye mkononi mwake kuna ufalme wa kila kitu, na yeye ndiye tajiri, na katika fadhila zake pia kuwa yeye ni Mgawaji (Wahhab), na hakuna kiumbe chochote isipokuwa riziki yake iko kwa Mwenyezi Mungu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na sikuumba majini na binadamu na kutuma Mitume wote isipokuwa kwa lengo tukufu, nalo niabudiwe mimi peke yangu, na sio asiyekuwa mimi".
Sitaki kutoka kwao riziki wala sitaki wanilishe.
Hakika Mwenyezi Mungu ndiye mtoaji riziki mwenye nguvu madhubuti"
(Surat Dhariat: 56-58)
Amani (Assalam): Mtukufu aliyetakasika na aibu na sifa za mapungufu zote, ambaye anasifa kamilifu na utukufu na uzuri, anayependa kwa waja wake kupeana salamu (amani) kwa kauli na vitendo, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu.
(Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila yeye)
[Al hashri: 23].
Mjuzi: (Al A'liim): Mwenyezi Mungu Mtukufu ni msikivu mwingi wa kuona na mjuzi, elimu yake imekienea kila kitu, yeye anayajua yanayoonekana, na yasiyoonekana, na yanayofichwa na vifua, na anayajua yaliyokuwa katika zama zilizopita, na yanayoendelea kwa wakati uliopo, na yale yatakayotokea katika wakati ujao, na yeye ni mlinzi anayeyatazama matendo ya waja, haiwezi kuficha kwake twa'a (jema) lolote la wenye kumtii wala maasi ya wenye kumuasi, wala hitajio la wasiojiweza wala sauti ya wenye kuomba, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
{Kwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu}.
[A Baqara: 231]
Ametakasika yeye Mola mlezi wa walimwengu, alikipa kila kitu umbile zuri, na kila aina ya uzuri na ukamilifu katika ulimwengu huu, hiyo ni katika athari za ukamilifu wake Mtukufu.
MSINGI WA PILI: NI IPI DINI YAKO?
Dini yangu ni Uislamu.
Na uislamu: Ni kujisalimisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kumpwekesha, na kunyenyekea kwa kumtii, na kujiepusha na ushirikina.
Muislamu ni yule anayeingia katika dini ya uislamu, na akasalimisha maisha yake kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, akiamini uwepo wake na umoja wake, akitii amri zake, na akiyaepuka makatazo yake, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Qur'ani tukufu:
"Hakuna yeyote aliye mwema wa dini kuliko yule aliyejisalimisha kwa Mwenyezi Mungu, aliyetukuka, peke yake, kwa moyo wake na viungo vyake vyote, hali ya kuwa ni mwema wa maneno na vitendo, mwenye kufuata amri ya Mola wake, akawa amefuata mila ya Ibrāhīm na Sheria aliyoileta na amejiepusha na itikadi mbaya na sheria zilizo batili".
[An Nisaai: 125]
Na anasema:
"Hakuna yeyote aliye na kauli nzuri zaidi kuliko yule anayelingania kupwekeshwa Mwenyezi Mungu na kuuabudiwa yeye peke yake, na akasema, «Mimi ni katika Waislamu wanaofuata amri ya Mwenyezi Mungu na Sheria yake.»
(Fuswilat: 33)
KATIKA MAZURI YA DINI YA UISLAMU:
Uislamu ni dini ya uadilifu: Unaamrisha uadilifu kumfanyia ndugu wa karibu au wa mbali, na adui na rafiki, na muumini na kafiri, anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha uadilifu".
[An Nahli: 90].
Na Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka ni muamuzi muadilifu hadhulumiwi kwake yeyote, anasema Mtukufu kuhusu siku ya kiyama:
"Leo italipwa kila nafsi kwa kile ilichokitenda duniani, chema au kiovu; hakuna uonevu leo wa kufanyiwa yeyote, ya kuongezewa dhambi zake au kupunguziwa thawabu zake. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwepesi wa kuhesabu, basi msiione Siku hiyo ni yenye kuchelewa kufika, kwani iko karibu."
[Ghaafir: 17].
UISLAMU NI DINI YA HURUMA: ANASEMA MWENYEZI MUNGU MTUKUFU:
"Na hatukukutuma , ewe Mtume, isipokuwa ni rehema kwa watu wote. Mwenye kukuamini atakuwa mwema na ataokoka, na asiyeamini atapita patupu na atapata hasara."
[Al Anbiyaai: 107].
Na anasema Mtume rehema na amani za Allah ziwe juu yake:
"Wenye huruma huwahurumia Ar-Rahmani -Mwingi wa huruma-, wahurumieni walioko ardhini atakuhurumieni aliyeko mbinguni."
Imepokelewa na Abuu Daud
UISLAMU NI DINI YA MAPENZI NA KUISHI PAMOJA NA KUZOEANA: ANASEMA NABII MUHAMMADI REHEMA NA AMANI ZIWE JUU YAKE:
"Hawezi kuwa na Imani mmoja wenu mpaka ampendelee ndugu yake anachokipenda yeye katika nafsi yake"
Imepokelewa na Bukhari.
Uislamu ni dini ya wepesi: Mafundisho yote ya uislamu ndani yake kuna wepesi na kuondoa uzito kwa watu kiasi kwamba analijua hili kila mwenye kufuatilia mafundisho yake, anasema Mtukufu:
"Anakutakieni wepesi Mwenyezi Mungu kwenu nyinyi na wala hakutakieni uzito" [Al baqara: 185],
Na anasema:
"Hataki Mwenyezi Mungu kukufanyieni uzito kwenu nyinyi"
[Al Maida: 6]
Na anasema:
"Hailazimishi Mwenyezi Mungu nafsi ila kwa kadiri ya nafasi yake"
[Al baqara: 286].
Uislamu ni dini ya elimu: Aya ya kwanza iliyoteremka ndani ya Qur'ani ni:
"Soma, ewe Nabii, Qur’ani uliyoteremshiwa ukianza kwa Jina la Mola wako aliyepwekeka kwa kuumba."
[Al A'laq: 1].
Na uislamu unamuhimiza kila muislamu mwanaume na mwanamke juu ya kujifunza na kuongeza elimu, amesema Mtukufu:
"Na sema, Mola wangu nizidishie elimu".
[Twaha: 114].
Na mwenye kujifunza ana daraja za juu, anasema aliyetakasika na kutukuka:
"Anawanyanyua (daraja) Mwenyezi Mungu wale walioamini miongoni mwenu, na wale waliopewa elimu daraja za juu zaidi, na Mwenyezi Mungu kwa yale mnayoyafanya ni mjuzi".
[Al-Mujadilah: 11].
Uislamu kuwa kwake ni dini ya ulimwengu:
Uislamu ni dini ya ulimwengu, haihusishi eneo fulani la ardhi pasina eneo jingine, na wala kwa watu fulani na si wengine, hii si dini ya waarabu peke yao, bali ni dini ya watu wote, amesema Mtukufu akimueleza nabii wake Muhammadi Rehema na Amani ziwe juu yake katika Qru'ani tukufu:
"Sema: Enyi watu! Hakika mimi ni Mtume kwenu nyinyi nyote, niliye tumwa na Mwenyezi Mungu Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Hapana mungu ila yeye anaye huisha na anaye fisha. Basi muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake asiyejua kusoma na kuandika, ambaye anamuamini Mwenyezi Mungu na maneno yake. Na mfuateni yeye ili mpate kuongoka."
[Al A'araf: 158].
Kama ambavyo dini hii si maalumu kwa zama zilizopita pekee, bali ndiyo dini ya kweli tangu kutumwa kwake Nabii Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- mpaka siku ya kiyama, amesema Mtukufu:
"Na atakeyetaka dini isiyokuwa dini ya uislamu, basi haitokubaliwa kwake naye akhera atakuwa ni mwenye hasara kubwa."
[Al-Imran: 85].
Uislamu kuwa kwake ni dini ya sekta zote:
Uislamu ni mfumo wa maisha; kwa muislamu mmoja mmoja na kwa jamii nzima kwa ujumla, na umma wa kiislamu, katika sekta na nyanja mbali mbali; katika maswala ya siasa na uchumi na ya kijamii na mengineyo.
Uislamu ni itikadi na sheria: ni dini iliyokusanya itikadi sahihi, na ibada tukufu, na miamala ya busara, na tabia njema, na nyenendo madhubuti.
Mafundisho ya uislamu na hukumu zake vinadhibiti mahusiano kati ya mtu na mola wake, na mahusiano kati ya mtu na nafsi yake, na mahusiano kati ya mtu na mwenzie miongoni mwa watu, na hata mahusiano yake na wanyama na visivyo na uhai.
Mafundisho ya uislamu yanakusanya kila yanayohusiana na roho na mwili.
Na kwa ujumla nikuwa: Uislamu umeleta kila kitu ambacho ndani yake kuna faida na masilahi kwa watu na furaha yao duniani na akhera.
MISINGI YA ITIKADI YA KIISLAMU (NGUZO ZA IMANI):
Inajikita misingi ya dini ya kiislamu katika imani na kusadikisha kikweli kwa mambo sita, ambayo huitwa jina la (Nguzo za imani), Nazo ni:
1- Kumuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu: Yaani ni kuamini uwepo wa Mwenyezi Mungu, nakwamba yeye pekee ndiye muumba na mmiliki na mpangiliaji wa ulimwengu wote kwa kila kitu kilichomo, nakwamba yeye ndiye anayestahiki kuabudiwa peke yake asiye na mshirika wake, nakwamba yeye anasifika kwa sifa za uzuri na utukufu, na kwamba yeye ni mkamilifu ameepukana na kila aibu na mapungufu, nakwamba hakuna kitu chochote mfano wake.
2- Kuwaamini Malaika: Nao ni viumbe katika viumbe wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, aliwaumba kwa ajili ya kumuabudu yeye, na utiifu uliokamilika wa amri yake, na kusimamia yale aliyowakabidhi miongoni mwa kazi mbali mbali, tunaamini uwepo wao kwa namna ya ujumla, kama ambavyo tunaamini majina na sifa na kazi ambazo wahyi umetueleza kuhusu wao, kwa namna ya kufafanua; kama Jibrili ambaye Mwenyezi Mungu humtuma kuleta wahyi kwa Manabii na Mitume, na Mikaeli ambaye kapewa jukumu la mvua na mimea, na Israfili ambaye kapewa jukumu la kupuliza baragumu, na Malaika wa kifo ambaye hutoa roho za watu, na Maaliki mlinzi wa moto.
3- Kuamini vitabu: Navyo ni vitabu ambavyo kaviteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mitume wake, iwe ni rehema kwa viumbe, na muongozo kwao; ili waweze kufika katika furaha ya dunia na akhera, tunaviamini kwa namna ya kiujumla, na tunaviamini vile ambavyo tumejua kwa majina yake kupitia wahyi kwa kufafanuliwa; kama Qur'ani iliyoteremshwa kwa Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- na Injili iliyoteremshwa kwa Issa Amani iwe juu yake, na Taurati iliyoteremshwa kwa Mussa Amani iwe juu yake, na Zaburi iliyoteremshwa kwa Daudi Amani iwe juu yake, na Nyaraka zilizoteremshwa kwa Ibrahim Amani iwe juu yake.
4- Kuamini Mitume: Nao ni wanadamu aliowateremshia wahyi Mwenyezi Mungu kwao kama miongozo, na akawatuma kwa watu ili wafikishe dini yake, wa mwanzo wao ni Nuhu Amani iwe juu yake, na wa mwisho wao ni Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake-, na walikuwa ni wakamilifu katika dini na tabia, na lengo kuu la kutumwa kwao ni kuwaita watu kuja kumpwekesha Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kwa ibada, na waache ushirikina na kuabudu visivyokuwa yeye, na wafanye mazuri, na waache shari.
Tunaamini kuwa Mwenyezi Mungu alituma Mitume miongoni mwa watu; Na akawawajibishia waja kuwaamini kwa yale waliyoyaeleza, na kuwatii na kuyafuata yale waliyoyaamrisha, na tunajua kuwa wako miongoni mwao aliotueleza Mwenyezi Mungu majina yao na visa vyao pamoja na watu wao, mfano: Idrisa,na Nuhu, na Ibrahim,na Mussa, na Hudi, na Swalehe, na Shuaibu, na wako miongoni mwao ambao hakutueleza Mwenyezi Mungu kwa majina yao; amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Hakika tuliwatuma kabla yako, ewe Mtume, Mitume wengi kwa watu wao wawalinganie na wavumilie udhia wao. Miongoni mwao kuna wale tuliokuhadithia habari zao, na miongoni mwao kuna wale ambao hatukukuhadithia. Na wote hao wameaminiwa kufikisha wahyi wa Mwenyezi Mungu kwa watu wao. Na haikuwa ni yenye kuwezekana kwa yeyote miongoni mwao kuleta alama yoyote miongoni mwa alama zinazo onekana au zinazofahamika isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu na matakwa yake. Basi itakapokuja amri ya Mwenyezi Mungu ya kuadhibiwa wakanushaji, itatolewa hukumu ya uadilifu baina ya Mitume na wale waliowakanusha, na hapo watapata hasara waliokuwa wabatilifu kwa kule kumzulia kwao Mwenyezi Mungu uongo na kuabudu kwao asiyekuwa yeye."
[Ghafiri: 78].
5- Kuamini siku ya mwisho: Nayo ni siku ya kiyama ambayo Mwenyezi Mungu atawafufua ndani yake watu kwa ajili ya kuhesabiwa na kulipwa juu ya matendo yao waliyoyafanya duniani; kiasi kwamba watu wamegawanyika katika makundi mawili, watakaa waumini peponi milele daima, na watakaa makafiri motoni milele daima, na aliyekuwa muumini lakini akawa anafanya maasi, ima Mwenyezi Mungu amsamehe, au amuadhibu kwa muda maalumu kisha amuingize peponi.
6- Kuamini makadirio kheri yake na shari yake: Hivyo muislamu anaamini kuwa Mwenyezi Mungu anajua yaliyokuwa na yatakayokuwa, nakwamba Mwenyezi Mungu aliandika makadirio ya viumbe na akataka makadirio hayo yawe na yakawa, hakitokei kitu katika ulimwengu isipokuwa kwa elimu yake, na kakiandika, na ni kwa matashi yake na ni kwa uumbaji wake, ikiwa ni jambo la kheri basi hilo ni rehema kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa jambo hilo, na ikiwa ni kinyume na hivyo basi huo ni mtihani kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na uadilifu wake, ambao watu hawawezi kuudhibiti kwa kuuelewa , kwa sababu ya utukufu wake na ukamilifu wake, na anapoamini mja makadirio kheri yake na shari yake moyo wake utatulia na roho yake itapumzika,, na atayakabidhi mambo yake yote kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu; kwa sababu yeye atakuwa anajua kuwa kila kitu kiko mkononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake; anayoyataka huwa, na asiyoyataka hayawi.
Nguzo za Uislamu:
Nguzo za Uislamu ndiyo msingi wake ambao hujengwa juu yake, nazo ni nguzo tano za wajibu kwa muislamu kuzitekeleza:
1- Kushuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu, na kuwa Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu: Nayo ni shahada inayotamkwa kwa ulimi, na moyo kuikubali, kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muabudiwa wa kweli peke yake asiye na mshirika wake, na kuwa Muhammadi Rehema na Amani ziwe juu yake ni Mtume mfikishaji kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
2- Kusimamisha swala: Ni wajibu kwa muislamu kuswali swala tano usiku na mchana, swala ina kisimamo na rukuu na sijida; kwa kumtukuza Mwenyezi Mungu Mtukufu, na zina nyakati ambazo huitwa kwa majina yake, nazo ni: swala ya Alfajiri, na swala ya Adhuhuri, na swala ya Lasiri, na swala ya Magharibi, na swala ya Ishaa, na kuna swala zingine zisizokuwa za lazima.
3- Kutoa zaka: Ni kwa muislamu kutoa kiwango kichache chenye idadi maalumu kwa yule mwenye mali katika mali yake, na anazipeleka kwa mwenye kustahiki miongoni mwa mafakiri, na masikini, na wengineo miongoni mwa wale ambao hupewa zaka.
4- Kufunga Ramadhani: Ni kujizuia muislamu na chakula, na vinywaji, na tendo la ndoa, na mfano wa hayo miongoni mwa yale yenye kufunguza, kuanzia kuchomoza kwa alfajiri mpaka kuzama jua katika kipindi chote cha Ramadhani; hayo ni kwa kumuabudu Mwenyezi Mungu.
5- Kuhiji katika nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu: Nako ni muislamu kwenda Makka Tukufu; kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu Mtukufu kupitia ibada ya hija, walau mara moja katika umri, kwa mwenye kuweza kufanya hivyo.
Ibada katika Uislamu:
Ibada: Ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu Mtukufu na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kila anayoyapenda na kuyaridhia katika kauli na matendo ya wazi na ya siri.
Miongoni mwa kauli ni: Kusoma Qur'ani, na dua, na kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kufundisha elimu yenye manufaa, na kutoa nasaha kwa wengine, na mengineyo.
Na katika matendo: Ni twahara, na swala, na Hija, na kwenda mbio kutimiza haja za watu, na mengineyo.
Na ibada za wazi: Ni matendo yanayoonekana wazi na yanaonekana kwa macho na yanasikilizika, na mfano wa hayo; kama swala, na hija, na kusoma Qur'ani, na kulingania katika njia ya Mwenyezi Mungu, na kuwaunga udugu ndugu wa karibu.
Na za siri: Ni amali ambazo huwa ziko moyoni; kama kumpenda Mwenyezi Mungu Mtukufu, nakuwa na matarajio kwake na kumuhofu, na kumnyenyekea, na kumtegemea Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Umuhimu wa Ibada katika Uislamu:
Ibada za Mwenyezi Mungu ndiyo lengo ambalo kwa ajili yake Mwenyezi Mungu aliwaumba viumbe, amesema Mtukufu:
"Na sikuumba majini na binadamu na kutuma Mitume wote isipokuwa kwa lengo tukufu, nalo niabudiwe mimi peke yangu, na sio asiyekuwa mimi".
[Adh Dhariyati: 56].
Na ibada zilifanywa kuwa ni sheria kwa hekima kubwa, na masilahi mengine ambayo yanatimia katika nafsi za watu na maisha yao, miongoni mwa fadhila za ibada nikuwa zinaisafisha nafsi, na zinaitwaharisha, na zinampandisha mtu daraja ya ukamilifu.
Na mwanadamu ana haja kubwa ya ibada, kama ambavyo mwili wake unahitaji chakula na vinywaji, na hivyo hivyo moyo wake na roho yake ina haja kubwa ya kuelekea kwa Mwenyezi Mungu kwa ibada; nafsi haiwezi kutulia ila kwa kumtaja Mwenyezi Mungu na kumuabudu, na wala moyo hauwezi kupata furaha wala kifua hakiwezi kufunguka isipokuwa kwa kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na mahusiano mazuri naye, watu walioshikamana na ibada kiukweli hao ndio watu wenye kuwa na furaha kuliko watu wote, na wenye mioyo mikunjufu, yeyote mwenye kutaka furaha basi ashikamane na kizingiti cha utumwa kwa Mwenyezi Mungu peke yake.
Kuenea kwa Ibada nyanja zote za Uislamu:
Ibada katika uislamu inakusanya amali zote njema ambao Mwenyezi Mungu anazipenda, na ambazo tunajikurubisha kwazo kwake aliyetakasika na kutukuka, hivyo zinakusanya:
- Alama zote za ibada: kama swala, zaka, swaumu, hija, na kusoma Qur'ani, na dua, na kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, na nyinginezo.
- Nakuwa na muamala mzuri: kama kuwafanyia wema wazazi wawili, na kuunga udugu, na kuishi vizuri na mke na watoto, na kuwa mzuri katika kuuza na kununua, na kuwa mfanisi wakati wa kutekeleza amali mbali mbali, na kumfanyia wema jirani, na kuwasaidia masikini, na kuwafanyia wema wanyama, na mengineyo.
- Na vile vile inakusanya tabia njema: kama kuwa mkweli katika mazungumzo, na kutekeleza amana, na kutimiza makubaliano, na kutabasamu, na kuwa na maneno mazuri, na kuwa na haya, na mengine miongoni mwa tabia njema.
Muislamu humuabudu Mwenyezi Mungu katika hali zake zote, anamuabudu Mwenyezi Mungu Msikitini, nyumbani, kazini, na kila mahali, maisha yake yote ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, amesema Mtukufu:
Sema,«Hakika Swala yangu na kuchinja kwangu wanyama,na uzima wangu na kufa kwangu vyote ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu muumba wa walimwengu wote."
[Al-an-aam 162].
MSINGI WA TATU: NI NANI MTUME WAKO?
Mtume wangu ni Muhammad - Rehema na amani za Allah ziwe juu yake-
Mtume wetu ni Muhammadi bin Abdallah bin Abdul Muttwalib bin Hashim, na unarudi ukoo wake kwa nabii wa Mwenyezi Mungu Ismaili mtoto wa Nabii wa Mwenyezi Mungu Ibrahim amani iwe juu yao wote wawili na kwa Nabii wetu sala na salamu bora zimfikie.
Alimtuma Mwenyezi Mungu katika mji wa Makka na alikuwa na umri wa miaka arobaini, na akamteremshia Qur'ani, akawaita watu katika kumpwekesha Mwenyezi Mungu na dini ya uislamu, jamii yake ikamuudhi maudhi makubwa, na wakawatesa wanafunzi wake na wakaua idadi kadhaa miongoni mwao, kisha akahamia katika mji wa Yathrib (kisha ukabadilishwa jina lake na kuitwa Madina Nabawia -yaani: Jiji la Mtume), baada ya miaka kumi na tatu ya utume akiwa Makka, na huko katika mji wa Madina alisimamisha dola ya kiislamu, na akaasisi jamii ya kiislamu, na akabakia Madina miaka kumi akiwaongoza watu na akiwaelekeza na akilingania na akifundisha, na akaendelea katika hali hiyo mpaka sheria ikatimia, uislamu ukatimia na dini ikakamilika, na ikateremka kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Leo hii nimekukamilishieni Dini yenu na nimekutimizieni neema zangu, na nimekuridhieni kuwa Uislamu ndiyo Dini yenu."
[Al Maida: 3]
Kisha akafariki Rehema na Amani ziwe juu yake baada yakuwa jicho lake limetulia kwa kuwaona watu wakiingia katika dini ya Mwenyezi Mungu mmoja mmoja na kwa makundi, kama alivyosema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka:
"Utakapotimia kwako , ewe Mtume, ushindi juu ya makafiri wa Kikureshi na ukaufungua mji wa Makkah."
"Na ukaona watu wengi wanaingia kwenye Dini ya Mwenyezi Mungu makundi kwa makundi."
"Yatakapotokea hayo, jitayarishe kukutana na Mola wako kwa kumtakasa na kumhimidi na kumuomba msamaha kwa wingi. Kwani yeye ni mwingi wa kuwakubalia toba wenye kumsabihi na kumuomba msamaha, kwa kuwasamehe na kuwarehemu."
[An Nasri: 1-3]
MTUME WA HURUMA:
Nabii wetu Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- ni Nabii wa huruma, huruma haikutengana naye katika historia yake yote, na katika hatua zake zote za kimaisha, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu.
"Na hatukukutimiliza,ewe Mtume, isipokuwa ni rehema kwa watu wote. Mwenye kukuamini atakuwa mwema na ataokoka, na asiyeamini atapita patupu na atapata hasara."
[Al Anbiyaai: 107].
Na miongoni mwa huruma yake Rehema na Amani ziwe juu yake nikuwa yeye alikuwa na pupa kubwa ya kutaka watu waongoke, na kuwatoa katika giza la ukafiri na ujinga na upotofu, kuwaleta katika mwangaza wa imani na elimu na uongofu, pindi walipokataa kumuamini watu wake alikaribia kuiangamiza nafsi yake kwa huzuni na masikitiko kwa kutoamini kwao, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Huenda wewe, ewe Mtume, ukajiangamiza nafsi yako kwa majonzi na masikitiko baada ya watu wako kukuepuka na kukupa mgongo, iwapo hawataiamini hii Qur’ani na kuifuata kivitendo."
[Kahfu: 6]
Na vile vile inaonekana wazi maana ya huruma yake kwa pupa yake kwa waumini na upole wake, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Hakika amekufikieni Mtume aliye jinsi moja na nyinyi, yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni na anakuhangaikieni, na kwa walioamini ni mpole na mwenye huruma."
[Al- taubah 128]
Na katika pupa ya kuifanya dini kuwa nyepesi na kutoulazimisha umma wake kwa mambo yanayowataabisha, na wala hawawezi kuyatekeleza, Alisema Rehema na Amani ziwe juu yake: "Fanyeni mambo kuwa mepesi na wala msiyafanye kuwa magumu, na wapeni watu habari njema na wala msiwakimbize" Kaipokea Bukhari na Muslim.
Na hakika imejaa nafsi ya Mtume mkarimu kwa huruma, alikuwa ni mtu mwenye huruma sana kuliko watu wote kwa wanawake na watoto, amesema mmoja wa maswahaba, naye ni Anasi bin Maliki -Radhi za Mwenyezi Mungu: "Sikuwahi kuona mtu mwenye huruma kubwa kwa familia kama Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na Amani ziwe juu yake" Kaipokea Muslim.
Haikuishia huruma yake Rehema na Amani ziwe juu yake kwa binadamu pekee, bali ilivuka na kufika hata kwa wanyama, akawahimiza watu kuwafanyia wema wanyama na akatahadharisha kuwaudhi, na akawabainishia wanafunzi wake kuwa mwanamke mmoja malaya alimnywesha maji mbwa, Mwenyezi Mungu akamsamehe mwanamke huyo na akamuingiza peponi, nakuwa mwanamke mwingine aliingia motoni kwakuwa alimfunga paka na akawa hakumlisha mpaka akafa.
Ujumbe wake una wahusu watu wote:
Walikuwa Manabii na Mitume waliotangulia -Sala na salamu ziwafikie- wakitumwa kwa watu wao maalumu, ama Nabii Muhammadi -Rehema na Amani ziwe juu yake- ujumbe wake ni wa jumla kwa watu wote katika kila zama na mahali.
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na hatukukutuma isipokuwa kwa watu wote uwe mbashiri na muonyaji"
[Suratu Sabai: 28].
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
{Sema: Enyi watu! Hakika mimi ni Mtume kwenu nyinyi nyote} ((259)).
[Al A'araf: 158].
Amesema Mtume rehema na Amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake:
"Na alikuwa mtume akitumwa kwa watu wake maalumu, na nimetumwa mimi kwa watu wote"
Imepokelewa na Al-Bukhaariy
Ni wajibu kwa kila mwanadamu tangu kutumwa kwake Rehema na Amani ziwe juu yake na katika zama hizi mpaka siku ya kiyama, kumfuata yeye na kuyakubali yale aliyokuja nayo, na kuingia katika dini yake, kwani Mwenyezi Mungu amekamilisha jumbe zote za mbinguni kupitia yeye, na akawajibisha kumtii; atakayemtii basi atapata furaha duniani, na ataingia peponi katika akhera, na atakayemuasi atapata tabu duniani, na ataingia motoni huko akhera, Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Yeyote atakayefuata muongozo wangu basi hatopotea na wala hatopata tabu"
"Na atakaye jiepusha na mawaidha yangu, basi kwa yakini atapata maisha yenye dhiki, na siku ya Kiyama tutamfufua hali ya kuwa kipofu".
[Twaha: 123-124]
Muongozo wake Mtume Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake nyumbani kwake pamoja na familia yake.
Nyumba ya mtu ndiyo mahala pakuonekana wazi uzuri wake na tabia zake, na ukamilifu wa adabu yake, na uzuri wa muamala wake, mtu anapokuwa na mke wake na watoto wake na wafanya kazi wake basi hapo hutoa maamuzi kulingana na huluka yake bila kulazimishwa.
Na mwenye kuchunguza hali ya Nabii wa umma wa kiislamu na kiongozi wake na mwalimu wake -Rehema na Amani ziwe juu yake- nyumbani kwake, ataona kuwa yeye katoa mifano mizuri sana ya namna ambavyo mwanaume mwenye busara anatakiwa kuwa nyumbani kwake pamoja na mke wake na watoto wake.
Aliambiwa Aisha mke wa Mtume -Radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- Ni nini alikuwa akifanya Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake nyumbani kwake? Akasema:
"Alikuwa mara nyingi katika shughuli za familia yake -Aisha anakusudia alikuwa akitoa huduma kwa familia yake- muda wa swala unapofika anatoka kwenda kuswali"
Imepokelewa na Imamu Muslim
Na alikuwa Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake ni mtu bora kuliko wote kwa familia yake na wake zake, na anatoa picha ya kustaajabisha katika uzuri wa kuishi na familia, na kuwa mpole, na kujua matakwa ya hisia za nafsi za mke wake, na akivuta hisia za namna ya kuweza kuleta furaha kwake na kumfanya awe na amani, anasema Aisha -Radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake:
"Hakika siku moja nilimuona Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake katika mlango wa chumba changu, na wahabeshi wakicheza msikitini, na Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake akinificha kwa nguo yake, nikitazama michezo yao"
Ameipokea Bukhari na Muslim.
Na alikuwa Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake akiwapenda watoto wake wa kike na akiwapa heshima, na alikuwa anapoingia binti yake Fatma anasimama na kumbusu na anamkalisha alipokaa yeye, na alikuwa akiwatembelea watoto wake wa kike ili kujua hali zao.
Na katika usia wake Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake kwa umma wake ni kauli yake:
"Kubalini kuishi na wanawake vizuri"
Ameipokea Bukhari na Muslim.
Na katika tabia zake Mtume rehema na amani za Allah ziwe juu yake:
Alikuwa Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake ni mtu mwenye tabia njema kuliko wote, na mwenye adabu kuliko wote, na alimsifia Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kauli yake:
"Na hakika wewe, ewe Mtume, ni mwenye tabia njema."
[Qalam: Aya ya: 4]
Alikuwa akistareheka kwa ukamilifu wa tabia zake kiasi ambacho hajawahi kukifikia yeyote, kwani yeye amekingwa na tabia za mapungufu, na akakusanya ukamilifu katika kila ubora, na ilikuwa tabia yake ni Qur'ani tukufu, na alikuwa na adabu nayo, na akiwaadabisha watu kwayo, na katika tabia zake Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake:
Nikuwa yeye alikuwa mpole sana kuliko watu wote, na alikuwa muadilifu, na alikuwa akijiheshimu, na mtoaji na mkarimu.
Na alikuwa ni mtu mwenye haya sana kuliko watu wote.
Na alikuwa mnyenyekevu akiitika wito wa mtu yeyote, na alikuwa akikubali zawadi hata kama ni ndogo, na akiilipa kwa wema.
Na alikuwa akitembelea wagonjwa, na akihudhuria majeneza (katika misiba) na akikaa pamoja na mafakiri, na akila pamoja na masikini, alikuwa akiwaheshimu watu wenye vyeo na tabia njema, na akitambua heshima za watu.
Hakuwahi kumjia yeyote mwenye shida isipokuwa alisimama na kwenda naye katika shida yake, na wala hakuwa mkali, wala msusuwavu, na wala hakuwa analipa ubaya kwa ubaya, na alikuwa akisamehe na kufuta, isipokuwa yanapotendwa maharamisho ya Mwenyezi Mungu; basi anakasirika kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na wala si kwa ajili ya nafsi yake.
Na ilikuwa katika tabia zake ni kuanza kumtolea salamu yule anayekutana naye, na alikuwa akikutana na yeyote katika wanafunzi wake anamuanza kwa kumpa mkono.
Na alikuwa akimpa yeyote mwenye kukaa mbele yake sehemu ya uso wake, na usikivu wake na mazungumzo yake, na sehemu ya mazuri yake na maelekezo yake.
Na alikuwa na huruma iliyopitiliza kuliko watu wote, na ni mtu bora kuliko wote, na alikuwa akipenda kuwanufaisha watu kuliko mtu yeyote.
Alikuwa akipenda utani ila alikuwa hasemi ila kweli, mwingi wa kutabasamu, alikuwa akicheka bila kujikohoza, na akifanya mashindano ya kukimbia na wake zake, na akiwafanyia upole.
Alikuwa anakula chakula chochote kinachotengwa, na wala hakirudishi alichokikuta, na wala hakuwahi kutoa dosari ya chakula hata mara moja, akikuta tende anakula, na akikuta nyama anakula, na akikuta mkate wowote anakula bila kubagua, na akikuta halua (pipi) au asali anakula, na akikuta maziwa bila mkate anatosheka nayo, na akikuta tikiti maji au tende mbichi anakula.
Na alikuwa akivaa anachopata, wakati mwingine alikuwa akivaa vazi la sufi, na wakati mwingine alikuwa akivaa kanzu pana, anachokipata katika nguo za halali basi anavaa.
Na alikuwa akipanda kipandwa kinachowezekana kwake, wakati mwingine alipanda Farasi, na wakati mwingine Ngamia, na wakati mwingine nyumbu, na wakati mwingine punda, au anatembea kwa miguu.
Na ulikuwa haupiti muda mwingi bila kuwa katika kazi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, au katika yale ambayo ni ya lazima kwake au kwa watu wa familia yake.
Na mengineyo katika tabia njema na muamala wake mzuri, Rehema na Amani ziwe juu yake.
Hitimisho
Uislamu ni dini tukufu, inahakikisha kupatikana raha na maisha mazuri kwa muislamu na kuwa katika hali nzuri katika dunia, na neema za kudumu na furaha ya milele katika akhera, na vile vile inahakikisha kwa jamii ya kiislamu iliyoshikamana na mafundisho yake, kuwa jamii hiyo itakuwa juu, na kupata maendeleo, na usafi, na kukua, na jamii kuwa kitu kimoja, na salama na amani.
Hongera kwako ewe uliyeongoka na kuingia katika uislamu kwa neema hii tukufu, jifunze itikadi yake na sheria yake, na mafundisho yake na hukumu zake, na tabia zake na adabu zake, na wakati huo ushikamane nazo, na ushikamane nazo katika kila nyanja za maisha yako kwa kadiri uwezavyo, ukifanya hivyo utakuja kuona athari ya uislamu kwako, na ni jinsi gani unavyomfanya mtu kuwa mwema, anavyopata furaha mwenyewe, na wanavyopata furaha pia wale wanaomzunguka, kuanzia wazazi wawili na mke na watoto, na ndugu wa karibu na majirani na marafiki, na kila mwenye kuamiliana na muislamu huyu ambaye Mwenyezi Mungu kamtukuza kwa kuingia katika dini, na kutembea katika njia inayomfikisha kwake.
Na kijitabu hiki ndio mwanzo wa njia yako katika kujifunza hukumu za dini yako, kisha baada ya hapa unatakiwa kujitahidi kuongeza elimu yenye manufaa na matendo mema na kusafisha nafsi yako na kuurekebisha moyo wako, kila inapo ongezeka elimu yako katika uislamu na kuyafanyia kazi yale uliyoyafahamu ndivyo unavyozidi ukaribu wako kwa mola wako mkarimu aliyetakasika na kutukuka, Fanya haraka kuiendea Qur'ani tukufu kwa kujifunza na kuisoma na kuzizingatia Aya zake, na ipitie historia ya Mtume Rehema na Amani ziwe juu yake na mafundisho yake; yeye ndiye kiigizo chako ambacho unatakiwa kuiga kutoka kwake katika maisha yako, na huyu ndiye wa pekee aliyekuamrisha Mwenyezi Mungu kuyakubali yote aliyokuja nayo, ama mtu mwingine asiyekuwa yeye vyovyote vile kitakavyofikia cheo chake basi maneno yake hukubaliwa baadhi yale yaliyoafikiana na Qur'ani na mafundisho ya Mtume na yanakataliwa yale yaliyokwenda kinyume na hivyo, na Ole wako! Jitahadhari na mijadala katika dini, na epukana na ubishi na kutofautiana na watu na kuzozana na ndugu zako waislamu.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu kwetu sisi na kwako pia taufiki na kudumu katika dini hii mpaka tutakapokutana naye akiwa radhi nasi, na kila sifa njema zinamstahiki Mwenyezi Mungu Mola mlezi wa walimwengu wote, na sala na salamu ziwe juu ya Nabii wetu Muhammadi na juu ya familia yake na maswahaba zake wote, na yeyote atakayemfuata mpaka siku ya malipo.