أحكام الهدي والأضاحي والتذكية
HUKUMU ZA AL-HADYU, AL-ADHWAHI NA KUCHINJA
HUKUMU ZA AL-HADYU, AL-ADHWAHI NA KUCHINJA
Utangulizi
Kila sifa njema anazistahiki Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu, na rehema na amani zimfikie yule aliyetumwa kuwa rehema kwa walimwengu, na kwa familia yake, na Maswahaba wake, na wale waliofuata mwenendo wake, na wakaongoka kwa muongozo wake, mpaka Siku ya Malipo. Ama baada ya hayo:
Huu ni ujumbe mfupi, uliokusanya mambo muhimu anayoyahitaji Muislamu kuhusu wanyama wanaopelekwa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka, wanyama wachinjwao katika siku za Idi na masuala ya kuchinja. Tumeyakusanya haya kwa ajili ya mwenye kutembelea Misikiti miwili Mitukufu, mwanaume na mwanamke; ili wawe na elimu na utambuzi wa mambo ya dini yao, tukitaraji kutoka kwa Mkarimu, Mwingi wa kuneemesha awanufaishe kwa ujumbe huu, na aufanye kuwa wenye kufaa, na kwamba uwe kwa ajili ya uso wake tu. Kwani, Yeye ndiye mbora wa wenye kuombwa, na Mkarimu zaidi mwenye kutarajiwa.
Kamati ya Kielimu ya Jumuia ya Kuhudumia Maudhui za Kiislamu kwa Lugha mbalimbali.
Hukumu za wanyama wanaopelekwa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka na wanyama wachinjwao katika siku za Idi
Neno (Al-hadyu) linamaanisha kila mnyama anayetolewa kama zawadi kwa Eneo Takatifu (Al-Haram) na kuchinjwa humo miongoni mwa ngamia na wanyama wengineo wa mifugo. Waliitwa kwa jina hilo kwa sababu hupelekwa huko kama zawadi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka.
Na maana ya neno “Udh-hiya” kwa kuitia alama ya dhwamma kwenye herufi hamza, yaani “Udhhiya” au kwa kutia kasra, yaani “Idhhiya” ni kila kinachochinjwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu siku ya Idi na siku za Tashriiq - yaani kutandaza nyama kwenye jua - kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu.
Na wamekubaliana Waislamu wote kwamba vyote viwili - yaani kuchinja wanyama wanaopelekwa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka na wanyama wachinjwao katika siku za Idi - ni mambo yaliyo katika sheria.
Na mnyama anayepelekwa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka aliye bora zaidi ni ngamia, kisha ng'ombe - ikiwa atatolewa mzima mzima - kwa kuwa thamani yake iko juu, na huwanufaisha mafukara kwa sababu ya wingi wa nyama zake - kisha anafuatia mbuzi na kondoo.
Na bora ya kila aina ya mnyama ni yule aliyenona, kisha anafuata mwenye thamani ghali; kwa maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Ndiyo hivyo! Na anayetukuza alama (ibada) za Mwenyezi Mungu, basi hakika hayo ni katika unyenyekevu wa nyoyo." [Surat Al-Hajj: 32]
Na hakikubaliki kichinjwa katika kondoo isipokuwa awe "Jadha'u", naye ni yule aliyetimiza miezi sita. Vile vile anapaswa kuwa "Thaniyyu" katika wanyama wengineo wote miongoni mwa ngamia, ng'ombe na mbuzi. Naye Thaniyyu katika ngamia ni yule aliyetimiza miaka mitano, na katika ng'ombe ni yule aliyefikisha miaka miwili, na katika mbuzi ni yule aliyefikisha mwaka mmoja.
Kondoo anatosha kuwa mnyama wa zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka kwa mtu mmoja, na katika wanyama wachinjwao siku za Idi anatosheleza kwa mtu mmoja na watu wa nyumbani kwake. Naye ngamia mmoja na ng'ombe wa zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka hutosheleza watu saba; kwa mujibu wa hadithi ya Jaabir bin Abdullahi, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya wawili hao, kwamba alisema: "Tulichinja pamoja na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, mwaka iliyofanyika suluhu ya Hudaybiya ngamia mmoja kwa watu saba na ng'ombe mmoja kwa watu saba." Na katika tamko lingine: "Tulitoka pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, tukiwa tumekusudia kufanya ibada ya Hija, na akatuamrisha Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, tushiriki katika ngamia na ng'ombe. Kila watu saba washiriki katika ngamia (au ng'ombe) mmoja." Na katika tamko lingine: "Tulifanya ibada ya Hija pamoja na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na tukamchinja ngamia mmoja kwa watu saba, na ng'ombe mmoja kwa watu saba."[1] [1] Ameipokea hadithi hii Imamu Muslim.
Na kwa hadithi ya Abii Ayub Al-answariy, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipoulizwa: Walikuwa wakichinjwa vipi wanyama wa siku za Idi katika zama za Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake? Akasema: "Mtu mmoja alikuwa akichinja kondoo (au mbuzi) mmoja kwa ajili yake na watu wa nyumbani kwake, wakawa wakila na wakiwalisha watu wengine, mpaka watu wakaanza kujionyesha kwa fahari, basi ikawa kama unavyoona."[2] [2] Ameipokea Tirmidhiiy na Ibn Majah.
Na kondoo (au mbuzi) mmoja ni bora kuliko watu saba kushirikiana katika ngamia na ng'ombe.
Haifai wala haitoshelezi kwa wanyama wapelekwao kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka au wanyama wachinjwao katika siku za Idi isipokuwa wanyama walio salimika kutokana na maradhi, mapungufu ya viungo na kukonda. Hivyo basi, hafai mwenye jicho chongo ambaye uchongo wake unaonekana wazi, wala kipofu, wala mnyama aliyekonda sana kiasi kwamba hana mafuta mwilini, wala aliye kilema asiyeweza kutembea pamoja na mwenye afya nzuri, wala mnyama asiye na meno ya mbele kabisa, wala ambaye maziwa yake yamekauka kutokana na uzee, wala hafai mnyama mwenye maradhi yanayoonekana wazi; kwa ushahidi wa hadithi ya Al-baraau bin 'Aazib, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Alisimama kati yetu Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na akasema: "Wanyama wa aina nne hawafai katika ibada ya kuchinja siku ya Idi: Mnyama mwenye jicho moja linaloonekana wazi, na mnyama mgonjwa ambaye ugonjwa wake unaonekana wazi, na mnyama kilema ambaye ulemavu wake unaonekana wazi, na mnyama aliyekonda sana asiye na mafuta mwilini."[3] [3] Ameipokea Abu Daud na Tirmidhiy na An-Nasaaiy, Ibn Majah.
Amesema imamu Tirmidhiy, Mwenyezi Mungu amrehemu, "Na hivi ndivyo inavyotekelezwa kulingana na wanazuoni (wetu)."[4] [4] Ameipokea Tirmidhiy.
Na wakati wa kuchinja mnyama anayepelekwa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka kwa mwenye kufanya Hija ya aina ya Tamattui, na mnyama anayechinjwa katika siku za Idi, ni baada ya swala ya Idi mpaka mwisho wa siku za Tashriiq (yaani siku za kutanda nyama kwenye jua) kulingana na kauli sahihi.
Na inapendekezwa kwa mtu aliyetoa mnyawa kama zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka kwamba ale kutoka katika kichinjwa chake hicho ikiwa ni kichinjwa cha Hija ya Tamattui au Qiraan[1], na kadhalika ikiwa ni mnyama aliyemchinja katika siku za Idi. Vile vile, atamtoa kama zawadi na sadaka kwa kugawa mafungu matatu; kwa maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na kuleni katika wanyama hao na mlisheni mwenye shida aliye fakiri." [Suratul-Hajj: 28]
Ama kuhusu kichinjwa cha fidia, navyo ni vichinjwa vinavyochinjwa kwa sababu ya kufanya jambo lililokatazwa kwa anayefanya Hija, au kwa sababu ya kuacha jambo la wajibu katika Hija. Hao haruhusiwi kula chochote katika nyama hizo.
Na mwenye kutaka kuchinja mnyama wa Udhuhiya, anatakiwa zitakapoingia siku kumi za mwanzo katika Mwezi wa Dhul-Hijja, asitoe chochote katika nywele zake wala kucha zake mpaka atakapokuwa amekwishamchinja mnyama wake. Hili ni kutokana na maneno yake Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, "Zitakapoingia siku kumi (za mwanzo katika Mwezi wa Dhul-Hijja), na akataka mmoja wenu kuchinja, basi na asiondoshe chochote katika nywele zake wala kucha zake mpaka atakapokuwa amemaliza kuchinja."[5] [5] Ameipokea imamu Muslimu.
Na ikiwa atafanya chochote katika hayo yaliyokatazwa, basi atamuomba Mwenyezi Mungu msamaha na wala hawajibiki kutoa fidia.
Namna ya kuchinja mnyama wa zawadi ya Msikiti Mtukufu wa Makka na mnyama achinjwaye katika Idi ya kuchinja ni kama ifuatavyo:
1- Asichinje isipokuwa Muislamu mwenye upambanuzi, mwenye akili timamu, au Mayahudi na Manaswara. Mchinjaji atakusudia kuchinja kwa sheria ya Kiislamu na wala asichinje kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na wala asilitaje jina la asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Atataja jina la Mwenyezi Mungu wakati wa kuchinja kwa kusema “bismillahi” au wakati wa kuchoma kooni. Atachinja kwa kutumia zana yenye ncha kali na siyo kutumia meno wala kucha, na ahakikishe kwamba amemwaga damu kutoka kwa mnyama huyo sawasawa. Vile vile, ni lazima kwa mchinjaji awe amepewa idhini ya kuchinja kisheria.[6] [6] Hukumu za Kuchinja Wanyama wa Idi, kitabu cha mwanazuoni mkubwa, Muhammad bin Uthaiymin, ukurasa wa 56-87.
2- Atachagua kichinjwa cha Idi, na ajitahidi kuchagua kichinjwa kilichokamilika zaidi. Kwani, "Alichinja Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kondoo wawili weupe wenye pembe. Aliwachinja kwa mikono yake na akataja jina la Mwenyezi Mungu, akatoa takbira na akaweka mguu wake kwenye mbavu zao."[7] [7] Ameipokea Bukhari na Muslimu.
3- Kumfanyia wema mnyama anayechinjwa. Atafanya kila ambalo litampa utulivu mnyama huyo wakati wa kumchinja. Miongoni mwayo ni kwamba achinje kwa kutumia zana yenye makali, na apitishe kwenye sehemu ya kuchinja kwa nguvu na haraka. Kwa sababu kinachotakikana katika kuchinja ni kuitoa roho haraka na kwa ukamilifu pasina kumuadhibu mnyama huyo. Haya ni kwa hadithi ya Shaddad bin Awsi, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Mambo mawili nimeyahifadhi kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu amewajibisha (kufanya) wema katika kila kitu. Kwa hivyo, mtakapoua, basi ueni kwa namna nzuri. Na mtakapochinja, basi chinjeni kwa namna nzuri. Na anoe mmoja wenu zana yake ya kuchinjia, na akitulize kichinjwa chake."[8] [8] Ameipokea Imamu Muslimu.
Na ni machukizo kukinoa kisu ilhali mnyama huyo anakiona; kwa mujibu wa yaliyokuja katika hadithi ya bin Umar, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na baba yake, kwamba alisema: Aliamrisha Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kukinoa kisu na kukificha asikione mnyama anayechinjwa na akasema: "Atakapochinja mmoja wenu, basi na achinje haraka."[9] [9] Ameipokea Ahmad na Ibin Maajah.
4- Ikiwa kichinjwa ni ngamia; atamchinja huku amesimama wima hali ya kuwa amemfunga mkono wake wa kushoto; kwa mujibu wa hadithi ya Abdullah bin Umar, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake yeye na baba yake, "Kuwa yeye alikuja kwa mtu akiwa amemuinamisha ngamia wake akitaka kumchinja. Basi akasema bin Umar: Mwachilie asimame huku umemfunga. Hii ndiyo sunna ya Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake."[10] [10] Ameipokea Imamu Bukhar na Muslimu.
5- Na ikiwa mnyama achinjwae si ngamia; atamchinja akiwa amelazwa kwa ubavu wake wa kushoto, na ataweka mguu wake pembeni mwa shingo yake; ili aweze kumdhibiti; kwa mujibu wa hadithi ya Anas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema, "Alichinja Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kondoo wawili weupe wenye pembe. Aliwachinja kwa mikono yake, akataja jina la Mwenyezi Mungu, akatoa takbira na akaweka mguu wake kwenye mbavu zao."[11] [11] Ameipokea Bukhari na Muslimu.
6- Kusema "Bismillahi (kwa jina la Mwenyezi Mungu)" wakati wa kuchinja au kudunga kooni. Kufanya hivyo ni wajibu kwa maneno yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi kuleni katika yale yaliyotajiwa jina la Mwenyezi Mungu, ikiwa mnaziamini Aya zake." [Surat An-'aam: 118] Na kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Wala msile katika vile ambavyo halikutajwa jina la Mwenyezi Mungu juu yake. Kwani huko hakika ni kuvuka mipaka. Na kwa yakini mashetani wanawaletea ufunuo (wahyi) marafiki zao ili wabishane nanyi. Na mkiwatii, basi nyinyi kwa hakika mtakuwa washirikina." [Surat An-'aam: 121] Na kwa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, "Kichinjwa chochote kilichomwagwa damu yake na likatajwa jina la Mwenyezi Mungu juu yake; basi kileni (kichinjwa hicho) maadamu hakikuchinjwa kwa meno wala kucha."[12] [12] Ameipokea Imamu Bukhari na Muslimu.
Inapendekezwa kuleta Takbira kwa kusema "Allahu Akbar (Mwenyezi Mungu ndiye Mkubwa)" pamoja na kusema "Bismillah (kwa jina la Mwenyezi Mungu)"; kwa mujibu wa hadithi ya Jaabir, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: Nilishuhudia nikiwa pamoja na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, swala ya Idul-adhha katika kiwanja. Alipomaliza hotuba yake, aliteremka kutoka katika mimbari yake, akaletewa kondoo dume, akalichinja kwa mkono wake na akasema: "Bismillah wallahu akbaru (ninaanza kwa jina la Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa). Kichinjwa hiki ni kwa ajili yangu na kwa ajili ya kila ambaye hajaweza kuchinja katika umma wangu."[13] [13] Ameipokea Abuu Daud, na Tirmidhiy, na imamu Al-albaniy alisema kwamba ni hadithi sahihi.
7-Kukata mshipa wa pumzi, umio, mishipa miwili ya shingo na kumwaga damu. Amesema imamu bin Baaz, Mwenyezi Mungu amrehemu: "Hakika uchinjaji wa kisheria wa ngamia, ng'ombe na kondoo (au mbuzi) una namna tatu:
Namna ya kwanza: Mchinjaji akate mshipa wa pumzi, umio na mishipa miwili ya shingo. Huu ndio uchinjaji uliokamilika zaidi na ulio mzuri zaidi. Kwa maana, ikiwa vitu hivi vinne vitakatwa, basi kichinjwa hicho kinakuwa halali kwa makubaliano ya maulamaa wote.
Namna ya pili: Mchinjaji akate mshipa wa pumzi, umio na mmoja wa ile mishipa miwili ya shingo. Uchinjaji huu ni halali, ni sahihi na ni mzuri, ingawa uko chini ya ule uchinjaji wa kwanza.
Namna ya tatu: Mchinjaji akate mshipa wa pumzi pamoja na umio peke yake. Hivi pia ni sahihi, na kauli hii wameisema kundi kubwa la wanazuoni na ushahidi wao ni maneno yake Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kichinjwa chochote kilichomwagwa damu yake na likatajwa jina la Mwenyezi Mungu juu yake, basi kileni, maadamu siyo kwa kutumia meno wala kucha."[14] Na hili ndilo chaguo bora katika suala hili.[15] [14] Ameipokea Bukhari na Muslimu. [15] Tazama: Mkusanyo wa Fatwa za bin Baaz, 18/26.
Na Mwenyezi Mungu pekee ndiye mwenye kuombwa atunufaishe kwa yale tuliyojifunza, na atufunze yenye kutunufaisha. Hakika Yeye ndiye Mpaji, Mkarimu. Na rehema na amani nyingi zimuendee Nabii wetu Muhammadi na watu familia yake.