المختصر المفيد للمسلم الجديد
الكتاب يعرض مبادئ الدين الإسلامي بشكل مختصر وواضح، يتناول أساسيات العقيدة الإسلامية، وأركان الإسلام والإيمان، والعبادات المفروضة والمنفولة كالصلاة والصيام والزكاة والحج. مع التأكيد على أهمية القرآن الكريم كمصدر إرشادي أساسي، ويوضح دور النبي محمد ﷺ كرسول الرحمة والهداية للعالمين.
Muhutasari wenye faida kwa Muislamu mpya.
Muandaaji
Muhammad Al-shihriy
2020-1441
Kwa Jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu
Utangulizi
Hakika sifa zote njema anastahiki Mwenyezi Mungu, tuna msifu na tunamuomba msaada na tunamuomba msamaha, na tuna jilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shari za nafsi zetu, mwenye kuongozwa na Mwenyezi Mungu hakuna wa kumpoteza, na mwenye kupotezwa na Mwenyezi Mungu hakuna wa kumuongoza, na nina shuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika, na nina shuhudia kuwa Muhammad ni mja wake na ni Mtume wake.
Baada ya hayo;
Amewatukuza Mwenyezi Mungu wanadamu na akawafanya kuwa bora zaidi kuliko viumbe wake wengi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hakika tumewatukuza wanadamu" [Al Israai: 70]. Na akauzidishia Umma huu utukufu akawatumia mtume bora zaidi katika mitume wake Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake- na akawateremshia juu yao kitabu chake bora zaidi miongoni mwa vitabu vyake, ambacho ni Qur'ani tukufu, na akawaridhia dini tukufu zaidi aliyoiweka nayo ni Uislamu, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Nyinyi mmekuwa umma bora kuliko umma zote zilizotolewa watu, mnaamrisha mema na mnakataza maovu, na mnamuamini Mwenyezi Mungu, na lau kama wale waliopewa kitabu wangeamini kama walivyo amrishwa ingelikuwa bora kwao, lakini miongoni mwao wapo walioamini na wengi wao wametoka katika kumtii Mwenyezi Mungu." [Al-Imran: 110]. Na katika neema kubwa za Mwenyezi Mungu Mtukufu alizompa mwanadamu ni kumpa muongozo wa kuelekea katika Uislamu na kudumu katika Uislamu, na kuzifanyia kazi hukumu zake na sheria zake, na katika kitabu hiki chenye umbile dogo na chenye madhumuni makubwa anajifunza muislamu mpya mambo ambayo hapasi kutoyajua mwanzoni mwa Uislamu wake, kwa njia nyepesi ambayo inamuwekea wazi mambo muhimu katika dini hii tukufu mpaka akishayafahamu na akayafanyia kazi kama inavyotakikana, huanza kutafuta elimu na kuitafuta zaidi ili uongezeke utambuzi wake wa kumjua Mola wake Mtukufu, na Mtume wake Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake-, na dini yake ya Uislamu, na amuabudu Mwenyezi Mungu kwa ujuzi na elimu, na utulie moyo wake na iongezeke imani yake kwa kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kumuabudu, na kufuata sunna za Mtume wake Muhammad -rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.
Na ninamuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu atie baraka kila neno katika kitabu hiki, na aunufaishe nacho Uislamu na waislamu, na akifanye kitabu hiki kiwe ni kwa ajili ya kutafuta radhi zake Mtukufu, na ajaalie malipo yake ni kwa ajili ya waislamu wote walio hai na walio kufa.
Na rehema na amani za Allah ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad na ali zake na Maswahaba zake.
Muhammad bin Shaiba Al-Shihriy
2/11/1441:H
Mola wangu Mlezi ni Mwenyezi Mungu.
Amesema Allah Mtukufu: "Enyi watu muabuduni Mola wenu Mlezi ambaye amekuumbeni na amewaumba walio kabla yenu ili mpate kuwa wachamungu" [Al Baqara: 21].
Amesema Allah Mtukufu: "Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Yeye" [Al-hashir: 22].
Amesema Allah Mtukufu: "Hakuna kitu mfano wake, naye ni Mwenye kusikia Mwenye kuona". [Ash-shura: 11].
Mwenyezi Mungu ndiye Mola wangu na ndiye Mola wa kila kitu, mmiliki, muumba, mwenye kuruzuku, mpangiliaji wa kila jambo.
Naye peke yake ndiye mwenye haki ya kuabudiwa hakuna muumba mwingine wala mola asiyekuwa yeye.
Ana majina mazuri na sifa za hali ya juu amezithibitisha sifa hizo yeye mwenyewe, na akamthibitishia sifa hizo Mtume wake -Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- sifa hizo zimefikia upeo wa ukamilifu na uzuri, hakuna chochote mfano wake naye ni mwenye kusikia na mwenye kuona.
Na katika majina yake mazuri:
Mgawa riziki, mwingi wa rehema, muweza, Mmiliki, mwenye kusikia, Amani, mwenye kuona, Msimamizi, Muumbaji, Mpole, mwenye kutosheleza, Msamehevu.
Al-Razzaq: Mwenye kudhamini riziki za waja ambazo kwa riziki hizo ndiyo unapatikana uhai wa mioyo yao na miili yao.
Al-Rahmaan: Mwenye huruma ya hali ya juu, na yenye kuenea viumbe vyake vyote.
Al-Qadiir: Mwenye uwezo uliokamilika, hashindwi wala hachoki.
Al-Maliki: Yeye ndiye mwenye kusifika na sifa ya utukufu na ushindi na upangiliaji wa mambo, mwenye kumiliki mambo yote na kuyaendesha atakavyo.
Al-Samiiu: Ambaye ana diriki kuvisikia vyote vyenye kusikika kwa siri na kwa wazi.
Al-Salaam: Aliye salimika na kila upungufu ubaya na aibu.
Al-Baswiir: ambaye uoni wake umezunguka kila kitu hata kikiwa cha ndani mno na kidogo, mwenye uoni wa vitu, mwenye kuvijua na mwenye kuviona undani wake.
Al-Wakiil: Mwenye kusimamia riziki za waja wake, na kuwasimamia masilahi yao, na mwenye kuwapenda vipenzi vyake na akawafanyia wepesi na akawatosheleza mambo mbalimbali.
Al-Khaaliq: Mletaji wa vitu na mgunduzi wake kwa namna ambayo hakuna mfano wake kabla yake.
Al-Latwiif: Ambaye anawakirimu waja wake na kuwarehemu na kuwapa wanachomuomba.
Al-Kaafi: Ambaye huwatosheleza waja wake mambo yote wanayoyahitajia kwake.
Al-Ghafuur: Ambaye anawakinga waja wake na shari ya madhambi yao, na wala hawaadhibu kwa madhambi hayo.
Anatafakari muislamu maajabu ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu na namna alivyoufanya kuwa mwepesi, na miongoni mwa ajabu ni kutilia umuhimu viumbe kwa udogo wake, kwa kupupia kuwalisha na kuwachunga mpaka waweze kujitegemea wenyewe, basi kutakasika na machafu ni kwake yeye muumba wa viumbe na mwenye kuvihurumia, na katika kuvionea huruma viumbe, ameviandalia vitu vyenye kuvisaidia na vyenye kutengeneza hali zake licha yakuwa viumbe hivyo vina madhaifu makubwa.
Mtume wangu Muhammad -Rehema na amani za Allah ziwe juu yake-
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika amekufikieni Mtume kutokana na nyinyi wenyewe, yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni na anakuhangaikieni sana, na kwa walioamini ni mpole na mwenye huruma." [At-Tauba: 128]
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na hatukukutuma, ewe Mtume, isipokuwa uwe ni rehema kwa walimwengu wote." [Al Anbiyaai: 107].
Muhammad - Rehema na amani za Allah ziwe juu yake- ni rehema iliyotolewa zawadi.
Naye ni Muhammad mtoto wa Abdillah -rehema na amani za Allah ziwe juu yake- mwisho wa manabii na mitume, alimtuma Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa dini ya Uislamu kwa watu wote, ili awajulishe mambo ya kheri na mambo makubwa katika kheri hiyo ni Tauhidi, na awakataze mambo ya shari, na jambo kubwa la shari ni ushirikina.
Na ni wajibu kumtii Mtume katika yale aliyo yaamrisha, na kumsadikisha katika yale aliyo yaeleza, na kujiepusha na yale aliyo yakataza na kuyakemea, na asiabudiwe Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa namna alivyo elekeza.
Ujumbe wake na ujumbe wa manabii wote waliokuwa kabla yake ni kulingania katika kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake hana mshirika wake.
Na miongoni mwa sifa zake -rehema na amani za Allah ziwe juu yake-:
Ukweli, Huruma, Upole, Subira, Ushujaa, Ukarimu,Tabia njema, Uadilifu, Unyenyekevu, Usamehevu.
Qur'ani tukufu ni maneno ya Mola wangu Mlezi
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Enyi watu, kwa hakika umekuja kwenu ushahidi kutoka kwa Mola wenu, na tumewateremshia Qur’ani ikiwa ni uongofu na ni nuru yenye kufafanua mambo waziwazi." [An Nisaai: 174].
Qur'ani tukufu ni maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ambayo ameyateremsha kwa Mtume wake Muhammad- rehema na amani za Allah ziwe juu yake- ili awatoe watu kutoka katika giza kuwapeleka katika nuru na kuwaongoza katika njia iliyonyooka.
Yeyote atakayeisoma atapata malipo makubwa, na atakayeufanyia kazi muongozo wake basi atakuwa amefuata njia iliyo sawa.
Najifunza nguzo za Uislamu
Amesema Mtume rehema na amani za Allah ziwe juu yake: "Uislamu umejengwa juu ya mambo matano: Kushuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mungu mmoja na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na kusimamisha swala na kutoa zaka na kufunga Ramadhani na kuhiji katika nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu".
Nguzo za Uislamu ni ibada inayomlazimu kila muislamu, na wala hauwi sawa Uislamu wa mtu isipokuwa kwa kuamini uwajibu wake na kutekeleza wajibu hizo zote, kwa sababu Uislamu umejengwa juu ya misingi hiyo, na ndiyo maana imeitwa nguzo za Uislamu.
Na nguzo hizo ni:
Nguzo ya kwanza: Ni kushuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake na Muhammad ni mtume wa Mwenyezi Mungu.
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi tambua ya kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu" [Surat Muhammad: 19]
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika amekufikieni Mtume anayetokana na nyinyi wenyewe, yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni na anakuhangaikieni sana, na kwa walioamini ni mpole na mwenye huruma". [At-Tauba:128]
Maana ya kushuhudia kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu: Yaani hakuna muabudiwa wa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu.
Na maana ya kushuhudia kuwa "Muhammad ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu": Ni kumtii Mtume katika yale aliyo yaamrisha, na kumsadikisha katika yale aliyo yaeleza, na kujiepusha na yale aliyo yakataza na kuyakemea, na asiabudiwe Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa namna alivyo elekeza.
Nguzo ya pili: Kusimamisha swala.
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na simamisheni swala" [Al-Baqara: 110].
Kusimamisha swala kunakuwa kwa kutekeleza kwa namna ambayo ameelekeza Mwenyezi Mungu Mtukufu na akatufundisha Mtume wake -rehema na amani za Allah ziwe juu yake-.
Nguzo ya tatu: Kutoa zaka
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na toeni zaka" [Al-Baqara:110].
Ameamrisha Mwenyezi Mungu Zaka ili kuupima ukweli wa imani ya muislamu, na kumshukuru Mola wake kwa kumneemesha neema ya mali, na kuwasaidia masikini na wenye kuhitajia.
Na kutoa zaka kunakuwa kwa kuwapa watu wenye kustahiki.
Nayo ni haki ya wajibu katika mali itakapokuwa imefikia kiwango maalumu, hupewa aina nane alizozitaja Mwenyezi Mungu katika Qur'ani tukufu, miongoni mwao ni mafukara na masikini.
Na katika kuitekeleza kwake kuna kusifika kwa sifa ya huruma na upole, na kusafisha tabia za muislamu na mali yake, na kuziridhisha nafsi za mafukara na masikini na kuyapa nguvu mafungamano ya kimapenzi na udugu kati ya mtu mmoja mmoja katika jamii ya kiislamu, na kwa hivyo muislamu mwema huitoa zaka kwa moyo safi na kufurahia utekelezaji wake, kwa sababu kutoa zaka kunafurahisha watu wengine.
Na kiwango cha zaka ya mali ni 2.5% katika mali iliyolimbikizwa miongoni mwazo ni Dhahabu na fedha, na pesa tasilim na bidhaa za biashara zilizo andaliwa kwa ajili ya kuuza na kununua ili kupata faida; zinapofikia thamani yake kiwango maalumu na zikazungukiwa na mwaka mzima.
Kama ambavyo ni wajibu kutoa zaka kwa mwenye kumiliki idadi maalumu ya wanyama wafugwao (Ngamia, Ngo'mbe, na Mbuzi) ikiwa wanakula majani ya malishoni mwaka mzima pasina kulishwa na mwenye wanyama.
Na hivyo hivyo ni wajibu kutoa zaka kwa kinachotoka katika ardhi miongoni mwa nafaka na matunda, madini na hazina ikiwa zitafikia kiwango maalumu.
Nguzo ya Nne: Kufunga Ramadhani
Amesema Allah Mtukufu: "Enyi mlioamini Mmefaradhishiwa kufunga, kama Walivyofaradhishiwa wale waliokuwa kabla yenu, ili mpate kumcha Mwenyezi Mungu}. [Al-Baqara:110].
Mwezi mtukufu wa Ramadhani ni mwezi wa tisa katika mwaka wa mpangilio wa kalenda ya Hijria (Tangu kuhama Mtume) nao ni mwezi mtukufu kwa waislamu, na una nafasi yake maalumu kuliko miezi mingine katika mwaka, na kuufunga mwezi huo ni moja ya nguzo tano za Uislamu.
Kufunga mwezi wa Ramadhani: Ni kumuabudu Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kujizuia na kula na kunywa na kufanya tendo la ndoa, na vyote vyenye kufunguza, kwanzia kuchomoza jua mpaka kuzama jua katika siku zote za mwezi wa Ramadhani wenye baraka.
Nguzo ya tano: Kuhiji nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na Mwenyezi Mungu amewawajibishia watu wafanye hija katika nyumba hiyo tukufu kwa mwenye kuweza kufunga safari ya kwenda huko." [Al-Imran: 97].
Hija inakuwa kwa mwenye uwezo wa kufunga safari kwenda huko mara moja katika umri wake, nako ni kukusudia nyumba tukufu na viwanja vitukufu vya Makkah kwa ajili ya kutekeleza ibada maalumu katika wakati maalumu, na hakika alifanya hija Mtume -rehema na amani za Allah ziwe juu yake- na pia Mitume wengine walifanya hija kabla yake, na akamuamrisha Mwenyezi Mungu ibrahim -Amani iwe juu yake- awaite watu kuja kutekeleza ibada ya hija kama alivyolieleza hilo Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Qur'an tukufu akasema: "Na tukamwambia utangaze kwa watu habari za hija watakujia wengine kwa miguu na wengine juu ya kila mnyama aliyekonda kwa uchovu wa safari watakujia kutoka kila njia ya mbali" [Al Haji: 27].
Najifunza nguzo za imani
Aliulizwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuhusu Imani: "Ni kumuamini Mwenyezi Mungu na Malaika wake na vitabu vyake na mitume wake na siku ya mwisho na kuamini Kadari kheri yake na shari yake."
Nguzo za imani ni ibada za moyoni ambazo zinamlazimu kila muislamu, na haufai Uislamu wa mtu isipokuwa kwa kuziamini nguzo hizo, ndio maana zikaitwa nguzo za imani. Na tofauti kati yake na kati ya nguzo za Uislamu, ni kuwa nguzo za Uislamu ni matendo ya wazi wazi anayoyatekeleza mwanadamu kwa viungo vyake kama vile kutamka shahada mbili na swala na zaka, na nguzo za imani ni matendo ya moyoni anayoyafanya mwanadamu kwa moyo wake mfano: Kumuamini Mwenyezi Mungu na vitabu vyake na mitume wake.
Ufahamu wa Imani na maana yake: Ni kumsadikisha Mwenyezi Mungu moyoni bila kuwa na shaka, na Malaika wake na vitabu vyake, na mitume wake na siku ya mwisho, na kuamini Kadari kheri yake na shari, na kufuata kila alilokuja nalo Mtume- rehema na amani za Allah ziwe juu yake- na kuyatekeleza kwa kutamka kwa ulimi, kama kusema: (Laa ilaaha illa llahu) hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu mmoja tu, na kusoma Qur'ani, na kuleta tas-bihi, na kuleta tahlili, na kumsifu Mwenyezi Mungu.
Na kutenda kwa viungo vya nje: Kama vile swala na kuhiji, na kufunga n.k. na viungo vya ndani vyenye kuhusiana na moyo kama kumpenda Mwenyezi Mungu na kunyenyekea, na kutegemea kwake na kumtakasia ibada yeye.
Na wanaielezea wabobezi kwa ufupi kuwa Imani ni kuitakidi moyoni, na kutamka kwa ulimi na kutenda kwa viungo, nayo inazidi kwa kutii na inapungua kwa maasi.
Nguzo ya kwanza: Kumuamini Mwenyezi Mungu
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika waumini wa kweli ni wale walio mwamini Mwenyezi Mungu" [Al-Nuur: 62].
Kumuamini Mwenyezi Mungu kunapelekea kupwekesha katika uumbaji wake na uungu wake na majina yake na sifa zake, na kunajumuisha mambo yafuatayo:
1- Kuamini uwepo wake Aliyetakasika na kutukuka.
2- Kuamini uumbaji wake Aliyetakasika na kutukuka, na kuwa yeye ni mmiliki wa kila kitu, na muumba wake na mwenye kuruzuku na mwendeshaji wa mambo yake.
3- Kuamini Uungu wake - Mtukufu - na kuwa yeye ndiye anayestahiki kuabudiwa peke yake hana mshirika wake kwa chochote, ibada hizo ni: kama vile swala, na dua, na kuweka nadhiri, na kutaka msaada, na ibada zingine zote.
Kuamini majina yake mazuri na sifa zake za hali ya juu ambazo amezithibitisha yeye mwenyewe au Mtume wake Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake- na akapinga sifa alizozipinga katika nafsi yake au kazipinga Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- miongoni mwa majina na sifa, na kuwa majina yake na sifa zake zimefika ukomo wa ukamilifu na uzuri, na kuwa yeye hakuna chenye kufanana naye, naye ni mwenye kusikia na kuona.
Nguzo ya pili: Kuwaamini Malaika
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu muumba wa mbingu na Ardhi, aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbili mbili na tatu tatu na nne nne huzidisha katika kuumba apendavyo, bila shaka Mwenyezi Mungu juu ya kila kitu ni muweza." [Fatwiri:1]
Tunaamini kuwa Malaika ni viumbe wasiyoonekana, na wao ni waja wa Mwenyezi Mungu amewaumba kutokana na nuru, na akawafanya ni wenye kunyenyekea na kujidhalilisha kwake.
Na hao Malaika ni viumbe wakubwa hakuna awezaye kudhibiti nguvu zao na idadi yao isipokuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kila mmoja katika wao ana sifa na majina na kazi zao ambazo amezifanya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwa maalumu kwao tu, na miongoni mwao ni Jibrili- amani iwe juu yake- aliyewakilishwa kwa ajili ya wahyi anateremka nao kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwenda kwa mitume wake.
Nguzo ya tatu: Kuamini vitabu
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Semeni enyi waumini: Tumemuamini Mwenyezi Mungu na yale tuliyoteremshiwa sisi, na yaliyoteremshwa kwa Ibrahim na Ismail na Is-haka na Yaakub, na kizazi chake, na yale aliyopewa Mussa na Issa na Manabii kutoka kwa Mola wao Mlezi; hatutofautishi kati ya yeyote miongoni mwao, na sisi tumenyeyekea kwake". [Baqara: 136].
Kusadikisha kusikokuwa na shaka kwamba vitabu vyote vya mbinguni ni maneno ya Mwenyezi Mungu.
Na vitabu hivyo vimeteremshwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu- Mwenye utukufu- kuja kwa Mitume wake kwenda kwa waja wake kwa haki iliyo wazi.
Na kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kumtuma kwake Mtume Muhammad- rehema na amani ziwe juu yake- kwa watu wote, amefuta kupitia sheria yake sheria zote zilizotangulia, na akaifanya Qur'ani tukufu ndiyo yenye kuvitawa na kuvifuta vitabu vyote vya mbinguni, na ameahidi Mwenyezi Mungu kuihifadhi Qur'ani tukufu kutokana na kubadilishwa au kugeuzwa, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika sisi tumeiteremsha Qur’ani na hakika sisi ndio tutakao ilinda." [Hijri: 9]. Kwa sababu Qur'ani tukufu ndicho kitabu cha mwisho cha Mwenyezi Mungu kimeletwa kwa wanadamu, na Mtume wake Muhammad - rehema na amani ziwe juu yake - ndiyo wa mwisho katika Manabii, na dini ya Uislamu ndiyo dini ambayo ameiridhia Mwenyezi Mungu kwa wanadamu mpaka siku ya Kiyama, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika dini inayo kubaliwa kwa Mwenyezi Mungu ni Uislamu" [Al-Imran: 19].
Na vitabu vya mbinguni ambavyo amevitaja Mwenyezi Mungu katika kitabu chake ni:
Qur'ani tukufu: Aliiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake-.
Taurati: Aliiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake Mussa- rehema na amani ziwe juu yake.
Injili: Aliiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake Issa- rehema na amani ziwe juu yake.
Zaburi: Aliiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake Daudi-rehema na amani ziwe juu yake
Nyaraka za Ibrahim: Aliziteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake Ibrahim -rehema na amani ziwe juu yake
Nguzo ya nne: Kuwaamini Mitume
Amesema Allah Mtukufu: "Na kwa hakika katika kila Umma tuliutumia Mtume, kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Shetani" [An Nahli: 36].
Ni kusadikisha kusikokuwa na shaka kwamba Mwenyezi Mungu ametuma katika kila Umma Mtume, anawalingania watu kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake hana mshirika wake, na kupinga kila kinachoabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Na kuwa Mitume wote hao ni wanadamu wanaume na ni waja wa Mwenyezi Mungu, nakuwa wao ni wakweli na wenye kusadikishwa, ni wachamungu na ni waaminifu, ni waongofu walioongoka, aliwatia nguvu Mwenyezi Mungu kwa miujiza yenye kujulisha ukweli wao, na hakika wao walifikisha yote aliyowatuma Mwenyezi Mungu, na kuwa wao wote walikuwa kwenye haki na muongozo ulio wazi.
Na bila shaka ulinganiaji wao ulikuwa mmoja kwanzia wa mwanzo wao mpaka wa mwisho wao katika msingi wa dini, nao ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu -Aliyetakasika na Kutukuka- katika kumuabudu na kutomshirikisha.
Nguzo ya Tano: Kuamini siku ya mwisho
Amesema Allah Mtukufu: "Mwenyezi Mungu, Ambaye hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila yeye, Ndiye atakaye wakusanya nyinyi siku ya Kiyama isiyokuwa na shaka, kwa kuhesabiwa na kulipwa. Na hakuna yeyote mkweli zaidi wa maneno anayoyatolea habari kuliko Mwenyezi Mungu". [An-Nisaa 87].
Ni kusadikisha kusikokuwa na shaka kila kinachohusiana na siku ya mwisho miongoni mwa yale aliyoyaeleza Mola wetu Mtukufu katika kitabu chake kitukufu au aliyotusimulia Mtume Muhammad -rehema na amani ziwe juu yake- kama kufa mwanadamu, na kufufuliwa kukusanywa, na uombezi, na mizani, na hesabu, pepo, na moto, na mengine yasiyokuwa hayo yenye kuhusiana na siku ya mwisho.
Nguzo ya sita: Kuamini Kadari kheri zake na shari zake
Amesema Allah Mtukufu: "Hakika sisi kila kitu tumekiumba kwa kipimo chake mahsusi". [Qamar: 49].
Kuamini kuwa kila jambo linalotokea kwa viumbe miongoni mwa matukio ya duniani, basi hutokea kwa kujua Mwenyezi Mungu, na amelikadiria- Aliyetakasika na kutukuka- na upangiliaji wake yeye peke yake hana mshirika wake, na kuwa makadirio haya yameandikwa kabla ya kuumbwa mwanadamu, na hakika mwanadamu ana matashi, na yeye ndiye mfanyaji wa vitendo vyake kiuhakika, lakini vyote hivyo havitoki nje ya ujuzi wa Mwenyezi Mungu matashi yake na kupenda kwake.
Hivyo, kuamini Kadari kunakuwa katika ngazi Nne:
Ngazi ya kwanza: Kuamini elimu ya Mwenyezi Mungu ilioenea katika kila kitu
Ngazi ya pili: Kuamini aliyoyaandika Mwenyezi Mungu kwa kila lililopo mpaka kusimama Kiyama.
Ngazi ya tatu: Kuamini matashi ya Mwenyezi Mungu yenye kutekelezwa na uwezo wake uliotimia, basi lolote alitakalo huwa na asilolitaka haliwi.
Ngazi ya Nne: Kuamini kuwa Mwenyezi Mungu ni muumba wa kila kitu, hana mshirika wake katika kuumba kwake.
Ninajifunza Udhu
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwa hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wenye kutubia na huwapenda wenye kujitwaharisha" [Baqara: 22].
Amesema Mtume rehema na amani za Allah ziwe juu yake: "Atakayetawadha mfano wa udhu wangu huu, kisha akasali rakaa ambazo hatokuwa na mawazo ya nje ya swala, Mwenyezi Mungu atamsamehe madhambi yake yaliyotangulia".
Na miongoni mwa utukufu wa swala ni kuwa Mwenyezi Mungu ameweka sheria ya kujisafisha kabla yake, na akafanya twahara (usafi) kuwa ni sharti la kukubalika swala, na twahara ndiyo ufunguo wa swala, na kuvuta hisia ya utukufu wake kunaufanya moyo uwe na shauku ya kutekeleza swala. Amesema Mtume rehema na amani za Allah ziwe juu yake: "Twahara (usafi) ni nusu ya imani, na swala ni nuru"
Na amesema Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-: "Atakayetawadha na akaufanya vizuri udhu, hutoka madhambi yake mwilini mwake".
Basi mja huenda kwa Mola wake hali yakuwa ni mwenye kujisafisha usafi wa kihisia (unaoonekana) kwa kutawadha, na usafi wa kimaana (usioonekana, kama usafi wa moyo) kwa kutekeleza ibada hizi, kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa kufuata muongozo wa Mtume -rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.
Yanayopaswa kufanywa ukiwa na Udhu
1- Swala ya aina yoyote sawa iwe ya Faradhi au iwe ya Sunna.
2- Kutufu Al-Kaaba (nyumba tukufu)
3- Kushika msahafu
Nina tawadha na ninaoga kwa kutumia maji safi
Maji safi ni kila maji yaliyoteremka toka mbinguni, au yakachimbuka kutoka ardhini na yakabakia katika asili ya umbile lake, na hayakubadilika moja kati ya sifa zake tatu, nazo ni, Rangi, Ladha, na Harufu, hayakubadilika kwa kitu chenye kuondosha usafi wa maji.
Ninajifunza Udhu
Hatua ya kwanza: Kutia nia, na mahala pake ni moyoni, na maana ya nia: Ni kuazimia moyoni kufanya ibada kwa kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Hatua ya pili: Kuosha viganja viwili:
Hatua ya tatu: Kusukutua.
Kusukutua ni Kuingiza maji mdomoni na kuyazungusha humo, kisha kuyatoa.
Hatua ya Nne: Kupandisha maji puani
Kupandisha maji puani: Ni kuyavuta maji kwa pumzi mpaka kwenye kilele cha pua.
Kisha kuyatoa: Nako ni kutoa kila kilichoko ndani ya pua miongoni mwa kamasi na vinginevyo kwa kusukuma pumzi.
Hatua ya tano: Kuosha uso.
Mipaka ya uso:
Uso: Ni ule unaoonekana wakati wa kukutana.
Na mpaka wake kwa upana ni kuanzia sikio mpaka sikio lingine.
Na mpaka wake kwa urefu: Ni kilichoko kati ya maoteo ya nywele za kichwa zilizozoeleka mpaka mwisho wa kidevu.
Unakusanya uoshaji wa uso kila kilicho katika uso kuanzia nywele hafifu, na vile vile weupe uliopo kati ya sikio na ndevu.
Na weupe ni ule uliopo kati ya nywele na nyama ya sikio.
Na nywele ambazo ziko juu ya mfupa uliotokeza, unaoelekeana na tundu la sikio lenye kupita mpaka ndani ya kichwa na kutumbukia mpaka kigingi cha sikio.
Na vile vile kunakusanya kuosha uso kila kilichoko wazi kuanzia nywele nyingi za ndevu na zilizo shuka katika ndevu.
Hatua ya sita: Kuosha mikono miwili kwa kuanzia ncha za vidole vya mikono miwili mpaka kwenye fundo mbili.
Na huingia kwenye fundo mbili kuosha mikono miwili iliyofaradhishwa.
Hatua ya saba: Kukipaka maji kichwa kizima pamoja na masikio mawili mara moja .
Ataanza mwanzo wa kichwa chake akienda na mikono yote mpaka kichogoni kisha atairudisha mpaka sehemu aliyoanzia.
Na ataingiza vidole vyake viwili ndani ya masikio yake.
Na akifuatishia kwa vidole gumba juu ya mgongo wa masikio yake, na atapaka hivyo nje ya masikio yake na ndani.
Hatua ya Nane: Kuosha miguu miwili kuanzia vidole vya miguu miwili mpaka kwenye kongo mbili, na huingia kwenye kongo mbili kuosha miguu miwili iliyofaradhishwa.
Kongo mbili ni: Mifupa miwili iliyoota chini ya miundi.
Na udhu huharibika kwa mambo haya yafuatayo:
1- kutoka kitu katika moja ya njia mbili kama mkojo, na haja kubwa, na upepo, na manii, na madhii.
2- Kuondokwa na akili kwa kulala usingizi au kuzimia, au kulewa, au kupatwa na wenda wazimu.
3- kila chenye kulazimisha kuoga kama Janaba, na Hedhi, na Nifasi.
Na mwanadamu akikidhi haja yake anapaswa kuondosha najisi, ima kwa maji safi, na hii ndiyo njia bora zaidi, au pasina kutumia maji safi kwa vitu vinavyoondosha najisi kama mawe na karatasi na vitambaa na mfano wake. na kwa sharti iwe kuondoa huko ni kwa kufuta mara tatu au zaidi kwa kitu chenye kutakasa na kilicho safi na halali kukitumia.
Kufuta juu ya Khofu mbili au soksi mbili
Katika hali ya kuvaa khofu mbili au soksi mbili, basi yawezekana kufuta juu yake pasina kuwa na haja ya kuosha miguu miwili, kwa masharti ambayo ni:
1- Ziwe zimevaliwa baada ya twahara iliyokamilika iliyosababishwa ima na hadathi ndogo au kubwa ambapo ilioshwa katika twahara hiyo miguu miwili.
2- Ziwe khofu au soksi mbili ni twahara na si zenye najisi.
3- Na iwe upakaji ni katika muda uliowekwa kwa ajili hiyo.
4- Na khofu hizo au soksi ziwe ni halali, zisiwe kwa mfano ni za wizi au za kupora.
Khofu mbili: Ni zile zenye kuvaliwa katika mguu, na hutokana na ngozi nyembamba na mfano wake, na mfano wa khofu ni viatu vinavyositiri miguu miwili.
Soksi mbili ni: ni zile ambazo huzivaa mtu mguuni mwake zinazotokana na kitambaa na mfano wake na ndizo zinazojulikana kwa jina la (Shurraab).
Hekima ya kuweka sheria ya kufuta juu ya khofu mbili
Hekima ya kuweka sheria ya kufuta juu ya khofu mbili: Ni kufanya wepesi kwa waislamu, ambao inakuwa kwao ni tabu kuvua khofu na soksi na kuosha hasa miguu miwili katika wakati wa masika na baridi kali na safarini.
Muda wa kupaka:
Mkaazi: (asiye kuwa msafiri) atapaka usiku na mchana (masaa 24)
Na Msafiri: Atafuta siku tatu na usiku wake (masaa 72)
Ataanza kuhesabu muda wa kufuta kuanzia mwanzo wa kufuta khofu mbili au soksi mbili baada ya kupatwa na hadathi.
Sifa za ufutaji juu ya khofu mbili au soksi mbili:
1- Hulowanishwa mikono miwili.
2- Hupitishwa mkono juu ya unyayo kuanzia kwenye vidole mpaka mwanzo wa muundi.
3- Hupakwa unyayo wa kulia kwa kutumia mkono wa kulia na unyayo wa kushoto kwa mkono wa kushoto.
Venye kuharibu ufutaji
1- Vyote vyenye kuwajibisha kuoga
2- Kuisha muda wa kupaka.
Kuoga
Ikitokea kwa mwanaume au mwanamke kitendo cha kujamiiana, au wote wawili yakawatoka manii kwa kutamani wakiwa katika hali ya kulala au kuamka, ni wajibu juu yao kujitwaharisha, na vile vile mwanamke akitwaharika kutoka kwenye Hedhi na Nifasi ni wajibu kwake kuoga kabla ya kuanza kutekeleza swala au kufanya mambo ambayo yanalazimu twahara.
Na sifa ya kuoga ni kama ifutavyo:
Na aueneze muislamu mwili wake wote kwa maji kwa njia yoyote ile, na katika hayo ni kusukutua, na kupandisha maji puani, na ikiwa ataeneza mwili wake kwa maji, itaondoka kwake hadathi kubwa, na itakuwa imetimia twahara yake.
Hutahadharishwa mwenye janaba kufanya mambo yafutayo mpaka aoge:
01- Kuswali:
02- Kutufu Al-Kaaba (nyumba tukufu)
03- Kukaa msikitini, na yafaa kwake kupita tu pasina kukaa.
04- Kushika msahafu.
05- Kusoma Qur'ani
Kutayammam
Ikiwa muislamu hajapata maji ambayo atajitwaharishia au hakuweza kuyatumia maji kutokana na maradhi na mfano wake na akahofia usimpite wakati wa swala basi atatayamamu kwa kutumia udongo.
Na namna yake: Ni apige kwa mikono yake miwili katika udongo mpigo mmoja, kisha atafuta uso wake na juu ya viganja vyake pekee kwa mikono hiyo miwili. Na ni sharti udongo uwe msafi.
Na tayamamu huharibika kwa mambo yafuatayo:
1- Huharibika tayamamu kwa kila chenye kuharibu udhu.
2- Maji yakipatikana, au akaweza kuyatumia kabla ya kuanza ibada aliyotayamamu kwa ajili yake.
Ninajifunza Swala
Mwenyezi Mungu kamfaradhishia muislamu swala tano usiku na mchana nazo ni: Al-fajiri na Adhuhuri na Lasiri na Magharibi na Ishaa. Na idadi ya rakaa za swala ya Al-fajiri ni mbili. Na swala ya Adhuhuri: Ni rakaa nne. Na swala ya Lasiri: Ni nne. Na swala ya Magharibi: Ni tatu. Na swala ya Ishaa: Ni nne.
Najiandaa kwa ajili ya swala
Ukiingia muda wa swala hujitwaharisha muislamu kutokana na hadathi (Uchafu) mdogo na mkubwa, ikiwa kapatwa na hadathi kubwa.
Na hadathi kubwa ni: Kila kinachomlazimisha muislamu kuoga.
Na hadathi kubwa ni: Kila kinachomlazimisha muislamu kutawadha.
Husali muislamu akiwa katika twahara na katika sehemu safi kutokana na najisi, akiwa ameusitiri uchi wake.
Anajipamba muislamu kwa mavazi yanayofaa wakati wa swala na husitiri kwa mavazi hayo mwili wake, na haifai kwa mwanaume wakati wa kuswali aache wazi sehemu yoyote kuanzia sehemu ya kitovuni mpaka magotini.
Ni wajibu kwa mwanamke kuusitiri mwili wake wote ndani ya swala isipokuwa uso na viganja viwili.
Hazungumzi muislamu akiwa katika swala maneno yasiyokuwa maalumu kwa ajili ya swala, na kumsikiliza imamu, na wala asigeuke geuke katika swala yake, na ikiwa atashindwa kuyahifadhi maneno maalumu kwa ajili ya swala, basi atamtaja Mola wake na kumsabbihi mpaka amalize swala.
Ninajifunza Swala
Hatua ya kwanza: Kutia nia kwa ajili ya faradhi ninayotaka kuitekeleza, na mahala pake ni moyoni.
Baada ya kutawadha naelekea Kibla, na ninaswali nikiwa nimesimama ikiwa naweza kufanya hivyo.
Hatua ya pili: Nina inua mikono yangu miwili usawa wa mabega mawili na ninasema (Allahu Ak-baru) huku nikinuia kuingia katika swala.
Hatua ya tatu: Ninasoma dua ya ufunguzi wa swala kama ilivyopokelewa, na katika dua hizo ni kusema: "Sub-haanaka llaahumma wabihamdika, watabaarakasmuka, wa taala jadduka walaa ilaaha ghairuka" -Kutakasika ni kwako ewe Mola Mlezi na kushukuriwa ni kwako, limetukuka jina lako, na umetukuka utukufu wako na hakuna Mola mwingine zaidi yako-.
Hatua ya Nne: Ninajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shetani aliye laaniwa na ninasema: (Audhubillaahi minash shaitwanir rajiim) Ninajikinga kwa Allah kutokana na shetani aliye laaniwa.
Hatua ya tano: Ninasoma suratul faatiha katika kila rakaa, nayo ni: Bismillahir Rahmanir Rahiim (1) Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu Al-hamdulillaahi Rabbil aalamiin (2) Sifa zote njema anastahiki Mola Mlezi wa viumbe vyote. Ar-Rahmaanir rahiim (3) Mwingi wa Rehema mwenye kurehemu Maaliki Yaumid diin (4) Mfalme wa siku ya malipo. Iyyaakana'budu wa iyyaka nastaiin (5) Wewe tu ndiye tunayekuabudu na wewe tu ndiye tunayekuomba msaada. Ih-dinasswiraatwal Mustaqiim (6) Tuongoze njia iliyonyooka. Swiraatwalladhiina an amta alaihim, ghairil magh-dhwubi alaihim waladh-dhwaalliin (7) Njia ya wale uliowaneemesha juu yao, siyo ya wale uliowakasirikia wala ya wale waliopotea.
Ninasoma baada ya suratul faatiha kilicho chepesi kwenye Qur'ani katika rakaa ya kwanza na ya pili tu katika kila swala, na kusoma huku siyo lazima lakini kufanya hilo kuna malipo makubwa.
Hatua ya sita: Ninasema (Allahu Akbaru) Mwenyezi Mungu ni mkubwa, kisha nina rukuu mpaka unakuwa mgongo wangu umelingana sawa na mikono yangu miwili inakuwa juu ya magoti mawili hali ya kutawanya vidole, kisha ninasema katika kurukuu: “Sub-haana rabbial Adhwiim” (Ametakasika Mola wangu Mtukufu).
Hatua ya saba: Ninainuka kutoka kwenye rukuu kwa kusema: "Samiallaahu liman hamidah" (Amemsikia Mwenyezi Mungu mwenye kumhimidi), huku nikinyanyua mikono yangu usawa wa mabega mawili, na ukisimama sawa sawa mwili wangu, ninasema: "Rabbanaa walakal-hamdu" (Mola wetu Mlezi, sifa njema ni zako).
Hatua ya Nane: Ninasema: "Allaahu Akbar" (Mwenyezi Mungu mkubwa) na ninasujudu kwa mikono miwili na magoti mawili na miguu miwili na paji la uso na pua, na ninasema katika sijida yangu: "Sub-haana rabbial a'laa" (Ametakasika Mola wangu Mlezi Aliye juu)
Hatua ya tisa: Ninasema: Allahu Akbaru (Mwenyezi Mungu mkubwa) Na ninainuka kutoka kwenye kusujudu mpaka ninalingana sawa) hali ya kunyoosha mgongo huku nikikalia mguu wa kushoto na nikiusimamisha mguu wa kulia, na ninasema: "Rabbigh-firli"- Ewe Mola wangu Mlezi, nisamehe-.
Hatua ya kumi: Ninasema: "Allahu Akbaru" Mwenyezi Mungu Mkubwa -Na ninasujudu mara nyingine tena mfano wa sijida ya kwanza.
Hatua ya kumi na moja: Ninainuka kutoka katika sijida na ninasema: "Allahu Ak-baru" mpaka niwe sawa nikiwa nimesimama, na ninafanya hivyo katika rakaa zilizobakia kama nilivyofanya katika rakaa ya kwanza.
Baada ya rakaa ya pili ya swala ya Adhuhuri na Alasiri, na Magharibi, na Ishaa, ninakaa kwa ajili ya kusoma tahiyatu ya kwanza nayo ni: "Attahiyyaatu lillaahi, wasswalawaatu wattwayyibaatu, assalaamu a'laika ayyuhan nabiyyu, warahmatullaahi wabarakaatuh, assalaamu a'lainaa wa a'laa ibaadillaahi sswaalihiin, ash-hadu anlaa ilaaha illa llaahu, wa ash-hadu anna Muhammadan 'abduhu warasuuluhu" Tafsiri yake: Maamkizi (Amani) ni ya Mwenyezi Mungu, na swala na vile vilivyo vizuri, amani iwe juu yako ewe Nabii na rehema ya Mwenyezi Mungu na baraka zake, amani iwe juu yetu na juu ya waja wema wa Mwenyezi Mungu, nashuhudia kuwa hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu, na ninashuhudia kuwa Muhammadi ni mja wake na ni mjumbe wake. Kisha ninanyanyuka kwa ajili ya rakaa ya tatu baada ya hapo.
Baada ya rakaa ya mwisho ya kila swala ninakaa kwa ajili ya kusoma tahiyatu ya mwisho, nayo ni: "Attahiyyaatulillahi, Wasswalawaatu wattwayyibaatu, Assalaamu alaika Ayyuha Nabiyyu Warahmatullahi Wabarakaatuhu, Assalaamu alaina wa'alaa ibadillahi sswaalihiina, Ash-hadu an-laailaaha illa llahu wa anna Muhammadan rasuulullahi" Allahumma swalli alaa Muhammadin wa'alaa aali Muhammadin, kamaa swallaita alaa ibrahiima wa'alaa aali ibrahiima Innaka hamiidun majiid, Allahumma baariki alaa Muhammadin wa alaa aali Muhammadin, kamaa baarakta alaa ibraahiima wa- alaa aali ibrahiima innaka hamiidun majiid" Tafsiri yake: Maamkizi (Amani) ni ya Mwenyezi Mungu, na swala na vile vilivyo vizuri, amani iwe juu yako ewe Nabii na rehema ya Mwenyezi Mungu na baraka zake, amani iwe juu yetu na juu ya waja wema wa Mwenyezi Mungu, nashuhudia kuwa hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu, na ninashuhudia kuwa Muhammadi ni mja wake na ni mjumbe wake. Ewe Mwenyezi Mungu mpe rehema Muhammad na watu wa Muhammad, kama ulivyompa rehema Ibrahim na watu wa Ibrahim, hakika Wewe ni msifiwa mwenye utukufu, ewe Mwenyezi Mungu mbariki Muhammad pamoja na watu wa Muhammad kama ulivyombariki Ibrahim na watu wa Ibrahim, hakika Wewe ni msifiwa mwenye utukufu.
Hatua ya kumi na mbili: Kisha baada yake nitageuka upande wa kulia na kusema "Assalaam alaikum warahmatullahi" kisha nageuka upande wangu wa kushoto nakusema: "Assalamu alaikum warahmatullahi" Na kwa kufanya hivyo ninakuwa nimekamilisha swala.
Stara ya mwanamke wa kiislamu
Amesema Allah Mtukufu: "Ewe Nabii! Waambie wake zako, na mabinti zako, na wake wa Waumini wajiteremshie nguo zao, (ili kufunika nyuso zao, vifua vyao na vichwa vyao). Kufanya hivyo ni karibu zaidi kuwafanya wao wajulikane wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kusamehe na kurehemu." [Al-Ahzab: 59]
Amemuwajibishia Mwenyezi Mungu mwanamke wa kiislamu kuvaa hijabu na kujisitiri mwili wake kwa wanaume wa kando, kwa kuvaa vazi la kawaida katika mji wake, na wala haifai kwake kuvua hijabu yake isipokuwa mbele ya mume wake au maharimu wake (walioharamishwa kumuoa), na hao ni wale ambao haifai kwa mwanamke kuolewa nao milele nao ni: (Baba na walio juu yake, na mtoto na walio chini yake, na baba wadogo, na wajomba, na kaka, na mtoto wa kaka na mtoto wa dada, na mume wa mama atakapokuwa tayari kashamwingilia, na baba wa mke na walio juu yake, na mtoto wa mume na walio chini yake, na mume wa binti, na wanaharamishwa ndugu wa kunyonya sawa sawa na ndugu wa nasaba).
Na huchunga mwanamke wa kiislamu katika mavazi yake vigezo kadhaa:
Kwanza: Vazi kuenea mwili mzima.
Pili: Lisiwe vazi analolivaa mwanamke ni kwa ajili ya kujipamba.
Tatu: Na lisiwe jepesi linaloonyesha mwili wake.
Nne: Liwe pana na siyo finyu likasifu sehemu ya mwili wake
Tano: Lisiwe limetiwa manukato.
Sita: Lisifanane na vazi la kiume.
Saba: Na lisifanane na vazi la wasiokuwa wanawake wa kiislamu wakiwa kwenye ibada zao au sikukuu zao.
Katika sifa za waumini:
Amesema Allah Mtukufu: "Hakika wenye kumuamini Mwenyezi Mungu kikweli ni wale ambao akitajwa Mwenyezi Mungu hulainika nyoyo zao na wasomewapo Aya za Mwenyezi Mungu zinawazidishia Imani na kwa Mola wao wanategemea" [Al-anfaal:2]
1- Muumini ni mkweli katika mazungumzo yake wala hasemi uongo.
2- Anatekeleza ahadi na miadi.
3- Hatendi uovu katika ugomvi.
4- Anatekeleza amana.
5- Anampendelea ndugu yake muislamu anayoyapenda katika nafsi yake.
6- Ni mkarimu.
7- Anawafanyia watu wema.
8- Anaunga udugu.
9- Anaridhika na alichokipanga Mwenyezi Mungu na anamshukuru katika hali ya raha, na husubiri katika hali ya matatizo.
10- Anasifika nakuwa na haya.
11- Anawaonea huruma viumbe.
12- Moyo wake umesalimika na vinyongo na mwili wake umesalimika na kuwashambulia watu wengine.
13- Anawasamehe watu.
14- Hali riba wala hafanyi miamala ya riba.
15- Hafanyi zinaa.
16- Hanywi pombe.
17- Anawatendea wema majirani zake.
18- Hadhulumu wala kufanya hiyana.
19- Haibi walala hafanyi hila za kuiba.
20- Huwatendea wema wazazi wawili, hata kama si waislamu, na huwatii katika mambo mema.
21- Na huwalea watoto wake kwa tabia njema, na huwaamrisha kutekeleza wajibu wa sheria, na huwakataza kufanya mambo machafu na ya haramu.
22- Hajifananishi katika matendo na wasiokuwa waislamu katika mambo yao maalumu ya kidini au desturi zao ambazo zimekuwa alama na nembo yao.
Furaha yangu ipo katika dini yangu ya kiislamu
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenye kutenda mema mwanaume au mwanamke, naye akawa ni Muumini, basi tutampa maisha mema yenye utulivu duniani (hata kama ni mchache wa mali), na tutawalipa huko Akhera thawabu zao kwa uzuri zaidi ya walivyofanya (duniani)". [An Nahli: 97].
Na katika mambo ambayo huingiza furaha na ukunjufu wa moyo katika moyo wa muislamu ni mafungamano ya moja kwa moja na Mola wake bila kupitia kwa viumbe walio hai au waliokufa au masanamu, na Mwenyezi Mungu Mtukufu ametaja katika kitabu chake kitukufu kuwa yeye yuko karibu na waja wake wakati wowote, anawasikia na anawajibu dua zao kama alivyosema Mtukufu: "Na watakapo kuuliza waja wangu kuhusu Mimi, «Mimi Niko karibu nao, Nasikia maombi ya muombaji yeyote anaponiomba. Basi, na wanitii Mimi na waniamini Mimi, wapate kuongoka". [Al Baqarah: 186]. Na ametuamrisha Mwenyezi Mungu Mtukufu kumuomba yeye, na akalifanya jambo hili kuwa ni katika ibada kubwa ambazo hujikurubisha muislamu kwa Mola wake, pale aliposema Mwenyezi Mungu: "Na amesema Mola wenu niombeni nikujibuni" [Surat ghaafir: 60] Na Muislamu mwema daima huhitaji kwa Mola wake, na hudumisha dua mbele zake, na kujikurubisha kwake kwa kufanya ibada njema.
Na kwa hakika ametuweka Mwenyezi Mungu katika ulimwengu huu kwa hekima kubwa na wala hakutuumba kimchezo mchezo; na lengo ni kumuabudu yeye peke yake hana mshirika wake, na akatuwekea dini ya kimalezi iliyotimia na kuenea, hupangilia mambo yetu yote maalumu na yasiyokuwa maalumu, na imehifadhi sheria hii yenye uadilifu mambo ya dharura katika maisha, na mambo hayo ni: Kuhifadhi Dini yetu, na nafsi, na heshima, na akili, na mali, na mwenye kuishi kwa kufuata maamrisho ya sheria na akawa ni mwenye kujiepusha na mambo ya haramu kwa hakika mtu huyo atakuwa kahifadhi dharura hizi, na ataishi kwa furaha na mwenye matumaini katika maisha yake bila shaka.
Na mafungamano ya muislamu kwa Mola wake ni yakina, yanapelekea kupata utulivu na raha ya nafsi, na kuhisi utulivu amani na furaha, na kuhisi kuwa pamoja na Mola Mlezi -Aliyetakasika na kutukuka- na kutilia kwake umuhimu na mapenzi yake kwa mja wake muumini, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mwenyezi Mungu ni kipenzi cha wale walioamini, huwatoa gizani na kuwaleta katika nuru" [Al Baqara: 257].
Na mahusiano haya makubwa ni hali ya hisia zinazopelekea kuneemeka kwa kumuabudu mwingi wa rehema, na kuwa na shauku ya kukutana naye na kuuchochea moyo wake kupaa katika anga la furaha kwa kuhisi kwake utamu wa imani.
Na utamu huo ambao hakuna awezaye kuielezea vizuri ladha yake, isipokuwa aliyeionja kwa kufanya ibada na kujiepusha na makosa, ndiyo maana anasema Mtume-Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-: "Amekwisha ionja ladha ya imani, yule mwenye kumridhia Mwenyezi Mungu kuwa ndiye Mola wake, na Uislamu ndiyo dini, na Muhammad ni Mtume"
Ndiyo ikiwa mwanadamu atahisi kila wakati kuwa yuko mbele ya muumba wake, na akamjua kwa majina yake na sifa zake nzuri, na akamuabudu kama vile anamuona, na akatakasa ibada yake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na wala hakukusudia katika ibada hiyo isipokuwa kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu -Aliyetakasika na kutukuka-, ataishi maisha mazuri yenye furaha katika dunia na mwisho mzuri huko akhera.
Hata matatizo ambayo yanamtokea muumini katika dunia, kwa hakika joto lake huondoka kwa baridi ya yakini na kuridhia Kadari ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kumshukuru yeye kwa Kadari zake, kheri zake na shari zake, na kuridhika kwa hayo yote kwa ukamilifu.
Na katika mambo ambayo muislamu anapaswa kuyapupia ili izidi furaha yake na utulivu wake, ni kuzidisha kumtaja Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kuisoma Qur'ani tukufu kama alivyosema Mtukufu: "Wale walioamini na zikatulia nyoyo zao kwa kumtaja Mwenyezi Mungu, basi fahamuni vyema kwa kumtaja Mwenyezi Mungu nyoyo hutulia". [Al- ra'd: 28] Na kila muislamu anavyozidi kumtaja kwake Mwenyezi Mungu na kusoma kwake Qur'ani huzidisha mafungamano yake na Mwenyezi Mungu, na hutakasika nafsi yake na imani yake.
Na hivyo ndivyo inampasa muislamu kuwa na pupa ya kujifunza mambo ya dini yake kutoka katika vyanzo sahihi, ili amuabudu Mwenyezi Mungu kwa elimu, kwani amesema Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-: "Kutafuta elimu ni lazima kwa kila muislamu". Na awe ni mwenye kujisalimisha na kufuata amri za Mwenyezi Mungu Mtukufu aliye muumba, sawa sawa amejua hekima ya kuumbwa au hakuijua, kwani amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kitabu chake kitukufu: "Na haipasi kwa Muumini mwanamume wala Muumini mwanamke iwapo Mwenyezi Mungu na Mtume Wake wametoa uamuzi wa jambo kwenda kinyume nao, kwa kuchagua lile ambalo si walilolihukumu kwao. Na anayemuasi Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, bila shaka amepotea upotofu ulio wazi". [Al-Ahzab: 36]
Na rehema na amani za Allah ziwe juu ya Mtume wetu Muhammad na ali zake na Maswahaba zake.
MWISHO
Mpangilio wa maudhui:
Namba
Maudhui.
Kurasa
Kurudi kwenye jalada.
Hama kwa mpangilio wa maudhui.
Shiriki nasi uzoefu wa kitabu.
Karibu kwa kutembelea tovuti.
Kitabu hiki hufunguka kupitia simu
Bonyeza kuhamia kwenye maudhui.
Bonyeza picha ili kurudi kwenye jalada.
Skani alama ya QR kodi.
Uonyeshaji kimafunzo (Powerpoint)
Matoleo ya mradi.
Kitabu kilicho chapishwa.
Kitabu cha simu.
Tovuti.
Muonekano wa kimafunzo (Powerpoint)
Nakala maalumu kwa ajili ya simu janja.